Padri Akubali Mashahidi Wana Mema-Adili
Na mleta-habari za Amkeni! katika Australia
KATIKA 1991 Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la Condobolin katika New South Wales, Australia, liliharibiwa na moto. Majuma machache baadaye, padri mwenyeji mmoja aliye Mwanglikana alitaja masikitiko yake katika barua yake ya eneo la kanisa “kwa sababu ya hasara ya mahali hapo pa ibada.” Barua yake iliendelea kusema:
“Ingawa kuna tofauti za wazi kati ya mazoea yetu na yao, kwa miaka mingi nimejawa na sifa kwa pande zile za zoea la imani yao niaminizo kuwa ni njema zenyewe.” Zilikuwa nini baadhi ya pande chanya hizi?
Kwanza: “Wao huhangaikia sana fundisho la imani yao. Wao hukutana pamoja pindi mbili au tatu kwa juma kwa kusudi hili.” Hii ni kweli—Mashahidi wa Yehova ni dini ya kusoma, kufundisha, na kuhubiri. Wao huwa na mikutano mitatu kila juma.
Jambo la pili la padri lilikuwa: “Wao . . . hufanya ziara za kueneza evanjeli kwa ukawaida kwenye nyumba za watu. . . . Wao hupenda tujue kwamba dhehebu lililo la tatu kwa ukubwa katika Australia ni ile jamii ya watu wasemao Hatutaki Dini (watu 3,841,000). Hao MY hawaridhiki kujiwekea imani peke yao bali hutaka kuishiriki pamoja na watu wengine.” Mashahidi wa Yehova wajua kwamba ni lazima waitikie Mathayo 24:14 na Marko 13:10 kwa kuihubiri habari njema.
Jambo la tatu: “Wao hawaonekani kuwa wenye kuchangisha fedha katika jumuiya kwa Vibanda vya Barabarani na jitihada nyingine za kuchangisha fedha. Fedha zao hutoka ndani ya jumuiya [yao].” Biblia husema, ‘mmepokea bure, toeni bure’ na, ‘kuna furaha nyingi zaidi katika kutoa kuliko katika kupokea.’ Hivyo, wao hawakusanyi sadaka. Masanduku ya michango hupatikana kwenye majumba yao yakiwa yamewekwa kwa busara.—Mathayo 10:8; Matendo 20:35, NW.
Ni upande gani wa sifa alioutaja mwisho? “Wao hujenga mahali pao pa ibada kwa kiasi cha chini zaidi cha wakati na fedha. . . . Huenda wewe ukapenda kunyoosha miguu uteremke Gum Bend Lake Road . . . uwaone hao MY wenyeji . . . wakifanya kazi ya kujenga Jumba la Ufalme jipya. Wao wakadiria kwamba kazi hiyo itawachukua siku tatu.” Halafu akawapa ushauri gani watu wa eneo lake la kanisa?
“Napendekeza kwamba nyinyi mrudie kuyasoma mambo manne ambayo nimedokeza juu na muulize yaweza kuwasaidiaje ili mfikirie kuizoea imani yenu kwa njia inayoonekana. . . . Ningedokeza kwamba kwa kuhusiana na yale mambo manne yaliyotajwa, hao MY wangefanya maeneo ya wastani ya makanisa ya Kianglikana na maeneo ya makanisa mengine ya Kikristo yaonekane yamekufa kwa kulinganishwa nao.”
Ikiwa wewe ungependa kuzuru Jumba la Ufalme ujionee mwenyewe jinsi Mashahidi wa Yehova waabuduvyo na yale waaminiyo, jihisi huru kwenda kwenye Jumba la Ufalme lililo karibu zaidi nawe, au tuandikie upate anwani ya jumba lililo karibu zaidi nawe.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Jumba la Ufalme katika Condobolin, New South Wales