Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 5/1 kur. 18-23
  • Kimbilia Ufalme wa Mungu!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kimbilia Ufalme wa Mungu!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • NAMNA YA KUFANIKIWA KUOKOKA
  • UKIMBILIE MJI WA MUNGU—SAYUNI
  • Tutaokokaje?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Kitabu cha Biblia Namba 58—Waebrania
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Jihadhari na Ukosefu wa Imani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • “Tokeni Kwake, Enyi Watu Wangu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 5/1 kur. 18-23

Kimbilia Ufalme wa Mungu!

1. Katika barua ya Paulo aliyowaandikia Waebrania, ni jambo gani linaloonekana kuhusiana na kuokoka?

MTUME Paulo, katika barua yake aliyoandikia Waebrania, ana mambo fulani ya maana kusema kuhusiana na wokovu. Anazungumza juu ya sehemu mbili: mambo yanayopaswa kufuatwa na mambo yanayopaswa kuepukwa. Katika kuunga mkono hoja yake, mara nyingi anataja maneno kutoka Maandiko ya Kiebrania, ambayo wasomaji wake wa wakati huo—Wayahudi waliokuwa wamekuwa Wakristo—walikuwa wanafahamiana nayo sana.

2. Paulo alimlinganishaje Mwana wa Mungu pamoja na malaika, hiyo inaongoza kwenye kukata shauri gani?

2 Katika sura ya kwanza ya Waebrania, Paulo anakazia cheo kikuu cha Mwana wa Mungu juu ya malaika. Kisha mtume huyo anasema hivi: “Ndiyo sababu ni lazima kwetu [sisi Wakristo] kuangalia sana kuliko kawaida mambo tuliyosikia, ili tusichukuliwe kamwe na mkondo wa maji. Kwa maana, ikiwa lile neno lililonenwa na malaika lilikuwa imara, . . . sisi je! tutaokokaje iwapo tumepuza wokovu mkuu namna hiyo maana ulianza kusemwa kupitia kwa Bwana yetu [Yesu Kristo] . . . ?”​—Ebr. 2:1-4, NW.

3. (a) Tumaini la wokovu kupitia kwa Kristo Yesu ni bora zaidi ya tumaini gani jingine, na katika njia gani? (b) Ni jambo gani linalohusianishwa na ‘tumaini hilo zuri zaidi’? (c) Kuna uhitaji gani, matumaini yetu yawe ni ya kimbinguni au ya kidunia?

3 Tumaini la wokovu lililotolewa kupitia kwa Yesu Kristo ni bora zaidi na kuu zaidi ya lililotolewa kupitia kwa Torati ‘iliyopitishwa kwa malaika’ katika Mlima Sinai. (Gal. 3:19, NW) Ni bora zaidi kwa sababu msingi wake ni “agano lililo bora zaidi . . . lililoamriwa juu ya ahadi zilizo bora,” dhabihu bora zaidi (iliyotolewa “mara moja tu,” ikitoa “matumaini yaliyo mazuri zaidi”) na ukuhani mkuu zaidi unaofanana na ule wa Melkizedeki. (Ebr. 7:15-25; 8:6; 9:23-28) Hata hivyo, hilo ‘tumaini zuri zaidi’ linahusianishwa na daraka kubwa zaidi. Hivyo, kuna uhitaji wa kukaza fikira sana kuangalia ili kuepuka kupuza kwa namna yo yote, “tusije tukayakosa.” Na ingawa ni wokovu wa kimbinguni unaotajwa hapa, madaraka ayo hayo yako juu ya wale wenye tumaini la wokovu wa kidunia chini ya ufalme wa Mungu.

4. Maana yake nini kuchukuliwa na mkondo wa maji nalo jambo hilo lawahusuje Wakristo?

4 Ni jitihada kadiri gani, inayohitajiwa ili mtu aanze kuchukuliwa na mkondo wa maji? Hakuna. Tukiwa mtoni, tuwe tu ndani ya mashua au ndani ya maji, tunachukuliwa na mkondo wa maji upande ambao maji yanaelekea. Ndivyo ilivyo maishani. Iwapo sisi, tukiwa Wakristo, tunaanza kuchukuliwa, twaenda pamoja na uvutano wo wote unaokuja tulipo, ama wa kutoka nje ama wa kutoka ndani wa maelekeo tuliyorithi. Tunaanza kukosa kuthamini sifa za kiroho. Jambo hilo laweza kusitawi polepole nalo lapaswa kuangaliwa. Kama sivyo, tusingekuwa ‘tukikamata kabisa uzima wa kweli’ nasi tungekuwa katika hatari ya kupoteza maisha kabisa. (1 Tim. 6:19, NW) Kama ambavyo Paulo alitaja, twaweza kuokokaje matokeo ya mwisho yenye msiba iwapo maoni hayo ya kupuza pamoja na mwendo hayazuiliwi?

5. Maneno yanayofuata ya Paulo aliyowaandikia Waebrania Wakristo yanatujulisha juu ya hali gani ya moyo yenye hatari?

5 Maneno yanayofuata ya mtume huyo aliyoandikia Waebrania Wakristo, yanatujulisha mwendo hatari zaidi. Yeye aliandika hivi: “Angalieni, ndugu zangu, usiwe katika mmoja wenu moyo mbovu wa kutokuamini, kwa kujitenga na Mungu aliye hai. Lakini mwonyane kila siku, maadamu iitwapo leo; ili mmoja wenu asifanywe mgumu kwa udanganyifu wa dhambi.”​—Ebr. 3:12, 13.

6. (a) Nini maana ya “kujitenga” na mtu? (b) Nini kinatokeza “kujitenga na Mungu aliye hai,” nalo jambo hilo laweza kuepukwaje?

6 Haihitaji jitihada ili mtu aanze kuchukuliwa na mkondo; walakini kuanza “kujitenga” na mtu fulani kunahitaji tendo fulani. Ingawa huenda tukawa tunamwelekea mtu katika kujaribu kuendelea kuwa na kibali yake, twaweza kuanza kurudi nyuma kutoka alipo kwa kupiga hatua kurudi nyuma. Sababu gani mtu ye yote anaweza kuanza “kujitenga na Mungu aliye hai”? Jibu ni hili: Kwa ajili ya kukosa imani. Kama ambavyo mistari inayozunguka inavyoonyesha, Paulo hazungumzi juu ya imani dhaifu ambayo imetokana na maarifa machache au ufahamu wa makosa. Mahali pake, anataja onyo hili, ‘Msifanye mioyo yenu kuwa migumu.’ Hivyo ndivyo Waisraeli wa kimwili walivyofanya jangwani, ijapokuwa walipokuwa humo walikuwa wameona ‘matendo ya Yehova ya miaka arobaini,’ wakiwa wakati wote wamefurahia misaada na ulinzi wake wa kimwujiza. (Ebr. 3:7-11) Kwa hiyo, Wakristo wote wa kweli leo wanapaswa kusaidiana na kutiana moyo wakati wote ili wasipige hatua za kurudi nyuma kwa ajili ya ‘kufanywa wagumu kwa udanganyifu wa dhambi.’ Twapaswa kutiana moyo ili imani yetu iendelee kuwa hai. Namna gani? Kwa matendo ya imani. Kumbuka, Abrahamu alitenda kwa kutii katika imani chini ya jaribu kali na hivyo ‘akaja kuitwa rafiki ya Yehova.’ Sisi, tukiwa mashahidi wa Yehova leo, tutashinda tu “kama tukishikamana na mwanzo wa uthabiti wetu kwa nguvu mpaka mwisho.”​—Ebr. 3:13, 14, UV; Yak. 2:21-26, NW.

7. Mwishoni mwa barua yake aliyowaandikia Waebrania, Paulo anaonyeshaje kwamba daraka walilo nalo Wakristo ni kubwa zaidi ya lile walilokuwa nalo Waisraeli wa kimwili?

7 Mwishoni mwa barua yake aliyowaandikia Waebrania, Paulo anazungumza kwa hoja ile ile aliyoizungumza katika Waebrania 2:1-4. Anaonyesha daraka kubwa zaidi walilo nalo Wakristo, ikilinganishwa na Waisraeli wa kimwili. Hata hivyo, anatumia usemi wenye nguvu zaidi na kusema hivi: “Maana ikiwa hawakuokoka wale waliomkataa yeye aliyewaonya juu ya [dunia], zaidi sana hatutaokoka sisi tukijiepusha na yeye atuonyaye kutoka mbinguni.”​—Ebr. 12:25.

8, 9. (a) Ni nini yanayotiwa ndani ya kujitenga na mtu, na, katika mambo ya kiroho, jambo hilo laweza kuongoza kwenye matokeo gani? (b) Twawezaje na sababu gani twapaswa kuweka mambo hayo moyoni mwetu (c) Ni nini kitatokea tukikubali adabu ya Mungu?

8 Kujitenga na mtu kunamaanisha kumgeuzia kisogo makusudi mtu huyo na mara nyingi kunaonyesha kukataa. Hayo ndiyo yaliyokuwa maoni na mwendo uliochukuliwa na Waisraeli wa kimwili wakiwa taifa mpaka wakati wa Malaki, wakati Yehova alipowaambia hivi: “Tokea siku za baba zenu mmegeuka upande, mkayaacha maagizo yangu wala hamkuyashika.” (Mal. 3:7) Naye Mkristo aliyetiwa mafuta, Mwisraeli wa kiroho, akichukua hatua hizo mbaya moja baada ya nyingine, matokeo yatakuwa nini? Kuna hatari mbaya sana kwamba atakuwa katika kikundi cha wale ambao Paulo aliandika hivi juu yao: “Kwa maana hao waliokwisha kupewa nuru, . . . wakaanguka baada ya hayo, haiwezekani kuwafanya upya tena hata wakatubu.” (Ebr. 6:4-6) Bila shaka, ni Yehova Mungu na Kristo Yesu peke yao wanaoweza kuamua kama mtu amekwisha kufika mahali ambapo haiwezekani akarudishwa tena kwenye toba.

9 Twapaswa kuweka maonyo hayo moyoni. Kukosa imani kwaweza kuanza kwa ajili ya kujiruhusu tuchukue mambo vivi hivi, tukionyesha roho ya ubaridi, tuchukuliwe bila kufahamu. Hatua moja ya uongo au maoni kwa urahisi huongoza kwenye nyingine mpaka twende mbali sana, nasi twajikuta tumeanguka tusiweze kupata nafuu tena. Bila shaka kabla hilo halijatokea Yehova atatupa adabu, ambayo Paulo anazungumza juu yake katika barua ii hii nalo ni shauri tupaswalo kulikubali kwa heshima: “Mmeyasahau yale maonyo, yasemayo nanyi kama kusema na wana, Mwanangu, [usidharau adabu ya Yehova], wala usizimie moyo [ukikaripiwa] naye; maana yeye ambaye [Yehova] ampenda, [humwadibu], naye humpiga kila mwana amkubaliye. . . . Kila [adabu] wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao aliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani.”​—Ebr. 12:5-11.

10. Sababu gani hatupaswi kuwa na maoni yasiyofaa au kuona mambo kuwa mabaya kwa habari ya ndugu zetu wa kiroho au hata sisi wenyewe?

10 Kutokana na hayo, hatupaswi kukaa shauri kwamba Paulo alikuwa na maoni yasiyofaa au ya kuona mambo kuwa mabaya kwa habari ya nduguze wa kiroho. Wala sisi hatupaswi kujiona wenyewe au wengine kundini katika njia hiyo. Hata baada ya mtume huyo kuwaambia Waebrania hao Wakristo kwamba walikuwa ‘wamekuwa wavivu wa kusikia’ nao walikuwa ‘wanahitaji maziwa wala si chakula kigumu’​—na baada ya kutoa onyo juu ya wale wanaoanguka wasiweze kutubu—anasema hivi: “Lakini, wapenzi, ijapokuwa twanena hayo, katika habari zenu tumesadiki mambo yaliyo mazuri zaidi, na yaliyo ya wokovu.” Kisha Paulo anatoa kitia-moyo kizuri kwamba “mkawe wafuasi wa hao wazirithio ahadi kwa imani na uvumilivu.”​—Ebr. 5:11, 12; 6:4-6, 9-12.

NAMNA YA KUFANIKIWA KUOKOKA

11. Danieli aliongozwa kwa roho atabiri juu ya kuokoka kwa watu wa Mungu katika unabii gani?

11 Jambo kuu katika kuokoka ko kote ni kukimbia kutoka mahali au hali yenye hatari na kufanya hivyo kwa uharaka. Je! Kuna uhitaji wa kuchukua tendo hilo leo? Hakika ndiyo. Yakihusiana moja kwa moja na hali yenye hatari ambayo katika hiyo Wakristo sasa wanajikuta ni maneno haya ambayo nabii Danieli aliongozwa kwa roho aandike: “Wakati huo Mikaeli atasimama, jemadari mkuu, asimamaye upande wa wana wa watu wako; na kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo; na wakati huo watu wako wataokolewa kila mmoja atakayeonekana ameandikwa katika kitabu kile.” (Dan. 1:1) Ndiyo, watu wa Danieli—kwa kweli watu wa Mungu—wangeokoka. Hilo lilikuwa hakikisho zuri ajabu kama nini!

12. (a) Yesu alitaja unabii wa Danieli wakati gani? (b) Ni wakati gani na ni kwa ajili ya nani Mikaeli alisimama na kuonyesha uwezo wake?

12 Akielekeza kwenye utimizo mkubwa wa ajabu katika siku zetu, “wakati wa mwisho,” Yesu alitaja maneno hayo alipokuwa akitoa unabii wake mkubwa ambao umeandikwa katika Mathayo sura ya 24. Yeye alisema hivi: “Kwa kuwa wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.” (Dan. 12:4; Mt. 24:21) Tangu mwaka 1914 W.K. Yesu Kristo amekuwa mkuu wa kimbinguni, Mikaeli, ambaye amesimama na kuonyesha uwezo wake kwa ajili ya watu wa Mungu leo. Nao ni akina nani? Si Waisraeli wa kimwili, bali mabaki ya Waisraeli wa kiroho ambao ‘tohara yao ni ya moyo, katika roho, si katika andiko.’​—Rum. 2:29.

13. Ni tokea wakati gani mabaki ya Waisraeli wa kiroho wametolewa mwito watoke katika Babeli Mkuu, nayo hali yao kabla ya wakati huo ilikuwaje?

13 Hata hivyo, sana sana tangu mwaka 1919 W.K. ndipo mabaki hawa waaminifu waliotakaswa wametii mwito huu: “Haya! haya! ikimbieni nchi ya kaskazini. . . . Haya! Ee Sayuni, jiponye, wewe, ukaaye pamoja na binti Babeli.” (Zek. 2:6, 7; Yer. 51:45) Kabla ya tarehe hiyo na wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, mabaki hawa walikuwako utumwani katika Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo.

14. (a) Ni nani wale ‘walioandikwa katika kitabu kile’? (b) Je! wengine wanaokoka kuharibiwa, na iwapo ndivyo, wao ni akina nani?

14 Kama ambavyo Danieli aliambiwa, kila mmoja wa mabaki hawa “ameandikwa katika kitabu kile.” Wao ni sehemu ya “kundi la mzaliwa wa kwanza ambao wameandikwa mbinguni.” (Ebr. 12:23, NW; angalia pia Malaki 3:16.) Kuongezea hawa wanaookoka kuharibiwa kwa waovu, kuna “mkutano mkubwa” si Waisraeli wa kiroho, walakini ambao ni “wageni” kwa kulinganisha. Walakini hawa, pia, ‘wanapenda jina la Yehova’ nao wamekuwa watumishi wake washikamanifu. Wakiwa na mataraja gani? Yehova anajibu, akisema hivi: “Nitawaleta hao nao hata mlima wangu mtakatifu, na kuwafurahisha katika nyumba yangu ya sala.” Hawa wa “mkutano mkubwa” wanamtolea Mungu utumishi mtakatifu katika hekalu lake. Wanaokoka “dhiki kubwa” nao wanaongozwa kwenye “chemchemi za maji yenye uhai.”​—Isa. 56:6, 7; Ufu. 7:9-17.

15. Ni onyo gani la mwisho linalotolewa juu ya kukimbia kutoka Babeli Mkuu?

15 Kuthibitisha unabii huo, twaendelea kusoma zaidi katika kitabu cha mwisho cha kiunabii cha Biblia, kinachohusu watu wa Mungu leo. Kinatoa onyo la mwisho kuhusiana na Babeli Mkuu, ile milki ya dini ya uongo, kwa maneno haya: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake. Kwa maana dhambi zake zimefika hata mbinguni, na Mungu amekumbuka maovu yake. . . . mapigo yake yatakuja katika siku moja . . . naye atateketezwa kabisa kwa moto. Kwa maana [Yehova] Mungu aliyemhukumu ni mwenye nguvu.”​—Ufu. 18:4-8.

16. (a) Sababu gani inaweza kusemwa kwamba kungali wakati wa kuokoka uharibifu wa Babeli Mkuu? (b) Unaweza ukaonwaje kuwa kati ya wale ambao Mungu anaita “watu wangu”?

16 Kungali wakati wa kuokoka! Onyo la kukimbia linatolewa kwa nguvu na waziwazi. Ni ujumbe wa haraka unaotangazwa na Mashahidi wa Yehova. Wakati huu si nyumba tu inayoteketea. Mahali pake, “mji” mzima utateketezwa kwa moto. Mara tu moto huo utakapowashwa, itakuwa kuchelewa sana kuweza kukimbia. Wale walio Wababeli katika moyo hawaitikii nao hawataitikia onyo hilo. Lakini kungali nafasi kwa wengine kuonyesha kwamba moyoni wanataka kumtumikia Yehova Mungu wakiwa washikamanifu kwa ufalme wake chini ya Kristo Yesu. Kwa hiyo wangali na wakati wa kuonyesha kwamba kwa kufaa wanaweza kuhesabiwa kati ya wale ambao Mungu anaita “watu wangu.” Hawa wanaalikwa wawe “kondoo wengine,” wanaofanyiza sehemu fulani ya washiriki wa “kundi moja na [chini ya] mchungaji mmoja.” (Yohana 10:16) Kwa furaha, kwa utumishi wako wa kutoka moyoni unaomtolea Yehova na ushikamanifu kwa ufalme wake wewe, pia, waweza kutambuliwa kati ya watu wa Mungu.

UKIMBILIE MJI WA MUNGU—SAYUNI

17. Yehova ametoa mpango gani kwa wale wanaookoka?

17 Kama ilivyotangulia kutajwa, si jambo tu la kuokoka kutoka mahali au hali fulani palipo na hatari kubwa. Vilevile kuna shauri la kupata na kusaidiwa kwenda kwenye mahali salama. Je! “Mtoaji wa wokovu” mkuu ametayarisha jambo hilo? Yeye ameonya watu wake wakikimbie kutoka “mji” huo unaokaribia kuharibiwa kwa moto, awaache tu wakitanga-tanga jangwani? Angalia jibu linalotolewa katika Neno lake: “Itakuwa ya kwamba mtu awaye yote atakayeliitia jina la [Yehova] ataponywa; kwa kuwa katika mlima Sayuni na katika Yerusalemu watakuwako watu watakaookoka, kama [Yehova] alivyosema; na katika mabaki hao awaitao [Yehova].”​—Yoeli 2:32.

18. Mji mkuu wa kale wa Israeli una mfano wa kisasa

18 Kwa hiyo Biblia inaeleza juu ya Miji miwili—ule wa kuukimbia na ule ambao tunaweza kuukimbilia tukiwa pamoja na wengine wengi. Mji mkuu wa kale Israeli, mara nyingi unaotajwa kama Sayuni, au Yerusalemu, unafananisha “Yerusalemu wa mbinguni,” ufalme wa Mungu wa kimbinguni, unaowakilishwa duniani na mabaki ya jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ambayo Yesu alizungumza juu yake katika Mathayo 24:45-47. (Ebr. 12:22) Yehova aliongoza kwa roho wengi wa watumishi wake waaminifu wa kale watoe vitia-moyo na uongozi kwa wote wanaoukimbilia ufalme wake.

19, 20. Ni uongozi na kitia-moyo gani kilichotolewa kupitia kwa Isaya (a) katika Isaya 2:2-4, na (b) katika Isaya 26:1-4?

19 Isaya alikuwa mmojawapo wa watumishi hao waaminifu, naye alitabiri juu ya wakati wenye furaha kweli kweli, kwa maneno haya: “Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova] . . . naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake; maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la [ Yehova] katika Yerusalemu.” Chini ya sheria na neno hilo watajifunza namna ya kuishi katika amani ‘wasijifunze vita tena.’​—Isa. 2:2-4; angalia pia Sefania 2:3.

20 Baadaye katika unabii wake, Isaya aliongozwa kwa roho atoe maelezo marefu juu ya namna jambo hilo lingetimizwa, akisema hivi: “Siku ile wimbo huu utaimbwa katika nchi ya Yuda; Sisi tunao mji ulio na nguvu; ataamuru wokovu kuwa kuta na maboma. Wekeni wazi malango yake, taifa lenye haki, lishikalo kweli, liingie. Utamlinda yeye ambaye moyo wake umekutegemea katika amani kamilifu, kwa kuwa anakutumaini. Mtumaini [Yehova] sikuzote, [Yah] Yehova ni mwamba wa milele.”​—Isa. 26:1-4.

21. Paradiso ya kiroho inaelezwaje katika njia yenye kupendeza katika Isaya 61:4-11?

21 Mwishoni mwa unabii wake, na akipanua njozi yake iingize nchi yote ya Sayuni, Isaya alisimulia kwa njia nzuri sana paradiso ya kiroho iliyorudishwa ambapo wote waliookolewa wangepata utendaji wenye kupendeza katika ‘kutengeneza upya sehemu zilizokuwa ukiwa kwa muda mrefu.’ Si kwamba tu Waisraeli wa kiroho wangeongozwa katika jambo hilo, bali inasemekana kwamba “wageni watasimama na kulisha makundi yenu, na watu wa kabila nyingine watakuwa wakulima wenu, na watunzaji wa mizabibu yenu.” Unabii huo unazungumza kwa sauti kubwa, si juu ya ‘kuponea chupuchupu’ bali kuokoka na kukombolewa kabisa. Kwa hiyo, sisi sote twaweza kujiunga kwa furaha pamoja na mabaki waaminifu waliotiwa mafuta wa “mtumwa” wa Yehova katika maneno haya ya kusifu: “Nitafurahi sana katika [Yehova], nafsi yangu itashangilia katika Mungu wangu.”​—Isa. 61:4-11.

22. (a) Kwa habari ya mtu binafsi, ni mpango gani umetolewa ili kuokoka? (b) Ili kupata faida yake, lazima tufanye sehemu gani?

22 Ingawa huenda ukakubali kwamba yote ambayo tumechunguza kufikia hapa ni ya kweli kwa habari ya watu wa Mungu kwa ujumla, huenda ukawa unauliza namna yanavyokuhusu wewe binafsi. Je! Unahitaji kuokoka kutokana na tatizo moja au zaidi la kibinafsi? Ni nani asiyetaka? Mithali ya kale ni ya kweli kwamba, kwa kusema kwa njia ya kibinadamu, maisha ni safari fupi ya kuzaliwa na kufa. Je! Hakuna kuokoka utumwa wa dhambi na kifo? Kwa kupendeza, dhambi na kifo vinatajwa kuwa wafalme, na vyote vitafutuliwa mbali. (Rum. 5:14; 6:12) Akiwaandikia Wakristo wenzake, mtume Paulo anaeleza namna njia ya kuokokea imefunguliwa, yaani, “kwa njia ya ukombozi ulio katika Kristo Yesu.” Maana ‘Mungu alimweka awe upatanisho kwa njia ya imani katika damu yake.’ (Rum. 3:24, 25) Ndiyo, kwa kuamini dhabihu hiyo yenye kuleta upatanisho, twaweza kuja kwenye kibali ya Mungu. Mradi, tungali wasiokamilika na tungali tunahitaji kila siku kuomba msamaha kwa ajili ya dhambi zetu. Walakini maelekeo yetu ya dhambi si lazima na hayapaswi kutawala maishani mwetu. Paulo aliandika hivi: “Basi, dhambi isitawale ndani ya miili yenu ipatikanayo na mauti. . . . maana dhambi haitawatawala ninyi.” Ili kutusaidia kuhusiana na jambo hilo, Mungu ametoa msaada kupitia kwa Neno lake na watumishi wake waaminifu, pamoja na roho yake takatifu.​—Rum. 6:12-14; 8:11; Yak. 5:14, 15.

23. Ni taraja gani bora lililoko mbele yetu, na chini ya ufalme wa nani?

23 Vilevile, baada ya hizi “nyakati za hatari” na baada ya “taratibu ya mambo” ya Shetani kukomeshwa kabisa, litakuwa taraja lenye utukufu kama nini litakalofunguka mbele yetu! (2 Tim. 3:1; 2 Kor. 4:4) Dhambi na mauti havitatawala tena kama wafalme. Mahali pake, wokovu kwenye uhuru kamili na wa kudumu utakuwa umekamilika. Baada ya warithi washirika wa Kristo kuingia kwenye zawadi yao ya kimbinguni, ndipo “viumbe vyenyewe navyo [wanadamu] vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa na uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.” Kristo Yesu “sharti amiliki yeye, hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti.” Ni furaha kama nini iliyoko mbele ya waokokaji wote washikamanifu—kwa wale wanaoukimbilia ufalme wa Mungu! Sifa na shukrani zote zimwendee Yehova, “Mtoaji wa wokovu” mkuu!—Rum. 8:19-21; 1 Kor. 15:25, 26.

​—Kutoka The Watchtower Dec. 1,1980.

namna gani?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki