Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jr sura 8 kur. 92-102
  • ‘Utaendelea Kuishi’ Kama Yeremia?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Utaendelea Kuishi’ Kama Yeremia?
  • Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • AMRI ISIYO YA KAWAIDA
  • JIFUNZE KUTOKANA NA USEJA WA YEREMIA
  • BURUDISHA NAWE UBURUDISHWE
  • Asiyefunga Ndoa Lakini Kamili kwa Utumishi wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Useja—Njia ya Maisha Yenye Kuthawabisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Waseja Ambao Hupata Uradhi Katika Utumishi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Mashauri ya Hekima Kuhusu Useja na Ndoa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
Pata Habari Zaidi
Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
jr sura 8 kur. 92-102

SURA YA NANE

‘Utaendelea Kuishi’ Kama Yeremia?

1, 2. Kwa nini ni muhimu kuhangaikia mtu mmoja-mmoja na familia pia?

BAADA ya Yoshua kuwahimiza Waisraeli wachague watakayemtumikia, alisema: “Mimi na nyumba yangu, tutamtumikia Yehova.” (Yos. 24:15) Yoshua aliazimia kuwa mshikamanifu kwa Mungu, naye alikuwa na hakika kwamba familia yake pia ingekuwa vivyo hivyo. Baadaye, uharibifu wa Yerusalemu ulipokaribia, Yeremia alimwambia Mfalme Sedekia kwamba ikiwa angejisalimisha mikononi mwa Wababiloni, ‘yeye mwenyewe na nyumba yake hakika wataendelea kuishi.’ (Yer. 38:17) Uamuzi mbaya wa mfalme ulikuwa na matokeo mabaya kwake, wake zake, na wana wake. Alishuhudia wana wake wakiuawa; kisha akapofushwa na kupelekwa uhamishoni Babiloni.—Yer. 38:18-23; 39:6, 7.

2 Katika visa hivyo viwili vilivyotajwa, ni mtu mmoja aliyehusika moja kwa moja. Lakini familia ya kila mmoja wao inatajwa pia. Inaeleweka. Kila mtu mzima anawajibika mbele za Mungu. Hata hivyo, Waisraeli wengi walikuwa sehemu ya familia fulani. Familia ni muhimu kwa Wakristo pia. Hilo linaonekana wazi kutokana na yale tunayosoma katika Biblia na yale tunayojifunza katika mikutano ya Kikristo kuhusu ndoa, kulea watoto, na kuwaheshimu watu wa familia.—1 Kor. 7:36-39; 1 Tim. 5:8.

AMRI ISIYO YA KAWAIDA

3, 4. Hali ya Yeremia ilikuwa tofauti jinsi gani, naye alipata faida gani?

3 Yeremia ni mmoja kati ya wale ‘walioendelea kuishi’ katika siku zake. Aliokoka uharibifu wa Yerusalemu, ingawa hali zake zilikuwa tofauti. (Yer. 21:9; 40:1-4) Mungu alikuwa amemwambia asioe, asiwe na watoto, na ajiepushe na shughuli nyingine za kawaida katika maisha ya Wayahudi wa siku zake.—Soma Yeremia 16:1-4.

4 Kulingana na utamaduni wa siku za Yeremia, ilikuwa kawaida kufunga ndoa na kuwa na watoto. Wanaume wengi Wayahudi walioa na kupata watoto, na hivyo wakadumisha nchi ya uzawa ya babu zao.a (Kum. 7:14) Kwa nini Yeremia hakuruhusiwa kufunga ndoa? Kwa sababu ya mambo ambayo yangetokea, Mungu alimwambia asijishughulishe na mambo ya kawaida kama vile pindi za huzuni au shangwe. Hakupaswa kuwafariji waombolezaji au kula nao baada ya mazishi; wala hakupaswa kushiriki katika sherehe za arusi za Kiyahudi. Karibuni sherehe zote hizo zingekoma. (Yer. 7:33; 16:5-9) Maisha ya Yeremia yaliupa uzito ujumbe wake na kukazia hukumu iliyokuwa karibu. Mwishowe siku hiyo ya hukumu ikafika. Wazia hisia za watu waliolazimika kula watu wengine au wale walioona maiti za wapendwa zikioza na kuwa kama mbolea! (Soma Yeremia 14:16; Omb. 2:20.) Hivyo basi, Yeremia ambaye hakuoa hakuhitaji kusikitikiwa. Ijapokuwa miezi 18 ya kuzingirwa na maafa yaliyotokea yaliangamiza familia nzima-nzima, Yeremia aliepushwa na huzuni ya kumpoteza mke au watoto.

5. Andiko la Yeremia 16:5-9 linawahusu Wakristo jinsi gani?

5 Hata hivyo, je, tunaweza kusema kwamba andiko la Yeremia 16:5-9 linatuhusu sisi pia? Hapana. Wakristo wanatiwa moyo “kuwafariji wale walio katika namna yoyote ya dhiki” na “kushangilia pamoja na watu wanaoshangilia.” (2 Kor. 1:4; Rom. 12:15) Yesu alihudhuria arusi na akachangia furaha ya arusi hiyo. Hata hivyo, mambo yatakayoupata mfumo huu mbovu wa mambo ni makubwa. Huenda Wakristo wakakabili hali ngumu na kukosa vitu fulani. Yesu alikazia uhitaji wa kuwa tayari kufanya yote tuwezayo kuvumilia na kuendelea kuwa waaminifu, kama walivyofanya ndugu zetu waliokimbia Yudea katika karne ya kwanza. Kwa hiyo, suala la kuwa mseja, kufunga ndoa, au kuwa na watoto ni jambo linalopaswa kufikiriwa kwa uzito.—Soma Mathayo 24:17, 18.

Picha katika ukurasa wa 94

6. Ni nani wanaoweza kufaidika kwa kutafakari maagizo ambayo Mungu alimpa Yeremia?

6 Tunaweza kujifunza nini kutokana na amri ya Mungu kwamba Yeremia asifunge ndoa wala kuwa na watoto? Leo, Wakristo fulani washikamanifu ni waseja au hawana watoto. Wanaweza kujifunza nini kutokana na kisa cha Yeremia? Na kwa nini hata Wakristo waliofunga ndoa na kuwa na watoto wanapaswa kufikiria kwa uzito hali ya Yeremia?

7. Kwa nini leo tunapaswa kufikiria kwa uzito amri ambayo Yeremia alipewa ya kutokuwa na watoto?

7 Kwanza, Yeremia hakupaswa kuwa na watoto. Yesu hakuwaagiza wafuasi wake wasiwe na watoto. Hata hivyo, kumbuka alisema kwamba wakati wa dhiki ya Yerusalemu mwaka wa 66-70 W.K., wanawake wenye mimba au wanaonyonyesha wangekuwa na “ole.” Huo ungekuwa wakati mgumu sana kwao. (Mt. 24:19) Dhiki iliyo kubwa hata zaidi iko mbele yetu. Wenzi wa ndoa Wakristo wanaofikiria kuwa na watoto wanapaswa kuzingatia hilo kwa uzito. Hukubali kwamba inazidi kuwa vigumu kushughulika na nyakati hizi za hatari? Na wenzi wengi wa ndoa wanakiri kwamba si rahisi kulea watoto ‘watakaoendelea kuishi’ na kuokoka mwisho wa mfumo huu. Ingawa wenzi wa ndoa wanapaswa kujiamulia ikiwa watakuwa na watoto, ni muhimu kufikiria kisa cha Yeremia. Namna gani amri ya Mungu kwamba hata asifunge ndoa?

Yeremia alipewa amri gani isiyo ya kawaida, nayo inapaswa kutuchochea kufikiria nini?

JIFUNZE KUTOKANA NA USEJA WA YEREMIA

8. Kwa nini tunaweza kusema kwamba si lazima mtu afunge ndoa ili ampendeze Mungu?

8 Kwa kumwambia Yeremia asifunge ndoa, Mungu hakuwa akianzisha jambo ambalo watumishi wake wote wanapaswa kufuata. Ndoa ni nzuri. Yehova alianzisha ndoa ili kuijaza dunia na kuwa chanzo cha furaha na shangwe. (Met. 5:18) Hata hivyo, si wote waliofunga ndoa. Huenda kulikuwa na matowashi fulani kati ya watu wa Mungu katika siku za Yeremia.b Isitoshe, lazima pia kulikuwa na wajane. Hivyo basi, si Yeremia tu kati ya waabudu wa kweli ambaye hakuwa na mwenzi. Bila shaka, alikuwa na sababu ya kutofunga ndoa, na ndivyo ilivyo pia kwa Wakristo fulani leo.

9. Ni shauri gani lililoongozwa na roho kuhusu ndoa tunalopaswa kufikiria kwa uzito?

9 Wakristo wengi hufunga ndoa, lakini si wote. Yesu hakufunga ndoa, naye alisema kwamba baadhi ya wanafunzi wake wangekuwa na zawadi ya ‘kuupa nafasi’ useja katika akili na mioyo yao. Aliwahimiza wale ambao wangeweza, wafanye hivyo. (Soma Mathayo 19:11, 12.) Kwa hiyo, ingefaa kumpongeza, wala si kumdhihaki, mtu anayebaki mseja ili kufanya mengi katika utumishi wa Mungu. Ni kweli kwamba Wakristo fulani ni waseja, angalau kwa muda, kwa sababu ya hali. Kwa mfano, huenda hawajapata mwenzi Mkristo anayefaa na hivyo wanaazimia kutii amri ya Mungu ya kufunga ndoa “katika Bwana tu.” (1 Kor. 7:39) Na bila shaka, watumishi fulani wa Mungu ni wajane, na hivyo ni waseja.c Hawapaswi kusahau kamwe kwamba Mungu (na Yesu) wameonyesha kwa muda mrefu kwamba wanawajali waseja.—Yer. 22:3; soma 1 Wakorintho 7:8, 9.

10, 11. (a) Ni nini kilichomsaidia Yeremia kufanikiwa akiwa mseja? (b) Mambo yaliyoonwa katika siku zetu yanathibitisha jinsi gani kwamba waseja wanaweza kuwa na maisha yenye kuridhisha?

10 Yeremia aliendelea kuwa mseja kwa kumtegemea Mungu. Jinsi gani? Kumbuka kwamba Yeremia alilipenda neno la Yehova. Neno hilo lilimwimarisha na kumpa uhakika kwa makumi ya miaka huku akikazia fikira zake huduma aliyopewa na Mungu. Isitoshe, aliepuka mashirika ya wale ambao wangemdhihaki kwa sababu ya kuwa mseja. Aliona afadhali ‘kuketi peke yake’ badala ya kuwa na watu wenye mtazamo mbaya.—Soma Yeremia 15:17.

11 Waseja wengi Wakristo—wanaume kwa wanawake, vijana kwa wazee—wanafuata mfano mzuri wa Yeremia. Mambo yaliyoonwa yanaonyesha kwamba kuna faida kubwa kujishughulisha na utumishi wa Mungu na kushiriki kikamili katika utendaji wa kiroho. Kwa mfano, dada mmoja Shahidi  anayeshirikiana na kutaniko la Kichina anasema: “Upainia umenipa kusudi maishani. Nikiwa mseja, ninakuwa na shughuli nyingi, mambo mengi ya kufanya, na hivyo sijioni mpweke. Kila siku mimi huhisi nimeridhika ninapoona jinsi huduma yangu inavyowasaidia watu. Hilo hunipa shangwe kubwa.” Painia mwenye umri wa miaka 38 anasema: “Nafikiri siri ya kuwa mwenye furaha ni kuwa na maoni yanayofaa kuhusu hali yoyote ile maishani.” Dada mmoja mseja huko Ulaya Kusini alisema hivi waziwazi: “Maisha yangu hayakwenda nilivyokusudia, hata hivyo, nina furaha nami nitaendelea hivyo.”

Picha katika ukurasa wa 97

12, 13. (a) Tunapaswa kuwa na maoni gani yanayofaa kuhusu useja na ndoa? (b) Maisha na shauri la Paulo yanakazia nini kuhusu useja?

12 Inawezekana kwamba Yeremia aliona kuwa maisha yake hayakwenda alivyotazamia alipokuwa kijana? Huenda alitambua pia kwamba hata kwa wale waliofunga ndoa na kuwa na watoto, mambo hayakwenda walivyotazamia. Dada mmoja painia nchini Hispania alisema: “Najua watu waliofunga ndoa walio na furaha na wengine wasio na furaha. Kujua hilo hunisaidia kuona kwamba furaha yangu haitegemei ikiwa nitafunga ndoa au hapana.” Bila shaka, kutokana na kisa cha Yeremia na wengine wengi, ni wazi kwamba mseja anaweza kuwa na maisha mazuri, yenye kuridhisha, na yenye furaha. Maneno ya Paulo pia yanathibitisha hilo: “Sasa nawaambia waseja na wajane, ni vema kwao wabaki kama mimi nilivyo.” (1 Kor. 7:8) Huenda Paulo alikuwa mjane. Vyovyote vile, alikuwa mseja alipokuwa na shughuli nyingi katika utumishi wa umishonari. (1 Kor. 9:5) Je, hudhani kwamba aliweza kutimiza mengi hivyo kwa kuwa alikuwa mseja? Kwake useja ulimaanisha “kumhudumia Bwana daima bila kukengeushwa fikira,” na hivyo akatimiza mambo mengi mazuri.—1 Kor. 7:35.

“Mimi huthamini sana pindi ninazokuwa peke yangu. Ninaweza kuongea na Yehova katika sala. Ninaweza kutafakari na kujifunza kibinafsi bila kukengeushwa fikira. . . . Useja umechangia pakubwa shangwe yangu.”—Babette

13 Paulo aliongozwa na roho kutaja jambo lingine: “Wale [wanaofunga ndoa] watakuwa na dhiki katika mwili wao.” Mungu alimwongoza Paulo kuandika pia ukweli huu muhimu: “Ikiwa yeyote ametulia katika moyo wake . . . kutunza ubikira wake mwenyewe, yeye atafanya vema. Kwa hiyo yeye pia anayeufungisha ndoa ubikira wake anafanya vema, lakini yeye asiyeufungisha ndoa atafanya vema zaidi.” (1 Kor. 7:28, 37, 38) Yeremia hakusoma maneno hayo, hata hivyo, maisha yake ni uthibitisho wa kutosha kwamba useja haumzuii mtu kuwa na maisha yenye kuridhisha katika utumishi wa Mungu. Badala yake unaweza kuchangia pakubwa katika kuwa na maisha yenye kusudi yanayotegemea ibada ya kweli. Ingawa alikuwa amefunga ndoa, Mfalme Sedekia hakutii shauri la Yeremia na ‘kuendelea kuishi’; lakini nabii huyo mseja alifuata mwendo uliomwezesha kuendelea kuishi.

Unaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yeremia wa kubaki akiwa mseja kwa miaka mingi?

BURUDISHA NAWE UBURUDISHWE

14. Uhusiano kati ya Paulo na familia ya Akila unaonyesha nini?

14 Kama tulivyoona mapema, wanaume na wanawake wengi wa siku za Yeremia walifunga ndoa na walikuwa sehemu ya familia. Ndivyo ilivyokuwa pia katika siku za Paulo. Bila shaka, Wakristo wengi wenye familia hawangeweza kwenda kuhubiri katika nchi nyingine, hata hivyo, walikuwa na mengi ya kufanya katika maeneo ya kwao kama vile kuwategemeza ndugu na dada waliokuwa waseja. Kumbuka kwamba Paulo alipofika Korintho, Akila na Prisila walimkaribisha nyumbani kwao na kufanya kazi pamoja naye. Si hayo tu. Urafiki wa Paulo pamoja na familia ya Akila ulimburudisha. Fikiria vyakula vitamu walivyokula pamoja na pindi nyingine walizofurahia kuwa pamoja. Je, Yeremia alichangamana hivyo na wengine? Alitumia useja wake katika utumishi wa Mungu, hata hivyo, hakujitenga na watu. Huenda alifurahia ushirika pamoja na familia za watumishi wa Mungu, labda familia ya Baruku, ya Ebed-meleki, au za wengine.—Rom. 16:3; soma Matendo 18:1-3.

15. Familia za Kikristo zinaweza kuwasaidia Wakristo waseja jinsi gani?

15 Vivyo hivyo leo Wakristo waseja hunufaika kutokana na ushirika kama ule ambao Paulo alikuwa nao pamoja na familia ya Akila. Ikiwa una familia, je, wewe huwashirikisha waseja? Dada mmoja alisema hivi waziwazi: “Nimeuacha ulimwengu nami sitamani kurudi huko. Hata hivyo, bado ninahitaji kuhangaikiwa na kupendwa. Natumaini kwamba Yehova atazidi kuandaa chakula cha kiroho pamoja na kitia-moyo kwa ajili yetu sisi tulio Wakristo waseja. Sisi pia ni watu, hata ingawa baadhi yetu hatuna haraka ya kufunga ndoa. Lakini, nyakati nyingine tunatendewa kana kwamba tuna ukoma. Ni kweli kwamba tunaweza kumtegemea Yehova, lakini tunapohitaji ushirika wa wengine, je, tunaweza kuzungumza na familia yetu ya kiroho?” Maelfu ya akina ndugu na dada waseja wanaweza kujibu ndiyo kwa unyoofu. Wanafurahia ushirika wa aina hiyo katika makutaniko yao. Rafiki zao si akina ndugu na dada wa rika lao tu. Kwa kuwa wanapenda ushirika wa watu, wana marafiki wenye umri mbalimbali, wazee kwa vijana katika familia za Kikristo.

Picha katika ukurasa wa 100

16. Ni mambo gani unayoweza kufanya kuwaburudisha Wakristo waseja katika kutaniko lenu?

16 Ukiwa mwenye ufikirio, unaweza kuwaburudisha waseja kwa kuwaalika katika shughuli za familia, kama vile jioni ya Ibada ya Familia yako. Kula pamoja na ndugu au dada mseja kunaweza kuburudisha sana. Je, mnaweza kupanga kuhubiri pamoja? Namna gani kumwalika Mkristo mseja kufanya kazi pamoja katika Jumba la Ufalme au kwenda madukani pamoja? Familia fulani zimemwalika mjane, au painia mseja ajiunge nao kusafiri kwenda kusanyikoni au likizoni. Ushirika wa aina hiyo huwaburudisha wote.

17-19. (a) Kwa nini watoto wanahitaji usawaziko wanapopanga kuwatunza wazazi waliozeeka au wanaohitaji msaada? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi ambavyo Yesu alitenda kuhusiana na kutunzwa kwa mama yake?

17 Jambo lingine la kufikiria kuhusu ndugu na dada waseja linahusiana na kuwatunza wazazi waliozeeka. Katika siku za Yesu, Wayahudi fulani mashuhuri walitumia ujanja ili kukwepa wajibu wa kuwatunza wazazi wao. Walidai kwamba wanatanguliza majukumu ya kidini waliyokuwa wamejitwika badala ya jukumu walilopewa na Mungu kuelekea wazazi wao. (Marko 7:9-13) Haipaswi kuwa hivyo katika familia za Kikristo.—1 Tim. 5:3-8.

18 Hata hivyo, namna gani ikiwa wazazi waliozeeka wana watoto kadhaa Wakristo? Ikiwa mmoja wa watoto hao ni mseja, je, ni yeye tu ndiye mwenye daraka la kuwatunza wazazi? Dada mmoja kutoka Japani anaandika hivi: “Ningependa kuolewa, lakini kwa sababu nina jukumu la kuwatunza wazazi wangu, siwezi kuolewa. Nina hakika kwamba Yehova anaelewa ugumu wa kuwatunza wazazi na maumivu ya moyo ambayo waseja hupata.” Je, inawezekana kwamba ana ndugu na dada waliofunga ndoa ambao, hata bila kumwuliza maoni yake, wameamua kwamba yeye ndiye atakayewatunza wazazi wao? Katika visa kama hivyo, ni vizuri kukumbuka kwamba Yeremia pia alikuwa na ndugu ambao hawakumtendea kwa haki.—Soma Yeremia 12:6.

19 Yehova anaelewa hisia za waseja na anawahurumia walio na hali ngumu. (Zab. 103:11-14) Hata hivyo, wazazi waliozeeka au wanaohitaji msaada ni wazazi wa watoto wote si wa watoto walio waseja tu. Ni kweli kwamba huenda baadhi ya watoto wakawa wamefunga ndoa na wana watoto wao. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba hawahitaji kuonyesha upendo wao wa asili kuelekea wazazi wao, wala haliwaondolei wajibu wao wa Kikristo wa kutoa msaada unapohitajika. Hata Yesu alipokuwa anakaribia kufa juu ya mti wa mateso, alikumbuka wajibu wake na kuchukua hatua ya kuhakikisha kwamba mama yake anatunzwa. (Yoh. 19:25-27) Biblia haitoi maagizo ya jinsi ambavyo watoto wanapaswa kuwatunza wazazi wao waliozeeka au wanaohitaji msaada; wala haisemi kwamba watoto waseja ndio wenye wajibu mkubwa zaidi wa kuwatunza wazazi. Katika suala hilo, mipango inapaswa kufanywa kwa usawaziko na ufikirio, na kukumbuka mfano ambao Yesu aliweka kwa kumtunza mama yake.

20. Unauonaje ushirika pamoja na waseja katika kutaniko lenu?

20 Akiongozwa na roho, Yeremia alitabiri: “Nao hawatafundishana tena kila mtu na mwenzake wala kila mtu na ndugu yake, wakisema, ‘Mjueni Yehova!’ kwa maana wote watanijua mimi.” (Yer. 31:34) Kwa njia fulani, tayari tunafurahia ushirika huo wa pekee katika kutaniko la Kikristo, kutia ndani ushirika pamoja na ndugu na dada waseja. Bila shaka, sisi sote tunataka kuburudika pamoja nao na kuwaona waseja hao ‘wakiendelea kuishi.’

Unaweza kufanya nini ili kuwaburudisha na pia kuburudishwa na baadhi ya ndugu na dada waseja?

a Katika Maandiko ya Kiebrania hakuna neno “mseja.”

b Isaya alizungumza kinabii na matowashi halisi wa siku zake ambao walishiriki kwa kiasi fulani katika ibada ya Israeli. Alitabiri kwamba kwa sababu ya utii wao matowashi wangepata “jambo lililo bora kuliko wana na mabinti,” wangepata “jina mpaka wakati usio na kipimo” katika nyumba ya Mungu.—Isa. 56:4, 5.

c Huenda wengine wanaishi peke yao kwa sababu wenzi wao, ambao labda si waamini, wamewaacha au wamewataliki kisheria.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki