Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 7/15 kur. 9-14
  • Jihadhari na Ukosefu wa Imani

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jihadhari na Ukosefu wa Imani
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mbona Shauri Kali Hivyo?
  • Mtu Mkuu Kuliko Musa
  • “Msifanye Mioyo Yenu Kuwa Migumu”
  • Somo Kwetu
  • Usife Moyo Katika Shindano la Mbio la Kupata Uhai!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Kitabu cha Biblia Namba 58—Waebrania
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Wakati Msiba wa Ulimwengu Ukaribiapo—‘Mfikirie Yesu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Lishike Sana Tumaini Lililo Mbele Yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 7/15 kur. 9-14

Jihadhari na Ukosefu wa Imani

“Jihadharini, akina ndugu, kwa kuhofu kusije kamwe kukasitawi katika yeyote kati yenu moyo mwovu unaokosa imani kwa kujiondoa kwa Mungu aliye hai.”—WAEBRANIA 3:12.

1. Maneno ya Paulo kwa Wakristo Waebrania hukazia fikira zetu uhalisi gani wenye kushtusha?

NI WAZO lenye kuogofya kama nini—kwamba watu ambao wakati mmoja walifurahia uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova wangeweza kusitawisha “moyo mwovu” na “kujiondoa kwa Mungu aliye hai”! Nalo ni onyo lililoje! Maneno hayo ya mtume Paulo yaliandikiwa watu waliokuwa wameweka maisha zao wakfu kwa Yehova kwa msingi wa imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, wala si watu wasioamini.

2. Twahitaji kuchunguza maswali gani?

2 Mtu aliyebarikiwa sana hivyo kiroho angewezaje kukuza “moyo mwovu unaokosa imani”? Kwa kweli, mtu yeyote ambaye alikuwa ameonja upendo na fadhili zisizostahiliwa za Mungu angewezaje kujiondoa kwake kimakusudi? Na je, jambo hilo lingeweza kumpata yeyote kati yetu? Hayo ni mawazo yastahiliyo kufikiriwa, nayo hutufanya tuchunguze sababu ya onyo hilo.—1 Wakorintho 10:11.

Mbona Shauri Kali Hivyo?

3. Fafanua hali zilizoathiri Wakristo wa karne ya kwanza katika Yerusalemu na sehemu zilizolizunguka.

3 Yaonekana Paulo aliwaandikia barua yake Wakristo Waebrania katika Yudea mwaka wa 61 W.K. Mwanahistoria fulani alionelea kwamba huo ulikuwa wakati ambapo “hakukuwa na amani na usalama kwa watu wowote waliokuwa wenye kuchukua mambo kwa uzito, wenye kufuatia haki, ama katika jiji la Yerusalemu au kwingineko kotekote katika mkoa huo.” Ulikuwa wakati wa uasi-sheria na jeuri, uliochochewa na mchanganyiko wa kuwapo kwa jeshi la Roma, ushujaa wa Wazeloti Wayahudi waliowapinga Waroma, na utendaji mbalimbali wa kihalifu wa wezi waliotumia nyakati hizo zenye ghasia kwa faida yao. Hayo yote yalifanya mambo yawe magumu kwa Wakristo waliojaribu sana kutonaswa katika mambo hayo. (1 Timotheo 2:1, 2) Kwa kweli, kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo, walionwa na wengine kuwa wasiofaa katika jamii, hata walionwa kuwa wachochezi. Mara nyingi Wakristo walitendwa vibaya, na afya yao ikaathiriwa.—Waebrania 10:32-34.

4. Wakristo Waebrania walikuwa chini ya mkazo gani wa kidini?

4 Wakristo Waebrania pia walikuwa chini ya mkazo mwingi wa kidini. Bidii ya wanafunzi waaminifu wa Yesu na mpanuko wa haraka uliotokea wa kutaniko la Kikristo ulitokeza wivu na ghadhabu ya Wayahudi—hasa viongozi wao wa kidini. Wangeweza kufanya lolote ili kuwasumbua na kuwanyanyasa wafuasi wa Yesu Kristo.a (Matendo 6:8-14; 21:27-30; 23:12, 13; 24:1-9) Hata ikiwa Wakristo fulani hawakupatwa na mnyanyaso wa moja kwa moja, hata hivyo, walidharauliwa na kudhihakiwa na Wayahudi. Ukristo ulidharauliwa ukionwa kuwa dini iliyoundwa majuzi ambayo haikuwa na fahari ya dini ya Kiyahudi, kwa vile haukuwa na hekalu, ukuhani, misherehekeo, dhabihu rasmi, na kadhalika. Hata kiongozi wao, Yesu, aliuawa kama mhalifu aliyehukumiwa adhabu. Ili kuabudu katika dini yao, Wakristo walilazimika kuwa na imani, ujasiri, na uvumilivu.

5. Kwa nini ilikuwa muhimu Wakristo katika Yudea waendelee kuwa chonjo kiroho?

5 Zaidi ya yote, Wakristo Waebrania katika Yudea walikuwa wakiishi katika wakati wa maana katika historia ya taifa hilo. Mambo mengi ambayo Bwana wao, Yesu Kristo, alisema yangetia alama mwisho wa mfumo wa Kiyahudi, tayari yalikuwa yametukia. Mwisho haungeweza kuwa mbali sana. Ili kuokoka, Wakristo walipaswa kuendelea kuwa chonjo kiroho na kuwa tayari ‘kukimbilia milimani.’ (Mathayo 24:6, 15, 16) Je, wangekuwa na imani na nguvu za kiroho zilizohitajiwa ili kuchukua hatua ya mara moja, kama vile Yesu alivyokuwa ameelekeza? Ilionekana ni kana kwamba kulikuwa na shaka fulani.

6. Wakristo katika Yudea walihitaji nini haraka?

6 Katika mwongo wa mwisho wa kuvunjwa kwa mfumo mzima wa mambo wa Kiyahudi, Wakristo Waebrania kwa wazi walikuwa chini ya mkazo mkali kutoka ndani na nje ya kutaniko. Walihitaji kitia-moyo. Lakini wao pia walihitaji shauri na mwelekezo ili kuwasaidia kuona kwamba walikuwa wamechagua mwendo ufaao na kwamba hawakuwa wameteseka na kuvumilia bure. Kwa kupendeza, Paulo alikabili hali hiyo na kuwasaidia.

7. Kwa nini twapaswa kupendezwa na yale ambayo Paulo aliandikia Wakristo Waebrania?

7 Mambo ambayo Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania yapaswa kutupendeza kwelikweli. Kwa nini? Kwa sababu twaishi katika kipindi kinachofanana na chao. Kila siku twahisi mikazo kutoka katika ulimwengu unaoongozwa na Shetani. (1 Yohana 5:19) Unabii mbalimbali wa Yesu na mitume wake kuhusu siku za mwisho na “umalizio wa mfumo wa mambo,” watimizwa siku zetu. (Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5; 2 Petro 3:3, 4; Ufunuo 6:1-8) Zaidi ya yote, twahitaji kukaa chonjo kiroho ili “[tu]pate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia.”—Luka 21:36.

Mtu Mkuu Kuliko Musa

8. Kwa kusema maneno yaliyorekodiwa kwenye Waebrania 3:1, Paulo alikuwa akiwahimiza Wakristo wenzake wafanye nini?

8 Akitaja hoja muhimu, Paulo aliandika hivi: “Mfikirieni mtume na kuhani wa cheo cha juu ambaye twaungama—Yesu.” (Waebrania 3:1) ‘Kufikiria’ humaanisha “kutambua waziwazi . . . , kuelewa kikamili, kufikiri kwa makini.” (Kichapo Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words) Kwa hiyo, Paulo alikuwa akiwahimiza waamini wenzake wajitahidi sana kuthamini kikweli fungu la Yesu katika imani na wokovu wao. Kufanya hivyo kungetia nguvu azimio lao la kusimama imara katika imani. Basi, Yesu alikuwa na fungu gani, na kwa nini twapaswa ‘kumfikiria’?

9. Kwa nini Paulo alimrejezea Yesu kuwa “mtume” na “kuhani wa cheo cha juu”?

9 Paulo alimrejezea Yesu kwa kutumia maneno “mtume” na “kuhani wa cheo cha juu.” “Mtume” ni mtu atumwaye na hapa neno hilo larejezea njia ya Mungu ya kuwasiliana na wanadamu. “Kuhani wa cheo cha juu” ni mtu ambaye kupitia kwake wanadamu waweza kumfikia Mungu. Maandalizi hayo mawili ni ya muhimu kwa ibada ya kweli, na Yesu huchukua mafungu yote mawili. Yeye ndiye aliyetumwa kutoka mbinguni ili kuwafundisha wanadamu kweli juu ya Mungu. (Yohana 1:18; 3:16; 14:6) Pia Yesu ndiye aliyewekwa kuwa Kuhani wa Cheo cha Juu aliyefananishwa katika mpango wa hekalu la kiroho la Yehova kwa ajili ya msamaha wa dhambi. (Waebrania 4:14, 15; 1 Yohana 2:1, 2) Ikiwa kwa kweli twathamini baraka ambazo twaweza kupata kupitia Yesu, tutakuwa na moyo mkuu na tutaazimia kuendelea kuwa imara katika imani.

10. (a) Paulo aliwasaidiaje Wakristo Waebrania wafahamu kwamba Ukristo ni bora kuliko dini ya Kiyahudi? (b) Paulo alitaja jambo gani lililo kweli ulimwenguni pote ili kutia nguvu hoja yake?

10 Ili kukazia thamani ya imani ya Kikristo, Paulo alimlinganisha Yesu na Musa, ambaye Wayahudi walimwona kuwa nabii mkuu zaidi miongoni mwa wazazi wao wa kale waliokufa. Ikiwa Wakristo Waebrania wangeweza kuelewa kwa moyo wote uhakika wa kwamba Yesu ni mkuu kuliko Musa, hawangekuwa na sababu yoyote ya kushuku uhakika wa kwamba Ukristo ni bora kuliko dini ya Kiyahudi. Paulo alionyesha kwamba ingawa Musa alionwa kuwa mwenye kustahili kukabidhiwa “nyumba” ya Mungu—taifa, au kutaniko la Israeli—yeye alikuwa mhudumu au mtumishi mwaminifu tu. (Hesabu 12:7) Kwa upande mwingine, Yesu alikuwa Mwana, bwana-mkubwa wa nyumba hiyo. (1 Wakorintho 11:3; Waebrania 3:2, 3, 5) Ili kukazia hoja yake, Paulo alitaja jambo hili lililo kweli ulimwenguni pote: “Bila shaka, kila nyumba imejengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyejenga vitu vyote ni Mungu.” (Waebrania 3:4) Hakuna yeyote ambaye angedai kwamba Mungu si mkuu kuliko yeyote, kwa kuwa yeye ndiye Mjenzi, au Muumba wa vyote. Kwa kupatana na akili basi, kwa kuwa Yesu alikuwa mfanyakazi-mwenzi wa Mungu, lazima awe mkuu kuliko viumbe wengine wote, kutia ndani na Musa.—Mithali 8:30; Wakolosai 1:15-17.

11, 12. Paulo aliwahimiza Wakristo Waebrania washikilie nini “imara hadi mwisho,” nasi twaweza kutumiaje shauri lake?

11 Kwa kweli, Wakristo Waebrania walikuwa na wadhifa uliopendelewa sana. Paulo aliwakumbusha kwamba walikuwa “washiriki wa mwito wa kimbingu,” pendeleo lililopasa kuthaminiwa sana kuliko kitu chochote ambacho mfumo wa Kiyahudi ungetoa. (Waebrania 3:1) Lazima maneno ya Paulo yawe yaliwafanya Wakristo hao watiwa-mafuta wawe na shukrani kwa sababu walitarajia kupokea urithi mpya badala ya kuhisi vibaya kwamba walikuwa wameacha vitu vilivyohusiana na utamaduni wa Kiyahudi. (Wafilipi 3:8) Akiwahimiza washikilie pendeleo lao na kutolipuuza, Paulo alisema hivi: “Kristo alikuwa mwaminifu akiwa Mwana juu ya nyumba ya [Mungu]. Sisi ndio nyumba ya Huyo, ikiwa twashikilia kwa imara hadi mwisho.”—Waebrania 3:6.

12 Naam, ikiwa Wakristo Waebrania wangeokoka mwisho uliokuwa ukikaribia wa mfumo wa mambo wa Kiyahudi, walihitaji kushikilia tumaini walilopewa na Mungu “kwa imara hadi mwisho.” Twapaswa kufanya vivyo hivyo ikiwa twataka kuokoka mwisho wa mfumo huu. (Mathayo 24:13) Hatupaswi kuruhusu mahangaiko ya maisha, ubaridi wa watu, au mielekeo ya kutokamilika kwetu wenyewe kutufanye tusitesite katika imani yetu katika ahadi za Mungu. (Luka 21:16-19) Ili kuona jinsi tuwezavyo kujiimarisha, acheni tukaze fikira juu ya maneno zaidi ya Paulo.

“Msifanye Mioyo Yenu Kuwa Migumu”

13. Paulo alitoa onyo gani, naye alitumiaje Zaburi 95?

13 Baada ya kuchunguza wadhifa wenye upendeleo wa Wakristo Waebrania, Paulo alitoa onyo hili: “Kama vile roho takatifu husema: ‘Leo ikiwa nyinyi watu mtaisikiliza sauti yake mwenyewe, msifanye mioyo yenu kuwa migumu kama katika pindi ya kusababisha hasira yenye uchungu, kama katika siku ya kufanya jaribu nyikani.’” (Waebrania 3:7, 8) Paulo alikuwa akinukuu Zaburi ya 95, na kwa hiyo angeweza kusema “roho takatifu husema.”b (Zaburi 95:7, 8; Kutoka 17:1-7) Maandiko yamepuliziwa na Mungu kupitia kwa roho takatifu yake.—2 Timotheo 3:16.

14. Waisraeli waliitikiaje mambo ambayo Yehova alikuwa amewafanyia, na kwa nini?

14 Baada ya kuwekwa huru kutoka katika utumwa katika Misri, Waisraeli walipewa heshima kubwa ya kuingia katika uhusiano wa kiagano pamoja na Yehova. (Kutoka 19:4, 5; 24:7, 8) Hata hivyo, badala ya kuonyesha uthamini kwa ajili ya mambo ambayo Mungu alikuwa amewafanyia, waliasi punde. (Hesabu 13:25–14:10) Hilo lingeweza kutukiaje? Paulo alitaja sababu: kuifanya mioyo yao kuwa migumu. Lakini mioyo inayoitikia Neno la Mungu yaweza kuwaje migumu? Nasi twapaswa kufanya nini kuepuka hilo?

15. (a) ‘Sauti ya Mungu mwenyewe’ imesikiwaje wakati uliopita na sasa? (b) Twahitaji kujiuliza maswali gani juu ya ‘sauti ya Mungu’?

15 Paulo alianza onyo lake kwa maneno haya “ikiwa nyinyi watu mtaisikiliza sauti yake mwenyewe.” Mungu alisema na watu wake kupitia Musa na manabii wengine. Kisha, Yehova alisema nao kupitia Mwana wake, Yesu Kristo. (Waebrania 1:1, 2) Leo, tuna Neno la Mungu lililopuliziwa likiwa zima, Biblia Takatifu. Pia tuna “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aliyewekwa rasmi na Yesu kuandaa ‘chakula cha kiroho kwa wakati ufaao.’ (Mathayo 24:45-47) Hivyo, Mungu angali anasema. Lakini je, tunasikiliza? Kwa kielelezo, sisi huitikiaje shauri juu ya mavazi na mapambo au uchaguzi wetu wa vitumbuizo na muziki? Je, sisi “husikiliza,” yaani, kukazia uangalifu na kutii tunayosikia? Ikiwa tuna tabia ya kutoa udhuru au kupinga shauri, tunajitia wenyewe katika hatari isiyo rahisi kutambulika ya kuifanya mioyo yetu iwe migumu.

16. Mojawapo ya njia ambazo mioyo yetu yaweza kufanywa migumu ni ipi?

16 Mioyo yetu yaweza pia kuwa migumu tukitoa udhuru wa kutofanya tunayopaswa kufanya. (Yakobo 4:17) Licha ya mambo yote ambayo Yehova alifanyia Waisraeli, walishindwa kudhihirisha imani, walimwasi Musa, wakachagua kuamini ripoti mbaya juu ya Kanaani, na kukataa kuingia Bara Lililoahidiwa. (Hesabu 14:1-4) Kwa hiyo, Yehova aliagiza kwamba wangekaa nyikani miaka 40—muda wa kutosha kwa washiriki wasio na imani wa kizazi hicho kufa. Akiwa amechukizwa nao, Mungu alisema hivi: “‘Wao sikuzote hupotea njia katika mioyo yao, nao wenyewe hawajaja kujua njia zangu.’ Kwa hiyo niliapa katika hasira yangu, ‘Hakika wao hawataingia katika pumziko langu.’” (Waebrania 3:9-11) Je, hilo linatufunza jambo lolote?

Somo Kwetu

17. Ingawaje Waisraeli waliona matendo yenye nguvu ya Yehova na kusikia hukumu zake, kwa nini walikosa imani?

17 Kizazi cha Waisraeli waliotoka Misri waliona kwa macho yao wenyewe na kusikia kwa masikio yao wenyewe matendo yenye nguvu na hukumu za Yehova. Na bado, hawakuamini kwamba Mungu angeweza kuwaongoza kwa usalama hadi Bara Lililoahidiwa. Kwa nini? “Nao wenyewe hawajaja kujua njia zangu,” asema Yehova. Walijua mambo ambayo Yehova alikuwa amesema na kufanya, lakini hawakuwa wamesitawisha uhakika na itibari katika uwezo wake wa kuwatunza. Pia walihitaji na kutaka mambo mengi sana ya kibinafsi hivi kwamba hawakufikiri sana njia za Mungu na kusudi lake. Naam, walikosa imani katika ahadi yake.

18. Kulingana na Paulo, ni mwendo gani ambao utaongoza kwenye “moyo mwovu unaokosa imani”?

18 Maneno haya zaidi kwa Waebrania yanatumika kwetu kwa kiwango kilekile: “Jihadharini, akina ndugu, kwa kuhofu kusije kamwe kukasitawi katika yeyote kati yenu moyo mwovu unaokosa imani kwa kujiondoa kwa Mungu aliye hai.” (Waebrania 3:12) Paulo alifikia kiini cha mambo kwa kutaja kwamba “moyo mwovu unaokosa imani” hutokezwa na “kujiondoa kwa Mungu aliye hai.” Mapema katika barua hiyo, alisema juu ya “kupeperushwa mbali” kwa sababu ya kutokaza uangalifu. (Waebrania 2:1) Hata hivyo, neno la Kigiriki litafsiriwalo “kupeperushwa mbali” humaanisha “kusimama kando” nalo lahusiana na neno “uasi-imani.” Hutoa wazo la kukinza kimakusudi, kujiondoa, kusaliti, kukiwa na kiasi fulani cha madharau.

19. Kukosa kusikiliza shauri kwaweza kuongoza kwenye matokeo gani mazito? Toa kielezi.

19 Kwa hiyo, somo ni kwamba tukisitawisha tabia ya kukosa ‘kuisikiliza sauti yake mwenyewe,’ tukipuuza shauri kutoka kwa Yehova kupitia Neno lake na jamii yake ya mtumwa mwaminifu, punde si punde mioyo yetu itakuwa sugu, migumu. Kwa kielelezo, huenda watu wawili ambao hawajaoana wakawa na uhusiano wa karibu zaidi kupita kiasi. Itakuwaje wakipuuza tu jambo hilo? Je, kufanya hivyo kungewazuia wasirudie kufanya walilofanya, au kungefanya iwe rahisi kwao kufanya hivyo tena? Vivyo hivyo, jamii ya mtumwa itoapo shauri juu ya uhitaji wa kuwa wateuzi katika uchaguzi wetu wa muziki na vitumbuizo, na kadhalika, je, sisi hulikubali kwa shukrani na kufanya marekebisho yahitajiwayo? Paulo alituhimiza ‘tusiachilie mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe.’ (Waebrania 10:24, 25) Lijapokuwa shauri hilo, watu fulani huwa na mtazamo wenye ubaridi kuelekea mikutano ya Kikristo. Huenda wakahisi kwamba kukosa baadhi ya mikutano hiyo au kuepuka mikutano fulani kabisa, hakuna madhara yoyote.

20. Kwa nini ni muhimu kuitikia shauri la Kimaandiko katika njia inayofaa?

20 Tusipoitikia ifaavyo “sauti” ya Yehova, itolewayo waziwazi katika Maandiko na vichapo vinavyotegemea Biblia, karibuni tutajikuta wenyewe “[tuki]jiondoa kwa Mungu aliye hai.” Kupuuza shauri kichinichini kwaweza kwa urahisi kuwa kudunisha, kuchambua, na kukinza shauri moja kwa moja. Kusiporekebishwa, tokeo ni “moyo mwovu unaokosa imani,” na kwa kawaida ni vigumu sana kuacha mwendo huo. (Linganisha Waefeso 4:19.) Yeremia aliandika hivi kwa kufaa: “Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha; nani awezaye kuujua?” (Yeremia 17:9) Kwa sababu hiyo, Paulo aliwahimiza waamini wenzake Waebrania hivi: “Fulizeni kuhimizana kwa bidii mtu na mwenzake kila siku, maadamu yaweza kuitwa ‘Leo,’ kwa kuhofu yeyote kati yenu asije akafanywa kuwa mgumu kwa nguvu ya udanganyifu ya dhambi.”—Waebrania 3:13.

21. Sisi sote twahimizwa kufanya nini, nasi tuna matumaini gani?

21 Tuna furaha kama nini kwamba Yehova angali anasema nasi leo, kupitia Neno lake na tengenezo lake! Twashukuru kwamba “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” huendelea kutusaidia “[kuu]shikilia sana uhakika tuliokuwa nao mwanzoni kwa imara hadi mwisho.” (Waebrania 3:14) Sasa ndio wakati wetu wa kuitikia upendo na mwelekezo wa Mungu. Tufanyapo hivyo, twaweza kufurahia mojawapo ya ahadi nyingine za Yehova zilizo nzuri ajabu—ahadi ya ‘kuingia’ katika pumziko lake. (Waebrania 4:3, 10) Hilo ndilo jambo ambalo Paulo afuatia kuzungumzia na Wakristo Waebrania, nalo pia ndilo tutakalochunguza katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

a Yosefo aliripoti kwamba punde baada ya Festo kufa, Ananus (Anania) wa farakano la Masadukayo alipata kuwa kuhani wa cheo cha juu. Alimleta Yakobo ndugu nusu ya Yesu, na wanafunzi wengine mbele ya Sanhedrini na kuwafanya wahukumiwe kifo na kupigwa mawe.

b Yaonekana Paulo alinukuu Septuagint ya Kigiriki, ambayo hutafsiri maneno ya Kiebrania “Meriba” na “Masa” kuwa “kugombana” na “kujaribu.” Ona ukurasa wa 350 na wa 379 katika Buku la 2 la Insight on the Scriptures, yaliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

Je, Waweza Kueleza?

◻ Kwa nini Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania shauri kali hivyo?

◻ Paulo aliwasaidiaje Wakristo Waebrania kufahamu kwamba walikuwa na kitu fulani bora zaidi kuliko maisha katika dini ya Kiyahudi?

◻ Moyo wa mtu hufanywaje kuwa mgumu?

◻ Twapaswa kufanya nini ili kuepuka kusitawisha “moyo mwovu unaokosa imani”?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Je, wewe unadhihirisha imani katika Yesu, Musa Mkuu Zaidi?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki