SOMO LA 10
Mkumbuke Mke wa Loti
Loti aliishi na Abrahamu mjomba wake, katika nchi ya Kanaani. Hatimaye, Abrahamu na Loti wakawa na mifugo mingi hivi kwamba hakukuwa na eneo la kutosha kwa ajili ya wanyama wao. Abrahamu alimwambia Loti: ‘Hatuwezi kuendelea kuishi pamoja katika eneo hili. Tafadhali, chagua upande utakaopenda kwenda nami nitaenda upande ule mwingine.’ Bila shaka Abrahamu hakuwa mbinafsi, sivyo?
Loti aliona sehemu ya nchi iliyo nzuri sana karibu na jiji la Sodoma. Kulikuwa na maji mengi na nyasi mbichi. Kwa hiyo akachagua eneo hilo na kuhamia yeye na familia yake.
Watu walioishi katika jiji la Sodoma na jiji jirani la Gomora walikuwa wabaya sana. Kwa kweli, walikuwa wabaya sana hivi kwamba Yehova aliamua kuharibu majiji hayo. Lakini Yehova alitaka kumwokoa Loti na familia yake, kwa hiyo aliwatuma malaika wawili wamwambie Loti hivi: ‘Ondokeni haraka mahali hapa, kwa sababu Yehova ataliangamiza jiji hili!’
Loti hakuondoka mara moja. Alichelewa. Kwa hiyo malaika walimchukua Loti, mke wake, na binti zake wawili na kuwatoa nje ya jiji, kisha wakawaambia hivi: ‘Kimbieni ili kuokoa uhai wenu! Msitazame nyuma, mkitazama nyuma mtakufa!’
Walipofika katika jiji la Soari, Yehova alinyesha mvua ya moto na kiberiti katika majiji ya Sodoma na Gomora. Majiji hayo mawili yaliharibiwa kabisa. Mke wa Loti alipokosa kumtii Yehova na kutazama nyuma akawa nguzo ya chumvi! Lakini Loti na binti zake walikuwa salama kwa sababu walimtii Yehova. Walihuzunika sana kwa sababu mke wa Loti hakumtii Yehova. Hata hivyo, walifurahi kwa kuwa walisikiliza maagizo ya Yehova.
“Mkumbukeni mke wa Loti.”—Luka 17:32