Sura ya 4
Ufalme ‘Waja’—kutoka Wapi?
1. Kwa kutegemea 1 Timotheo 1:17 na Ufunuo 15:3, ni maulizo gani ya maana yanayoulizwa?
KWA kuwa Biblia inasimulia kuwa Yehova ndiye “Mfalme wa umilele,” sababu gani ni lazima ufalme “uje” kutakasa jina lake? (1 Timotheo 1:17; Ufunuo 15:3, NW) Na unakuja kutoka wapi?
2. Ni hali gani katika serikali zimeleta suto juu ya jina la Mungu, na kwa njia gani?
2 Kwanza, ni wazi kwamba ni lazima badiliko kubwa litokee ili kurudisha uadilifu, amani na furaha kwenye dunia hii. Serikali moja moja hazikushindwa tu kutimiza masilahi ya raia zao katika njia nyingi, bali pia mataifa yamo katika msukosuko yenyewe kwa yenyewe. Chuki, mashindano na utukuzo wa taifa unagawanya watu na jamii mbalimbali. Hali hizo zinasingizia vibaya sana lile kusudi la Muumba na zimefanya masuto mengi yalundikwe juu ya jina lake.—Warumi 2:24; Ezekieli 9:9.
3. (a) Ufalme wa Mungu ‘unakujaje’ katika habari hii? (b) Lililo la pekee sana juu ya Ufalme huo ni nini?
3 Ili kusahihisha hali hiyo, serikali ya pekee sana inahitajiwa. Na hiyo ndiyo Yehova anaandaa. Inakuja kutoka wapi? Kutoka kwa Yehova mwenyewe, anayekaa katika mbingu. Ni ufalme wenye kutegemea mamlaka fulani unaoonyesha enzi kuu ya ulimwengu mzima ya Yehova mwenyewe. Inapata mamlaka kutoka kwa uufalme ambao Yehova ametumia tangu mwanzo, zamani kabla ya kuumbwa kwa mbingu na dunia yetu. Kwa kuwa unazaliwa kutoka tengenezo la kimbingu la Mungu, serikali hiyo ya kimungu iliyo ya pekee sana inarithi tabia za ajabu za enzi kuu ya zamani sana ya Yehova.—Ufunuo 12:1, 2, 5.
ENZI KUU YA ULIMWENGU MZIMA YA YEHOVA
4. Ni usemi gani katika Ufunuo 4:11 unaoisimulia vya kufaa enzi kuu ya Yehova?
4 Kwa sababu ‘aliumba vitu vyote,’ Mungu ndiye Mwenye Enzi Kuu aliye na haki hiyo juu ya viumbe vyote vilivyopo. Hata wale ambao Mungu anakweza kwenye uufalme katika mbingu lazima ‘waanguke mbele ya Yeye anayeketi katika kiti cha enzi na kuabudu Yeye anayeishi milele na milele.’ Hao wanaikubali kwa unyenyekevu ile enzi kuu zaidi ya “Mfalme wa umilele”—kama masimulizi haya zaidi juu yao yanavyoonyesha:
“Nao wanayatupa mataji yao mbele ya kiti cha enzi, wakisema: ‘Wewe unastahili, Yehova, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na uwezo, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vikawako na vikaumbwa.’ ” (Ufunuo 4:10, 11, “NW”; Waefeso 3:9)
Je! hayo ndiyo maoni yako juu ya enzi kuu ya Mungu? Yamepasa kuwa hivyo.
5. Ukilinganishwa na serikali za kibinadamu, uufalme wa Yehova unaunganisha mambo yote namna gani?
5 Kati ya wanadamu ufalme unaongoza kulingana na sheria. Hilo ni jambo la lazima kwa kudumisha utengemano. Kwa kawaida, serikali zinakuwa na mahakimu wanaoamua kesi mahakamani, mabunge ya kutunga sheria, na mfalme au rais anayetekeleza sheria. Katika ulimwengu mzima alioumba, Yehova Mungu anajazia afisi tatu zote hizo, kama vile nabii Isaya anavyoonyesha, akisema: “Yehova ni Hakimu wetu, Yehova ni Mpaji-sheria wetu, Yehova ni Mfalme wetu.” (Isaya 33:22, NW) Na kwenye jambo hilo Mfalme Daudi anaongeza maneno haya: “[Yehova] ameweka kiti chake cha enzi mbinguni, na ufalme wake unavitawala vitu vyote.” (Zaburi 103:19) Na tuchunguze sehemu fulani za uufalme huo.
SHERIA ZA ULIMWENGU MZIMA ZA MUNGU
6. Ni nini kinachoonyesha ubora wa sheria za Mungu?
6 Serikali za wanadamu zinatafuta kuongoza matendo ya raia zao za kibinadamu, lakini haziwezi kuongoza kani za asili zinazovuta sana maisha zao. Yehova, Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Mzima, anaweza, na anaziongoza. Mara nyingi wanasayansi wamestaajabia usahihi wa sheria zinazoendelea kuuongoza ulimwengu mzima unaoonekana. Hizo ni sheria za Mungu. Kwa sababu sheria hizo zinatumika bila kubadilika-badilika wanadamu wameweza kutua juu ya mwezi, wakapeleka habari kupitia setilaiti, wakaweza kutabiri kupatwa kwa mwezi na kwa jua na kubuni maelfu ya vitu vyenye mambo magumu-magumu. Sheria za Mungu pia zinaongoza jua na mvua, naye anaweza kurekebisha vitu hivyo viwe baraka kwa wale wanaomtii.—Zaburi 89:8, 11-13; Ayubu 38:33, 34: Zekaria 14:17.
7. (a) Sheria za Yehova zinashuhudiaje uungu wake? (b) Kama Ayubu, imetupasa tuzioneje njia za Mungu?
7 Kwa habari ya mpango wa ajabu wa vitu vya kimbingu, nabii wa Mungu anasema: “Inueni macho yenu juu sana na kuona. Ni nani ameumba vitu hivi? Ni Yeye anayetokeza jeshi lavyo hata kwa hesabu, navyo vyote huviita hata kwa jina. Kwa sababu ya wingi wa nishati zenye msukumo, yeye akiwa pia mwenye kutenda kwa uwezo, hakuna kimoja chavyo kinachokosekana. Je! wewe hujapata kujua au hujapata kusikia? Yehova, Muumba wa ncha za dunia, ni Mungu kwa wakati usiojulikana.” (Isaya 40:26, 28, NW) Katika mabilioni ya miaka Yehova ameongoza ulimwengu wake mzima ulio mkubwa mno kwa kutumia zile zinazoitwa sheria “za asili” (maumbile). Wanadamu wamejaribu kufumbua siri za sheria hizo, lakini kuna nyingi sana ambazo hawajajifunza bado! Wameendelea mbele kidogo tu kuliko yule mwanamume mwaminifu wa miaka 3,500 iliyopita, aliyetangaza hivi: “Tazama! Hizo ndizo taraza za njia zake, na jambo ambalo limesikiwa juu yake ni mnong’ono mdogo kama nini! Lakini kwa habari ya mngurumo wake mkubwa nani anaweza kuonyesha ufahamu?”—Ayubu 26:14, NW.
8. Ni sifa gani nyingine za Mungu zinazochanganyikana, kuonyesha yeye ni Mwandalizi Mkuu?
8 Walakini, katika kuumba dunia yetu, Yehova alifanya mengi zaidi ya kuiimarisha juu ya msingi wa sheria zake za asili. Hekima yake isiyo na mwisho na upendo wake usiopimika yalichanganywa pamoja na uwezo wake na sheria zake katika kufanya matayarisho ya ajabu ya wakaaji wa dunia ambao wangetokea baadaye. Ni akili yenye fadhili kama nini, ni ufundi wenye uhodari kama nini, unaoonwa katika kazi za Mungu za uumbaji hapa duniani! (1 Yohana 4:8; Zaburi 104:24; 145:3-5, 13) Kama tulivyoangalia katika sura moja iliyotangulia, Yehova ndiye Mwandalizi Mkuu kweli kweli!
9. Ni baadhi ya mambo gani tunayopaswa tumshukuru Mungi kwayo?
9 Imetupasa tumshukuru Mungu kwa maandalizi yake yote ya ajabu. Pia, imetupasa tumshukuru kwa jinsi alivyotubuni na kutufanya sisi wanadamu, tukiwa na uwezo wetu wa mwili na wa akili na hisia zeta ambazo kwazo tunaweza kuona upendezi katika viumbe vyake. Ndiyo, imetupasa tuwe tayari kumwambia Mungu kama mtunga zaburi: “Nitakusifu wewe kwa sababu kwa njia yenye kutia hofu mimi nimeumbwa kiajabu. Kazi zako ni za ajabu, kama nafsi yangu inavyojua sana. Mifupa yangu hukufichwa wewe wakati mimi niliumbwa kwa siri, wakati katika sehemu za chini za dunia. Macho yako yaliona hata kiinitete cha mimi, na katika kitabu chako [cha mpangilio] sehemu zake zote zilikuwa zimewekwa katika mwandiko, kwa habari za siku zile zilipofanywa na bado kulikuwa hakuna moja miongoni mwazo.”—Zaburi 139:14-16, NW.
10. Ni nini kinachoonyesha Yehova anaweza sana kunyosha mambo duniani?
10 Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu, aliyeuumba ulimwengu mzima na vitu vyote vilivyomo, akaimarisha mifumo ya mambo katika upendo na hekima yake, na kulingana na sheria zake za uadilifu, ndiye pia Biblia inasema juu yake: “Uadilifu na hukumu ndiyo mahali imara pa kiti cha enzi chako; fadhili za upendo na ukweli zenyewe huingia mbele za uso wako.” (Zaburi 89:14, NW) Bila shaka Yehova yuko katika hali ya kutokeza serikali ya Ufalme itakayonyosha mambo katika dunia hii. (Zaburi 40:4, 5) Lakini atafanyaje hivyo?
KUFUNUA SIRI
11. (a) Sababu gani imetupasa leo tufurahi kwa vile maarifa ya kweli yanapatikana? (b) Tunaweza kumtam buaje “Mikaeli,” na jina lake na maana gani?
11 Katika Biblia tunapata unabii mwingi unaotaja kusimamishwa kwa ufalme utakaotakasa jina lake na kutendesha mapenzi yake hapa duniani. Mmoja ni ule unabii wa Danieli, unaotaja “wakati wa mwisho” ambapo “maarifa [ya kweli] yataongezeka.” Tunaweza kuwa wenye furaha kwamba leo tunayo maarifa hayo. Maana Danieli anatuambia hivi:
“Kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo; na wakati huo watu wako wataokolewa.”
Kama Danieli anavyoeleza, hiyo itakuwa wakati yule Mikaeli aliye mwana-mfalme mkuu atakaposimama kwa ajili ya kutetea watu wa Mungu. Biblia inatambulisha Mikaeli kuwa Yesu Kristo, anayepigana vita juu ya maadui wa Mungu ili alitakase jina la Yehova. Basi, kwa kufaa, jina “Mikaeli” maana yake “Ni Nani Aliye Kama Mungu?” maana ni Mikaeli anayethibitisha kwamba hakuna mtu anayeweza kupinga enzi kuu ya Yehova na kufaulu.—Danieli 12:1, 4; Ufunuo 12:7-10.
12. Ile ndoto katika Daniel 2:31-33 inafananisha nini, na sababu gani itupendeze leo?
12 Pia unabii wa Danieli unasimulia ndoto ya Mfalme Nebukadreza wa Babuloni, ndoto juu ya mfuatano wa falme. Upesi mfalme huyo alisahau ndoto ilivyokuwa, ijapokuwa iliendelea kumsumbua sana. Mwishowe, “yeye afunuaye siri,” Yehova Mungu, akamtumia Danieli amjulishe mfalme si ile ndoto tu bali pia tafsiri yake. (Danieli 2:29) Kwa kuwa utimizo wa ndoto hiyo ya kiunabii unaendelea mpaka wakati wetu na baada yake, imetupasa tupendezwe sana na maana yake. Ndoto hiyo ilikuwa juu ya “sanamu kubwa sana” ya umbo la kibinadamu—yenye sura ya kuogopesha sana. Unaweza kuisoma katika Danieli 2:31-33. Sanamu hiyo inafananisha nini
