Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 7/22 kur. 18-20
  • Kwa Nini Siwezi Kukaza Fikira?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Siwezi Kukaza Fikira?
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kubadilika kwa Mawazo Yako
  • Hisia-Moyo na Homoni
  • Mazoea Yako ya Kulala
  • Mlo na Kukaza Fikira
  • Kizazi cha Televisheni na Kompyuta
  • Naweza Kukazaje Fikira?
    Amkeni!—1998
  • Kwa Nini Ni Vigumu Sana Kwangu Kuacha Kufikiria Watu wa Jinsia Tofauti?
    Amkeni!—1994
  • Kubalehe—Kujitayarisha Kuwa Mtu Mzima
    Amkeni!—2011
  • Kwa Nini Mwili Wangu Unabadilika?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 7/22 kur. 18-20

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Siwezi Kukaza Fikira?

“Nyakati nyingine hutukia bila kukusudia. Nasikiliza kwenye mkutano wa kutaniko, kisha, kwa ghafula, akili zangu zaanza kutangatanga. Dakika kumi baadaye nasikiliza tena.”—Jesse.

“KAZIA UANGALIFU!” Je, mara nyingi wewe husikia maneno hayo kutoka kwa walimu au wazazi wako? Ikiwa ndivyo, basi huenda ukawa na tatizo la kukaza fikira. Tokeo laweza kuwa, kupata maksi za chini. Waweza kupata kwamba wengine wana maoni yasiyofaa kukuelekea, wakikupuuza kuwa mlevi, au mjeuri.

La maana zaidi, kutoweza kukazia uangalifu kwaweza kuathiri vibaya hali yako ya kiroho. Kwani, Biblia huamuru hivi: “Kazieni uangalifu jinsi msikilizavyo.” (Luka 8:18) Kwa kweli, Wakristo huamuriwa ‘wakazie uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida’ mambo ya kiroho. (Waebrania 2:1) Na ikiwa waona ugumu wa kukaza fikira, waweza kupata ugumu wa kutii shauri hili.

Tatizo laweza kuwa nini? Katika visa fulani ukosefu wa kukaza fikira waweza kuwa tokeo la tatizo la kimwili. Kwa kielelezo, watafiti fulani huamini kwamba Kasoro ya Upungufu wa Makini inahusika katika kutotenda kwa mifumo ya neva ya ubongo.a Vijana fulani wana matatizo ambayo hayajatambuliwa kama vile kukosa kusikia au kutoona. Matatizo haya pia yaweza kuzuia uwezo wa mtu wa kukazia uangalifu. Watafiti wamepata kwamba kwa ujumla vijana wana ugumu mwingi wa kukaza fikira kuliko watu wazima. Hivyo kutosikiliza ni jambo la kawaida miongoni mwa vijana, ingawa mara chache sana huwa ni tokeo la kasoro ya kitiba.

Kubadilika kwa Mawazo Yako

Ikiwa una matatizo ya kukaza fikira, kuna uwezekano mkubwa kwamba unasumbuliwa na kukua. Mtume Paulo aliandika hivi: “Nilipokuwa kitoto, nilikuwa nikisema kama kitoto, nikifikiri kama kitoto, nikiwazawaza kama kitoto; lakini kwa kuwa sasa nimekuwa mtu mzima, nimeziondolea mbali tabia za kitoto.” (1 Wakorintho 13:11) Unapozidi kufikia utu mzima, mwelekeo wako wa kufikiri hubadilika. Kulingana na kitabu Adolescent Development, “uwezo wa dhana mpya . . . huibuka wakati wa mapema wa ubalehe.” Unakuza uwezo wa kufahamu na kuchanganua dhana na mawazo ya kinadharia. Unaanza kufahamu kwa undani maadili na masuala mengine yawezayo kutumika. Unaanza kufikiri juu ya wakati wako ujao ukiwa mtu mzima.

Tatizo laweza kuwa nini? Kuwa na fikira, mawazo, na dhana mpya zinazozunguka akilini mwako kwaweza kukukengeusha. Hufikiri tena kwa kiwango sahili cha watoto. Sasa akili zako zasukumwa kuchanganua na kusababu juu ya mambo uonayo na kusikia. Elezo la mwalimu au mhadhiri laweza kutokeza ukengeufu wa akili wenye kusisimua. Lakini usipojifunza kudhibiti mawazo yako yanayotangatanga, waweza kupitwa na habari muhimu. Kwa kupendeza, Biblia husema kwamba mwanamume mwadilifu Isaka alitumia wakati akitafakari kwa ukimya. (Mwanzo 24:63) Labda kuweka kando muda fulani kila siku kupumzika, kutafakari, na kutatua mambo fulani kwaweza kukusaidia kukaza fikira nyakati nyingine.

Hisia-Moyo na Homoni

Hisia-moyo zako zaweza pia kuwa chanzo cha ukengeufu. Wajaribu kuwa makini na unayosoma au kusikiliza, lakini wajipata ukifikiria mambo mengine. Wageuka kutoka hali ya uchoshi na msisimko, hadi mshuko-moyo na furaha. Usiwe na wasiwasi! Hupatwi na kichaa. Kuna uwezekano kwamba ni homoni zinazokuletea hali hizo. Unapatwa na mabadiliko ya kubalehe.

Kathy McCoy na Charles Wibblesman waandika hivi: “Kuna hisia nyingi katika miaka ya kubalehe . . . Kwa kiwango fulani, badiliko hili la kihisia ni sehemu ya mbalehe. Kwa kiwango fulani badiliko hili lahusisha mkazo wa mabadiliko yote unayopata sasa.” Isitoshe, unakaribia “mchanuko wa ujana”—wakati tamaa za ngono zinapofikia kilele. (1 Wakorintho 7:36) Mwandishi Ruth Bell asema hivi: “Mara nyingi mabadiliko ya ubalehe hutokeza hisia zenye nguvu za ngono. Waweza kujipata ukifikiri sana juu ya ngono, kushikwa kwa urahisi na tamaa ya ngono, hata nyakati nyingine ukifikiria tu ngono.”b

Jesse, aliyenukuliwa mwanzoni mwa makala hii, huacha akili zake zitangetange kama ilivyo kawaida na matineja wengi: “Nyakati nyingine mimi hufikiri juu ya wasichana au wasiwasi fulani nilio nao au nitakalofanya baadaye.” Hatimaye, hizo hisia nyingi zitatulia. Kwa wakati huu, jaribu kujitia nidhamu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Napiga-piga mwili wangu ngumi na kuuongoza kama mtumwa.” (1 Wakorintho 9:27) Kadiri ujifunzavyo kudhibiti hisia-moyo zako, ndivyo utakavyoweza kukaza fikira zaidi.

Mazoea Yako ya Kulala

Mwili wako unaokua unahitaji usingizi wa kutosha ili kukusaidia kukua kimwili na kuruhusu akili yako ichanganue fikira na hisia nyingi unazokumbana nazo kila siku. Hata hivyo, matineja wengi huwa na shughuli nyingi zinazowafanya wasipate wakati wa kutosha wa kulala usingizi. Mtaalamu mmoja wa neva aeleza hivi: “Mwili hauwezi kusahau kudai mtu saa za usingizi unaohitaji. Na sikuzote mwili utakumbuka na kumtaka mtu alipie gharama hiyo ambayo yaweza kuwa usahaulifu, matatizo ya kukaza fikira, na kufikiri polepole.”

Watafiti fulani huamini kwamba kuongeza saa moja tu au zaidi ya usingizi kila siku kwaweza kuboresha uwezo wa mtu wa kukaza fikira. Ni kweli kwamba Biblia hulaumu uvivu na kupenda usingizi. (Mithali 20:13) Hata hivyo, ni jambo linalofaa kupumzika vya kutosha ili kutenda kwa njia bora.—Mhubiri 4:6.

Mlo na Kukaza Fikira

Tatizo jingine laweza kuwa mlo. Vyakula vyenye mafuta na sukari nyingi hupendwa sana na vijana. Watafiti wanasema kwamba ingawa vyakula visivyo na lishe bora huenda vikawa na ladha nzuri, hupunguza uwezo wa akili wa kushika mambo. Hali kadhalika utafiti huonyesha kwamba utendaji wa akili hupungua baada ya mlo wa wanga, kama vile mkate, nafaka, mchele, au pasta. Huenda hii ikawa ni kwa sababu wanga huongeza kiwango cha kemikali iitwayo serotonin katika akili na kumfanya mtu asinzie. Hivyo watafiti fulani wa lishe hupendekeza kula vyakula vyenye protini nyingi kabla ya kujihusisha na utendaji wowote unaohitaji akili kuwa chonjo.

Kizazi cha Televisheni na Kompyuta

Kwa miaka mingi walimu wamehisi kwamba televisheni na picha zake zenye kusonga haraka-haraka hupunguza muda wa kukazia uangalifu wa vijana, na wengine sasa wanalaumu kompyuta. Ingawa kuna mjadala mkubwa miongoni mwa wataalamu kuhusu namna hasa tekinolojia ya kisasa inavyowaathiri vijana, kutumia muda mwingi kupita kiasi katika kutazama televisheni au kucheza michezo ya kompyuta si jambo zuri kamwe. Kijana mmoja akiri hivi: “Tukiwa na vitu kama vile michezo ya vidio, kompyuta, na Internet, sisi watoto tumezoea kupata tunachohitaji upesi.”

Tatizo ni kwamba mambo mengi maishani hupatikana tu kupitia jitihada, uvumilivu, na kwa saburi ambayo wengine huona kuwa sifa ya kikale. (Linganisha Waebrania 6:12; Yakobo 5:7.) Kwa hiyo usidhani kamwe kwamba lazima mambo yaende haraka-haraka na yaburudishe ili yawe yenye mafaa. Ingawa kutazama televisheni na kucheza michezo ya kompyuta kwaweza kuburudisha, kwa nini usipake rangi, uchore, au ujifunze kucheza ala ya muziki? Stadi za namna hiyo zaweza kuzidisha nguvu zako za kukaza fikira.

Je, kuna njia nyinginezo ambazo zinaweza kukuza uwezo wako wa kukaza fikira? Kwa kweli, ziko, na makala moja ya wakati ujao itachunguza baadhi yake.

[Maelezo ya Chini]

a Ona matoleo ya Amkeni! ya Novemba 22, 1994, ukurasa wa 3-12; Juni 22, 1996, ukurasa wa 11-13; na Februari 22, 1997, ukurasa wa 5-10.

b Ona makala “Vijana Huuliza . . . Naweza Kuachaje Kufikiria Watu wa Jinsia Tofauti?” katika toleo letu la Agosti 8, 1994.

[Blabu katika ukurasa wa 20]

Watafiti wanasema kwamba vyakula visivyo na lishe bora, hupunguza uwezo wa akili wa kushika mambo

[Blabu katika ukurasa wa 20]

“Nyakati nyingine mimi hufikiri juu ya wasichana au wasiwasi fulani nilio nao”

[Picha katika ukurasa wa 19]

Je, mara nyingi wewe hupata ugumu wa kukazia uangalifu darasani?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki