Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 5/1 kur. 12-18
  • Tutaokokaje?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tutaokokaje?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “MTOAJI WA WOKOVU”
  • KUOKOKA GHARIKA
  • KUOKOKA KWA LOTI KUTOKA SODOMA
  • Kimbilia Ufalme wa Mungu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Yehova Alikuwa “Mwokoaji” Katika Nyakati za Biblia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Yehova Ni “Mwokoaji” Wetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Tayarisha kwa Ajili ya Kukombolewa Kuingia Ndani ya Ulimwengu Mpya
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 5/1 kur. 12-18

Tutaokokaje?

“Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu.”​—Luka 21:36.

1. Sababu gani sikuzote kutajwa kwa wokovu kunasisimua (kunafurahisha), nalo jambo hilo laweza kuonyeshwaje?

KUOKOKA! Sikuzote hilo ni neno lenye kusisimua. Hatulitumii isipokuwa kuna hatari ya kweli na uhitaji wa tendo la haraka. Kwa mfano, baada ya mkutano wa Kikristo kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova mahali petu, huenda tukafanya haraka kwenda nyumbani kwa sababu fulani. Lakini hatuwezi kusema kwamba tulilazimika kuokoka, isipokuwa tuliona moshi. Au fikiria mfano mwingine: Twaona nyumba ya orofa ikiwaka moto nasi twafanya haraka kwenda mahali hapo. Hapo kwenye dirisha ya orofani kuna mwanamke mwenye hofu akiwa na mtoto mikononi mwake! Yuko juu sana asiweze kuruka na ingekuwa hatari sana kumtupa mtoto huyo. Kuna tumaini gani? Ama wazima-moto lazima wafikie watu hao kwa ngazi, ama wanapaswa kutumia mara moja njia ya kutorokea wakati wa moto.

2. Ni mambo gani yanayohusika katika kuokoka?

2 Kwa kweli, kuna zaidi ya sehemu moja katika masimulizi ya kuokoka. Kuna sehemu hizi kubwa: (1) mahali au hali yenye hatari ambayo twapaswa kuitoroka kwa haraka; (2) uhitaji wa mahali pa kukimbilia ambapo twaweza kupata ulinzi na usalama; na (3) lazima ya kutii maagizo ya mtu fulani anayeona hali yetu mbaya, anayeweza kutupa mahali salama na mwenye nia ya kutusaidia kufika hapo. Mtu wa namna hiyo ni wa maana sana.

“MTOAJI WA WOKOVU”

3. (a) Zaburi 18 yaweza kutukumbusha juu ya nini (b) Ni mambo gani yanayokaziwa katika Zaburi 18:1-6?

3 Yehova Mungu ni Mtoaji wa wokovu asiyelinganika. Tafadhali fungua Zaburi 18 iliyotungwa na Daudi ‘katika siku ile ambayo Yehova alimwokoa kutokana na mkono wa adui zake zote na kutoka katika mkono wa Sauli.’ Kutaja tu mfalme mwanadamu wa kwanza wa Israeli, Sauli, kwaweza kutukumbusha vizuri sana namna Daudi alivyokuwa akiona kwamba kifo kilikuwa kinamwelekea. Ala, mara tatu mfalme huyo alijaribu kumpigilia Daudi ukutani kwa mkuki! (1 Sam. 18:11; 19:10) Baadaye, kwa miaka kadha Daudi alifanywa awe mtorokaji, akiwindwa wakati wote na Sauli. (1 Sam. 26:20) Tukikumbuka hayo, twaweza kuwaza vizuri shauku ambayo Daudi alisema maneno ya utangulizi ya Zaburi 18, ambapo twasoma hivi: “Nitakuwa na shauku kwako, Ee Yehova nguvu yangu. Yehova ni jabali langu na ngome yangu na Mtoaji wa wokovu wangu. Mungu wangu ni mwamba wangu. Nitakimbilia kwake, ngao yangu na pembe yangu ya wokovu, mwinuko wangu salama. Yeye anayepaswa kusifiwa, Yehova, nitamwita, nami nitaokolewa kutoka kwa adui zangu. Kamba za mauti zilinizunguka; mafuriko ya ghafula ya watu wasiofaa kitu yaliniogopesha pia. . . . Katika taabu yangu niliendelea kumwita Yehova, nami nikaendelea kumlilia Mungu wangu anipe msaada. Akiwa hekaluni mwake akasikia sauti yangu, nacho kilio changu cha kutaka msaada kikafika masikioni mwake.”​—Mist. 1-6, NW.

