Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 7/15 kur. 15-21
  • Lishike Sana Tumaini Lililo Mbele Yako

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Lishike Sana Tumaini Lililo Mbele Yako
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Si Aina ya Warudio Nyuma Kwenye Uharibifu”
  • Na ‘Tusipeperuke’
  • ‘Usianguke’
  • Kudhihirisha Imani “Leo”
  • Usife Moyo Katika Shindano la Mbio la Kupata Uhai!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Toeni Dhabihu Ambazo Zampendeza Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Jihadhari na Ukosefu wa Imani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Wakati Msiba wa Ulimwengu Ukaribiapo—‘Mfikirie Yesu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 7/15 kur. 15-21

Lishike Sana Tumaini Lililo Mbele Yako

1, 2. Kwa sababu gani inakupasa ufikirie kwa uzito shauri la kulishika sana tumaini lako?

MTUME Paulo aliandika kwamba “sisi kwa kweli tunakuwa washiriki wa Kristo ikiwa tu tunalishika sana tumaini hakika tulilokuwa nalo huko mwanzo liwe imara mpaka mwisho.” (Waebrania 3:14, NW) Pia alinena juu ya uhitaji wetu wa “kulishika sana tumaini lililowekwa mbele yetu.”​—Waebrania 6:18, NW.

2 Labda wewe umekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova hivi juzi na una juhudi ya kuamini sana mambo uliyosadikishwa. Au labda wewe umekuwa shahidi Mkristo kwa miongo mingi ya miaka na unajisikia uko imara katika njia ya ile kweli. Vyo vyote iwavyo, inaelekea kwamba kila mmoja wetu anaweza kukumbuka watu fulani tunaowajua ambao wamekoma kutembea katika njia ya ile kweli, sawa na ilivyotukia katika karne ya kwanza. (Wafilipi 3:18; Matendo 20:30) Huenda ikawa wengine walipoteza imani yao pole kwa pole, wakawa wenye shughuli nyingi mno za kutafuta faida za kimwili au wakajiachilia washindwe na kishawishi na kutenda dhambi.

3-5. Kitabu cha Waebrania kinaweza kutusaidiaje katika tumaini letu?

3 Tunaweza kuzuiaje jambo hilo lisitupate sisi? Acheni tufikirie mashauri yaliyo katika kitabu cha Waebrania. Tutaona namna yalivyo ya maana kwa wakati wetu, kwa kuona uvumilivu wa uaminifu wa mashahidi wengi wa kisasa wa Yehova ambao wametiwa nguvu na mashauri hayo.

4 Kitabu cha Waebrania kiliandikwa kwa “wenye kuushiriki mwito wa mbinguni.” Wao walitiwa mafuta kwa roho ya Mungu na walikuwa na tumaini imara la kumfuata Kristo aliyekuwa mtangulizi wa kuingia mbinguni. Kama unavyoweza kuwazia, ‘tumaini hili lilikuwa nanga kwa nafsi, iliyo hakika na imara pia.’ Hata hivyo, Paulo alivuta fikira kwenye uhitaji wa “kulishika sana tumaini lililowekwa mbele yetu.” (Waebrania 3:1; 6:18-20) Ikiwa wao walikuwa na uhitaji huo, ni zaidi sana sasa kwa wale mabaki watiwa mafuta na “mkutano mkubwa” wanaotazamia kuiokoka ‘dhiki kubwa’ inayokuja.​—Ufunuo 7:9, 15.

5 Katika Waebrania Yehova anatuamsha tuone hatari kama zile za ‘kupeperuka,’ ‘kuanguka,’ ‘kuwa wavivu,’ ‘kurudi nyuma kwenye uharibifu’ au ‘kukataa wajibu kwa kutoa udhuru.’ (Waebrania 2:1, NW; 6:6, 12; 10:39, NW; 12:25, NW) Kitabu hicho kinatoa mashauri mazuri kutusaidia ‘tuonyeshe “hali ya kufanya kazi kwa bidii ili tuwe na uhakikisho kamili wa lile tumaini mpaka kwenye mwisho” na kuwa ‘aina ya wale walio na imani mpaka kwenye kuhifadhi nafsi hai.’​—Waebrania 6:11; 10:39 NW.

“Si Aina ya Warudio Nyuma Kwenye Uharibifu”

6. Wakristo Waebrania walikuwa wamekwisha kupatwa na nini, hata hivyo walikuwa na uhitaji gani?

6 Inaonekana kuwa wengi wa Wakristo Waebrania walikuwa wamepatwa na mateso. ‘Walivumilia shindano kubwa chini ya hali za kutaabika,’ kama vile kuwekwa kwenye uwanja wa Kiroma wa maonyesho ya kikatili au wakajihatirisha kwa kwenda kusaidia waliokuwa gerezani. (Waebrania 10:32-34) Hata hivyo, walilazimika kutia bidii wasiwe “aina ya warudio nyuma kwenye uharibifu, bali [wawe] aina ya walio na imani kuhifadhi hai nafsi.”​—Waebrania 10:39, NW.

7. (a) Taraja la kupatwa na mateso linaweza kuwa na matokeo gani juu ya Mkristo? (b) Inakupasa ujiulize nini?

7 Kwa hiyo kuna hatari ya kwamba huenda Mkristo akakuza woga wa kupingwa, na hiyo inaweza kumfanya ‘arudi nyuma’ au akubaliane na wapinzani wake. Namna gani sisi? Labda tumepatwa na kiasi kidogo cha upinzani, kama vile kutoka kwa wanashule na wafanya kazi wenzetu. Hata kutendwa vibaya mwilini, kwa mfano na mwenzi au mzazi asiyeamini, ni jambo ambalo limepata wengine. Hata hivyo katika nchi nyingi si jambo la kawaida sana kwa Shahidi kuteswa vikali kwa sababu ya imani yake. Jambo hilo linaweza kumfanya akose kujitayarisha sana kwa ajili ya mateso makali kisha aelekee zaidi kuwa mtu wa ‘kurudi nyuma’ mateso yakija. Na tujiulize hivi, ‘Baada ya mimi kuwa nimeishi maisha ya starehe, je! naweza kushawishika nirudi nyuma nikitishwa kweli kweli, kwa mfano kuambiwa nitanyang’anywa nyumba yangu, nipoteze kazi ya kuajiriwa au ninyimwe ruhusa ya kuonana na jamaa yangu, au nifungwe gerezani na kutendwa vibaya mwilini?’

8. Kitabu cha Waebrania kinatutolea mauidha gani juu ya kupambana na mateso?

8 Paulo alipokuwa akitoa maelezo juu ya kuonyesha imani chini ya hali za shida, yeye alituhimiza tufikirie namna Yesu alivyovumilia. (Waebrania 12:2, 3) Halafu Paulo akatukumbusha kwamba mateso makali yakija, inatupasa tuyaone kuwa namna ya nidhamu yenye kutufaidisha. Bila shaka, siye Mungu anayeyasababisha mateso; yeye anayaruhusu tu. Hata hivyo, mateso yanaweza kutuzoeza au kutusaidia tufanye maendeleo katika sifa za Kikristo zinazohitajiwa, kama vile uvumilivu, subira, ushikamanifu na kumtumaini Yehova.​—Waebrania 12:4-11; Yakobo 1:2-4.

9. (a) Tunajuaje kwamba wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kuvumilia mateso? (b) Ni jambo gani lililopata dada wengine katika nchi ya kikomunisti miaka ya 1960?

9 Ili tusije kuwa na maoni ya kwamba ni mwanadamu mkamilifu tu anayeweza kuvumilia, kama alivyofanya Yesu, kitabu cha Waebrania kinakazia habari za wanaume na wanawake waliokuwa wamekosa ukamilifu kama sisi na wakavumilia kwa kuwa na imani. (Waebrania 11:35-40; 12:1) ‘Wingu la mashahidi’ ambao wamevumilia kwa imani limeongezewa ukubwa nyakati za kisasa. Katika mwezi Agosti wa mwaka 1982 jarida la Kiswisi lilichapa makala yenye kuhusu mambo ambayo mwanamke mmoja aliona akiwa gerezani pamoja na Mashahidi wa Yehova kwenye kambi ya kazi ya wanawake katika nchi ya kikomunisti miongo kadha ya miaka kabla ya hapo. Haya ni mawazo makuu kati ya maelezo aliyotoa:

Ni makanisa yale makubwa-makubwa tu yaliyo na uhuru kidogo kwa sababu yanahubiri mambo yanayoruhusiwa na Serikali. Sivyo ilivyo kwa zile dini ndogo-ndogo zinazokutana katika nyumba za watu. Wenye kuteswa zaidi sana ni Mashahidi wa Yehova. Mashahidi wengi ambao katika nyumba zao Mnara wa Mlinzi ulipatikana wamehukumiwa kifungo cha miaka 10. Basi, inaweza kufahamiwa sababu iliyofanya wakuu wa kambi waudhike wakati Mashahidi walipozidi kwa njia fulani kupokea vitabu kwa wingi. Kila mfungwa alikuwa amekwisha kuvuliwa mavazi yote akawa uchi na kupekuliwa-pekuliwa, na mavazi yao yalipekuliwa tangu wapi mpaka wapi, hata kwenye nyuzi za mavazi yenyewe. Pia, mfungwa ye yote mwenye kufanya kazi mashambani alichunguliwa na walinzi wenye silaha na kupekuliwa aliporudi kupitia kwenye lango. Lakini wapi, vitabu vikawa vikiingia. Ilikuwa ni kama kwamba wakati wa usiku malaika waliruka juu na kuviangusha ndani. Wengi wa Mashahidi hao walikuwa vijana wanawake. Kifungo cha kwanza kilikuwa cha kuanzia miaka 5 mpaka 7, na cha pili cha muda usiopungua miaka 10. Mashahidi ndio waliotifua kivumbi kweli kweli kambini. Wakati zaidi ya watatu kati yao walipokutana, waliamriwa watawanyike.

10. Kitabu cha Waebrania kinatusaidia tupige moyo konde (tujikaze) namna gani kwa habari ya mateso?

10 Kwa habari ya mifano ya kale ya watu walioonyesha imani chini ya mateso, kitabu cha Waebrania kinasema kwamba “ulimwengu haukustahili kuwa nao,” lakini kwamba Yehova atahakikisha ‘wamekamilishwa’ katika ile Paradiso ya kidunia. Kweli kuna kitu kingine ambacho mtu anaweza kuomba ambacho kinaizidi Paradiso hiyo kwa uzuri? Kwa hiyo acheni tuithamini mifano ya watu wenye imani, wa kale na wa kisasa pia. Badala ya ‘kurudi nyuma kwenye uharibifu,’ ni lazima tupige moyo konde ‘tuwe na imani ya kuhifadhi hai nafsi.’​—Waebrania 11:38, 40; 10:39, NW.

Na ‘Tusipeperuke’

11. ‘Kupeperuka’ kunawezaje kuwa hatari kwa mtu ambaye amekuwa Mkristo kwa muda mrefu kidogo?

11 Kama kitabu cha Waebrania kinavyoonyesha, hatari nyingine ni ‘kupeperuka.’ (Waebrania 2:1, NW) Fikiria namna jambo hilo linavyoweza kutukia. Mtu fulani​—na huenda akawa ni ye yote kati yetu​—anaweza kuwa alipata kuwa Mkristo na akajawa na shauku kwa kuvutiwa sana. Kwa utayari alishiriki katika huduma ya shambani hata alipokuwa na maarifa machache tu ya Biblia. (Matendo 3:1-9; 8:39; 13:48, 49) Baada ya miaka kadha kupita shauku yake ingalipasa kuwa imekomaa na kuwa juhudi yenye kuwaka moto kisha ajitolee huduma kweli kweli. Je! ndivyo amekuwa? Je! anaiona huduma ya Kikristo kuwa njia ya kuonyesha upendo wake kwa Mungu na kusaidia wengine, kama vile yeye mwenyewe alivyosaidiwa? Au imekuwa ni kawaida inayofanywa kwa sababu ni wajibu, kikazi kisichoepukika? Kama yeye ana watoto, je! yeye anawahimiza kwa ukawaida na kwa shauku wawe wahudumu wa wakati wote? Au anawatajia jambo hilo kijuu-juu tu bila kuwasadikisha sana kama vile anavyofanya anapowatajia wawe na masomo ya juu, wawe na kazi yenye mshahara mnono au wajitafutie nyumba yenye upendezi?​—Ufunuo 2:4.

12. (a) Kitabu cha Waebrania kinatutolea pendekezo gani ili tuepuke ‘kupeperuka’? (b) Ingefaa tufikirie maulizo gani juu ya kulitii lile Neno?

12 Hatua moja ya kuepuka ‘kupeperuka’ ni ‘kuyaangalia kwetu zaidi kuliko kawaida mambo yaliyosikiwa.’ (Waebrania 2:1, NW) Wengine wa Wakristo Waebrania walishindwa kufanya hivyo. Baada ya kujifunza “fundisho la msingi juu ya Kristo,” wao ‘hawakusonga mbele kufikia ukomavu.’ Wakati ambao ‘wangalipaswa kuwa wamekwisha kuwa walimu,’ wao walikuwa bado kwenye mambo ya msingi. (Waebrania 5:12–6:2, NW) Namna gani sisi? Je! tunaambaa-ambaa kando-kando tu au tunafanya maendeleo kwa kujali funzo la kibinafsi? Je! tunajaribu kusoma kisehemu cha Biblia kila siku? Je! tunajifunza vitabu vya Kikristo kwa kupendezwa kikweli, hata kuzungumza pamoja na wengine mambo mapya tunayojifunza? Je! sisi tunasaidia watoto wetu wafanye maendeleo makubwa kuliko unywaji wa ‘maziwa ya lile Neno’? Je! wao wanaweza kueleza kwa kutumia Biblia ile kweli inayohusu nafsi, ufufuo, Utatu, dunia-Paradiso, na kadhalika? Je! wanafanya hivyo katika utumishi wa shambani, bila kukwama pale pale walipokuwa mwaka jana?​—1 Petro 3:15.

13. Dada zetu waliofungwa gerezani waliweka kiolezo gani juu ya kujifunza, na hiyo inatudokezea nini?

13 Kwa habari ya Mashahidi waliofungwa gerezani, makala ile ilisimulia hivi:

Katika wakati mchache waliokuwa nao kufanya mambo yao wenyewe walikuwa wakijitahidi kushika kwa moyo vifungu vya Biblia. Pia, walijitahidi kujifunza lugha za kigeni, hasa Kiingereza, Kifaransa na Kijeremani. Vitabu walivyopata vilikuwa vya lugha hizo nyakati nyingine, na wale waliojifunza lugha hizo wangeweza kwa njia hiyo kutafsiria dada wenzao habari zilizokuwamo.

Ingawa ni wachache kati yetu wanaolazimishwa kama hao kufanya kazi saa nyingi wakiwa na chakula kidogo kilichopimwa, je! tunafanya bidii kutumia wakati wa mambo yetu wenyewe ili ‘kuyaangalia zaidi kuliko kawaida mambo yaliyosikiwa’?

‘Usianguke’

14. Ni nini kinachoweza kupata hata watu ambao wamekuwa Wakristo kwa muda mrefu?

14 Baada ya kutuhimiza tuzidi kufanya maendeleo, kitabu cha Waebrania kinaonya kwamba wale “waliokwisha kupewa nuru mara moja kwa wakati wote” wanaweza ‘kuanguka,’ labda wafikie kiasi cha kutokuweza kutubu. (Waebrania 6:4-8) Ndiyo, Wakristo ambao wamekuwa wakitumikia Mungu kwa muda mrefu, hata watiwa mafuta ambao ‘wanakuwa washiriki wa roho takatifu,’ huenda wakavutwa kwa kuelekezwa kwenye kitu fulani chenye ushawishi katika mfumo wa sasa.

15. Wengine wameangukaje kuhusiana na ngono na shughuli za kibiashara?

15 Watu kadha wameanguka kupitia tamaa ya mwili au tamaa ya utajiri. (1 Yohana 2:16) Bila shaka, nyege zinahusika wakati vijana wanapojiachilia waingilie ngono kabla ya kuoana. Lakini fikiria upande mwingine. Watu fulani waliooa au walioolewa wamechoka na mwenzi wao kisha wakachukuana na mtu mwingine anayeonekana wa kuvutia zaidi, anayefanya maongezi yawe matamu zaidi au mwenye ufanisi mwingi zaidi katika ulimwengu huu. Looo, jambo hilo limetokeza talaka na ndoa zenye kufanywa upya kiuasherati. Wengine ‘wameangushwa’ na ufuatiaji wa vitu vya kimwili, wakavutwa kuingia katika mazoea ya kibiashara ambayo kwa wazi ni ya udanganyifu au yasiyojali matakwa ya serikali ya kupata leseni na kulipa kodi. (Mathayo 22:21) Au wameendeleza shughuli za kujipatia pesa kwa njia za mikato au wakatumia njia za ujanja za kujitajirisha upesi ambazo zinashawishi watu wawe na pupa ya kujipatia faida kwa kuumiza ndugu zao. (Linganisha Matendo 20:33; 2 Wathesalonike 3:10, 11.) Zaidi ya jitihada hizo kugandamiza faida za Ufalme nyakati nyingine zimefanya watu waoneane uchungu mwingi na kugombana-gombana, hata wakashtakiana juu ya kupunjana. Biblia imethibitishwa kuwa kweli inaposema: “Hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi.”​—1 Timotheo 6:9.

16. Wale dada waliofungwa gerezani waliweka mfano gani mwema katika kupinga sana vishawishi?

16 Ikiwa tunatambua kwa unyenyekevu kwamba sisi si wenye nguvu sana hata tusiweze kuanguka, hapo inatupasa tupige moyo konde tusijiachilie tushindwe nguvu na mianzo ya ushawishi na dhambi. (Warumi 12:3; 1 Wakorintho 10:12) Akina dada waliokuwa katika kambi ya kazi ni mfano mwema kwetu:

Wengine wao walipelekwa, mmoja mmoja, kwenye jiji ambako kulikuwa na maduka, majumba ya sinema na tafrija nyingine. Kwa mfano, wawili wa makachero waliingiza dada ndani ya duka lenye wonyesho wa vyakula tele. Wakamwambia, ‘Chagua unachotaka.’ Yeye akasema hakuhitaji cho chote. Lilikuwa jambo baya sana kumwonyesha mtu aliyekuwa amepata chakula haba miaka mingi vimeza vya ukutani vyenye mikate iliyookwa sasa hivi na vitu vingine vitamu-vitamu. Vishawishi vingine kama hivyo vilitumiwa kwenye maduka ya idara hiyo na kwenye majumba ya sinema. Ingawa walimweka dada hapo kwa majuma kadha na kumwahidi kwamba angewekwa huru akiacha imani yake, ilikuwa kazi bure. Waliweza kumgeuza dada mmoja tu. Miezi kadha baadaye alirudi kambini, akiwa amekwisha kunenepa na sasa akiwa na mavazi mazuri sana. Huyo akawahutubia muda wa saa mbili wale waliokuwa dada zake hapo kwanza, nao hawakutaka hata kumsalimu. Inaonekana makachero walifikiri kwamba walifanya akili sana kwa kutumia jitihada hiyo na kwamba akina dada wangejipanga kwenye mstari kisha waikane imani yao. Lakini ng’o.

17. Imetupasa tuwe na maoni gani juu ya vishawishi tunavyoelekeana navyo?

17 Je! kama ingalikuwa ni wewe, unaona kwamba ungalishikilia azimio lako kwa kuelekeana na vishawishi hivyo? Lakini namna gani juu ya vishawishi unavyoelekeana navyo kwa sasa? Paulo aliandika hivi: “Angalieni, ndugu zangu, usiwe katika mmoja wenu moyo mbovu wa kutokuamini, kwa kujitenga na Mungu aliye hai. Lakini mwonyane kila siku, maadamu iitwapo leo; ili mmoja wenu asifanywe mgumu kwa [uwezo wa] udanganyifu wa dhambi.” (Waebrania 3:12, 13) Ili tuepuke kuanguka au kujitenga, tunahitaji kukaza fikira juu ya “leo.”

Kudhihirisha Imani “Leo”

18. Kwa sababu gani Waisraeli walishindwa kuingia katika pumziko la Mungu?

18 Paulo alitegemeza maelezo yake kuhusu neno “leo” juu ya mtajo wa maneno yaliyotokana na Zaburi 95:7-11. (Waebrania 3:7-11) Kama kifungu hicho kinavyotaja, Waisraeli walikuwa wamefanya mioyo yao ikawa migumu siku za Musa. Walipokwisha kusikia habari zilizoletwa na Yoshua na Kalebu juu ya Nchi ya Ahadi, Waisraeli walidhihirisha ukosefu wa imani. (Hesabu 13:17–14:38) Ingawa wakiwa huko wangeweza kufurahia amani na baraka nyingi wakati wa siku ya pumziko la Mungu iliyokuwa ikiendelea, kwa mioyo migumu na ukosefu wa imani Waisraeli walikataa kuiingia nchi hiyo waishi humo. Kwa hiyo Mungu akawapasisha kutanga-tanga jangwani miaka 40.​—Waebrania 3:17-19.

19. Ni wakati gani na namna gani tunaweza kuingia katika pumziko la Yehova?

19 Sabato kuu ya Mungu, au siku ya pumziko yake, inaendelea. (Mwanzo 1:31-2:3) Paulo aliandika kwamba “ikaliko ahadi ya kuingia katika raha [pumziko] yake.” (Waebrania 4:1, 9) Kwa hiyo, sisi Wakristo tunaweza kuingia sasa au kubaki katika pumziko hilo. Namna gani? Kwa kuonyesha imani, si katika Yoshua wa nyakati za kale, bali katika Yoshua Mkubwa Zaidi, kiongozi wetu Yesu. Tunahitaji pia kukomesha kazi za kutokuamini, kama zile zinazodhihirishwa na watu wasioamini kweli kweli kwamba siku moja Taratibu Mpya itakuja. Maisha zao zinategemea hasa tafrija au anasa. Huenda wakataka kujulikana kuwa “wamo,” kwa mfano kwa kujipatia cheo au daraja. Au huenda wakafuatia falsafa ya kutaka kujitengenezea jina la kuitwa ‘mtu mzuri.’

20, 21. (a) Ni kazi gani tunazohitaji kuepuka? (b) Ni kazi gani njema inatupasa kuishiriki, kama tulivyowekewa mfano na wale dada waliofungwa gerezani?

20 Ikiwa tuna imani katika Yesu na mambo yaliyoko mbele ya watu wa Mungu, utendaji wetu mbalimbali unapasa uonyeshe hivyo. Paulo aliandika hivi: “Mtu ambaye ameingia ndani ya pumziko la Mungu amepumzika mwenyewe pia kutoka kazi zake mwenyewe.” (Waebrania 4:10, NW) Kwa hiyo, badala ya sisi kuwa na kazi za kutokuamini au zile ambazo mtu anajaribu kutetea haki yake mwenyewe, ni lazima tuwe na kazi zinazoonyesha tuna imani.

21 Kazi kuu ya Kikristo ni kunena juu ya Yehova Mungu na Mwanaye. Kumhusu Yesu, Paulo alihimiza hivi: “Na tuyashike sana maungamo yetu [juu yake].” (Waebrania 4:14) Ni wazi kwamba tunaweza na inatupasa kufanya hivyo katika mikutano ya Kikristo tunapofanya huko tangazo la hadharani la tumaini letu. (Waebrania 10:23-25, NW) Lakini hilo “tangazo la hadharani” linapasa litie ndani kutolea watu wa nje ungamo la imani tu na matumaini yetu. Kwa kweli, inatupasa tujisikie tukilazimika kutoa “dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake [Mungu].” (Waebrania 13:15; 1 Wakorintho 9:16) Mwandikaji wa ile makala iliyotangulia kutajwa anasimulia mazungumzo yaliyoendeshwa pamoja na dada mmoja:

Nilisema wenye mamlaka wanawatia ninyi nyote magerezani kwa sababu mnawahubiria wengine, si kwa sababu ya imani zenu. Kama mngeketi peke yenu nyumbani na kuomba kwa unyamavu, hakuna mtu angewagundua. Dada akajibu, ‘Hiyo ni kweli, lakini wajibu wetu ni kusema na watu na kujipatia ndugu na dada wapya. Hatuwezi kufikiria mambo yetu tu na kujitayarishia wenyewe tu uzima wa kukaa duniani wakati wa ile mileani. Watu wote lazima wajulishwe uzima utakuwa namna gani wakati huo.’

22. Wewe una usadiki gani unaotegemea kitabu cha Waebrania?

22 Unaweza kuona kwamba wazo kuu katika kitabu cha Waebrania ni kwamba lazima sisi ‘tufanye yote tuwezayo tuingie ndani ya pumziko la Mungu, asije mtu ye yote akaanguka katika kutokutii.’ (Waebrania 4:11, NW) Tunaweza kuridhika sana sana kwa sababu ya kuwa katika pumziko hilo sasa hivi, na pia kwa sababu ya tumaini lililohakikishwa la kuendelea kuwa katika pumziko hilo wakati wote walio hai duniani watakapomwabudu Mungu. Hakuna shaka kwamba Yehova ana nia ya kupenda kubariki na kuhifadhi wale wanaoingia sasa ndani ya pumziko lake kupitia imani na utii. Yeye ndiye “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii nyingi.” (Waebrania 11:6, NW) Kama kuna shaka lo lote, basi shaka hilo ni upande wetu. Hata hivyo, si lazima sisi tuwe katika shaka. Kwa imani na uvumilivu wetu, na kwa msaada wa Mungu, sisi tunaweza “kulishika sana tumaini lililowekwa mbele yetu.”​—Waebrania 6:18, NW.​—Kutoka The Watchtower, February 15, 1983.

Wewe Umefaidika?

□ Ni shauri gani hasa au somo ulilopata kutokana na Waebrania?

◻ Unaweza kufaidikaje kutokana na mfano wa dada fulani waliofungwa gerezani?

◻ Unahimizwa na Waebrania 2:1 ufanye nini ili kuepuka kupeperuka?

◻ Wewe unaweza kuingiaje katika pumziko la Mungu?

[Blabu katika ukurasa wa 16]

Mashahidi wengi ambao katika nyumba zao Mnara wa Mlinzi ulipatikana wamehukumiwa kifungo cha miaka 10

[Blabu katika ukurasa wa 17]

Mashahidi ndio waliotifua kivumbi kweli kweli kambini. Wakati zaidi ya watatu kati yao walipokutana, waliamriwa watawanyike

[Picha katika ukurasa wa 20]

Waisraeli walisikia habari zilizoletwa na Yoshua na Kalebu walakini wakaonyesha ukosefu wa imani. Kwa hiyo hawangeweza kuliingia pumziko la Mungu katika Nchi ya Ahadi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki