Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 12/15 kur. 7-12
  • Tumefanywa Tengenezo Tumtumikie Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tumefanywa Tengenezo Tumtumikie Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je! Mungu Anatujali Sisi?
  • Yehova Ni Mungu wa Tengenezo
  • Namna Gani Ukristo?
  • Sababu Gani Tufanywe Tengenezo Zuri Leo?
  • Je, Mungu Ana Watu Wanaomtumikia kwa Utaratibu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Yehova Ni Mungu Mwenye Utaratibu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Tengenezo la Mungu Linaloonekana
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Kwa Nini Mungu Ana Kikundi au Tengenezo la Watu Wanaomwabudu?
    Habari Njema Kutoka kwa Mungu!
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 12/15 kur. 7-12

Tumefanywa Tengenezo Tumtumikie Yehova

“Sababu niliyokuacha wewe katika Krete ilikuwa ili wewe ufanye kila jambo kitengenezo huko.”​—TITO 1:5, The Jerusalem Bible.

1. Rais wa kwanza wa Marekani alisema nini juu ya tofauti ya maoni ya kidini?

KATIKA barua ya kibinafsi ya Oktoba 20, 1792, rais wa kwanza wa Marekani, George Washington, aliandika: “Kati ya uadui wote ambao umekuwapo kati ya wanadamu, ule ambao unasababishwa na tofauti ya maoni ya kidini unaonekana kuwa ndio wenye chuki zaidi na wenye kuhuzunisha zaidi na wapaswa kupingwa sana. Nilikuwa na matumaini kwamba mwongozo wa maarifa na uhuru, ambao umetia alama kipindi hiki, angalau ungewapatanisha Wakristo wa kila madhehebu hata kwamba tusione tena kamwe magomvi yao ya kidini yenye kufikia kadiri ya kuhatirisha amani ya ujamii.”

2. Wengi wametendaje kwa ajili ya kupita kiasi kwa dini?

2 Vivyo hivyo, leo, wengi wamehuzunishwa sana na kupita kiasi kwa dini na wamejiepusha na mashirika yote ya kidini. Wengine ni washiriki wa kanisa lakini wanasema wana ‘uhusiano wao wenyewe wa kibinafsi pamoja na Mungu.’ Basi, mambo ya hakika ni nini? Je! Mungu anashughulika na watu wakiwa binafsi peke yake? Biblia inaonyesha nini?

Je! Mungu Anatujali Sisi?

3. Kwa kutumia maandiko, ungejibuje ulizo hili, Je! Mungu anatujali sisi tukiwa watu mmoja mmoja?

3 Maandiko yanafunua kwamba Yehova anahangaikia watu wakiwa mmoja mmoja. Kwa mfano, katika habari ya uhusiano wa kibinadamu, Neno la Mungu linasema mambo kama haya: “Amdhihakiye maskini humsuta Muumba wake.” “Amwoneaye maskini humsuta Muumba wake; Bali yeye awahurumiaye wahitaji humheshimu” Yehova Mungu. (Mithali 17:5; 14:31) Kwa kweli, “Mungu aliupenda ulimwengu [wa wanadamu], hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16, 36) Zaidi ya hayo, mtume Petro alisema: “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.” (Matendo 10:34, 35) Kwa hiyo Yehova anawajali watu mmoja mmoja na anawakubali wale wanaomwogopa na wanaofanya yaliyo ya uadilifu.

4. Ni maulizo gani yanayotokezwa tupate kuyachunguza?

4 Pia Biblia inasema: “[Yehova] awajua walio wake.” (2 Timotheo 2:19) Lakini je, hiyo maana yake ni kwamba watu mmoja mmoja hapa na hapa katika matengenezo yote ya kidini yaliyo mengi ya ulimwengu wanakubaliwa na Mungu? Au, ingetazamiwa kwamba watu wa namna hiyo wangekuwa wakishirikiana pamoja, wakiwa wamefanywa tengenezo ili kumtumikia Yehova?

Yehova Ni Mungu wa Tengenezo

5. Malaika watakatifu wanatendaje kwa kukamatana na Yehova?

5 Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho yake linatupa ufahamu fulani kuhusu njia yake ya kufanya mambo. Kwa mfano, fikiria mbingu zisizoonekana. Je! hali ni zenye mchafuko huko? Hapana! Maelfu ya viumbe wa kiroho hawatendi kwa njia ya ovyo-ovyo kwa kujitegemea, bila kumtegemea Yehova. Badala yake, tunasoma hivi: “Mhimidini [Yehova], enyi malaika zake, ninyi mlio hodari, mtendao neno lake, mkiisikiliza sauti ya neno lake. Mhimidini [Yehova], enyi majeshi yake yote, ninyi watumishi wake mfanyao mapenzi yake.” (Zaburi 103:20, 21) Ni wazi kwamba malaika watakatifu wamefanywa kuwa tengenezo zuri ili wamtumikie Yehova.

6. Jamaa ya Noa ilianza ikiwa nini baada ya Gharika?

6 Lakini namna gani makao ya kibinadamu? Gharika ya siku za Noa ilikomesha matengenezo yote ya kabla ya Gharika ambayo huenda yakawa yalikuwapo duniani​—isipokuwa tengenezo moja. Noa na wale waokokaji wengine saba wa Gharika walitoka katika safina wakiwa tengenezo la kijamaa. Jambo la muhimu sana kwao lilikuwa ni kumtolea Mungu ibada ya umoja, kwa maana tunasoma: “[Noa] akamjengea [Yehova] madhabahu; akatwaa katika kila mnyama aliye safi, na katika kila ndege aliye safi, akavitoa sadaka za kuteketezwa juu ya madhabahu.” Waokokaji hao wa Gharika hawakuenda kila mmoja njia yake ya kidini, lakini wote walikuwa pamoja kwa ajili ya tukio hilo la maana ambalo upeo walo ulikuwa ni baraka, maagizo na agano lenye kutokana na Mungu. (Mwanzo 8:18–9:17) Ndiyo, baada ya Gharika, jamaa ya Noa ilianza ikiwa tengenezo lililomtumikia Yehova.

7. Kwa habari ya tengenezo, tunajifunza nini katika kitabu cha Kutoka?

7 Wazao wa Abrahamu walipendelewa sana na Yehova, na hakuna mtu anayeweza kukanusha kwa njia ya akili kwamba mwishowe walikuja kuwa tengenezo la kitaifa. Kitabu cha Kutoka peke yake kinaonyesha jinsi walivyokombolewa katika utumwa wa Misri na kufanywa tengenezo wakiwa theokrasi! Kitabu hicho kinamtambulisha Yehova kuwa Mungu wa tengenezo la kitheokrasi. Waisraeli walipotii Sheria (Torati) ya Mungu, waliweza kumwabudu wakiwa tengenezo lenye utaratibu, salama na lenye furaha. Bila kupingwa walikuwa wamefanywa kuwa tengenezo wamtumikie Yehova.a

8. Ni ushuhuda gani wa kuwa na tengenezo zuri ulioonekana kuhusiana na utumishi kwenye patakatifu pa kidunia pa Yehova?

8 Ushuhuda wa tengenezo zuri ulionyeshwa kuhusiana na utumishi katika patakatifu pa kidunia pa Yehova. Kwa mfano, kuwahusu Walawi, tunasoma: “Daudi aliwafanya tengenezo kwa migawanyo kulingana na wana wa Lawi: Gershoni, Kohathi, na Merari.” Vivyo hivyo, “migawanyo ya wana wa Haruni” ilifanywa. Kwa msaada wa Sadoki na Ahimeleki, “Daudi aliwafanya kuwa tengenezo kulingana na kazi zilizowekwa rasmi katika utumishi wao . . . Waliwafanya kuwa tengenezo kwa kura.” Juu ya nyakati za baadaye, tunasoma: “Yehoyada akaweka walinzi kwa ajili ya nyumba ya Bwana chini ya uongozi wa makuhani wa Kilawi na Walawi ambao Daudi alikuwa amewafanya kuwa tengenezo wasimamie nyumba ya Bwana ili kutoa sadaka za kuteketezwa kwa Bwana, kama ambavyo imeandikwa katika sheria ya Musa, kwa furaha na kwa kuimba, kulingana na agizo la Daudi.” (1 Mambo ya Nyakati 23:2-6; 24:1-6; 2 Mambo ya Nyakati 23:18, Revised Standard Version) Ndiyo, migawanyo ya makuhani na Walawi ilifanywa kuwa tengenezo ili kumtumikia Yehova.

Namna Gani Ukristo?

9. Kuna ushuhuda gani kwamba Yesu Kristo aliwafanya wafuasi wake wakawa tengenezo kwa ajili ya kumtolea Yehova utumishi?

9 Yesu Kristo alipokuwa duniani, hakuwaambia wale wote waliomwamini waende kila mmoja njia yake na kukaza fikira tu juu ya ‘uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu.’ Badala yake, wanafunzi walijikusanya kwa Yesu, na kati yao akachagua wanaume 12 kuwa mitume. Kuchaguliwa kwao kulifanywa baada ya usiku wa kutoa sala na kwa hiyo kwa msaada na kibali ya Yehova. (Luka 6:12-16) Huo ni ushuhuda wa tengenezo ambalo lilikuwa na tegemezo la kimungu. Zaidi ya hayo, Yesu aliwafanya wafuasi wake wawe tengenezo la kikundi cha watangazaji wa Ufalme walioagizwa vizuri. Kwa mfano, alitoa maagizo yenye kuhitajiwa kwa wanafunzi 70 aliowatuma kwa njia ya kitengenezo.​—Luka 10:1-24.

10. Maandiko yanaonyeshaje kwamba wafuasi wa kwanza wa Yesu walikuwa wamefanywa wakawa tengenezo zuri?

10 Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanaonyesha wazi kwamba wafuasi wa kwanza wa Yesu walikuwa wamefanywa vizuri kuwa tengenezo. Hawakutegemea usomaji wa kibinafsi wa Maandiko. Badala yake, makundi yalisimamishwa na kukusanyika kwa ukawaida ili kujifunza Neno la Mungu. Makundi hayo hayakuwa yakijitegemea, yenye kujisimamia, lakini yalifanya kazi pamoja katika upendo. Kwa mfano, makundi yalisalimiana kwa moyo, na vikundi vilivyofanywa tengenezo katika Makedonia ‘waliendelea kuomba pendeleo la kuwapa’ kitu “watakatifu” wenye uhitaji mahali kwingineko. (1 Wakorintho 16:19, 20; 2 Wakorintho 8:1-7, NW; Wakolosai 4:14-16) Ndiyo, makundi ya kwanza ya Kikristo yalishirikiana chini ya uongozi wa baraza linaloongoza ambalo washiriki walo walikuwa mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu.​—Matendo 15:1–16:5.

11. Kwa sababu gani tutazamie “kundi la Mungu” liwe limefanywa tengenezo zuri?

11 Mtume Paulo alisaidia kusimamisha baadhi ya makundi yaliyofanywa kuwa tengenezo zuri ambayo yalikuja kuwapo kwa sababu ya baraka za Mungu juu ya kazi ya kuhubiri. Zaidi ya hayo, Paulo alisema kwamba Yehova “si Mungu wa machafuko, bali wa amani.” Pia mtume huyo alitaja kwamba “Mungu amefanya kuwa tengenezo mwili” wa wafuasi wapakwa mafuta wa Yesu Kristo kama inavyompendeza Yeye. Kwa hiyo, tunapaswa kutazamia “kundi la Mungu” liwe limefanywa kuwa tengenezo zuri na litende kwa amani, kwa upatano.​—1 Wakorintho 14:33; 12:24, The Riverside New Testament; 1 Timotheo 3:5, NW.

12, 13. (a) Ni mambo gani ambayo yamesemwa juu ya makundi yaliyofanywa yakawa tengenezo na mitume wa Yesu? (b) Kwa kupatana na kielelezo cha karne ya kwanza, ni nani wanaoangalia mambo ya kundini kati ya Mashahidi wa Yehova?

12 Kuhusu tengenezo la wafuasi wa Yesu, mwana-historia J. L. von Mosheim aliandika: “Ikiwa . . . kuna jambo ambalo Mkristo ye yote hawezi kutilia shaka, [ni kwamba] mitume wa Yesu Kristo walitenda kwa amri na mwongozo wa kimungu, basi aina hiyo ya makanisa ya awali ambayo walipata katika kanisa la Yerusalemu, lililosimamishwa na kufanywa tengenezo na mitume wenyewe, lazima liwe lilikuwa la kimungu.”​—Institutes of Ecclesiastical History, Ancient and Modern, Buku la I, kurasa 67-8.

13 Mashahidi wa Yehova wamesadikishwa kwamba makundi ya karne ya kwanza ya wafuasi wa Yesu yalikuwa yamefanywa kuwa tengenezo kwa kulingana na mapenzi ya kimungu. Kwa kupatana na kielelezo hicho, basi, kati ya Mashahidi leo waangalizi na watumishi wa huduma wanawekwa rasmi na roho takatifu ili waangalie mambo ya kikundi.​—Matendo 20:28; Wafilipi 1:1.

14. (a) Makundi ya Kikristo ya karne ya kwanza yalisimamiwaje? (b) Kwa sababu gani mtume Paulo alimwacha Tito katika Krete?

14 Katika karne ya kwanza, mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu kwa ujumla walisimamia makundi, ijapokuwa watu fulani waliangalia maeneo fulani na wangeweza kuwapa wengine mamlaka. (Matendo 14:21-23; 15:1, 2) Kwa hiyo, mtume Paulo alimpa mgawo mwangalizi Mkristo Tito aangalie mambo fulani kwenye kisiwa cha Mediterania cha Krete. Kwa habari hiyo, Paulo alimwambia Tito hivi: “Sababu niliyokuacha wewe katika Krete ilikuwa ili wewe ufanye kila jambo kitengenezo huko na kuweka rasmi wazee katika kila mji, katika njia niliyokuambia.” (Tito 1:5, JB) Tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba maagizo yaliyotolewa katika barua aliyoandikiwa Tito yalimsaidia atimize mgawo huo ili Wakristo huko waweze kufanywa tengenezo zuri wamtumikie Yehova.

Sababu Gani Tufanywe Tengenezo Zuri Leo?

15, 16. Ni kwa sababu gani zilizotolewa hapa tunaweza kusema kwamba wale wanaokubaliwa na Yehova hawawezi kuwa na ‘uhusiano wa kibinafsi tu pamoja na Mungu’ na wawe wametawanyika-tawanyika katika mashirika ya kidini ya ulimwengu?

15 Kufikia hapa, imekwisha kuonyeshwa kwa Maandiko kwamba tengenezo zuri lilikuwa kitambulisho cha watumishi wa Yehova katika nyakati zilizopita. Kwa hiyo, hali ziko vivyo hivyo leo. Na kuna sababu nzuri sana kwa nini mashahidi wa kisasa wa Yehova wanapaswa kuwa tengenezo zuri.

16 Haiwezi kuwa kila mmoja wa wale wanaokubaliwa na Yehova ana ‘uhusiano wa kibinafsi tu na Mungu’ kisha watawanyike-tawanyike katika mashirika ya kidini ya ulimwengu. Yehova anadai ibada ya kweli na anakaribia kukomesha Babuloni Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. (Yohana 4:24; Yakobo 1:27; Ufunuo 18:1-8) Zaidi ya hayo, umoja unatakwa kwa Wakristo wa kweli. Leo hasa wanapaswa kuwa pamoja katika tengenezo moja ili wajipatanishe kabisa na shauri la mtume Paulo: “Basi ndugu, nawasihi, kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba nyote mnene mamoja; wala pasiwe kwenu faraka, bali mhitimu katika nia moja na shauri moja.”​—1 Wakorintho 1:10.

17. Maneno ya Waebrania 10:24, 25 yanaonyeshaje kwamba watumishi wa Yehova Mungu na Yesu Kristo lazima wote wawe sehemu ya tengenezo moja?

17 Zaidi ya hayo, Wakristo wa kweli hawapaswi kuacha kujikusanya pamoja katika mikutano ya ukawaida. Hasa inatakwa kuwa hivyo leo, kwa kuwa mwisho wa huu mfumo wa mambo unakaribia. (Waebrania 10:24, 25) Kwa wazi, ili kufuata shauri hilo lililoongozwa na Mungu watumishi wa kweli wa Yehova Mungu na Yesu Kristo ni lazima wote wawe sehemu ya tengenezo moja.

18. (a) Andiko la 1 Yohana 1:3 linaonyeshaje kwamba Wakristo wote waliopakwa mafuta wanapaswa kuwa pamoja katika tengenezo moja? (b) Wafuasi wa Yesu waliopakwa mafuta wameungana na nani katika huu “wakati wa mwisho,” na mambo ya hakika ni nini kuhusu ushirikiano kati ya Mashahidi wa Yehova wote?

18 Maandiko yanatoa takwa la kwamba wafuasi wapakwa mafuta wa Yesu wawe na shirika pamoja. Kwa habari hiyo, mtume Yohana aliandika: “Tuliyoona na kusikia tunayaripoti kwenu pia ili ninyi pia mwe na muungano [shirika] pamoja na sisi. Na, pia, muungano wetu uko na Baba na mwanaye Yesu Kristo.” (1 Yohana 1:3, Byington; New World Translation; Union Version) Kama kila mmoja wa wafuasi wapakwa mafuta wa Yesu angekuwa na ‘uhusiano wa kibinafsi tu na Mungu’ na wasishirikiane pamoja katika tengenezo moja, wangewezaje kuwa na muungano au shirika? Takwa hilo laweza kutimizwa tu kwa kufanywa tengenezo. Leo, wafuasi wa Yesu waliozaliwa kwa roho wameungana na “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine.” Kulingana na maelezo ya Yesu ya wenye mfano wa kondoo, twapaswa kutazamia “kondoo wengine” hao washirikiane kwa ukamili sana na wafuasi wake wapakwa mafuta ili wote pamoja wawe “kundi moja” chini yake akiwa “mchungaji mmoja.” (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Na tunaona ndivyo ilivyo kabisa kati ya watumishi wa Yehova katika huu “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Wakiwa udugu wa duniani pote, Mashahidi wa Yehova wote wamefanywa tengenezo ili wamtumikie Mungu.​—Linganisha 1 Petro 2:17.

19. Kwa sababu gani kutimiza agizo la kuhubiri kunataka ushirikiano ndani ya tengenezo moja lenye kuongozwa na roho?

19 Kutimiza agizo la kuhubiri na kufanya wanafunzi pia kunataka ushirikiano ndani ya tengenezo moja lenye umoja. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:6-8) Kama kila anayedai kuwa Mkristo angekuwa tu na ‘uhusiano wa kibinafsi na Mungu’ na angeshirikiana na kikundi cho chote tu cha kidini, agizo la kutoa ushuhuda lingetimizwaje? Ndiyo kusema wengine wangekuwa wakisema “Shibolethi” na wengine “Sibolethi”! (Waamuzi 12:4-6) Wenye kusikia ujumbe huo mbali-mbali wenye kutofautiana wangejuaje watasadiki upi? Wakristo waliopakwa mafuta ni lazima ‘wajitahidi sana kushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani,’ na kati yao kwapasa kuwe “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja; Mungu mmoja na Baba ya watu wote.” (Waefeso 4:1-6, NW) Ni lazima kuwepo ukubaliano kati ya Wakristo wote wa kweli, ujumbe wenye umoja, endapo watu watasikia yaliyo sahihi, wamwamini kikweli Mungu wa kweli na kuliitia jina la Yehova wakiwa na taraja la kuokolewa. Zaidi ya hayo, ni lazima tengenezo moja lenye kuongozwa na roho litumiwe kuhusiana na kuwatuma wahubiri hao wa “habari njema” wenye kusema ukweli.​—Warumi 10:11-15.

20. Ni tengenezo gani moja linalotimiza sasa Mathayo 24:14, na kuna ushuhuda gani kwamba Mungu anapendezwa na utendaji huo uliofanywa kuwa tengenezo zuri?

20 Halafu, pia, kwa kupatana na unabii wa Yesu kuhusu “kuwapo” kwake na “umalizio wa mfumo wa mambo,” ni lazima kuwepo tengenezo moja lililoungana lenye ‘kuhubiri habari njema hizi za ufalme katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote kabla ya mwisho kuja.’ (Mathayo 24:3, 14, NW) Leo, Mashahidi wa Yehova peke yao ndio wanaotangaza habari njema kwamba Ufalme huo umekuwa ukitenda mbinguni tangu mwaka wa 1914, Yesu Kristo akiwa Mfalme wa Ufalme huo. Kuna zaidi ya 2,650,000 ya watangazaji hao wa Ufalme waliofanywa tengenezo zuri, na hesabu yao inaongezeka haraka sana kwa sababu ya baraka za Mungu.​—Isaya 43:10-12; 60:22.

21. Kuhusu tengenezo la Yehova, tutachunguza nini halafu?

21 Katika hizi “siku za mwisho” zenye hatari, ni pendeleo kama nini kuwa kati ya umati mkubwa uliofanywa ukawa tengenezo zuri sana ili kumtumikia Yehova! (2 Timotheo 3:1) Kuna msingi mzuri sana wa Kimaandiko kwa wale wote waliojitoa kwa moyo wote kwa Mungu waendelee kutumikia kwa ushikamanifu pamoja na watu wake waliofanywa tengenezo. Na kama tutakavyoona, kuna sababu nzuri za kujenga wakati ujao ulio salama na wenye furaha pamoja na tengenezo la Yehova.

[Maelezo ya Chini]

a Tafadhali ona Mnara wa Mlinzi wa Agosti 1, 1984, kurasa 19-23.

Wewe Ungesema Nini?

◻ Malaika watakatifu wanatendaje kwa kukamatana na Yehova?

◻ Kuna ushuhuda gani kwamba kulikuwako tengenezo zuri katika Israeli wa kale?

◻ Ungeweza kuthibitishaje Kimaandiko kwamba wafuasi wa kwanza wa Yesu Kristo walikuwa wamefanywa tengenezo?

◻ Kwa sababu gani kuhubiri ujumbe wa Ufalme kunahitaji ushirikiano ndani ya tengenezo moja?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Katika siku za Daudi, migawanyo ya makuhani na Walawi ilikuwa imefanywa tengenezo ili kumtumikia Yehova

[Picha katika ukurasa wa 9]

Baraza linaloongoza lilitoa mwongozo kwa makundi ya karne ya kwanza yaliyokuwa yamefanywa yakawa tengenezo zuri

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki