Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 12/15 kur. 3-5
  • Ni Nini Siri ya Kupata Furaha?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Nini Siri ya Kupata Furaha?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je! Mungu Anaweza Kuongezea Furaha Yetu?
  • Mungu Anatufanyia Nini?
  • Wewe Unaweza Kupata Furaha
  • Kupata Furaha ya Kweli kunategemea Wewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Furaha ya Kweli Katika Kumtumikia Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Jinsi ya Kupata Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Wenye Furaha Ni Watu Wanaomtumikia “Mungu Mwenye Furaha”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 12/15 kur. 3-5

Ni Nini Siri ya Kupata Furaha?

ILI uwe mwenye furaha, ni lazima uwe tajiri, uwe na sura nzuri na ujulikane na watu wengi. Huenda wewe ukawa unafikiri hivyo ikiwa unaamini matangazo ya kibiashara, sinema na vitabu vya hadithi.

Lakini baada ya muda kupita, je! pesa na mali nyingi zinaleta furaha ya kweli na yenye kudumu? Je! ni lazima wewe uwe na ujana na uzuri wa mwili ndipo uweze kuwa na furaha? Mara nyingi watoto wenye kucheza-cheza wanaonekana kuwa wenye furaha. Lakini ni nini hasa siri ya kupata furaha?

Je! Mungu Anaweza Kuongezea Furaha Yetu?

Huenda ukaambiwa kwamba furaha inategemea kuwa na uhusiano mwema pamoja na Mungu. Hata hivyo watu wengi wanaona ni vigumu kuamini kuna Mtu Mwenye Nguvu Kupita Wote. Wao hawamwoni, hawamjui na wanafikiri ni lazima wakubali tu kwamba yeye yuko. Kwa hiyo wanashindwa kuona ni namna gani Mungu anaweza kuongezea mtu furaha.

Ni kweli kwamba hatuwezi kuona Mungu kwa macho yetu kwa sababu “Mungu ni Roho.” (Yohana 4:24) Hata hivyo, si kweli kwamba kuna vitu vingi tunavyokubali kwamba viko ingawa hatuwezi kuviona? Tunafurahia urafiki lakini hatuyaoni yale maoni ya urafiki ambayo sisi na rafiki zetu tunajisikia tukiwa nayo. Sisi tunafikiri, lakini je! kuna mtu ye yote aliyepata kuona mawazo? Sisi tuko hai, lakini je! tunaweza kuiona ile kani (nguvu) ya uhai?

Kila kitu kilichopo duniani ambacho bado hakijaharibiwa na mwanadamu kina utaratibu, uzuri wa kupendeza na kinatenda kazi kwa njia nzuri. Kwa hiyo bila shaka kuna mtu ambaye amefikiri kwa makini akatunga maumbo ya vitu, mtu fulani mwenye ustadi wa kutengeneza maumbo na mwenye kujua kutayarisha vitu kwa njia ya kuvuta macho​—ndiyo, mtu fulani anayejua ni nini kitakachotufurahisha. Mwandikaji wa nyakati za kale alitoa maoni yenye kuvuta sana fikira kwa kusema kwamba sifa zisizoonekana za Mungu zinafahamiwa kutokana na vitu ambavyo Yeye amefanya. Je! picha iliyochorwa kwa rangi yenye kupendeza au sanaa ya kuchongwa haifunui mambo mengi yenye kuonyesha stadi aliyeifanyiza ni mtu wa namna gani? Ni hali moja na Mungu. Inawezekana ‘kumwona’ yeye katika uumbaji na katika kila jambo analotufanyia.​—Warumi 1:20.

Mungu Anatufanyia Nini?

Mungu anaweza kutusaidia tuwe wenye furaha, hata kama tunaona nguvu zake, hekima na upendo wake kwa kiasi kidogo tu katika kazi zake za kuumba. Yeye yuko tofauti na watawala wengi wa kilimwengu kwa maana hajifanyi mtu baridi-baridi kama wao kwa kujitenga na watu anaowatawala. Kwa sababu ya upendo, Yehova Mungu anawapa viumbe wake mafunzo mengi yanayoweza kuwasaidia waishi maisha yenye furaha. Kwa kweli, Biblia imejaa “makumbusha” ya Mungu yanayoongezea furaha.​—Zaburi 25:8-10.

Akitaja sheria fulani-fulani zinazotujulisha maoni ya Mungu juu ya matendo mbalimbali, Yesu Kristo alisema: “Usiue, Usizini, Usiibe, Usishuhudie uongo, Waheshimu baba yako na mama yako, na, Mpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mathayo 19:18, 19) Wewe unafikiri ulimwengu ungekuwa namna gani kama mafunzo hayo yangefuatwa? Kwa uhakika, kama kusingekuwa na mwuaji, mzinzi, mwivi na mtu wa namna nyingine kama hizo, wanadamu wangekuwa wenye furaha nyingi zaidi sana.

Maandiko yanasema: “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!” (Zaburi 144:15, NW) Hiyo ni kweli kama nini! Watu wengi wamefuata mashauri ya Mungu, na kufanya hivyo kumewapa utulivu na tumaini hakika ambalo ni la lazima ili mtu apate furaha ya kweli. (Wafilipi 4:6, 7) Acheni tuone wachache kati yao wanasema nini.

Ni jambo gani lingeweza kufurahisha mtu mwenye kukaa eneo fulani bila ruhusa ya kisheria, mwenye mazoea asiyoacha ya kutumia dawa za kulevya? Mtu wa namna hiyo alikuwa amechagua kuishi maisha ya ufisadi, kunywa sana, kupendezwa na sherehe zinazopendwa na wengi na kupigana. Bila shaka aliweza kuona kwamba jamii ya watu aliowachukia haikugeuzwa na mambo aliyoyafanya. Kulingana na maoni yake, jambo la pekee lililobaki ni kujifurahisha mwenyewe na kutenda atakavyo. Lakini wazazi wa msichana aliyemwoa wakamwonyesha njia ya kuifikia jamii mpya ya watu ambayo sasa inaendelea kusitawi. Yeye anasema: “Nilipokwisha kuoa, naweza kusema ni kama nililazimika kuona kwamba maisha niliyoishi kufikia wakati huo yangeweza kuniletea msiba tu. Sasa mimi nina utambuzi wenye kina kirefu wa kujua kwamba kufuata mauidha ya Biblia kunaweza kuleta mabadiliko makubwa yenye faida katika maisha ya mtu. Nikiwa pamoja na mke wangu na watoto wetu wawili, mimi natumikia Mungu nikiwa shahidi aliyebatizwa wa Yehova.” Mtu huyo amepata furaha ya kweli ya kuwa Mkristo.

Tafadhali fikiria kisa kingine. Lakini kwanza ujiulize hivi: Mimi ningekuwa na furaha ya kiasi gani kama juzi tu ndipo ningekuwa nimepasuliwa kwa sababu ya ugonjwa wa kansa, na bado niwe nikiendelea kutibiwa kwa kuchomwa kwa miale ya umeme na labda nilazimike kupasuliwa mara ya pili? Mwanamke fulani mwenye kuumizwa na ugonjwa huo alikuwa wakati mmoja amejulikana katika ujirani wote kuwa malaya. Ilimchukua muda mrefu kabla hajaweza kuyafuata kwa matendo mashauri yote ya Kimaandiko aliyopokea. Lakini kumtegemea Mungu kumemwezesha afanye mabadiliko makubwa maishani mwake. Katika kijiji cha kwao kabisa katika nchi ya Netherlands, ambako kila mtu anaijua sifa mbaya aliyokuwa nayo, yeye sasa anaenda nyumba kwa nyumba kuzitangaza “habari njema” na kusaidia wengine wapate furaha ya kweli. Ingawa mwanamke huyo ana matatizo mazito ya afya, yeye anasema: “Mimi nimeweka tumaini langu lote katika Yehova Mungu, naye atanisaidia.” Yeye pia amekwisha kupata furaha ya kweli.

Maono ya mwanamke mmoja mwenye umri mkubwa katika mji wa Amsterdam yanahakikisha kwamba mtu hapotezi furaha ya kweli hata akipatwa na mambo mengi ya kutaka kumrudisha nyuma katika huu ulimwengu usio na furaha. Mwanamke huyo alikuwa amekuwa katika ndoa yenye furaha muda wa miaka 57, na bado miezi kadha baada ya kuwa mjane yeye aliweza kusema hivi: “Mimi nina furaha ya kutosha, ninajisikia nikiwa salama katika nyumba yangu wala siogopi.” Ni nini siri ya kupata furaha aliyo nayo? Yeye anasema: “Ukitii sheria za Mungu, basi hapo unakuwa mwenye furaha.”

Wewe Unaweza Kupata Furaha

Kwa hiyo ingeelekea kuwa kwamba utulivu na furaha ya kindani haitegemei sana hali za mtu kama afya, utajiri, heshima anayopewa, na mambo mengine kama hayo. Furaha yenye kudumu inategemea dhamiri njema, hali ya mtu kujiheshimu mwenyewe, kuwa na rafiki za kweli​—na, zaidi ya yote, kuwa na urafiki pamoja na Mungu. Jaribu ‘kumwona’ yeye kwa kutazama uumbaji wake ukiwa na hali nzuri zaidi ya kufahamu na hasa kwa kufanya uchunguzi wa Biblia. Huenda wewe ukapata furaha nyingi ajabu kwa sababu ya kuthamini mambo unayosoma katika Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho yake.

Lakini je! watu wanaokuwa Mashahidi wa Yehova ni wenye furaha kabisa sikuzote’? Tukisema mambo kwa unyofu wa moyo, tutasema Hapana. Kama makala inayofuata inavyoonyesha, wanadamu wote wasio wakamilifu wana matatizo na wanahitaji msaada katika kupambana nayo. Hata hivyo Neno la Mungu, Biblia, linasaidia Wakristo wenye moyo mweupe waendelee kutembea katika kipito cha furaha isiyo na mwisho.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki