Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 4/1 kur. 19-23
  • Kukua Pamoja na Tengenezo la Yehova Katika Afrika Kusini

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kukua Pamoja na Tengenezo la Yehova Katika Afrika Kusini
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Malezi ya Kikristo
  • Biashara Yenye Mafanikio
  • Sababu kwa Nini Niliacha Shule Mapema
  • Utumishi wa Betheli na Shule ya Gileadi
  • Huduma Yangu ya Kuendelea
  • Somo Chungu
  • Baraka Zaidi
  • Maisha Chini ya Ubaguzi wa Rangi
  • Upanuzi wa Betheli
  • Kupokea ‘Haja za Moyo Wangu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Maisha Yenye Furaha Katika Utumishi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Je, Waweza Kujitolea?
    Huduma Yetu ya Ufalme—2001
  • Je, Hii Yaweza Kuwa Kazi-Maisha Inayokufaa Zaidi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 4/1 kur. 19-23

Kukua Pamoja na Tengenezo la Yehova Katika Afrika Kusini

Kama Ilivyosimuliwa na Frans Muller

WAKATI kaka yangu David na mimi tulipokaribia gari-moshi la jioni ambalo tulikuwa tukilichukua kwa ukawaida kutoka kituo kikuu cha Cape Town, tulishangaa kuona ishara zilizosema “Weupe Pekee.” Chama kiitwacho Nationalist Party kilikuwa kimeshinda uchaguzi katika 1948 na kilikuwa kimeanzisha sera ya ubaguzi wa rangi.

Bila shaka, ubaguzi wa rangi ulikuwa umezoewa kwa muda mrefu katika Afrika Kusini, kama ulivyokuwa umezoewa katika nchi nyingi za Afrika katika nyakati za ukoloni. Lakini sasa ulikuwa ukitekelezwa na sheria, na hatukuruhusiwa tena kusafiri katika behewa moja pamoja na Waafrika wa Kusini weusi-weusi. Miaka 44 baadaye, ubaguzi wa rangi unaondoshwa.

Katika kipindi chote cha ubaguzi wa rangi wa kisheria, kilichotokeza magumu katika kuendeleza huduma yetu kwa njia ambayo tungalipenda, nilitumikia nikiwa mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Kwa sasa, nikiwa na umri wa 65, naweza kutazama nyuma kwa ule ukuzi mzuri ajabu wa tengenezo la Yehova katika kusini mwa Afrika, na ninashukuru kwa ajili ya pendeleo la kukua pamoja nalo.

Malezi ya Kikristo

Baba yangu alipokuwa kijana, mapema kila asubuhi alitakwa amsomee babu yangu Biblia kwa sauti. Hatimaye baba alikuza upendo wenye kina kirefu kwa Neno la Mungu. Nilipozaliwa katika 1928, baba yangu alikuwa akitumikia kwenye baraza la kanisa la Dutch Reformed Church katika Potgietersrust. Mwaka huo mjomba wangu alimpa nakala ya kitabu The Harp of God.

Hata hivyo, baba, alimwambia mama akichome kitabu hicho, akisema kwamba kilitoka kwa dhehebu fulani. Lakini mama alikiweka, na siku moja baba alipopata kukiokota, kilifunguka kwenye kichwa “Je! Mungu Hutesa Yeyote?” Ingawa alihisi kwa hakika kwamba Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo, hawakuwa sahihi, udadisi wake ulimshinda, akaanza kusoma. Hakuweza kuacha kukisoma. Alfajiri, alipoingia kitandani, alisema: “Ma, sitaki kukubali, lakini wanayo kweli.”

Siku iliyofuata, baba alienda mwendo wa kilometa 50 kwa baiskeli ili kupata vitabu vingine kutoka kwa Mwanafunzi wa Biblia aliyekuwa karibu zaidi. Kwa ukawaida, alikuwa akisoma hadi usiku sana. Hata alijaribu kumsadikisha padri wa Dutch Reformed juu ya kweli za Biblia aliyokuwa akijifunza, akitazamia kwamba kanisa lingefanya marekebisho fulani. Lakini jitihada zake hazikufaulu, kwa hiyo alijiuzulu kutoka kanisa akaanza kuhubiri kwa bidii. Kweli ya Biblia ikawa ndilo jambo la maana zaidi maishani mwake na jambo la maana zaidi katika nyumba yetu. Nilikua nikiwa katika mazingira hayo.

Baadaye, baba akawa painia, au mhudumu wa wakati wote. Alisafiri miendo mirefu katika aina ya zamani ya gari liitwalo Ford T, ili kuhubiri. Baada ya miaka michache, mahitaji ya familia yetu iliyokuwa ikiongezeka yalimlazimisha aache kufanya upainia, lakini alibaki mwenye bidii sana katika kazi ya kuhubiri. Jumapili nyinginezo tulikuwa tukisafiri hadi kilometa 90 ili kuhubiri pamoja na yeye katika mji wa Pietersburg.

Biashara Yenye Mafanikio

Hatimaye baba akafungua duka dogo la rejareja la kuuzia bidhaa mbalimbali. Upesi duka hilo likaongezeka ukubwa mara mbili, na duka la pili likafunguliwa. Wakulima wengine matajiri wakafanya ushirikiano wa kibiashara pamoja na baba, na baadaye wao wote wakaendesha duka la uuzaji jumla pamoja na mfululizo wa maduka sita ya rejareja kotekote katika eneo kubwa.

Baadhi ya kaka zangu walijiunga na biashara hiyo na sasa wakawa na taraja la kuwa matajiri. Hata hivyo, hali yetu ya kiroho ikaanza kuathiriwa. Tulikuja kukubalika zaidi na marafiki na majirani wa kilimwengu, waliotualika kwenye karamu zao. Akiiona hatari hiyo, baba aliikutanisha familia akaamua kuuza biashara hiyo na kuhamia Pretoria ili tuweze kufanya zaidi katika utumishi wa Yehova. Alibaki na duka moja tu, iliyotunzwa na wafanyakazi wa kuajiriwa.

Kaka zangu Koos na David wakaanza kufanya upainia, hivyo wakijiunga na dada yangu Lina, mwenye umri mkubwa zaidi, pamoja na kaka yangu mwenye umri mkubwa zaidi, ambaye, kwa kusikitisha, aliacha ibada ya kweli baadaye. Katika mwezi mmoja wa 1942, familia yetu yenye washiriki kumi ilitumia jumla ya muda wa saa 1,000 katika kazi ya kuhubiri. Mwaka huo nilifananisha kuwekwa wakfu maisha yangu kwa Yehova kwa njia ya kuzamishwa majini.

Sababu kwa Nini Niliacha Shule Mapema

Katika 1944, wakati Vita ya Ulimwengu 2 ilikuwa katika upeo wayo, Gert Nel, mwangalizi asafiriye wa Mashahidi wa Yehova, aliniuliza kama nilikuwa ninapanga kuingia utumishi wa upainia. “Ndiyo,” nikajibu, “baada ya miaka miwili, ninapomaliza shule ya upili.”

Akifikiri juu ya mtazamo wa Mashahidi wa Yehova wengi wakati huo, alionya hivi: “Uwe mwangalifu usije ukapatwa na Har–Magedoni ukiwa ungali waketi kwenye benchi za shule.” Kwa kuwa sikutaka hilo litukie, niliacha shule na kuingia kazi ya upainia katika Januari 1, 1945.

Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa Vereeniging, karibu na Johannesburg, na washiriki wangu walikuwa Piet Wentzel na Danie Otto. Mara nyingi nilikuwa nikitumia zaidi ya muda wa saa 200 kwa mwezi nikihubiri. Hatimaye, Piet alipewa mgawo mwingine kwenda jiji la Pretoria, na Danie akalazimika kuacha kufanya upainia ili kumsaidia baba yake mzee-mzee kwenye shamba. Hilo liliniacha mimi nikiwa Shahidi pekee wa kutunza mafunzo ya Biblia nyumbani 23 katika Vereeniging.

Upesi baadaye, nilipokea barua kutoka kwa ofisi ya tawi iliyonipa mgawo kwenda Pretoria. Ingawa wakati huo sikuelewa sababu ya mgawo huo mpya, nilikuja kutambua baadaye kwamba lisingalikuwa jambo la hekima kumwacha kijana mwenye umri wa miaka 17 asiye na ujuzi akiwa peke yake. Bado nilihitaji mazoezi mengi na ningaliweza kuvunjika moyo.

Baada ya kutumikia katika Pretoria na kupata ujuzi uliohitajiwa, nilialikwa kuwa painia wa pekee. Kisha Piet Wentzel na mimi tukapanga kutoa mazoezi ya kihuduma yenye mafaa sana kwa wachanga waliokuja Pretoria ili kufanya upainia. Kufikia wakati huo Piet alikuwa amepewa mgawo kuwa mwangalizi asafiriye katika eneo hilo. Baadaye alimwoa dada yangu Lina, na sasa wanatumikia pamoja kwenye ofisi ya tawi la Afrika Kusini.

Miongoni mwa wale waliokuja kufanya upainia katika Pretoria alikuwa Martie Vos, mwanamke mchanga mwenye kuvutia aliyekuwa amelelewa katika familia ya Mashahidi. Tulivutiana kimahaba, lakini tulikuwa tungali matineja, wachanga mno kuoana. Hata hivyo, tulipopokea migawo kwenda mahali mbalimbali, tuliwasiliana kwa barua.

Utumishi wa Betheli na Shule ya Gileadi

Katika 1948, nilialikwa kutumikia kwenye ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Cape Town. Wakati huo, hatukuwa na mahali pamoja pa kukaa kwa sisi 17 tuliofanya kazi katika ofisi tatu zilizokodiwa pamoja na kiwanda kidogo kilichokuwa karibu. Baadhi yetu walikaa pamoja na familia mbalimbali, na wengine waliishi katika nyumba za bweni.

Kila siku ya kazi wale washiriki 17 wa familia ya Betheli walikusanyika pamoja kwa ajili ya ibada ya asubuhi katika chumba cha kubadilishia nguo cha kile kiwanda kidogo. Wengi wetu tulihitaji kujipangia milo yetu wenyewe ya mchana. Halafu, baada ya siku nzima ya kazi, tungesafiri kwenda kwenye makao yetu katika sehemu tofauti-tofauti za Cape Town. Ilikuwa katika mojayapo safari hizo kwamba, kama ilivyotaja tayari, ndugu yangu David na mimi tulishangazwa na ile ishara iliyotangaza, “Weupe Pekee.”

Nilipowasili kwenye ofisi ya Cape Town kwa mara ya kwanza, nilitambua kwamba nilikuwa ningali na mengi ya kujifunza, kwa hiyo nilimwuliza Ndugu Philips, mwangalizi wetu wa tawi, hivi: “Nifanye nini ili nifahamu yote?”

“Frans,” yeye akajibu, “usihangaikie kufahamu yote. nenda sambamba tu!” Nimejaribu sikuzote kufanya hivyo, na nimejifunza kwamba kwa kwenda sambamba na yale ambayo tengenezo la Yehova huandaa kwa njia ya chakula na mwelekezo wa kiroho, mtu ataendelea kukua pamoja nalo.

Katika 1950, nilialikwa kuhudhuria darasa la 16 la Watchtower Bible School of Gilead ili kupata mazoezi ya umishonari. Wakati huo shule ilikuwa katika South Lansing, New York, yapata kilometa 400 kaskazini mwa Brooklyn, New York. Nilipokuwa nikifanya kazi kwa muda tu kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, nilijionea mwenyewe kitovu chenyewe cha tengenezo la Yehova lionekanalo. Ujitoaji wa moyo wote wa wale wanaoongoza huko ulinifanya nithamini sana tengenezo la Yehova.

Huduma Yangu ya Kuendelea

Baada ya kurudi Afrika Kusini, niliwekwa rasmi kutumikia nikiwa mwangalizi asafiriye katika kaskazini mwa Transvaal, nilikokulia. Baada ya kuandikiana kwa miaka sita, Martie na mimi tulioana katika Desemba 1952, na yeye akajiunga na mimi katika kazi ya kusafiri. Uthamini ambao ndugu wetu wa Kikristo walikuwa nao kwa ajili ya ziara zetu ulichangamsha moyo.

Kwa kielelezo, wakati mmoja tulipotumikia kundi moja katika jumuiya ya ukulima, tulikaa pamoja na familia walioomba msamaha kwa ajili ya kutokuwa na maziwa ya chai au kahawa. Baadaye tulipata kujua kwamba walikuwa wameuza ng’ombe wao pekee wa maziwa ili kuwa na fedha za kutosha za kununua petroli ya kutuchukua kuzuru sehemu za mbali za eneo lao kuwatolea ushahidi wakulima. Jinsi tulivyowapenda ndugu wa aina hiyo!

Nyakati nyingine nilihisi kutostahili vya kutosha kwa kazi ya mzunguko, hasa niliposhughulikia matatizo yaliyohusu watu wenye umri mkubwa zaidi. Wakati mmoja nilihisi nimeishiwa sana kihisiamoyo hivi kwamba nilimwambia Martie kwamba hapaswi kushangaa ikiwa tungepewa mgawo mwingine wa kazi ya upainia kwa sababu ya ukosefu wangu wa ujuzi. Alinihakikishia kwamba angefurahia kutumikia katika kazi yoyote maadamu tungebaki katika huduma ya wakati wote.

Ebu wazia mshangao wetu tulipofika kundi lililofuata na barua zetu zikatia ndani mgawo wa kutumikia katika kazi ya wilaya! Kwa karibu miaka miwili, tulisafiri kotekote katika Afrika Kusini na Namibia, ambayo wakati huo iliitwa Afrika Kusini Magharibi. Hata hivyo, kwa sababu ya mfumo wa ubaguzi wa rangi, mara nyingi kazi yetu ilikuwa ngumu. Mara nyingi tulikatazwa hati za ruhusa za kuingia miji ya watu weusi na nyakati nyingine hatukupewa ruhusa za makusanyiko.

Kwa kielelezo, katika 1960, tulipata ruhusa ya kuwa na mkusanyiko wa wilaya katika Soweto. Ndugu weusi kutoka makundi ya mbali walikuwa tayari wamenunua tikiti za gari-moshi na za basi ili kuja, lakini serikali ikasikia juu ya mipango yetu na ikaifuta ruhusa. Kwa busara, tukamwendea msimamizi mwenye urafiki wa mji ulio kilometa 20 upande ule mwingine wa Johannesburg. Alituandalia kwa fadhili vifaa vilivyo bora hata zaidi, na tukawa na mkusanyiko mzuri ajabu, uliofurahiwa na watu zaidi ya 12,000!

Hali imebadilika kama nini katika miaka ya hivi majuzi! Sasa, ubaguzi wa rangi ukiwa unaondoshwa, twaweza kukutana pamoja kwa uhuru mahali popote katika maeneo ya weusi, weupe, machotara, au Wahindi. Wote, haidhuru rangi yao, wanaweza kuketi pamoja na kufurahia ushirika. Ni tofauti za lugha tu zilizo na uvutano juu ya mahali ambapo mtu huenda akataka kuketi.

Somo Chungu

Nyuma katika 1947, baba yangu alifanya kosa kubwa. Duka lake, lililokuwa zaidi ya kilometa 200 kutoka mahali yeye na mama walipokuwa wakiishi, lilikosa kuwa na faida kwa ajili ya usimamizi usiofuatia haki, kwa hiyo alihamia huko peke yake ili kulisimamia mwenyewe. Vipindi virefu vya kutengwa na mama vilimsababisha atumbukie katika kishawishi. Tokeo likawa, alitengwa na ushirika.

Hilo lilikaza juu yangu kwa njia ya binafsi, yenye uchungu, kwamba kuwa na bidii kwa ajili ya kweli ya Biblia hakutoshi. Ni lazima wote washikamane na kanuni za Biblia. (1 Wakorintho 7:5) Baada ya miaka mingi, baba alirudishwa kuwa sehemu ya kundi la Kikristo akatumikia kwa uaminifu mpaka kifo chake katika 1970. Mama yangu mpendwa alibaki mwaminifu mpaka kifo chake katika 1991.

Baraka Zaidi

Katika 1958, Martie na mimi tulihudhuria ule mkusanyiko mkubwa zaidi uliopata kufanywa na Mashahidi wa Yehova, kwenye Yankee Stadium na Polo Grounds katika New York. Tulifurika sana kwa shangwe kuweza kuwa sehemu ya tengenezo zuri ajabu la Yehova. Kuwa pamoja na umati huo mkubwa wa watu zaidi ya 253,000 Jumapili alasiri kulikuwa ono ambalo hatutasahau kamwe. Kwetu sisi, huo ulikuwa uhalisi wa ule ‘mkutano mkubwa kutoka kwa kila taifa’ ukiwa umekusanyika pamoja kwa amani. (Ufunuo 7:9, 10) Martie alibaki nyuma katika New York ili kuhudhuria Shule ya Gileadi, nami nikarudi kwenye kazi ya wilaya katika Afrika Kusini.

Katika 1959, baada ya Martie kurudi baada ya kuhudhuria darasa la 32 la Shule ya Gileadi, tulialikwa kutumikia kwenye ofisi ya tawi ya Afrika Kusini, iliyokuwa karibu na Elandsfontein, mashariki mwa Johannesburg. Muda wote wa miaka iliyopita, nimeona maendeleo ya tengenezo katika njia nyingi sana, hasa ukuzi walo katika upendo na hisia-mwenzi. Nimejifunza kwamba Yehova huelekeza tengenezo lake kupitia Yesu Kristo na atawatumia wale wanajitoa wenyewe.

Katika 1962, nilirudi Brooklyn, New York, ili kuhudhuria mtaala wa mazoezi ya tawi wa muda wa miezi kumi. Hilo lilithibitika kuwa lenye msaada katika 1967, nilipowekwa rasmi kuwa mwangalizi wa tawi wa Afrika Kusini. Katika 1976, Halmashauri za Tawi ziliwekwa rasmi, kwa hiyo sasa daraka la kufanya maamuzi ya maana katika Afrika Kusini ni la wazee wa Kikristo watano.

Maisha Chini ya Ubaguzi wa Rangi

Sheria za ubaguzi wa rangi ziliathiri utendaji wa tawi letu. Kao la Betheli la Elandsfontein lilipojengwa katika 1952, sheria ilitaka jengo jingine lijengwe nyuma ili kuandaa makao ya akina ndugu weusi na machotara. Sheria ilitaka pia kwamba wale chakula kando na weupe katika yaitwayo eti makao ya Kiafrika. Baadaye, ilipangwa wale chakula katika jiko la Betheli. Hilo ndilo lililokuwa mpango wa kula tulipofika Betheli katika 1959. Nilipinga sana kutenganisha huko kwa msingi wa rangi.

Hatimaye, serikali ilikataa kuwaruhusu ndugu zetu weusi waishi katika jengo lililokuwa nyuma ya Kao la Betheli kuu. Ndugu hao walilazimika wakae katika mji wa watu weusi yapata kilometa 20 kutoka hapo. Wengine wao waliishi katika makao yaliyokodiwa na wengine katika hosteli ya wanaume waseja. Hali hiyo isiyopendeza iliendelea kwa miaka mingi.

Upanuzi wa Betheli

Wakati uo huo, Betheli ya Elandsfontein ilihitaji kupanuliwa. Baada ya kuipanua mara tatu, tulikuwa tumefikia upeo wa nafasi yetu. Baraza Linaloongoza likaelekeza kwamba tulipaswa kutafuta nafasi nyingine katika eneo ambako wenye mamlaka wa mahali hapo kwa kutumaini wangeturuhusu tujenge majengo makubwa ya Betheli ambamo ndugu zetu weusi pia wangeweza kukaa. Kila asubuhi familia ya Betheli ilikuwa ikisali kwamba Yehova aweze kwa njia fulani kufungulia jambo hilo njia.

Ilikuwa siku ya kushangilia kama nini tulipopata hatimaye shamba lifaalo kwenye sehemu za njenje za Krugersdorp, magharibi mwa Johannesburg! Hata hivyo, tulitakwa tena tujenge jengo la kando kwa ajili ya ndugu zetu weusi. Tulitii hilo lakini hatukuweza kupata ruhusa ya watu weusi zaidi ya 20 kukaa huko. Kwa shukrani, kufikia miaka ya katikati ya 1980, hali ilianza kubadilika. Serikali ililegeza sheria hizo kali za ubaguzi wa rangi, na ndugu wengine zaidi, weusi, machotara, na Wahindi wakaitwa kutumikia pamoja na sisi Betheli.

Sasa tuna familia ya Betheli yenye furaha, iliyounganika, ambamo watu mmoja mmoja, haidhuru taifa au rangi yao, wanaweza kuishi katika jengo lolote wanalochagua. Pia, baada ya miaka mingi ya kung’anga’nia, tulipewa hatimaye utambuzi wa kisheria kuwa dini. Shirika la kisheria la mahali hapa limefanyizwa ambalo limesajiliwa kwa jina “Jehovah’s Witnesses of South Africa.” Sasa tuna maafisa wetu wenyewe wa kufanya shughuli za ndoa, na katika maeneo ya makao ya watu weusi Majumba ya Ufalme yanaongezeka kwa haraka.

Tengenezo la Yehova limefanya maendeleo kama nini tangu siku za mapema nilipotumikia katika ofisi ya tawi ya Cape Town! Kutoka familia ndogo ya washiriki 17 bila Kao la Betheli, tumekua sasa kufikia familia ya Betheli ya watu zaidi ya 400, tukiwa na majengo makubwa yenye kompyuta za kimambo-leo, matbaa za rotari, na Kao la Betheli lenye kupendeza! Naam, nimekuwa na pendeleo la kukua pamoja na tengenezo la Yehova katika Afrika Kusini. Tumeongezeka kutoka wahubiri wa Ufalme wapatao 400 nilipoanza huduma miaka 50 hivi iliyopita hadi karibu 55,000 leo!

Namshukuru Yehova kwamba, kwa miaka 39 iliyopita, nimekuwa na mke mwenye kuniunga mkono sana akiwa kando yangu. “Kikombe changu kinafurika.” (Zaburi 23:5) Martie na mimi twashukuru kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova lenye kuelekezwa kwa roho na tunaazimia kuendelea kumtumikia Yehova katika nyumba yake, katika Betheli, na kwenda sambamba na tengenezo lake linalosonga mbele.

[Ramani katika ukurasa wa 19]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

ANGOLA

ZAIRE

ZAMBIA

ZIMBABWE

BOTSWANA

NAMIBIA

SWAZILAND

LESOTHO

AFRIKA KUSINI

Pretoria

Johannesburg

Cape Town

Port Elizabeth

BAHARI YA ATLANTIKI YA KUSINI

BAHARI YA HINDI

MLANGOBAHARI WA MUSUMBIJI

[Picha katika ukurasa wa 20]

Piet Wentzel na Frans Muller (kushoto) katika kazi ya upainia katika 1945

[Picha katika ukurasa wa 23]

Frans na Martie Muller

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki