Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 10/1 kur. 10-15
  • Watumishi wa Mungu—Watu Waliopangwa Kitengenezo na Wenye Furaha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Watumishi wa Mungu—Watu Waliopangwa Kitengenezo na Wenye Furaha
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Watumishi wa Kisasa Wamepangwa Kitengenezo Pia
  • Waliopangwa Kitengenezo na Bado Wenye Furaha
  • Upendo Hutokeza Furaha
  • Furaha ya Kadiri Sasa
  • Kupata Furaha ya Kweli kunategemea Wewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Furaha ya Kweli Katika Kumtumikia Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Tumefanywa Tengenezo Tumtumikie Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Jinsi ya Kupata Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 10/1 kur. 10-15

Watumishi wa Mungu—Watu Waliopangwa Kitengenezo na Wenye Furaha

“Wenye furaha ni watu ambao Yehova ni Mungu wao!”—ZABURI 144:15, NW.

1, 2. (a) Kwa nini Yehova ana haki ya kuwekea watumishi wake viwango? (b) Ni zipi sifa mbili za Yehova ambazo hasa twapaswa kuiga?

YEHOVA ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima, Mungu mweza yote, Muumba. (Mwanzo 1:1; Zaburi 100:3) Kwa hiyo, yeye ana haki ya kuweka viwango vya tabia kwa watumishi wake, akijua yaliyo bora kwao. (Zaburi 143:8) Naye ndiye Kiolezo chao Kikuu ambaye sifa zake wao wahitaji kuiga. “Mfuateni [“Mwigeni,” NW] Mungu, kama watoto wanaopendwa,” akaandika mtume mmoja.—Waefeso 5:1.

2 Sifa moja ya Mungu tunayohitaji kuiga inahusika na mpango wa kitengenezo. Yeye “si Mungu wa machafuko.” (1 Wakorintho 14:33) Tuchunguzapo kwa uangalifu vitu ambavyo Mungu ameumba, twasukumwa kukata kauli kwamba yeye ndiye Mtu mwenye kupanga mambo kitengenezo zaidi katika ulimwengu wote mzima. Hata hivyo, sifa nyingine ya Mungu ambayo anataka watumishi wake waige ni furaha, kwa kuwa yeye ni “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11, NW) Kwa hiyo, uwezo wake wa kupanga mambo kitengenezo unasawazishwa na furaha. Sifa moja haijitokezi sana kwa hasara ya sifa nyingine.

3. Mbingu zenye nyota zaonyeshaje uwezo wa Mungu wa kupanga mambo kitengenezo?

3 Vitu vyote ambavyo Yehova amefanyiza, tokea kile kikubwa zaidi hadi kile kidogo zaidi, vyatoa uthibitisho kwamba yeye ni Mungu wa mpango wa kitengenezo. Kwa kielelezo, fikiria ulimwengu wote mzima uonekanao. Una maelfu ya mabilioni ya nyota. Lakini hizi hazijatawanyika ovyoovyo. Mwaastrofizikia George Greenstein aonelea kwamba kuna “utaratibu fulani kwa mpango wa kitengenezo wa nyota.” Zimepangwa kitengenezo katika vikundi viitwavyo galaksi, baadhi yazo zikiwa na mamia ya mabilioni ya nyota. Na inakadiriwa kwamba kuna mabilioni ya galaksi! Galaksi hizo pia zimepangwa kitengenezo, hesabu fulani yazo (kuanzia chache hadi maelfu kadhaa) zikiwekwa pamoja katika kikundi cha galaksi. Na vikundi vya galaksi vyadhaniwa kuwa vimepangwa kitengenezo katika vikundi vikubwa zaidi.—Zaburi 19:1; Isaya 40:25, 26.

4, 5. Toa vielelezo vya mpango wa kitengenezo miongoni mwa viumbe-hai vya dunia.

4 Mpango bora zaidi wa kitengenezo wa uumbaji wa Mungu waonekana kila mahali, si katika mbingu tuonazo tu bali pia katika dunia, ikiwa na mamiriadi ya viumbe-hai. Kuhusu vitu hivyo vyote, Paul Davies, profesa wa fizikia, aliandika kwamba watazamaji “hushangaa sana” kwa “mpango wa kitengenezo wenye utata na utukufu wa dunia halisi.”—Zaburi 104:24.

