Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 12/8 kur. 8-11
  • Yesu Alivyo Sasa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yesu Alivyo Sasa
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Isemavyo Biblia
  • Mtawala Mwenye Huruma
  • Yesu Sasa Ni Mfalme “Mzuri Sana”
  • ‘Kuvuna Tufani’
  • Watu Wenye Mioyo ya Haki Wajifunza Kweli
  • Kusudi la Mungu Lasonga Kuelekea Utimizo
    Je, Kweli Mungu Anatujali?
  • Ufalme wa Mungu—Utawala Mpya wa Dunia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Yesu Kristo Ni Nani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • ‘Ule Ufalme Umekaribia’
    “Ufalme Wako Uje”
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 12/8 kur. 8-11

Yesu Alivyo Sasa

INGAWA tunapendezwa na jinsi Yesu alivyofanana, ni muhimu zaidi kujua yeye ni nani sasa na mahali alipo. Yeye anatimiza fungu gani katika kusudi la Mungu kuelekea familia ya kibinadamu?

Hatuwezi kupata majibu kutoka kwa historia ya kilimwengu. Majibu yaweza kupatikana tu katika hati iliyotungwa na Mungu kwa manufaa ya watafutao kweli. Nayo ni Biblia Takatifu, au Maandiko Matakatifu, buku ambalo limeenezwa sana katika historia ya ulimwengu.

Biblia si kitabu kingine tu kilichotungwa na wanadamu. Ingawa wanadamu walitumiwa kuandika, Mungu ndiye mtungaji halisi: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 Timotheo 3:16, 17.

Mtume Paulo alitambua Maandiko, kwani aliandika: “Mlipopokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali, si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.

Mungu ndiye Muumba mwenye nguvu zote wa ulimwengu wenye mabilioni ya magalaksi na mabilioni ya nyota katika kila galaksi. Ana nguvu zenye kutisha kama nini kumwezesha kuumba vitu hivyo vyote! Kwa kweli Mweza Yote, aliyeumba ulimwengu wenye kustaajabisha, angeweza kutunga kitabu ambacho kingekuwa mwongozo wenye kutegemeka kwa yeyote anayetafuta kweli.

Isemavyo Biblia

Neno la Mungu hufunua nadharia nyingi na makisio mengi kuhusu Yesu. Ona baadhi ya habari inayotoa kumhusu:

• Yesu alikuwa kiumbe cha kwanza na cha pekee kuumbwa moja kwa moja na Mungu katika mbingu miaka mingi iliyopita, kabla ya malaika na ulimwengu wa asili. Ndiyo sababu anaitwa “Mwana mzaliwa-pekee” wa Mungu. Viumbe vingine vyote viliumbwa kupitia Mwana huyu, “stadi wa kazi” wa Mungu, kabla hajawa binadamu.—Yohana 3:16; 6:38; 8:58; Mithali 8:30; Wakolosai 1:16.

• Miaka ipatayo 2,000 iliyopita, Mungu aliuhamisha uhai wa Yesu hadi kwenye tumbo la uzazi la bikira Myahudi, ili azaliwe akiwa binadamu. Hata sasa, kwa kutumia njia za kuzalisha kwa chupa, wanadamu wanaweza kufanya jambo ambalo kwa njia fulani linakaribia hili.—Mathayo 1:18; Yohana 1:14.

• Yesu hakuwa mtu mwema tu. Akiwa mtu mzima, alidhihirisha kikamilifu utu wa Baba yake wa kimbingu, Yehova Mungu, wenye upendo, huruma, na uadilifu.—Yohana 14:9, 10; Waebrania 1:3; 1 Yohana 4:7-11, 20, 21.

• Akiwa mwakilishi wa Mungu duniani, Yesu alihangaikia mahitaji ya maskini na walioonewa, na bado hakuwabagua matajiri. Akitegemezwa na roho takatifu ya Mungu yenye nguvu nyingi, Yesu aliwaponya wagonjwa kimwujiza na hata akafufua wafu. Kwa kufanya kazi hizo zenye kustaajabisha, alionyesha kwa kiwango kidogo yale ambayo angefanya duniani pote baada ya kufufuliwa kutoka kwa wafu hadi kwenye uhai wa kimbingu na kuwa Mfalme wa Ufalme wa kimbingu wa Mungu.—Mathayo 11:4-6; Luka 7:11-17; Yohana 11:5-45.

• Ufalme huo wa kimbingu ndio Yesu aliwafundisha wafuasi wake wauombee na kuutanguliza maishani mwao. Utakaposimamishwa kabisa, “utavunja falme hizi [zilizopo leo] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” Kisha, Ufalme huo utakuwa serikali ya pekee ya dunia. Ndio tumaini pekee kwa wanadamu wanaotaabika.—Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10.

• Mungu alikuwa Baba ya Yesu na Yesu alikuwa mwaminifu kwa Mungu. Hivyo, Yesu alipouawa, alikuwa mwanadamu mkamilifu. Alitoa kwa utayari uhai wake mkamilifu kwa Mungu kuwa dhabihu ya fidia ili kukomboa kile ambacho Adamu alipoteza alipomwasi Mungu. Kwa kufanya hivyo, Yesu alifungua njia kwa ajili ya uhai wa milele kwa wote wanaodhihirisha imani katika yeye.—Yohana 3:16; Waroma 3:23, 24; 1 Yohana 2:2.

• Akiwa mfalme wa kimbingu aliyewekwa rasmi na Mungu, Yesu atatekeleza kusudi la Mungu la kuondoa uovu duniani na kuinua wanadamu watiifu kwenye ukamilifu wa akili na mwili. Kisha wanadamu wataishi kwa amani na furaha kwenye dunia paradiso, wakiwa na makao mazuri na chakula cha kuwatosha wote. Ugonjwa, majonzi, na kifo zitatoweka milele. Hata wafu watafufuliwa na kupata fursa ya kuishi milele duniani.—Mwanzo 1:26-28; 2:8; Zaburi 37:10, 11, 29; Mithali 2:21, 22; Isaya 25:6; 65:21-23; Luka 23:43; Matendo 24:15; Ufunuo 21:3, 4.

Hivyo, Biblia hutuambia waziwazi kwamba Yesu ndiye mwenye daraka kuu katika kusudi la Mungu la kusimamisha ulimwengu wenye uadilifu hapa duniani. Kwa sababu ya daraka muhimu alilo nalo, kwa kufaa Yesu angeweza kusema hivi: “Mimi ndiyo njia na kweli na uhai. Hakuna ajaye kwa Baba ila kupitia mimi.”—Yohana 14:6; 2 Petro 3:13.

Mtawala Mwenye Huruma

Watu wanyenyekevu wanataka Yesu awe mtawala wao katika ulimwengu mpya, jinsi atakavyokuwa mtawala tofauti na mwenye kupendeza! Njia moja aliyoonyesha hivyo ni kupitia kazi zenye kustaajabisha za maponyo alizofanya alipokuwa hapa duniani. (Mathayo 15:30, 31) Lakini, ona pia, atakuwa mtawala wa aina gani.

Kwanza fikiria rekodi ya watawala wa ulimwengu huu. Historia inaonyesha kwamba katika karne ambazo zimepita, mara nyingi wamekuwa wakatili bila huruma, wakiingiza watu wao kwenye vita, ukatili, mateso, na mauaji ya kinyama chungu nzima. Katika karne hii ya 20 pekee, zaidi ya watu milioni 100 wameuawa vitani.

Tofautisha mtazamo huo na rekodi ya watawala wa ulimwengu huu na mtazamo na rekodi ya Yesu katika kushughulika na maskini, wenye kuonewa, wanyonge na kadhalika: “Alipouona umati alihisi sikitiko kwa ajili yao, kwa sababu ulikuwa umechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” Hivyo akawaambia: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha nyinyi. Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni ya fadhili na mzigo wangu ni mwepesi.”—Mathayo 9:36; 11:28-30.

Jinsi Yesu alivyokuwa mwenye huruma kuelekea watu! Katika habari hii aliiga Baba yake wa kimbingu. Yesu alikuwa wonyesho halisi wa upendo, na aliwafundisha wanafunzi wake wawe na upendo wa kweli unaoongozwa na kanuni kwa mtu na mwenzake. Kwa hiyo hawangeruhusu jamii, taifa, hali ya maisha, dini ya hapo awali, au kitu chochote kihitilafiane na muungano wao wa kimataifa. (Yohana 13:34, 35; Matendo 10:34, 35) Kwa kweli, Yesu aliwapenda sana watu hivi kwamba akatoa uhai wake kwa ajili yao. (Waefeso 5:25) Ndiye mtawala ambaye ulimwengu huu unahitaji na utapata.

Yesu Sasa Ni Mfalme “Mzuri Sana”

Neno la kiunabii la Mungu hutusaidia kuelewa kwamba sasa Yesu ni Mfalme wa kimbingu mwenye nguvu. Mtunga-zaburi alitabiri hivi kumhusu: “Wewe u mzuri sana kuliko wanadamu; . . . Katika fahari yako usitawi uendelee kwa ajili ya kweli na upole na haki . . . Umeipenda haki; umeichukia dhuluma. Kwa hiyo MUNGU, Mungu wako, amekupaka mafuta, mafuta ya furaha kuliko wenzako.”—Zaburi 45:2, 4, 7.

Akiwa Mfalme wa kimbingu aliyetiwa mafuta na Mungu, Yesu amepewa utume wa kuchukua hatua ya kudhihirisha kupenda kwake uadilifu na kuchukia kwake uovu. Hivyo, katika Biblia anasimuliwa kuwa mshindi asiyeweza kufa, “Mfalme wa wafalme,” ambaye karibuni atafisha maadui wote wa Mungu. Isitoshe, atairudisha dunia kuwa paradiso na kuinua wanadamu wanaoweza kukombolewa hadi kwenye ukamilifu.—Ufunuo 19:11-16.

Daraka jipya la Yesu halitakuwa lile la ‘Mesiya anayeteseka’ ambaye anadhihakiwa, kupigwa, na kuuawa na wapinzani. Badala ya hivyo, daraka lake jipya ni lile la “Mungu mwenye nguvu,” mtawala wa dunia. (Isaya 9:6) Habari hizi hazifurahiwi na watawala wengi wa kibinadamu, kwa kuwa hivi karibuni falme zao zitaharibiwa zisiwemo, kama itabiriwavyo kwenye Danieli 2:44. Akitumia Kristo kuwa mfishaji wake, Mungu ‘ataseta wafalme siku ya ghadhabu yake. Atahukumu kati ya mataifa.’—Zaburi 110:5, 6.

Isaya alitabiri kwamba kwa kufanya hivi, Kristo ‘atawastusha mataifa mengi. Wafalme watamfumbia vinywa vyao.’ Kwa nini? “Maana mambo wasiyoambiwa [na wasiri wao wa kidini] watayaona; na mambo wasiyoyasikia watayafahamu.”—Isaya 52:15.

‘Kuvuna Tufani’

Isaya alikuwa akitabiri hali ya viongozi wa kidini kuachilia daraka. Mathalani, hawafundishi kweli ya Biblia na badala yake wanafundisha makundi yao mafundisho yasiyokuwa ya Kimaandiko kuhusu kuteswa milele katika helo yenye moto, utatu wa miungu watatu katika mmoja, na kutokufa kwa nafsi—yote yakiwa ya kipagani. Na makasisi wameunga mkono vita vyote vya mataifa yao, hata ilipomaanisha kuua watu wa dini yao wenyewe. Jambo hili hukiuka amri za Mungu moja kwa moja.—1 Yohana 2:3, 4; 3:10-12; 4:8, 20, 21.

Pia makasisi hutolea makundi yao vitu ambavyo huenda vikavutia lakini ambavyo ni bure machoni pa Mungu kama vile, sanamu za kidini, mavazi ya makasisi, makanisa ghali sana, na michoro iliyorembwa kwa dhana za kipagani, kutia ndani nuru inayozunguka picha ya mungu-jua. Wamefanya mambo haya licha ya amri hii ya Mungu kwa watumishi wake: “Nendeni zenu, nendeni zenu, tokeni huko, msiguse kitu kichafu . . . , ninyi mnaochukua vyombo vya BWANA.”—Isaya 52:11; 2 Wakorintho 6:14-18.

Wale wanaodai kumwakilisha Mungu lakini ambao hukiuka amri zake na kufundisha wengine wafanye hivyo hivyo, watavuna walichopanda. Watahukumiwa adhabu na watatozwa hesabu mfumo huu wa mambo utakapoharibiwa. Kama alivyosema nabii Hosea, “wamepanda upepo, na watavuna tufani.”—Hosea 8:7, King James Version; ona pia Ufunuo 17:1-3, 15, 16.

Watu Wenye Mioyo ya Haki Wajifunza Kweli

Hali ya makasisi kuwapotosha watu juu ya Mungu na Yesu haitazuia watu wenye mioyo ya haki wasijifunze kweli juu ya Yesu. Katika karne ya kwanza, haikuwazuia, kwa kuwa kama alivyoandika Paul Barnett katika kitabu chake The Two Faces of Jesus, “Kristo si mtu arukaye kwa mwavuli aliyeanguka tu kutoka angani na kujipata katika historia bila kutangazwa.” Naam, huko nyuma unabii wa Biblia ‘ulitangaza’ Mesiya kwa usahihi, ukiwahakikishia wanafunzi wake waaminifu-washikamanifu kuja kwake. Leo kuna uthibitisho mwingi zaidi unaotangaza uhakika wa kwamba Yesu amepewa mamlaka na Mungu ya kutawala akiwa “Mfalme wa wafalme” wa kimbingu mwenye utukufu.—Mathayo 24:3-13; 2 Timotheo 3:1-5, 13.

Kwa kweli, “habari njema hii ya ufalme [wa Mungu Kristo akiwa mtawala] itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Hilo linafanywa na Mashahidi wa Yehova, ambao sasa ni zaidi ya milioni tano ulimwenguni pote. Kwa hiyo wale wanaotaka kumjua Yesu wa kweli, kwa kweli wanaweza kumjua. (Yohana 10:14; 1 Yohana 5:20) Kumjua na kumtii ni kwa maana ili kuokoka “dhiki kubwa” itakayokumba dunia hivi karibuni.—Ufunuo 7:9-14; Yohana 17:3; 2 Wathesalonike 1:6-10.

Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova watapendezwa kukusaidia uchunguze ufafanuzi wa Biblia wenye kuvutia juu ya Mwana wa Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Katika mamlaka ya Ufalme Kristo atafuta kabisa uovu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Dunia hii itakuwa paradiso, chini ya utawala wenye upendo wa Kristo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki