“Wapiga Mbiu ya Ufalme” Waabiri kwa Ukawaida Yale Maji Mengi ya Guyana
GUYANA.a Neno hilo la Kiamerindia humaanisha “bara la maji mengi.” Jinsi linavyofafanua ifaavyo sura ya nchi hii ambayo ni nchi pekee ya Amerika Kusini inayosema Kiingereza. Bara hilo linapitiwa-pitiwa na mito mingi pamoja na vijito vyayo, vinavyopita kama nyoka kutoka Mabara ya Juu ya Guiana kupitia msitu wa kitropiki hadi Bahari ya Atlantiki. Mito hiyo ndiyo hutegemeza uhai wa vile vijiji na yale mashamba mengi yaliyotawanyika njiani.
Mashahidi wa Yehova katika Guyana hutambua kwamba Yesu alipotabiri kwamba “habari njema ya ufalme [ingehubiriwa] katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote,” hilo lingetia ndani kuhubiri habari njema kwa watu wanaoishi katika maeneo hayo yaliyo kando ya mto. (Mathayo 24:14) Hivyo, kwa miaka mingi, vikundi vya Mashahidi, wengi wao wakiwa mapainia, wametumia mashua, makubwa kwa madogo, kuabiri maji ya Guyana ili kuwaletea watu habari njema.
Ili kusaidia na kazi hiyo, Watch Tower Society katika Guyana imeendesha, hadi sasa, vyombo vitano viitwavyo Kingdom Proclaimer I hadi Kingdom Proclaimer V. Hizo ni mashua za mbao ziitwazo balahoo zenye urefu wa meta saba, zenye sehemu ya juu iliyo wazi, na sehemu ya chini yenye umbo la herufi V, zilizojengwa na kutunzwa na familia moja ya Mashahidi. Zikiitwa kwa shauku, Proclaimers, na Mashahidi wa huko, mashua za kwanza mbili zimeacha kutumiwa baada ya kutumiwa kwa miongo mingi. Hata hivyo, mashua namba III, IV, na V, zingali zikitumiwa kwenye mito ya Pomeroon, Mahaica, na Demerara.
Kwenye Demerara
Katika Uingereza na sehemu nyinginezo za Ulaya, neno “demerara” huenda likamkumbusha mtu juu ya ile sukari-muwa ya rangi kahawia-dhahabu, itokayo sana-sana kwa mashamba makubwa yaliyo kando ya mto huo wenye matope na uliojaa mchanga. Kwenye ukingo wa magharibi, ile barabara kutoka pwani inaishia mahali ambapo mashamba ya miwa yanaishia. Mbele ya hapo, Mashahidi hutegemea vyombo vya Kingdom Proclaimers ili kupeleka ule ujumbe mtamu wa Ufalme wa Yehova kwa wale wakaaji kando ya mto huo—Wahindu, Waislamu, na walio Wakristo kwa jina.
Kampeni za kuhubiri kwenye Demerara zaweza kuwa safari za siku moja au zaweza kudumu majuma kadhaa, kutoka kituo kimoja hadi kingine, kutoka asubuhi hadi jioni. Kwenye safari za usiku kucha, mapainia hawapiki na kula tu kwenye mashua bali pia wanalala juu zazo. Usiku unapofika, Proclaimer inafungwa kwenye mkoko au kutiwa nanga kando ya gudi ikiwa moja inapatikana. Magongo mawili yenye urefu wa meta mbili na nusu yanasimamishwa kwenye omo na kwenye tezi. Kamba inanyooshwa kwa kukazwa kutoka upande moja hadi mwingine kwenye sehemu ya juu ya magongo hayo, na hema kubwa linawekwa juu yayo ili kufanyiza paa, au kifuniko. Bao za kuchukua mahali pa vitanda, na blanketi na shiti zatumikia kama godoro. Hali iweje, usingizi huja kwa urahisi baada ya siku ndefu.
“Je! mnaoga katika maji hayo yenye matope?” mapainia waliulizwa.
“Sivyo ikiwa twaweza kuepuka hilo!” ndilo jibu. “Wakati wowote tunapopita hori yenye maji safi, tunajaza vyombo vyetu na maji ya kupikia, kunywa, na ya kuogea.”
Uvumilivu wao unathawabishwa na maono mengi mazuri. Kwenye pindi moja, mtu mmoja alikuja kituoni, akasimama miguu yake ikiwa imetenganishwa, mikono ikiwa imekunjwa, akatutazama kwa kupendezwa sana. “Kingdom Proclaimer V”! Akasoma kwa sauti jina lililo kwenye omo la mashua. “Ni lazima iwe nyinyi ni Mashahidi wa Yehova. Ni nyinyi tu mnaotumia neno ‘ufalme’ katika njia hiyo. Mna Jumba la Ufalme lenu na sasa Kingdom Proclaimer [Mpiga Mbiu ya Ufalme].”
Kutoka Gileadi Hadi Pomeroon
Kazi kando ya Mto Pomeroon ni ya aina tofauti kwa kadiri fulani, kama Frederick McAlman akumbukavyo. Mwaka mmoja baada ya kuhitimu kwake kutoka Watchtower Bible School of Gilead katika 1970, alikuja Charity, kijiji cha mashambani cha mto kilicho kilometa 34 ndani kutoka ukingo wa mashariki wa Pomeroon, kulikokuwa kikundi cha wahubiri wa Ufalme watano.
“Kwa muda wa miaka mitano mirefu, tulikuwa na ‘furaha’ ya kuvuta makasia ya Proclaimer II tukienda chini na juu kwenye Pomeroon kabla ya sisi kupata kutumia, mota yenye kutumiwa nje ya chombo yenye nguvufarasi sita,” akumbuka Ndugu McAlman. “Tukipiga makafi na kupelekwa na maji, tulikuwa tukihubiri kuelekea chini ya ukingo wa mashariki mpaka tulipofika Hackney, kilometa 11 kutoka mahali mto unapoingia baharini. Hapo, tulikuwa tunapata usingizi mzuri usiku kwenye nyumba ya Dada DeCambra, mzalishi aliyetumikia eneo hilo wakati huo. Mapema asubuhi ifuatayo, tulikuwa tunaendelea kuelekea chini mahali mto unapoingia baharini kabla ya kuvuka kwenye ukingo wa magharibi. Kisha tulikuwa tunafanya kazi kuelekea Charity tena, mwendo wa [kilometa 34].”
Mota yenye nguvufarasi sita iliwatumikia vema kwa muda wa miaka kumi. Halafu, katika 1986, mahali payo palichukuliwa na aina mpya yenye nguvufarasi 15. Baada ya kutumikia kwa uaminifu kwenye Pomeroon kwa muda wa miaka 21, Ndugu McAlman aweza, akiwa na hisi ya utimizo, kutazama Jumba la Ufalme katika Charity, linalotumiwa sasa na lile kundi la Wahubiri 43, waliotoka sehemu za juu na chini za mto huo. Hudhurio la mkutano la wastani huzidi 60, na kwenye Ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo cha 1992, walikuwa na umati wa watu 190!
Kumtafuta Yule “Mtu wa Mnara wa Mlinzi”
Jumatatu ni siku ya soko katika Charity. Watu hutoka mbali kufikia Santa Rosa kwenye Moruka, ambao ni mto ufuatao kwenye Pwani ya Atlantiki. Kwa hiyo ni wakati mzuri wa kuhubiri habari njema, na Mashahidi huwa huko pamoja na magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Siku moja katika miaka ya mwanzo-mwanzo ya 1970, Monica Fitzallen kutoka Warimuri kwenye Moruka alikuja sokoni akakubali magazeti mawili kutoka Ndugu McAlman. Lakini alipofika nyumbani, aliyaweka magazeti hayo chini ya kabati lake la nguo.
“Yalibaki hapo kwa muda wa miaka miwili nisiyasome,” Monica akumbuka. “Halafu nikawa mgonjwa nikalazimika kulala kitandani kwa muda fulani. Nilipokuwa nikipona, nilianza kutafuta kila habari ambayo ingeweza kusomwa iliyokuwa nyumbani ili nijishughulishe mwenyewe. Mwishoni, niliyakumbuka yale magazeti mawili yaliyokuwa katika kabati la nguo nikaanza kuyachunguza.” Habari hiyo ilisikika kuwa kweli kwake mara hiyo.
Monica alipopona, alimwomba mume wake, Eugene, atafute kazi kwenye Pomeroon ili aweze kumtafuta yule mtu aliyempa magazeti hayo. Eugene alikubali lakini aliweza tu kupata kazi kwenye shamba kando ya eneo la Pomeroon ya muda wa juma moja, kutoka Jumatatu hadi Jumamosi alasiri.
Kufikia Jumamosi hiyo, Monika hakuwa bado amepata yule mtu aliyempa magazeti. Karibu na alasiri, alimwuliza mume wake kama kiasi cha maji kingewaruhusu wapige makafi hadi Charity ili kumtafuta yule “mtu wa Mnara wa Mlinzi.” Mara alipomaliza kusema, walisikia mtu akitembea kwenye kijia wakaona sura yenye kutabasamu ya dada mmoja aliyekuwa akija kuwatolea nakala za magazeti za karibuni. “Je! wewe ni mmoja wa wale watu wa Mnara wa Mlinzi?” akauliza Monica. Maswali mengi sana yalifuata hivi kwamba dada huyo alihitaji kurudi kwenye mashua ili kupata msaada. Msaada huo ulikuwa kutoka kwa nani? Si mwingine ila Ndugu McAlman!
Funzo la Biblia kwa barua likapangwa. Muda mfupi baadaye, Monica alipeleka barua yake ya kujiuzulu kutoka kwa Kanisa la Anglikana. Katika jibu alipata kijibarua hiki kutoka kwa padri: “Usiwasikilize Mashahidi wa Yehova. Wanaielewa Biblia kijuujuu tu. Nitakuja kuzungumzia jambo hilo na wewe.” Hadi sasa, padri huyo hajaja. Kwa muda huo, Monica alibatizwa katika 1975. Mwaka mmoja baadaye, mume wake, ambaye sasa huitwa kwa shauku na akina ndugu, Mjomba Eugene, alibatizwa pia baada ya yeye kuyachunguza Maandiko kwa uangalifu. (Matendo 17:10, 11) Ingawa wanaishi mwendo wa muda wa saa 12 kwa mtumbwi kutoka kwa kundi lililo karibu zaidi katika Charity, wao wangali wahubiri wa Ufalme wenye bidii hadi leo.
Safari za Mishonari Hadi Maeneo ya Ndani
Katika miaka ya hivi karibuni Watch Tower Society imekuwa ikidhamini safari za mishonari za kawaida hadi maeneo ya ndani sana. Kwa kutumia mashua zenye mota za kutumiwa nje ya chombo, wenye kujitolea kwa hiari wameonja msisimuko wa kuchukua habari njema kwa watu wanaoishi kwenye maeneo ya uhifadhi wa wanyama ya Kiamerindia na katika jumuiya za mbali za kukata miti na za ukulima zilizo kando ya mito ya maeneo ya ndani. Wakiwa mapainia kulingana na maana yenyewe ya neno hilo, wana pendeleo la kuleta “jina la Bwana [Yehova, NW]” lenye kuokoa uhai kwa maeneo hayo ya mbali kwa mara ya kwanza kabisa. (Warumi 10:13-15) Ndugu hao wanahitaji kuvumilia magumu mengi, nyakati nyingine wakiabiri mito hiyo hadi siku tatu nzima ili kufikia baadhi ya mahali hapo. Lakini thawabu zastahili hilo sana.
Kijana mmoja, wa dini ya Kipentekoste aliyeishi karibu na jumuiya ya kukata miti ya Kwebanna kwenye Mto Waini, alitembelewa wakati wa safari ya kwanza ya mishonari kwenye eneo hilo katika Julai 1991. Kwenye ziara ya kurudia katika Oktoba, Funzo la Biblia lilianzishwa. Kwa mara ya kwanza, aliona kutoka kwa Biblia yake mwenyewe kwamba jina la Mungu ni Yehova, kwamba Yesu si yule Mweza Yote, na kwamba fundisho la Utatu si la Kimaandiko. (Zaburi 83:18; 1 Wakorintho 11:3) Alikuwa na idili nyingi sana hivi kwamba, baada ya akina ndugu kuondoka, alikusanya pamoja baadhi ya Wapentekoste wenzake akaanza kuwaonyesha kutoka kwa Biblia zao wenyewe kweli juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo. Wengi walipokataa kukubali kweli, aliamua kwamba huo ulikuwa wakati wa kujiuzulu na kutoka katika “Babuloni Mkubwa.” (Ufunuo 18:2, 4, NW) Akina ndugu waliporudi kumwona katika Februari 1992, aliwaambia yale yaliyokuwa yametukia akaongeza hivi: “Nataka kujiunga nanyi. Nataka kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nataka kuwafundisha watu kweli!”
Maono kama hayo huwasaidia akina ndugu waendelee katika kazi hiyo ngumu. Ni lazima wale wanaoenda kwenye safari hizo za mishonari wadhabihu starehe za nyumbani, wajihatirishe na magonjwa kama vile malaria, na wavumilie hatari za maisha ya msituni. Lakini wale wanaobaki nyumbani hujidhabihu pia. Familia huwakosa wapendwa wao, nyakati nyingine kwa majuma kadhaa kwa wakati. Makundi yanalazimika kukaa bila wazee na vijana wayo wengineo kwa kuwa, katika visa vingine, ni ndugu mmoja tu anayeachwa nyuma ili kutunza mahitaji ya kundi. Hata hivyo, kuna shangwe na kitia-moyo kama nini wakati kundi linaposikia maono yao yenye kuchochea wanaporudi! Shangwe hiyo huzishinda gharama.
Wapiga mbiu ya Ufalme wanaoyaabiri yale maji mengi ya Guyana wakiwa na habari njema hufurahia ono la pekee kikweli. Pamoja na wafanyakazi wenzao kotekote ulimwenguni, wao ‘humpa Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake,’ kwa moyo mkubwa na kwa hiari.—Waebrania 13:15.
[Maelezo ya Chini]
a Iliyokuwa British Guiana, jina lilibadilishwa kuwa Guyana baada ya nchi hiyo kupata uhuru kutoka Uingereza katika 1966.
[Ramani katika ukurasa wa 24]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
HONDURAS
NIKARAGUA
KOSTA RIKA
PANAMA
VENEZUELA
KOLOMBIA
GUYANA
SURINAME
FRENCH GUIANA
BRAZILI
BOLIVIA
BAHARI YA ATLANTIKI
[Picha katika ukurasa wa 26, 27]
Kushoto: Kutoa ushahidi siku ya soko
Juu: Kuzungumza habari njema kwenye Mto Demerara
Juu kulia: Kikundi cha mishonari kikipiga makafi kurudi kambini