Vijana Huuliza . . .
Naweza Kuwaje na Wakati Wenye Kufurahisha?
“Mimi nahisi kwamba sisi hupata kufanya mambo mengi yenye kufurahisha. Katika kutaniko letu sisi hufanya jitihada ya kweli ya kukutana pamoja. Sisi hupata kujifurahisha kwa njia yenye kujenga. Watoto wengi katika ulimwengu hawawezi kusema hivyo.”—Jennifer.
TAFRIJA—kila mtu huihitaji pindi kwa pindi. The World Book Encyclopedia husema kwamba tafrija yaweza hata “kuchangia kwa maana afya ya mtu ya kiakili na kimwili.” Kwani, Biblia yenyewe husema kwamba kuna “wakati wa kucheka,” yaani, wakati wa kujifurahisha!—Mhubiri 3:1, 4.a
Neno la Kilatini la “tafrija” humaanisha “kuumba upya, kurudisha, kuburudisha.” (Webster’s New Collegiate Dictionary) Kwa kusikitisha, mengi ya mambo ambayo vijana hufanya kwa ajili ya “kujifurahisha”—kama vile karamu zisizo na kiasi au kujiingiza katika utumizi mbaya wa dawa za kulevya na alkoholi au ngono haramu—kwa kweli hayaburudishi hata kidogo, bali yanaharibu. Kwa hivyo kupata utendaji wa kitafrija ambao unafurahisha na vilevile kujenga kwaweza kuwa tatizo kweli. Lakini kama aonyeshavyo Jennifer, aliyenukuliwa mwanzoni, hilo lawezekana!
Kufanya Mambo Pamoja
Hivi majuzi Amkeni! lilihoji vijana kadhaa kuhusu habari hii. Wengi walisema kwamba walifurahia kukutana pamoja na vijana wengine. Je, wewe wahisi vivyo hivyo—lakini mara nyingi hualikwi? Basi kwa nini usichukue hatua ya kwanza? Kwa mfano, msichana mmoja kutoka Afrika Kusini aitwaye Leigh, asema: “Ikiwa natamani kuona sinema fulani, nampigia simu mmoja wa rafiki zangu, nasi twawaeleza rafiki zetu wengine.” Kwa kawaida wao huhudhuria wonyesho wa mapema wa sinema hiyo. Baadaye, wazazi wao huwachukua na kwenda kula pamoja katika mkahawa wa mahali hapo.
Utendaji wa michezo pia huandaa fursa za mazoezi ya mwili yajengayo na ushirika wenye kujenga. (1 Timotheo 4:8) Roelien mchanga asema: “Kwanza mimi nazungumza pamoja na familia yangu mahali ninapotaka kwenda, kisha twaalika kikundi kidogo kijiunge nasi.” Kwa kweli, vijana Wakristo wamegundua michezo mingi ya aina mbalimbali yenye kujenga ambayo wanaweza kushiriki pamoja na wengine: kuteleza kwenye barafu, kuendesha baiskeli, kukimbia-kimbia, na kucheza tenisi, besiboli, kandanda, na voliboli, kutaja michezo michache tu.
La, huhitaji kutumia fedha nyingi au kununua vifaa vya hali ya juu ili kuwa na wakati wenye kufurahisha. “Wazazi wangu, marafiki na mimi tumetumia saa nyingi zenye kufurahisha tukitembea katika milima na maeneo ya pori yaliyo karibu,” asema msichana mmoja Mkristo aliye tineja. “Kuwa tu nje katika hewa safi pamoja na marafiki wazuri kunafurahisha sana!”
Vikusanyiko vya Kirafiki Vijengavyo
Hata hivyo, kwa vijana wengi, kujifurahisha humaanisha kuhudhuria vikusanyiko vya kirafiki. “Sisi hufurahia kualika marafiki ili kula na kusikiliza muziki,” asema Aveda mchanga. Vikusanyiko vya kirafiki vina sehemu ifaayo miongoni mwa Wakristo. Yesu Kristo mwenyewe alihudhuria milo ya kipekee, arusi, na vikusanyiko vinginevyo vya kirafiki. (Luka 5:27-29; Yohana 2:1-10) Wakristo wa mapema vivyohivyo walifurahia pindi ambapo walikutana pamoja kwa ajili ya milo na ushirika wenye kujenga.—Linganisha Yuda 12.
Ikiwa wazazi wako wakuruhusu kukaribisha kikusanyiko, waweza kufanya nini ili kuepuka matatizo na kuhakikisha kila mtu anafurahia? Ufunguo ni kupanga kwa uangalifu. (Mithali 21:5) Kwa kutoa kielezi: Ni jambo la kiakili kualika rafiki zako kwa idadi inayoweza kusimamiwa ifaavyo. Vikusanyiko vidogo zaidi havitaelekea sana kugeuka kuwa “karamu za ulevi,” (NW) au “karamu zenye kelele.”—Wagalatia 5:21, Byington.
Wakristo katika karne ya kwanza walionywa waepuke kushirikiana na wale “waendao bila utaratibu.” (2 Wathesalonike 3:11-15) Na njia hakika ya kuharibu kikusanyiko leo ni kualika vijana ambao wanajulikana kuwa wenye fujo na wasioweza kudhibitiwa. Ingawa unataka kuwa mwangalifu kuhusu unayealika, usijiwekee mipaka kwa marafiki walewale. ‘Panuka,’ na upate kujua wengine, kutia ndani wenye umri mkubwa zaidi, kutanikoni.—2 Wakorintho 6:13.
Je, utaandaa viburudisho? Ikiwa ndivyo, havihitaji kuwa vingi au vya bei ya juu ili wageni wako wawe na wakati wenye kufurahisha. (Luka 10:38-42) “Nyakati fulani sisi huwa na usiku wa pizza,” asema Sanchia, msichana kutoka Afrika Kusini. Mara nyingi wageni watajitolea kuleta vitu kadhaa.
Ni yapi baadhi ya mambo mwezayo kufanya katika kikusanyiko—mbali na kutazama televisheni, kusikiliza muziki, au kuzungumza tu? “Sisi kwa kawaida hupangia jioni hiyo kimbele,” asema Sanchia. “Tumepata kucheza michezo au mtu fulani kucheza piano, ili tuweze kuimba pamoja.” Kijana fulani Mwafrika aitwaye Masene asema: “Nyakati fulani sisi hucheza karata, dama, na mchezo wa sataranji.”
Jennifer, aliyenukuliwa mapema, aliliambia Amkeni!: “Tuna mzee katika kutaniko letu ambaye hutualika tucheze michezo ya Biblia. Unahitaji kuwa na ujuzi mzuri wa Biblia ili kucheza vyema.” Mwakilishi wa Amkeni! aliuliza vijana wengine: “Je, hamfikiri kucheza michezo ya Biblia ni jambo lisilofaa pindi hiyo?” Karibu wote walijibu, “La!”
“Ni yenye kutahini,” akasema msichana mmoja tineja. “Inafurahisha!” akasema mwingine. Michezo ya Biblia inapochezwa ili kujifurahisha, na roho ya kushindana inadhibitiwa, yaweza kuwa yenye kupendeza na yenye kuelimisha!—Ona “Kufanya Vikusanyiko vya Kirafiki Vifurahishe na Bado Vinufaishe,” katika toleo la Amkeni! la Juni 22, 1972, la Kiingereza.
Kujifurahisha kwa Familia
Katika nyakati za Biblia lilikuwa jambo la kawaida kwa familia kufurahia aina fulani za tafrija pamoja. (Luka 15:25) Hata hivyo, watungaji wachanga wa The Kids’ Book About Parents wanaonelea kwamba “wazazi na watoto wana shughuli nyingi mno siku hizi hivi kwamba hakuna aliye na wakati wa kupangia utendaji . . . Twafikiri kwamba ni jambo la maana kwa wazazi na watoto kuhakikisha wanatumia wakati pamoja kila juma wakifanya utendaji wenye kufurahisha tu.”
“Ijumaa ndiyo siku yetu ya familia,” asema kijana Mwafrika aitwaye Paki. “Kwa kawaida sisi hucheza pamoja.” Na tusisahau ndugu zetu. Bronwyn mchanga asema: “Mimi hufurahia kuchora na kufanya mambo mengine ya kisanaa pamoja na dada yangu mdogo.” Je, waweza kuchukua hatua ya kwanza na kudokeza utendaji fulani wenye kufurahisha mtakaofanya pamoja na familia yako?
Unapokuwa Peke Yako
Namna gani ukiwa peke yako? Hilo halimaanishi utalazimika kuchoshwa na kuwa mpweke. Kuna njia nyingi zenye kujenga, zenye kufurahisha za kutumia vipindi hivyo vya wakati. Kwa kielelezo, hobi. Tangu nyakati za Biblia wanaume na wanawake wamepata kujifunza muziki kuwa kwenye kujenga. (Mwanzo 4:21; 1 Samweli 16:16, 18) “Mimi hucheza piano,” asema Rachel. “Ni jambo uwezalo kufanya unapokuwa umechoshwa.” Ikiwa hupendi muziki, huenda ukafurahia kushona, kutunza bustani, kukusanya stampu, au kujifunza lugha ya kigeni. Kwa kuongezea, huenda hata ukasitawisha ustadi utakaokusaidia katika miaka ya baadaye.
Biblia hutuambia kwamba wanaume wa imani, kama vile Isaka, walitafuta vipindi vya kuwa peke yao ili kutafakari. (Mwanzo 24:63) Mwanamume kijana Mwaustria aitwaye Hans asema: “Pindi kwa pindi, mimi hutoka nje tu hadi mahali palipo kimya bustanini na kuketi ili kutazama machweo. Hilo huniletea shangwe nyingi na hunisaidia kuhisi nikiwa karibu zaidi na Mungu wangu, Yehova.”
“Furaha” Katika Utumishi wa Yehova
Biblia ilitabiri kwamba Kristo angepata “furaha” katika kumtumikia Yehova Mungu. (Isaya 11:3) Na ingawa utumishi mtakatifu kwa Mungu si tafrija hasa, huo waweza kuburudisha na kuleta uradhi.—Mathayo 11:28-30.
Hans, aliyenukuliwa mapema, akumbuka jambo jingine lenye kufurahisha. Yeye asema: “Rafiki zangu nami hupenda kukumbuka ile miisho-juma tuliyotumia kwenye mahali pa ujenzi wa Jumba la Kusanyiko [kwa ajili ya ibada]. Tulijifunza jinsi ya kufanya kazi pamoja, na tulipata kujuana vyema. Tukitazama nyuma, tunahisi uradhi kwamba tulifanya jambo lenye kustahili ambalo lilikuwa lenye kufurahisha.”
Ushuhuda wa hawa vijana Wakristo hutokeza waziwazi jambo moja la hakika: Huhitaji kukosa kuwa na wakati wenye kufurahisha. Fuata kanuni za Biblia. Uwe mwenye ubuni! Chukua hatua za kwanza zenye kujenga! Utapata kwamba unaweza kujifurahisha katika njia ambazo zitakujenga kiroho na vilevile kimwili na ambazo hazitakubomoa.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Vijana Wengine Hupata Raha Yote?” katika toleo letu la Julai 22, 1996.
[Blabu katika ukurasa wa 22]
“Kuwa tu nje katika hewa safi pamoja na marafiki wazuri kunafurahisha sana!”
[Picha katika ukurasa wa 23]
Huhitaji kutumia fedha nyingi mno ili kuwa na wakati wenye kufurahisha pamoja na marafikiy