Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • es25 kur. 26-36
  • Machi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Machi
  • Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025
  • Vichwa vidogo
  • Jumamosi, Machi 1
  • Jumapili, Machi 2
  • Jumatatu, Machi 3
  • Jumanne, Machi 4
  • Jumatano, Machi 5
  • Alhamisi, Machi 6
  • Ijumaa, Machi 7
  • Jumamosi, Machi 8
  • Jumapili, Machi 9
  • Jumatatu, Machi 10
  • Jumanne, Machi 11
  • Jumatano, Machi 12
  • Alhamisi, Machi 13
  • Ijumaa, Machi 14
  • Jumamosi, Machi 15
  • Jumapili, Machi 16
  • Jumatatu, Machi 17
  • Jumanne, Machi 18
  • Jumatano, Machi 19
  • Alhamisi, Machi 20
  • Ijumaa, Machi 21
  • Jumamosi, Machi 22
  • Jumapili, Machi 23
  • Jumatatu, Machi 24
  • Jumanne, Machi 25
  • Jumatano, Machi 26
  • Alhamisi, Machi 27
  • Ijumaa, Machi 28
  • Jumamosi, Machi 29
  • Jumapili, Machi 30
  • Jumatatu, Machi 31
Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025
es25 kur. 26-36

Machi

Jumamosi, Machi 1

Tumaini halikatishi tamaa.—Rom. 5:5.

Bado ulimwengu mpya haujafika. Hata hivyo, fikiria baadhi ya mambo tunayoona—nyota, miti, wanyama, na wanadamu wenzetu. Hakuna mtu anayeweza kutilia shaka kwamba vitu hivyo ni halisi hata ingawa kuna wakati ambapo havikuwepo. Vipo sasa kwa sababu tu Yehova aliviumba. (Mwa. 1:​1, 26, 27) Pia, Mungu wetu ameahidi kwamba ataleta ulimwengu mpya. Atatimiza ahadi hiyo. Katika ulimwengu mpya, watu watafurahia kuishi milele wakiwa na afya kamilifu. Wakati ambao Mungu ameweka utakapofika, ulimwengu mpya utakuwa halisi kama ulimwengu tunaouona leo. (Isa. 65:17; Ufu. 21:​3, 4) Kwa wakati huu, fanya yote unayoweza ili kuimarisha imani yako. Sitawisha uthamini kuelekea fidia. Tafakari kuhusu nguvu za Yehova. Shiriki katika utendaji mbalimbali wa kiroho. Ukifanya hivyo, unaweza kuwa kati ya “wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.”—Ebr. 6:​11, 12. w23.04 31 ¶18-19.

Jumapili, Machi 2

Je, sikukuambia kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu?—Yoh. 11:40.

Yesu akatazama mbinguni na kusali hadharani. Alitaka kumpa Yehova utukufu kwa jambo ambalo lingefuata. Yesu akaita hivi kwa sauti kubwa: “Lazaro, njoo huku nje!” (Yoh. 11:43) Na Lazaro akatoka kwenye kaburi! Yesu alifanya jambo ambalo wengine walifikiri haliwezekani. Simulizi hilo linaimarisha imani yetu katika tumaini la ufufuo. Jinsi gani? Kumbuka ahadi ambayo Yesu alimpa Martha: “Ndugu yako atafufuka.” (Yoh. 11:23) Kama Baba yake, Yesu anatamani na ana nguvu za kutimiza ahadi hiyo. Machozi yake yanafunua kwamba anatamani sana kuondoa kifo na huzuni inayosababishwa na kifo. Na Lazaro alipotoka kwenye kaburi, Yesu alithibitisha kwamba ana nguvu za kuwafufua wafu. Pia, fikiria jambo ambalo Yesu alimkumbusha Martha katika andiko la leo. Tuna sababu nzuri za kuamini kwamba ahadi ya Mungu ya ufufuo itatimia. w23.04 11-12 ¶15-16

Jumatatu, Machi 3

Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia, wote wanaomwitia yeye katika ukweli.—Zab. 145:18.

Huenda tukahitaji kubadili jambo tunaloomba katika sala tunapotambua waziwazi zaidi mapenzi ya Yehova. Tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova ana kusudi, na atalitimiza kulingana na ratiba yake aliyoweka. Kusudi hilo linatia ndani kuondoa kabisa matatizo yote yanayosababisha mateso mengi leo—matatizo kama vile misiba ya asili, magonjwa, na kifo. Yehova atatimiza kusudi lake kupitia Ufalme wake. (Dan. 2:44; Ufu. 21:​3, 4) Hata hivyo, kabla ya wakati huo kufika, Yehova amemruhusu Shetani atawale ulimwengu huu. (Yoh. 12:31; Ufu. 12:9) Ikiwa Yehova angetatua matatizo ya wanadamu sasa, huenda ingeonekana kwamba utawala wa Shetani una mafanikio. Basi, ingawa tunalazimika kusubiri hadi Yehova atimize baadhi ya ahadi, hilo halimaanishi kwamba ametuacha bila msaada. Yehova atatusaidia. w23.05 8 ¶4; 9-10 ¶7-8

Jumanne, Machi 4

Mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.—Kol. 4:6.

Tunaweza kuwasaidiaje wengine wanufaike na Ukumbusho? Bila shaka, hatua ya kwanza ni kwa kuwaalika. Zaidi ya kuwaalika wale tunaokutana nao katika huduma kwa ukawaida, tunaweza kuandika orodha ya watu tutakaowaalika. Orodha hiyo inaweza kutia ndani watu wetu wa ukoo, wafanyakazi wenzetu, wanafunzi wenzetu, na watu wengine tunaowajua. Hata ikiwa hatuna mialiko ya kutosha iliyochapishwa, tunaweza kuwatumia kiunganishi cha mwaliko wa kielektroni. Huenda tukashangaa kuona jinsi watu wengi watakavyoitikia vizuri! (Mhu. 11:6.) Kumbuka kwamba wale tunaowaalika wanaweza kuwa na maswali—hasa ikiwa hawakuwahi kuhudhuria mikutano yetu. Itafaa kufikiria mapema maswali watakayouliza na kutayarisha majibu. Hata baada ya kuhudhuria Ukumbusho, inawezekana wapya wakawa na maswali ya ziada. Tungependa kufanya yote tuwezayo—kabla, wakati, na baada ya Ukumbusho—ili kuwasaidia wale “walio na mwelekeo unaofaa” wanufaike na mwadhimisho huo.—Mdo. 13:48. w24.01 12 ¶13, 15; 13 ¶16

Jumatano, Machi 5

Ninyi ni ukungu unaotokea kwa muda kidogo na kisha kutoweka.—Yak. 4:14.

Katika Biblia kuna masimulizi ya watu wanane waliofufuliwa. Kwa nini usichunguze kwa makini kila simulizi? Unapofanya hivyo, tafuta masomo unayoweza kujifunza. Fikiria jinsi kila mfano unavyoonyesha kwamba Mungu anatamani na ana nguvu za kuwafufua wafu. Zaidi ya yote, tafakari kuhusu ufufuo muhimu zaidi—ufufuo wa Yesu. Kumbuka kwamba ufufuo wake ulithibitishwa na mamia ya watu na unatupatia msingi thabiti wa imani yetu. (1 Kor. 15:​3-6, 20-22) Tunamshukuru sana Yehova kwa ahadi ya ufufuo. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba ahadi hiyo itatimizwa, kwa kuwa Yehova anatamani na ana nguvu za kuitimiza. Acheni tuendelee kuimarisha imani yetu katika tumaini hilo lenye thamani. Tukifanya hivyo, tutaendelea kumkaribia zaidi Mungu ambaye ni kana kwamba anamwahidi kila mmoja wetu hivi, ‘Wapendwa wako watafufuka!’—Yoh. 11:23. w23.04 8 ¶2; 12 ¶17; 13 ¶20

Alhamisi, Machi 6

Utembee kwa kiasi na Mungu wako!—Mika 6:8.

Kuna ulinganifu mkubwa kati ya sifa ya kiasi na unyenyekevu. Tunaonyesha kwamba tuna sifa ya kiasi kwa kuwa na maoni yanayofaa kujihusu sisi wenyewe na mambo tunayoweza kufanya. Tunaonyesha kwamba tuna sifa ya unyenyekevu kwa kuwaheshimu wengine na kuwaona kuwa bora kuliko sisi. (Flp. 2:3) Kwa kawaida, mtu mwenye kiasi ni mnyenyekevu pia. Gideoni alikuwa mwanamume mwenye kiasi na mnyenyekevu. Malaika wa Yehova alipomwambia Gideoni kwamba alikuwa amechaguliwa kuwakomboa Waisraeli kutoka kwa Wamidiani wenye nguvu, mwanamume huyo mnyenyekevu alijibu hivi: “Ukoo wangu ndio mdogo zaidi katika kabila la Manase, nami ni mdogo kabisa katika nyumba ya baba yangu.” (Amu. 6:15) Alihisi kwamba hawezi kutimiza mgawo huo, lakini Yehova alijua kwamba angeweza. Kwa msaada wa Yehova, Gideoni alifanikiwa kutimiza mgawo wake. Wazee hujitahidi sana kuonyesha sifa ya kiasi na unyenyekevu katika mambo yote. (Mdo. 20:​18, 19) Wazee hawajigambi kuhusu uwezo wao au mambo waliyotimiza; wala hawahisi kwamba hawafai kwa sababu ya udhaifu au makosa yao. w23.06 3 ¶4-5

Ijumaa, Machi 7

Yeye atakuponda kichwa.—Mwa. 3:15.

Kupondwa kwa kichwa cha Shetani, kutatokea baada ya zaidi ya miaka 1,000 ijayo. (Ufu. 20:​7-10) Kabla ya hilo kutukia, Biblia inatabiri kwamba matukio haya ya kustaajabisha yatatokea. Kwanza, mataifa yatatoa tangazo la “amani na usalama!” (1 The. 5:​2, 3) Kisha “ghafla” dhiki kuu itaanza, mataifa yatakaposhambulia dini zote za uwongo. (Ufu. 17:16) Baada ya hapo, Yesu atawahukumu wanadamu, akitenganisha kondoo na mbuzi. (Mt. 25:​31-33, 46) Hata hivyo, bado Shetani ataendelea kumpinga Yehova. Akiongozwa na chuki, atachochea muungano wa mataifa ambao Biblia inauita Gogu wa nchi ya Magogu ili kuwashambulia waabudu wa kweli wa Yehova. (Eze. 38:​2, 10, 11) Kufikia pindi fulani, watiwa-mafuta waliobaki duniani watakusanywa na kwenda mbinguni ili wajiunge na Kristo na jeshi lake la mbinguni kupigana vita vya Har–​Magedoni, sehemu ya mwisho ya ile dhiki kuu. (Mt. 24:31; Ufu. 16:​14, 16) Kisha Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo juu ya dunia utaanza.—Ufu. 20:6. w23.10 20-21 ¶9-10

Jumamosi, Machi 8

Mtumishi wako nimemwogopa Yehova tangu nilipokuwa kijana.—1 Fal. 18:12.

Leo, watumishi wengi wa Yehova wanaishi katika nchi ambazo kazi yetu imepigwa marufuku. Wanawaonyesha heshima wenye mamlaka, lakini kama Obadia, ndugu na dada hao wapendwa wanampa Yehova kile anachostahili kupokea, yaani, ibada ya pekee. (Mt. 22:21) Wanaonyesha wanamwogopa Mungu kwa kumtii yeye badala ya wanadamu. (Mdo. 5:29) Wanafanya hivyo kwa kuendelea kuhubiri habari njema na kukutana pamoja kisiri. (Mt. 10:​16, 28) Wanajitahidi kuhakikisha kwamba ndugu na dada zao wanapata chakula cha kiroho wanachohitaji. Fikiria kisa cha Henri, ambaye anaishi katika nchi moja barani Afrika ambako kazi yetu ilipigwa marufuku kwa muda fulani. Wakati wa marufuku, Henri alijitolea kusambaza machapisho kwa Mashahidi wenzake. Aliandika hivi: “Kwa kawaida, mimi ni mwenye haya. . . . Yehova . . . alinipa ujasiri niliohitaji.” Je, wewe unaweza kuwa na ujasiri kama wa Henri? Unaweza ikiwa utasitawisha woga unaofaa kumwelekea Mungu. w23.06 16 ¶9, 11

Jumapili, Machi 9

Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu.—Rom. 5:12.

Adamu na Hawa walipoasi, huenda ilionekana kwamba Shetani alizuia kusudi la Mungu la kuijaza dunia wanadamu wakamilifu na watiifu. Huenda Shetani alifikiri kwamba Yehova amebaki na njia chache za kushughulikia jambo hilo. Njia moja ilikuwa kuwaua Adamu na Hawa na kuwaumba wenzi wa ndoa wengine wakamilifu ili watimize kusudi Lake kwa ajili ya wanadamu. Lakini ikiwa Mungu angefanya hivyo, Ibilisi angedai kwamba Mungu ni mwongo. Kwa nini? Kwa sababu, kama ilivyoandikwa kwenye Mwanzo 1:​28, Yehova aliwaambia Adamu na Hawa kwamba wazao wao wangeijaza dunia. Au inawezekana Shetani alifikiri kwamba Yehova angewaruhusu Adamu na Hawa wazae watoto wasio wakamilifu ambao hawangeweza kamwe kuufikia ukamilifu. (Mhu. 7:20; Rom. 3:23) Ikiwa ingekuwa hivyo, bila shaka Ibilisi angedai kwamba Yehova ameshindwa. Kwa nini? Kwa sababu njia hiyo haingetimiza kusudi la Mungu, yaani, kuijaza dunia paradiso wazao wa Adamu na Hawa walio wakamilifu na watiifu. w23.11 6 ¶15-16

Jumatatu, Machi 10

Msipite mambo yaliyoandikwa.—1 Kor. 4:6.

Yehova anatupatia mwongozo ulio wazi kupitia Neno lake na tengenezo lake. Hatupaswi kuongeza sheria zetu kwenye maagizo anayotupatia. (Met. 3:​5-7) Kwa hiyo, hatupiti mambo yaliyoandikwa katika Biblia au kuwawekea sheria waabudu wenzetu kuhusu mambo ya kibinafsi. Shetani anatumia “udanganyifu mtupu” na “mambo ya msingi ya ulimwengu” huu ili kuwapotosha watu na kusababisha migawanyiko. (Kol. 2:8) Katika karne ya kwanza, mambo hayo yalitia ndani falsafa zilizotegemea mawazo ya wanadamu, mafundisho ya Wayahudi yasiyotegemea Maandiko, na fundisho la kwamba Wakristo wanapaswa kufuata Sheria ya Musa. Huo ulikuwa udanganyifu kwa sababu ulifanya watu waache kumkazia fikira yule aliye Chanzo cha hekima ya kweli, Yehova. Leo, Shetani anatumia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii ili kusambaza uvumi usio na msingi na habari za uwongo zinazoenezwa na viongozi wa kisiasa. w23.07 16 ¶11-12

Jumanne, Machi 11

Jinsi kazi zako zilivyo kuu, Ee Yehova! Jinsi mawazo yako yalivyo na kina sana!—Zab. 92:5.

Yehova alisuluhisha uasi wa Shetani na wanadamu wa kwanza kwa njia ambayo Shetani hangeweza kuiwazia kamwe. Badala ya kuonekana kuwa mwongo, Yehova alithibitika kuwa msema kweli kwa kuwaruhusu Adamu na Hawa wapate watoto. Na badala ya kuonekana kuwa ameshindwa, Yehova alithibitika kuwa mshindi. Alihakikisha kusudi lake lingetimia kwa kuandaa “uzao” ambao ungewaokoa wazao watiifu wa Adamu na Hawa. (Mwa. 3:15; 22:18) Ni lazima Shetani alipigwa na butwaa alipotambua mpango wa fidia wa Yehova! Kwa nini? Kwa sababu ni mpango unaotegemea upendo usio na ubinafsi. (Mt. 20:28; Yoh. 3:16) Shetani hana sifa hiyo. Yeye ni mbinafsi. Hivyo, mpango wa fidia utafanya jambo gani liwezekane? Mwishoni mwa ile Miaka Elfu Moja ya Utawala wa Kristo, wazao watiifu wa Adamu na Hawa walio wakamilifu wataishi katika dunia paradiso—kama Yehova alivyokusudia mwanzoni. w23.11 6 ¶17

Jumatano, Machi 12

Mungu atawahukumu.—Ebr. 13:4.

Tunatii sheria ya Yehova kuhusu utakatifu wa uhai na damu. Kwa nini? Kwa sababu Yehova anasema kwamba damu inawakilisha uhai, ambao ni zawadi yenye thamani kutoka kwake. (Law. 17:14) Kwa mara ya kwanza Yehova alipowaruhusu wanadamu wale nyama, aliwaamuru wasile damu. (Mwa. 9:4) Alitaja tena amri hiyo alipowapatia Waisraeli Sheria ya Musa. (Law. 17:10) Na aliliongoza baraza linaloongoza la karne ya kwanza litoe agizo kwamba Wakristo wote waendelee “kujiepusha . . . na damu.” (Mdo. 15:​28, 29) Tunatii amri hiyo kwa uthabiti tunapofanya uamuzi kuhusu matibabu. Pia, tunafuata kabisa viwango vya juu vya maadili kutoka kwa Yehova. Akitumia lugha ya mfano, mtume Paulo anatushauri ‘tuviue’ viungo vya mwili wetu, yaani, tufanye yote tunayoweza ili kuondoa tamaa zisizofaa za mwili. Tunaepuka kutazama au kufanya jambo lolote ambalo linaweza kutuongoza tufanye uasherati.—Kol. 3:5; Ayu. 31:1. w23.07 15 ¶5-6

Alhamisi, Machi 13

Mwishowe akamfunulia moyo wake.—Amu. 16:17.

Je, Samsoni alimwamini sana Delila na kupofushwa na upendo kumwelekea hivi kwamba akakosa kutambua njama yake? Vyovyote vile, Delila alimshinikiza Samsoni tena na tena amfunulie chanzo cha nguvu zake, na mwishowe Samsoni akamwambia. Kwa kusikitisha, Samsoni alijiruhusu kuingia katika hali ambayo ilimfanya apoteze nguvu zake na pia kukosa kibali cha Yehova kwa muda fulani. (Amu. 16:​16-20) Samsoni alipatwa na matokeo mabaya kwa sababu ya kumwamini Delila badala ya kumtegemea Yehova. Wafilisti walimkamata Samsoni na kumpofusha. Alifungwa gerezani katika jiji la Gaza, na walimfanya kuwa mtumwa aliyesaga nafaka. Kisha Wafilisti wakamfedhehesha kwa kumleta katika sherehe yao. Walimtolea dhabihu kubwa mungu wao wa uwongo Dagoni, kwa sababu waliamini kwamba yeye ndiye aliyewasaidia kumkamata Samsoni. Walimtoa Samsoni gerezani na kumleta kwenye sherehe hiyo ili “awatumbuize”—na ili wamdhihaki.—Amu. 16:​21-25. w23.09 5-6 ¶13-14

Ijumaa, Machi 14

Zingatieni mambo yaliyo mema kulingana na maoni ya watu wote.—Rom. 12:17.

Labda mfanyakazi au mwanafunzi mwenzetu anauliza maswali kuhusu msimamo wetu wa Kikristo kuhusiana na suala fulani la maadili. Tutafanya yote tunayoweza ili kutetea imani yetu huku tukiheshimu maoni ya yule tunayezungumza naye. (1 Pet. 3:15) Badala ya kuona swali lake kuwa njia ya kukushambulia, fikiria jinsi swali hilo linavyoweza kukusaidia kutambua mambo anayoona kuwa muhimu. Hata iwe mtu ana sababu gani anapouliza swali, ni vizuri kujibu kwa njia ya upole na fadhili. Jibu letu linaweza kumsaidia kubadili maoni yake. Kwa mfano, ikiwa mfanyakazi mwenzetu anatuuliza kwa nini hatusherehekei siku ya kuzaliwa, tunaweza kujiuliza hivi: Je, angependa kujua kama tunaruhusiwa kufurahia pindi nzuri? Huenda tukafaulu kupunguza mahangaiko ya mfanyakazi mwenzetu kwa kumweleza kwamba tunathamini jinsi anavyopendezwa na wafanyakazi wenzake. Hilo linaweza kutupatia fursa ya kuzungumzia maoni ya Biblia kuhusu siku ya kuzaliwa. w23.09 17 ¶10-11

Jumamosi, Machi 15

Jilindeni ili msipotoshwe pamoja nao kwa kosa la waasi sheria, na kuanguka kutoka kwenye msimamo wenu imara.—2 Pet. 3:17.

Tuna pendeleo la kutumia wakati uliobaki kuwahubiria watu wa mataifa yote. Mtume Petro anatuhimiza tuweke “karibu akilini” siku ya Yehova. (2 Pet. 3:​11, 12) Tunawezaje kufanya hivyo? Ikiwezekana kila siku tunapaswa kutafakari kuhusu baraka tutakazofurahia katika ulimwengu mpya. Jiwazie ukipumua hewa safi kabisa, ukila chakula chenye lishe, ukiwakaribisha wapendwa wako baada ya kufufuliwa, na kuwafundisha watu walioishi karne nyingi zamani kuhusu utimizo wa unabii wa Biblia. Kutafakari kwa njia hiyo kutakusaidia kuendelea kutarajia wakati huo, na kuwa na uhakika kwamba hizi ni siku za mwisho. ‘Tukiwa na ujuzi huu wa mapema’ kuhusu wakati wetu ujao, ‘hatutapotoshwa’ na walimu wa uwongo. w23.09 27 ¶5-6

Jumapili, Machi 16

Watiini wazazi wenu katika muungano na Bwana, kwa maana hilo ni jambo la uadilifu.—Efe. 6:1.

Vijana wamezungukwa na vijana wenzao ambao wana mwelekeo wa ‘kutotii wazazi.’ (2 Tim. 3:​1, 2) Kwa nini wengi wao si watiifu? Baadhi yao wanafikiri kwamba wazazi wao ni wanafiki. Watoto wanatarajiwa kufanya mambo ambayo wazazi wao hawafanyi. Wengine wanaona kwamba ushauri wa wazazi wao umepitwa na wakati, hauwezi kuwasaidia, au unawabana sana. Ikiwa wewe ni kijana, je, wakati mwingine unahisi hivyo? Ni vigumu kwa wengi kutii amri ya Yehova inayopatikana katika andiko la leo. Ni nini kinachoweza kukusaidia kuitii? Unaweza kujifunza kuwa mtiifu kutokana na mfano bora kabisa, yaani, Yesu. (1 Pet. 2:​21-24) Alikuwa mwanadamu mkamilifu aliyelelewa na wazazi wasio wakamilifu. Lakini Yesu aliwaheshimu wazazi wake hata walipofanya makosa au kukosa kumwelewa wakati fulani.—Kut. 20:12. w23.10 7 ¶4-5

Jumatatu, Machi 17

Ile amri ya zamani inawekwa kando kwa sababu ni dhaifu na haifai.—Ebr. 7:18.

Mtume Paulo alieleza kwamba dhabihu zilizotolewa kulingana na Sheria ya Musa hazingeweza kuondoa kabisa dhambi. Kwa sababu hiyo, Sheria ilikuwa ‘imewekwa kando.’ Basi, Paulo akawafundisha baadhi ya kweli zenye kina zaidi. Aliwakumbusha Wakristo wenzake kuhusu “tumaini bora” linalotegemea dhabihu ya Yesu ambayo kwa kweli ingewasaidia ‘wamkaribie Mungu.’ (Ebr. 7:19) Paulo aliwaeleza ndugu zake Waebrania kwa nini ibada ya Kikristo ilikuwa bora zaidi kuliko jinsi walivyoabudu zamani. Utaratibu uliotumiwa katika dini ya Kiyahudi ulikuwa “kivuli cha mambo yanayokuja, bali uhalisi ni wa Kristo.” (Kol. 2:17) Kivuli kinachoonekana kwa kawaida ni umbo la kitu halisi ambacho kinatokeza kivuli hicho. Vivyo hivyo, njia ambayo Wayahudi walitumia kuabudu zamani, ilikuwa kivuli tu cha uhalisi ambao ungekuja. Tunahitaji kuelewa mpango ambao Yehova ameweka ili tusamehewe dhambi zetu na ili tumwabudu kwa njia inayokubalika. w23.10 25 ¶4-5

Jumanne, Machi 18

Wakati wa mwisho mfalme wa kusini atasukumana naye, na mfalme wa kaskazini atamshambulia vikali.—Dan. 11:40.

Danieli sura ya 11 inazungumza kuhusu wafalme wawili, au serikali za kisiasa ambazo zinashindana kuutawala ulimwengu. Kwa kulinganisha unabii huo na unabii mwingine katika Biblia, tunaweza kusema kwamba “mfalme wa kaskazini” ni serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono. Na “mfalme wa kusini” ni Muungano wa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Watu wa Mungu wanaoishi chini ya utawala wa “mfalme wa kaskazini” wanateswa moja kwa moja na mfalme huyo. Baadhi ya Mashahidi wamepigwa na kufungwa gerezani kwa sababu ya imani yao. Badala ya kuwafanya waogope, mateso ya “mfalme wa kaskazini” dhidi ya ndugu zetu yameimarisha imani yao. Kwa nini? Kwa sababu ndugu zetu wanajua kwamba watu wa Mungu wanapoteswa, hilo linatimiza unabii uliotolewa na Danieli. (Dan. 11:41) Kujua jambo hilo kunaweza kutusaidia kuwa na tumaini imara na kudumisha utimilifu wetu. w23.08 11 ¶15-16

Jumatano, Machi 19

Yeyote anayewagusa ninyi anaigusa mboni ya jicho langu.—Zek. 2:8.

Kwa sababu Yehova anatupenda, anatambua haraka hisia zetu na yuko tayari kutulinda. Anahuzunika tunapoumia. Hivyo, tunaweza kusali hivi tukiwa na uhakika: “Nilinde kama mboni ya jicho lako.” (Zab. 17:8) Jicho ni kiungo cha mwili chenye thamani sana na kinachopaswa kutunzwa vizuri. Hivyo, Yehova anapotulinganisha na mboni ya jicho lake, ni kana kwamba anasema, ‘Yeyote anayewadhuru ninyi, watu wangu, anadhuru kitu chenye thamani kwangu.’ Yehova anataka tusadiki kwamba anatupenda kibinafsi. Lakini anajua kwamba kwa sababu ya mambo mabaya tuliyopitia maishani, huenda tusiwe na uhakika kwamba anaweza kutupenda. Au huenda kwa sasa tunakabili hali ambazo zinafanya tusiwe na uhakika kwamba Yehova anatupenda. Ni nini kitakachoimarisha uhakika wetu? Kujifunza jinsi Yehova anavyoonyesha upendo wake kwa Yesu, watiwa-mafuta, na kwetu sote. w24.01 27 ¶6-7

Alhamisi, Machi 20

Mkono wa Mungu wetu ulikuwa juu yetu, naye akatuokoa kutoka mikononi mwa maadui.—Ezra 8:31.

Ezra alikuwa ameona jinsi Yehova alivyowategemeza watu Wake wakati wa majaribu. Miaka mingi mapema, mwaka wa 484 K.W.K., huenda Ezra alikuwa akiishi Babiloni wakati Mfalme Ahasuero alipotoa agizo la kuwaangamiza Wayahudi wote katika Milki ya Uajemi. (Esta 3:​7, 13-15) Uhai wa Ezra ulikuwa hatarini! Ili kukabiliana na tishio hilo, Wayahudi “katika kila mkoa” walifunga na kuomboleza, na bila shaka walisali kwa Yehova ili awapatie mwongozo. (Esta 4:3) Wazia jinsi Ezra na Wayahudi wenzake walivyohisi mambo yalipowageukia wale waliopanga njama ya kuwaangamiza Wayahudi! (Esta 9:​1, 2) Huenda mambo ambayo Ezra alijionea wakati huo mgumu yalimtayarisha kwa ajili ya majaribu ya wakati ujao na bila shaka yaliimarisha uhakika wake katika uwezo wa Yehova wa kuwalinda watu Wake. w23.11 17 ¶12-13

Ijumaa, Machi 21

Mungu humhesabu kuwa mwadilifu bila matendo.—Rom.4:6.

Kimsingi mtume Paulo alikuwa akirejelea “matendo ya sheria,” yaani, sheria ya Musa, iliyotolewa kwenye Mlima Sinai. (Rom. 3:​21, 28.) Inaonekana kwamba katika siku za Paulo, haikuwa rahisi kwa baadhi ya Wakristo Wayahudi, kuamini kwamba Sheria ya Musa na matendo yaliyopaswa kufanywa kulingana na Sheria hiyo yalikuwa yameondolewa. Hivyo, Paulo alitumia mfano wa Abrahamu kuthibitisha kwamba msimamo wa uadilifu mbele za Mungu hautokani na “matendo ya sheria.” Unatokana na kuwa na imani. Kujua jambo hilo kunatia moyo kwa sababu kunatupatia uhakika kwamba tunaweza kuwa na msimamo mzuri mbele za Mungu. Kunamaanisha kwamba tunaweza kusitawisha imani katika Mungu na Kristo, jambo ambalo linaweza kutupatia kibali cha Mungu. Kwa upande mwingine, “matendo” yanayozungumziwa kwenye Yakobo sura ya 2 si “matendo ya sheria” yaliyotajwa na Paulo. Yakobo anarejelea matendo, au mambo, ambayo Wakristo hufanya kila siku maishani. (Yak. 2:24) Matendo hayo yanaonyesha ikiwa Mkristo ana imani ya kweli katika Mungu au la. w23.12 3 ¶8; 4-5 ¶10-11

Jumamosi, Machi 22

Mume ni kichwa cha mke wake.—Efe. 5:23.

Akina dada wanaofikiria kufunga ndoa, wanapaswa kuchagua mwenzi wao kwa makini sana. Kumbuka, utakuwa chini ya ukichwa wa mwanamume unayefunga ndoa naye. (Rom. 7:2; Efe. 5:33) Hivyo jiulize: ‘Je, mwanamume huyo ni Mkristo mkomavu? Je, anatanguliza masilahi ya kiroho maishani mwake? Je, anafanya maamuzi ya hekima? Je, anaweza kukiri makosa yake? Je, anaheshimu wanawake? Je, ana ustadi unaohitajika ili kunitegemeza kiroho, kimwili, na kihisia? Bila shaka, ikiwa unataka kupata mume mzuri, unahitaji kuwa mke mzuri pia. Mke mzuri ni “msaidizi” wa mume wake na “kikamilisho” chake. (Mwa. 2:18) Na kwa kuwa mke anampenda Yehova, anajitahidi kuwasaidia wengine waone sifa nzuri za mume wake. (Met. 31:​11, 12; 1 Tim. 3:11) Unaweza kujitayarisha kwa ajili ya jukumu hilo kwa kuimarisha upendo wako kwa Yehova na kwa kuwa msaidizi wa wengine nyumbani na kutanikoni. w23.12 22-23 ¶18-19

Jumapili, Machi 23

Kwa hiyo, ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu.—Yak. 1:5.

Yehova ametuahidi kwamba atatupatia hekima tunayohitaji ili tufanye maamuzi mazuri. Tunahitaji hasa hekima kutoka kwa Mungu tunapofanya maamuzi ambayo yataathiri maisha yetu yote. Pia, anatupatia nguvu za kuvumilia. Kama vile alivyomsaidia mtume Paulo, Yehova atatupatia nguvu tunazohitaji ili tuvumilie majaribu yetu. (Flp. 4:13) Njia moja anayotumia ili kutusaidia, ni kupitia ndugu na dada zetu. Usiku kabla ya Yesu kutoa uhai wake uwe dhabihu, alisali kwa bidii. Alimsihi Yehova amwondolee shutuma ya kuonwa kuwa mkufuru. Badala ya kufanya hivyo, Yehova alimsaidia Yesu kwa kumtuma malaika ili amwimarishe Yesu. (Luka 22:​42, 43) Njia nyingine ambayo huenda Yehova akatusaidia ni wakati tunapotiwa moyo kwa kupigiwa simu au kutembelewa na mmoja wa ndugu au dada zetu. Sisi sote tunaweza kutafuta fursa za kuwapa “neno jema” waabudu wenzetu.—Met. 12:25. w23.05 10-11 ¶9-11

Jumatatu, Machi 24

Endeleeni kutiana moyo na kujengana.—1 The. 5:11.

Wahubiri wasiotenda wanaohudhuria Ukumbusho huenda waliogopa kwamba hawatakaribishwa vizuri. Hivyo, epuka kuwauliza maswali yatakayowaaibisha au kusema jambo litakalowaumiza. Ndugu na dada hao ni waamini wenzetu. Tunafurahi kuabudu pamoja nao tena! (Zab. 119:176; Mdo. 20:35) Tunashukuru sana kwamba Yesu alituambia tuadhimishe Ukumbusho wa kifo chake kila mwaka. Na tunaelewa kwa nini jambo hilo ni muhimu sana. Tunapohudhuria Ukumbusho tunajinufaisha wenyewe na wengine katika njia nyingi. (Isa. 48:​17, 18) Upendo wetu kwa Yehova na Yesu unaongezeka. Tunaonyesha jinsi tunavyoshukuru kwa mambo yote ambayo wametufanyia. Tunaimarisha uhusiano wetu pamoja na ndugu na dada zetu. Na huenda tukawasaidia wengine wajifunze jinsi wanavyoweza kufurahia baraka tunazopata kwa sababu ya fidia. Hivyo, acheni tufanye yote tunayoweza ili kuwa tayari kwa ajili ya siku ya Ukumbusho wa mwaka huu—siku muhimu zaidi katika mwaka! w24.01 14 ¶18-19

Jumanne, Machi 25

Mimi, Yehova, [ndiye] . . . ninayekuongoza.—Isa. 48:17.

Yehova anatuongozaje? Kwanza kabisa, anatumia Neno lake, Biblia. Pia, anatumia wawakilishi wake duniani. Kwa mfano, anamtumia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ili kuandaa chakula cha kiroho kinachotusaidia kufanya maamuzi kwa hekima. (Mt. 24:45) Yehova pia anatumia wanaume wengine wenye uwezo kutuongoza. Kwa mfano, waangalizi wa mzunguko na wazee wa kutaniko wanatutia moyo na kutupatia mwongozo unaotusaidia kukabiliana na nyakati ngumu. Tunashukuru sana kwa mwongozo wenye kutegemeka tunaopata katika siku hizi za mwisho zilizo hatari! Mwongozo huo unatusaidia kuendelea kuwa na kibali cha Yehova na kubaki katika barabara ya uzima. Ingawa hivyo, huenda pindi fulani tukaona ni vigumu kufuata mwongozo wa Yehova, hasa ikiwa tunaupata kupitia wanaume wasio wakamilifu. Katika pindi hizo, tunahitaji kuwa na uhakika kwamba Yehova anawaongoza watu wake na kwamba kufuata mwongozo wake huleta baraka. w24.02 20 ¶2-3

Jumatano, Machi 26

Tunapaswa kupendana, si kwa neno au kwa ulimi bali kwa tendo na kweli.—1 Yoh. 3:18.

Tunaweza kuimarisha upendo wetu kwa Mungu kwa kujifunza Neno lake kwa bidii. Unaposoma Biblia jaribu kutambua jambo ambalo kila simulizi linafunua kumhusu Yehova. Jiulize hivi: ‘Simulizi hili linaonyeshaje kwamba Yehova ananipenda? Linanipatia sababu gani za kumpenda Yehova?’ Njia nyingine ambayo tunaweza kuimarisha upendo wetu kwa Yehova ni kwa kumfunulia moyo wetu kwa ukawaida katika sala. (Zab. 25:​4, 5) Naye Yehova atajibu sala zetu. (1 Yoh. 3:​21, 22) Tunapaswa pia kuimarisha upendo wetu kwa wengine. Miaka kadhaa baada ya kuwa Mkristo, mtume Paulo alikutana na kijana aliyeitwa Timotheo. Timotheo alimpenda Yehova, na pia aliwapenda watu. Paulo aliwaambia hivi Wafilipi: “Sina mtu mwingine aliye na mwelekeo kama [wa Timotheo] atakayejali kwa unyoofu mahangaiko yenu.” (Flp. 2:20) Ni wazi kwamba Paulo alifurahishwa na jinsi Timotheo alivyowapenda ndugu na dada. Bila shaka, makutaniko ambayo Timotheo alitumikia yalitazamia kwa hamu awatembelee.—1 Kor. 4:17. w23.07 9 ¶7-10

Alhamisi, Machi 27

Sitakutupa kamwe.—Ebr. 13:5.

Musa alikufa kabla ya Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi. Je, watu wa Mungu walikosa mwongozo baada ya mwanamume huyo mwaminifu kufa? Hapana. Maadamu wangeendelea kuwa waaminifu, Yehova angewatunza. Kabla ya kifo cha Musa, Yehova alimwambia amkabidhi Yoshua mgawo wa kuwaongoza watu wake. Musa alikuwa akimzoeza Yoshua kwa miaka mingi. (Kut. 33:11; Kum. 34:9) Pia, kulikuwa na wanaume wengine wengi wenye uwezo waliokuwa wakiongoza, yaani, wakuu wa maelfu, wa mamia, wa hamsini, na hata wa makumi. (Kum. 1:15) Watu wa Mungu walitunzwa vizuri. Eliya ni mfano mwingine. Alikuwa akiongoza ibada safi katika Israeli kwa miaka mingi. Lakini wakati ulifika ambapo Yehova alimhamisha kwenda kwenye mgawo mwingine, upande wa kusini huko Yuda. (2 Fal. 2:1; 2 Nya. 21:12) Je, watu waaminifu katika ufalme wa kaskazini wa Israeli uliokuwa na makabila kumi walikuwa wameachwa? Hapana. Eliya alikuwa amemzoeza Elisha kwa miaka mingi. Naam, Yehova aliendelea kutimiza kusudi lake, na aliwatunza waabudu wake waaminifu. w24.02 5 ¶12

Ijumaa, Machi 28

Endeleeni kutembea kama watoto wa nuru.—Efe. 5:8.

Wakristo wa Efeso walikuwa wamekubali nuru ya kweli ya Kimaandiko. (Zab. 119:105) Waefeso hao waliacha mazoea ya dini zao za uwongo na mwenendo mpotovu. Walikuwa wamekuwa “waigaji wa Mungu” na walifanya yote wawezayo ili kumwabudu na kumfurahisha. (Efe. 5:1) Kwa njia hiyohiyo, kabla hatujajifunza kweli tulikuwa katika giza kwa sababu ya dini za uwongo na maadili mapotovu. Baadhi yetu tulisherehekea sikukuu za dini za uwongo; na wengine tuliishi maisha mapotovu kiadili. Lakini baada tu ya kujifunza viwango vya Yehova vya mema na mabaya, tulifanya mabadiliko. Tulianza kuishi kupatana na viwango vyake vya uadilifu. Matokeo ni kwamba tumenufaika sana. (Isa. 48:17) Hata hivyo, kwa sasa tunaendelea kukabili changamoto. Tunahitaji kukaa mbali na giza tuliloliacha na kuendelea “kutembea kama watoto wa nuru.” w24.03 21 ¶6-7

Jumamosi, Machi 29

Kwa kadiri ambavyo tumefanya maendeleo, na tuendelee kutembea kwa utaratibu katika mwendo huohuo.—Flp. 3:16.

Huenda unahisi kwamba huko tayari kujiweka wakfu na kubatizwa. Labda bado unahitaji kufanya mabadiliko maishani mwako ili yapatane na viwango vya Yehova, au labda unahitaji muda zaidi ili kuimarisha imani yako. (Kol. 2:​6, 7) Si kila mwanafunzi atafanya maendeleo ya kiroho kwa kiwango kilekile, na si kila kijana atakuwa tayari kwa ajili ya kujiweka wakfu na kubatizwa katika umri uleule. Jitahidi kupima maendeleo yako ya kiroho kulingana na mambo unayoweza kufanya, na si kwa kujilinganisha na mtu mwingine. (Gal. 6:​4, 5) Hata ikiwa umetambua kwamba huko tayari kujiweka wakfu kwa Yehova, endelea kufanya jambo hilo kuwa lengo lako. Sali kwa Yehova na umwombe abariki jitihada zako za kufanya mabadiliko yoyote unayohitaji kufanya. (Flp. 2:13) Unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atasikiliza sala yako na kuijibu.—1 Yoh. 5:14. w24.03 5 ¶9-10

Jumapili, Machi 30

Waume, . . . endeleeni kukaa [na wake zenu] kulingana na ujuzi.—1 Pet. 3:7.

Pindi moja, Sara alikuwa na mahangaiko, na akamweleza Abrahamu hisia zake, na hata alimlaumu kwa tatizo hilo. Abrahamu alijua kwamba Sara alikuwa mke mwenye ujitiisho na aliyemuunga mkono. Abrahamu alimsikiliza na akajaribu kusuluhisha tatizo hilo. (Mwa. 16:​5, 6) Tunaweza kujifunza nini? Mume, una mamlaka ya kufanya maamuzi kwa ajili ya familia yako. (1 Kor. 11:3) Hata hivyo, jambo la upendo ni kumsikiliza mke wako kwa makini na kufikiria maoni yake kabla ya kufanya uamuzi, hasa ikiwa uamuzi huo utamwathiri. (1 Kor. 13:​4, 5) Pindi nyingine, Abrahamu aliamua kuwakaribisha wageni ambao hawakutarajiwa. Alimwomba Sara aache kazi ambayo alikuwa akifanya na atayarishe kiasi kikubwa cha mkate. (Mwa. 18:6) Sara alitenda upesi na akaunga mkono uamuzi wa Abrahamu. Mke, unaweza kumwiga Sara kwa kuunga mkono maamuzi wa mume wako. Ukifanya hivyo, utaimarisha ndoa yenu.—1 Pet. 3:​5, 6. w23.05 24-25 ¶16-17

Jumatatu, Machi 31

Hekima inayotoka juu . . . [iko] tayari kutii.—Yak. 3:17.

Baada ya Gideoni kuwekwa rasmi kuwa mwamuzi, alihitaji kutii na kuwa jasiri. Alipewa mgawo hatari wa kuharibu madhabahu ambayo baba yake alikuwa ametengeneza kwa ajili ya ibada ya Baali. (Amu. 6:​25, 26) Pindi nyingine, baada ya kukusanya wanajeshi, Gideoni aliagizwa mara mbili apunguze idadi yao. (Amu. 7:​2-7) Mwishowe, aliambiwa ashambulie kambi ya maadui usiku wa manane. (Amu. 7:​9-11) Wazee wanapaswa kuwa “tayari kutii.” Mzee mtiifu yuko tayari kufuata Maandiko na mwongozo unaotoka katika tengenezo la Mungu. Akifanya hivyo, anawawekea wengine mfano mzuri. Hata hivyo, wakati mwingine inaweza kuwa vigumu kwake kufanya mabadiliko haraka baada ya kupata mwongozo. Katika hali nyingine, huenda akahisi kwamba si jambo lenye busara au hekima kufuata mwongozo fulani. Au huenda akaombwa kufanya mgawo fulani ambao unaweza kuhatarisha uhuru wake. Wazee wanawezaje kuiga utii wa Gideoni katika hali kama hizo? Sikiliza mwongozo kwa makini na uufuate. w23.06 4-5 ¶9-11

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki