Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • su sura 16 kur. 121-128
  • Wewe Binafsi Utafanya Nini?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wewe Binafsi Utafanya Nini?
  • Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ISHARA AMBAYO MATAIFA YANAGEUKIA
  • ‘WASIKIA LAKINI HAWATENDI’
  • WALIFANYA UAMUZI UNAOFAA
  • Kiongozi Mpya na Wanawake Wawili Jasiri
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
  • Hakuna Kudhuru Wala Kuharibu Katika Paradiso ya Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Wanawake Hodari Wawili
    Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia
  • ‘Nilisimama kama Mama katika Israeli’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
Pata Habari Zaidi
Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
su sura 16 kur. 121-128

Sura 16

Wewe Binafsi Utafanya Nini?

1. Ni uamuzi gani ambao ni lazima ufanywe kibinafsi?

HAKUNA mtu mwingine anayeweza kukufanyia uamuzi wa kumtumikia Yehova. Ikiwa mwenzi wako wa ndoa ni mtumishi mwaminifu wa Mungu, hilo laweza kuwa baraka bora sana. Hali kadhalika, ikiwa wazazi wako wanampenda Yehova, umo katika hali yenye pendeleo. Hali hizo za nyumbani zinaweza kutoa kitia-moyo cha kuelekea kushirikiana na wale wanaomwabudu Yehova “kwa roho na kweli.” (Yohana 4:23, 24) Lakini baadaye ni lazima wewe ufanye uamuzi wa binafsi. Je! wampenda Yehova kweli kweli na wataka kuwa mmoja wa watumishi wake? Je! kweli wataka kuishi katika ulimwengu ambao ndani yake uadilifu utakaa?

2. (a) Kwa nini mwelekeo wa mzazi juu ya kumtumikia Yehova ni wa maana sana? (b) Ni mambo gani matano ambayo wazazi wanaweza kufanya ili wawape watoto wao mwanzo mzuri?

2 Ikiwa wewe ni mzazi, bila shaka wataka watoto wako waje wafurahie baraka ya uzima wa milele chini ya Ufalme wa Mungu. Huwezi kuongoza wanayofanya wanapokuwa watu wazima kujiongozea mwendo wao wenyewe maishani. Lakini yale ambayo wewe binafsi unafanya juu ya ibada ya kweli yanaweza kutumia uvutano wenye nguvu—ama kwa mema ama kwa mabaya. Ikiwa ungekataa kumtumikia Yehova, huko kungewanyima watoto wako kile ambacho kingekuwa nafasi yao bora zaidi ya kuanzishwa katika njia inayoongoza kwenye uzima wa milele. Au ikiwa ungejiweka wakfu kwa Mungu kisha ukose kuishi kulingana nao, hilo lingeongoza kwenye msiba wa kiroho kwa jamaa nzima, na kuja kupata hasara ya kila kitu katika dhiki kubwa. Lakini ukiweka mfano wa kuwa mwaminifu, ikiwa wewe binafsi unasaidia watoto wako wajifunze Neno la Mungu, ikiwa unasitawisha ndani yako na ndani yao upendo kwa Yehova na kuheshimu tengenezo lake linaloonekana, ikiwa unawasaidia wafahamu jinsi wanavyolindwa kwa kufanya mapenzi ya Mungu, ikiwa unawaonyesha jinsi ya kuona furaha katika utumishi mtakatifu, hapo unawapa mwanzo bora sana wa kuingia katika barabara inayoongoza kwenye uzima. Jambo hilo lawezekana kwa baraka ya Yehova tu. (Linganisha 2 Timotheo 1:5.) Toa sala kwa ajili ya hilo bila kukoma. Jitihada nyingi zahitajiwa pia kwako. Lakini yatakayotokea ni yenye kustahili kufanyiwa jitihada kama nini!

3. (a) Ukikabili upinzani kutoka kwa washiriki wa jamaa, unaweza kufanya nini? (b) Lakini namna gani ikiwa upinzani unaendelea?

3 Labda hali inayokukabili ni ya kwamba washiriki wengine wa jamaa yako hawashiriki upendo wako kwa Yehova. Je! wanajaribu kukuvunja moyo ‘usijiingize’? Au kuna upinzani wa moja kwa moja? Ungeweza kufanya nini ili uwasaidie washiriki furaha yako ya kufahamu kusudi la Mungu? Mara nyingi vipingamizi vinaweza kushindwa kwa kuwaalika washiriki wa jamaa yako waende pamoja nawe kwenye Jumba la Ufalme wakajionee yanayotendeka huko. Wanapokuwa huko wangesema na mmoja wa wazee ili wajibiwe maulizo waliyo nayo juu ya imani na mazoea ya Mashahidi wa Yehova. Lakini namna gani ikiwa upinzani unaendelea? Ndipo unahitaji ujiulize hivi: ‘Je! kweli nampenda Yehova na Mwanaye Yesu Kristo na je, ninashukuru sana kwa mambo yote ambayo wametufanyia hata niko tayari kuvumilia shida fulani ili nionyeshe upendo wangu na shukrani? Je! naipenda jamaa yangu mwenyewe vya kutosha kuweka mfano unaofaa ili, ikiwezekana, wao pia wapate kusaidiwa waje wafaidike na maandalizi ya Mungu ya kupata uzima wa milele?’—Mathayo 10:36-38; 1 Wakorintho 7:12, 13, 16.

ISHARA AMBAYO MATAIFA YANAGEUKIA

4. Twaweza kuonyeshaje kwamba twampenda Yehova kweli kweli?

4 Sasa nafasi inatolewa kwa watu kila mahali ili waonyeshe upendo wao kwa Yehova kwa kujipanga wenyewe pamoja na Ufalme wa Kimasihi. Serikali hiyo ndiyo njia itakayotumiwa ili jina la Yehova liondolewe malawama. Mwelekeo wetu juu ya Ufalme huo unatoa ushahidi wa jinsi tunavyohisi juu ya Yehova mwenyewe.

5. (a) Ni nini kilichotabiriwa kifanyike wakati wetu katika Isaya 11:10? (b) Kinamaanisha nini?

5 Yehova kwa roho yake alimwongoza nabii Isaya aandike hivi: “Na itakuwa katika siku hiyo, shina la Yese lisimamalo kuwa ishara kwa kabila za watu, yeye ndiye ambaye mataifa watamtafuta; na mahali pake pa kupumzikia patakuwa na utukufu.” (Isaya 11:10) Hilo “shina la Yese” ni Bwana Yesu Kristo aliyetukuzwa. Alipoanza kutumia mamlaka ya Ufalme, akiwa “shina” lenye kutoa uzima alitoa uzima kwa ukoo wa wafalme wa Kimasihi waliokuja kutoka Yese kupitia Mfalme Daudi, mwanaye. (Ufunuo 5:5; 22:16) Tangu mwaka wa 1914 amekuwa ‘akisimama kuwa ishara kwa kabila za watu,’ mahali pa kujikusanya watu wanaotamani sana serikali ya uadilifu. Yehova mwenyewe amemwinua awe Ishara hiyo, Mfalme wa kweli wa Kimasihi.—Isaya 11:12.

6. (a) Ni nini kimesaidia wanadamu wajikusanye kuzunguka Mfalme wa kimbingu? (b) Watu wamejifunza nini, yakiwa ni matokeo ya ‘kutafuta’ ile “ishara”?

6 Lakini wanadamu waliopo hapa duniani wangeweza kujikusanyaje kuzunguka Mfalme wa kimbingu? Wanahitaji wapewe taarifa kutoka Biblia ili waweze kumwona kwa macho ya ufahamu. Kwa kuelekezwa na roho takatifu, mabaki ya Israeli wa kiroho wamekuwa wakitimiza kwa nguvu utendaji huo, wakitangaza kote kote duniani habari njema za Ufalme wa Kimasihi wa Mungu uliosimamishwa. Watu mmoja mmoja kutoka mataifa yote wamesikiliza kwa kuthamini. Wameulizia juu ya matakwa ya kimungu wayatimize ili wawe raia za Ufalme huo, waje wafurahie umilele wa uzima katika dunia ya Paradiso. Kwa kuridhika na majibu ambayo wamepewa kutoka Biblia, wametenda kupatana na hayo, wakachukua msimamo wao upande wa Ufalme wa Kimasihi wa Yehova. Je! wewe umefanya hivyo?

‘WASIKIA LAKINI HAWATENDI’

7. Ni tendo gani kuelekea ujumbe wa Biblia lilitabiriwa katika Ezekieli 33:30-33?

7 Kwa sababu ya utendaji wenye bidii wa Mashahidi wa Yehova, mara nyingi wanasemwa sana na watu. Lakini watu hao wanahisije juu ya ujumbe ambao Mashahidi wa Yehova wanatangaza? Kutenda kwa wengi ni kama kule kwa wahamishwa wenzi wa Ezekieli katika Babuloni. Kwa habari yao, Yehova alisema: “Nawe, mwanadamu, wana wa watu wako husimulia habari zako . . . wakisema, Haya! twende tukasikie ni neno gani hilo litokalo kwa [Yehova]. Nao huja kama watu wajavyo, nao hukaa mbele yako kama watu wangu, nao husikia maneno yako, wasiyatende; maana kwa vinywa vyao hujifanya kuwa wenye upendo mwingi, lakini mioyo yao inatafuta faida yao. Na tazama, wewe umekuwa kwao kama wimbo mzuri sana, wa mtu mwenye sauti ipendezayo, awezaye kupiga kinanda vizuri; maana, wasikia maneno yako, lakini hawayatendi. Na hayo yatakapokuwapo (tazama, yanakuja), ndipo watakapojua ya kuwa nabii amekuwapo kati yao.”—Ezekieli 33:30-33.

8. Watu fulani wanatoaje ushahidi wa mwelekeo wao?

8 Kuna watu wengi wanaosifu sana Mashahidi wa Yehova na wanaopenda vitabu vyao vya Biblia. Huenda wakakubali toleo la kuwa na funzo la bure la Biblia nyumbani. Baadhi yao hata wanakuja wakiwa na rafiki zao kwenye mikutano ya pekee inayofanywa na Mashahidi. Kwa mfano, penye Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Yesu Kristo, si ajabu kuona hesabu ya wahudhuriaji ikiongezeka mara mbili ya hesabu ya mashahidi watendaji wa Yehova. Katika nchi fulani, hudhurio linaongezeka mara tano ya hesabu ya Mashahidi. Lakini watazifanyia nini zile kweli za Biblia wanazosikia? Zaidi ya milioni mbili na nusu wamezingatia kweli hizo kibinafsi moyoni, wakapatanisha maisha zao na kweli hizo. Lakini wengine wameziona kana kwamba ni muziki mzuri tu, jambo fulani la kuwatumbuiza. Wanachagua kutofanya lo lote, labda wakisema maneno ya kutia moyo lakini wasiweke maisha zao wakfu kwa Mungu wala kushiriki utumishi mtakatifu wake.

9. Badala ya kutia shaka na kungojea, watu wenye hekima wanafanya nini?

9 Ni faida gani itakayopatikana kwa kutia shaka na kungojea? Kwa hakika hakutaleta kibali ya Yehova na ulinzi katika siku ya kisasi inayokuja. Ili uwe kati ya watakaookoka, ni lazima utoe ushahidi wenye kusadikisha sasa kwamba ‘umejiunga na Yehova’ na kwamba wewe ni wake.—Zekaria 2:11; Mathayo 7:21.

WALIFANYA UAMUZI UNAOFAA

10, 11. (a) Hobabu alikuwa nani, na ni mwaliko gani aliopewa? (b) Twajuaje uamuzi aliofanya?

10 Wote ambao wamekuwa waabudu wa Yehova wakiwa wafuasi wa Yesu Kristo wamefanya uamuzi wa kibinafsi wawe hivyo. Hivyo ndivyo wamefanya wote walio warithi wa Ufalme wa kimbingu. Sasa nafasi bora inapatikana kwa wengine wachague, wawe na tazamio la kuja kuokoka dhiki kubwa na kuishi katika ukamilifu duniani. Hobabu aliwawekea mfano unaostahili kufuatwa.

11 Hobabu alikuwa shemeji ya Musa. Hakuwa Mwisraeli lakini alikuwa mtu wa kabila la Wakeni waliokuwa wakiishi katika eneo la Wamidiani. Waisraeli walipokwisha kupokea Torati kupitia Musa, wakawa wamelijenga hema takatifu la ibada ya Yehova, ukafika wakati wa kuhama kaskazini waelekee Nchi ya Ahadi. Ile nguzo ya wingu lenye kuwakilisha kuwapo kwa Yehova lingewatangulia, lionyeshe njia ya kufuata na mahali pa kupiga kambi. Lakini lingekuwa jambo lenye kusaidia wawe na mtu ambaye angejua nchi hiyo na mahali pa kupata vitu walivyohitaji kambini. Musa akamwalika Hobabu ajiunge nao, lakini kwanza Hobabu akakataa, akiona ingekuwa afadhali akae pamoja na watu wa ukoo wake mahali alipozaliwa. Ingawa hivyo, Musa akamwomba sana afikirie tena jambo hilo kisha aende nao ili ‘awe macho’ ya Israeli na kwa njia hiyo ajiweke tayari kuja kupokea baraka ambazo Yehova angewapa watu wake. Kwa hekima Hobabu akakubali, kama inavyoonyeshwa katika Waamuzi 1:16.—Hesabu 10:29-32.

12. (a) Ni nani leo walio kama Hobabu, na kwa njia zipi? (b) Ni mwaliko gani leo unaofanana na huo ambao Musa alimpa Hobabu?

12 Leo kuna watu waliofananishwa na Hobabu. Wasijapokuwa Waisraeli wa kiroho, wanajiunga na hao wanaposafiri kuelekea Utaratibu Mpya. Ili wafanye hivyo, ni lazima wakate vifungo vyao na watu wa ukoo wao wa kilimwengu na pia serikali za kibinadamu. Wakiwa chini ya uongozi wa aliye Musa Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo, wametumika kwa furaha pamoja na mabaki ya “ndugu” za Kristo, mara nyingi wakipelelezea maeneo mapya ili yahubiriwe habari njema. Wengi wao wamehamia sehemu ambazo watangazaji wa Ufalme walihitajiwa sana, mara nyingi wanafanya hivyo wakiwa mapainia au wamisionari, wakitumia wakati wao kwa ukamili ili watangaze Ufalme wa Mungu kuwa tumaini pekee la kweli la wanadamu. Kungali kuna nafasi nyingi za kushiriki utumishi mtakatifu huo. Watu wenye kustahili wanaalikwa wajiweke tayari kutumika na hivyo washiriki baraka zinazotokana na utumishi huo uliopanuka. Je! wewe unaweza kujiweka tayari kutumika?

13. (a) Yaeli alikuwa nani, na mume wake alikuwa na msimamo gani kuhusu watumishi wa Yehova? (b) Yaeli alikabiliwaje na jaribu?

13 Miaka kama 180 baada ya Hobabu kuamua kwenda pamoja na Waisraeli, mmoja wa wazao wake, mwanamume jina lake Heberi, alikuwa akiishi na Yaeli, mkeye, mahali ambapo si mbali sana kutoka Megido. Heberi alikuwa amejitenga mwenyewe na Wakeni wengine, akawa ameingia katika uhusiano wa amani pamoja na Yabini, mfalme Mkanaani aliyewaonea sana Waisraeli. Yehova alipomwinua Baraki awe mkombozi wa Israeli, Sisera, mkuu wa jeshi la Yabini, alikusanya jeshi lake na magari ya vita mia tisa yakiwa yamefungiwa miundu ya chuma kwenye magurudumu. Lakini Yehova alipigania watu wake, akatia fujo katika kambi ya adui, na mafuriko makubwa ya maji ili atopeze magari hayo. Sisera mwenyewe akaliacha gari lake akachomoa mbio ya miguu kuelekea hema la Yaeli mkeye Heberi. Kama Sisera alivyotumaini, Yaeli akamkaribisha ndani ya hema.—Waamuzi 4:4-17; 5:20, 21.

14. Ni uamuzi gani ambao Yaeli alifanya, na kwa uamuzi huo alitoa ushahidi wa nini?

14 Basi jaribu likaanza. Yaeli angemtenda nini adui huyu wa watu wa Yehova? Akamfunika Sisera blanketi, akatuliza kiu yake kwa maziwa-mgando kisha akangojea mpaka adui huyo alipolala usingizi. Ndipo “akatwaa kigingi cha hema, akashika nyundo mkononi mwake, akamwendea polepole, akamtia kile kigingi katika kipaji chake, nacho kikapenya, hata kuingia mchangani; kwa maana usingizi mzito ulikuwa umemshika; basi akazimia, akafa.” Jambo alilofanya lilihitaji ujasiri, na upendo kwa Yehova na kwa watu wake. Pia lilihusu kuchukua hatua na kujitumikisha upande wake.—Waamuzi 4:18-22; 5:24-27, 31.

15. Watu leo wanaonyeshaje kwamba wako kama Yaeli?

15 Kama waabudu wengine wa Yehova wasio Waisraeli, Yaeli anafananisha “kondoo wengine” wanaotendea ndugu za kiroho za Kristo mambo mema. Bila kujali uhusiano walio nao watu wa ukoo wao wa karibu pamoja na ulimwengu na pamoja na watawala wake, “kondoo wengine” hawakubali watawala wa kilimwengu wawaonee watu wa Yehova. Wanampa ushikamanifu wao Baraki Mkubwa Zaidi, Bwana Yesu Kristo, na wafuasi wake wa kweli. Hao walio wa jamii ya Yaeli hawainui binafsi mkono juu ya watawala wa kilimwengu, bali wanatumia cho chote walicho nacho ili wapinge jitihada za kuonea watumishi wa Yehova. Hawasiti kujulisha kwamba wanakubaliana kabisa na kusudi la Yehova la kuja kuwaangamiza adui zake wote.

16, 17. (a) Ni mfano gani ulioandikwa katika Matendo sura ya 8 unaostahili tuufuate? (b) Baada ya hapo imetupasa tuendelee kufanya nini?

16 Hakuna wakati wa kupoteza. Ikiwa unamwamini Yehova na kuuamini Ufalme wa Kimasihi wake kweli kweli, na ikiwa umepatanisha maisha yako na matakwa ya Biblia, basi, onyesha hivyo waziwazi bila kukawia. Onyesha roho ya yule towashi Mwethiopia anayeripotiwa katika Matendo sura ya 8. Mara alipofahamu aliyotakwa kufanya, alimuuliza Filipo aliyekuwa amemweleza habari njema juu ya Kristo, hivi: “Ni nini kinachonizuia nisibatizwe?” Na bila kukawia akazamishwa katika maji.

17 Ukiisha kuwa na mwanzo mzuri hivyo, utie nguvu kila siku uhusiano wako pamoja na Yehova. Tafuta njia za kutumia kikamili zaidi Neno lake katika maisha yako. Na shiriki kikamili iwezekanavyo kazi ya lazima ya kutangaza Ufalme, inayofanywa wakati wa siku za kumalizia za huu mfumo wa mambo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki