Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 4/1 kur. 28-31
  • Uwe Mwenye Furaha na Mwenye Utaratibu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uwe Mwenye Furaha na Mwenye Utaratibu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wenye Utaratibu na Wenye Furaha
  • Usijitendee Kikatili
  • Mbwa Aliye Hai au Simba Aliyekufa?
  • Jishughulikie kwa Njia ya Kuthawabisha
  • Shughulika na Wengine kwa Njia ya Kuthawabisha
  • Utunzaji wa Kila Mtu Mmoja Mmoja
  • Kaa Karibu na Kundi
  • Watumishi wa Mungu—Watu Waliopangwa Kitengenezo na Wenye Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Ni Nini Siri ya Kupata Furaha?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Wenye Furaha Ni Watu Wanaomtumikia “Mungu Mwenye Furaha”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
  • Tumefanywa Tengenezo Tumtumikie Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 4/1 kur. 28-31

Uwe Mwenye Furaha na Mwenye Utaratibu

KUWA wenye utaratibu hutuwezesha tufanye mambo vizuri. Kuwa wenye kupanga mambo hutusaidia tutumie wakati na nyenzo kwa njia bora iwezekanavyo. (Wagalatia 6:16; Wafilipi 3:16; 1 Timotheo 3:2) Lakini mengi zaidi yanahusika maishani kuliko kupanga mambo na kuwa wenye utaratibu. Mtunga zaburi aliyepuliziwa aliandika hivi: “Heri [wenye furaha ni, NW] watu wenye BWANA [Yehova, NW] kuwa Mungu wao.” (Zaburi 144:15) Jambo gumu ni kuwa wenye furaha na pia kuwa wenye utaratibu katika yote tunayofanya.

Wenye Utaratibu na Wenye Furaha

Yehova Mungu ndiye kielelezo kikuu zaidi cha utaratibu mzuri. Uumbaji wake wote, kutoka zile chembe moja moja hadi vile viumbe hai vilivyo vigumu kufahamika, kutoka atomi ndogo sana hadi galaksi kubwa mno, huonyesha utaratibu na usahihi. Sheria zake za ulimwengu wote mzima hutuwezesha kupanga maisha zetu kwa uhakika. Twajua kwamba jua litatokea kila asubuhi na kwamba kiangazi kitafuata kipupwe.—Mwanzo 8:22; Isaya 40:26.

Lakini Yehova si Mungu wa utaratibu pekee. Yeye ni “Mungu wa furaha” pia. (1 Timotheo 1:11, NW; 1 Wakorintho 14:33) Furaha yake huonwa katika uumbaji wake. Paka watoto wenye kuchezacheza, machweo yenye kupendeza, chakula chenye kuchapukia, muziki wenye kuchochea, kazi yenye kusisimua, na mambo mengine mengi yanayoonyesha kwamba alikusudia tufurahie uhai. Sheria zake si vizuizi vyenye kulemea bali ni ulinzi kwa ajili ya furaha yetu.

Yesu Kristo humwiga Baba yake. Yeye ndiye “aliyehimidiwa, [mwenye furaha, NW], Mwenye uweza peke yake” naye hutenda sawasawa na vile Baba yake hutenda. (1 Timotheo 6:15; Yohana 5:19) Alipofanya kazi pamoja na Baba yake katika uumbaji, alikuwa zaidi ya “stadi wa kazi” mwenye utaratibu. Alikuwa na furaha katika yale aliyofanya. Alikuwa “[aki]furahi daima mbele za [Yehova], [aki]ifurahia dunia inayokaliwa na watu; na furaha [yake] ilikuwa pamoja na wanadamu.”—Mithali 8:30, 31.

Tunataka kuonyesha fadhili, furaha, na upenzi uo huo kwa watu katika yote tufanyayo. Lakini nyakati nyingine, tunapojaribu kuwa wenye utaratibu, huenda tukasahau kwamba “kutembea kwa utaratibu . . . kwa roho [ya Mungu]” hutia ndani kutokeza matunda ya roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22-25, NW) Kwa hiyo twafanya vema kuuliza hivi, Tunaweza kuwaje wenye utaratibu na wenye furaha pia katika utendaji wetu wenyewe na pia katika kuelekeza kazi ya wengine?

Usijitendee Kikatili

Fikiria lile shauri zuri lililorekodiwa kwenye Mithali 11:17. Kwanza mwandishi aliyepuliziwa atuambia kwamba “mwenye rehema huitendea mema nafsi yake.” Kisha asema hivi kwa kutofautisha: “Aliye mkali hujisumbua mwili wake.” New International Version husema hivi: “Mtu mwenye fadhili hujifaidi mwenyewe, lakini mtu mkatili hujiletea mwenyewe dhara.”

Tungeweza kujitendeaje kikatili bila kukusudia? Njia moja ni kwa kuwa na nia njema lakini kutokuwa na utaratibu hata kidogo. Tokeo likiwa nini? Mstadi mmoja asema hivi: “Kusahau-sahau, kujaza hati kimakosa, kutoelewa agizo vya kutosha, kutorekodi habari za simu kwa usahihi—hayo ndiyo mambo madogomadogo yanayosababisha kutofaulu, buu wanaokula zile nyuzi za utaratibu na kuharibu nia zilizo njema kabisa.”—Teach Yourself Personal Efficiency.

Hilo lakubaliana na yule mwandishi mwenye kupuliziwa aliyesema hivi: “Yeye naye aliye mvivu katika kazi yake, ni ndugu yake aliye mharabu.” (Mithali 18:9) Naam, watu wasiopanga mambo, wasiofanya mambo kwa utaratibu wanaweza kusababisha msiba na kujiharibia mambo wenyewe na wengine. Kwa sababu hiyo, mara nyingi wengine huwaepuka kabisa. Kwa sababu ya uvivu wao, wanajisababisha wenyewe waepukwe kabisa.

Mbwa Aliye Hai au Simba Aliyekufa?

Lakini twaweza kujitenda kikatili kwa kujiwekea wenyewe viwango vya juu kupita kiasi. Mwandikaji juu ya utaratibu aliyenukuliwa juu asema kwamba, tunaweza kulenga shabaha kwenye “kiwango cha ukamilifu kisichoweza kutimizwa kwa ukamili.” Tokeo asema ni “kujiletea wenyewe mvunjiko wa moyo na kufadhaika.” Mtu anayetaka mambo yawe makamilifu huenda akawa mwenye kupanga mambo vizuri na mwenye utaratibu, lakini yeye hatakuwa kamwe mwenye furaha kikweli. Hatimaye yeye hupata mvunjiko wa moyo tu.

Ikiwa twaelekea kuwa watu wanaotaka mambo yawe makamilifu, twafanya vema kukumbuka kwamba, “ni afadhali mbwa aliye hai kuliko simba aliyekufa.” (Mhubiri 9:4) Huenda tusijiue wenyewe kihalisi kupitia jitihada isiyo ya kihalisi ya kutafuta ukamilifu, lakini tunaweza kujidhuru vibaya sana kupitia uchovu. Mamlaka moja yasema kwamba huo huhusisha “uchovu wa kimwili, wa kihisiamoyo, wa kiroho, wa kiakili, na wa mahusiano pamoja na wengine.” (Job Stress and Burnout) Kujichosha wenyewe kwa kujitahidi kufikia miradi isiyoweza kutimizika kwa hakika ni kujitenda kikatili na bila shaka kwatunyang’anya furaha yetu.

Jishughulikie kwa Njia ya Kuthawabisha

Kumbuka: “Mtu mwenye fadhili-upendo huishughulikia nafsi yake mwenyewe kwa njia ya kuthawabisha.” (Mithali 11:17, NW) Tunajishughulikia kwa njia ya kuthawabisha tunapoweka miradi ya kihalisi na ya kiasi, tukikumbuka kwamba yule Mungu mwenye furaha, Yehova, ajua mipaka yetu. (Zaburi 103:8-14) Tunaweza kuwa na furaha ikiwa sisi pia tunatambua mipaka hiyo na kisha ‘kujitahidi,’ ndani ya uwezo wetu, ili kutimiza wajibu wetu vizuri.—Waebrania 4:11; 2 Timotheo 2:15; 2 Petro 1:10.

Bila shaka, sikuzote kuna ile hatari ya kupita kiasi kwenda upande ule mwingine—kuwa wenye fadhili mno kwa nafsi zetu. Usisahau jibu la Yesu kwa dokezo la mtume Petro, “Uwe mwenye fadhili kwa nafsi yako, Bwana,” wakati ambapo, kwa kweli, hatua ya kuazimia ilihitajiwa. Petro alikuwa akifikiri kwa njia ya hatari sana hivi kwamba Yesu alisema: “Nenda nyuma yangu Shetani; u kikwazo kwangu; maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu.” (Mathayo 16:22, NW, 23) Kuishughulikia nafsi yako kwa njia ya kuthawabisha hakuruhusu mtazamo wa kutojali, wa kujifurahisha kupita kiasi. Hilo laweza pia kutunyang’anya furaha yote. Kiasi, wala si bidii ya kupita kiasi, ndilo jambo tunalohitaji.—Wafilipi 4:5.

Shughulika na Wengine kwa Njia ya Kuthawabisha

Waandishi na Mafarisayo wa siku ya Yesu yaelekea walifikiri kwamba wao walikuwa wenye utaratibu wa hali ya juu na wenye kupanga mambo vizuri sana. A Dictionary of the Bible husema hivi juu ya njia yao ya ibada: “Kila amri ya kibiblia ilihusisha maagizo mengi madogomadogo. Hakukuwa na ruhusio la hali zenye kubadilika; utii kamili wa sheria kwa habari zayo zote ulitakwa kwa lazima kutoka kwa kila Myahudi . . . Mambo madogomadogo ya kisheria yaliongezwa mpaka dini ikawa biashara, na maisha yakawa yenye kulemea sana. Watu walifanywa wafuate kanuni za adili bila kusababu. Dhamiri ilizuiwa; nguvu iliyo hai ya neno la Kimungu ilikatishwa na kusongwa chini ya mtungamano wa kanuni zisizo na mwisho.”

Haishangazi kwamba Yesu Kristo aliwalaumu kwa hilo. “Wao hufunga mizigo mizito,” akasema “na kuwatwika watu mabegani mwao; wasitake wenyewe kuigusa kwa kidole chao.” (Mathayo 23:4) Wazee wenye upendo huepuka kulilemea kundi kwa kanuni na maagizo mengi madogomadogo. Wao hushughulikia kundi la Mungu kwa njia ya kuthawabisha kwa kufuata kile kielelezo chenye fadhili, kinachoburudisha cha Kristo Yesu.—Mathayo 11:28-30; Wafilipi 2:1-5.

Hata wakati madaraka ya kitengenezo yanapoongezeka, wazee wenye kujali hawatasahau kamwe uhakika wa kwamba wao wanashughulika na watu—watu wapendwao na Mungu. (1 Petro 5:2, 3, 7; 1 Yohana 4:8-10) Hawatakuwa kamwe wenye kujishughulisha mno na mambo au taratibu za kitengenezo hivi kwamba wasahau daraka lao kuu la kuwa wachungaji, watunzaji, na walinzi wa kundi.—Mithali 3:3; 19:22; 21:21; Isaya 32:1, 2; Yeremia 23:3, 4.

Kwa kielelezo, kujishughulisha mno na ratiba na tarakimu kwaweza kuchukua mahali pa ufikirio kwa watu. Fikiria dereva wa basi anayefikiri kwamba wajibu wake mkuu ni kushikamana na ratiba yake kwa utaratibu hata hali iweje. Anashughulika na tamaa ya kwenda kutoka upande mmoja hadi ule mwingine wa njia aliyoratibiwa kwa wakati uliowekwa. Kwa kusikitisha, kulingana na maoni yake, maabiria humzuia. Wanaenda polepole na hawana utaratibu na sikuzote wao hufika kituo cha basi wakati tu anapokuwa akiondoka. Badala ya kukumbuka kwamba kusudi hasa la kazi yake ni kuyatumikia mahitaji ya maabiria wake, yeye huwaona kuwa kizuizi cha utaratibu na huwaepuka.

Utunzaji wa Kila Mtu Mmoja Mmoja

Dereva asiye na huruma kwa ajili ya kuwa na utaratibu hupuuza mahitaji ya watu mmoja mmoja. Walio dhaifu zaidi, wasio na utaratibu huenda wakaonwa kuwa vizuizi. Hilo likitokea, matokeo mabaya hufuata. Kwa kielelezo, katika jimbo-jiji moja la Ugiriki wa kale la Sparta, watoto waliokuwa dhaifu na waliokuwa wagonjwa-wagonjwa waliachwa wafe. Wao wasingekuwa askari-jeshi walio na nguvu, wenye utaratibu ambao wangelinda jimbo hilo lenye nguvu, na utaratibu. “Mtoto alipozaliwa,” asema mwanafalsafa Bertrand Russel, “baba alimleta mbele ya wazee wa familia yake ili achunguzwe: ikiwa alikuwa na afya, alirudishwa kwa baba ili alelewe; ikiwa sivyo, alitumbukizwa ndani ya shimo la maji lenye kina kirefu.”—History of Western Philosophy.

Ugumu na ukali, si furaha, ndio ulioenea katika jimbo hilo lililokosa huruma. (Linganisha Mhubiri 8:9.) Bila shaka wenye mamlaka wa Sparta walihisi kwamba utaratibu wao ulitetea matendo yao, lakini mwenendo wao haukuwa na huruma wala fadhili yoyote. Njia yao haikuwa njia ya Mungu. (Zaburi 41:1; Mithali 14:21) Kwa kutofautisha, waangalizi katika kundi la Kikristo hukumbuka kwamba kondoo wote wa Mungu ni wenye thamani machoni pake, nao hushughulika na kila mmoja wao kwa njia ya kuthawabisha. Hawajali wale 99 tu walio na afya bali pia wanamjali yule mmoja aliye dhaifu au anayesumbuka kihisiamoyo.—Mathayo 18:12-14; Matendo 20:28; 1 Wathesalonike 5:14, 15; 1 Petro 5:7.

Kaa Karibu na Kundi

Wazee hukaa karibu na kundi lililo chini ya utunzaji wao. Lakini huenda utafiti wa ki-siku-hizi wa njia za kibiashara, ukadokeza kwamba ili kuwa na utaratibu kamili meneja au mwangalizi hapaswi kuwa na urafiki sana na wale anaowasimamia. Mtafiti mmoja afafanua matokeo tofauti yaliyoonwa na afisa mmoja wa jeshi la wanahewa alipokuwa na ama urafiki sana ama kutokuwa na urafiki na wale waliokuwa chini yake: “Alipokuwa na mahusiano ya karibu pamoja na maafisa [wake], yaonekana walihisi usalama na hawakuhangaika sana juu ya utaratibu wa vikundi vyao. Mara alipoacha kuwa na uhusiano wa karibu akawa mwenye kujali zaidi cheo chake cha juu zaidi, makamanda waliokuwa chini yake walianza kuwa na wasiwasi kama jambo fulani lilikuwa limeharibika . . . wakayaelekeza mahangaiko yao kwenye kukaza fikira zaidi juu ya kazi yao. Likiwa tokeo, kulikuwako utaratibu zaidi wenye kutokeza katika kituo hicho cha kijeshi.”—Understanding Organizations.

Lakini, kundi la Kikristo si tengenezo la kijeshi. Wazee wa Kikristo wanaosimamia kazi ya wengine humwiga Yesu Kristo. Sikuzote alikuwa karibu na wanafunzi wake. (Mathayo 12:49, 50; Yohana 13:34, 35) Hakutumia wasiwasi wao kwa njia ya ubinafsi ili kupata utaratibu mwingi zaidi. Alijenga vifungo imara vya kutumainiana na kuaminiana kati yake na wafuasi wake. Vifungo vya karibu vyenye shauku nyororo vilitia alama wanafunzi wake. (1 Wathesalonike 2:7, 8) Ukaribu wa jinsi hiyo unapokuwako, kundi lenye furaha, linalosukumwa kikamili na upendo wa Mungu, litaitikia vema mwelekezo bila kulazimishwa na litajitahidi lenyewe katika utumishi wenye nia kwake.—Linganisha Kutoka 35:21.

Maandiko mengi hukazia sifa za Kikristo kama vile furaha na upendo kwa udugu. (Mathayo 5:3-12; 1 Wakorintho 13:1-13) Ni machache kwa kulinganishwa yanayokazia uhitaji wa utaratibu. Kwa uhakika, kuna uhitaji wa kuwa na utaratibu mzuri. Watu wa Mungu wamekuwa wenye utaratibu sikuzote. Lakini, kwa kielelezo, ebu fikiri ni mara nyingi kadiri gani waandishi wa zaburi, huwasimulia watumishi wa Mungu kuwa wenye furaha. Zaburi 119, ambayo ina mengi ya kusema juu ya sheria, makumbusho, na maagizo ya Yehova huanza hivi: “Heri [wenye furaha ni, NW] walio kamili njia zao, waendao katika sheria ya BWANA [Yehova, NW]. Heri [wenye furaha ni, NW] wazitiio shuhuda zake, wamtafutao kwa moyo wote.” (Zaburi 119:1, 2) Je! wewe waweza kukabiliana na ule ugumu wa kuwa mwenye utaratibu na mwenye furaha pia?

[Picha katika ukurasa wa 28]

Duara ya Amilari—chombo cha mapema cha kuwakilishia zile duara

[Picha katika ukurasa wa 31]

Yehova, akiwa mchungaji mwenye upendo, si Mungu wa utaratibu tu bali pia ni Mungu wa furaha

[Hisani]

Garo Nalbandian

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki