Kupata Upatano wa Jamii za Rangi Tofauti-tofauti Katika Afrika Kusini Yenye Matata
Kama ilivyosimuliwa na Merlyn Mehl
MIMI ni mtu wa Afrika Kusini, au chotara wa Afrika Kusini, kama vile inavyopendelewa zaidi kusemwa katika nchi hii. Mimi ni profesa pia kwenye Chuo Kikuu cha Kepu (Rasi) ya Magharibi, ambacho ndicho chuo kikubwa zaidi cha weusi hasa nchini. Nina shahada ya udaktari katika elimu ya fizikia. Kwa miaka 20 iliyopita, nimekuwa pia mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo ni ipi kati ya hali hizi mbili ambayo imenisaidia kupata upatano wa jamii za rangi tofauti katika bara hili la uzozano na uhitilafiano?
Kukua Katika Afrika Kusini
Kepu Tauni, iliyo kwenye ncha ya kusini ya Afrika, imeelezwa kuwa ‘ndiyo Kepu ya kupendeza zaidi katika dunia yote.’ Mtu huguswa moyo anapozitazama nyota wakati wa usiku usio na mawingu akiwa katika Kepu Tauni. Wakati mmoja, nilipokuwa nikifanya hivyo, nakumbuka nikisema hivi kwa rafiki: “Yote haya yana faida gani? Kwa uhakika ni lazima yawe na maana fulani; na bado, huku kwetu mambo yamekosa sana maana. Watu wanawezaje kubaguana jinsi hii? Mbona haki imekosekana sana?”
Mtu akizaliwa Afrika Kusini hupata kujua habari za ubaguzi wa rangi akiwa na umri mdogo. Matatizo ya ubaguzi wa rangi huelekea kuwako kila mahali. Tangu utoto wa mapema, watu hutenganishwa na kupangwa vikundi-vikundi kulingana na rangi yao. Jamaa yetu imepangwa na sheria za Afrika Kusini kuwa katika kikundi cha “machotara.” Tukiwa watoto, tulifundishwa kwamba weupe ndio waoneaji na sisi ni miongoni mwa waonewa. Na kwa sababu watu wa rangi tofauti-tofauti hawakushirikiana hata kidogo shuleni wala katika shughuli za kijamii wakati sisi tulipokuwa tukikua, inaeleweka ni kwa nini watu wa rangi nyingine walitiliwa shuku. Kwetu sisi ilionekana ni kama weupe ndio waliopata vitu vizuri vyote—kutia na nyumba, vifaa, na shule. “Ubaguzi wa rangi,” utenganisho wa kisheria wa rangi tofauti-tofauti, likawa neno tulilolichukia zaidi katika msamiati wetu.
Kabla sijamaliza shule ya msingi, jamaa yetu ililazimishwa kuondoka nyumbani katika ujirani uliochangamana jamii za rangi tofauti-tofauti, ambako dada yangu na mimi tulizaliwa. Kwa nini? Kwa sababu ya Kifungu cha Sheria ya Maeneo ya Vikundi, kilichoruhusu eneo fulani hasa lipangiwe jamii ya rangi moja tu. Tulihamia eneo jingine, ambako tuliishi kwa miaka kadhaa mpaka mbiu ilipopigwa kusema ni “eneo la weupe.” Haya, sisi hao tukahama tena.
Kwa sababu ya matendo ya wazi ya ukosefu wa usawa, wazazi wangu na pia walimu wetu walituhimiza tujifunze kwa bidii shuleni. “Ni lazima mmwonyeshe mtu mweupe kwamba nyinyi ni bora kuliko yeye,” tukaambiwa. Jambo hili liliathiri mwelekeo wangu kuhusu shule. Ingawa nilikuwa mwenye haya nyingi, nilipenda kujifunza. Nilitumia wakati mwingi nikisoma chochote kile. Kwa sababu hiyo, nilimaliza shule nikiwa miongoni mwa wanafunzi wenye maksi za juu zaidi nchini. Kwa hiyo ikawa wazi kabisa kwamba napaswa kwenda chuo kikuu. Kwa sababu nilipata shangwe kwa kufanya sayansi na hisabati, ilikuwa rahisi kuamua kufuatia digrii katika sayansi, masomo yaliyo makubwa yakiwa ni fizikia na hisabati.
Kwa kuwa Kifungu cha Sheria ya Vyuo vya Mbali Mbali kilianza kutenda kazi katika 1960 (mwaka ule ule nilioanza chuo kikuu), nililazimika kuhudhuria chuo kikuu kilichokuwa cha jamii ya rangi yangu. Habari za wanafunzi kwenye hivi vyuo vikuu vya mbali mbali zilikuwa zikitangazwa sana. Mimi nilihitimu kila mwaka kwa kupata maksi za kiwango bora zaidi na mwishowe nikapata digrii ya Stadi wa Sayansi katika fizikia ya nyukilia, na hiyo ikavuta sana fikira za watu, hasa kwa sababu baada ya hapo niliwekwa cheoni niwe kwenye kitivo cha Chuo Kikuu cha Kepu ya Magharibi—mwanafunzi wa kwanza mchotara kuwekwa kwenye cheo cha jinsi hiyo.
Hata hivyo, mambo yalipofika hapo nilihisi nimevurugika sana akili. Sikuwa na jibu kwa swali hili muhimu la maisha: Kusudi la maisha ni nini hasa? Karibu na wakati huu ndipo nilipomtolea rafiki yangu maelezo yaliyotajwa juu.
Maswali Yangu Yajibiwa
Kufikia hapa, dini haikuwa imehusika sana maishani mwangu. Nikiwa mtoto, nilikuwa nimehudhuria Kanisa la Anglikana na nikapewa kipaimara nikiwa na miaka 16. Lakini sikujibiwa kamwe lolote la maswali yangu. Kwa hiyo nilipoendelea kukua, nilipunguza kuhudhuria kanisa na mwishowe nikaacha.
Halafu siku moja nikazuru nyumba ya mwenzangu mmoja wa chuo kikuu. Mke wake, Julia, alitumia Biblia kuonyesha kwamba kulikuwako jibu kwa matatizo ya kisiasa na ubaguzi wa rangi si yale ya Afrika Kusini tu bali pia ya ulimwengu mzima. Nilishangaa na nikawa mwenye mashaka-mashaka. Lakini nilikikubali kijitabu Basis for Belief in a New World (Msingi wa Kuamini Katika Ulimwengu Mpya), nikaenda nyumbani, nikaanza kukisoma kwa hamu ya kujua tu.
Nilikuwa bado nikisoma hata kufikia saa nane ya usiku huo! Nikawa nimepata humo hoja zenye kusababiwa vizuri kwa nini Biblia ni ya kweli, kwa nini manabii yayo yanategemeka, kwa nini aina ya binadamu imo katika matata mengi hivyo, kwa nini 1914 ni tarehe ya maana sana, na kwa nini tunaweza kutumainia mfumo mpya wenye uadilifu hapa duniani. Kwa uhakika ni lazima huu uwe ndio ukweli!
Kesho yake nikarudi nyumbani kwa mwenzangu. “Mna fasihi zaidi kama hii?” nikauliza mke wake. Nilienda zangu nikiwa na rundo la vitabu vinavyohusu mafundisho ya msingi ya Biblia, maelezo ya manabii ya Danieli na Ufunuo, hali ya zile siku sita za uumbaji, na mengine mengi sana. Jambo la maana sana ni kwamba, walionyesha kuwa katika Biblia hamna uhaki wowote wa kutetea ubaguzi wa rangi, kwa kuwa “Mungu hana upendeleo.” (Matendo 10:34) Nilizisoma fasihi zote fyu. Nikawa nimeyapata majibu kwa maswali yaliyokuwa yamenisumbua sikuzote. Baada ya mwaka mmoja hivi wa kujifunza Biblia kwa bidii sana, nilibatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Hiyo ilikuwa Novemba 21, 1967.
Wakiwa tengenezo, kwa kweli Mashahidi wa Yehova hawana ubaguzi wa rangi wala hawahusiki katika siasa. Wao wanaipa serikali moja utii wao wa ushikamanifu, Ufalme wa Mungu. Cheo cha kijamii si jambo la maana kwao. Lakini katika Afrika Kusini, sikuzote kuna matatizo ya masuala yanayohusu jamii za rangi tofauti-tofauti. Kwa sababu ya kile Kifungu cha Sheria ya Maeneo ya Vikundi, makundi yanaenda kulingana na watu walio katika maeneo yaliyomo. Kwa hiyo katika Kundi la Claremont nilikohudhuria, watu walio wengi walikuwa machotara. Weupe wachache waliohudhuria walikuwa wamisionari au wanaume wenye vyeo vya uangalizi.
Mimi ningali nakumbuka, baada ya miaka yote hii, vituko viwili vinavyoonyesha jinsi ilivyo vigumu kujiondolea kabisa mielekeo ya ubaguzi wa rangi. Kwenye makusanyiko, weupe waliokuwako walikuwa wakienda mbele ya mistari ya kafeteria, wanachukua chakula chao, na kwenda zao wakale wakiwa peke yao, hali sisi wengine tulisimama tukingoja. Hiyo ilinikoroga. Mashahidi weupe pia walikuwa na elekeo la kujulisha mtu kwa wake zao kwa njia hii: “Mpenzi, huyu ni Merlyn. Yeye anajifunza Biblia.” “Merlyn, huyu ni mke wangu, Dada Fulani wa Fulani.” Wao walinitaja mimi kwa jina langu la kwanza, lakini ilikuwa lazima mimi nitumie “Dada” au “Ndugu.” Nilihisi vibaya sana!
Lakini ndipo nikaanza kufikiri. Tatizo ni kwamba sikuzote mtu huhisi kwamba mwenzake ndiye mwenye ubaguzi wa rangi. Na hata hivyo jamii yenye kupendelea sana watu wa rangi moja kama Afrika Kusini ni lazima iwe inaathiri kila mtu anayeishi hapa. Ni kweli, Mashahidi fulani weupe walihitaji kujitahidi kutengeneza mahusiano yao na watu wa rangi tofauti. Lakini hata mimi nilihitaji kufanya hivyo. Kuhusu jambo hili Biblia inatoa ushauri huu mwema: “Usiwe na haraka ya kuonyesha uchukizo; kwa maana uchukizo hutunzwa moyoni na wapumbavu.” (Mhubiri 7:9, The New English Bible) Ndiyo, ilikuwa lazima nijitahidi kupunguza hisia yangu ya kukasirika upesi na kutochukua kwamba vikosa vidogo vilimaanisha ubaguzi wa rangi.
Inanipasa pia kutaja kwamba hali ya ujumla nchini imebadilika kidogo tangu wakati huo. Katika miaka ya zamani, ni weupe wachache tu walioruhusiwa kuhudhuria makusanyiko ya kidini ya rangi nyinginezo, na ilikuwa lazima wale mbali mbali. Sivyo ilivyo tena.
Ingawa hivyo, jambo la maana zaidi ni kwamba hili ni tengenezo la watu waliochangamana kwa uhuru, waliokuwa huru kutembeleana nyumbani kwao, na walioitana ndugu na dada na kumaanisha hivyo kihalisi! Masadikisho haya yalifuatwa kwa imara na kutegemezwa juu ya kanuni za Biblia. Kwa hiyo vituko vya ubaguzi wa rangi vinapotokea—na katika Afrika Kusini inakuwa ni kama haviepukiki kabisa—sikuzote mimi hutuliza hisia zangu kwa kufikiria mambo haya ya uhakika. Miaka inapozidi kupita, mimi hujifunza kutumia kanuni za Biblia vizuri zaidi na hivyo ninapata amani kubwa zaidi ndani yangu mwenyewe kuhusu mambo ya jamii za rangi tofauti-tofauti. Lakini ni lazima mtu ajitahidie jambo hilo!
Huduma ya Wakati Wote
Mara baada ya ubatizo wangu, nilihisi uhitaji wa kuongeza huduma yangu. Nilikuwa mseja na nilikuwa na madaraka machache, kwa hiyo siku ya Oktoba 1, 1968, nikaanza kuwa painia wa kawaida. Jambo hili lilichokora mambo, kwa kuwa lilimaanisha niache chuo kikuu na kuacha kabisa ile ambayo wengi waliiona kuwa kazi-maisha yenye kumeta-meta. Makala moja ya karatasi-habari ilikuwa na kichwa hiki kikubwa kuhusu mhamo wangu: “Mwanasayansi wa Daraja la Juu Aenda Kuieneza Biblia.” Muda si muda nikawa nikiongoza mafunzo kumi au zaidi ya Biblia kwa watu au jamaa tofauti-tofauti. Kwenye kusanyiko moja wawili wa watu hawa walibatizwa, kwenye lile lililofuata, wanne; halafu saba, na hivyo hivyo.
Siku ya Septemba 17, 1969, nilifunga ndoa na Julia, Shahidi yule aliyekuwa amenijulisha ukweli. Yeye alikuwa amejipatia talaka kwa sababu za kisheria na za Kimaandiko muda fulani kabla ya ndoa yetu. Hii ikamaanisha nimerithi jamaa ya moja kwa moja, kwa maana alikuwa na wavulana wawili, John na Leon. Tuliazimia kuendelea katika utumishi wa painia kwa muda mrefu iwezekanavyo, na hiyo ikathibitika kuwa njia njema ya kuwawekea msingi wavulana wetu na kunisaidia nifanikishe jamaa yetu ya kambo.
Lilikuwa jambo la kusisimua sana kuwa katika utumishi wa wakati wote miaka ya mapema ya 1970, kama vile maono haya yanavyoonyesha. Tukiwa katika kuhubiri nyumba kwa nyumba, tulikuta bibi mmoja jina lake Annabel. Mara hiyo akakubali kitabu Kweli Iongozayo kwenye Uzima wa Milele na Biblia. (Baadaye tukajua kwamba alilipia fasihi zile kwa pesa zote alizokuwa nazo—muuza maziwa alilazimika kurudi juma lililofuata ili apate pesa zake!) Tangu mwanzo, bibi huyo alijitayarisha vizuri kwa ajili ya funzo lake la Biblia la kila juma, ajapokuwa na mtoto mchanga asiyetulia. Alianza pia kueleza jamaa yake aliyokuwa akijifunza. Muda si muda mume wake, Billy, akaandamana naye mikutanoni. Wazazi wa Annabel walikuwa wamewapa watoto wao majina ya mfuatano wa kialfabeti. Beattie dada yake akaanza kujifunza. Nao Charlie na mke wake hawakutaka kuachwa nyuma. Daphne naye akaonyesha upendezi, na Edna na mume wake wakajiunga katika funzo. Leo hiyo jamaa nzima imekuwa ikitumikia kwa uaminifu kwa miaka mingi. Wanaume wenyewe ni wazee au watumishi wa huduma, na wengi kati ya wanawake hao wametumikia wakiwa mapainia.
Halafu kuna Stanley. Sisi tulimkuta tukiwa katika kazi ya nyumba kwa nyumba, ikiwa ndiyo ziara ya mwisho katika alasiri baridi ya Jumatatu moja. Lakini tukapokewa vizuri kama nini! Mke wake alitualika tuingie, ikawa wazi mara hiyo kwamba tulikuwa tukishughulika na mwanamume mchaji. Kwa uhakika, alikuwa ametoka sasa tu kusali akiomba msaada wa kuielewa Biblia. Zungumzo letu la kwanza lilizungukia fundisho la Utatu. Baada ya zungumzo la saa moja, alionekana kusadikishwa. Juma lililofuata, alitusalimu kwa maneno haya: “Nyinyi watu mnasema kweli. Mimi nimelisoma ‘Agano Jipya’ lote, na hakuna Utatu. Nilienda kumwona mhudumu kumuuliza kwa nini amekuwa akiniongoza vibaya. Yeye akakataa kuniona, kwa hiyo nikamrudishia zile bahasha za sadaka nilizokuwa nikikusanyia sadaka kutoka washiriki wengine wa kanisa.” Tena ajabu ni kwamba alifanya yote haya kabla hata hajapata kichapo chochote kile kutoka kwetu! Alitaka kuhudhuria mikutano, nasi tukaahidi kwenda kumchukua. Lakini Jumapili hiyo tulichelewa dakika tano kuliko tulivyokuwa tumeahidi. Tukakutana naye akiendesha baiskeli yake kwenda mkutanoni! “Nilifikiri mmenisahau,” yeye akasema. Tulijifunza mara tatu kwa juma, naye akabatizwa miezi mitatu baada ya safari yetu ya kwanza kuonana naye. Stanley ametumikia kwa miaka mingi akiwa na bidii ile ile aliyokuwa nayo hapo kwanza.
Julia na mimi tulihesabu tukaona kwamba muda wa miaka hiyo, tumependelewa kusaidia watu kama 50 wakawa Mashahidi wa Yehova.
Kurudia Kazi ya Kimwili
Baada ya miaka minne katika utumishi wa painia, pesa zetu zikakaribia kumalizika. Gharama za maisha zilikuwa zimepanda, na wavulana walizidi kuwa wakubwa. Kwa hiyo, kwa kusikitika sana na bila kutaka, tukaamua kuacha huduma ya wakati wote. Hiyo ilikuwa katika Septemba 1972. Halafu? Kidogo tu zaidi ya mwaka mmoja baadaye, siku ya Januari 1, 1974, mimi nilirudia kuwa mhadhiri kwenye chuo kikuu wakati cheo fulani kilipopatikana katika somo la fizikia. Hii ilimaanisha nirekebishe sana hali zangu na pia nijilinde nisikate tumaini. Lakini kwa kuungwa mkono sana na Julia, niliweza kuyafanya marekebisho. Likathibitika kuwa jambo lenye msaada kubaki nikiwa mtendaji sana sana katika huduma na kundi—kuendelea kikweli ‘kuutafuta kwanza ufalme.’—Mathayo 6:33.
Kwa kuwa wakufunzi wote wa chuo kikuu wanatazamiwa kufanya utafiti, suala la kurudia fizikia ya nyukilia lilitokea. Niliona ikiwa vigumu sana sana kuwazia kufanya namna hii ya utafiti uliosomewa na watu wachache sana, hali kule nje ya chuo kikuu nilitumia wakati wangu nikijaribu kufundisha watu ukweli wa Biblia. Ilionekana kuwa kazi-bure kuhusika katika utafiti usio na lengo lolote ila kutafiti mambo tu. Na, bila shaka, utafiti wa fizikia ya nyukilia ungeweza hata kuwa ni wa matumizi ya kijeshi tu, na hii ingeweza kuleta matatizo kuhusiana na kutokuwamo kwa Kikristo.—Isaya 2:2-4.
Katika Afrika Kusini chuo kikuu kama kile cha Kepu ya Magharibi kina wanafunzi wengi wanaotajwa kuwa “wasiofaidika sana.” Wao huja chuo kikuu bila matayarisho kamili kwa sababu ya kupata masomo haba na mambo mengine yanayohusu uchumi wa kijamii. Katika visa vingi wao huwa hawana ukosefu wa kuyaweza masomo—ni kwamba tu huwa hawakuipata fursa yenyewe. Kwa miaka 13 iliyopita, nimekuwa nikifanya utafiti wa kuyajua magumu ya wanafunzi hao na kupanga mbinu tofauti za kuwafunza, hiyo ikiwa ni sehemu ya kazi yangu ya chuo kikuu. Utafiti huu umeniwezesha kupata shahada ya udaktari katika elimu ya fizikia na ukafanya nipandishwe cheo kuwa profesa. Programu za utafiti wa kiushirika sasa zinaendeshwa katika United States na Israeli. Inapendeza kulinganisha magunduzi ya utafiti huu pamoja na mbinu za kufundisha za Mashahidi wa Yehova.
Nadharia moja iliyositawishwa na Profesa Reuven Feuerstein na wafanya kazi wenzake katika Israeli inaitwa Ujuzi wa Kupatanisha Njia za Kujifunza. Kiini hasa cha nadharia yenyewe ni kwamba watoto husitawisha uwezo wa kufikiri si kutokana tu na vichochezi vinavyowafikia kutoka nje ya miili yao kupitia zile hisia zao za maarifa, bali pia kutokana na mpatanishi wa kibinadamu anayewafasiria maana ya vichochezi hivyo. Jambo hili lisipofanywa, watoto hawasitawishi uwezo wao wa kufikiri kwa kadiri ambayo wangeweza.
Mashahidi wa Yehova wanatia mkazo mwingi juu ya fungu la mzazi kuwa mkufunzi wa msingi wa mtoto. Wazazi Mashahidi wanatumia saa nyingi wakichunguza misaada ya kujifunza Biblia iliyotiliwa vielezi, wakiwa pamoja na watoto wao, wakiwauliza maswali juu ya mambo wanayoona na kuwasaidia kushika akilini umaana wa hadithi za Biblia. Zaidi ya kukazia uhitaji wa funzo la Biblia la kila juma wanakazia pia kufunzwa daima, hasa katika kanuni za Biblia. (Kumbukumbu 6:6-8) Utafiti uliotajwa juu unaelekea kuonyesha kwamba kwa kufanya hivyo, kwa kweli wazazi wanakuwa wakisitawisha akili ya uelewevu ya watoto wao.
Elimu ya kuwaza na kuwazua ni nadharia nyingine inayoshikilia kwamba kufundisha si kuhamisha habari tu kutoka akili ya mkufunzi na kuzipeleka kwenye akili ya mfunzwa. Bali, kila mtu anajifanyizia fikira zake mwenyewe kwa kuwaza na kuwazua mambo aliyoona au akayasikia au yaliyompata yeye binafsi. Hiyo ndiyo sababu watu wawili wanaweza kusikiliza habari zile zile na wakate mashauri tofauti-tofauti. Ili watu wajifunze kwa matokeo mazuri, ni lazima washughulike wenyewe na habari zile.
Hilo hasa ndilo jambo linalotiwa moyo na mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Kila mmoja anatazamiwa ajitayarishe mapema kuhusu habari zitakazozungumzwa kutokana na fasihi zinazopatikana. Wakati wa mkutano wenyewe, maelezo yanachotwa kutoka kwenye wasikilizaji kuhusu habari zilizotayarishwa. Kwa njia hii watu wanatiwa moyo si kueleza tu waliyojifunza bali pia kunufaika kutokana na matayarisho ambayo wengine wamefanya.
Kuingia kwa elimu inayotegemea kompyuta kumeshangiliwa kuwa njia ya kuwezesha watu wajifunze wenyewe. Hata hivyo, kazi ya mafunzo ya Biblia ambayo Mashahidi wamefuatia kwa miaka mingi katika nyumba za watu imekuwa na matokeo bora zaidi katika jambo hilo! Mkufunzi mmoja husaidia mtu mmoja, wawili, au watatu (ni mara chache wanapokuwa wengi zaidi ya hao) ili wafikirie mambo yaliyochapishwa kuhusu habari fulani ya Biblia ambayo mwanafunzi ameipitia katika kujitayarisha. Mwanafunzi anatiwa moyo aeleze mambo anayoelewa, fungu kwa fungu, halafu mambo hayo yanazungumziwa—hilo likiwa ni funzo la Biblia la kibinafsi kweli kweli. Kwa sababu ya utumizi wa kanuni hizo timamu za kufunzia, si ajabu kwamba Mashahidi wa Yehova wanasitawi sana kama vile walivyo. Bila shaka, si lazima wao wajifunze kanuni hizi kutoka kwenye chuo kikuu. Wanajipatia kanuni zenyewe kutokana na chanzo kikuu zaidi—Biblia.—Mathayo 28:19, 20; Yohana 6:45.
Upatano Wachukua Mahali pa Msukosuko Kati ya Jamii za Rangi Tofauti-tofauti
Zaidi ya miaka ishirini imepita mbio tangu nilipopata kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. John na Leon, wana wangu wa kambo, sasa wamekua, na wote wawili wamebatizwa na wanatumikia kwa uaminifu. Katika 1976 Graeme mwana wetu alizaliwa. Ni pendeleo kumlea yeye pia katika njia ya ukweli. Jamaa yetu imebarikiwa kwa sababu Julia anaweza tena kupainia, hali mimi hufanya upainia msaidizi angalau mara tatu kwa mwaka. Sehemu zinazotuzunguka katika Afrika Kusini, kumekuwa na ongezeko la kutazamisha la msukosuko kati ya jamii za rangi tofauti-tofauti. Mtu huona msukosuko huo katika maneno yalichorwa-chorwa katika kuta za majengo na huuhisi hewani. Hata hivyo, katikati ya hali yote ile ya kuipendelea zaidi jamii ya rangi moja tu, muujiza wa ki-siku-hizi unatukia. Sheria zinazohusu kushirikiana kwa watu zilipolegezwa kidogo na Serikali, sasa Mashahidi wa Yehova wanaweza kukutana pamoja kwa uhuru wa kadiri fulani, hasa kwenye makusanyiko makubwa. Mimi nimependelewa kushiriki katika kuyapanga kitengenezo baadhi ya makusanyiko haya kwa ajili ya jamii za rangi zote. Huko sisi huona matendo ya kutobaguana kirangi, watu wakielimishwa na vile viwango adhimu vya Biblia ili wawe kama vipofu wasiotofautisha rangi! Hapa unapata watu wanaoona jinsi wengine walivyo kwa ndani, wala si rangi ya ngozi yao tu.
Leo Mashahidi wa Yehova wanajumlika kuwa ule udugu mmoja tu na wa kweli uliopo kati ya aina ya binadamu duniani pote. Karibuni, katika mfumo wake mpya wa mambo, Yehova “atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.” Nikiwa pamoja na mamilioni ya ndugu na dada zangu ulimwenguni pote, mimi nautazamia huo ulimwengu mpya wa kupendeza sana, wenye uadilifu na usio na ubaguzi wa jamii za rangi tofauti-tofauti.—Ufunuo 21:3-5.