Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • es25 kur. 47-57
  • Mei

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mei
  • Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025
  • Vichwa vidogo
  • Alhamisi, Mei 1
  • Ijumaa, Mei 2
  • Jumamosi, Mei 3
  • Jumapili, Mei 4
  • Jumatatu, Mei 5
  • Jumanne, Mei 6
  • Jumatano, Mei 7
  • Alhamisi, Mei 8
  • Ijumaa, Mei 9
  • Jumamosi, Mei 10
  • Jumapili, Mei 11
  • Jumatatu, Mei 12
  • Jumanne, Mei 13
  • Jumatano, Mei 14
  • Alhamisi, Mei 15
  • Ijumaa, Mei 16
  • Jumamosi, Mei 17
  • Jumapili, Mei 18
  • Jumatatu, Mei 19
  • Jumanne, Mei 20
  • Jumatano, Mei 21
  • Alhamisi, Mei 22
  • Ijumaa, Mei 23
  • Jumamosi, Mei 24
  • Jumapili, Mei 25
  • Jumatatu, Mei 26
  • Jumanne, Mei 27
  • Jumatano, Mei 28
  • Alhamisi, Mei 29
  • Ijumaa, Mei 30
  • Jumamosi, Mei 31
Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025
es25 kur. 47-57

Mei

Alhamisi, Mei 1

Njaa kubwa ilikuwa karibu kutokea.—Mdo. 11:28.

Wakristo wa karne ya kwanza waliathiriwa pia njaa kubwa ilipotokea “juu ya dunia yote inayokaliwa.” Bila shaka, vichwa vya familia walihangaika kuhusu jinsi ambavyo wangeziandalia chakula familia zao. Namna gani vijana ambao walikuwa na malengo ya kupanua huduma yao? Je, huenda walifikiri kwamba walipaswa kuahirisha malengo yao? Licha ya hali zao, Wakristo hao walibadilikana kulingana na hali. Waliendelea kuhubiri kwa njia yoyote waliyoweza na wakashiriki kwa furaha vitu vyao vya kimwili pamoja na waabudu wenzao huko Yudea. (Mdo. 11:​29, 30) Wale waliopokea msaada waliona jinsi Yehova alivyowasaidia moja kwa moja. (Mt. 6:​31-33) Bila shaka, walihisi wakiwa karibu zaidi na waabudu wenzao ambao waliwasaidia. Na wale waliotoa michango au kushiriki kwa njia nyingine katika kazi ya kutoa msaada, walipata furaha inayotokana na kutoa.—Mdo. 20:35. w23.04 16 ¶12-13

Ijumaa, Mei 2

Tunajua kwamba tutapata mambo tuliyomwomba, kwa kuwa tumeyaomba kwake.—1 Yoh. 5:15.

Nyakati nyingine, Yehova hujibu sala za watu wake kwa kuwachochea watu wasiomwabudu wawasaidie waabudu wake. Kwa mfano, alimchochea Mfalme Artashasta amruhusu Nehemia arudi Yerusalemu ili asaidie katika kazi ya kujenga upya jiji. (Neh. 2:​3-6) Leo pia, Yehova anaweza kuwachochea watu ambao hawamwabudu watusaidie tunapohitaji msaada. Kwa kawaida, sala zetu hazijibiwi kwa njia ya kustaajabisha. Lakini majibu tunayopata yanatupatia hasa jambo tunalohitaji ili kuendelea kuwa washikamanifu kwa Baba yetu wa mbinguni. Basi, uwe macho kutambua jinsi Yehova anavyojibu sala zako. Mara kwa mara, tua na utafakari jinsi Yehova anavyojibu sala zako. (Zab. 66:​19, 20) Ni lazima tuonyeshe imani si kwa kusali tu kwa Yehova, bali pia kwa kukubali njia yoyote anayotumia kujibu sala zetu.—Ebr. 11:6. w23.05 11 ¶13; 12 ¶15-16

Jumamosi, Mei 3

Ee Mungu wangu, ninafurahia kufanya mapenzi yako.—Zab. 40:8.

Tulipojiweka wakfu kwa Yehova, tuliahidi kwamba tutamwabudu yeye na kufanya mapenzi yake. Ni lazima tutimize ahadi hiyo. Kuishi kulingana na wakfu wetu si mzigo mzito. Hilo ni kwa sababu Yehova alituumba ili tufanye mapenzi yake. (Ufu. 4:11) Alituumba tukiwa na uhitaji wa kiroho na pia alituumba kwa mfano wake. Matokeo ni kwamba tunaweza kumkaribia na kufurahia kufanya mapenzi yake. Isitoshe tunapofanya mapenzi ya Mungu na kumfuata Mwana wake, sisi wenyewe ‘tunapata burudisho.’ (Mt. 11:​28-30) Hivyo, endelea kuimarisha upendo wako kwa Yehova kwa kutafakari kuhusu mambo yote mazuri ambayo amekufanyia na baraka za wakati ujao ambazo amekuahidi. Kadiri upendo wako kwa Yehova unavyozidi kukua, ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kwako kumtii. (1 Yoh. 5:3) Yesu alifaulu kufanya mapenzi ya Mungu kwa sababu alisali kwa Yehova ili kupata msaada na akakazia fikira zawadi ambayo angepata. (Ebr. 5:7; 12:2) Kama Yesu, mwombe Yehova akupe nguvu na uendelee kuweka tumaini la uzima wa milele wazi kabisa akilini mwako. w23.08 27-28 ¶4-5

Jumapili, Mei 4

Je, wewe unadharau utajiri wa fadhili zake na uvumilivu na subira, kwa sababu hujui kwamba Mungu kwa fadhili zake anajaribu kukuongoza wewe kwenye toba?—Rom. 2:4.

Sisi sote tunapenda kushirikiana na watu wenye subira. Kwa nini? Tunawaheshimu watu ambao wanaweza kusubiri kwa ajili ya jambo fulani bila kukasirika. Tunashukuru wengine wanapotuonyesha subira tunapokosea. Na tunashukuru kwamba ndugu au dada aliyetufundisha Biblia alituonyesha subira tulipokuwa tukipambana kujifunza, kukubali, na kuishi kulingana na fundisho fulani la Biblia. Na zaidi ya yote, tunashukuru kwamba Yehova Mungu ni mwenye subira kutuelekea! Ingawa tunafurahi kushirikiana na watu wenye subira, huenda isiwe rahisi sikuzote sisi wenyewe kuonyesha subira. Kwa mfano, huenda ikawa vigumu kwetu kuwa watulivu tunapolazimika kusubiri kwenye foleni ndefu ili kupata huduma fulani, hasa ikiwa tumechelewa. Huenda tukakasirika wengine wanapofanya jambo linalotuudhi. Na wakati mwingine, inaweza kuwa vigumu kwetu kuendelea kuusubiri ulimwengu mpya ambao Yehova ametuahidi. Hata hivyo, katika visa hivyo vyote, tunahitaji kuwa wenye subira zaidi. w23.08 20 ¶1-2

Jumatatu, Mei 5

Akawaambia wote warudi nyumbani, akabaki na wale 300 peke yao.—Amu. 7:8.

Baada ya kuagizwa na Yehova, Gideoni aliwapunguza wanajeshi wake kwa zaidi ya asilimia 99. Huenda alijiuliza: ‘Je, kweli mabadiliko haya yanahitajika? Je, tutafanikiwa?’ Ingawa hivyo, Gideoni alitii. Leo, wazee wanamwiga Gideoni kwa kutekeleza mabadiliko na kwa kutii mwongozo wa kitheokrasi. (Ebr. 13:17) Gideoni alimtii Yehova ingawa alikuwa na woga na alikabili hatari. (Amu. 9:17) Baada ya kupata uhakikisho kutoka kwa Yehova, Gideoni alisadiki kabisa kwamba Mungu angemsaidia kuwalinda watu Wake. Wazee wanaoishi katika maeneo ambayo kazi yetu imepigwa marufuku humwiga Gideoni. Kwa ujasiri wanaongoza katika mikutano na huduma licha ya hatari ya kukamatwa, kuhojiwa, kupoteza kazi, au kutendewa kikatili. Wakati wa dhiki kuu, wazee watahitaji ujasiri ili kutii mwongozo watakaopokea—licha ya hatari zitakazokuwepo. w23.06 5-6 ¶12-13

Jumanne, Mei 6

Wale wanaoniheshimu nitawaheshimu.—1 Sam. 2:30.

Yehova alihakikisha kwamba matendo mazuri ya Kuhani Mkuu Yehoyada yaliandikwa ili kutufundisha. (Rom. 15:4) Na Yehoyada alipokufa, alipewa heshima ya pekee kwa kuzikwa “katika Jiji la Daudi pamoja na wafalme, kwa sababu alikuwa ametenda mema katika Israeli kwa ajili ya Mungu wa kweli na nyumba Yake.” (2 Nya. 24:​15, 16) Simulizi kuhusu Yehoyada linaweza kutusaidia sisi sote kusitawisha woga kumwelekea Mungu. Wazee Wakristo wanaweza kumwiga Yehoyada kwa kuendelea kuwa chonjo na kulilinda kwa ushikamanifu kundi la Mungu. (Mdo. 20:28) Wale walio na umri mkubwa wanaweza kujifunza kutokana na Yehoyada kwamba ikiwa watamwogopa Yehova na kuendelea kuwa washikamanifu kwake, anaweza kuwatumia ili kutimiza kusudi Lake. Vijana wanaweza kujifunza jinsi Yehova alivyomtendea Yehoyada na wanaweza kumwiga Yehova kwa kuwastahi na kuwaheshimu watumishi washikamanifu wenye umri mkubwa, hasa wale ambao wametumikia kwa uaminifu kwa muda mrefu. (Met. 16:31) Acheni tuwaunge mkono kwa ushikamanifu “wale wanaoongoza” kwa kuwatii.—Ebr. 13:17. w23.06 17 ¶14-15

Jumatano, Mei 7

Midomo ya mwadilifu huwalisha wengi.—Met. 10:21.

Katika mikutano, tumia utambuzi unapoamua mara ambazo utanyoosha mkono ili kutoa maelezo. Ikiwa tutainua mkono mara nyingi sana, huenda tukamfanya yule anayeongoza ahisi kwamba analazimika kutuchagua tena na tena hata ingawa wengine bado hawajapata nafasi. Hilo linaweza kuwafanya wengine wasiinue mkono. (Mhu. 3:7) Ikiwa wahubiri wengi wanainua mkono wakati wa funzo, huenda tusitoe maelezo mara nyingi kama tunavyopenda. Wakati mwingine, huenda yule anayeongoza asituchague. Hilo linaweza kutuvunja moyo, lakini hatupaswi kukasirika tunapokosa kuchaguliwa. (Mhu. 7:9) Ikiwa huwezi kutoa maelezo mara nyingi kama unavyopenda, kwa nini usiwasikilize wengine kwa makini wanaposhiriki kisha baada ya mkutano uwapongeze kwa maelezo yao? Huenda ndugu na dada zako wakatiwa moyo unapowapongeza kama vile ambavyo wangetiwa moyo ikiwa ungetoa maelezo. w23.04 23-24 ¶14-16

Alhamisi, Mei 8

Moyo wangu uko imara, Ee Mungu.—Zab. 57:7.

Jifunze Neno la Mungu na kulitafakari. Kama vile mti unavyoweza kuwa imara kwa sababu ya mizizi yenye kina, tunaweza kubaki imara ikiwa imani yetu imetia mizizi kabisa katika Neno la Mungu. Mti unapozidi kukua, mizizi yake huzidi kupenya ardhini na kusambaa. Tunapojifunza na kutafakari, tunaimarisha imani yetu na kusadiki hata zaidi kwamba njia za Mungu zinafaa kabisa. (Kol. 2:​6, 7) Tafakari jinsi maagizo, mwongozo, na ulinzi wa Yehova ulivyowasaidia watumishi wake nyakati za kale. Kwa mfano, Ezekieli alimkazia uangalifu malaika alipokuwa akipima kwa makini vipimo vya hekalu kwenye maono. Maono hayo yalimwimarisha Ezekieli na yanatupatia masomo hususa kuhusu jinsi tunavyoweza kuunga mkono viwango vya Yehova vya ibada safi. (Eze. 40:​1-4; 43:​10-12) Tunanufaika pia tunapotenga wakati ili kujifunza na kutafakari mambo mazito zaidi ya Neno la Mungu. Tunaweza kuwa na moyo imara kwa kumtegemea kabisa Yehova.—Zab. 112:7. w23.07 18 ¶15-16

Ijumaa, Mei 9

Linda . . . uwezo wa kufikiri.—Met. 3:21.

Biblia ina mifano mingi mizuri ambayo wanaume vijana wanaweza kuiga. Wanaume hao wa zamani walimpenda Mungu na kushughulikia majukumu mbalimbali ili kuwatunza watu wa Mungu. Pia, unaweza kupata mifano mizuri ya wanaume Wakristo wakomavu katika familia yenu na katika kutaniko lenu. (Ebr. 13:7) Na una mfano mkamilifu wa Yesu Kristo. (1 Pet. 2:21) Unapochunguza kwa makini mifano hiyo, fikiria sifa zao za pekee. (Ebr. 12:​1, 2) Kisha uamue jinsi utakavyowaiga wanaume hao. Mwanamume mwenye uwezo wa kufikiri anatafakari kwa makini kabla ya kuamua atakachofanya. Hivyo, jitahidi kusitawisha uwezo huo na kuudumisha. Anza kwa kujifunza kanuni za Biblia na kufikiria kwa nini kanuni hizo zina manufaa. Kisha utumie kanuni hizo ili zikusaidie kufanya maamuzi yatakayomfurahisha Yehova. (Zab. 119:9) Hiyo ni hatua kubwa kuelekea kuwa mwanamume Mkristo mkomavu.—Met. 2:​11, 12; Ebr. 5:14. w23.12 24-25 ¶4-5

Jumamosi, Mei 10

[Muwe] tayari kujitetea mbele ya kila mtu anayewauliza sababu ya tumaini mlilo nalo, lakini mkifanya hivyo kwa upole na heshima kubwa.—1 Pet. 3:15.

Wazazi wanaweza kuwazoeza vizuri watoto wao kujibu kwa upole imani yao inapojaribiwa. (Yak. 3:13) Baadhi ya wazazi wanakuwa na vipindi vya mazoezi wakati wa ibada ya familia. Wanachunguza habari zinazoweza kujitokeza shuleni, wanazungumzia na kuigiza jinsi ya kujibu, na kuwafundisha watoto wao jinsi ya kuongea kwa upole, na kwa njia yenye kupendeza. Vipindi vya mazoezi vinaweza kuwasaidia Wakristo waeleze sababu zenye kusadikisha na kujisadikishia wao wenyewe kwamba wana sababu hakika inapohusu mambo wanayoamini. Mfululizo “Vijana Huuliza” kwenye jw.org unatia ndani madaftari kwa ajili ya matineja. Madaftari hayo yamekusudiwa kuwasaidia vijana waimarishe imani yao na kuwasaidia kujitayarisha kujibu kwa maneno yao wenyewe. Kwa kujifunza mfululizo huo kama familia, sisi sote tunaweza kujifunza jinsi ya kutetea imani yetu kwa upole, na kwa njia inayopendeza. w23.09 17 ¶10; 18 ¶15-16

Jumapili, Mei 11

Tusife moyo katika kufanya mema, kwa maana kwa wakati unaofaa tutavuna ikiwa hatutachoka kabisa.—Gal. 6:9.

Je, umewahi kujiwekea lengo la kiroho lakini ukashindwa kulitimiza? Ikiwa ndivyo, huko peke yako. Kwa mfano, Philip alitaka kuboresha sala zake na kusali mara nyingi zaidi, lakini ilikuwa vigumu kupata muda wa kusali. Erika alikuwa na lengo la kufika kwa wakati kwenye mkutano wa utumishi wa shambani, lakini alichelewa karibu kila mkutano. Ikiwa kuna lengo ambalo umeshindwa kulitimiza, usife moyo. Mara nyingi unahitaji muda na jitahidi nyingi ili kutimiza hata lengo rahisi. Kwa kuwa bado unatamani kutimiza lengo lako, hilo linaonyesha kwamba unathamini uhusiano wako pamoja na Yehova na unataka kumpa kilicho bora. Yehova anathamini jitihada zako. Bila shaka, hatarajii ufanye mambo yanayopita uwezo wako. (Zab. 103:14; Mika 6:8) Basi, unapaswa kuwa mwenye usawaziko unapojiwekea lengo, ukizingatia hali zako. w23.05 26 ¶1-2

Jumatatu, Mei 12

Ikiwa Mungu yuko upande wetu, ni nani atakayekuwa dhidi yetu?—Rom. 8:31.

Huenda watu wenye ujasiri wakapatwa na woga, lakini hawaruhusu woga uwazuie kufanya mambo yanayofaa. Danieli alikuwa kijana mwenye ujasiri sana. Alijifunza mambo ambayo manabii wa Mungu waliandika, kutia ndani unabii wa Yeremia. Kutokana na mambo aliyojifunza, baadaye alitambua kwamba utekwa wa muda mrefu wa Wayahudi huko Babiloni ulikuwa karibu kwisha. (Dan. 9:2) Danieli alipoona unabii wa Biblia ukitimizwa, bila shaka hilo lilimsaidia kumtumaini Yehova hata zaidi, na wale wanaomtumaini Mungu kabisa wanaweza kuwa na ujasiri mwingi. (Linganisha Waroma 8:​32, 37-39.) Jambo muhimu zaidi, Danieli alisali kwa Baba yake wa mbinguni mara nyingi. (Dan. 6:10) Aliungama dhambi zake kwa Yehova na akamweleza hisia zake. Na Danieli aliomba msaada. (Dan. 9:​4, 5, 19) Alikuwa mwanadamu kama sisi, basi, hakuzaliwa akiwa jasiri. Badala yake, alisitawisha sifa hiyo kupitia kujifunza, kusali, na kumtumaini Yehova. w23.08 3 ¶4; 4 ¶7

Jumanne, Mei 13

Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili waone matendo yenu mema na kumtukuza Baba yenu aliye mbinguni.—Mt. 5:16.

Tunapotii mamlaka zilizo kubwa, tunajinufaisha sisi wenyewe na wengine. Jinsi gani? Jambo moja ni kwamba tunaepuka adhabu inayotolewa kwa wale wanaovunja sheria. (Rom. 13:​1, 4) Utiifu wetu tukiwa mtu mmojammoja unaweza kuathiri maoni ya wenye mamlaka kuhusu Mashahidi wa Yehova kwa ujumla. Kwa mfano, miaka mingi iliyopita nchini Nigeria, wanajeshi waliingia katika Jumba la Ufalme wakati wa mkutano wa kutaniko, wakiwatafuta waandamanaji ambao walikuwa wakipinga malipo ya kodi. Lakini ofisa aliyekuwa akiwasimamia aliwaambia wanajeshi hao waondoke, akisema hivi: “Sikuzote Mashahidi wa Yehova hulipa kodi.” Kila mara unapotii sheria, unadumisha sifa nzuri ya watu wa Yehova, sifa ambayo huenda siku moja ikawalinda waabudu wenzako. w23.10 9 ¶13

Jumatano, Mei 14

Mnahitaji uvumilivu, ili baada ya kufanya mapenzi ya Mungu, mpokee utimizo wa ile ahadi.—Ebr. 10:36.

Baadhi ya watumishi wa Yehova wamekuwa wakisubiri kwa muda mrefu mwisho wa mfumo huu wa mambo. Kwa maoni ya kibinadamu, huenda ikaonekana kwamba kutimizwa kwa ahadi ya Mungu kunakawia. Yehova anaelewa jambo hilo, na alimhakikishia hivi nabii Habakuki: “Kwa maana maono hayo bado yatatimia kwa wakati wake uliowekwa, nayo yanasonga haraka kuelekea mwisho wake, nayo hayatasema uwongo. Hata yakikawia, endelea kuyatarajia! Kwa maana hakika yatatimia. Hayatachelewa!” (Hab. 2:3) Je, Mungu alitoa uhakikisho huo kwa ajili tu ya Habakuki? Au je, maneno yake yanatuhusu leo? Akiongozwa na roho, mtume Paulo alielekeza maneno hayo kwa Wakristo ambao wanatarajia ulimwengu mpya. (Ebr. 10:37) Naam, tunaweza kuwa na uhakika kwamba hata ikiwa inaonekana kwamba ahadi ya Mungu ya kutukomboa inachelewa, ‘hakika itatimia. Haitachelewa!’ w23.04 30 ¶16

Alhamisi, Mei 15

Waisraeli wote wakaanza kumnung’unikia Musa.—Hes. 14:2.

Waisraeli walikataa uthibitisho ulio wazi kwamba Yehova alikuwa akimtumia Musa akiwa mwakilishi Wake. (Hes. 14:​10, 11) Tena na tena, walikataa kukubali kwamba Yehova alikuwa akimtumia Musa kuwaongoza. Matokeo ni kwamba kizazi hicho cha Waisraeli kilizuiliwa kuingia katika Nchi ya Ahadi. (Hes. 14:30) Hata hivyo, baadhi ya Waisraeli walifuata mwongozo wa Yehova. Kwa mfano, Yehova alisema hivi: “Kalebu . . . aliendelea kunifuata kwa moyo wote.” (Hes. 14:24) Mungu alimthawabisha Kalebu, na hata alimpatia eneo alilochagua Kalebu mwenyewe katika nchi ya Kanaani. (Yos. 14:​12-14) Pia, Waisraeli walioruhusiwa kuingia katika Nchi ya Ahadi waliweka mfano mzuri wa kufuata mwongozo wa Yehova. Yoshua alipochukua nafasi ya Musa akiwa kiongozi aliyewekwa rasmi, Waisraeli “wakamheshimu sana sikuzote za maisha yake.” (Yos. 4:14) Matokeo ni kwamba Yehova aliwabariki kwa kuwaingiza katika nchi aliyowaahidi.—Yos. 21:​43, 44. w24.02 21 ¶6-7

Ijumaa, Mei 16

Yeyote anayempenda Mungu lazima pia ampende ndugu yake.—1 Yoh. 4:21.

Kama tu ambavyo daktari anaweza kupata habari fulani kuhusu afya ya moyo wetu anapochunguza mapigo ya moyo, tunaweza kujua ikiwa upendo wetu kwa Mungu una nguvu au ni dhaifu kwa kuchunguza jinsi tunavyowapenda wengine. Tukitambua kwamba upendo wetu kwa waabudu wenzetu umeanza kuwa dhaifu kwa kiwango fulani, hiyo inaweza kuonyesha kwamba upendo wetu kwa Mungu umeanza kuwa dhaifu pia. Lakini tunapowaonyesha waabudu wenzetu upendo kwa ukawaida, hiyo ni ishara kwamba upendo wetu kwa Mungu uko imara. Ikiwa upendo wetu kwa ndugu na dada zetu unakuwa dhaifu, hilo ni tatizo kubwa. Kwa nini? Kwa sababu hilo linamaanisha uhusiano wetu na Yehova uko hatarini. Mtume Yohana anaonyesha jambo hilo waziwazi anapotukumbusha hivi: “Mtu ambaye hampendi ndugu yake, ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hajamwona.” (1 Yoh. 4:20) Tunajifunza nini? Tutamfurahisha Yehova ikiwa tu ‘tutapendana.’—1 Yoh. 4:​7-9, 11. w23.11 8 ¶3; 9 ¶5-6

Jumamosi, Mei 17

Baba yako na mama yako watafurahi.—Met. 23:25.

Alipokuwa kijana, Mfalme Yehoashi alifanya uamuzi wenye hekima. Kwa kuwa hakuwa na baba, alifuata mwongozo kutoka kwa Kuhani Mkuu mwaminifu Yehoyada. Kuhani huyo alimshauri Yehoashi kana kwamba alikuwa mwana wake mwenyewe. Matokeo ni kwamba Yehoashi, kwa hekima, aliamua kuwaongoza watu katika ibada safi na kumtumikia Yehova. Yehoashi hata alifanya mpango ili hekalu la Yehova lifanyiwe marekebisho. (2 Nya. 24:​1, 2, 4, 13, 14) Ikiwa unafundishwa kumpenda Yehova na kuishi kulingana na viwango vyake, unapewa zawadi yenye thamani sana. (Met. 2:​1, 10-12) Wazazi wako wanaweza kukuzoeza kwa njia nyingi. Unapofuata ushauri wa Maandiko unaopewa, utawafurahisha wazazi wako. Jambo muhimu zaidi, utamfurahisha Mungu na utajenga urafiki wa kudumu pamoja naye. (Met. 22:6; 23:​15, 24) Je, hilo halikupatii sababu nzuri ya kuiga mfano wa Yehoashi alipokuwa kijana? w23.09 8-9 ¶3-5

Jumapili, Mei 18

Nitawasikiliza.—Yer. 29:12.

Yehova anaahidi kusikiliza sala zetu. Mungu wetu anawapenda waabudu wake waaminifu, hivyo hatapuuza kamwe sala zao. (Zab. 10:17; 37:28) Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba atatupatia kila kitu tunachomwomba. Huenda tukapata baadhi ya mambo tunayoomba katika ulimwengu mpya. Yehova anazingatia jinsi maombi yetu yanavyohusiana na kusudi lake. (Isa. 55:​8, 9) Mojawapo ya mambo anayotaka ni kwamba dunia ijae watu wanaomtii yeye kwa shangwe akiwa Mtawala wao. Lakini Shetani alidai kwamba wanadamu wangekuwa na maisha mazuri zaidi ikiwa wangejitawala. (Mwa. 3:​1-5) Yehova aliwaruhusu wanadamu wajitawale ili kuthibitisha kwamba madai ya Ibilisi ni ya uwongo. Hata hivyo, serikali za wanadamu zimesababisha matatizo mengi ambayo tunakabili leo. (Mhu. 8:9) Tunajua kwamba Yehova hataondoa sasa matatizo haya yote. w23.11 21 ¶4-5

Jumatatu, Mei 19

Nimekuweka uwe baba ya mataifa mengi.—Rom. 4:17.

Yehova aliahidi kwamba kupitia Abrahamu mataifa mengi yangebarikiwa. Lakini Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 100 na Sara miaka 90, mwana aliyeahidiwa hakuwa amezaliwa. Kwa maoni ya wanadamu, ilionekana kwamba haiwezekani kwa Abrahamu na Sara kuwa na mwana. Hilo lilikuwa jaribu kubwa kwa Abrahamu. “Lakini kwa kutegemea tumaini, alikuwa na imani kwamba angekuwa baba ya mataifa mengi.” (Rom. 4:​18, 19) Na hatiMeie, tumaini la Abrahamu lilitimia. Alikuja kuwa baba ya Isaka, mwana aliyemsubiri kwa muda mrefu. (Rom. 4:​20-22) Tunaweza kuwa na kibali cha Mungu, kuhesabiwa kuwa waadilifu, na kuwa rafiki za Mungu kama Abrahamu. Hilo ndilo jambo ambalo Paulo alikazia alipoandika hivi: “Maneno ‘ilihesabiwa kwake’ hayakuandikwa kwa ajili [ya Abrahamu] tu, bali pia kwa ajili yetu ambao itahesabiwa, kwa sababu tunamwamini Yeye aliyemfufua Yesu.” (Rom. 4:​23, 24) Kama Abrahamu, tunahitaji kuwa na imani, matendo, pamoja na tumaini. w23.12 7 ¶16-17

Jumanne, Mei 20

Umeona dhiki yangu; unajua mateso makali yaliyo ndani yangu.—Zab. 31:7.

Unapokabili jaribu linalokufanya uogope, kumbuka kwamba Yehova anajua jaribu unalokabili na jinsi linavyokufanya uhisi. Kwa mfano, Yehova aliona jinsi Waisraeli walivyotendewa isivyo haki nchini Misri na pia ‘alijua maumivu yao.’ (Kut. 3:7) Hata hivyo, huenda usitambue jinsi Yehova anavyokusaidia unapokabili jaribu linalokuogopesha. Basi, unaweza kufanya nini? Mwombe Yehova akusaidie uone jinsi anavyokutegemeza. (2 Fal. 6:​15-17) Kisha fikiria maswali haya: Je, kuna hotuba yoyote au maelezo katika mkutano wa kutaniko yaliyokuimarisha? Je, kuna chapisho lolote, video, au wimbo uliotungwa ambao umekutia moyo? Je, kuna mtu yeyote ambaye amekueleza jambo au kukusomea andiko lililokutia moyo? Inaweza kuwa rahisi kusahau jinsi ndugu na dada wanavyotupenda na jinsi chakula cha kiroho kinavyotunufaisha. Hata hivyo, hizo ni zawadi za pekee kutoka kwa Yehova. (Isa. 65:13; Marko 10:​29, 30) Zinathibitisha kwamba Yehova anakujali. (Isa. 49:​14-16) Na zinathibitisha kwamba anastahili kutumainiwa. w24.01 4-5 ¶9-10

Jumatano, Mei 21

Uwawezeshe watumwa wako waendelee kutangaza neno lako kwa ujasiri wote.—Mdo. 4:29.

Muda mfupi kabla ya kurudi mbinguni, Yesu aliwakumbusha wanafunzi wake kuhusu mgawo wao wa kutoa ushahidi kumhusu “katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8; Luka 24:​46-48) Muda mfupi baadaye, viongozi wa Kiyahudi walimkamata mtume Petro na Yohana na kuwaleta mbele ya Sanhedrini, wakawaamuru wanaume hao waaminifu waache kuhubiri, na hata wakawatisha. (Mdo. 4:​18, 21) Petro na Yohana walisema hivi: “Kama ni sawa machoni pa Mungu kuwasikiliza ninyi badala ya Mungu, hukumuni ninyi wenyewe. Lakini sisi hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.” (Mdo. 4:​19, 20) Petro na Yohana walipoachiliwa huru, wanafunzi walipaza sauti zao kwa Yehova katika sala ambayo ilikazia kufanya mapenzi yake. Yehova alijibu sala hiyo ya unyoofu.—Mdo. 4:31. w23.05 5 ¶11-12

Alhamisi, Mei 22

Huyu ni Mwanangu, mpendwa.—Mt. 17:5.

Kwa miaka mingi sana, Yehova na Mwana wake mpendwa walijenga uhusiano wa karibu sana na wenye upendo mwingi. Huo ndio uhusiano uliodumu kwa muda mrefu zaidi katika ulimwengu wote. Yehova alieleza waziwazi upendo wake kwa Yesu kama tunavyosoma kwenye andiko la leo. Yehova angeweza kusema tu, ‘Huyu ni mtu ninayemkubali.’ Hata hivyo, kwa kuwa alitaka tujue jinsi anavyompenda Yesu, alimwita “Mwanangu, mpendwa.” Yehova alijivunia kuwa na mwana kama Yesu, hasa kwa sababu Yesu alikuwa tayari kutoa uhai wake. (Efe. 1:7) Na Yesu hakuwa na shaka hata kidogo kuhusu jinsi Baba yake alivyompenda. Yesu alikuwa na uhakika kabisa na upendo wa Baba yake hivi kwamba aliuhisi moyoni mwake. Alieleza tena na tena kwa uhakika kwamba Baba yake anampenda.—Yoh. 3:35; 10:17; 17:24. w24.01 28 ¶8

Ijumaa, Mei 23

Ni afadhali kuchagua jina jema kuliko mali nyingi.—Met. 22:1.

Wazia jambo hili: Mtu unayempenda anasema jambo fulani baya kukuhusu. Unajua kwamba jambo alilosema ni uwongo, lakini baadhi ya watu wanamwamini. Jambo baya hata zaidi, wanaanza kuwaambia wengine uwongo huo, na wengine wengi wanaamini jambo hilo. Ungehisije? Inaelekea kwamba uchongezi huo utakufanya ujihisi vibaya, sivyo? Mfano huo unaweza kutusaidia kuelewa jinsi Yehova alivyohisi sifa yake nzuri ilipochafuliwa. Mmoja kati ya wana wake wa kiroho alimweleza mwanamke wa kwanza, Hawa, uwongo kumhusu. Naye Hawa aliamini uwongo huo. Kwa sababu ya uwongo huo, wazazi wetu wa kwanza walimwasi Yehova. Matokeo ni kwamba dhambi na kifo vikaenea katika familia ya wanadamu. (Mwa. 3:​1-6; Rom. 5:12) Matatizo yote tunayoona ulimwenguni leo—vifo, vita, huzuni—yametokana na uwongo ambao Shetani ameeneza. Je, Yehova anaumia kwa sababu ya uchongezi huo na matokeo yake mabaya? Bila shaka. Hata hivyo, Yehova hana kinyongo. Isitoshe, anaendelea kuwa “Mungu mwenye furaha.”—1 Tim. 1:11. w24.02 8 ¶1-2

Jumamosi, Mei 24

Ninawezaje kufanya uovu huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?—Mwa. 39:9.

Unawezaje kuiga mfano wa Yosefu unaposhawishiwa? Unaweza kuamua sasa jambo utakalofanya kishawishi kitakapotokea. Jifunze kukataa mara moja mambo ambayo Yehova anachukia, na kuepuka kuendelea kuyafikiria. (Zab. 97:10; 119:165) Kwa njia hiyo, hutatenda dhambi unaposhawishiwa. Huenda unajua kwamba umeipata kweli na unataka kumtumikia Yehova kwa moyo wako wote, lakini bado kuna kitu kinachokuzuia kujiweka wakfu na kubatizwa. Unaweza kujifunza kutokana na mfano wa Mfalme Daudi. Mwombe Yehova hivi: “Nichunguze kabisa, Ee Mungu, uujue moyo wangu. Nipime, uyajue mawazo yangu yanayonihangaisha. Angalia ikiwa kuna njia yoyote yenye madhara ndani yangu, uniongoze katika njia ya milele.” (Zab. 139:​23, 24) Yehova huwabariki wale “wanaomtafuta kwa bidii.” Kujitahidi kufikia lengo lako la kujiweka wakfu na kubatizwa kunamwonyesha kwamba unamtafuta kwa bidii.—Ebr. 11:6. w24.03 6 ¶13-15

Jumapili, Mei 25

Hahitaji kutoa dhabihu kila siku.—Ebr. 7:27.

Kuhani mkuu alikuwa na jukumu la kuwawakilisha watu mbele za Mungu. Haruni kuhani mkuu wa kwanza wa Israeli, alichaguliwa na Yehova mpango wa hema la ibada ulipoanzishwa. Hata hivyo, kama mtume Paulo alivyoeleza, “wengi walikuwa makuhani mmoja baada ya mwingine kwa sababu kifo kiliwazuia wasiendelee kuwa makuhani.” (Ebr. 7:​23-26) Na kwa sababu walikuwa wanadamu wasio wakamilifu, makuhani hao wakuu walihitaji kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi zao wenyewe. Hiyo ni tofauti kubwa sana kati ya makuhani wakuu wa Israeli na Kuhani Mkuu sana, Yesu Kristo. Akiwa Kuhani wetu Mkuu, Yesu Kristo ni “mhudumu . . . wa hema la kweli, ambalo limesimamishwa na Yehova, na si mwanadamu.” (Ebr. 8:​1, 2) Paulo alieleza kwamba “kwa sababu [Yesu] anaendelea kuishi milele, hakuna anayerithi ukuhani wake.” Paulo aliongezea kwamba Yesu ni kuhani “asiye na unajisi, aliyetenganishwa na watenda dhambi” na tofauti na makuhani wakuu wa Israeli, “hahitaji kutoa dhabihu kila siku” kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe. w23.10 26 ¶8-9

Jumatatu, Mei 26

Mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza zilikuwa zimepitilia mbali.—Ufu. 21:1.

“Mbingu ya kwanza” inarejelea serikali za kisiasa zinazoongozwa na Shetani na roho wake waovu. (Mt. 4:​8, 9; 1 Yoh. 5:19) Katika Biblia, neno “dunia” linaweza kurejelea watu wanaoishi duniani. (Mwa. 11:1; Zab. 96:1) Hivyo, “dunia ya kwanza” inarejelea jamii ya wanadamu waovu leo. Si kwamba Yehova atarekebisha au kuboresha “mbingu” na “dunia” ya kwanza; badala yake, ataziondoa kabisa kwa kuzibadili. Ataondoa mbingu na dunia ya sasa na kuleta “mbingu mpya na dunia mpya”—yaani, serikali mpya na jamii mpya ya wanadamu. Yehova ataifanya dunia kuwa mpya na atawafanya wanadamu kuwa wapya kwa kuwarudishia hali yao ya ukamilifu. Kama Isaya alivyotabiri, dunia nzima itafanywa kuwa bustani maridadi—kama ilivyokuwa bustani ya Edeni. Kila mmoja wetu atafanywa kuwa mpya, kwa kuponywa kikamili. Vilema, vipofu, na viziwi wataponywa, na hata waliokufa watarudishiwa uhai.—Isa. 25:8; 35:​1-7. w23.11 4 ¶9-10

Jumanne, Mei 27

Iweni tayari.—Mt. 24:44.

“Dhiki kuu” itaanza ghafla. (Mt. 24:21) Hata hivyo, tofauti na misiba mingine mingi, tunatarajia kwamba dhiki kuu itatokea. Miaka 2,000 hivi iliyopita, Yesu aliwaonya wafuasi wake wajitayarishe kwa ajili ya siku hiyo. Ikiwa tumejitayarisha, itakuwa rahisi zaidi kwetu kuvumilia kipindi hicho kigumu na kuwasaidia wengine wafanye hivyo pia. (Luka 21:36) Tutahitaji sifa ya uvumilivu ili kumtii Yehova, tukitumaini kwamba atatulinda. Tutafanya nini ikiwa ndugu zetu watapoteza baadhi ya mali zao au mali zao zote? (Hab. 3:​17, 18) Tutahitaji sifa ya huruma ili tuchochewe kuwasaidia. Tutatendaje ikiwa baada ya kushambuliwa na muungano wa mataifa, tutalazimika kuishi na ndugu na dada zetu kwa muda fulani katika nyumba moja? (Eze. 38:​10-12) Tutahitaji kuwaonyesha upendo wenye nguvu ili tufaulu kukabiliana na kipindi hicho kigumu. w23.07 2 ¶2-3

Jumatano, Mei 28

Endeleeni kuangalia sana jinsi mnavyotembea, si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkiutumia vizuri kabisa wakati wenu.—Efe. 5:​15, 16.

Wenzi wa ndoa wanaweza kujifunza kutokana na mfano wa Akila na Prisila, wenzi wa ndoa waliopendwa na Wakristo wengi wa karne ya kwanza. (Rom. 16:​3, 4) Walifanya kazi ya kimwili, walihubiri, na kuwasaidia wengine wakiwa pamoja. (Mdo. 18:​2, 3, 24-26) Kila mara Biblia inapowataja Akila na Prisila, sikuzote wanatajwa pamoja. Wenzi wa ndoa wanawezaje kuwaiga? Fikiria mambo mengi ambayo wewe na mwenzi wako mnahitaji kufanya. Je, unaweza kushirikiana na mwenzi wako kufanya baadhi ya mambo hayo, badala ya kuyafanya peke yako? Kwa mfano, Akila na Prisila walihubiri pamoja. Je, mnapanga kuhubiri pamoja kwa ukawaida? Akila na Prisila pia walifanya kazi pamoja. Huenda wewe na mwenzi wako hamfanyi kazi ileile, lakini je, mnaweza kufanya kazi za nyumbani pamoja? (Mhu. 4:9) Mnaposaidiana kufanya kazi fulani, mtahisi mna ushirikiano zaidi na mtapata fursa za kuzungumza. w23.05 22-23 ¶10-12

Alhamisi, Mei 29

Ninapoogopa, ninakutumaini wewe.—Zab. 56:3.

Sisi sote huhisi woga nyakati fulani. Kwa mfano, Mfalme Sauli alipokuwa akimwinda Daudi, Daudi aliamua kukimbilia kwenye jiji la Wafilisti la Gathi. Baada ya muda mfupi, Akishi, mfalme wa Gathi, alijua kwamba Daudi ndiye yule shujaa ambaye aliimbiwa wimbo kwamba ameua “makumi ya maelfu” ya Wafilisti. Daudi ‘akaogopa sana.’ (1 Sam. 21:​10-12) Aliogopa mambo ambayo Akishi angemtendea. Daudi alishindaje woga wake? Kwenye Zaburi ya 56, Daudi anaeleza hisia zake alipokuwa Gathi. Zaburi hiyo inataja waziwazi jinsi Daudi alivyoogopa, na pia jinsi alivyoshinda woga huo. Alipoogopa, Daudi alimtumaini Yehova. (Zab. 56:​1-3, 11) Daudi alikuwa na sababu nzuri za kumtumaini Yehova. Kwa msaada wa Yehova, Daudi alitumia mbinu isiyo ya kawaida lakini yenye matokeo mazuri. Alijifanya mwenda wazimu! Badala ya kumwona kuwa tishio, Akishi alimwona Daudi kuwa kero, hivyo Daudi aliweza kutoroka.—1 Sam. 21:13–22:1. w24.01 2 ¶1-3

Ijumaa, Mei 30

Wale walio pamoja naye walioitwa na waliochaguliwa na walio waaminifu watawashinda.—Ufu. 17:14.

Ni nani wanaotajwa kwenye andiko la leo? Watiwa-mafuta waliofufuliwa! Kwa hiyo, watiwa-mafuta wa mwisho watakapochukuliwa kwenda mbinguni mwishoni mwa dhiki kuu, mojawapo ya migawo yao ya kwanza ni kupigana. Baada ya kuchukuliwa kwenda mbinguni, watatumikia pamoja na Kristo na malaika wake watakatifu, katika vita vya mwisho dhidi ya maadui wa Mungu. Fikiria jambo hili! Wakiwa duniani, baadhi ya Wakristo watiwa-mafuta wamezeeka, au hata ni dhaifu. Lakini watakapofufuliwa na kwenda mbinguni, watakuwa viumbe wa roho wenye nguvu na wasioweza kufa, ambao wamepewa mgawo wa kupigana pamoja na Mfalme-Shujaa, Yesu Kristo. Baada ya vita vya Har–​Magedoni kupiganwa, watashiriki katika kuwaongoza wanadamu kwenye ukamilifu. Bila shaka, wakati huo wakiwa mbinguni wataweza kuwasaidia hata zaidi ndugu na dada zao wapendwa walio duniani, kuliko walivyofanya walipokuwa wanadamu wasio wakamilifu! w24.02 6-7 ¶15-16

Jumamosi, Mei 31

Endeleeni kutembea kwa roho nanyi hamtatenda kwa tamaa za mwili hata kidogo.—Gal. 5:16

Baadhi ya watu ambao wako tayari kwa ajili ya ubatizo husita kujiweka wakfu na kubatizwa. Huenda wakajiuliza, ‘Namna gani nikifanya dhambi nzito na kutengwa na ushirika?’ Ikiwa una woga huo, uwe na uhakika kwamba Yehova atakupatia kila kitu unachohitaji ili ‘utembee kwa kumstahili yeye ili kumpendeza kikamili.’ (Kol. 1:10) Pia, atakupatia nguvu za kufanya yaliyo sawa. Tayari amethibitisha kwamba anaweza kufanya hivyo kwa kuwasaidia watu wengine wengi wafanye yaliyo sawa. (1 Kor. 10:13) Hiyo ni mojawapo ya sababu zinazofanya watu wachache tu watengwe na kutaniko la Kikristo. Yehova anawasaidia watu wake waendelee kuwa waaminifu. Kila mwanadamu ambaye si mkamilifu anashawishiwa kufanya mambo mabaya. (Yak. 1:14) Hata hivyo, wewe ndiye unayeamua ikiwa utatenda kulingana na kishawishi hicho au la. Ukweli ni kwamba wewe ndiye unayeamua jinsi utakavyoishi. Ingawa baadhi ya watu huenda wakadai haiwezekani, unaweza kujifunza kujidhibiti usinaswe na kishawishi. w24.03 5 ¶11-12

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki