Maoni ya Biblia
Je, Muungano wa Kikristo Huruhusu Kuwe na Unamna-Namna?
MUUNGANO katika kutaniko la Kikristo ni muhimu. Ukosefu wa muungano katika itikadi za kimafundisho ungesababisha mabishano makali, ugomvi, na hata uadui. (Matendo 23:6-10) Biblia husema kwamba “Mungu ni Mungu, si wa kukosa utaratibu, bali wa amani.” (1 Wakorintho 14:33) Kwa sababu hiyo, Wakristo wanaonywa kwa upole waseme kwa upatano na waunganishwe katika akili ileile na katika mstari uleule wa fikira.—1 Wakorintho 1:10.
Je, maneno haya na vifungu vya Biblia kama hivi hutia moyo usare hasa miongoni mwa Wakristo katika kila jambo? (Yohana 17:20-23; Wagalatia 3:28) Je, Ukristo wa kweli kama unavyofafanuliwa katika Biblia hupinga unamna-namna kwa habari ya utu wa mtu mmoja-mmoja? Je, Wakristo wote wanatarajiwa wawe na namna fulani ya tabia zinazofanana na zisizoweza kubadilishwa?
Mungu Hutuvutia Tukiwa Mtu Mmoja-Mmoja
Watu fulani huamini kwa dhati kwamba Biblia ni chombo kingine tu kwa ajili ya kuongoza kwa uthabiti matungamo ya watu. Kwa kweli, mara nyingi imetumiwa vibaya kwa njia hiyo na mafarakano fulani. Hata hivyo, Yesu, alishikilia maoni tofauti sana ya Maandiko na Mtungaji wake wa Kimungu. Alimfafanua Mungu kuwa mwenye upendezi mwingi katika kila kimoja cha viumbe vyake.
Kwenye Yohana 6:44, Yesu alieleza: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye.” Kitenzi kilichotumika hapa hakidokezi kwamba Mungu hukokota watu, dhidi ya mapenzi yao. Badala yake, Mungu huvutia kwa uanana, akisisimua tamaa ndani ya mioyo yetu. Kama alivyoeleza msomi mmoja wa Biblia, kuna, ‘uvutano kutoka kwa Mungu wa kuelekeza akili iamini.’ Muumba haoni familia ya kibinadamu kuwa matungamo ya watu wasio na sifa za kibinafsi. Yeye hufanya kadirio la watu na kuvutia kwa uanana wale walio na moyo wenye mwelekeo ufaao.—Zaburi 11:5; Mithali 21:2; Matendo 13:48.
Angalia jinsi mtume Paulo alivyokuwa mwenye kubadilikana. Alitambua mahitaji ya pekee ya watu na kutambua kwamba maoni fulani yalikuwa ya kawaida kwa mataifa au malezi fulani hususa. Kisha akabadilisha mfikio wake ifaavyo. Aliandika: “Kwa Wayahudi nilipata kuwa kama Myahudi, ili niweze kuwapata Wayahudi . . . Kwa walio dhaifu nilipata kuwa dhaifu, ili niweze kuwapata walio dhaifu. Nimekuwa mambo yote kwa watu wa namna zote, ili nipate kwa vyovyote kuokoa wengine.”—1 Wakorintho 9:20-22.
Waziwazi, Paulo hakufanya watu washikilie maoni yaleyale au kuwatendea wote kwa njia ileile. Aliwapa kitia-moyo hiki: “Acheni tamko lenu liwe na upendezi sikuzote, lenye kukolezwa chumvi, ili kujua jinsi mpaswavyo kumpa jibu kila mmoja.” (Wakolosai 4:6) Ndiyo, Paulo na Wakristo wengine walihitaji kutambua na kustahi hali ya pekee katika kila mtu kusudi wamsaidie.
Kusudi la Awali la Mungu
Staha hii kwa ajili ya mtu akiwa na sifa za kibinafsi huendelea baada ya mmoja kuwa sehemu ya kutaniko la Kikristo. Watu wa Mungu hawapotezi sifa zao za kibinafsi ndani ya tengenezo la usare kamili ili wafaane na upendeleo wa wale walio na madaraka. Badala ya hivyo, wanaonea shangwe unamna-namna wa nyutu mbalimbali na wana uwezo, mazoea, na kauli tofauti. Sifa za kibinafsi za kila mmoja hazionwi kuwa zenye kusumbua au kukera. Ni sehemu ya kusudi la awali la Mungu.
Kwa sababu hiyo, katika ulimwengu mpya ulioahidiwa katika Biblia kwa ajili ya waadilifu, ukamilifu miongoni mwa wanadamu utaruhusu tofauti nyingi. (2 Petro 3:13) Chini ya kichwa “Ukamilifu,” ensaiklopedia ya Biblia Insight on the Scripturesa kwa kufaa hutoa maelezo yafuatayo: “Ukamilifu haumaanishi mwisho wa unamna-namna, ingawa, watu hudhania hivyo mara nyingi. Katika jamii ya wanyama, ambayo ni tokeo la ‘utendaji mkamilifu’ wa Yehova (Mwa[nzo] 1:20-24; Kum[bukumbu la Torati] 32:4), ina unamna-namna ulio mwingi mno.”
Kitabu Insight chaongezea: “Ukamilifu wa Dunia-sayari hivyohivyo si usiopatana na unamna-namna, badiliko, au tofauti; unatoa nafasi kwa ajili ya vilivyo sahili na vilivyo tata, vilivyo vya kawaida na vyenye kupendeza, vilivyo vitamu na vyenye gwadu, vyenye kukwaruza na vilivyo laini, makonde ya majani na miti, milima na mabonde. Unaruhusu msisimuko wenye kuburudisha wa mwanzo wa masika, joto la kiangazi lenye anga ya samawati, rangi zenye kupendeza za vuli, uzuri wenye kutakata wa theluji iliyotoka tu kuanguka. (Mwa[nzo] 8:22) Hivyo wanadamu wakamilifu hawatakuwa wenye nyutu, vipawa, na uwezo unaofanana.”
Hangaiko kwa Ajili ya Wengine
Hata hivyo, Ukristo wa kweli hupinga mwelekeo wa kujifikiria na wa kukosa kustahi wale wanaotuzunguka. Mtume Paulo aliangalia kwa makini kila sehemu ya maisha na mwenendo wake kusudi aepuke kuwakwaza wengine. Katika barua yake kwa kutaniko la Korintho alisema: “Katika njia yoyote sisi hatutoi sababu yoyote ya kukwaza, ili huduma yetu isitafutiwe kosa.” (2 Wakorintho 6:3) Nyakati nyingine, ni lazima tudhibiti tamaa zetu za kibinafsi na kutanguliza mahitaji ya wengine kuliko mapendezi yetu. Kwa kielelezo, Paulo aliwaandikia Wakristo katika Roma: “Ni vema kutokula nyama au kunywa divai au kufanya jambo lolote ambalo juu yalo ndugu yako akwazika.”—Waroma 14:21.
Vivyo hivyo leo, mtu aweza kuchagua kujiepusha na alkoholi anapokuwa pamoja na mtu ambaye ana tatizo la kudhibiti unywaji wake. (1 Wakorintho 10:23, 24) Hili hufanywa, si kwa sababu ya kushurutishwa kupatana na mapendezi ya mtu mwingine, lakini kama kitendo cha adili chenye fadhili na upendo. “Hata Kristo hakujipendeza mwenyewe.” Yesu alikuwa mtu mwenye sifa za kibinafsi, lakini hakusisitiza mapendezi yake na kuumiza hisia za wengine.—Waroma 15:3.
Hata hivyo, upande mojawapo wenye kuburudisha zaidi wa Ukristo wa kweli ni kule kustahi uhuru na mapendezi ya mtu ndani ya mipaka ya miongozo ya Biblia. Inafundisha kwamba Mungu alitufanya tuwe tofauti na wa kipekee. Kwenye 1 Wakorintho 2:11, twasoma: “Ni nani miongoni mwa wanadamu ayajuaye mambo ya mwanadamu isipokuwa roho ya mwanadamu iliyo katika yeye?” Sisi hujaribu kuwaelewa wengine kwa kadiri tuwezavyo. Lakini mstari huu hudokeza kwamba kila mmoja wetu ana jambo fulani la kipekee ambalo ni sisi na Muumba wetu tu tunaolielewa. Tuna “mtu wa siri wa moyoni” ambaye sisi humdhihirisha tuchaguavyo.—1 Petro 3:4.
Muungano na Unamna-Namna—Usawaziko Unaotaka Uangalifu Mkubwa
Mtume Paulo aliweka kielelezo kizuri cha usawaziko wa Kikristo. Ijapokuwa alikuwa na mamlaka akiwa mtume wa Kristo, alikuwa mwangalifu kutotwika wengine kauli yake.
Mathalani, Paulo alikuwa na kauli yenye nguvu sana kuhusu faida za useja katika ulimwengu huu usio mkamilifu. Yeye mwenyewe alikuwa mseja wakati alipoandika: “Wale [wanaooa] watakuwa na dhiki katika mwili wao,” na, “[mjane] ni mwenye furaha zaidi akibaki kama alivyo, kulingana na kauli yangu.” Uhakika wa kwamba maneno yake yalikuja kuwa sehemu ya Neno la Mungu lililopuliziwa huonyesha ya kwamba hakukuwa na ubaya wowote na kauli yake. Na bado alieleza: “Hata kama ungeoa, hungefanya dhambi.”—1 Wakorintho 7:28, 40.
Kwa wazi, wengi wa mitume walikuwa wanaume waliooa, kama Paulo alivyokiri kwa maneno: “Sisi tuna mamlaka ya kuongoza dada huku na huku akiwa mke, hata kama vile wale wengine wa mitume na ndugu za Bwana na Kefa, sivyo?” (1 Wakorintho 9:5) Wakristo walijua kwamba katika jambo hili wangeweza kufanya machaguzi yaliyo tofauti na ya Paulo na bado angewastahi.
Sikuzote waabudu wa Mungu wameruhusiwa kuonyesha imani yao kwa kupatana na utu wao wa kipekee. Kwa kweli, Mungu hata aliruhusu waandikaji wa Biblia watumie mtindo wa mtu mmoja-mmoja wa kuandika walipokuwa wakifanya hivyo. Kwa kielelezo, ijapokuwa Nehemia alikuwa mnyenyekevu aliandika simulizi lake kwa usemi wa kujitaja. (Nehemia 5:6, 19) Kwa upande mwingine, kwa sababu ya kuwa na kiasi mtume Yohana hakutumia kamwe jina lake hata mara moja katika usimulizi wake wa Gospeli na alijirijezea mara chache sana. Mungu alikubali mitindo hiyo miwili ya uandishi na kuihifadhi katika Biblia.
Vielelezo vinavyofanana na hivyo vya usawaziko na hali ya ukubalifu vinapatikana kotekote katika Maandiko. Waziwazi, muungano wa Kikristo huruhusu unamna-namna. Bila shaka, tofauti za malezi na kauli zaweza kuongoza kwenye ukosefu wa muungano wakati sifa za kiroho zinapokosekana. (Waroma 16:17, 18) Lakini wakati ‘tunapojivika wenyewe upendo, kifungo kikamilifu cha muungano,’ twajifunza kuonea shangwe nyutu za kipekee za wengine.—Wakolosai 3:14.
“Kwa hiyo karibishaneni,” husema Biblia, “kama vile Kristo pia alivyotukaribisha sisi, kwa tazamio la utukufu wa Mungu.” (Waroma 15:7) Kwa msaada wa roho ya Mungu, Wakristo wanaweza kupata usawaziko wenye kutaka uangalifu mkubwa wa kudumisha muungano huku wakionea shangwe unamna-namna wa nyutu za kipekee katika kutaniko.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Babu katika ukurasa wa 14]
Muumba haoni familia ya kibinadamu kuwa matungamo ya watu wasio na sifa za kibinafsi
[Blabu katika ukurasa wa 15]
Kila mmoja wetu ana jambo fulani la kipekee ambalo ni sisi na Muumba wetu tu tunaolielewayy