Aprili
Jumanne, Aprili 1
Ni jambo gani hili ulilonitendea? . . . Kwa nini umenitendea hila?—Mwa. 29:25.
Watumishi wa Yehova wanaotajwa katika Biblia walikabili changamoto ambazo hawakutarajia. Mfikirie Yakobo. Baba yake alimwambia achukue mke kutoka kwa binti za Labani, mtu wao wa ukoo aliyemwabudu Yehova, na akamhakikishia kwamba Yehova angembariki sana. (Mwa. 28:1-4) Basi, Yakobo akafanya jambo linalofaa. Aliondoka nchi ya Kanaani na kusafiri kwenda nyumbani kwa Labani, ambaye alikuwa na mabinti wawili—Lea na Raheli. Yakobo alimpenda Raheli, binti mdogo wa Labani, na akakubali kumfanyia baba yake kazi kwa miaka saba kabla ya kumwoa Raheli. (Mwa. 29:18) Lakini mambo hayakwenda kama Yakobo alivyotarajia. Labani alimdanganya Yakobo na akamwoa Lea, binti yake mkubwa. Baada ya juma moja, Labani alimruhusu Yakobo amwoe Raheli, lakini ikiwa tu angefanya kazi kwa miaka mingine saba. (Mwa. 29:26, 27) Pia, Labani alimtendea Yakobo isivyo haki katika makubaliano ya kazi. Kwa ujumla, Labani alimtendea Yakobo isivyo haki kwa miaka 20!—Mwa. 31:41, 42. w23.04 15 ¶5
Jumatano, Aprili 2
Mwageni mioyo yenu mbele zake.—Zab. 62:8.
Tunaweza kuzungumza na nani tunapohitaji faraja na mwongozo? Tunajua jibu la swali hilo. Tunaweza kuzungumza na Yehova Mungu katika sala. Yehova anatukaribisha tufanye hivyo. Anataka tusali mara nyingi—‘tusali bila kuacha.’ (1 The. 5:17) Tunaweza kusali kwake kwa uhuru na kumwomba mwongozo kuhusu jambo lolote katika maisha yetu. (Met. 3:5, 6) Kwa kuwa Yehova ni Mungu mkarimu, anatukaribisha tusali kwake mara nyingi tupendavyo. Yesu alielewa kwamba Yehova anathamini sana sala zetu. Muda mrefu kabla ya kuja duniani alimwona Baba yake akijibu sala za wanaume na wanawake waaminifu. Kwa mfano, Yesu alikuwa kando ya Baba yake alipojibu sala za unyoofu za Hana, Daudi, Eliya, na watumishi wengine wengi waaminifu. (1 Sam. 1:10, 11, 20; 1 Fal. 19:4-6; Zab. 32:5) Ndiyo sababu Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wasali mara nyingi na wakiwa na uhakika!—Mt. 7:7-11. w23.05 2 ¶1, 3
Alhamisi, Aprili 3
Kuwaogopa wanadamu ni mtego, lakini yule anayemtumaini Yehova atalindwa.—Met. 29:25.
Kuhani Mkuu Yehoyada alimwogopa Yehova. Jambo hilo lilikuwa wazi wakati Atalia, binti ya Yezebeli, alipochukua mamlaka kwa nguvu na kuanza kutawala Yuda. Alikuwa mkatili na mwenye pupa sana ya kupata mamlaka hivi kwamba alijaribu kuwaua warithi wote, yaani, wajukuu wake mwenyewe! (2 Nya. 22:10, 11) Mmoja wa watoto hao—Yehoashi—aliokoka kwa sababu Yehoshabeathi, mke wa Yehoyada, alimwokoa. Yeye na mume wake walimficha mtoto huyo na kumtunza. Kwa njia hiyo, Yehoyada na Yehoshabeathi walilinda ukoo wa wafalme waliotokana na Daudi. Yehoyada alikuwa mshikamanifu kwa Yehova na hakutetemeka kwa woga kwa sababu ya Atalia. Yehoashi alipokuwa na umri wa miaka saba, Yehoyada alionyesha ushikamanifu wake tena kwa Yehova. Alifanya mpango fulani. Ikiwa mpango huo ungefaulu, Yehoashi angekuwa mfalme, mrithi wa Daudi aliyestahili. Hata hivyo, ikiwa mpango huo ungekosa kufaulu, Yehoyada angeuawa. Yehova alibariki mpango huo, nao ukafaulu. w23.06 17 ¶12-13
Ijumaa, Aprili 4
[Jua] kwamba Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu na kwamba yeye humpa ufalme huo yeyote anayetaka kumpa.—Dan. 4:25.
Ingekuwa rahisi kwa Mfalme Nebukadneza kumwona Danieli kuwa mwasi kwa kutangaza ujumbe huo na hata kuagiza Danieli auawe. Lakini Danieli alionyesha ujasiri na kutangaza ujumbe huo. Huenda ni nini kilichomsaidia Danieli awe jasiri katika maisha yake yote? Alipokuwa mtoto, Danieli aliiga mfano mzuri wa baba na mama yake. (Kum. 6:6-9) Danieli hakujua mambo ya msingi tu kuhusu Sheria, kama vile zile amri kumi, bali pia alijua habari nyingi kuhusu chakula ambacho Mwisraeli angeweza kula au kutokula. (Law. 11:4-8; Dan. 1:8, 11-13) Pia, Danieli alijifunza kuhusu historia ya watu wa Mungu na alijua kilichowapata walipokosa kuishi kulingana na viwango vya Yehova. (Dan. 9:10, 11) Mambo ambayo Danieli alijionea katika maisha yake yote, yalimpa uhakika kwamba Yehova na malaika Wake wenye nguvu walikuwa wakimsaidia.—Dan. 2:19-24; 10:12, 18, 19. w23.08 3 ¶5-6
Jumamosi, Aprili 5
Wenye kiasi wana hekima.—Met. 11:2.
Rebeka alikuwa mwanamke mwenye hekima, alifanya maamuzi kwa ujasiri, na katika maisha yake yote hakusita kuchukua hatua kwa njia inayofaa. (Mwa. 24:58; 27:5-17) Hata hivyo, alikuwa na heshima na ujitiisho. (Mwa. 24:17, 18, 65) Ikiwa kwa unyenyekevu utaunga mkono mipango ya Yehova kama alivyofanya Rebeka, utakuwa mfano mzuri katika familia yako na kutanikoni pia. Sifa ya kiasi ni sifa inayohitajika kwa Wakristo wote wakomavu. Esta alikuwa mwanamke mwaminifu mwenye sifa ya kiasi. Sifa ya kiasi ilimlinda asitende kwa kimbelembele. Alisikiliza ushauri wa binamu yake mwenye umri mkubwa, Mordekai, na aliufuata. (Esta 2:10, 20, 22) Unaweza kuonyesha sifa hiyo ya kiasi kwa kutafuta ushauri mzuri na kuutumia. (Tito 2:3-5) Esta alionyesha sifa ya kiasi katika njia nyingine. Alikuwa “mrembo na mwenye umbo zuri”; hata hivyo, hakutenda kwa njia iliyofanya wengine wamkazie fikira.—Esta 2:7, 15. w23.12 19-20 ¶6-8
Jumapili, Aprili 6
Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.—1 Yoh. 3:20.
Hatupaswi kuendelea kubeba uzito wa kuhisi hatia kupita kiasi. Ikiwa tuliungama dhambi yetu, tukatubu, na tunachukua hatua ili kuepuka kurudia dhambi hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ametusamehe. (Mdo. 3:19) Baada ya kuchukua hatua hizo, Yehova hangependa tuendelee kuhisi hatia. Anajua madhara yanayoweza kutokea ikiwa tutaendelea kuhisi hatia. (Zab. 31:10) Ikiwa tutalemewa na huzuni, huenda tukaacha kukimbia mbio za uzima. (2 Kor. 2:7) Ikiwa unaendelea kuhisi hatia kupita kiasi, kazia fikira “msamaha wa kweli” unaotoka kwa Mungu. (Zab. 130:4) Anapowasamehe wale wanaotubu kwa unyoofu, anaahidi hivi: “Sitaikumbuka tena dhambi yao.” (Yer. 31:34) Hilo linamaanisha kwamba baada ya hapo, Yehova hatakumbuka tena dhambi ulizofanya wakati uliopita. Usijikasirikie kwa sababu makosa yako ya zamani yanakuzuia kufanya mengi katika utumishi wa Yehova. Yehova haendelei kufikiria kuhusu dhambi zako, nawe hupaswi kufanya hivyo. w23.08 30-31 ¶14-15
Jumatatu, Aprili 7
Iweni imara, thabiti.—1 Kor. 15:58.
Wakati wa janga la COVID-19, Mashahidi wa Yehova waliosikiliza mwongozo kutoka kwenye tengenezo letu, waliepuka mahangaiko ambayo yaliwapata wale waliosikiliza habari za uwongo. (Mt. 24:45) Tunapaswa kuendelea kukazia fikira “mambo muhimu zaidi.” (Flp. 1:9, 10) Mambo yanayokengeusha fikira yanaweza kuchukua muda na nguvu zetu nyingi na hivyo tushindwe kufanya mambo yanayofaa. Mambo ya kawaida maishani—kama vile kula, kunywa, burudani, na kazi ya kimwili—yanaweza kutukengeusha fikira ikiwa tutayaona kuwa mambo muhimu zaidi maishani. (Luka 21:34, 35) Isitoshe, kila siku tunasikia habari kuhusu mizozo katika jamii na mijadala ya kisiasa. Hatupaswi kuruhusu mambo hayo yatukengeushe fikira. La sivyo, huenda tukaanza kuunga mkono upande fulani katika akili na moyo wetu. Shetani anatumia mbinu mbalimbali akiwa na lengo la kudhoofisha azimio letu la kufanya mambo yanayofaa. w23.07 16-17 ¶12-13
Jumanne, Aprili 8
Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka.—Luka 22:19.
Ukumbusho wa kifo cha Kristo ndiyo siku muhimu zaidi kwa watu wa Yehova. Ndilo tukio pekee ambalo Yesu aliagiza kihususa wafuasi wake waadhimishe. (Luka 22:19, 20) Linatukumbusha njia ambazo tunaweza kuonyesha shukrani zetu kwa ajili ya dhabihu ya Yesu. (2 Kor. 5:14, 15) Pia, linatupatia nafasi ya kufurahia “ubadilishanaji wa kitia moyo” pamoja na ndugu na dada zetu. (Rom. 1:12) Na watu wengi wanaopendezwa wamechochewa kuanza kufuata barabara ya uzima kwa sababu ya mambo waliyosikia na waliyojionea. Fikiria pia jinsi Ukumbusho unavyouunganisha undugu wetu wa ulimwenguni pote. Hivyo, haishangazi kwamba Ukumbusho ni siku ya pekee sana kwetu! w24.01 8 ¶1-3
Usomaji wa Biblia wa Ukumbusho: (Matukio ya mchana: Nisani 9) Luka 19:29-44
Jumatano, Aprili 9
Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.—Yoh. 3:16.
Kadiri tunavyotafakari gharama kubwa ambayo Yehova na Yesu walilipia, ndivyo tunavyoelewa zaidi jinsi wanavyompenda sana kila mmoja wetu. (Gal. 2:20) Fidia ni zawadi ya upendo. Yehova amethibitisha upendo wake kwetu kwa kutoa dhabihu yenye thamani zaidi kwake, yaani, Yesu. Yehova aliruhusu Mwana wake ateseke na kufa kwa ajili yetu. Yehova hafichi hisia zake, bali anatueleza waziwazi jinsi anavyotupenda sana. (Yer. 31:3) Yehova ametuvuta kwake kwa sababu anatupenda. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 7:7, 8) Hakuna kitu chochote wala mtu yeyote anayeweza kututenganisha na upendo wake. (Rom. 8:38, 39) Upendo huo unakufanya wewe uhisije? w24.01 28 ¶10-11
Usomaji wa Biblia wa Ukumbusho: (Matukio ya mchana: Nisani 10) Luka 19:45-48; Mathayo 21:18, 19; 21:12, 13
Alhamisi, Aprili 10
Kwa msingi wa tumaini . . . , uumbaji . . . utawekwa huru.—Rom. 8:20, 21.
Wakristo watiwa-mafuta wanalithamini sana tumaini lao la kwenda mbinguni. Mmoja wao ni Ndugu Frederick Franz, ambaye alisema hivi kutoka moyoni: “Tumaini letu ni jambo la hakika, na litatimizwa kikamili kwa kila mmoja wa wale washiriki 144,000 wa kundi dogo kwa kadiri inayopita hata yale ambayo tumeweza kuwazia.” Mwaka wa 1991, Ndugu Franz alisema hivi kwa uhakika: “Hatujapoteza maoni yetu ya thamani ya tumaini hilo. . . . Tunalithamini hata zaidi tunapozidi kulingojea. Ni jambo linalostahili kungojewa. Ninaliona tumaini letu kuwa lenye thamani kubwa zaidi kuliko wakati mwingine wowote.” Iwe tunatarajia kufurahia uzima wa milele mbinguni au duniani, tuna tumaini lenye utukufu linalotupa sababu ya kushangilia. Na tumaini letu lenye shangwe linaweza kuwa imara hata zaidi. w23.12 9 ¶6; 10 ¶8
Usomaji wa Biblia wa Ukumbusho: (Matukio ya mchana: Nisani 11) Luka 20:1-47
Ijumaa, Aprili 11
Damu ya ng’ombe dume na ya mbuzi haiwezi kuondoa dhambi.—Ebr. 10:4.
Nje ya mwingilio wa hema la ibada la kale kulikuwa na madhabahu ya shaba ambayo ilitumiwa kumtolea Yehova dhabihu za wanyama. (Kut. 27:1, 2; 40:29) Hata hivyo, dhabihu hizo hazingeandaa msamaha kamili kwa ajili ya dhambi za watu. (Ebr. 10:1-3) Mpango wa kutoa dhabihu za wanyama kwa kuendelea kwenye hema la ibada ulifananisha dhabihu moja ambayo ingewakomboa wanadamu kikamili. Yesu alijua kwamba Yehova alikuwa amemtuma duniani ili atoe uhai wake wa kibinadamu uwe dhabihu ya fidia kwa ajili ya wanadamu. (Mt. 20:28) Hivyo, wakati wa ubatizo wake, Yesu alijitoa mwenyewe ili kufanya mapenzi ya Yehova. (Yoh. 6:38; Gal. 1:4) Yesu alitoa uhai wake “mara moja kwa wakati wote” ili kutoa fidia au kufunika kabisa dhambi za kila mtu ambaye anaonyesha imani katika Kristo.—Ebr. 10:5-7, 10. w23.10 26-27 ¶10-11
Usomaji wa Biblia wa Ukumbusho: (Matukio ya mchana: Nisani 12) Luka 22:1-6; Marko 14:1, 2, 10, 11
TAREHE YA UKUMBUSHO
Baada ya Jua Kushuka
Jumamosi, Aprili 12
Zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.—Rom. 6:23.
Hatungeweza kujikomboa kutoka kwenye dhambi na kifo kwa uwezo wetu wenyewe. (Zab. 49:7, 8) Hivyo, Yehova alipanga Yesu atoe uhai wake kwa ajili yetu, jambo ambalo lilimgharimu sana yeye na Mwana wake mpendwa. Kadiri tunavyotafakari mambo ambayo Yehova na Yesu wamejidhabihu kwa ajili yetu, ndivyo tutakavyoithamini zaidi fidia. Adamu alipofanya dhambi, alipoteza tumaini lake la kuishi milele na pia la watoto wake wote. Ili kulipia kile ambacho Adamu alipoteza, Yesu alitoa uhai wake mkamilifu kuwa dhabihu. Wakati wa maisha yake yote akiwa duniani, Yesu “hakufanya dhambi wala udanganyifu haukupatikana kinywani mwake.” (1 Pet. 2:22) Wakati wa kifo cha Yesu, uhai wake mkamilifu ulilingana kabisa na uhai ambao Adamu alipoteza.—1 Kor. 15:45; 1 Tim. 2:6. w24.01 10 ¶5-6
Usomaji wa Biblia wa Ukumbusho: (Matukio ya mchana: Nisani 13) Luka 22:7-13; Marko 14:12-16 (Matukio ya baada ya jua kushuka: Nisani 14) Luka 22:14-65
Jumapili, Aprili 13
liingia mahali patakatifu, si kwa damu ya mbuzi na ya ng’ombe dume wachanga, bali kwa damu yake mwenyewe, mara moja kwa wakati wote, na kupata ukombozi wa milele kwa ajili yetu.—Ebr. 9:12.
Baada ya kufufuliwa Yesu aliingia Patakatifu zaidi pa hekalu la kiroho. Basi, tunaona mpango bora wa Yehova wa ibada unaotegemea fidia ya dhabihu na ukuhani wa Yesu Kristo. Kuhani mkuu wa Israeli aliingia katika Patakatifu Zaidi palipotengenezwa na wanadamu, akiwa na damu ya dhabihu za wanyama, lakini Yesu “aliingia mbinguni kwenyewe,” mahali patakatifu zaidi, ili kuwa mbele za Yehova. Akiwa huko, alitoa thamani ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kwa ajili yetu “ili kuondoa dhambi kupitia dhabihu yake mwenyewe.” (Ebr. 9:24-26) Iwe tuna tumaini la kwenda mbinguni au kuishi duniani, sote tunaweza kumwabudu Yehova katika hekalu lake la kiroho. w23.10 28 ¶13-14
Usomaji wa Biblia wa Ukumbusho: (Matukio ya mchana: Nisani 14) Luka 22:66-71
Jumatatu, Aprili 14
Basi na tukikaribie kiti cha ufalme cha fadhili zisizostahiliwa tukiwa na uhuru wa kusema.—Ebr. 4:16.
Fikiria kuhusu jukumu la Yesu akiwa Mfalme wetu anayetawala mbinguni na Kuhani Mkuu mwenye huruma. Kupitia kwake, tunaweza kukikaribia ‘kiti cha Ufalme cha Mungu cha fadhili zisizostahiliwa’ katika sala na kumwomba rehema na msaada kwa “wakati unaofaa.” (Ebr. 4:14, 15) Acheni kila siku tuendelee kutafakari kuhusu mambo ambayo Yehova na Yesu wametufanyia na yale ambayo wanatufanyia. Upendo wao kwetu unapaswa kugusa kabisa mioyo yetu na kutuchochea kuwa wenye bidii katika utumishi na ibada yetu. (2 Kor. 5:14, 15) Mojawapo ya njia bora zaidi ya kuonyesha kwamba tunashukuru ni kuwasaidia wengine wawe Mashahidi wa Yehova na wanafunzi wa Yesu. (Mt. 28:19, 20) Hivyo ndivyo mtume Paulo alivyofanya. Alijua mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Tim. 2:3, 4. w23.10 22-23 ¶13-14
Usomaji wa Biblia wa Ukumbusho: (Matukio ya mchana: Nisani 15) Mathayo 27:62-66
Jumanne, Aprili 15
Kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.—Ufu. 21:4.
Sisi hutumia ujumbe huo wa Biblia unaogusa moyo, tunapowahubiria wengine kuhusu maisha katika Paradiso. Tunawezaje kuwahakikishia wengine—na sisi wenyewe—kwamba baraka zinazotajwa katika Ufunuo 21:3, 4 zitatimia? Yehova hakutoa tu ahadi hiyo inayogusa moyo, bali pia alitoa sababu zinazotuhakikishia kwamba atatimiza ahadi hiyo. Mistari inayofuata katika Ufunuo sura ya 21 inaonyesha sababu za kutumaini ahadi ya Yehova ya Paradiso. Mistari hiyo inasema hivi: “Yule aliyeketi kwenye kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’ Pia anasema: ‘Andika, kwa maana maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.’ Naye akaniambia: ‘Yametimia! Mimi ndiye Alfa na Omega, mwanzo na mwisho.’”—Ufu. 21:5, 6a. w23.11 3 ¶3-5
Usomaji wa Biblia wa Ukumbusho: (Matukio ya mchana: Nisani 16) Luka 24:1-12
Jumatano, Aprili 16
Endelea kuwahimiza wanaume vijana wawe na utimamu wa akili.—Tito 2:6.
Mwanamume kijana huonyesha kwamba amesitawisha uwezo wa kufikiri kwa kufanya maamuzi mazuri kuhusu mavazi na mapambo. Mara nyingi, mitindo inayopendwa ya mavazi imebuniwa na kutangazwa na watu ambao hawamheshimu Yehova au wanaoishi maisha yasiyo na maadili. Njia yao ya kufikiri iliyopotoka kimaadili inaonekana kupitia mitindo ya mavazi yanayobana sana au yanayofanya mwanamume aonekane kama mwanamke. Anapochagua mavazi, mwanamume kijana anayetaka kuwa Mkristo mkomavu ataongozwa na kanuni za Biblia na mifano mizuri kutanikoni. Anaweza kujiuliza hivi: ‘Je, maamuzi yangu yanaonyesha kwamba nina utimamu wa akili na ninawafikiria wengine? Je, jinsi ninavyovalia inafanya iwe rahisi kwa wengine kuamini kwamba mimi ni mtumishi wa Mungu mwenye bidii?’ (1 Kor. 10:31-33) Mwanamume kijana mwenye uwezo wa kufikiri ataheshimiwa, si na ndugu na dada tu, bali pia na Baba yake wa mbinguni. w23.12 26 ¶7
Alhamisi, Aprili 17
Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama Ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangenipigania.—Yoh. 18:36.
Wakati uliopita “mfalme wa kusini” aliwashambulia moja kwa moja watu wa Yehova. (Dan. 11:40) Kwa mfano, katika miaka 50 ya kwanza ya karne ya 20, ndugu wengi walifungwa gerezani kwa sababu ya msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote na baadhi ya watoto wa Mashahidi walifukuzwa shuleni kwa sababu hiyohiyo. Hata hivyo, katika miaka ya hivi karibuni, watumishi wa Yehova wanaoishi chini ya utawala wa mfalme huyo wamekabili mashambulizi yasiyo ya moja kwa moja kuelekea ushikamanifu wao kwa Ufalme wa Mungu. Kwa mfano, wakati wa kampeni za uchaguzi, huenda Mkristo akashawishiwa kuunga mkono chama fulani cha kisiasa au mgombeaji fulani. Huenda Mkristo asifikie hatua ya kupiga kura; lakini katika akili na moyo wake anaweza kuunga mkono upande fulani. Ni jambo muhimu kwamba tuendelee kutounga mkono upande wowote kisiasa, si kwa matendo tu, bali pia katika mawazo na hisia zetu!—Yoh. 15:18, 19. w23.08 12 ¶17
Ijumaa, Aprili 18
Na asifiwe Yehova, anayetubebea mzigo wetu kila siku.—Zab. 68:19.
Tukiwa wakimbiaji katika mbio za uzima, tunapaswa ‘kukimbia kwa njia itakayotuwezesha kushinda tuzo.’ (1 Kor. 9:24) Yesu alisema kwamba tunaweza ‘kulemewa na kula na kunywa kupita kiasi na mahangaiko ya maisha.’ (Luka 21:34) Andiko hilo na maandiko mengine, yanaweza kukusaidia utambue mabadiliko ambayo huenda unahitaji kufanya unapokimbia katika mbio za uzima. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutashinda mbio za uzima kwa sababu Yehova atatupatia nguvu tunazohitaji. (Isa. 40:29-31) Kwa hiyo, usipunguze mwendo! Mwige mtume Paulo ambaye alijitahidi kabisa kupata tuzo iliyokuwa mbele yake. (Flp. 3:13, 14) Hakuna mtu anayeweza kukimbia mbio hizo kwa ajili yako, lakini kwa msaada wa Yehova unaweza kufanikiwa. Yehova anaweza kukusaidia ubebe majukumu yako na kuondoa uzito usio wa lazima. Yehova akiwa upande wako, utafaulu kukimbia katika mbio kwa uvumilivu na kushinda! w23.08 31 ¶16-17
Jumamosi, Aprili 19
Mheshimu baba yako na mama yako.—Kut. 20:12.
Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, alibaki Yerusalemu wazazi wake walipoondoka kurudi nyumbani. (Luka 2:46-52) Yosefu na Maria walikuwa na jukumu la kuhakikisha kwamba watoto wao wote walikuwa miongoni mwa kikundi kilichokuwa kikisafiri kurudi nyumbani baada ya sherehe. Hatimaye, Yosefu na Maria walipompata Yesu, Maria alimlaumu Yesu kwa sababu ya usumbufu aliowasababishia! Huenda Yesu angesema kwamba hawakumtendea kwa haki. Badala yake, aliwajibu wazazi wake kwa maneno machache yenye heshima. Hata hivyo, Yosefu na Maria “hawakuelewa mambo aliyokuwa akiwaambia.” Ingawa hivyo, Yesu ‘aliendelea kuwatii.’ Vijana, je, wakati mwingine ni vigumu kwenu kuwatii wazazi wenu wanapofanya makosa au wanapokosa kuwaelewa? Ni nini kinachoweza kuwasaidia? Fikiria jinsi Yehova anavyohisi. Biblia inasema kwamba mnapowatii wazazi wenu, “hilo humpendeza Bwana.” (Kol. 3:20) Yehova anajua kwamba wakati fulani wazazi wenu wanakosa kuwaelewa au wanaweka sheria ambazo si rahisi kutii. Lakini mnapoamua kuwatii licha ya hali hizo, mnamfurahisha Yehova. w23.10 7 ¶5-6
Jumapili, Aprili 20
Wawe na usawaziko, wakionyesha upole wote kwa watu wote.—Tito 3:2.
Huenda mwanafunzi mwenzetu akasisitiza kwamba Mashahidi wa Yehova wanapaswa kubadili maoni yao kuhusu ngono za watu wa jinsia moja. Huenda tukahitaji kumhakikishia kwamba kwa heshima tunatambua kwamba kila mtu ana haki ya kujifanyia maamuzi. (1 Pet. 2:17) Kisha huenda tukapata nafasi ya kumwambia kuhusu manufaa ya kufuata viwango vya maadili vya Biblia. Tunapozungumza na mtu anayetupinga kwa uthabiti, hatupaswi kufikia mkataa haraka kwamba tunajua mambo anayoamini. Kwa mfano, namna gani ikiwa mwanafunzi mwenzako anakudhihaki kwa sababu unaamini kuna Mungu? Je, unapaswa kufikiri kwamba anaamini kabisa fundisho la mageuzi na anajua mengi kulihusu? Ukweli ni kwamba huenda anarudia kusema mambo ambayo amesikia. Labda unaweza kumwonyesha habari kuhusu uumbaji zinazopatikana kwenye jw.org. Baadaye, huenda akawa tayari kuzungumzia makala au video iliyo kwenye tovuti hiyo. Naam, kujibu kwa heshima kunaweza kumsaidia abadili maoni yake. w23.09 17 ¶12-13
Jumatatu, Aprili 21
Wewe, Ee Yehova, ni mwema na uko tayari kusamehe;una upendo mwingi mshikamanifu kwa wote wanaokuitia.—Zab. 86:5.
Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ataturuhusu tumtumikie na atatubariki, hata iwe tulifanya makosa, ikiwa tu tumefanya yote tunayoweza kurekebisha mwenendo wetu na kuendelea kumtegemea. (Met. 28:13) Samsoni alikuwa mwanadamu asiye mkamilifu; ingawa hivyo, hakuacha kujitahidi kumtumikia Yehova hata alipofanya kosa kuhusiana na Delila. Na Yehova aliendelea kumtumia Samsoni. Mungu alimtumia tena Samsoni kwa njia kubwa sana. Bado Yehova alimwona kuwa mwanamume mwenye imani ya pekee, na kumtaja kwenye orodha ya watumishi waaminifu inayopatikana kwenye Waebrania sura ya 11. Inatia moyo kujua kwamba tunamtumikia Baba wa mbinguni mwenye upendo ambaye anatamani kutuimarisha hasa tunapokuwa dhaifu! Basi kama Samsoni, acheni tumsihi hivi Yehova: “Nikumbuke, tafadhali, na kunitia nguvu.”—Amu. 16:28. w23.09 7 ¶18-19
Jumanne, Aprili 22
[Weka] karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.—2 Pet. 3:12.
Tunapoweka karibu akilini siku ya Yehova, tunachochewa kuwahubiria wengine habari njema. Hata hivyo, huenda wakati mwingine tukasita kufanya hivyo. Kwa nini? Huenda pindi fulani tukalemewa na woga wa wanadamu. Petro alipatwa na jambo hilo. Usiku ambao kesi ya Yesu ilifanywa, Petro aliogopa kujitambulisha kuwa mmoja wa wanafunzi wa Yesu na akakana mara kadhaa kwamba hamjui Yesu. (Mt. 26:69-75) Hata hivyo, baadaye, mtume huyo alisema hivi kwa usadikisho: “Msiogope kile wanachokiogopa, wala msiwe na wasiwasi.” (1 Pet. 3:14) Maneno ya Petro yanatuhakikishia kwamba tunaweza kushinda woga wa wanadamu. Ni nini kinachoweza kutusaidia kushinda woga wa wanadamu? Petro anatuambia hivi: “Mtakaseni Kristo kuwa Bwana katika mioyo yenu.” (1 Pet. 3:15) Hilo linatia ndani kutafakari cheo na mamlaka ya Bwana na Mfalme wetu, Kristo Yesu. w23.09 27-28 ¶6-8
Jumatano, Aprili 23
Uasherati na kila namna ya ukosefu wa usafi . . . visitajwe kamwe miongoni mwenu.—Efe. 5:3.
Ni lazima tuendelee kupambana ili tusinaswe “katika matendo yasiyozaa matunda, ambayo ni ya giza.” (Efe. 5:11) Visa mbalimbali vinaonyesha kuwa kadiri mtu anavyotazama, kusikiliza, au kuzungumza kuhusu mambo machafu na mapotovu kiadili, ndivyo inavyokuwa rahisi zaidi kwake kufanya dhambi. (Mwa. 3:6; Yak. 1:14, 15) Ulimwengu wa Shetani unajaribu kutudanganya na kutufanya tuamini kwamba mambo ambayo Yehova anayaona kuwa machafu na mapotovu si mabaya. (2 Pet. 2:19) Mbinu moja ambayo Ibilisi ameitumia kwa muda mrefu ni kuwachanganya watu ili wasitambue mambo yaliyo sawa na yasiyo sawa. (Isa. 5:20; 2 Kor. 4:4) Haishangazi kwamba sinema nyingi, vipindi vya televisheni, na tovuti zinaendeleza mawazo yaliyo kinyume na viwango vya uadilifu vya Yehova! Shetani anajaribu kutudanganya tufikiri kwamba matendo na mwenendo mchafu hauna madhara.—Efe. 5:6. w24.03 22 ¶8-10
Alhamisi, Aprili 24
Watu hao hufanya utumishi mtakatifu kwa mfano wa uhalisi na kivuli cha vitu vya mbinguni.—Ebr. 8:5.
Mwanzoni, Waisraeli walibeba hema la ibada walipoondoka sehemu moja kwenda nyingine. Walilitumia kwa karibu miaka 500 hadi hekalu la kudumu lilipojengwa huko Yerusalemu. (Kut. 25:8, 9; Hes. 9:22) Hema hilo la ibada lilikuwa kituo ambacho Waisraeli wangetoa dhabihu zao na kufanya ibada. (Kut. 29:43-46) Hata hivyo, hema la ibada liliwakilisha jambo bora zaidi. Lilikuwa “kivuli cha vitu vya mbinguni,” na lilifananisha hekalu kubwa la kiroho la Yehova. Mtume Paulo alisema kwamba “hema hili ni mfano kwa ajili ya wakati huu.” (Ebr. 9:9) Basi, wakati alipowaandikia Waebrania barua, tayari hekalu la kiroho lilikuwa jambo halisi kwa Wakristo. Hekalu hilo lilianzishwa mwaka wa 29 W.K. Mwaka huo, Yesu alibatizwa na akaanza kutumikia akiwa “kuhani mkuu sana” wa Yehova katika hekalu la kiroho.—Ebr. 4:14; Mdo. 10:37, 38. w23.10 25-26 ¶6-7
Ijumaa, Aprili 25
Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.—Flp. 4:5.
Ili kusitawi kiroho, Wakristo wanapaswa kuwa na uwezo wa kunyumbulika, tayari kujipinda. Jinsi gani? Tunapaswa kuwa wenye usawaziko kwa kunyumbulika hali zetu za kibinafsi zinapobadilika na kwa kuheshimu maoni na maamuzi ya wengine. Tukiwa watumishi wa Yehova, tunapaswa kuwa wenye usawaziko. Pia, tunapaswa kuwa wanyenyekevu na wenye huruma. Yehova anaitwa “Mwamba” kwa sababu yuko thabiti na imara. (Kum. 32:4) Hata hivyo, pia ni mwenye usawaziko. Mambo yanapobadilika ulimwenguni, Mungu wetu anaendelea kunyumbulika ili kufanya kusudi lake litimie. Yehova aliwaumba wanadamu kwa mfano wake wakiwa na uwezo wa kunyumbulika hali zinapobadilika. Alituandalia kanuni zilizo wazi katika Biblia ambazo zinatusaidia kufanya maamuzi yenye hekima hata tukabili changamoto gani maishani. Mfano ambao Yehova ameweka na kanuni ambazo ametupatia zinathibitisha kwamba ingawa yeye ni “Mwamba,” pia Yehova ni mwenye usawaziko. w23.07 20 ¶1-3
Jumamosi, Aprili 26
Mahangaiko yaliponilemea, ulinifariji na kunibembeleza.—Zab. 94:19.
Katika Biblia, Yehova anajifananisha na mama mwenye upendo. (Isa. 66:12, 13) Wazia mama anayemtunza kwa upendo mtoto wake mchanga na anahakikisha kwamba anapata anachohitaji. Tunapokuwa na maumivu, tunaweza kuwa na uhakika katika upendo wa Yehova. Hataacha kutupenda tunapofanya jambo fulani baya. (Zab. 103:8) Waisraeli walimkatisha tamaa Yehova tena na tena; hata hivyo, alieleza kuhusu upendo wake mshikamanifu kwa watu wake waliotubu alipowaambia hivi: “Ulikuwa mwenye thamani machoni pangu, uliheshimiwa, nami nimekupenda.” (Isa. 43:4, 5) Upendo wa Mungu haujabadilika. Hata ikiwa tumefanya makosa mazito, tukitubu na kumrudia Yehova, tutajionea kwamba bado anatupenda. Anaahidi kwamba “atasamehe kwa njia kubwa.” (Isa. 55:7) Biblia inasema kwamba msamaha huo ni kama “majira yenye kuburudisha . . . kutoka kwa Yehova mwenyewe.”—Mdo. 3:19. w24.01 27 ¶4-5
Jumapili, Aprili 27
Mkono wa Yehova Mungu ulikuwa juu yangu.—Ezra 7:28.
Yehova anaweza kutusaidia tunapokabili hali ngumu. Kwa mfano, tunapomwomba mwajiri wetu ruhusa ya kuhudhuria kusanyiko au tunapomwomba arekebishe ratiba ya kazi ili tuweze kuhudhuria mikutano yote, tunatengeneza fursa ya kujionea mkono wa Yehova katika maisha yetu. Huenda tukashangazwa sana na matokeo mazuri tutakayopata. Jambo hilo, litaimarisha uhakika wetu katika Yehova. Kwa unyenyekevu, Ezra aliomba msaada wa Yehova. Ezra alisali kwa unyenyekevu kwa Yehova kila mara alipohisi amelemewa na majukumu yake. (Ezra 8:21-23; 9:3-5) Kwa kuwa Ezra alimtegemea Yehova, wengine walikuwa tayari kumtegemeza na kuiga imani yake. (Ezra 10:1-4) Tunapolemewa na mahangaiko kuhusu mahitaji yetu ya kimwili au usalama wa familia yetu, tunapaswa kusali kwa Yehova tukiwa na uhakika. w23.11 18 ¶15-17
Jumatatu, Aprili 28
[Abrahamu] akawa na imani katika Yehova, Naye akamhesabu kuwa mwadilifu.—Mwa. 15:6.
Yehova hasemi kwamba ikiwa tunataka kutangazwa kuwa waadilifu ni lazima tufanye mambo yaleyale ambayo Abrahamu alifanya. Kwa kweli, kuna njia nyingi ambazo tunaweza kuonyesha imani kwa matendo yetu. Tunaweza kuwakaribisha wapya kutanikoni, kuwasaidia ndugu na dada ambao kwa kweli wana uhitaji, na kuwafanyia mema watu wa familia yetu; mambo hayo yote Mungu atayakubali na kuyabariki. (Rom. 15:7; 1 Tim. 5:4, 8; 1 Yoh. 3:18) Kuhubiri kwa bidii habari njema ni mojawapo ya matendo mema muhimu zaidi yanayoonyesha kwamba tuna imani. (1 Tim. 4:16) Sisi sote tunaweza kuonyesha kwa matendo yetu kuwa tuna imani kwamba ahadi za Yehova zitatimia na kwamba njia zake ni bora. Na tukifanya hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba Mungu atatuona kuwa waadilifu, na atatuita rafiki zake. w23.12 2 ¶3; 6 ¶15
Jumanne, Aprili 29
Uwe imara na ujithibitishe kuwa mwanamume.—1 Fal. 2:2.
Alipokuwa anakaribia kufa, Mfalme Daudi alimwambia Sulemani maneno yanayopatikana katika andiko la leo. (1 Fal. 2:1, 3) Ushauri huo ni muhimu kwa wanaume wote Wakristo leo. Ili wafanikiwe, ni lazima wajifunze kutii sheria za Mungu na kutumia kanuni za Biblia katika kila sehemu ya maisha yao. (Luka 2:52) Kwa nini ni muhimu sana kwa ndugu vijana kuwa wanaume Wakristo wakomavu? Mwanamume Mkristo anatimiza majukumu muhimu katika familia na kutanikoni. Bila shaka, ninyi ndugu vijana mmefikiria kuhusu majukumu mnayoweza kuwa nayo wakati ujao. Huenda una lengo la kuwa mtumishi wa wakati wote, mtumishi wa huduma, na baadaye mzee wa kutaniko. Pia, huenda ukataka kufunga ndoa na kuwa na watoto. (Efe. 6:4; 1 Tim. 3:1) Ili ufikie malengo hayo na kufanikiwa, unahitaji kuwa Mkristo mkomavu. w23.12 24 ¶1-2
Jumatano, Aprili 30
Nitakosa wakati nikiendelea kusimulia kuhusu Gideoni.—Ebr. 11:32.
Wazee Wakristo wamepewa jukumu la kuwatunza kondoo wenye thamani wa Yehova. Wanaume hao wenye bidii wanathamini pendeleo lao la kuwatumikia ndugu na dada zao, na wanajitahidi sana kuwa ‘wachungaji ambao kwa kweli wanawachunga’ kondoo. (Yer. 23:4; 1 Pet. 5:2) Tunashukuru sana kuwa na wanaume kama hao kutanikoni! Wazee wanaweza kujifunza kutokana na mfano wa Mwamuzi Gideoni. (Ebr. 6:12) Aliwalinda na kuwachunga watu wa Mungu. (Amu. 2:16; 1 Nya. 17:6) Kama Gideoni, wazee wamechaguliwa ili kuwatunza watu wa Mungu katika kipindi hiki kigumu. (Mdo. 20:28; 2 Tim. 3:1) Tunaweza kujifunza kutokana na jinsi Gideoni alivyokuwa na sifa ya kiasi, unyenyekevu, na utii. Uvumilivu wake ulijaribiwa alipokuwa akitimiza migawo yake. Iwe sisi ni wazee wa kutaniko au la, tunaweza kuwathamini wazee wetu hata zaidi. Tunaweza kuwaunga mkono wanaume hao wanaofanya kazi kwa bidii.—Ebr. 13:17. w23.06 2 ¶1; 3 ¶3