4. Yehova anapewa cheo gani bora, nayo Zaburi 18 inaonyeshaje kufaa kwa cheo hicho?

4 Yehova alipewa cheo bora na chenye kufariji kama nini kwa sababu ya hayo—“Mtoaji wa wokovu.”Na je! Yehova Mungu alijionyesha kuwa hivyo? Hakika ndiyo, kwa maana baada ya kusimulia vitendo vikuu vya Yehova, Daudi aliendelea kusema hivi:“Alikuwa akiniokoa kutoka kwa adui yangu mwenye nguvu, na kutoka kwa wale wenye kunichukia; kwa sababu walikuwa wenye nguvu kunishinda. Wakawa wananikabili katika siku ya msiba wangu, walakini Yehova akawa tegemezo langu. Naye akaniingiza ndani ya mahali penye nafasi tele; alikuwa akiniokoa, kwa sababu alikuwa amependezwa nami.”​—Zab. 18:17-19, NW.

5, 6. (a) Zaburi 37 inasaidiaje watu wa Yehova waweke uhakika kwake akiwa “Mtoaji wa wokovu”? (b) Hali ya uharaka inakaziwaje katika Zaburi 70?

5 Mara nyingi katika Zaburi yote Daudi ajitumia kichwa icho hicho. Katika Zaburi nne kati ya hizo, anamwita Yehova kuwa “Mtoaji wa wokovu.” (Zab. 18:2, 40:17, NW; 70:5, NW; 144:2, NW) Wakati sisi, tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunapozungumza na wengine juu ya sifa na makusudi ya Yehova, mara nyingi tunatumia visehemu vya Zaburi 37. Walakini sasa angalia namna inavyomalizia kwa njia nzuri sana: “Wokovu wa wenye haki unatoka kwa Yehova; yeye ni boma lao wakati wa taabu. Naye Yehova atawasaidia na kuwatolea wokovu. Atawatolea wokovu kutokana na watu waovu na kuwaokoa, kwa sababu wamekimbilia kwake.” (Mist. 39, 40, NW) Maneno hayo yanapaswa kuchochea watu wa Yehova kama nini wapate kuweka uhakika wao kwake!

6 Zaburi 70 inaonyesha hali ya uharaka kwa waziwazi. Ni wakati Daudi alipokuwa na uhitaji sana alipoomba hivi: “Ee Mungu, njoo uniokoe, Ee Yehova, njoo unisaidie haraka. . . . Mimi mwenye taabu maskini. Ee Mungu, tenda haraka kwa ajili yangu. Wewe u msaada wangu na mtoaji wa wokovu wangu. Ee Yehova, usichelewe sana.”​—Zab. 70:1, 5, NW.

7. Twaweza kusali kwa Yehova kwa kufaa tukiwa na maoni gani tunapohitaji msaada kwa haraka?

7 Je! umepata kuona hivyo? Inafariji na kutia imani nguvu kujua kwamba sisi, tukiwa watumishi wa Yehova, twaweza kuwa na hakika kwamba ‘atatenda haraka’ kwa ajili yetu. Yeye anajua mahitaji yetu na namna ya kuyatosheleza. Baba yetu wa kimbinguni mwenye upendo kwa hakika ni “Mtoaji wa wokovu” wakati tunapouhitaji. Nyakati nyingine, kama Daudi, twakubali kwamba makosa yetu wenyewe yametuingiza katika hali mbaya. Lakini, kama Daudi, twaweza kumfikia Yehova kwa unyofu wa moyo, pengine kwa “roho iliyovunjika,” tukiwa na hakika kwamba Yeye atasikia na kujibu sala yetu. Twaweza kusihi, kama vile Daudi alivyosihi: “Ee Mungu, uniumbie moyo safi, uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.”​—Zab. 51:10, 17.

8. Yesu Kristo anafanya sehemu gani katika kupokea kwetu “msaada wakati wa mahitaji”?

8 Jambo jingine la kukumbuka ni kwamba Mungu wetu ametoa Kuhani Mkuu anayeweza “kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu” na ambaye kupitia kwake twaweza kufikia “kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.” Hakika twashukuru kwa ajili ya Kuhani Mkuu huyo mwenye huruma, Yesu Kristo, ambaye, chini ya uongozi wa Babaye, aweza ‘kutuacha huru’ au kutoa njia ya kuokoka kutoka kwa utumwa wa kiroho.​—Ebr. 2:15; 4:15, 16.

9. (a) Ni wakati gani peke yake Yesu alipozungumza juu ya “kuokoka”? (b) Ni mambo gani mawili yanayopaswa kuangaliwa wakati wa kuokoka?

9 Kulingana na maandishi ya Injili, ni mara moja tu Yesu Kristo, Daudi Mkuu, alipotaja “kuokoka.” Alipokuwa akizungumza juu ya “mwisho wa taratibu ya mambo,” aliwasihi wanafunzi wake hivi: “Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu.” (Luka. 21:36; Mt. 24:3, NW) Walakini, kabla ya kuchunguza kifungu hicho cha maneno kwa urefu, tutarudia masimulizi fulani yenye kusisimua ya wokovu yaliyoandikwa katika Maandiko ya Kiebrania, tukiangalia baadhi ya masomo ya maana tunayopaswa kujifunza na kuyatumia kwetu. Tunapokuwa hatarini, kuna hatua za lazima zisizobadilika zinazopaswa kuchukuliwa na mambo fulani yanayopaswa kuepukwa ili kufaulu kuokoka. Tutaona hayo tutakapokuwa tukichunguza visa vilivyotokea.

KUOKOKA GHARIKA

10, 11. Kuokoka kwa Noa na jamaa yake kulitegemea nini, walakini kuokoka kunakuwa hakuwezekani wakati gani?

10 Masimulizi ya kwanza tutakayochunguza yanasisimua kweli kweli, maana yalihusu uharibifu wa dunia yote ya waovu. Je! kungekuwako wokovu kwa ye yote? Kumbuka, Yehova alimwaambia Noa hivi: “Na tazama, nitaleta gharika ya maji juu ya [dunia], niharibu kila kitu chenye mwili na pumzi ya uhai, kisiwepo chini ya mbingu; kila kilichoko duniani kitakufa.” (Mwa. 6:17) Hata hivyo, tayari Yehova alikuwa amempa Noa maagizo marefu ya kujenga safina. Baada ya onyo hilo la gharika ya duniani pote, Mungu alimwagiza Noa juu ya yale ambayo yeye na jamaa yake wangepaswa kufanya ili wao, pamoja na viumbe vingine vyenye uhai, wahifadhiwe hai na kuokoka wasigharikishwe na gharika yenye kuharibu.

11 Kuokoka kulitegemea nini? Hiyo inaonyeshwa wazi na maneno haya: “Ndivyo alivyofanya [Noa], sawasawa na vyote alivyoamuru Mungu, hivyo ndivyo alivyofanya.” (Mwa. 6:22) Mungu anapotoa amri iliyo wazi au maagizo, kutii bila mashaka kunatakiwa. Iwapo cho chote kama agizo au onyo kinapuzwa, kuokoka kunakuwa hakuwezekani. Kisha matokeo yanakuwa sawasawa na yale yaliyopata sehemu nyingine ya jamaa ya kibinadamu katika siku za Noa. Yesu alisema hivi juu ya maoni yao na yaliyowapata: “Wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawa chukua wote.” (Mt. 24:39) Watu hao hawakuweza kuokoka kwa sababu hawakubali hali mbaya iliyowaelekea nao hawakukaza fikira kwenye maagizo yo yote ya kuokoka yaliyotolewa na “Mtoaji wokovu” kupitia kwa Noa.

12. Kulingana na 1 Petro 3:20, zile “nafsi nane” ziliokokaje katika siku za Noa?

12 Katika masimulizi hayo, jambo moja jingine ni la kuangaliwa sana sana. Hizo “nafsi nane” ziliokokaje? Angalia vizuri jibu la mtume Petro. “Walichukuliwa salama katika maji.” (1 Pet. 3:20 NW) Walikuwa ndani kabisa mwa mambo yaliyokuwa yakitendeka nao hawakuokolewa kwa kutolewa duniani, kwa mfano, kwenda kwenye safari ya mwezini. Kama tutakavyoona, jambo kama hilo laweza kuwapata wale wanaomtumikia Yehova leo.

KUOKOKA KWA LOTI KUTOKA SODOMA

13. Ikawaje Loti akaja kuishi Sodoma?

13 Kisha, na tukumbuke kuokoka kwa Loti kutoka Sodoma. Kumbuka msingi wa mambo hayo. Kwa sababu ya kutokuwapo kwa ardhi ya kulishia wanyama wao wote, Abrahamu alimpa Loti nafasi ya kuamua mahali ambapo angeenda. “Basi [Loti] akajichagulia Bonde lote la Yordani; [Loti] akasafiri kwenda upande wa mashariki. . . . Akaiongeza hema yake mpaka Sodoma. Lakini watu wa Sodoma walikuwa wabaya, wenye kufanya dhambi nyingi sana juu ya [Yehova].” Bila shaka Loti alikuwa anajua wakaaji wa Sodoma walikuwa na sifa mbaya. Walakini nafasi ya kufanikiwa kupata mali ilikuwapo katika wilaya hiyo, maana ‘ilikuwa na maji . . . ilikuwa kama bustani ya [Yehova].’​—Mwa. 13:5-13.

14. Wakati onyo la haraka lilipotolewa, lilikuwaje itikio la: (a) Wakwe za Loti? (b) Loti mwenyewe mara mbili? (c) Mkewe Loti?

14 Muda si muda, malaika wawili, walijivika miili ya kibinadamu, wakaja Sodoma na kumwambia Loti juu ya uamuzi wa Yehova ‘kuharibu mji huo.’ Mara moja, Loti akawaonya waliokuwa wanatarajia kuwa wakwe zake. Walakini je! wakubali hali mbaya iliyokuwa inawaelekea na uhitaji wa kutoroka haraka, jambo ambalo linakuwa la kwanza katika kuokoka ko kote kunakofanikiwa? Hapana, “lakini [Loti] akawa kama achezaye machoni pa wakweze.” (Mwa. 19:12-14) Kulipopambazuka, “wakamhimiza [Loti],” kwamba atende bila kuchelewa. Aliitikiaje? “Akakawia-kawia.” Lakini “kwa jinsi [Yehova] alivyomhurumia,” kwa kufanya haraka malaika hao walimwongoza Loti, mkewe na bintize wawili kutoka mjini. Nao wakasihiwa wasonge mbele kwa maneno haya: “Jiponye nafsi yako; usitazame nyuma. . . . ujiponye mlimani, usije ukapotea!” Kwa mara nyingine, Loti aliitikiaje? “[Loti] akawaambia, Sivyo, [Yehova]! . . . Basi mji huu u karibu, niukimbilie, nao ni mdogo, nijiponye sasa huko, sio mdogo huu? Na nafsi yangu itaishi.” Kwa huruma na rehema za Yehova, ombi la Loti lilikubaliwa naye akakimbilia kwenye mji wa Soari. Lakini namna gani mke wa Loti? Kwa kukusudia alipuza maagizo yaliyokuwa wazi. “Mkewe [Loti] akatazama nyuma yake, akawa nguzo ya chumvi.”​—Mwa. 19:15-26.

15. (a) Je! Loti aliokoka kuharibiwa kwa ajili ya mambo aliyofanya? (b) Kuokoka kwa Loti kwaweza kutokeza maulizo gani ya kibinafsi?

15 Twajifunza nini kutokana na yote hayo? Je! Loti alifanikiwa akaokoka kwa sababu ya aliyofanya mwenyewe? Sivyo, kwa maana maombi ya bidii ya Abrahamu aonyeshwe rehema vilevile yalisaidia. (Mwa. 18:20-33) Basi, “ikawa Mungu alipoiharibu miji ya Bondeni, Mungu akamkumbuka [Abrahamu], akamtoa [Loti] katika maangamizi.” (Mwa. 19:29) Zaidi ya hayo, Mungu alimwokoa Loti kwa sababu, akiwa mtu “mwenye haki,” alisikitika kabisa kwa ajili ya mwenendo mwovu wa “watu wenye kuasi sheria” ambao alikuwa akikaa kati yao. (2 Pet. 2:7, NW) Hata hivyo, Loti hakufanya haraka kutoka Sodoma, ambapo palikuwa na baadhi ya mali zake. Ilikuwa lazima ahimizwe na hata kushikwa mkono. (Mwa. 19:16) Kwa kufikiria kuokoka kwa Loti, twaweza kujiuliza hivi kwa kufaa: Je! tunasikitika kweli kweli kwa ajili ya watu wasiomcha Mungu, wanaoasi sheria? Na, ili kuokoka, je! tuna nia ya kukazia zaidi faida za kiroho kuliko faida za kimwili?​—Mt. 6:33.

16. Kulikuwako tofauti gani kati ya kuitikia kwa Loti na kwa Abrahamu?

16 Tofauti na kunyamaza kwa Loti asikimbie haraka, fikiria yaliyotokea wakati “Mungu alimjaribu [Abrahamu]” na kumwambia amtoe mwanawe mpendwa Isaka awe dhabihu ya kuteketezwa. Ni kweli kwamba kuokoka hakukuhusika. Walakini Abrahamu aliitikiaje? Je! alikawia-kawia? Au je! alisihi apewe jambo jingine la kutoa kama dhabihu? Hasha! “[Abrahamu] akaondoka alfajiri!” na mara moja akaanza safari hiyo ya siku tatu, akiwa na Isaka kando yake. Hata alifikia hatua ya kutwaa “kisu ili amchinje mwanawe,” wakati Mungu alipomsimamisha hata Isaka akahifadhiwa hai.​—Mwa. 22:1-14.

17. (a) Kwa kufikiria mambo ambayo yamezungumzwa sasa hivi, twapaswa kuweka somo gani mioyoni? (b) Ni maneno gani ya Yesu yanayotusaidia, tukiwa wafuasi wake, ili tuchanganue hali yetu kuhusiana na taratibu ya mambo iliyopo?

17 Hapo kuna somo tunalopaswa kuweka moyoni. Tusifuate mwendo wa haki kwa njia ya kutotenda tu, tukitosheka na kuepuka mwenendo mbaya peke yake. Tusikawie-kawie wakati wo wote tupate kuona namna tunavyoweza kukaa karibu na taratibu hii mbovu ya mambo, tukiwa na uhusiano mwema nayo na kujaribu kupata faida zake zote za kimwili na anasa yote tuwezayo. Ilionyeshwa wazi kwamba wafuasi wa Yesu wasingekuwa na maoni ya kilimwengu wakati Kristo aliposema hivi katika kusali Mungu: “Mimi nimewapa neno lako; na ulimwengu umewachukia; kwa kuwa wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.”​—Yohana 17:14.

18. Yesu alihusianishaje masimulizi ya Noa na Loti, nayo mambo hayo yanatuhusu sisi leo?

18 Pindi moja, Yesu alihusianisha sana masimulizi ya Noa na Loti, akasema kwamba yalikuwa na maana ya kiunabii ya kuja kwa “siku zake Mwana wa Adamu.” Ingawa mambo hayo yalitimizwa juu ya kizazi cha siku za Yesu, yana utimizo mkubwa zaidi katika siku zetu, katika huu “wakati wa mwisho.” (Luka 17:26-33; Dan. 12:1-4) Katika ‘siku za mwisho za Loti,’ kulingana na masimulizi ya Biblia, si kwamba tu watu walikuwa wakila na kunywa, kama vile katika siku za Noa, bali pia walikuwa wakiuza, kununua, kupanda na kujenga. Inafanana na leo kama nini, wakati ambapo ni rahisi sana kushughulika sana na mambo ya maisha ya kila siku! Hakika, mikazo mibaya inayotokana na mambo kama infuleshoni na utukuzo wa taifa, pamoja na vishawishi vya “fanya jambo lako mwenyewe” na kuingilia ulimwengu, ni vikubwa zaidi ya wakati mwingineo uliotangulia.

19. Katika unabii wake mkubwa duniani, Yesu alisema ni mambo gani yangetokeza hali yenye hatari, kisha akatoa onyo gani?

19 Sasa, fikiria unabii mkubwa wa Yesu unaosimulia kutokea kwa mambo ambayo yangetokea katika siku zetu, yakitokeza hali yenye kutisha na ya hatari sana ambayo kuokoka kutoka kwayo kungekuwa kwa lazima. Alisema kwamba kungekuwako “huzuni kuu ya mataifa, . . . huku wanadamu wakizimia moyo kwa sababu ya hofu na kutazamiwa kwa mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu.” Hayo yangefikia upeo wayo katika “dhika kubwa,” wakati ‘mbingu na dunia’ za Shetani zitakapoondolewa. (Luka 21:10-33, NW; Mt. 24:21; 2 Pet. 3:7) Kisha laja onyo la wakati wake: “Basi, jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajilia ghafula, kama mtego unasavyo; kwa kuwa ndivyo Itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima. Basi, kesheni ninyi kila wakati mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu.”​—Luka 21:34-36.

20. (a) Noa ‘alitembeaje pamoja na Mungu wa kweli nyakati zote? (b) Vivyo hivyo, twapaswa kuwa waangalifu kufanya nini?

20 Basi, tutaokokaje? Si kwa kuondolewa mahali ambapo mambo yatakuwa yakitendeka. Mahali pake, twapaswa kutafuta mfano wa Noa, ambaye alikuwa mwangalifu kutii katika kujenga na kisha pamoja na jamaa yake, kuingia ndani ya mpango wa kimungu, safina. Katika miaka yote hiyo migumu, aliendeleza msimamo unaokubalika mbele za Yehova. “Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli.” (Mwa. 6:9, NW) Kama vile Noa twapaswa kutambua kwamba kuna hali yenye hatari ambayo twapaswa kuitoroka kwa uharaka. Vilevile kama vile mwanamume yule wa imani, twapaswa kuwa waangalifu kutii “Mtoaji wa wokovu,” tukitenda kupatana na maagizo ya kimungu katika nyakati hizi zenye hatari. Kwa upande mmoja, twapaswa kuepuka kujiingiza sana katika kutosheleza tamaa zetu kupita kiasi au kulemewa na mahangaiko ya riziki ya kila siku, jambo ambalo lingetokeza maoni ya kusinzia na kukawia-kawia. Hivyo tutapata hasara wakati siku hiyo itakapokuja kama mtego wa ghafula. Kwa upande mwingine, nyakati zote twapaswa kuwa macho na twapaswa kukesha kiroho, kwa njia ya sala tukimwendea Mungu kwa maombi ya bidii. Hakupaswi kuwe mashaka akilini mwetu juu ya upande tulioko—upande wa ufalme wa Mungu chini ya Mfalme wake, Kristo Yesu.​—Mt. 6:31-34.

21. Tunatiwaje moyo tuendeleze msimamo wa kukubalika nyakati zote?

21 Ni jambo la lazima kwamba tutafute kuendeleza msimamo wa kukubalika mbele ya Mwana wa Adamu, Yesu Kristo, kupitia kabisa katika hizi nyakati za hatari. Kufanya hivyo kwaweza kuwa kwenye kujaribu, walakini haitakuwa vigumu zaidi ya tunavyoweza kuvumilia tukiendelea kuwa macho na watiifu. Mtume Paulo anatuhakikishia hivi: “Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea [kwa lazima si kutolewa katika hali hiyo, bali], ili mweze kustahimili.” Hivyo, tunahitaji kusitawisha uvumilivu, ili tushinde majaribu na vishawishi tupate kuendelea ‘kusimama,’ tukiwa waaminifu, katika huu ‘mwisho wa taratibu ya mambo.’​—1 Kor. 10:11-13; Mt. 24:3, NW.

22. Twapaswa kuangalia wapi tupate uongozi ili tuokoke, na sababu gani?

22 Hata hivyo, kuna zaidi yanayoweza kusemwa katika kujibu maulizo haya: Tutaokokaje? Tutatorokaje? Ndiyo, katika habari hii, ebu tuchunguze zaidi Neno la Mungu, Yehova, anayejua mahitaji yetu naye atatuangalia tunapoendelea kutafuta uongozi wake kwa unyenyekevu. 1 Pet. 5:6, 7.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Noa na jamaa yake walitii onyo la Mungu

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kutii onyo la kimalaika katika siku za Loti

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki