Mikutano ya Kuhimizana Ili Kupenda na Kufanya Kazi Nzuri
Wakristo wa kwanza walikutana pamoja, kwa ukawaida wakiwa katika nyumba za faragha, ili wapokee agizo na kufurahia ushirika wenye kujenga. Leo, makundi ya Mashahidi wa Yehova yanakutana mara tatu kila juma. Unaalikwa uhudhurie yo yote ya mikutano hiyo. Mikutano yao haifuati desturi ya kidini, bali inakaza fikira juu ya elimu ya kimungu. Mikutano ya kundi inafunguliwa na kufungwa kwa wimbo na sala. Hudhurio halilipiwi fedha, na hakuna sadaka za fedha zinazochukuliwa. —Matendo 4:23-31; 14:22; 15:32, 35; Warumi 16:5; Wakolosai 4:15.
Labda mkutano wa kwanza ambao utahudhuria utakuwa ni hotuba ya watu wote ya dakika 45, ikishughulika na mafundisho ya Biblia, unabii, au shauri juu ya maisha ya Kikristo. Baada ya hotuba hiyo, kuna funzo la Biblia, lenye kutumia makala katika Mnara wa Mlinzi ambayo imekusudiwa hasa kwa ajili ya funzo la kundi. Funzo hilo linafuata mtindo huo: Fungu kutoka Mnara wa Mlinzi linasomwa, kiongozi anauliza maswali juu ya habari hiyo, na wale wanaotaka kutoa maelezo wanaonyesha hivyo kwa kuinua mkono wao. Mkutano huo unachukua saa moja.
Baadaye juma hilo, mikutano mingine miwili yenye dakika 45 inafanywa. Mmoja ni Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Mkutano huu unatoa mazoezi juu ya jinsi ya kukusanya habari juu ya masomo ya Biblia na kuifundisha kwa njia yenye matokeo. Baada ya dakika 21 za agizo la pekee, wanafunzi ambao wamepewa mgawo mapema wanatoa hotuba zao fupi. Baada ya kila hotuba, mwalimu wa shule hutoa shauri kuonyesha jinsi mwanafunzi anavyoweza kufanya maendeleo. Vitabu kadha vya masomo vimetayarishwa vitumiwe katika shule hii. Wote wanaohudhuria mikutano kwa kawaida wanaweza kujiandikisha, mradi wanaishi kwa njia inayopatana na kanuni za Kikristo.
Mkutano unaofuata unaitwa Mkutano wa Utumishi. Katika mkutano huo mna sehemu tatu au nne zinazoshughulika na kutangaza habari njema nyumba kwa nyumba na pia sehemu nyinginezo za huduma. Sehemu hizo zinatolewa kama hotuba, mazungumzo, au mawonyesho, pamoja na ushirika fulani wa wasikilizaji. Sehemu kubwa ya programu inategemea habari inayopatikana katika Huduma ya Ufalme Yetu, ambayo ni karatasi ya maagizo yenye kurasa nne inayochapishwa kila mwezi na Watch Tower Society.
Mkutano mwingine ni funzo la kila juma linalofanywa katika vikundi vidogo vidogo, kwa kawaida katika nyumba za faragha katika eneo lote la kundi. Funzo hilo linategemea Biblia na kitabu cha karibuni kilichochapishwa na Sosaiti. Kwa kuwa kikundi ni kidogo zaidi, kuna nafasi bora kwa wote kushiriki mazungumzo, na kuna nafasi nzuri kwa wahudhuriaji kufahamiana vizuri wao kwa wao.
Makundi mengi yanafanya mikutano yao katika Jumba la Ufalme lililojengwa na Mashahidi wa Yehova. Gharama zinalipiwa na michango ya kujitolea kutoka kwa Mashahidi wenyewe, na mara nyingi zaidi kazi hiyo inafanywa bila malipo na wafanya kazi wa kujitolea. Visanduku vya michango vinapatikana kwenye mikutano yote kwa matumizi ya wale wanaotaka kuchanga.
Mikutano ya kundi inasaidia Mashahidi wa Yehova walifuate shauri katika Waebrania 10:24, 25: “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri [tu]onavyo siku ile kuwa inakaribia.”
• Ni sehemu gani za mikutano ya Wakristo wa kwanza zinazoweza kuonwa katika mikutano ya Mashahidi wa Yehova?
• Ebu eleza yanayotolewa kwenye mikutano mitano inayofanywa kwa ukawaida na Mashahidi.
• Majumba ya mikutano yamepatikanaje?
[Picha katika ukurasa wa 14]
Mzee anaongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi, United States
Tamasha kutoka Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, Visiwa vya Faeroe
Funzo la kikundi katika nyumba ya faragha, Yap
Jumba la Ufalme, New Braunfels, Texas, U.S.A., lililojengwa katika siku mbili na Mashahidi wa Yehova
[Picha katika ukurasa wa 15]
Majumba ya Ufalme katika nchi mbalimbali
Japani
Australia
Austria
Hispania