Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 7/1 kur. 9-13
  • Kupokea ‘Haja za Moyo Wangu’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kupokea ‘Haja za Moyo Wangu’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mavutano ya Pale Mwanzoni
  • Kuutafuta Ukweli
  • Tunaunda Kundi Lililo Dogo
  • Kuingia Utumishi wa Wakati Wote
  • Kupokea ‘Haja Nyingine ya Moyo Wangu’
  • Kujifunza Masomo Yenye Maana
  • Kukua Pamoja na Tengenezo la Yehova Katika Afrika Kusini
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Yehova ni Ngome Yangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Yehova Amenipa Nguvu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Kupata Upatano wa Jamii za Rangi Tofauti-tofauti Katika Afrika Kusini Yenye Matata
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 7/1 kur. 9-13

Kupokea ‘Haja za Moyo Wangu’

Kama ilivyosimuliwa na P. J. Wentzel

WAKATI meli yetu ilipotia nanga katika bandari ya New York kutoka Afrika ya Kusini, mwanamume mweusi alitulaki bandarini. Alikuwapo ili atumie gari kunipeleka mimi, mke wangu Lina, na mwanamke mzee-mzee aliyekuwa akisafiri pamoja nasi twende mahali ambapo tungelala. Tulisimama katika ujirani wa watu weusi, na yule dereva akatoka nje aangalie ni wapi angempeleka yule mwenzi mwenye kusafiri pamoja nasi. “Lakini Piet,” mwanamke huyo akaniambia, “hapa ni pa watu weusi tu!”

“Hii ni Amerika,” nikamkumbusha. “Hakuna tofauti kati ya weusi na weupe hapa; sisi sote ni sawa.” (Lakini kwa ndani mimi nilitumaini kwamba mke wangu na mimi tungepelekwa kwenye nyumba ya weupe!) Halafu yule dereva akarudi kumchukua mwenzi wetu, aliyekaribishwa kwa uchangamfu na jamaa ya weusi.

Sasa ikawa zamu yetu​—bado katika lile eneo la weusi. Mwenye nyumba na mkeye walipokaribia gari letu, mimi nilimpelekea Mungu sala ya bidii anisaidie kuondoa maoni yo yote ya ubaguzi wa rangi ambayo huenda bado yalibaki ndani yangu​—jambo nililorithi kwa wazazi wangu.

Wenye nyumba weusi waliotukaribisha katika New York walitutolea ukaribishaji mchangamfu. Walituingiza upesi katika chumba chetu, ambamo kila kitu kilikuwa safi kwa kutakata. Walipotuacha tukiwa peke yetu, kwanza tulinyamaza. Halafu Lina akaenda kitandani, akainua ncha ya shuka iliyofunika na kusema: “Piet, ebu fikiri kwamba usiku wa leo, kwa mara yangu ya kwanza maishani, itanilazimisha kulala katika kitanda cha mwanamke mweusi!” Lakini tulikuja kuwajua na kuwapenda sana wakaribishaji wetu.

Kwa sababu gani kushinda maoni mabaya ya ubaguzi wa rangi kulihitaji jitihada kubwa kwangu na wasafiri wenzangu?

Mavutano ya Pale Mwanzoni

Bonnievale, nilikozaliwa mwaka 1922, ni mji mdogo zapata kilomita 160 mashariki ya Cape Town, Afrika ya Kusini. Baba alikuwa mshiriki wa Kanisa Dutch Reformed. Lilikuwa kanisa la weupe tu. Weusi walikuwa na makanisa yao wenyewe katika mji tofauti ambako waliishi. Kwa hiyo sisi tulilelewa kukubali mtengano wa watu wa rangi mbalimbali.

Nayo maoni mabaya kuhusu watu wa rangi tofauti yanaweza kuingia sana moyoni! Tulifundishwa kwamba watu wa rangi yetu ndiyo bora. Tuliwatazama weusi kuwa watu wa kutendwa kama wanadamu lakini si wa cheo kimoja cha kijamii. Katika siku zangu za mwanzo-mwanzo, desturi ilikuwa kuwapokea kwenye mlango wa nyuma, na ikiwa tuliwapa chai, tulipaswa kuwatilia chai hiyo katika kikombe kikubwa cha pekee walichowekewa weusi tu. Tuliongozwa kuamini kwamba huenda mambo yakaja kuwa tofauti mbinguni, lakini duniani ni lazima ubaguzi ufuatwe sana.

Mara tu nilipofika umri wa miaka 17, niliuliza baba kama ningeweza kupewa kipa-imara, lakini yeye akaona kwamba mimi nilikuwa mdogo mno. Lakini, mwaka uliofuata, akaniambia kwamba wakati ulikuwa umefika wa kipa-imara. Nilichukua jambo hilo kwa uzito sana. Kwangu lilimaanisha kujitoa kwa Mungu na kufanya mapenzi yake. Na kwa kuwa mimi niliishi kwa ajili ya ulimwengu na anasa zao, kutia na uvutaji mwingi wa sigareti, nilitambua kwamba ilinipasa kufanya mabadiliko makubwa katika maisha yangu.

Kwa hiyo kila wakati wa pumziko la chakula cha mchana, nilikuwa nikitumia mwingi wa wakati wangu kwa kusoma Biblia. Kwangu huo ulikuwa ufunuo​—niliweza kuona kwamba njia yangu ya maisha na ile ya jamaa yetu ilipungukiwa sana matakwa ya Maandiko. Na ingawa mimi nilikuwa nikisoma Biblia katika lugha yangu mwenyewe, Kiafrikaama, yalikuwako mambo mengi ambayo sikuelewa. Kwa hiyo, sikusoma tu bali pia nilipelekea Mungu sala anisaidie kuielewa Biblia.

Wakati wa madarasa ya kipa-imara ulipokaribia, nilikuwa nimekwisha kusoma sehemu kubwa ya Biblia. Nikamwuliza baba ni wapi kipa-imara kimeelezwa katika Biblia ili niweze kujifunza jambo hilo.

“Hakimo ndani ya Biblia,” akajibu. “Hilo ni takwa la kanisa.” Niligutuka!

“Lakini ikiwa kipa-imara hakimo katika Neno la Mungu, nawezaje kukikubali?” Nikauliza. “Na ikiwa tunadanganywa katika jambo hili la maana sana, nawezaje kukabithi kanisa maisha yangu?”

Basi, tangu hapo nikaanza kuutafuta ukweli.

Kuutafuta Ukweli

Siku moja rafiki alinikaribisha kwenda kwenye ibada katika Kanisa la Dutch Reformed​—sikuwa nimehudhuria muda fulani. Mhudumu kule alihutubu juu ya tumaini​—“Tukikitarajia kitu tusichokiona, twakingojea kwa saburi.” (Warumi 8:24, 25) Ah, hilo ndilo jambo nililotaka kujua! Lakini taraja letu ni nini? Mimi naishi kwa ajili ya nini? Je! sasa ningepata majibu? Lakini mhubiri yule akashindwa kueleza taraja la wakati ujao. Nilipokuwa nikiketi pale, nilimwomba sana Mungu amsaidie yule mhubiri ili anisaidie mimi!

Jambo jingine lilinisumbua. Niliona kwamba watu wengi walikuwa wakisinzia. Mimi nilikuwa na hamu nyingi ya kuusikia ukweli, na ebu angalia, watu walikuwa wakilala! Niliondoka kanisani nikijisikia nimekatishwa tamaa, nami sikurudi kamwe kule.

Baadaye nilijifunza Biblia pamoja na rafiki aliyekuwa na maoni ya Kipentekoste. Yeye alisema kwamba mtu anayetaka kutumikia Mungu ni lazima abatizwe kwa kuzamishwa kabisa katika maji. Kwa hiyo nikahudhuria ibada iliyofuata ya kikundi hicho kidogo na kubatizwa mtoni. Jambo hilo lilimkasirisha baba kweli kweli. Hata alitisha kuniua kwa kuthubutu kujiunga na dhehebu! Sikuweza tena kusoma Biblia nyumbani lakini nilifanya hivyo nikiwa na kile kikundi kidogo nilichojiunga nacho. Sikuweza tena hata kula pamoja na baba yangu, na wakati wo wote nilipoonana naye, aliniambia nielekeze uso wangu kando Hakutaka kuuona!

Mambo tu yaliyofanywa na kile kikundi kidogo cha Kipentekoste yalikuwa ni kusoma Biblia, kuimba na kusali pamoja, na kusema katika lugha. Kufikia wakati huo mimi nilikuwa nimesafisha maisha yangu, kutia ndani kuacha kuvuta sigareti. Nilijaribu sana nipokee roho kama wale wengine, hata nikafunga kula kwa siku chache, lakini sikuipata. Halafu nikarudia kufikiria mambo. Nilijua kwamba walikuwako wengine mjini waliodai kuwa wanasema katika lugha, lakini wao waliishi maisha ya ukosefu wa adili. Kwa hiyo Mungu angewezaje kuwapa roho takatifu yake watu ambao maisha zao hazikupatana na mapenzi yake? Tena jambo jingine lilinishangaza. Niliamua kumwuliza kiongozi wa kikundi chetu.

“Je! roho takatifu ambayo ninyi na wengine mnapokea ndiyo roho takatifu ile ile iliyoongoza kuandikwa kwa Biblia?” nikauliza.

“Ndiyo,” akajibu.

“Basi, je, dunia itakuwa makao ya milele ya mwanadamu au itaharibiwa?”

“Dunia itaharibiwa, na Wakristo wataishi mbinguni.”

“Lakini hapo pana kosa,” nikajibu, “kwa kuwa Biblia inasema kwamba dunia inabaki milele​—hayo yakiwa ni maneno yaliyoongozwa na roho ya Mungu​—roho ile ile ambayo ninyi mnadai kuwa nayo.”​—Mhubiri 1:4.

Hapo nikajua kwamba kikundi chetu kidogo hakikuwa na ukweli. Mimi nikaendelea kuutafuta.

Siku moja yule kiongozi wa kikundi cha Kipentekoste aliniletea kitabu chenye kichwa Riches, kilichochapishwa na Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi. Mara tu nilipoanza kukisoma, niliweza kuona kwamba kilipatana na yale niliyokuwa nimejifunza katika Biblia. Hatimaye nilikuwa nimeupata ukweli! Nikaandika barua nipate vichapo zaidi. Vilikubaliwa kwa shauku nyingi na kikundi chetu kidogo, nasi tukavitumia kujifunza Biblia na kuwapa wengine ushuhuda. Muda mfupi baada ya hapo, Mashahidi wa Yehova wachache walikuja Bonnievale kwa ziara fupi, nasi tukawa na mazungumzo mazuri pamoja nao. Zaidi ya hilo, wanne katika kikundi chetu walijiunga nao kuhubiri nyumba kwa nyumba Jumapili iliyofuata.

Tunaunda Kundi Lililo Dogo

Ili tuweze kuendelea kueneza ujumbe wa tumaini, tuliagiza vitabu zaidi kutoka afisi ya tawi la Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi kule Cape Town. Walijibu kwamba ni lazima kwanza tupeleke barua ya maombi ya kuunda kundi. Kwanza tuliogopeshwa na jambo hilo, lakini tulipozidi kukazwa na uhitaji wa kupata vitabu zaidi, mwishowe tuliandika barua ya maombi nasi tukaundwa kuwa kundi jipya​—sisi wanne tu, ingawa hakuna ye yote kati yetu aliyekuwa Shahidi aliyebatizwa!

Kila mwezi, tuliripoti kiasi cha kazi ya kuhubiri tuliyokuwa tumefanya. Lakini kwa kuwa hatukuwa tumepata mazoezi, hatukufanya ziara za kurudia kwa watu walioonyesha kupendezwa. Afisi ya tawi ilituonyesha uhitaji wa kufanya hivyo mwezi baada ya mwezi. Mwishowe wawili kati yetu tulipiga moyo konde tukaenda nyumba moja ambako watu walielekea kuwa wenye kuitikia. Tulikusanya jamaa ile tukaimba wimbo mmoja tukiwa pamoja. Halafu mimi nikafungua kwa sala na kupiga moja ya sahani zenye habari za Kibiblia za hotuba za J. F. Rutherford. Wote walisikiliza kwa makini. Ndipo tukamalizia kwa wimbo mwingine na sala. Tulipokuwa tukienda nyumbani, mimi nilisema: “Haya basi, hilo lilikuwa ‘rudio’ letu la kwanza’!”

Muda huu upinzani wa baba uliendelea bila kupungua. Maarifa yangu juu ya Biblia yalikuwa kidogo sana. Hata hivyo niliyaamini sana moyoni mambo niliyoyajua. Siku moja Raheli, mmoja wa dada zangu, alikuja kututembelea. Wakati wa pumziko langu la chakula cha mchana, akaanza kutoa ubishi juu ya Utatu.

“Kwa sababu gani ninyi mnalikataa fundisho la Utatu?” akauliza. “Kanisa letu linafundisha waziwazi kwamba Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu wako sawa wote katika kuwako kwao na uwezo wao.”

“Ikiwa roho takatifu inalingana cheo na Baba na Mwana,” mimi nikajibu, “basi inaweza kunifanyia mambo yale yale ambayo Baba na Mwana wanaweza. Kwa hiyo ingekuwa ni sawa tu nikipelekea sala roho takatifu.

Raheli hakutoa elezo lo lote. Lakini baba, aliyekuwa katika chumba kile kingine, alipaaza sauti: “Raheli, wewe mwache huyu. Yeye hatakusaidia kwa njia yo yote.” Jamaa nzima ikakusanyika hapo karibu kumwunga mkono Raheli. Ndipo baba akaingia haraka, akiwa amekasirika vilivyo. Alikunja ngumi, akaileta karibu na kipaji cha kichwa changu​—lakini akaacha na kwenda zake. Mimi nilibaki nikiwa nimenyamaza sana na kutulia.

“Wewe keti hapo ukiwa kama malaika mnafiki,” baba akapiga kelele. Alinikumbusha juu ya wakati nilipokuwa nimejitolea kupigana dhidi ya Hitler lakini yeye akaninyima ruhusa, kwa kuwa umri wangu ulikuwa mdogo. “Laiti ungalienda ukauawe!” akanguruma. Nilimshukuru kwa kimya kwa sababu alinizuia nisijiandikisha jeshini.

Kituko hicho kilipomalizika, nilienda nje nikafikiri. Kabla mimi sijaanza kupendezwa na Biblia, kulikuwa na amani. Sasa kukawa na mzozo wa kijamaa. Nifanye nini? Je! nirudie kanisa na hivyo nirudishe amani ya kijamaa? Kama ningefanya hivyo, ningekuwa nikiziacha zile kweli za thamani kubwa nilizokuwa nimejifunza. Wazazi wangu ndio waliokuwa wamenileta ulimwenguni, lakini ni Mungu peke yake angeweza kunipa uzima wa milele. Nikiwa nimelalia kwa mkono mti wa kupendeza wa tende, na nikiwa nimesimama wima na imara, nikafanyia pale pale uamuzi: “Wakitaka kuniua wanaweza kufanya hivyo, lakini mimi sitarudi nyuma.”

Kuingia Utumishi wa Wakati Wote

Kwa kuwa nilikuwa mseja, kijana, na mwenye nguvu, nilianza kujisikia nikiwa na vizuizi vingi mno kazini katika kiwanda cha eneo hilo cha kutengeneza jibini. Nilifanya kazi pale siku sita kwa juma nipate mshahara kidogo lakini niliweza kutumia siku moja tu kwa juma katika kumtolea Yehova utumishi mtakatifu, yeye ambaye kutoka kwake nilitazamia uzima wa milele. Mbona niendelee kutengeneza jibini hali nilikuwa na kweli zenye thamani kubwa ambazo. zingeweza kuokoa maisha za watu? Nilitaka kuwa mtumishi wa wakati wote.

Niliandikia Sosaiti nikawaambia kwamba nilitaka kuwa “painia,” au mfanya kazi wa wakati wote. “Lakini jinsi gani?” nikauliza. Mimi nilikuwa na umri wa miaka 18 na baba hangekubali kamwe. Nilipokea jibu lililoyataja maneno haya ya kupendeza sana: “Nawe utajifurahisha kwa [Yehova], naye atakupa haja za moyo wako.” (Zaburi 37:4) Tamaa yangu ya moyoni ingeweza kutimizwaje hali baba alikuwa akipinga sana? Hata hivyo, niliyafikiria maneno hayo na kuendelea kusali.

Mwishowe nilifanya mpango. Nilimwambia baba kwamba mimi sikuona nikiwa na wakati ujao katika mji wa Bonnievale na kwamba nilitaka kuhamia Cape Town. Yeye akasema: “Najua sababu yako. Unataka kwenda ukauze vile vitabu vya Hakimu Rutherford!” Lakini alinipa ruhusa!

Katika Cape Town nilifanya kazi kwa bidii nipate pesa za kutosha kununua vitu vichache ambavyo ningehitaji ili kuanza huduma ya wakati wote. Nilipokutana na mwangalizi wa tawi, George Phillips, nilikuwa na tatizo fulani. Kwa sababu mimi nilikuwa mtu wa kutoka katika jamii ya Waafrikaana, Kiingereza changu kilikuwa kibaya sana hata nikalazimika kusema naye kwa kutumia mkalimani. Na kwenye mikutano nilielewa mambo machache sana hivi kwamba wakati mmoja kusanyiko lilipopangwa lifanyike Cape Town mimi nililikosa kwa sababu sikuwa nimelielewa tangazo!

Katika mwezi Novemba Ndugu Phillips alinijulisha kwamba kulikuwa na nafasi ya kupainia katika Kimberley, na ningeweza kuanza mwezi uliofuata. Nikaenda nyumbani kusema kwaheri kwa jamaa yetu. Nilijizuia machozi yasinilenge-lenge machoni kwa sababu nilidhani nisingeweza kuwaona tena kabla ya Har–Magedoni! Lakini sikuwaambia ningeenda kuwa painia.

Tarehe ya 1 ya mwezi Desemba, 1941, nikiwa na umri wa miaka 19, ndipo nilipoanza kazi yangu ya maisha ya painia katika Kimberley. Nikiwa kule nikawaandikia wazazi wangu barua. Mimi sikuwa na uchungu kwa baba yangu kwa jinsi alivyonitenda. Mama akajibu kwamba alifurahi kwamba mimi niliweza kutimiza tamaa ya moyo wangu. Kwa kweli, nilikuwa nimeweza ‘kujifurahisha kwa Yehova’ kwa maana yeye alikuwa amenipa ‘haja ya moyo wangu.’​—huduma ya wakati wote.

Kupokea ‘Haja Nyingine ya Moyo Wangu’

Mwaka 1942, kwenye kusanyiko langu la kwanza la kitaifa katika Johannesburg, nilionyesha wakfu wangu kwa Mungu kwa kubatizwa. Miaka miwili baadaye nilikutana na dada kijana painia, Lina Muller. Kila mmoja wetu alivutiwa na mwenzake, lakini tukakubaliana tungoje mpaka baada ya dhiki kubwa kabla ya kufikiria ndoa kwa uzito.

Shughuli ya mikutano ya watu wote ilianza mwaka wa 1945. Wakati huo nilikuwa nikitumikia Vereeniging nikiwa na mapainia wengine wawili, mmoja wao akiwa ni Frans Muller, ndugu ya Lina. Tuliposikia kwa mara ya kwanza juu ya shughuli mpya hiyo, tulikubaliana kwamba haikuwa kwa ajili yetu​—sisi hatukuwa wasemaji wenye ujuzi mbele ya watu wote. Ingawa hivyo, kwa kutiwa moyo na Sosaiti, tulichagua hotuba kadha. Ili kufanya mazoezi ya utoaji tukachagua mahali patulivu karibu na Mto Vaal, ambapo tulihutubia “wasikilizaji” wetu wa kuwaziwa tu, nao walikuwa ni ule mto! Tulijisikia tumethawabishwa wakati, mwezi mmoja baadaye, watu 37 badala ya wale wa kawaida 4 au 5 wenye kuwapo katika mkutano wa kikundi chetu walipokuja kwenye hotuba ya kwanza!

Mwaka 1947 nilipewa mgawo kwenye kazi ya mzunguko. Mwaka uliofuata Lina na mimi tukaoana. Tangu wakati huo mpendwa wangu amekuwa akifanya kazi kando yangu​—mwenzi mshikamanifu sana. Kwa hiyo nikapewa ‘haja nyingine ya moyo wangu.’

Kujifunza Masomo Yenye Maana

Mwaka 1953 Lina na mimi tulipata pendeleo kuu la kuhudhuria “Sosaiti ya Ulimwengu Mpya” Kusanyiko katika New York U.S.A.​—safari yetu ya kwanza kwenda ng’ambo. Huo ndio wakati mmoja wa ndugu zetu Wakristo alipotuchukua pale bandarini kutupeleka kwenye nyumba ya jamaa Mashahidi weusi ambao tulikaa nao. Tulikuja kuwapenda sana ndugu na dada hawa wapendwa!

Tukio hilo lilitusaidia sana baadaye nilipotumikia nikiwa mwangalizi wa wilaya kwa ajili ya Mashahidi weusi katika Afrika ya Kusini, ambako mara nyingi tulipokewa ndani ya nyumba za hali ya chini sana, nyakati nyingine tukaketi sakafuni na mara moja hata tukalala sakafuni.

Tangu mwaka 1966 mke wangu na mimi tumekuwa tukitumikia hapa Betheli katika Afrika ya Kusini. Baada ya kutumia miaka karibu 20 nikiwa mwangalizi mwenye kusafiri, mara ya kwanza niliona ni vigumu kuzoea maisha katika Betheli. Nilipenda sana kuwa nje nikihubiri, nikifundisha, na kuzoeza wengine. Lakini wakati ulipozidi kupita, nilijifunza kuthamini sana utumishi wa Betheli. Baadaye nikapendelewa kufanya kazi katika Idara ya Utumishi na kwa miaka kadha sasa nimekuwa mshiriki wa Halmashari ya Tawi.

Ninapotazama nyuma, ninakumbuka kwamba katika 1942, wakati nilipokuwa ningali Kimberley, tulisikia juu ya kifo cha msimamizi wa Sosaiti, J. F. Rutherford, ripoti moja ya habari iliyotangazwa ilieleza hivi: ‘Kwa sababu sasa kiongozi wa Mashahidi wa Yehova amekufa, tengenezo lao litanyauka life, kama mmea wa maboga katika jua lenye joto jingi.’ Badala ya kuwa hivyo, tengenezo limeendelea kusitawi kwa njia nzuri kama nini muda wa miaka iliyopita​—hata wakati wa joto lenye kuchoma la mateso! Na ni ukuzi mkubwa kama nini umetokea katika Afrika ya Kusini tangu miaka ile ya mwanzoni katika Bonnievale! Wakati huo kulikuwa na Mashahidi 1,000 katika Afrika ya Kusini; sasa kuna zaidi ya 36,000.

Ninapofikiria mambo ambayo Yehova na tengenezo lake wamenifanyia na kunifaidi muda wa miaka iliyopita, nawatia moyo kwa shauku ya ndani Mashahidi wote wenzangu vijana wautafutie nafasi utumishi wa wakati wote​—ikiwa inawezekana. Huo unaleta thawabu nyingi. Mimi najua kwamba nikiendelea kufurahia sana kufanya mapenzi ya Yehova, yeye atanipa haja za moyo wangu​—umilele wa utumishi wenye kujawa na furaha.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Tulikuja kuwajua na kuwapenda sana wenye nyumba weusi waliotukaribisha

[Blabu katika ukurasa wa 12]

“Wewe keti hapo ukiwa kama malaika mnafiki,” baba akapiga kelele, “Laiti ungalienda ukauawe!”

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Tengenezo limeendelea kusitawi kwa njia ya kupendeza kama nini muda wa miaka iliyopita​—hata wakati wa joto la mateso

[Picha katika ukurasa wa 10]

P. J. Wentzel na mkeye Lina

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki