Februari
Jumamosi, Februari 1
Nitawasikiliza.—Yer. 29:12.
Mfalme Hezekia alipokuwa mgonjwa sana, alimsihi Yehova amponye. Yehova alijibu sala yake kwa kumponya. (2 Fal. 20:1-6) Kwa upande mwingine, mtume Paulo alipomsihi Yehova amwondolee “mwiba katika mwili,” Yehova hakuondoa tatizo hilo. (2 Kor. 12:7-9) Mfalme Herode alitaka kumuua mtume Yakobo na pia mtume Petro. Yakobo aliuawa, lakini Petro aliokolewa kimuujiza. (Mdo. 12:1-11) Huenda tukajiuliza, ‘Kwa nini Yehova alimwokoa Petro na hakumwokoa Yakobo?’ Biblia haielezi jambo hilo. Jambo tunaloweza kuwa na uhakika nalo ni kwamba njia za Yehova ‘kamwe hazina ukosefu wa haki.’ (Kum. 32:4) Wakati mwingine, huenda Yehova asijibu sala zetu kwa njia tunayotarajia. Lakini kwa kuwa tunaamini kwamba sikuzote jibu la Yehova litakuwa la upendo na la haki, hatutilii shaka njia anayochagua kujibu sala zetu.—Ayu. 33:13. w23.11 21 ¶6
Jumapili, Februari 2
Hekima inayotoka juu . . . [iko] tayari kutii.—Yak. 3:17.
Mwandikaji Yakobo ambaye aliongozwa na roho takatifu alisema watu wenye hekima wako “tayari kutii.” Fikiria maana ya jambo hilo. Tunapaswa kuwa tayari kabisa kuwatii wale ambao Yehova amewapatia mamlaka ya kadiri. Bila shaka, Yehova hatarajii kwamba tumtii mtu ambaye anatuambia tupuuze amri za Mungu. (Mdo. 4:18-20) Huenda ikawa rahisi zaidi kwetu kumtii Yehova kuliko kumtii mwanadamu. Kwa sababu sikuzote Yehova hutoa mwongozo mkamilifu. (Zab. 19:7) Lakini wanadamu wenye mamlaka si wakamilifu. Hata hivyo, Baba yetu wa mbinguni amewapatia mamlaka ya kadiri wazazi, maofisa wa serikali, na wazee wa kutaniko. (Met. 6:20; 1 The. 5:12; 1 Pet. 2:13, 14) Tunapowatii, kwa kweli tunamtii Yehova. w23.10 6 ¶2-3
Jumatatu, Februari 3
Maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.—Ufu. 21:5.
Njia moja ya kuimarisha imani yetu ni kwa kutafakari kuhusu nguvu za Yehova. Yeye ana nguvu za kutimiza kila jambo analoahidi kufanya. Hiyo ni kwa sababu yeye ni Mungu Mweza-Yote. (Ayu. 42:2; Marko 10:27; Efe. 3:20) Aliwahakikishia Abrahamu na Sara kwamba wangepata mtoto uzeeni. (Mwa. 17:15-17) Pia, alimwambia Abrahamu kwamba wazao wake wangepewa nchi ya Kanaani. Wakati wa kipindi cha miaka mingi ambacho wazao wa Abrahamu, yaani Waisraeli, walikuwa watumwa nchini Misri, huenda ilionekana kwamba ahadi hiyo haingetimia kamwe. Lakini ilitimia. Alimwambia Maria, aliyekuwa bikira kwamba angemzaa Mwana wa Mungu, ambaye Yehova alikuwa ameahidi angefika, maelfu ya miaka mapema katika bustani ya Edeni, na ahadi hiyo ilitimizwa! (Mwa. 3:15) Tunaimarisha imani yetu katika nguvu za Yehova za kuleta ulimwengu mpya kwa kutafakari ahadi mbalimbali alizotoa na kuzitimiza.—Yos. 23:14; Isa. 55:10, 11. w23.04 28 ¶10-12
Jumanne, Februari 4
Ee Yehova, isikie sala yangu; sikiliza sihi yangu ya kuomba msaada.—Zab. 143:1.
Yehova alijibu sala ya Daudi kwa kumkomboa. (1 Sam. 19:10, 18-20; 2 Sam. 5:17-25) Sisi pia tunaweza kuwa na uhakika huo. (Zab. 145:18) Huenda Yehova asijibu sala zetu kwa njia tunayotarajia. Paulo alimwomba Mungu amwondolee “mwiba katika mwili.” Katika pindi tatu, Paulo alisali kihususa kuhusu tatizo hilo gumu. Je, Yehova alijibu sala hizo? Ndiyo, lakini kwa njia ambayo Paulo hakutarajia. Badala ya kuondoa tatizo hilo, Yehova alimpa nguvu alizohitaji ili aendelee kumtumikia kwa uaminifu. (2 Kor. 12:7-10) Wakati mwingine, huenda sisi pia tukapata jibu lililo tofauti na lile tulilotarajia. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anajua kihususa njia bora ya kutusaidia. Hata anaweza “kufanya kwa wingi zaidi kupita mambo yote tunayoomba au tunayofikiri.” (Efe. 3:20) Kwa sababu hiyo, huenda akajibu sala zetu wakati au kwa njia ambayo hatukutarajia. w23.05 8-9 ¶4-6
Jumatano, Februari 5
Saa inakuja ambayo wote walio katika makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.—Yoh. 5:28, 29.
