Tulikuwa Mateka Wakati wa Maasi ya Gereza
SAA tisa hivi alasiri, Jumamosi, Machi 30, 1996, Edgardo Torres, Rubén Ceibel, nami tulifika kwenye Gereza la Ulinzi Mkali la Sierra Chica, katika mkoa wa Buenos Aires, Argentina. Likiwa limeundwa kuwa na wafungwa 800 hivi, ngome hii iliyojaa watu kupita kiasi ilikuwa na wahalifu waliohukumiwa 1,052. Uhalifu wao ulikuwa kuanzia unyang’anyi wa mabavu hadi uuaji wa mfululizo. Tulienda pale tukiwa wageni.
Kwa Edgardo na Rubén, hii ilikuwa moja ya safari nyingi za Jumamosi kuja kwenye gereza hili lijulikanalo sana. Wakiwa wazee katika kutaniko la mahali hapo la Mashahidi wa Yehova, wao walizuru kwa ukawaida sehemu hiyo ili kutoa hotuba za Biblia za kila juma kwa wafungwa wapatao 15. Kwangu, nikiwa mwangalizi asafiriye, hii ilikuwa fursa nadra, kwa kuwa sikuwa nimepata kuongoza mkutano katika gereza.
Gereza hilo lina majengo 12 ya jela yaliyoundwa katika umbo la kipepea-hewa. Tulipokuwa tukiingia katika majengo hayo, tuliona kwa mbali wafungwa wanne wakitupungia mikono kwa idili. Wafungwa hawa walikuwa wameendelea katika mafunzo yao ya Biblia kufikia hatua ya kuwa watangazaji wasiobatizwa wa habari njema za Ufalme wa Mungu. Tuliongozwa haraka kwenye jengo la jela nambari tisa, ambapo tulipaswa kufanya mkutano. Huko, chumba kimoja kilikuwa kimepakwa rangi na kupambwa na pazia, ikikipatia sura ya kuheshimika.
Maasi Yaanza
Ingawa hivyo, kulikuwa na kasoro fulani. Kulikuwa na wafungwa 12 waliohudhuria badala ya wale 15 wa kawaida. Sote tulijiuliza ni kwa nini. Mkutano ulianza kama kawaida, kwa wimbo na sala. Baada ya dakika chache, tuligutushwa kwa mipigo ya bunduki yenye sauti kubwa ikifuatiwa na milipuko ya bunduki ya kumimina risasi. Kisha tukasikia mipaazo ya sauti na vilio. Maasi ya gereza yalikuwa yameanza tu!
Wafungwa kadhaa waliojifunika uso na waliojihami kwa visu vya kujitengenezea waliingia kwa kishindo katika chumba chetu cha kukutania. Walishangaa kutupata—wageni watatu! Haraka tulipelekwa kupitia ukumbi uliojaa moshi. Kulikuwa na magodoro yanayoungua, wafungwa wakikimbia kwa mvurugo, na askari aliyejeruhiwa akiwa amelala sakafuni. Mnara wa mlinzi ulioko katikati ya uwanja wa gereza ulikuwa umefunikwa kwa moto kutoka kwa bomu la kujitengenezea. Tulipelekwa nje na kulazimishwa kusimama meta 50 hivi kutoka kwenye ua mkuu. Tukitazama mbele moja kwa moja, tuliweza kuona polisi na walinzi wa gereza nje ya ua, wakituelekezea bunduki zao. Kikundi cha wafungwa kikijificha nyuma yetu kilishikilia visu vyao kwenye koo zetu. Walikuwa wakitutumia kama ngao za kibinadamu.
Mateka Zaidi
Muda wa saa tano baadaye, baada ya machweo, viongozi wa maasi walimruhusu daktari aingie gerezani ili kutibu waliojeruhiwa. Daktari huyo pia akawa mateka. Mwishowe, saa tatu hivi jioni, tulipelekwa kwenye hospitali ya gereza. Huko tulijiunga na kikundi cha walinzi ambao pia walizuiwa wakiwa mateka. Sasa wafanya-fujo hao walilazimisha mateka wote watumike kwa zamu wakiwa ngao za kibinadamu.
Baada ya muda mfupi, hakimu na karani wake waliruhusiwa kukutana na wafanya-fujo hao, katika jaribio la kutuliza mambo kwa amani. Lakini tatizo hili liliongezeka wakati wafungwa hao walipowazuia kwa ushupavu wote wawili wawe mateka.
Kulikuwa na vita vya mara kwa mara usiku wote. Tulijaribu kulala, lakini ilionekana kwamba kila wakati tuliposinzia, mlio mkubwa ungetushtua na kutuamsha. Kisha, mapema sana asubuhi, zamu yetu ya kusimama tukiwa ngao hai ikafika tena.
Jeuri Yaongezeka
Jumapili, Machi 31, siku ya pili ya maasi hayo, hali ilikuwa mbaya. Viongozi wa maasi hawakuweza kukubaliana kuhusu madai yao. Hilo lilizusha hali ya hasira na jeuri. Vikundi vya wafanya-fujo vilitokeza vurumai, vikiharibu na kuchoma kila kitu njiani mwavyo. Ugomvi wa zamani ulitulizwa kwa jeuri na uuaji-kimakusudi. Wafungwa kadhaa ambao walikataa kujiunga na fujo hiyo waliuawa. Miili fulani ilichomwa katika jiko la kuokea mikate.
Namna zote za uvumi na ripoti zenye kupingana kuhusu kufunguliwa kwetu zilienea gerezani. Ilikuwa hali yenye mabadiliko-badiliko kihisia-moyo kwetu mateka. Nyakati fulani tuliruhusiwa kutazama habari kwenye televisheni. Tulishangaa kuona jinsi masimulizi ya televisheni yalivyo tofauti na mambo hakika. Ilivunja moyo sana.
Tulikabilije hali? Tulikaza akili zetu katika sala, kusoma Biblia, na kusema na wengine juu ya ahadi za Biblia za wakati ujao wenye furaha. Huo ndio uliokuwa ufunguo wa nguvu zetu za kihisia-moyo wakati wa masaibu hayo.
Jumatatu, viongozi wa maasi walikubali kuanza maafikiano pamoja na wenye mamlaka. Ilionekana kana kwamba mwisho wa maasi ulikuwa karibu. Wafanya-fujo hao walikuwa wakimtumia Edgardo na walinzi kadhaa wa gereza kuwa ngao wakati pigano la bunduki lilipozuka miongoni mwa wafungwa fulani. Katika mvurugo uliofuata, polisi, kwa kukisia kwamba mateka walikuwa wakipigwa risasi, walifyatua silaha zao. Edgardo alinusurika mlipuko wa mfululizo wa risasi, lakini walinzi fulani mateka walipigwa risasi.
Ilionekana Kifo Kitatokea
Walitupeleka sisi mateka juu ya paa ili kuonyesha wenye mamlaka kwamba bado tulikuwa hai. Lakini polisi waliendelea kufyatua risasi. Hilo liliwakasirisha wafanya-fujo hao. Kila mtu alianza kupiga kelele kwa wakati uleule. Wengine walipiga kelele: “Wachinjeni mateka! Wachinjeni!” Wengine wakasihi: “Bado! Acheni tungojee!” Ilionekana kifo kitatokea. Rubén nami tulitazamana kana kwamba kusema, ‘Hadi ulimwengu mpya.’ Kisha sote tukasali kimya-kimya. Mara hiyo, tulihisi utulivu wa ndani na amani ya akili, ambayo chini ya hali hizo, ingekuja kutoka kwa Yehova tu.—Wafilipi 4:7.
Ghafula, polisi waliacha kufyatua risasi, na mmoja wa viongozi akaamuru tusiuawe. Mfungwa mchanga ambaye alikuwa akinishikilia aliamrishwa anitembeze kwenda na kurudi kwenye paa, kama onyo kwa polisi. Alikuwa mwenye wasiwasi sana. Papo hapo, niliweza kuanzisha mazungumzo ambayo yalitutuliza sote wawili. Nilieleza kwamba kuteseka kwa binadamu kulichochewa na Shetani na roho waovu wake na kwamba karibuni Yehova Mungu atamaliza kuteseka kote huko.—Ufunuo 12:12.
Tuliporudishwa kwenye hospitali ya gereza tulipata kwamba wengi wa mateka walikuwa na wasiwasi mno. Tulijaribu kushiriki imani yetu katika ahadi za Yehova pamoja na mateka wenzetu. Tulizungumza nao juu ya tumaini la wakati ujao lenye kutegemea Biblia katika Paradiso duniani. Baadhi ya mateka walianza kumwita Yehova kwa jina. Yule daktari alidhihirisha upendezi wa kipekee na kuuliza maswali kadhaa hususa. Hilo liliongoza kwenye mazungumzo marefu ya Biblia kwa kutumia kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele.
Kusherehekea Ukumbusho
Jumanne, siku yetu ya nne utekwani, ilikuwa ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo. Siku hiyo mamilioni ya Mashahidi wa Yehova na watu wenye kupendezwa ulimwenguni pote hukutana ili kuadhimisha tukio hili kwa kutii amri ya Yesu. (Luka 22:19) Sisi pia tulifanya mipango ili kusherehekea Ukumbusho.
Pembe moja ya chumba ilichaguliwa kwa ajili ya usiri. Hakukuwa na mkate usiotiwa chachu au divai nyekundu kutumiwa kama mifano. Lakini sisi watatu tulifurahia kumwimbia Yehova sifa, kusali, na kupitia simulizi la Biblia juu ya usiku wa mwisho wa Yesu na matukio mengine yanayozunguka kifo chake. Tulihisi tukiwa karibu sana na familia zetu na ndugu na dada zetu wa kiroho walipokuwa wakisherehekea Ukumbusho wakati uleule kotekote nchini.
Masaibu Yaisha
Hali ya mkazo, hofu, na kutojua kitakachotukia iliendelea kwa siku nne zilizofuata. Hata hivyo, tulifarijiwa na barua kadhaa kutoka kwa watu wa ukoo na marafiki, ambazo wafungwa walituruhusu kuzipata. Katika pindi moja tuliruhusiwa hata kuwasiliana na familia zetu kwa simu. Iliburudisha kama nini kusikia sauti zao na kusoma maonyesho yao ya upendo na hangaiko!
Jumamosi, siku yetu ya nane utekwani, wafanya-fujo walifikia mwafaka na wenye mamlaka. Tulielezwa kwamba siku iliyofuata tungefunguliwa. Jumapili, Aprili 7, saa 8:30 alasiri, tulipokea habari: “Jitayarisheni kuondoka!” Wafungwa hao walipanga ‘mlinzi wa heshima’ atusindikize hadi kwenye uhuru! Tulipokuwa tukiondoka hospitali, msemaji wa viongozi hao alimkaribia Edgardo na kusema: “Ndugu, nimependezwa sana na mwenendo wenu. Naahidi kwamba kuanzia sasa na kuendelea nitakuwa nikihudhuria mikutano ya Jumamosi gerezani. Bado mtafanya mikutano hata baada ya yaliyotukia hapa, sivyo?” Edgardo alitabasamu na kujibu: “Bila shaka!”
Jambo la kushangaza lilitungojea nje. Mara tu tulipotoka kwenye jengo hilo, idadi yote ya wafungwa ilipiga makofi kwa heshima yetu. Hiyo ilikuwa njia yao ya kuonyesha kwamba walisikitika kwa kile kilichotendeka. Ilikuwa pindi yenye kugusa hisia. Hakuna shaka kwamba mwenendo wetu wa Kikristo wakati wa siku tisa zilizotangulia ulikuwa umewapendeza wote, kwa sifa ya Yehova.
Nje ya ua wa gereza, tulikutana na familia zetu na ndugu na dada zetu 200 hivi. Tulikumbatiana tukiwa na hisi kubwa sana ya kitulizo. Tulikuwa tumesalimika! Mmoja wa mateka alimkaribia mke wangu na kumwambia: “Nafikiri Yehova amenifikia moyo na ataka nimtumikie.”
Edgardo, Rubén, nami tulijifunza katika njia ya kipekee sana kwamba Yehova aweza kuwategemeza watumishi wake, hata wakati wa taabu mbaya sana. Tulijionea jinsi inavyostaajabisha kusali kwa Yehova na kusikiwa naye. Kama mtunga-zaburi, twaweza kusema: “Ee BWANA, nitakutukuza kwa maana umeniinua, wala hukuwafurahisha adui zangu juu yangu. Ee BWANA, Mungu wangu, nalikulilia ukaniponya. Umeniinua nafsi yangu, Ee BWANA, kutoka kuzimu, umenihuisha na kunitoa miongoni mwao washukao shimoni.” (Zaburi 30:1-3)—Kama ilivyosimuliwa na Darío Martín.
Blurb katika ukurasa wa 19]
Wafungwa kadhaa waliojifunika uso na waliojihami kwa visu vya kujitengenezea waliingia kwa kishindo katika chumba chetu cha kukutania
[Blabu katika ukurasa wa 20]
Wafanya-fujo walikuwa wakimtumia Edgardo na walinzi kadhaa wa gereza kuwa ngao
[Blabu katika ukurasa wa 21]
Wafungwa walipanga ‘mlinzi wa heshima’ atusindikize hadi kwenye uhuru!
[Picha katika ukurasa wa 18]
Wahudumu watatu wenye kuzuru (kushoto hadi kulia): Edgardo Torres, Rubén Ceibel, na Darío Martín