Aimarishwa na Imani Yake
MSICHANA mmoja mwenye umri wa miaka 17 aliandikia ofisi ya Watch Tower Society katika Moldova, iliyokuwa jamhuri ya Muungano wa Sovieti, ili kuweza kuonyesha uthamini wake kwa ajili ya makala iliyokuwa katika Amkeni! la Juni 8, 1998. Kichwa cha makala hiyo kilikuwa “Uchaguzi Wangu Kati ya Baba Wawili,” na ilisimulia mambo yaliyompata kijana mmoja Mwarmenia.
“Nilipokuwa nikisoma makala hiyo,” msichana huyo aeleza, “nilitoa machozi sana kwa sababu mambo yaliyompata ni sawa na yaliyonipata.” Yeye aliendelea kuandika: “Nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilianza kujifunza Biblia, na wazazi wangu hawakupinga mwanzoni. Lakini nilipoanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, walipinga kwa dhati. Kisha, mwaka wa 1997, nilipoanza kushiriki na wengine mambo niliyokuwa nikijifunza wakaniambia hivi: ‘Nenda kwa rafiki zako Mashahidi ili wakulishe, wakununulie mavazi, na wakupe kazi. Wewe ni binti asiyetii!’ Wazazi wangu walinichapa pia, wakikigongesha kichwa changu ukutani.
“Hilo lilikuwa jaribu kali kwangu. Mara nyingi nilihisi kama kijana huyo Mwarmenia, aliyesema kwamba nyakati fulani alikuwa na shaka iwapo Yehova alipendezwa naye. Nilijiuliza, ‘Je, kweli mimi sifai kitu? Je, Yehova atasamehe dhambi zangu za awali? Je, kweli Yehova angali ananipenda?’
“Ulikuwa wakati mgumu sana, hasa nilipodhani kwamba Yehova hakunipenda tena kamwe. Nilimsihi sana Yehova katika sala, kwa machozi, anisaidie na kuniimarisha ili nisimwache kamwe. Na, kwa kweli, niliona kwamba Yehova alisikiliza sala zangu na akajibu dua zangu. Aliniimarisha, na kunipa ushupavu na ujasiri. Na alifanya hivyo kupitia Neno lake hasa, ambamo mtunga-zaburi alitangaza hivi kwa uhakika: ‘Baba yangu na mama yangu wakiniacha, BWANA atanikaribisha kwake.’—Zaburi 27:10.
“Nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa kubatizwa Septemba 27, 1997, katika kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova huko Kagul. Naona waziwazi kwamba Yehova, Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo, anatimiza ahadi yake iliyoandikwa katika Zaburi 84:11: “BWANA, Mungu ni jua na ngao, BWANA atatoa neema na utukufu. Hatawanyima kitu chema hao waendao kwa ukamilifu.”
“Ninamshukuru sana kijana huyo Mwarmenia aliyetoa simulizi lake lenye kuimarisha imani katika gazeti la Amkeni! Ninatumaini kwamba hatimaye wazazi wangu na wazazi wake watapendezwa na mafundisho ya Biblia.”