13. Zile sehemu mbalimbali za ile sanamu zinafananisha nini?
13 Danieli alimjulisha Nebukadreza kwamba kichwa chayo cha dhahabu kilifananisha yule “mfalme” wa Babuloni, na kwamba zile sehemu za chini za mwili wayo zilifananisha falme nyingine ambazo zingetokea baada ya Babuloni. Leo, tunaweza kuzifahamu hizo kuwa tawala zenye nguvu za Umedi na Uajemi, Ugiriki na Roma, nayo “miguu” ikishuka chini mpaka kuwa Serikali ya Ulimwengu ya mwungano wa sasa wa Uingereza na Amerika. Lakini namna gani zile nyayo za miguu zenye kufanyizwa “kuwa nusu udongo wa mfinyanzi, na nusu chuma”? Miaka ya karibuni, vyama vya kisoshalisti (kiujamaa) vyenye kupendwa na watu wengi vimepunguza sana nguvu ya mamlaka iliyo kama chuma katika Serikali ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika, kama vile nyayo za miguu ya hiyo sanamu kubwa sana zilivyofanywa kuwa zenye kuvunjika upesi kwa “vile chuma kisivyoshikamana na udongo.” Kwa hiyo, sanamu hiyo yenye kuogopesha sana inafananisha “wafalme” wa kibinadamu wenye kufuatana, au mamlaka za ulimwengu zitakazokoma wakati ufalme wa Mungu utakapoziharibu. —Danieli 2:36-44.
14, 15. Lile “jiwe” linaifanya nini sanamu, na tunaweza kutambuaje “jiwe” hilo?
14 Maana, tazama! “Jiwe” lachongwa kimwujiza kutoka mlima, “bila kazi ya mikono.” Hakuna chombo kionekanacho cha kibinadamu kinachosababisha tendo hilo. Badala yake, Yehova mwenyewe analitokeza, kulingana na mapenzi yake matakatifu. Likienda vurururu kuielekea ile sanamu yenye nguvu, jiwe hilo laipiga pa! kwenye nyayo. Linausaga tikitiki mwundo mzima huo wa utawala wa kibinadamu, hata masalio yanatawanywa kama vile makapi mbele ya upepo. Ndipo jiwe lenyewe lageuka kuwa mlima mkubwa unaoijaza dunia nzima.—Danieli 2:34, 35.
15 “Jiwe” hilo lingeweza kuwa nini? Unabii huo unaondoa mashaka yote unapoeleza hivi:
“Katika siku za wafalme hao [yaani, Serikali ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika na masalio yaliyopo ya zile serikali za ulimwengu ambazo zimetangulia hiyo] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.
16. Katika kusali, “Ufalme wako uje,” ni mambo gani tunayoomba?
16 Hiyo ina maana gani kwetu leo? Maana yake ni kwamba tunapoomba ufalme wa Mungu “uje,” kwa kweli tunaomba ufalme huo wa kimbingu utumie nguvu zake za uharibifu uziponde-ponde serikali zote zilizofanywa na wanadamu, ambazo zimeshindwa sana kuleta amani na ufanisi. Inafurahisha kwamba, “jiwe” hilo litakapomaliza kazi ya kuharibu, lenyewe litakua liwe mlima wa kiserikali utakaoijaa dunia nzima. Litaleta amani ambayo wanadamu hawajapata kuijua tangu siku za Mfalme Sulemani, “wingi wa amani mpaka mwezi utakapokuwa haupo”—maana yake milele!—Zaburi 72:7, NW.
17. (a) Sababu gani uhusiano wa lile “jiwe” na ule “mlima” linakotoka umepasa utupe uhakika? (b) Ni hatua gani zaidi ambayo Ufalme huo unachukua? (c) Kama inavyoelezwa katika Zaburi 85:8-12, ni uhakika gani ambao tumepaswa kuwa nao?
17 Walakini, namna gani “mlima” ambao katika huo “jiwe” hilo la Ufalme linachongwa? (Danieli 2:45) Ni lazima “jiwe” hilo liwe linategemea kitu fulani, na kufanyizwa kwa kitu kile kile kama mlima huo, na kwa kweli ndivyo ilivyo. Utawala huo wa Ufalme una chongwa kutoka enzi kuu yote ya Mfalme wa umilele—Yehova Mungu. Kama vile enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu mzima inavyoonyesha sifa zake zote zilizo njema, ndivyo ule ufalme unaochongwa kutoka enzi kuu hiyo unavyopasa kumtukuza Yehova Mungu na makusudi yake yaliyo bora sana. Unatakasa jina lake kwa kuponda-ponda maadui wake, kuonyesha yeye si mshiriki wa matendo yao maovu. Ndipo ufalme huo kupitia Kristo Yesu unaijaza dunia sheria na utengemano, na upendo na furaha, ukiigeuza kuwa mahali penye uadilifu na amani ambapo Mungu alikusudia tangu mwanzo. Kweli kweli, imetupasa tuwe tukiomba huo ‘Ufalme uje’!—Zaburi 85:8-12.