5 Ebu fikiria mifano michache ya “mpango wa kitengenezo wenye utata” unaopatikana katika viumbe-hai. Mpasuaji wa mfumo wa neva Joseph Evans alisema hivi kuhusu ubongo wa binadamu na uti wa mgongo: “Kuwapo kihalisi kwa mpangilio wa hali ya juu ni kwingi mno.” Kuhusu chembe-hai zilizo ndogo sana, mtaalamu wa bakteria H. J. Shaughnessy alisema hivi: “Utata na mpangilio mzuri wa vitu vidogo-vidogo umefanyizwa kwa jinsi ya ajabu sana hivi kwamba waonekana kuwa sehemu ya mfumo uliowekwa kimungu.” Na mwanabiolojia wa molekuli Michael Denton alisema hivi kuhusu kanuni zinazoongoza urithi (DNA) katika chembe: “Inafanya kazi kwa njia bora sana kiasi cha kwamba habari zote . . . zihitajikazo kupambanua kihususa ubuni wa kila aina ya viumbe vilivyopata kuishi katika dunia hii . . . zaweza kutoshea kijiko cha chai na bado kuwe na nafasi ya habari zote zilizomo katika kila kitabu kilichopata kuandikwa.”—Ona Zaburi 139:16.

6, 7. Ni mpango gani wa kitengenezo uonyeshwao miongoni mwa viumbe vya kiroho, nao waonyeshaje uthamini kwa Mfanyi wao?

6 Yehova hapangi tu kitengenezo viumbe vyake halisi bali pia amepanga kitengenezo viumbe vyake vya kiroho katika mbingu. Danieli 7:10 yatueleza kwamba malaika wapatao ‘elfu kumi mara elfu kumi walikuwa wakisimama mbele ya Yehova.’ Milioni mia moja ya viumbe vya kiroho wenye nguvu sana wakiwapo, kila mmoja akiwa na mgawo wake ufaao! Yastaajabisha sana kufikiria ustadi unaohitajika kupanga kitengenezo idadi kubwa kama hizo. Kwa kufaa, Biblia yasema hivi: “Mhimidini BWANA, enyi malaika zake, ninyi mlio hodari, mtendao neno lake, mkiisikiliza sauti ya neno lake. Mhimidini BWANA, enyi majeshi [ya kimalaika] yake yote, ninyi watumishi wake mfanyao mapenzi yake.”—Zaburi 103:20, 21; Ufunuo 5:11.

7 Kazi za Muumba zimepangwa kitengenezo kwa njia nzuri ajabu na kufanikiwa kama nini! Si ajabu kwamba viumbe vya kiroho vyenye nguvu katika kao la kimbingu vyatangaza hivi kwa njia ya ajabu na kwa unyenyekeo: “Umestahili wewe, Bwana wetu na Mungu wetu, kuupokea utukufu na heshima na uweza; kwa kuwa wewe ndiwe uliyeviumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako, navyo vikaumbwa.”—Ufunuo 4:11.

8. Ni vielelezo vipi vionyeshavyo kwamba Yehova hupanga kitengenezo watumishi wake walio duniani?

8 Yehova pia hupanga kitengenezo watumishi wake duniani. Alipoleta ile Gharika ya siku ya Noa katika 2370 K.W.K., Noa na wengine saba waliokoka Furiko hilo kama tengenezo la familia. Katika kule Kutoka kwa 1513 K.W.K., Yehova alileta mamilioni kadhaa ya watu wake kutoka utumwa katika Misri na kuwapa kanuni yenye sheria nyingi ili wapange kitengenezo mambo yao ya kawaida na ibada. Na baadaye, katika Bara Lililoahidiwa, makumi ya maelfu kati yao walipangwa kitengenezo kwa ajili ya utumishi wa kipekee katika hekalu. (1 Mambo ya Nyakati 23:4, 5) Katika karne ya kwanza, makutaniko ya Kikristo yalipangwa kitengenezo chini ya mwelekezo wa kimungu: “Naye alitoa wengine kuwa mitume; na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti; na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke.”—Waefeso 4:11, 12.

Watumishi wa Kisasa Wamepangwa Kitengenezo Pia

9, 10. Yehova amepangaje kitengenezo watu wake katika wakati wetu?

9 Yehova vilevile amepanga kitengenezo watumishi wake wa kisasa ili waweze kufanya kazi yake ya wakati wetu kwa mafanikio—kuhubiri habari njema za Ufalme wake kabla alete mwisho wa mfumo huu wa mambo wa sasa usiomcha Mungu. (Mathayo 24:14) Ebu fikiria mambo yahusikayo katika kazi hii ya duniani pote na umuhimu wa kuwa na mpango mzuri wa kitengenezo. Mamilioni ya wanaume, wanawake, na watoto wanazoezwa kufundisha wengine kweli za Biblia. Ili kusaidia mazoezi hayo, kiasi kikubwa cha Biblia na vichapo vyenye kutegemea Biblia huchapishwa. Kwani, kila toleo la Mnara wa Mlinzi sasa huchapishwa kwa kiasi kinachozidi milioni 16 katika lugha 118, na Amkeni! karibu milioni 13 katika lugha 73. Karibu matoleo yote huchapwa kwa wakati mmoja hivi kwamba karibu watumishi wote wa Yehova wanapata habari ileile kwa wakati mmoja.

10 Kwa kuongezea, makutaniko zaidi ya 73,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote yamepangwa kitengenezo yakutanike kwa ukawaida kwa ajili ya mafunzo ya Biblia. (Waebrania 10:24, 25) Pia kuna maelfu ya mikutano mikubwa—makusanyiko ya mzunguko na mikusanyiko ya wilaya—kila mwaka. Kuna ujenzi mkubwa wenye kuenea duniani pote wa Majumba ya Ufalme mapya au yaliyorekebishwa, Majumba ya Kusanyiko, makao ya Betheli, na vifaa vya kuchapisha fasihi ya Biblia. Kuna shule za mazoezi ya juu ya walimu wa Biblia, kama vile Watchtower Bible School of Gilead kwa ajili ya wamishonari na Shule ya Utumishi wa Painia, ziongozwazo katika nchi za duniani kote.

11. Kuna manufaa gani ya wakati ujao itakayotokana na kujifunza mpango mzuri wa kitengenezo?

11 Yehova amepanga kitengenezo watu wake kwa njia nzuri kama nini ili ‘watimilize huduma yao kikamili,’ wakisaidiwa na malaika! (2 Timotheo 4:5; Waebrania 1:13, 14; Ufunuo 14:6) Kwa kufundisha watumishi wake sasa katika njia za mpango mzuri wa kitengenezo, Mungu anatimiza jambo jingine. Watumishi wake wanatayarishwa vema ili kwamba waokokapo mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo, tayari watakuwa wamepangwa kitengenezo kuanza maisha katika ulimwengu mpya. Kisha, kwa njia ya kitengenezo wakiwa chini ya mwelekezo wa Yehova, wao wataanza kujenga Paradiso ya duniani pote. Wao pia watakuwa wamejitayarisha vizuri kufundisha mabilioni ya watu watakaofufuliwa kutoka kwa wafu matakwa mengi ya Mungu kwa ajili ya uhai.—Isaya 11:9; 54:13; Matendo 24:15; Ufunuo 20:12, 13.

Waliopangwa Kitengenezo na Bado Wenye Furaha

12, 13. Kwa nini twaweza kusema kwamba Yehova huwataka watu wake wawe na furaha?

12 Ingawa Yehova ni mfanyakazi wa ajabu na mpangaji-mambo kitengenezo kwa njia bora zaidi, yeye si mtu asiyejali, asiyebadilikana, afanyaye mambo bila kufikiri. Badala ya hivyo, yeye ni Mtu mchangamfu na mwenye furaha sana anayehangaikia furaha yetu. “Yeye huwajali nyinyi,” yatangaza 1 Petro 5:7, NW. Twaweza kuona utunzi wake na tamaa yake ya kutaka watumishi wake wafurahie mambo aliyowafanyizia wanadamu. Kwa kielelezo, Mungu alipomwumba mwanamume na mwanamke wa kwanza wakamilifu, aliwaweka katika paradiso ya starehe. (Mwanzo 1:26-31; 2:8, 9) Aliwapa kila kitu walichohitaji ili wafurahie zaidi. Lakini walipoteza vitu hivyo vyote kwa kuasi. Kwa sababu ya dhambi yao, tulirithi kutokamilika na kifo.—Warumi 3:23; 5:12.

13 Ingawa hatujakamilika sasa, sisi wanadamu bado twaweza kufurahia vitu alivyofanya Mungu. Kuna vitu vingi vyenye kutufurahisha—milima yenye fahari; maziwa, mito, bahari, na fuo zenye kuvutia sana; maua maridadi yenye manukato na mimea mingine ya aina nyingi sana; wingi wa vyakula vitamu, machweo mazuri ajabu tusiyochoka kuyatazama; mbingu zenye nyota ambazo sisi hutafakari wakati wa usiku; uumbaji wa namna nyingi za wanyama na watoto wao wenye michezo mingi ya kuchekesha; muziki wa kuamsha hisia; kazi ipendezayo na yenye manufaa; marafiki wazuri. Ni wazi kwamba Mtu aliyepanga vitu hivyo ni mwenye furaha anayefurahia kufanya wengine wafurahi.

14. Yehova ataka usawaziko gani kwetu tunapomwiga?

14 Hivyo, Yehova hataki kupanga mambo kitengenezo kwa njia bora zaidi tu. Yeye ataka pia watumishi wake wawe wenye furaha, jinsi alivyo mwenye furaha. Yeye hataki wapange mambo kitengenezo kishupavu kwa njia ya kuharibu furaha yao. Ni lazima watumishi wa Mungu wasawazishe stadi zao za kupanga mambo kitengenezo na furaha, kama afanyavyo yeye, kwa kuwa popote ilipo roho yake takatifu yenye nguvu sana, pana shangwe. Kwa kweli, Wagalatia 5:22 yaonyesha kwamba tunda la pili la roho takatifu ya Mungu litendalo kazi kwa watu wake ni “shangwe.”

Upendo Hutokeza Furaha

15. Kwa nini upendo ni muhimu sana kwa habari ya furaha yetu?

15 Yapendeza sana kuona kwamba Biblia yataja: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8, 16) Haisemi kwamba: “Mungu ni mpango wa kitengenezo.” Upendo ni sifa kuu ya Mungu, na ni lazima watumishi wake waiige. Hiyo ndiyo sababu tunda la kwanza la roho ya Mungu lililoorodheshwa kwenye Wagalatia 5:22 ni “upendo,” likifuatwa na “shangwe.” Upendo hutokeza shangwe. Tuigapo upendo wa Yehova tunaposhughulika na wengine, furaha hufuatia, kwa kuwa watu wenye upendo huwa wenye furaha.

16. Yesu alionyeshaje umuhimu wa upendo?

16 Umuhimu wa kuiga upendo wa kimungu wakaziwa katika mafundisho ya Yesu. Yeye alisema: “Baba alivyonifundisha ndivyo ninenavyo.” (Yohana 8:28) Ni nini hasa Yesu alifundishwa, ambalo naye, alifundisha wengine? Ilikuwa kwamba amri mbili zilizo kuu zaidi ya zote ni kumpenda Mungu na kumpenda jirani. (Mathayo 22:36-39) Yesu alionyesha upendo kama huo. Yeye alisema hivi: “Nampenda Baba,” akithibitisha maneno hayo kwa kuyafanya mapenzi ya Mungu hadi kifo. Naye alionyesha upendo wake kwa watu kwa kufa kwa ajili yao. Mtume Paulo alieleza Wakristo katika Efeso: ‘Kristo aliwapenda, tena akajitoa kwa ajili yenu.’ (Yohana 14:31; Waefeso 5:2) Kwa hiyo, Yesu aliwaeleza wafuasi wake hivi: “Amri yangu ndiyo hii, Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi.”—Yohana 15:12, 13.

17. Paulo alionyeshaje kwamba ni muhimu kuwaonyesha wengine upendo?

17 Paulo alionyesha umuhimu wa upendo huu wa kimungu kwa kusema hivi: “Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi. Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu. . . . Sasa inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo.”—1 Wakorintho 13:1-3, 13.

18. Twaweza kutarajia nini kutoka kwa Yehova kinachoongeza furaha yetu?

18 Tuigapo upendo wa Yehova, twaweza kuwa na uhakika wa upendo wake kwetu, hata tufanyapo makosa, kwa kuwa yeye ni “Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli.” (Kutoka 34:6) Tukitubu kwa moyo wote tufanyapo makosa, Mungu haweki hesabu ya makosa hayo bali kwa upendo yeye atatusamehe. (Zaburi 103:1-3) Naam, “Bwana ni mwingi wa rehema, mwenye huruma.” (Yakobo 5:11) Kujua jambo hili kwachangia furaha yetu.

Furaha ya Kadiri Sasa

19, 20. (a) Kwa nini furaha kamili haiwezekani sasa? (b) Biblia yaonyeshaje kwamba twaweza kuwa na furaha ya kadiri wakati huu?

19 Lakini je, yawezekana kuwa mwenye furaha leo, tukiishi katika siku za mwisho za ulimwengu huu wa Shetani uliojawa na uhalifu, jeuri, ukosefu wa adili, ambamo twakabiliwa na ugonjwa na kifo? Bila shaka, hatuwezi kujua sasa kadiri ya furaha itakayokuwapo katika ulimwengu mpya wa Mungu, kama litabirivyo Neno lake: “Mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini [“chachaweni,” “NW”], mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo.”—Isaya 65:17, 18.

20 Kwa sasa watumishi wa Mungu waweza tu kuwa na furaha ya kadiri kwa sababu wao wajua mapenzi yake nao wana ujuzi sahihi wa baraka nzuri za ajabu zitakazokuja karibuni katika ulimwengu wake mpya wa kiparadiso. (Yohana 17:3; Ufunuo 21:4) Hiyo ndiyo sababu Biblia yasema: “Ee Yehova wa majeshi, mwenye furaha ni mtu yule akutumainiye,” “mwenye furaha ni kila mtu amhofuye Yehova, mtu atembeaye katika njia zake,” “wenye furaha ni wenye tabia ya upole, kwa kuwa wao watairithi dunia.” (Zaburi 84:12; 128:1; Mathayo 5:5; NW) Kwa hiyo, yajapokuwapo magumu ya sasa ambayo ni lazima tuyakabili, twaweza kuwa na kadiri fulani ya furaha. Hata mambo mabaya yatupatapo, hatuhuzuniki kama wale wasiomjua Yehova ambao hawana tumaini la uhai wa milele.—1 Wathesalonike 4:13.

21. Kujitoa kwa watumishi wa Yehova kwachangiaje furaha yao?

21 Furaha huwajia pia watumishi wa Yehova kwa sababu wao hutumia wakati, nishati, na mali katika kufundisha kweli za Biblia kwa wengine, hasa watu “wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote” yanayofanywa katika ulimwengu wa Shetani. (Ezekieli 9:4) Biblia yasema: “Mwenye furaha ni mtu yeyote anayetendea mwenye upole kwa fadhili; katika siku ya msiba Yehova atamwokoa. Yehova mwenyewe atamlinda na kuuhifadhi uhai wake. Yeye atatangazwa kuwa mwenye furaha duniani.” (Zaburi 41:1, 2, NW) Kama alivyosema Yesu, “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35, NW.

22. (a) Kuhusu furaha, pambanua watumishi wa Mungu na wale wasiomtumikia. (b) Kwa sababu gani ya kipekee tutazamie kuwa wenye furaha?

22 Kwa hiyo ingawa watumishi wa Mungu hawawezi kutarajia kupata furaha kuu zaidi wakati huu wa sasa, wao waweza kupata furaha ambayo wale wasiomtumikia Mungu hawana. Yehova atangaza: “Tazama, watumishi wangu wataimba kwa furaha ya moyo, bali ninyi mtalia kwa huzuni ya moyo; mtapiga kelele kwa sababu ya uchungu wa roho zenu.” (Isaya 65:14) Pia, wale wanaomtumikia Mungu wana sababu ya pekee sana ya kuwa na furaha sasa—wao wana roho yake takatifu ambayo “Mungu amewapa wote wamtiio.” (Matendo 5:32) Na kumbuka, palipo na roho ya Mungu, pana furaha pia.—Wagalatia 5:22.

23. Tutazungumzia nini katika funzo letu lifuatalo?

23 Leo, katika tengenezo la watumishi wa Mungu, kuna fungu la maana linalotimizwa na “wazee,” wanaoongoza katika makutaniko, wakichangia furaha ya watu wa Yehova. (Tito 1:5) Hawa wanapaswa kuyaonaje madaraka yao na uhusiano wao pamoja na ndugu na dada zao wa kiroho? Makala yetu ifuatayo itazungumzia haya.

Ungejibuje?

◻ Uumbaji washuhudiaje kwamba Yehova ni mwenye kupanga mambo kitengenezo?

◻ Yehova amepangaje kitengenezo watumishi wake katika wakati uliopita na wakati huu?

◻ Yehova ataka tuwe na usawaziko upi?

◻ Upendo ni muhimu kadiri gani kwa furaha yetu?

◻ Twaweza kutazamia furaha ya aina gani katika wakati wetu?

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]

Juu: Kwa hisani ya ROE/Anglo-Australian Observatory, picha na David Malin

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki