Maoni ya Biblia
Je, Wakristo Wapaswa Kuwa Wapinga-Vita?
“Makanisa yapaswa kupinga-vita tena kama yalivyokuwa katika karne za kwanza za Ukristo.” Hubert Butler, mwandikaji wa Ireland.
BAADA ya kuzuru Yugoslavia baada ya Vita ya Ulimwengu 2, Hubert Butler alijasiria kuandika maneno yaliyo juu katika insha iliyoandikwa 1947 lakini ambayo haikuchapishwa hadi mwaka uliopita! Alishtushwa na jinsi “Kanisa la Kikristo katika wakati wa vita ya ulimwengu 2 lilivyokaa kimya juu ya uhalifu mbaya sana na kujitenga mbali sana na mafundisho ya Kristo.”
Butler hakuogopa kusema kwa ujasiri kwa kutetea harakati zisizopendwa au vikundi vya watu visivyopendwa. Alipofanya hivyo, hakukuwa na mtu wa kumuunga mkono. Alijieleza bila hofu alipotofautisha tabia ya makanisa na msimamo wenye moyo mkuu wa Mashahidi wa Yehova, ambao walitajwa katika gazeti The Irish Times kuwa “kwa hakika farakano la kidini lisilojihusisha na siasa kabisa na lisilo na hatia na lawama hata kidogo.” Katika insha yake, “Ripoti juu ya Yugoslavia,” Butler aliandika kwamba Mashahidi, ambao “walikataa mbinu zote za hila ambazo viongozi wa kisiasa na kidini walizitumia kuhalalisha vita,” walishtakiwa na wenye mamlaka wa Yugoslavia kwa sababu walikataa kujiunga na harakati za vita.
Lakini, je, ni sahihi Kimaandiko kuwataja Mashahidi wa Yehova kuwa ni wapinga-vita? Ili kuliweka jambo hilo wazi, itatagemea juu ya kile kinachomaanishwa na neno “mpinga-vita.” Butler alitumia neno hilo ili kuwapongeza Mashahidi kwa sababu wao walikataa kijasiri, wakiteseka sana kibinafsi, kubeba silaha. Lakini, kwa kusikitisha, wengi wanaoshikwa na kichaa cha vita humwona mpinga-vita kuwa ni “mwoga au ni msaliti tu ambaye anataka kuepa wajibu wake kwa taifa lake.” Je, maoni hayo ni sahihi?
Kupinga-Vita au Jeuri
Kamusi ya Webster’s Ninth New Collegiate Dictionary husema kwamba mpinga-vita ni mtu ambaye “apinga kwa dhati pambano na hasa vita.” Hufafanua “upingaji-vita” kuwa “upingaji-vita au jeuri ikiwa njia ya kumaliza mabishano; kimahususi: kukataa kubeba silaha kwa misingi ya adili au ya kidini.” Jinsi gani mafafanuzi hayo yangetumika kwa waamini wa kutaniko la Kikristo la mapema?
Walikataa ‘kubeba silaha kwa misingi ya adili na kidini’ na waliepuka ‘mapambano yote na vita.’ Kwa nini? Kwa sababu walijua kwamba Yesu alikuwa amesema kwamba wafuasi wake ‘hawakuwa sehemu ya ulimwengu’ na kwamba “wale wote wauchukuao upanga wataangamia kwa upanga.” (Yohana 15:19; Mathayo 26:52) Katika kitabu The Early Church and the World, mwanahistoria mmoja atuambia kwamba “hadi wakati wa utawala wa Marcus Aurelius [161-180 W.K.], hakuna Mkristo angekuwa askari-jeshi baada ya ubatizo wake.” Katika kitabu The New World’s Foundations in the Old, mwanahistoria mwingine asema: “Wakristo wa kwanza walifikiri ni makosa kupigana, wasingetumika katika jeshi hata wakati Milki ilipohitaji askari-jeshi.”
Utume wa Wakristo ulikuwa kuhubiri habari njema. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Walielewa kwamba hawakuwa na utume kutoka kwa Mungu wa kupigana vita na maadui wao, kutenda kana kwamba wanatenda wakiwa wafishaji wa Mungu. (Mathayo 5:9; Waroma 12:17-21) Wakati tu wenye kuitwa isivyofaa Wakristo ‘wajitengapo mbali sana na mafundisho ya Kristo,’ kama Butler alivyosema, ndipo wanapojitenga katika vita vya mataifa. Kisha makasisi wabariki majeshi na wasali kwa ajili ya ushindi, kwa kawaida katika pande zote za mabishano. (Linganisha Yohana 17:16; 18:36.) Kwa mfano, katika karne zilizopita, Waprotestanti na Wakatoliki walipigana katika vita vingi vya umwagaji damu mkubwa, ikitokeza “hofu kuu ambayo ilienea hadi Ulaya Magharibi, pande zote mbili zikidai kuwa zinatumiwa kutekeleza hasira ya kisasi ya Mungu,” aandika Kenneth Clark katika kitabu chake Civilisation. Hoja zitolewazo ili kuhalalisha aina hii ya vita, yasema Cyclopedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature ya McClintock na Strong “kwa wazi ni tamaa ya kufurahisha mamlaka za kilimwengu, na kwa wazi zinapingana na mafundisho ya Kikristo ya kale na ya roho yote ya Gospeli.”—Yakobo 4:4.
Je, Wakristo Wanapinga Kabisa Vita?
Lakini, je, mafundisho ya Wakristo wa kale na roho yote ya Gospeli kwelikweli ni ya kupinga-vita? Je, Wakristo wa kale kwa kweli wangeweza kufafanuliwa kuwa wapinga-vita kama ilivyofafanuliwa mapema? Hapana! Kwa nini? Sababu moja ni kwamba, wao walitambua haki ya Mungu ya kupigana vita. (Kutoka 14:13, 14; 15:1-4; Yoshua 10:14; Isaya 30:30-32) Kwa kuongezea hilo, kamwe hawakubisha haki ya Mungu ya kuamuru Israeli la kale kupigana kwa ajili yake wakati taifa hilo lilipotumika likiwa chombo chake pekee duniani.—Zaburi 144:1; Matendo 7:45; Waebrania 11:32-34.
Mungu hana haki tu bali pia ana wajibu unaotegemea haki wa kuondoa watu wabaya duniani. Watenda-maovu wengi hawataitikia sihi za Mungu zenye subira kuwaelekea ili wabadilishe mienendo yao. (Isaya 45:22; Mathayo 7:13, 14) Uvumilivu wa Mungu juu ya uovu una mipaka. (Isaya 61:2; Matendo 17:30) Kwa hiyo, Wakristo, watambua kwamba hatimaye Mungu atawaondoa kwa nguvu watu waovu kutoka katika dunia. (2 Petro 3:9, 10) Kama vile Biblia itabirivyo, hili litakuwa “kwenye ufunuo wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu katika moto wenye kuwaka mwali, aletapo kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.”—2 Wathesalonike 1:6-9.
Kitabu cha mwisho cha Biblia chaelezea pambano hili kuwa “vita ya siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote,” au Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Chasema kwamba Yesu Kristo atachukua uongozi katika jambo hili, kwamba “aendeleza vita katika uadilifu.” (Ufunuo 19:11, 14, 15) Kwa kufaa Yesu Kristo aitwa “Mkuu wa Amani.” (Isaya 9:6) Lakini yeye si mpinga-vita. Tayari amesha pigana vita mbinguni kuondoa maadui wa Mungu wenye kuasi. (Ufunuo 12:7-9) Karibuni atapigana vita nyingine “kuwaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia.” Hata hivyo, wafuasi wake duniani hawatashiriki katika hukumu hiyo ya kimungu.—Ufunuo 11:17, 18.
Wakristo wa kweli wapenda amani. Wabaki bila kuunga mkono upande wowote katika mapigano ya kijeshi, kisiasa, na kikabila. Lakini, katika maana ya kweli, wao si wapinga-vita. Kwa nini? Kwa sababu wanakaribisha vita ya Mungu ambayo hatimaye itatimiza mapenzi yake duniani—vita ambayo itamaliza lile suala kuu la enzi kuu ya ulimwengu wote mzima na kuondolea mbali milele maadui wote wa amani duniani.—Yeremia 25:31-33; Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 22]
Kristo Adhihakiwa/The Doré Bible Illustrations/Dover Publications, Inc.