Mara kwa mara, ni vizuri sisi sote tutafakari ahadi ya Biblia kuhusu ufufuo wa wakati ujao. Kwa nini? Kwa sababu hatujui wakati ambapo huenda tukakabili ugonjwa unaohatarisha uhai au kufiwa na mtu tunayempenda. (Mhu. 9:11; Yak. 4:13, 14) Tumaini letu la ufufuo linaweza kutusaidia kuvumilia changamoto kama hizo. (1 The. 4:13) Maandiko yanatuhakikishia kwamba Baba yetu wa mbinguni anatujua vizuri na anatupenda sana. (Luka 12:7) Yehova Mungu anatujua vizuri sana hivi kwamba anaweza kutufufua tukiwa na utu na kumbukumbu zilezile. Yehova anatupenda sana hivi kwamba ametupatia nafasi ya kuishi milele, hata ikiwa itamaanisha kutufufua! Kwa nini tunaweza kuamini ahadi ya ufufuo? Ni kwa sababu tunasadiki kwamba Yule anayetoa ahadi hiyo anatamani na ana nguvu, au uwezo, wa kuitimiza. w23.04 8-9 ¶2-4
Alhamisi, Februari 6
[Yosefu na Maria] walikuwa na desturi ya kwenda Yerusalemu kila mwaka kwa ajili ya sherehe ya Pasaka.—Luka 2:41.
Yosefu na Maria walishirikiana ili kuimarisha uhusiano wao pamoja na Yehova. Walielewa umuhimu wa kumwabudu Yehova pamoja wakiwa familia. (Luka 2:22-24; 4:16) Huo ni mfano bora kwa wenzi wa ndoa leo! Ikiwa mna watoto, kama ilivyokuwa kwa Yosefu na Maria, huenda mkakabili changamoto inapohusu kuhudhuria mikutano au kupanga ratiba ya ibada ya familia. Hata huenda ikawa vigumu zaidi kupata wakati wa kujifunza na kusali pamoja mkiwa wenzi wa ndoa. Hata hivyo, kumbuka kwamba mnapomwabudu Yehova pamoja, mnamkaribia hata zaidi na kuwa na uhusiano wa karibu kati yenu. Basi, tangulizeni ibada katika familia yenu. Ikiwa mna matatizo katika ndoa yenu, huenda hata msifurahie wazo la kufanya ibada ya familia pamoja. Ikiwa ndivyo, anzeni kwa kujifunza jambo fupi na lenye kufurahisha. Hatua hii itawasaidia kuimarisha uhusiano wenu na tamaa yenu ya kufanya mambo ya kiroho mkiwa wenzi wa ndoa. w23.05 22 ¶7-8
Ijumaa, Februari 7
Obadia alimwogopa sana Yehova.—1 Fal. 18:3.
Woga unaofaa ulimsaidiaje Obadia? Jambo moja ni kwamba ulimsaidia kuwa mnyoofu na mwenye kutegemeka; hivyo, mfalme alimchagua asimamie makao ya mfalme. (Linganisha Nehemia 7:2.) Pia, woga wa Obadia kumwelekea Mungu ulimpatia ujasiri mwingi usio wa kawaida—sifa ambayo aliihitaji sana. Aliishi katika kipindi cha mtawala mwovu Mfalme Ahabu. (1 Fal. 16:30) Pia, Yezebeli, mke wa Ahabu ambaye alimwabudu Baali, alimchukia sana Yehova hivi kwamba alijaribu kukomesha kabisa ibada safi katika ufalme wa kaskazini. Hata aliwaua manabii wengi wa Mungu. (1 Fal. 18:4) Yezebeli alipoanza kuwatafuta manabii wa Mungu ili awaue, Obadia aliwachukua 100 kati yao na kuwaficha ‘manabii 50 katika kila pango, na kuwapa mikate na maji.’ (1 Fal. 18:13, 14) Ikiwa angegunduliwa, kwa hakika Obadia mwenye ujasiri angeuawa. Bila shaka, Obadia alikuwa na hofu na hakutaka kufa, lakini Obadia alimpenda Yehova na wale waliomtumikia kuliko alivyopenda uhai wake mwenyewe. w23.06 16 ¶9-10
Jumamosi, Februari 8
Mimi, Yehova, [ndiye] . . . ninayekuongoza.—Isa.48:17.
Yehova anaendelea kuwaongoza watu wake leo kama alivyofanya zamani. Amekuwa akifanya hivyo kupitia Neno lake na Mwana wake, ambaye ni kichwa cha kutaniko. Je, tunajionea uthibitisho kwamba katika nyakati zetu Mungu ameendelea kutumia wawakilishi wake hapa duniani? Ndiyo. Kwa mfano, fikiria mambo fulani yaliyotukia mwishoni mwa miaka ya 1800. Charles Taze Russell na wenzake walianza kuelewa kwamba mwaka wa 1914 ungekuwa mwaka muhimu inapohusu kusimamishwa kwa Ufalme wa Mungu. (Dan. 4:25, 26) Walitegemea unabii wa Biblia, ili kufikia mkataa huo. Je, Yehova alikuwa akiongoza utafiti wao katika Biblia? Ni wazi alikuwa akifanya hivyo. Mambo yaliyotukia ulimwenguni mwaka wa 1914 yalithibitisha kwamba Ufalme wa Mungu ulikuwa umeanza kutawala. Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilianza, na kufuatiwa na magonjwa, matetemeko ya ardhi, na upungufu wa chakula. (Luka 21:10, 11) Kwa kweli, Yehova alikuwa akiwatumia wanaume hao wanyoofu ili kuwasaidia watu wake. w24.02 22 ¶11
Jumapili, Februari 9
Mwadilifu ana matatizo mengi, lakini Yehova humwokoa kutoka katika matatizo hayo yote.—Zab. 34:19.
Tukiwa watu wa Yehova, tunajua kwamba anatupenda na anataka tufurahie maisha bora kabisa. (Rom. 8:35-39) Pia, tunasadiki kwamba sikuzote tunanufaika tunapofuata kanuni za Biblia. (Isa. 48:17, 18) Hata hivyo, namna gani ikiwa tutakabili changamoto tusizotarajia? Kwa mfano, huenda mtu wa familia akatuvunja moyo kwa njia fulani. Huenda tukakabili matatizo makubwa ya kiafya yanayotuzuia kufanya mengi katika utumishi wa Yehova. Huenda tukakabiliana na madhara yanayosababishwa na janga la asili. Au huenda tukateswa kwa sababu ya imani yetu. Tunapokabili majaribu kama hayo, tunaweza kujiuliza: ‘Kwa nini ninapatwa na jambo hili? Je, nimefanya kosa fulani? Je, jambo hili linamaanisha kwamba Yehova hanibariki?’ Je, umewahi kuhisi hivyo? Ikiwa ndivyo, usife moyo. Watumishi wengi washikamanifu wa Yehova wamepambana na hisia kama hizo.—Zab. 22:1, 2; Hab. 1:2, 3. w23.04 14 ¶1-2
Jumatatu, Februari 10
Nimeazimia kuyatii masharti yako nyakati zote.—Zab. 119:112.
Tunaposhawishiwa, tunakataa mara moja wazo au tendo lolote ambalo linaweza kuharibu urafiki wetu pamoja na Mungu. Yehova anatarajia tuwe “watiifu kutoka moyoni.” (Rom. 6:17) Sikuzote mwongozo wake unatunufaisha, na hatuwezi kubadili sheria zake. (Isa. 48:17, 18; 1 Kor. 6:9, 10) Ibilisi anatumia mashambulizi ya kimwili na kihisia ili kujaribu kudhoofisha azimio letu. Lengo lake ni ‘kutumeza,’ anataka kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova. (1 Pet. 5:8) Wakristo wa karne ya kwanza walitishwa, walipigwa, na kuuawa kwa sababu ya azimio lao la kusimama imara. (Mdo. 5:27, 28, 40; 7:54-60) Leo, Shetani anaendelea kutumia mateso. Hilo linaonekana wazi kupitia jinsi ndugu na dada zetu wanavyotendewa kikatili huko Urusi na katika nchi nyingine, na kupitia mashambulizi ya kibinafsi kutoka kwa wapinzani. Mbali na kutumia mashambulizi ya moja kwa moja, Shetani anatumia pia “matendo yenye hila.”—Efe. 6:11. w23.07 15-16 ¶6-9
Jumanne, Februari 11
Kupitia upendo na tuendelee kukua katika mambo yote.—Efe. 4:15.
Kadiri unavyozidi kujifunza Neno la Mungu, ndivyo upendo wako kwa Yehova utakavyozidi kukua. Upendo huo unakuchochea kutumia mambo unayojifunza. Unafanya maamuzi mazuri yanayotegemea kanuni za Biblia. Unaboresha mtazamo na mwenendo wako kwa sababu unatamani kumfurahisha Mungu. Kama vile mtoto anavyomwiga mzazi mwenye upendo, unajitahidi kumwiga Baba yako wa mbinguni. (Efe. 5:1, 2) Huenda tukajiuliza hivi: ‘Je, sasa ninampenda Yehova zaidi kuliko nilivyompenda nilipobatizwa? Tangu nilipobatizwa, je, njia yangu ya kufikiri na kutenda ni kama ya Yehova—hasa katika kuwaonyesha upendo ndugu na dada zangu?’ Ikiwa “upendo uliokuwa nao mwanzoni” umepoa kwa kadiri fulani, usivunjike moyo. Wakristo wa karne ya kwanza walipatwa na jambo kama hilo. Yesu hakuwakataa na hatatukataa sisi pia. (Ufu. 2:4, 7) Anajua kwamba tunaweza kusitawisha upendo tuliokuwa nao mwanzoni tulipojifunza kweli. w23.07 8 ¶2-3
Jumatano, Februari 12
Wewe, Ee Yehova, ni mwema na uko tayari kusamehe.—Zab. 86:5.
Mtume Petro alifanya makosa mbalimbali. Kwanza, Petro alijiamini kupita kiasi, alijigamba kwamba angekuwa mwaminifu hata ikiwa wengine wangemwacha Yesu. (Marko 14:27-29) Pili, Petro alishindwa kuendelea kukaa macho. (Marko 14:32, 37-41) Kisha, Yesu alipokamatwa na umati wenye silaha, Petro alimwacha. (Marko 14:50) Mwishowe, Petro alikana mara tatu kwamba hamjui Yesu, hata aliapa aliposema uwongo huo. (Marko 14:66-71) Petro alitendaje alipotambua uzito wa dhambi yake? Alilemewa na hisia na akaanza kulia. (Marko 14:72) Badala ya kumkemea Petro kwa sababu ya makosa yake, baadaye Yesu alimwambia Petro, rafiki yake, kwamba angepokea majukumu mazito. (Yoh. 21:15-17) Petro alijua kwamba alikuwa amefanya dhambi nzito, lakini hakukata tamaa. Kwa nini? Kwa sababu alisadiki kwamba Yesu, Bwana wake, bado alikuwa akimpenda. Tunajifunza nini? Yehova anataka tusadiki kwamba anatupenda na yuko tayari kutusamehe.—Rom. 8: 38, 39. w24.03 18-19 ¶13-15
Alhamisi, Februari 13
Wale aliowaua ni wengi sana.—Met. 7:26.
Uasherati unaweza kusababisha aibu, kujihisi kwamba hufai, mimba zisizotakikana, na kuvunjika kwa familia. Ni wazi kwamba ni jambo la hekima kuepuka “nyumba” ya mwanamke mpumbavu. Mbali na kupoteza kibali cha Yehova, wengi wanaofanya uasherati hupatwa na magonjwa ambayo yanasababisha kifo cha mapema. (Met. 7:23) Methali 9:18 inamalizia kwa kusema hivi: “Wageni wake wamo katika vina vya kaburi.” Basi, kwa nini watu wengi hukubali mwaliko wa mwanamke huyo unaoongoza kwenye msiba? (Met. 9:13-18) Mtego mmoja wa kawaida ni ponografia. Baadhi ya watu wanafikiri kwamba kutazama ponografia hakuna madhara yoyote. Kinyume chake, ponografia husababisha madhara, hufanya watu wakose kujiheshimu, na kuwa waraibu wa ponografia. Mtu anapotazama ponografia ni vigumu sana kuondoa picha hizo akilini. Isitoshe, ponografia haiwezi kutusaidia kushinda tamaa zisizofaa; badala yake, inachochea tamaa hizo. (Kol. 3:5; Yak. 1:14, 15) Naam, baada ya kutazama ponografia, watu wengi hujihusisha na mwenendo mpotovu. w23.06 23 ¶10-11
Ijumaa, Februari 14
Utazipondaponda na kuzikomesha falme hizi zote, nao pekee utasimama milele.—Dan. 2:44.
Ingawa huenda mataifa mengine yakaipinga Serikali Kuu ya Uingereza na Marekani, hayawezi kuchukua nafasi ya serikali hiyo. Tunajua hivyo kwa sababu “jiwe” linalofananisha Ufalme wa Mungu litaponda nyayo, sehemu ya sanamu hiyo inayofananisha muungano wa Uingereza na Marekani. (Dan. 2:34, 35, 44, 45) Je, unasadiki kwamba unabii wa Danieli kuhusu nyayo za chuma na udongo wa mfinyanzi ni wa kweli? Ikiwa ndivyo, jambo hilo litakusaidia kuamua jinsi utakavyoishi maisha yako. Utaepuka kukazia fikira kujikusanyia vitu vya kimwili katika ulimwengu ambao utaangamizwa hivi karibuni. (Luka 12:16-21; 1 Yoh. 2:15-17) Kuelewa unabii huo kutakusaidia uelewe umuhimu wa kazi ya kuhubiri na kufundisha. (Mt. 6:33; 28:18-20) Baada ya kujifunza unabii huo, unaweza kujiuliza swali hili: ‘Je, maamuzi ninayofanya yanaonyesha ninasadiki kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utaondoa serikali zote za wanadamu?’ w23.08 11 ¶13-14
Jumamosi, Februari 15
Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.—Rom. 14:12.
Uwe mwenye kiasi na kukubali kwamba huenda usiweze kutimiza mengi kwa sababu ya umri, afya, au hali zako. Kama Barzilai, uwe tayari kukataa mapendeleo fulani ikiwa hali yako ya kimwili inakuzuia kutimiza mapendeleo hayo. (2 Sam. 19:35, 36) Kama Musa, kubali msaada na uwape wengine majukumu inapofaa. (Kut. 18:21, 22) Kuwa mwenye kiasi kutakusaidia usiwe na matarajio yasiyo halisi ambayo yanaweza kukufanya uchoke. Pia, hatupaswi kuhisi kwamba tunawajibika kwa sababu ya maamuzi mabaya ambayo wengine wanafanya. Hatuwezi kuwafanyia wengine maamuzi; wala hatuwezi sikuzote kuwalinda wasipatwe na matokeo ya maamuzi mabaya wanayofanya. Kwa mfano, huenda mwana au binti akaamua kuacha kumtumikia Yehova. Uamuzi huo unaweza kuwasababishia wazazi wake huzuni nyingi. Hata hivyo, wazazi ambao wanajilaumu kwa sababu ya uamuzi mbaya wa mtoto wao, wanabeba mzigo mzito sana. Yehova hataki wabebe mzigo huo. w23.08 29 ¶11-12
Jumapili, Februari 16
[Samsoni] akampenda mwanamke fulani . . . aliyeitwa Delila.—Amu. 16:4.
Samsoni alikuwa mwanadamu asiye mkamilifu kama sisi, basi wakati mwingine alifanya maamuzi mabaya. Uamuzi mmoja aliofanya hasa ulisababisha matokeo mabaya sana. Baada ya Samsoni kutumikia akiwa mwamuzi kwa muda fulani, “akampenda mwanamke fulani katika Bonde la Soreki, aliyeitwa Delila.” Hapo awali, Samsoni alikuwa amemchumbia mwanamke Mfilisti, lakini Yehova ndiye ‘aliyeongoza jambo hilo’ kwa sababu “alikuwa akitafuta nafasi ya kuwapiga Wafilisti.” Baadaye, Samsoni alikaa katika nyumba ya kahaba katika jiji la Wafilisti lililoitwa Gaza. Katika pindi hiyo, Mungu alimwezesha Samsoni kung’oa na kubeba malango ya jiji hilo, na kuliacha bila ulinzi. (Amu. 14:1-4; 16:1-3) Hata hivyo, kisa cha Delila kilikuwa tofauti kwa sababu inaelekea kwamba alikuwa Mwisraeli. Delila alikubali kiasi kikubwa cha pesa kutoka kwa Wafilisti ili amsaliti Samsoni. w23.09 5 ¶12-13
Jumatatu, Februari 17
Ufahamu wa mtu hakika hutuliza hasira yake.—Met. 19:11.
Ufahamu unaweza kutusaidia kuwa wapole. Mtu mwenye ufahamu anajizuia watu wanapopinga mambo anayoamini. Baadhi ya maswali ni kama sehemu ndogo inayoonekana ya barafu baharini, huku sehemu kubwa ya barafu ikiwa imefichwa ndani ya bahari. Kwa mfano, huenda mtu akatuuliza swali lakini hatujui sababu iliyomfanya atuulize swali hilo. Basi kabla ya kujibu, ni vizuri kutambua kwamba huenda hatujui sababu iliyomfanya mtu huyo atuulize swali hilo. (Met. 16:23) Fikiria jinsi Gideoni alivyowajibu wanaume wa Efraimu. Kwa hasira walimuuliza kwa nini hakuwaita mapema wajiunge naye alipokuwa akipigana na maadui wa Israeli. Lakini ni sababu gani isiyo wazi ambayo ilifanya wawe na hasira? Je, walihisi kwamba wamedharauliwa? Vyovyote vile, kwa hekima Gideoni alionyesha kwamba alielewa hisia zao na akawajibu kwa upole. Matokeo yalikuwaje? Walitulia na “hasira yao ikapoa.”—Amu. 8:1-3. w23.09 16 ¶8-9
Jumanne, Februari 18
Mimi ndiye aliyenipenda sana siku baada ya siku.—Met. 8:30
Uhusiano wa Yehova na Yesu ni uhusiano wa karibu zaidi kati ya baba na mwana. Bila shaka, Yehova aliumia sana alipoona Mwana wake akitendewa kwa njia isiyofaa, akikataliwa, na kuteswa. Mzazi yeyote aliyefiwa na mtoto anaelewa vizuri hisia kali za huzuni zinazotokana na kifo cha mtoto. Tuna imani yenye nguvu katika ufufuo, lakini hilo haliondoi maumivu tunayohisi tunapofiwa na mtu tunayempenda. Mfano huo, unatusaidia kuelewa jinsi Yehova alivyohisi alipoona Mwana wake mpendwa akiteseka na kufa katika majira ya kuchipua ya mwaka wa 33 W.K. (Mt. 3:17) Kuanzia sasa hadi wakati wa Ukumbusho, jitahidi kujifunza zaidi kuhusu fidia kwenye funzo lako la kibinafsi au katika Ibada ya Familia. Na katika siku ya Ukumbusho, usisahau kutazama programu ya pekee ya Ibada ya Asubuhi. Tunapotayarisha moyo wetu kwa ajili ya Ukumbusho, tutaweza kuwasaidia wengine wanufaike pia na Ukumbusho.—Ezra 7:10. w24.01 11 ¶10-12
Jumatano, Februari 19
Atawatia nguvu.—1 Pet. 5:10.
Njia moja ambayo tunaweza kupokea nguvu kutoka kwa Yehova ni kwa kusali kwake. Yehova anajibu sala zetu kwa kutupatia “nguvu zinazopita zile za kawaida.” (2 Kor. 4:7) Pia, tunaweza kutiwa nguvu kwa kusoma Neno lake na kulitafakari. (Zab. 86:11) Ujumbe ambao Yehova ametupatia katika Biblia ni ‘wenye nguvu.’ (Ebr. 4:12) Unaposali kwa Yehova na kusoma Neno lake, utapata nguvu unazohitaji ili uendelee kuvumilia, kudumisha shangwe yako, na kutimiza mgawo mgumu. Ona jinsi Yehova alivyomtia nguvu nabii Yona. Yona alikuwa amekimbia mgawo mgumu ambao Yehova alikuwa amempa. Matokeo ni kwamba alikuwa karibu kupoteza uhai wake katika dhoruba kali sana na alihatarisha uhai wa wasafiri wenzake katika meli. Alipotupwa baharini, alijikuta mahali ambapo hakuwahi kufika kabla ya hapo—alikuwa gizani ndani ya tumbo la samaki mkubwa. Yona alifanya nini ili apate nguvu akiwa katika tumbo la samaki? Alisali.—Yona 2:1, 2, 7. w23.10 13 ¶4-6
Alhamisi, Februari 20
Mwisho wa mambo yote umekaribia.—1 Pet. 4:7.
Ingawa mtume Petro aliwaandikia barua Wakristo wa karne ya kwanza, Yehova alitia ndani barua hizo katika Neno Lake. Basi, leo tunaweza kunufaika na barua hizo. (Rom. 15:4) Tumezungukwa na watu ambao hawaamini unabii wa Biblia. Huenda wapinzani wakatudhihaki kwa sababu kwa miaka mingi tumekuwa tukisema kwamba mwisho unakaribia. Baadhi ya watu husema kwamba mwisho hautakuja kamwe. (2 Pet. 3:3, 4) Tukisikia maneno kama hayo kutoka kwa mtu tunayemhubiria, mfanyakazi mwenzetu, au mtu wa familia yetu, imani yetu inaweza kutikiswa. Petro alieleza jambo linaloweza kutusaidia. Huenda baadhi ya watu wakahisi kwamba Yehova anakawia kuleta mwisho wa mfumo huu wa mambo. Maneno ya Petro yanaweza kutusaidia kudumisha mtazamo unaofaa, kwa sababu yanatukumbusha kwamba maoni ya Yehova kuhusu wakati yanatofautiana sana na maoni ya wanadamu. (2 Pet. 3:8, 9) Kwa Yehova miaka elfu ni kama siku moja. Yehova ni mwenye subira kwa sababu hataki yeyote aangamizwe. Hata hivyo, mfumo huu utafikia mwisho, siku yake itakapofika. w23.09 26-27 ¶2-5
Ijumaa, Februari 21
Ni lazima tuyakazie uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo tuliyosikia, ili tusipeperushwe kamwe.—Ebr. 2:1.
Kwa nini mtume Paulo aliwaandikia barua Wakristo Waebrania huko Yudea? Inaelekea ni kwa sababu mbili kuu. Kwanza, ili kuwatia moyo. Wengi wao walishirikiana na dini ya Kiyahudi kabla ya kuwa Wakristo. Huenda viongozi wa dini ya Kiyahudi waliwadhihaki kwa kuwa Wakristo. Kwa nini? Kwa sababu Wakristo hawakuwa na hekalu la kifahari ambamo wangeabudu, na hawakuwa na madhabahu ambayo wangetumia kumtolea Mungu dhabihu, wala hawakuwa na makuhani wa kuwahudumia. Huenda hilo lingewavunja moyo Wanafunzi wa Kristo na kudhoofisha imani yao. (Ebr. 3:12, 14) Hata huenda baadhi yao walishawishiwa kurudi katika dini ya Kiyahudi. Pili, Paulo aliwaambia Wakristo hao Waebrania kwamba hawakuwa wakijitahidi kuelewa mafundisho mapya au mafundisho ya kiroho yenye kina, yaani, “chakula kigumu” kinachopatikana katika Neno la Mungu. (Ebr. 5:11-14) Inaonekana kwamba bado baadhi yao walikuwa wakifuata Sheria ya Musa. w23.10 24-25 ¶3-4
Jumamosi, Februari 22
[Watendee] wanawake vijana kama dada, kwa usafi wote wa kiadili.—1 Tim. 5:2.
Baadhi ya wanawake wamechagua kutoolewa. (Mt. 19:10-12) Uwe na hakika kwamba Yehova na Yesu wanawathamini Wakristo waseja. Ulimwenguni kote, dada waseja ni mfano mzuri katika makutaniko. Upendo wao kwa wengine na jinsi wanavyowahangaikia kutoka moyoni kunawachochea wanawake hao Wakristo wawe dada na mama wa kiroho kwa wengi. (Marko 10:29, 30) Baadhi wamekuwa watumishi wa wakati wote. Wanawake Wakristo wanatimiza sehemu kubwa katika kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. (Zab. 68:11) Je, unaweza kupanga sasa kuingia katika utumishi wa wakati wote? Unaweza kutumikia ukiwa painia, mjenzi, au Mwanabetheli. Sali kuhusu lengo lako. Zungumza na wale ambao wamefikia lengo kama hilo, na ujifunze unapaswa kufanya nini ili ustahili. Kisha panga mipango hususa. Kufikia lengo lako kutakufungulia nafasi nyingi zenye kusisimua katika utumishi wa Yehova. w23.12 22 ¶16-17
Jumapili, Februari 23
Lazima habari njema ihubiriwe kwanza.—Marko 13:10.
Kwa kuwa dhiki kuu inakaribia, tunatambua jinsi ilivyo muhimu sana kutii amri ya kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, huenda ikawa vigumu kukazia fikira huduma yetu ikiwa tunakabili hali ngumu ya kiuchumi au upinzani katika kazi yetu ya kuhubiri. Ni nini kitakachotusaidia kutanguliza masilahi ya Ufalme? Kuendelea kuwa na uhakika kwamba “Yehova wa majeshi” yuko upande wetu. Atatutegemeza ikiwa tutaendelea kutanguliza masilahi ya Ufalme badala ya masilahi yetu. Hivyo, hatuhitaji kuogopa chochote. (Hag. 2:4) Yehova anataka tukazie fikira kazi ya kufanya wanafunzi inayookoa uhai. Hagai aliwasihi watu wa Yehova waanze upya utumishi wao mtakatifu. Ikiwa wangefanya hivyo, Yehova aliahidi ‘kuwaletea baraka.’ (Hag. 2:18, 19) Sisi pia tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zetu ikiwa tutatanguliza kazi aliyotuagiza kufanya. w23.11 16 ¶8; 17 ¶11
Jumatatu, Februari 24
Wote wamefanya dhambi.—Rom. 3:23.
Katika barua yake kwa Waroma, mtume Paulo alisema kwamba wanadamu wote ni watenda dhambi. Basi, inawezekanaje kwa mtu kuonwa kuwa mwadilifu au asiye na hatia na hivyo kupata kibali cha Mungu? Ili kuwasaidia Wakristo wote wanyoofu kujibu swali hilo, Paulo alitumia mfano wa Abrahamu. Yehova alimtangaza Abrahamu kuwa mwadilifu alipokuwa akiishi katika nchi ya Kanaani. Kwa nini Yehova aliweza kumtangaza Abrahamu kuwa mwadilifu? Je, ni kwa sababu Abrahamu alishika kikamili Sheria ya Musa? La hasha. (Rom. 4:13) Taifa la Israeli lilipewa Sheria hiyo zaidi ya miaka 400 baada ya Mungu kumtangaza Abrahamu kuwa mwadilifu. Basi, ni kwa msingi gani Mungu alimtangaza Abrahamu kuwa mwadilifu? Kupitia fadhili Zake zisizostahiliwa, Yehova alimtangaza Abrahamu kuwa mwadilifu kwa sababu ya imani yake.—Rom 4:2-4. w23.12 3 ¶4-5
Jumanne, Februari 25
Fanya jambo lolote lililo moyoni mwako.—1 Nya. 17:2.
Usiku huohuo ambao nabii Nathani alisema maneno hayo kwa Mfalme Daudi, Yehova alimwambia Nathani kwamba Daudi hangejenga hekalu. (1 Nya. 17:3, 4, 11, 12) Daudi alitendaje alipopokea ujumbe huo? Alikazia fikira kukusanya pesa na vifaa ambavyo mwanaye, Sulemani, angehitaji kwa ajili ya mradi huo. (1 Nya. 29:1-5) Mara tu baada ya kumjulisha Daudi kwamba si yeye ambaye angejenga hekalu, Yehova alifanya agano pamoja naye. Yehova alimwahidi Daudi kwamba mmoja wa wazao wake angetawala milele. (2 Sam. 7:16) Katika ulimwengu mpya, wazia jinsi Daudi atakavyofurahi kujua kwamba anafurahia maisha chini ya Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Yesu, Mfalme aliyetokana na familia yake! Simulizi hili linatusaidia kuona kwamba hata ikiwa hatuwezi kutimiza yote tuliyotarajia kufanya katika utumishi wa Yehova, huenda Mungu wetu akatubariki kwa njia nyingine ambazo hatungetarajia kamwe. w23.04 16 ¶8-10
Jumatano, Februari 26
Yehova hatawaacha watu wake.—Zab. 94:14.
Huenda ukaona kwamba sehemu fulani hususa za Biblia zinaweza kukufariji hasa unapoogopa. Kwa mfano, unaweza kupata faraja katika kitabu cha Ayubu, Zaburi, Methali, na pia maneno ya Yesu yanayopatikana katika Mathayo sura ya 6. Kadiri unavyosali kwa Yehova na kusoma Neno lake, ndivyo utakavyohisi faraja yake. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakuwa pamoja nasi tunapopitia hali ngumu maishani. Kamwe hatutakuwa peke yetu. (Zab. 23:4) Yehova anaahidi kutulinda, kutuimarisha, kututegemeza, na kutufariji. Isaya 26:3 inasema hivi kumhusu Yehova: “Utawalinda wale wanaokutegemea kikamili; utawapa amani inayodumu, kwa sababu wanakutumaini wewe.” Kwa hiyo, mtumaini Yehova, na utumie njia anazoandaa ili kukusaidia. Ukifanya hivyo, utapata nguvu tena hata wakati wa hali ngumu. w24.01 25 ¶16-17
Alhamisi, Februari 27
Hakuna silaha yoyote itakayotokezwa dhidi yako itakayofanikiwa.—Isa. 54:17.
Maneno hayo yaliyoongozwa na roho katika andiko la leo yanatimia leo. Pia, maneno yafuatayo yenye kufariji yanahusu nyakati zetu: “Wana wako wote watafundishwa na Yehova, na amani ya wana wako itakuwa nyingi. Utaimarishwa kabisa katika uadilifu. . . . Hutaogopa chochote na hutakuwa na sababu yoyote ya kuhofu, kwa maana haitakukaribia.” (Isa. 54:13, 14) Hata Shetani, “mungu wa mfumo huu wa mambo,” hana uwezo wa kuzuia kazi ya kutoa elimu inayofanywa na watu wa Yehova. (2 Kor. 4:4) Ibada safi imerudishwa, na haitachafuliwa tena kamwe. Itadumu kwa umilele wote. Hakuna silaha yoyote itakayotokezwa dhidi yetu itakayofanikiwa! w24.02 4 ¶10
Ijumaa, Februari 28
Yeyote anayempenda baba au mama kuliko anavyonipenda hanistahili.—Mt. 10:37.
Tukiwa Wakristo, tunachukua kwa uzito nadhiri tuliyotoa tulipojiweka wakfu kwa Yehova. Hilo linaongoza maamuzi na matendo yetu inapohusu masuala ya kifamilia. Tunatimiza kwa bidii majukumu yetu ya Kimaandiko inapohusu familia, lakini sikuzote tunatanguliza matakwa ya Yehova, badala ya maoni ya watu wa familia. (Mt. 10:35, 36; 1 Tim. 5:8) Nyakati nyingine, huenda hilo likamaanisha kudhabihu kwa kadiri fulani amani pamoja na watu wetu wa ukoo ili kumfurahisha Yehova. Alianzisha mpango wa familia, na anataka tuwe na familia yenye furaha. (Efe. 3:14, 15) Ikiwa tunataka kuwa na furaha ya kweli, tunahitaji kufanya mambo kwa njia ya Yehova. Kamwe usitilie shaka kwamba Yehova anathamini jitihada zako za kujidhabihu unapomwabudu huku ukiitunza familia yako na kuwatendea kwa upendo na heshima.—Rom. 12:10. w24.02 18 ¶11, 13