Udugu wa Duniani Pote Ni Hakika!
MISIONARI huyo hakuwa amekuwa katika Afrika Magharibi kwa muda mrefu alipohudhuria mkusanyiko wa kidini katika jimbo fulani la ndani-ndani. Alipokuwa akikaribia familia moja ya huko, mvulana wa miaka miwili alianza kulia, bila sababu yoyote yenye kuonekana wazi.
Misionari huyo alijaribu kufariji mtoto huyo, lakini vilio vya kivulana huyo vikageuka kuwa mayowe. “Kuna nini?” misionari akamwuliza mama. Kwa aibu ya kiasi fulani mama akajibu hivi: “Nafikiri ni wewe. Anaogopa rangi yako. Hajapata kamwe kumwona mtu mweupe.”
Tangu utoto mchanga huenda tukapata kujua juu ya tofauti za kimwili zilizo kati ya jamii za watu. Maoni ya ubaguzi husitawishwa baadaye. Maoni ya watoto hufinyangwa waonapo mielekeo na mwenendo wa watu wenye umri mkubwa zaidi, kama vile wazazi wao. Shuleni wao huathiriwa zaidi na walimu, marafiki, na wanadarasa wenzao.
Kulingana na uchunguzi wa muda mrefu katika United States, watoto wafikiapo umri wa miaka 12, tayari wao huwa wamesitawisha maoni na mielekeo iliyokazika kikiki juu ya vikundi vya kikabila, vya jamii za rangi mbalimbali, na vya kidini vinavyowazunguka. Kufikia utu mzima maoni hayo huwa yamekwama kwa kina kirefu.
Mashahidi wa Yehova Ni Tofauti
Katika ulimwengu ambamo ubaguzi ni mwingi sana, Mashahidi wa Yehova hutokeza wazi kuwa tofauti sana. Wao wajulikana kimataifa kwa upatano wao wa jamii za rangi mbalimbali. Jambo hili huonwa mara nyingi na watazamaji kwenye mikusanyiko yao mikubwa ya kila mwaka.
Kwa kielelezo, gazeti la habari States-Item lilitoa habari hii juu ya mkusanyiko mkubwa mmoja wa Mashahidi katika United States ya kusini: “Hisia ya udugu ilijaa katika Ukumbi Mkuu wa Louisiana huku Mashahidi wa Yehova vijana na wazee, weusi na weupe wakitulia kuanza . . . kujifunza na kushirikiana waliyoona. . . . Ubaguzi wa rangi ya kijamii . . . si tatizo kwa mashahidi.”
Kwenye mkusanyiko mmoja wa Mashahidi, katika Afrika Kusini, mwanamke mmoja Mxhosa alisema hivi: “Inastaajabisha kwamba hapa katika Afrika Kusini watu wa jamii za rangi zote waweza kuungamana hivyo. Ni tofauti sana na jambo lile ambalo nimezoea katika makanisa.”
Kulingana na ripoti moja, wenye kuzuru kutoka Amerika ya Kaskazini na ya Kusini na pia Ulaya walipohudhuria mikusanyiko mikubwa ya Mashahidi katika Mashariki ya Mbali na Pasifiki ya Kusini, “hakukuwa na hata kidalili kimoja cha ubaguzi wa rangi kwa upande wao, wala kwa upande wa wenyeji wao.”
Hivyo, kilicho tofauti sana juu ya wale mamilioni ya Mashahidi wa Yehova duniani pote ni mwungamano wao wa kweli na upatano kati ya watu wa jamii za rangi mbalimbali. Wao wamefunganishwa pamoja na upendo wa kweli wa Kikristo. Hiyo ni sawasawa na vile Yesu alivyosema ingekuwa: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.”—Yohana 13:35.
Hivyo basi tayari Mashahidi wa Yehova wana udugu wa kweli wa kimataifa wenye kudumu! Wao huzingatia moyoni yale ambayo Yesu alisema kwenye Mathayo 23:8: “Nanyi nyote ni ndugu.” Tena iko hivyo katika wakati ule ule ambapo migawanyiko na chuki kati ya jamii za watu wa makabila mbalimbali inachana-chana ushikamano wa mataifa.—Ona pia 1 Wakorintho 1:10; 1 Yohana 3:10-12; 4:20, 21; 5:2, 3.
Jinsi Mwungamano Hufikiwa
Jambo la msingi kwa mwungamano huo ni maagizo yenye kutegemea Biblia ambayo Mashahidi wa Yehova hupokea kwenye Majumba ya Ufalme yao na kujifunza kwao Biblia kibinafsi. Wao ni kama wale Wakristo katika Thesalonike, ambao kwa habari yao mtume Paulo alisema hivi: “Mlipopata lile neno la ujumbe la Mungu mlilolisikia kwetu, mlilipokea si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu; na ndivyo lilivyo kweli kweli; litendalo kazi pia ndani yenu ninyi mnaoamini.”—1 Wathesalonike 2:13.
Hivyo, Mashahidi huamini yale ambayo Biblia husema, nao hujaribu kwa bidii ya moyo kuiga njia ya Mungu ya kufikiri. Wao huzingatia moyoni yale ambayo mtume Mkristo Petro alisema kwa kuvuviwa roho: “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.”—Matendo 10:34, 35.
Kupatana na hilo, Yesu aliagiza wafuasi wake wafanye wanafunzi wa watu “wa mataifa yote.” (Mathayo 28:19, Habari Njema kwa Watu Wote) Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova huwa watendaji wakitafuta wapendao uadilifu katika vikundi vyote vya jamii za rangi na makabila, bila kubagua. Na wakati wale wenye malezi tofauti na wa jamii za rangi mbalimbali waungamanapo kuabudu, kufanya kazi, na kukutanika pamoja kirafiki, fikira zilizokazika kikiki hushindwa. Wao hujifunza kuthaminiana, kupendana.
Ni kweli, mtu ambaye kwa muda mrefu amekuwa na maoni ya ubaguzi huenda asibadili maoni yake ghafula. Lakini awapo Shahidi, yeye huanza ‘kuuvaa utu mpya’ wa Mkristo wa kweli, naye hujitahidi kushinda maoni aliyoshikilia hapo kwanza. (Waefeso 4:22-24) Hajaribu kutetetea maoni yake ya ubaguzi kuwa ya haki akisema, ‘Hivyo ndivyo nilivyolelewa.’ Sivyo, yeye hujitahidi kufanyiza upya akili yake na ‘kuwa na upendo kwa ajili ya ushirika mzima wa ndugu.”—1 Petro 2:17, NW.
Unabii Mbalimbali wa Biblia Unaotimizwa
Linalotukia miongoni mwa Mashahidi wa Yehova leo lina umaana mkubwa. Kwa kweli, lilisemwa kwa unabii katika Biblia.
Angalia yale ambayo Isaya 2:2-4 ilitabiri yangetukia katika “sehemu ya mwisho ya zile siku,” katika hizi “siku za mwisho” za mfumo huu mwovu wa mambo. (2 Timotheo 3:1-5, 13, NW) Unabii huo wa Isaya ulisema kwamba ibada ya kweli ya Yehova ingesimamishwa imara katika kizazi hiki, na watu wa “mataifa yote watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa BWANA [Yehova, NW], nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.”
Unabii wa Isaya pia ulitaja tokeo linalofuata lisilo la kawaida, ambalo limeonekana kwa kadiri ya kimataifa miongoni mwa Mashahidi wa Yehova muda wote wa karne nzima hii: “Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”
Pia, kitabu cha Biblia cha Ufunuo, kikisema juu ya wakati wetu, kilitabiri kwamba umati mkubwa wa watu “wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha” ungekuja pamoja katika udugu wa kweli kumtumikia Mungu kwa mwungamano.—Ufunuo 7:9, 15.
Huku si kuwazia-wazia tu. Ule umati mkubwa kutoka mataifa yote, kutoka vikundi vyote vya jamii za rangi na makabila mbalimbali, tayari unafanyizwa. Udugu wa kweli wenye kudumu wa tufeni pote unajengwa sasa hivi! Ndio msingi wa jamii mpya kabisa ya tufeni pote ya watu wenye mwungamano na furaha, ambayo itachukua mahali pa jamii hii ya sasa yenye ufisadi itakayoharibiwa karibuni na Mungu. Jamii hii yenye mwungamano ‘itarithi dunia’ kama Yesu alivyosema, nao wataishi milele juu yayo chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu.—Mathayo 5:5; 6:9, 10; Zaburi 37:10, 11, 28, 29, 37, 38.
Kwa nini usijionee hilo wewe mwenyewe? Wakaribishwa kuzuru Jumba la Ufalme lolote la Mashahidi wa Yehova ujionee upatano wao kati ya watu wa jamii za rangi mbalimbali. Au wakati ule mwingine Mashahidi wakuzurupo, waalike ndani na uwaombe wakuonyeshe kutokana na Biblia ni nini ulio msingi wa upatano wao kati ya watu wa jamii za rangi mbalimbali. Waombe wakuonyeshe tumaini lao la Kibiblia la ulimwengu mpya ambapo udugu wa kweli utakuwa juu ya dunia nzima.
Mungu Mweza Yote, Yehova, hutoa uhakikisho wake kamili kwamba kusudi lake kuanzisha udugu wa ainabinadamu yote litatimizwa. Ataarifu hivi: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”—Isaya 55:11.
Twakualika uchunguze ushuhuda kutokana na unabii mbalimbali wa Biblia na kutokana na utimizo wa unabii huo. Ukifanya hivyo, utaona kwamba upatano wa watu wa jamii za rangi mbalimbali si kwamba tu wawezekana bali hauepukiki!
[Blabu katika ukurasa wa 9]
Linalotukia miongoni mwa Mashahidi wa Yehova leo lilisemwa kwa unabii katika Biblia
[Picha katika ukurasa wa 10]
Mashahidi wa Yehova hawana kifani katika kuwa na upatano wa kweli wa watu wa jamii za rangi mbalimbali miongoni mwao wenyewe