Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ws sura 17 kur. 136-143
  • Kulikumbuka Kishikamanifu Tengenezo la Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kulikumbuka Kishikamanifu Tengenezo la Yehova
  • Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mateka Katika Babuloni Walikumbuka Kishikamanifu Sayuni
  • Kushikamana Kwa Moyo na Tengenezo la Yehova
  • Yehova Abaki Akiwa Mshikamanifu kwa Tengenezo Lake
  • Ushikamanifu kwa Tengenezo Lionekanalo la Mungu Leo
    Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani”
  • “Wewe Peke Yako Ni Mwaminifu-Mshikamanifu”
    Mkaribie Yehova
  • Watazame Wale Waaminifu-Washikamanifu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Kuamini Tengenezo lishindalo la Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
Pata Habari Zaidi
Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani”
ws sura 17 kur. 136-143

Sura 17

Kulikumbuka Kishikamanifu Tengenezo la Yehova

1. Imetupasa tuwe tukifikiria juu ya ushikamanifu kwa nani, na Mfalme Daudi alisema nini juu ya hilo?

MENGI yanasemwa sana leo juu ya ushikamanifu kwa nchi ya mtu. Lakini watawala na vikundi vya watu wa ulimwengu huu wanasema mengi kadiri gani juu ya ushikamanifu kwa Mungu, ambaye ndiye Muumba wa lile jimbo linalokaliwa na nchi ya mtu? Katika nyakati za kale, Mfalme Daudi wa Israeli alikuwa mwabudu mshikamanifu wa Muumba, Yehova Mungu. Akimwambia huyu Mungu mshikamanifu, Daudi alisema maneno haya kwake: “Kwa mtu mshikamanifu wewe utatenda kwa ushikamanifu.” (2 Samweli 22:26, NW; Zaburi 18:25) Je! Maneno hayo yanaonyesha mwelekeo wako kwa Mungu?

2. Tunajuaje kwamba Yehova amebaki akiwa mshikamanifu kwa jamaa ya kibinadamu?

2 Kwa ujumla mwelekeo wa wanadamu leo si ule wa kuhangaikia sana ushikamanifu kwa Mungu. Lakini bila kujali hilo Yehova ni mshikamanifu kwa jamaa ya kibinadamu. Yeye hakuitupilia mbali. Mwanaye mshikamanifu alisema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Mungu hakuuachia ulimwengu wa wanadamu yule adui wao mkubwa zaidi Shetani, aliyekuwa amewashawishi wazazi wetu wa kwanza kukosa ushikamanifu kwa Mungu. Vilevile Mungu alionyesha ushikamanifu wake kwa jamaa ya kibinadamu mwaka wa 2370 K.W.K. kwa kuhifadhi Noa na jamaa yake kuipita ile gharika ya duniani pote iliyofutilia mbali wanadamu wengine wote. (2 Petro 2:5) Katika njia hiyo Muumba aliipa jamaa ya kibinadamu mwanzo mpya.

3. (a) Ni jambo gani linaloweza kusemwa juu ya jeuri leo, na Mungu amekusudia kufanya nini juu yayo? (b) Ni nini thawabu ya kuwa mshikamanifu kwa Yehova?

3 Leo ile jeuri ya duniani pote inashinda ile ya wakati wa Noa zaidi ya miaka 4,000 iliyopita. (Mwanzo 6:11) Kwa hiyo kuna sababu nzuri kwa Mungu uyo huyo kuufutilia mbali usiwepo huu mfumo wa mambo wa kilimwengu uliopo. Hilo amekusudia kulifanya, lakini afanyapo hivyo, yeye hatawaharibu washikamanifu wake duniani. Wakati huo yeye atatenda kupatana na Zaburi 37:28, NW: “Yehova ni mpenda haki, na yeye hataacha washikamanifu wake.” Kama katika siku za Noa, yeye atatoa mwanzo wenye uadilifu kwa ule mfumo mpya wa mambo wenye “mbingu mpya na dunia mpya.” (2 Petro 3:13, NW) Thawabu ya kuwa mshikamanifu ni kubwa. Inatoa uzima!

4. Tunajuaje kwamba taifa la Israeli lilikuwa tengenezo lionekanalo la Yehova wakati huo?

4 Wakati wa utawala wa Mfalme Daudi, taifa la Israeli lilithibitika kuwa jaminifu kwa Yehova. Daudi aliweka kielelezo kwa taifa zima. Taifa hilo lilikuwa tengenezo lionekanalo la Yehova. Walikuwa watu waliofanywa kuwa tengenezo, watu wake mwenyewe pekee. Bila shaka ndilo linalomaanishwa na kikumbusho cha Mungu, kama kilivyoandikwa kwenye Amosi 3:1, 2: “Lisikieni neno hili alilolisema [Yehova] juu yenu, enyi wana wa Israeli, juu ya jamaa yote niliowapandisha kutoka nchi ya Misri, nikisema, ni ninyi tu niliowajua katika jamaa zote zilizo duniani.”—Linganisha 1 Wafalme 8:41-43.

5. (a) Katika siku za mitume wa Yesu Kristo, je! jitihada zilifanywa za kuingiza makosa katika kundi la Kikristo? (b) Ni nini lililotabiriwa kutukia baada ya kifo cha mitume?

5 Kulingana na uhakika huo wa historia ya Biblia, Mungu uyu huyu Yehova, ana watu waliofanywa kuwa tengenezo, tengenezo lionekanalo duniani leo. Ni tengenezo ambalo ni lake mwenyewe peke yake. Hata hivyo, jitihada zilifanywa ili kuingiza makosa katika tengenezo la Mungu hata katika mwanzo walo siku za mitume wa Yesu Kristo, waliokuwa wapiganiaji shupavu wa ukamilifu wa kundi la Kikristo. (1 Wakorintho 15:12; 2 Timotheo 2:16-18) Kufuata kifo cha mtume Yohana, kwa wazi si muda mrefu baada ya 98 W.K., ule uasi-imani uliotabiriwa ulianza.—Matendo 20:30; 2 Petro 2:1, 3; 1 Timotheo 4:1.

6. (a) Uasi-imani huo ulitawala kwa muda gani, na kukiwa na matokeo gani? (b) Matengenezo ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo yalikuja kwenye utekwa gani, na ni maulizo gani yanayotokea?

6 Uasi-imani huo ulitawala kwa karne zaidi ya 17, kufikia nusu ya pili ya karne ya 19. Kufikia wakati huo Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imegawanyika ikawa mamia ya madhehebu za kidini. Kile kitambulisho cha watu wa kweli wa Mungu kilififishwa. Jumuiya ya Wakristo ilikuwa ni mchafuko wa matengenezo ya kidini, makubwa kwa madogo, yakisema mchanganyiko wa lugha za kidini ambazo hazikuwa na msingi imara wa lugha ya kidini ya Maandiko yaliyoongozwa na Mungu. Matengenezo hayo ya kidini kwa kweli yalikuwa yamechukuliwa mateka na milki iliyokuwa kubwa zaidi ya milki ya Kibabuloni iliyouharibu Yerusalemu. Lakini Babuloni ya kale ilikuwaje, na ni lazima mwelekeo wa Wayahudi waaminifu waliokuwa wameshikwa mateka uwe ulikuwaje?

Mateka Katika Babuloni Walikumbuka Kishikamanifu Sayuni

7. (a) Kusema kwa jinsi ya kidini, nchi ya Babuloni ya kale ilikuwaje? (b) Ni lazima hilo liwe lilikuwa na matokeo gani kwa mateka Wayahudi?

7 Babuloni ya kale ilikuwa nchi ya miungu mingi ya uwongo, ambayo sanamu zayo za kuabudiwa zilikuwa nyingi sana. (Danieli 5:4) Tunaweza kuwazia ibada hii ya miungu mingi ya uwongo ilikuwa na matokeo gani katika mioyo ya Wayahudi waaminifu waliokuwa wakiabudu Mungu wa kweli mmoja tu bila kuwa na mfano wa aina yo yote. Badala ya kuona hekalu la Yehova katika uzuri walo wote katika Yerusalemu, waliona mahekalu ya miungu hiyo ya uwongo pamoja na sanamu zayo kote kote katika nchi ya Babuloni.a Ni lazima waabudu wa Mungu wa kweli mmoja tu wawe walichukizwa sana na yote hayo!

8. (a) Wayahudi wangelazimika kuvumilia utekwa wao kwa muda gani, nao Wayahudi washikamanifu wangekuwa na tamaa gani? (b) Zaburi 137:1-4 inaelezaje hali ya kuvunjika moyo ya mateka Wayahudi washikamanifu?

8 Kulingana na unabii wa Yeremia, wangelazimika kuvumilia hayo kwa miaka 70 kabla ya kurudishwa kwao. (2 Mambo ya Nyakati 36:18-21; Yeremia 25:11, 12) Hali ya kuvunjika moyo ya Wayahudi mateka waliompenda Yehova na waliotamani kumwabudu yeye katika hekalu lililowekwa wakfu kwake katika mji wake uliochaguliwa inasimuliwa kwa ajili yetu katika Zaburi 137:1-4: “Kando ya mito ya Babeli ndiko tulikoketi, tukalia tulipoikumbuka Sayuni. Katika miti iliyo katikati yake tulivitundika vinubi vyetu. Maana huko waliotuchukua mateka walitaka tuwaimbie; na [wenye kudhihaki sisi] walitaka furaha; Tuimbieni baadhi ya nyimbo za Sayuni. Tuuimbeje wimbo wa [Yehova] katika nchi ya ugeni?”

9. Wababuloni wangekuonaje kuimbwa kwa “wimbo wa [Yehova],” lakini ni jambo gani lililotazamiwa litukie mwishoni mwa miaka 70?

9 “Wimbo wa [Yehova]” unapasa kuwa wimbo wa watu walio huru wakimwabudu yeye katika hekalu lake takatifu. Kwa Wababuloni hao, Wayahudi hao kuimba “wimbo wa [Yehova]” katika nchi ya utekwa wao kungekuwa pindi ya watekaji hao kulidhihaki jina la Yehova kuwa jina la mungu mdogo kuliko miungu ya Babuloni. Jina lake takatifu tayari lilikuwa limeshutumiwa sana kwa yeye kuruhusu watu wake wachukuliwe kutoka nchi ya nyumbani kwao waliyopewa na Mungu na kupelekwa mbali kwenye nchi ya miungu mingi. Lakini wakati wa Wababuloni hao kumdhihaki na kuwavunjia heshima watu wa jina lake ungekuwa kipindi chenye kikomo—miaka 70 tu. Basi, chini na iende miungu ya uwongo ya Babuloni na, juu na ainuliwe Mungu wa kweli, Yehova!

Kushikamana Kwa Moyo na Tengenezo la Yehova

10. Ni ulizo gani linalotokea kuhusu watu wa Yehova wa karne hii ya 20 walioletwa kwenye utekwa wa Babuloni Mkuu?

10 Leo kuna tengenezo la kidini liitwalo Babuloni Mkuu ambalo haliko katika nchi ya Babuloni ya awali pekee bali liko ulimwenguni pote. Je! mwelekeo wa moyoni wa Wayahudi katika Babuloni wa kale unaweka kielelezo kinachofaa kwa watu wa Yehova wa karne hii ya 20 walioingizwa kinguvu katika utekwa wa Babuloni Mkuu ikiwa nidhamu kutoka kwa Mungu wa Israeli wa kale?

11. (a) Je! Wayahudi washikamanifu walijiruhusu waisahau nchi ya nyumbani kwao? (b) Mtunga zaburi mtekwa alielezaje hisia za mateka wenzake?

11 Ijapokuwa wangaliselea katika Babuloni wa kale na kujistarehesha, kwa kuwa uhamisho wao ungeendelea kwa muda wa kama kizazi kimoja hivi, je! walijiacha waisahau nchi ya nyumbani kwao? Yule mtunga zaburi mtekwa anaieleza kwa uzuri anaposema juu ya hisia za mateka wenzake hivi: “Ee Yerusalemu, nikikusahau wewe, mkono wangu wa kuume na usahau. Ulimi wangu na ugandamane na kaakaa la kinywa changu, nisipokukumbuka. Nisipoikuza Yerusalemu zaidi ya furaha yangu iliyo kuu.”—Zaburi 137:5, 6.

12. Mwelekeo wa moyoni wa mtunga zaburi mtekwa huyo ulionyesha nini?

12 Mwelekeo wa moyoni huo wa Mwisraeli mtekwa huyo ulionyesha nini? Hili: Ushikamanifu kwa tengenezo lionekanalo la Yehova la wakati huo alipoona nchi ambayo Mungu alikuwa amewapa watu Wake waliochaguliwa ikikaa ukiwa kwa miaka 70. Ndiyo, tengenezo lionekanalo la Yehova liliendelea kuishi katika mioyo ya Waisraeli hao.

13. Ushikamanifu kwa tengenezo la Yehova lionekanalo ulithawabishwaje?

13 Ushikamanifu huo kwa tengenezo la kale lionekanalo la Mungu ulithawabishwa ilivyofaa. Ilikuwa wakati Babuloni, ikiwa ndiyo mamlaka ya ulimwengu ya tatu ya historia ya Biblia, ilipopinduliwa, na Wamedi na Waajemi, ile mamlaka ya nne ya ulimwengu, ilipotekeleza mapenzi ya Mungu wa Israeli. Jinsi gani? Kwa kuwarudisha Wayahudi mateka kwenye nchi ya tengenezo la Yehova lionekanalo, wakiwa na maagizo ya kulijenga tena hekalu la Mungu wao likiwa mahali pa kati pa utendaji pa mji mkuu, Yerusalemu. (2 Mambo ya Nyakati 36:22, 23) Si kwamba tu hekalu la ibada ya kweli lilijengwa tena bali pia kuta za mji wa Yerusalemu zilijengwa upya, ukawa mji ambao kutoka hapo Yehova alitawala akiwa Mfalme juu ya watu wake.

14. (a) Karne nyingi baadaye, Masihi alisema nini juu ya tengenezo la Yehova lionekanalo? (b) Ni katika maana gani Yehova alitawala kutoka Yerusalemu?

14 Zaidi ya karne sita baada ya Yerusalemu kuharibiwa, Yesu alisema hivi: “Usiape kabisa; hata kwa mbingu, kwa maana ndicho kiti cha enzi cha Mungu; wala kwa [dunia], kwa maana ndiyo pa kuwekea miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa maana ndio mji wa Mfalme mkuu.” (Mathayo 5:34, 35) Masihi alipokuwa duniani, hekalu lililojengwa upya la Yehova lilisimama katika Yerusalemu, na, kusema kwa jinsi ya mfano, Yehova Mungu alitawala katika Patakatifu Zaidi Sana pa hekalu hilo. Hivyo kutoka Yerusalemu ukiwa ndio mji mkuu wa watu wake, Yehova alitawala juu ya tengenezo lake lionekanalo.

Yehova Abaki Akiwa Mshikamanifu kwa Tengenezo Lake

15. Je! Yesu alikuwa akikatalia mbali sehemu ionekanayo ya tengenezo la Yehova alipowafichua viongozi wa kidini wasio waaminifu wa Israeli? Eleza.

15 Basi, sasa, je! Yesu alilitupilia mbali tengenezo lionekanalo la Mungu wakati alipowafichua na kuwalaani viongozi wa kidini wa Israeli wasio waaminifu? Ndiyo, kwa kuwa alisema: “Ee, Yerusalemu, Yerusalemu, uwauaye manabii, na kuwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwako! ni mara ngapi nimetaka kuwakusanya pamoja watoto wako, kama vile kuku avikusanyavyo pamoja vifaranga vyake chini ya mabawa yake, lakini hamkutaka! Angalieni, nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 23:37, 38) Yesu alipoukatalia mbali Yerusalemu na “watoto” wao, je! alikuwa hapo akiacha Baba yake wa kimbingu bila tengenezo la kidunia? La! Kwa kuwa Yesu mwenyewe alikuwa ndiye msingi wa tengenezo jipya lionekanalo ambalo Muumba wa ulimwengu mzima alikuwa akitayarisha kujenga.

16. Wakati wa kifo cha Yesu kwenye mti wa mateso, kukataliwa mbali kwa Israeli wa asili kulionyeshwaje?

16 Kukataliwa mbali kwa Israeli wa asili hakika kulionyeshwa wakati kwenye kifo cha Yesu juu ya mti wa mateso, lile pazia zito lililotenganisha Patakatifu Zaidi Sana na Patakatifu katika hekalu la Yerusalemu lilipopasuliwa vipande viwili “toka juu hata chini.” Wakati uo huo, “nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka.” Hayo yalikuwa matendo ya kimwujiza kwa upande wa Mungu aliyekuwa akitawala hapo kwa njia ya mfano, akionyesha alikuwa amelikatalia mbali taifa la Israeli na dini yalo.—Mathayo 27:51.

17. Yesu na Yehova walionyeshaje ushikamanifu kwa wale waliotazamiwa kuwa washiriki wa tengenezo jipya lionekanalo la Mungu?

17 Waliotazamiwa kuwa washiriki wa tengenezo jipya lionekanalo ambalo Yehova Mungu angejenga karibuni waliachwa humo katika makao ya Yerusalemu. Yesu aliwakabidhi kwenye uangalizi wa Mungu, aliyekuwa akiacha mji huo wa kidunia kwa kupendelea kitu kilicho bora zaidi. (Yohana 17:9-15) Hivyo Yehova alibaki akiwa mshikamanifu kwa tengenezo lake, akiwafikiria kipekee babu zao waaminifu, Abrahamu, Isaka, na Yakobo na wale wana 12 wa Yakobo. (Danieli 12:1) Sura inayofuata itaendeleza mazungumzo yetu juu ya ushikamanifu, ambao msingi wake ni Zaburi 137.

[Maelezo ya Chini]

a Mwandiko wa michoro kutoka Babuloni ya kale unaripoti hivi: “Yote pamoja kuna mahekalu 53 katika Babuloni ya ile miungu mikuu, makanisa madogo 55 ya Marduki, makanisa madogo 300 kwa ajili ya miungu ya kidunia, 600 kwa ajili ya miungu ya kimbingu, madhabahu 180 kwa ajili ya mungu-mke Ishta, 180 kwa ajili ya miungu Nergali na Adadi na madhabahu nyingine 12 kwa ajili ya miungu mbalimbali.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki