Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • es25 kur. 7-17
  • Januari

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Januari
  • Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025
  • Vichwa vidogo
  • Jumatano, Januari 1
  • Alhamisi, Januari 2
  • Ijumaa, Januari 3
  • Jumamosi, Januari 4
  • Jumapili, Januari 5
  • Jumatatu, Januari 6
  • Jumanne, Januari 7
  • Jumatano, Januari 8
  • Alhamisi, Januari 9
  • Ijumaa, Januari 10
  • Jumamosi, Januari 11
  • Jumapili, Januari 12
  • Jumatatu, Januari 13
  • Jumanne, Januari 14
  • Jumatano, Januari 15
  • Alhamisi, Januari 16
  • Ijumaa, Januari 17
  • Jumamosi, Januari 18
  • Jumapili, Januari 19
  • Jumatatu, Januari 20
  • Jumanne, Januari 21
  • Jumatano, Januari 22
  • Alhamisi, Januari 23
  • Ijumaa, Januari 24
  • Jumamosi, Januari 25
  • Jumapili, Januari 26
  • Jumatatu, Januari 27
  • Jumanne, Januari 28
  • Jumatano, Januari 29
  • Alhamisi, Januari 30
  • Ijumaa, Januari 31
Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025
es25 kur. 7-17

Januari

Jumatano, Januari 1

Kulikuwa na watu waliokuwa wamebeba maiti wakiipeleka nje, yule aliyekufa alikuwa mwana pekee, na mama yake alikuwa mjane.—Luka 7:12.

Yesu ‘alimwona’ yule mama aliyekuwa akiomboleza kisha “akamsikitikia.” (Luka 7:13) Lakini Yesu hakuwa tu na hisia za kumsikitikia yule mama; alimwonyesha pia huruma. Alizungumza naye, bila shaka kwa sauti yenye kufariji, na kumwambia: “Acha kulia.” Kisha akachukua hatua na kufanya jambo fulani. Alimfufua mwana huyo na “akamkabidhi kwa mama yake.” (Luka 7: 14, 15) Tunaweza kujifunza nini kutokana na muujiza wa Yesu wa kumfufua mwana wa mjane? Tunajifunza somo la kuwaonyesha huruma wale wanaoomboleza. Kama Yesu, tunaweza kusitawisha huruma kuwaelekea wale wanaoomboleza kwa kuwa macho. Tunaweza kuchukua hatua ya kwanza kuonyesha huruma kwa kusema na kufanya mambo tunayoweza ili kuwasaidia na kuwafariji. (Met. 17:17; 2 Kor. 1:​3, 4; 1 Pet. 3:8) Hata maneno rahisi na matendo madogo ya fadhili yanaweza kuwafariji sana. w23.04 5-6 ¶13-15

Alhamisi, Januari 2

Lengo la ugonjwa huu si kusababisha kifo, bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu.—Yoh. 11:4.

Ingawa Yesu alijua kwamba rafiki yake amekufa, alibaki mahali alipokuwa kwa siku mbili zaidi, kisha akaanza safari ya kwenda Bethania. Basi, wakati ambao Yesu aliwasili, Lazaro alikuwa amekufa kwa siku nne. Yesu alikusudia kufanya jambo ambalo lingewanufaisha rafiki zake na kumtukuza Mungu. (Yoh. 11:​6, 11, 17) Tunajifunza somo kuhusu urafiki kutokana na simulizi hilo. Fikiria jambo hili: Maria na Martha walipotuma ujumbe kwa Yesu, hawakumwomba aje Bethania. Walisema tu kwamba rafiki yake mpendwa alikuwa mgonjwa. (Yoh. 11:3) Lazaro alipokufa, Yesu angeweza kumfufua hata akiwa mbali. Ingawa hivyo, Yesu aliamua kwenda Bethania ili awe pamoja na rafiki zake, Maria na Martha. Je, una rafiki anayeweza kukusaidia bila kumwomba msaada? Basi, unajua kwamba unaweza kumtegemea akusaidie “nyakati za taabu.” (Met. 17:17) Kama Yesu, acheni tuwe rafiki kama huyo kwa wengine! w23.04 10 ¶10-11

Ijumaa, Januari 3

Yule aliyeahidi ni mwaminifu.—Ebr. 10:23.

Tunapokabiliana na jaribu, huenda tukahisi kwamba ulimwengu mpya wa Yehova hautakuja kamwe. Je, hilo linamaanisha kwamba imani yetu ni dhaifu? Si lazima iwe hivyo. Fikiria mfano ufuatao. Katikati ya majira ya baridi kali sana, huenda tukahisi kwamba majira ya joto hayatafika kamwe. Hata hivyo, sikuzote majira ya joto hufika. Vivyo hivyo, tunapokuwa tumevunjika moyo sana, huenda tukahisi kwamba ulimwengu mpya hautakuja kamwe. Hata hivyo, ikiwa tuna imani yenye nguvu tunajua kwamba ahadi za Mungu zitatimia. (Zab. 94:​3, 14, 15; Ebr. 6:​17-19) Tukiwa na uhakika huo, tunaweza kuendelea kutanguliza ibada ya Yehova maishani mwetu. Pia, tunahitaji imani yenye nguvu tunapofanya kazi ya kuhubiri. Watu wengi wanafikiri kwamba “habari njema” kuhusu ulimwengu mpya wa Mungu unaokuja ni jambo lisilowezekana. (Mt. 24:14; Eze. 33:32) Usiruhusu kamwe mtazamo wao wa kuwa na shaka utuathiri. Ili tusiathiriwe na mtazamo huo, tunapaswa kuendelea kuimarisha imani yetu. w23.04 27 ¶6-7; 28 ¶14

Jumamosi, Januari 4

Tunajua kwamba tutapata mambo tuliyomwomba, kwa kuwa tumeyaomba kwake.—1 Yoh. 5:15.

Je, umewahi kujiuliza ikiwa kweli Yehova anajibu sala zako? Ikiwa ndivyo, huko peke yako. Ndugu na dada wengi wamejiuliza swali hilo, hasa wanapokabiliana na hali ngumu. Ikiwa tunateseka, huenda ikiwa vigumu zaidi kwetu kutambua jinsi Yehova anavyojibu sala zetu. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anajibu sala za waabudu wake? Maandiko yanatuhakikishia kwamba Yehova anatupenda sana na kwamba sisi ni wenye thamani kwake. (Hag. 2:7; 1 Yoh. 4:10) Ndiyo sababu anatukaribisha tumwombe msaada kupitia sala. (1 Pet. 5:​6, 7) Anataka kutusaidia tuendelee kuwa karibu naye na tufanikiwe kuvumilia hali ngumu tunazokabili. Katika Biblia, mara nyingi tunasoma kwamba Yehova alijibu sala za waabudu wake. Je, unaweza kufikiria mfano wowote? w23.05 8 ¶1-4

Jumapili, Januari 5

Maria akasema: “Nafsi yangu inamtukuza Yehova.”—Luka 1:46.

Maria alikuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova, na imani yake haikutegemea mambo ambayo Yosefu alikuwa anafanya. Maria aliyafahamu Maandiko vizuri. Pia, alitenga muda ili atafakari. (Luka 2:​19, 51) Bila shaka, Maria alikuwa mke bora kwa sababu alikuwa na urafiki wa karibu pamoja na Yehova. Leo, wake wengi hujitahidi kumwiga Maria. Kwa mfano, Dada anayeitwa Emiko anasema hivi: “Nilipokuwa mseja nilikuwa na ratiba ya kibinafsi ya mambo ya kiroho. Lakini baada ya kufunga ndoa, nilitambua kwamba kwa kuwa mume wangu alikuwa akisali kwa niaba yetu na kuongoza ibada ya familia, imani yangu ilitegemea mambo aliyofanya. Nilitambua kwamba mimi mwenyewe nilihitaji kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Basi, sasa ninatenga wakati wa kuwa pamoja na Mungu wangu—ili kusali, kusoma Maandiko, na kutafakari kuhusu mawazo yake.” (Gal. 6:5) Mke, unapoendelea kuimarisha urafiki wako pamoja na Yehova, mume wako atakuwa na sababu nyingi hata zaidi za kukusifu na kukupenda.—Met. 31:30. w23.05 22 ¶6

Jumatatu, Januari 6

Nitawafundisha kumwogopa Yehova.—Zab. 34:11.

Hatuzaliwi tukiwa na woga kumwelekea Yehova; tunapaswa kusitawisha woga huo. Njia moja ya kusitawisha woga huo ni kwa kuchunguza uumbaji. Kadiri tunavyoona hekima, nguvu, na upendo mwingi wa Mungu kutuelekea kupitia “vitu vilivyoumbwa,” ndivyo tunavyomheshimu na kumpenda zaidi. (Rom. 1:20) Njia nyingine ambayo tunaweza kusitawisha woga kumwelekea Mungu ni kwa kusali kwa ukawaida. Kadiri tunavyosali, ndivyo Yehova anavyozidi kuwa halisi kwetu. Kila mara tunapomwomba atuimarishe ili tuvumilie jaribu fulani, tunakumbuka kwamba ana nguvu nyingi sana. Tunapomshukuru kwa ajili ya zawadi ya Mwana wake, tunakumbuka kwamba Yehova anatupenda. Na tunapomsihi Yehova atusaidie kushughulikia tatizo fulani, tunakazia kwenye mioyo yetu kwamba yeye ni mwenye hekima. Sala kama hizo hutusaidia kumheshimu Yehova hata zaidi na zinaimarisha azimio letu la kuepuka kufanya jambo lolote ambalo litaharibu uhusiano wetu pamoja naye. w23.06 15 ¶6-7

Jumanne, Januari 7

Yehova ni Mpaji-sheria wetu.—Isa. 33:22.

Sikuzote Yehova amewapa watu wake sheria zilizo wazi. Kwa mfano, katika karne ya kwanza, baraza linaloongoza lilitaja njia tatu ambazo Wakristo wanapaswa kuendelea kuwa imara: (1) kwa kuepuka ibada ya sanamu, na kumwabudu Yehova peke yake, (2) kwa kuheshimu utakatifu wa damu, na (3) kwa kutii viwango vya juu vya maadili vilivyo katika Biblia. (Mdo. 15:​28, 29) Leo, Wakristo wanawezaje kudumisha msimamo imara katika njia hizo tatu? Kwa kumwabudu na kumtii Yehova. Aliwaamuru Waisraeli wamwabudu yeye peke yake. (Kum. 5:​6-10) Yesu alipojaribiwa na Ibilisi, alisema waziwazi tunapaswa kumwabudu Yehova peke yake. (Mt. 4:​8-10) Kwa hiyo, hatuabudu sanamu za kidini. Pia, hatuabudu wanadamu—iwe ni viongozi wa kidini, watawala wa kisiasa, au watu maarufu katika michezo na burudani—na hatuwatendei kama miungu. Tunamwabudu yule ‘aliyeumba vitu vyote.’—Ufu. 4:11. w23.07 14-15 ¶3-4

Jumatano, Januari 8

Kwa kumwogopa Yehova mtu hujiepusha na uovu.—Met. 16:6.

Ulimwengu wa Shetani unakazia sana uasherati na ponografia. (Efe. 4:19) Basi, ni lazima tuendelee kusitawisha woga kumwelekea Mungu na kujiepusha na uovu. Methali sura ya 9, inalinganisha hekima na upumbavu, na wanawake wawili wa mfano. Kila mmoja anatoa mwaliko kwa wajinga, yaani, wale “wasio na busara.” Ni kana kwamba kila mwanamke anasema hivi, ‘Karibu nyumbani kwangu tule chakula.’ (Met. 9:​1, 4-6) Lakini kila mwaliko una matokeo yaliyo tofauti sana. Fikiria mwaliko unaotoka kwa “mwanamke mpumbavu.” (Met. 9:​13-18) Kwa ujasiri na kwa sauti kubwa anawaambia hivi wale wasio na busara, ‘Njooni hapa’ mle chakula. Wanapatwa na matokeo gani? “Wale waliokufa ambao hawana uwezo wako hapo.” Tunaonywa kuhusu “mwanamke aliyepotoka” na “mwanamke mwasherati.” Tunaambiwa hivi: “Nyumba yake huzama katika kifo.” (Met. 2:​11-19) Methali 5:​3-10 inatoa onyo kuhusu ‘mwanamke mwingine aliyepotoka’ ambaye “miguu yake hushuka kwenye kifo.” w23.06 21-22 ¶6-7

Alhamisi, Januari 9

Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.—Flp. 4:5.

Wazee wa kutaniko wanapaswa kuweka mfano mzuri kuhusu usawaziko. (1 Tim. 3:​2, 3) Kwa mfano, mzee hapaswi kutarajia kwamba sikuzote maoni yake yatakubaliwa kwa sababu tu ana umri mkubwa kuliko wazee wengine. Anatambua kwamba roho ya Yehova inaweza kumchochea mzee yeyote katika baraza la wazee atoe mapendekezo ambayo yatachangia kufanya uamuzi wenye hekima. Na ikiwa hakuna kanuni ya Biblia inayovunjwa, wazee wenye usawaziko huunga mkono kwa hiari uamuzi wa wazee wengi katika baraza, hata ingawa walikuwa na pendekezo tofauti. Wakristo wanapata baraka nyingi wanapokuwa na usawaziko. Tunakuwa na uhusiano mzuri zaidi na ndugu na dada zetu, na kutaniko linafurahia amani. Tunafurahia kushirikiana na watu wenye nyutu na tamaduni mbalimbali miongoni mwa waabudu wa Yehova wenye umoja. Zaidi ya yote, tunafurahi kujua kwamba tunamwiga Yehova, Mungu wetu mwenye usawaziko. w23.07 25 ¶16-17

Ijumaa, Januari 10

Wale walio na ufahamu wataelewa.—Dan. 12:10.

Danieli alichunguza unabii akiwa na nia nzuri, alitaka kujua ukweli. Pia, Danieli alikuwa mnyenyekevu, alitambua kwamba Yehova huwapatia uelewaji wale wanaomfahamu na wanaoishi kulingana na viwango vyake safi. (Dan. 2:​27, 28) Danieli alithibitisha kwamba alikuwa mnyenyekevu kwa kumtegemea Yehova ili amsaidie. (Dan. 2:18) Pia, Danieli alijifunza kwa makini. Alifanya utafiti katika Maandiko yaliyoongozwa na roho ambayo yalipatikana wakati huo. (Yer. 25:​11, 12; Dan. 9:2) Unawezaje kumwiga Danieli? Chunguza nia yako. Je, unajifunza unabii wa Biblia kwa sababu unatamani sana kujua ukweli? Ikiwa ndivyo, Yehova atakusaidia. (Yoh. 4:​23, 24; 14:​16, 17) Baadhi yao hujifunza wakitumaini watapata uthibitisho unaoonyesha kwamba Biblia haijaongozwa na roho ya Mungu. Wanapofanya hivyo, wanahisi kwamba wana haki ya kujiwekea viwango vyao wenyewe kuhusu mambo yanayofaa na yasiyofaa na kuishi kulingana na viwango hivyo. Hata hivyo, tunahitaji kujifunza tukiwa na nia nzuri. w23.08 9 ¶7-8

Jumamosi, Januari 11

Ukivunjika moyo . . . , nguvu zako zitakuwa chache.—Met. 24:10.

Tunaweza kujiongezea mzigo mzito kwa kuwa na matarajio yasiyo halisi ikiwa tutajilinganisha na wengine. (Gal. 6:4) Ikiwa tutajilinganisha na wengine, tunaweza kuanza kuoneana wivu na kushindana. (Gal. 5:26) Ili kujaribu kufanya mambo ambayo wengine wametimiza, huenda tukajitahidi sana kufanya mambo yanayopita uwezo wetu, au ambayo yanazidi hali zetu. Na kwa kuwa “matarajio yaliyoahirishwa hufanya moyo uwe mgonjwa,” tutavunjika moyo hata zaidi ikiwa tutajiwekea matarajio ambayo hatuwezi kamwe kuyatimiza! (Met. 13:12) Kufanya hivyo, kunaweza kufanya tuchoke na kupunguza mwendo katika mbio zetu za uzima. Usitarajie kutimiza mengi kuliko yale ambayo Yehova anataka ufanye. Hatarajii kamwe umpe kile ambacho huna. (2 Kor. 8:12) Uwe na uhakika kwamba Yehova halinganishi mambo unayofanya na yale ambayo wengine wanafanya. (Mt. 25:​20-23) Anathamini utumishi wako wa moyo wote, uaminifu wako, na uvumilivu wako. w23.08 29 ¶10-11

Jumapili, Januari 12

Je, sasa nife kwa kiu?—Amu. 15:18.

Yehova alijibu kilio cha Samsoni cha kuomba msaada kwa kumwandalia maji kimuujiza. Samsoni alipokunywa maji hayo, “nguvu zake zikamrudia akapata nguvu tena.” (Amu. 15:​19, maelezo ya chini) Inaonekana kwamba chemchemi hiyo ya maji ilikuwepo miaka mingi baadaye nabii Samweli alipoongozwa na roho kuandika kitabu cha Waamuzi. Waisraeli waliojionea maji hayo yakitiririka huenda walikumbuka kwamba ikiwa watamtegemea, Yehova atawasaidia waabudu wake waaminifu wakati wa uhitaji. Sisi pia tunahitaji kumtegemea Yehova ili kupata msaada hata iwe tuna vipawa au uwezo gani, au licha ya mambo ambayo tumetimiza katika utumishi wake. Tunapaswa kuwa wenye kiasi na kukubali kwamba tunaweza kupata mafanikio ya kweli ikiwa tu tutamtegemea Yehova. Kama vile Samsoni alivyotiwa nguvu alipokunywa maji ambayo Yehova alimwandalia, sisi pia tutatiwa nguvu kiroho ikiwa tutatumia maandalizi yote ambayo Yehova anatuandalia.—Mt. 11:28. w23.09 4 ¶8-10

Jumatatu, Januari 13

Jibu la upole hutuliza hasira, lakini neno kali huchochea hasira.—Met. 15:1.

Tunaweza kufanya nini tunapochokozwa, kwa mfano mtu fulani anaposema mambo mabaya kumhusu Mungu au kudhihaki Biblia? Tunapaswa kumwomba Yehova roho yake na hekima yake ili tujibu kwa njia ya upole. Namna gani ikiwa baadaye tunatambua kwamba hatukuitikia kwa njia nzuri? Tunaweza kusali tena kuhusu jambo hilo na kufikiria jinsi tunavyoweza kutenda vizuri zaidi pindi nyingine. Naye Yehova atatupatia roho yake takatifu ili tuweze kudhibiti hasira yetu na kuonyesha upole. Baadhi ya mistari ya Biblia inaweza kutusaidia kudhibiti usemi wetu tunapokabiliana na hali ngumu. Roho ya Mungu inaweza kutukumbusha maandiko hayo. (Yoh. 14:26) Kwa mfano, kanuni tunazopata katika kitabu cha Methali zinaweza kutusaidia kuwa wapole. (Met. 15:18) Kitabu hicho cha Biblia kinaonyesha manufaa ya kuwa watulivu tunapokabili hali zenye mkazo.—Met. 10:19; 17:27; 21:23; 25:15. w23.09 15 ¶6-7

Jumanne, Januari 14

Sikuzote ninakusudia kuwakumbusha mambo haya.—2 Pet. 1:12.

Mtume Petro alijua kwamba alikuwa anakaribia kufa. Katika kipindi cha miaka mingi ambacho alitumikia kwa uaminifu, alishirikiana na Yesu, alianza kuhubiri katika maeneo mapya, na akatumikia akiwa mshiriki wa baraza linaloongoza. Lakini bado alikuwa na kazi ya kufanya. Karibu mwaka wa 62-64 W.K., aliongozwa na roho kuandika barua mbili—kitabu cha 1 na cha 2 cha Petro katika Biblia. (2 Pet. 1:​13-15) Petro aliandika barua zake zilizoongozwa na roho wakati ambao Wakristo wenzake walikuwa ‘wamehuzunishwa kwa majaribu mbalimbali.’ (1 Pet. 1:6) Watu waovu walikuwa wakijaribu kuingiza mafundisho ya uwongo na mwenendo usio safi kutanikoni. (2 Pet. 2:​1, 2, 14) Baada ya muda mfupi Wakristo waliokuwa wakiishi huko Yerusalemu, wangekabili “mwisho wa mambo yote,” yaani, jeshi la Waroma lingeharibu jiji hilo na mifumo ya mambo ya Wayahudi. (1 Pet. 4:7) Bila shaka, barua za Petro ziliwasaidia Wakristo watambue mambo ambayo wangeweza kufanya ili kuvumilia majaribu waliyokabili wakati huo na ya wakati ujao. w23.09 26 ¶1-2

Jumatano, Januari 15

[Kristo] alijifunza kutii kutokana na mateso yaliyompata.—Ebr. 5:8.

Kama Yesu, mara nyingi tunajifunza kutii tunapokabili hali ngumu. Kwa mfano, mwanzoni mwa janga la COVID-19 tulipoambiwa tuache kukutana katika Majumba ya Ufalme na tuache kuhubiri nyumba kwa nyumba, je, ilikuwa vigumu kwako kutii? Ingawa hivyo, kwa sababu ya kutii ulipata ulinzi, ulitenda kwa umoja pamoja na waabudu wenzako, na kumfurahisha Yehova. Sasa sisi sote tuko tayari zaidi kutii mwongozo wowote ambao tutapokea wakati wa dhiki kuu. Kutii mwongozo huo kutaokoa uhai wetu! (Ayu. 36:11) Tunaamua kumtii Yehova hasa kwa sababu tunampenda na tunataka kumfurahisha. (1 Yoh. 5:3) Hatuwezi kamwe kumlipa Yehova kwa mambo yote ambayo ametufanyia. (Zab. 116:12) Lakini tunaweza kumtii yeye na pia wale walio na mamlaka juu yetu. Tunapotii, tunaonyesha kwamba sisi ni wenye hekima. Na watu wenye hekima huufanya moyo wa Yehova ushangilie.—Met. 27:11. w23.10 11 ¶18-19

Alhamisi, Januari 16

Mwabuduni Yule aliyeziumba mbingu na dunia.—Ufu. 14:7.

Ikiwa malaika angezungumza nawe, je, ungesikiliza mambo ambayo angekwambia? Leo, malaika anazungumza na “kila taifa na kabila na lugha na watu.” Anasema nini? “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu . . . Mwabuduni Yule aliyeziumba mbingu na dunia.” (Ufu. 14:​6, 7) Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli ambaye kila mtu anapaswa kumwabudu. Tunashukuru kwamba ametupatia pendeleo lenye thamani sana la kumwabudu katika hekalu lake kubwa la kiroho! Hekalu la kiroho ni nini hasa, na tunaweza kupata wapi ufafanuzi kulihusu? Hekalu la kiroho si jengo halisi. Ni mpango wa Yehova wa kumtolea ibada inayokubalika kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu. Mtume Paulo alifafanua mpango huo katika barua aliyoandikia Wakristo Waebrania katika karne ya kwanza walioishi huko Yudea. w23.10 24 ¶1-2

Ijumaa, Januari 17

“Si kwa jeshi, wala si kwa nguvu, bali kwa roho yangu,” asema Yehova.—Zek. 4:6.

Mwaka wa 522 K.W.K., maadui wa Wayahudi walifanikiwa kusababisha kazi ya kujenga upya hekalu la Yehova ipigwe marufuku. Hata hivyo, Zekaria aliwahakikishia Wayahudi kwamba Yehova angetumia roho yake yenye nguvu kuondoa vipingamizi vyovyote. Mwaka wa 520 K.W.K., Mfalme Dario aliondoa marufuku na kuwaruhusu Wayahudi waendelee na ujenzi wa hekalu na hata aliwapa pesa za kufanya hivyo. Pia, aliwaagiza magavana wa eneo hilo wawasaidie. (Ezra 6:​1, 6-10) Yehova aliwaahidi watu wake kwamba angewasaidia ikiwa wangetanguliza kazi ya kujenga upya hekalu. (Hag. 1:​8, 13, 14; Zek. 1:​3, 16) Baada ya kutiwa moyo na manabii hao, Wayahudi waliorudi walianza tena kazi ya kujenga hekalu mwaka wa 520 K.W.K. na walikamilisha kazi hiyo kabla ya miaka mitano. Kwa kuwa Wayahudi walitanguliza kufanya mapenzi ya Mungu licha ya changamoto zisizotarajiwa, Yehova aliwasaidia. Matokeo ni kwamba walimwabudu Yehova kwa shangwe.—Ezra 6:​14-16, 22. w23.11 15 ¶6-7

Jumamosi, Januari 18

Tembea kwa utaratibu katika hatua za imani ambayo baba yetu Abrahamu alikuwa nayo.—Rom. 4:12.

Ingawa watu wengi wamesikia kuhusu Abrahamu, hawajui mengi kumhusu. Hata hivyo, unajua mambo mengi kumhusu Abrahamu. Kwa mfano, unajua kwamba Biblia inasema Abrahamu alikuwa “baba ya wale wote walio na imani.” (Rom. 4:11) Hata hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Je, ninaweza kutembea katika hatua za Abrahamu na kuwa na imani kama ile aliyokuwa nayo?’ Ndiyo, unaweza. Njia moja tunayoweza kusitawisha imani kama ya Abrahamu ni kwa kujifunza kuhusu mfano wake. Sikuzote Abrahamu alifanya mambo ambayo Mungu alimwagiza. Alihamia nchi ya mbali na nyumbani kwake, aliishi kwenye mahema kwa miaka mingi, na alikuwa tayari kumtoa dhabihu mwana wake mpendwa, Isaka. Matendo hayo yalionyesha ana imani yenye nguvu. Imani na matendo ya Abrahamu yalifanya apate kibali cha Mungu na kuwa rafiki yake. (Yak. 2:​22, 23.) Yehova anataka—wewe pia—ufurahie baraka hizo. Kwa sababu hiyo, aliwaongoza waandikaji wa Biblia Paulo na Yakobo, warejelee mfano wa Abrahamu. w23.12 2 ¶1-2

Jumapili, Januari 19

Kila mtu lazima awe mwepesi wa kusikia, si mwepesi wa kusema.—Yak. 1:19.

Akina dada, sitawisheni ustadi wa kuwasiliana vizuri. Wakristo wanahitaji kuwasiliana vizuri. Kuhusu jambo hilo, mwanafunzi Yakobo alitoa ushauri unaotufaa aliposema maneno yanayopatikana katika andiko la leo. Unaposikiliza kwa makini wengine wanapozungumza unawaonyesha “hisia-mwenzi.” (1 Pet. 3:8) Ikiwa huna uhakika kama umeelewa kile ambacho mtu amesema au jinsi anavyohisi, muulize maswali kwa busara. Kisha, tua kidogo na ufikiri kabla ya kuongea. (Met. 15:​28, maelezo ya chini) Jiulize hivi: ‘Je, jambo ninalotaka kusema ni la kweli na linajenga? Je, ni maneno ya busara na fadhili?’ Jifunze kutoka kwa akina dada wakomavu wanaosikiliza kwa makini na kuzungumza kwa fadhili. (Met. 31:26) Kazia uangalifu jinsi wanavyozungumza. Ukijifunza vizuri ustadi huu, utakuwa na uhusiano mzuri na wengine. w23.12 21 ¶12

Jumatatu, Januari 20

Yeyote anayejitenga . . . hukataa hekima yote inayotumika.—Met. 18:1.

Leo, Yehova anaweza kutumia familia, marafiki, au wazee wa kutaniko ili kututegemeza. Hata hivyo, ikiwa tumeumizwa, huenda tukawa na mwelekeo wa kujitenga na wengine. Na tukataka tu kuwa peke yetu. Ni jambo la kawaida kuhisi hivyo. Tunaweza kufanya nini ili tupate utegemezo wa Yehova? Epuka kujitenga na wengine. Tunapojitenga na wengine, mara nyingi tunajikazia fikira sisi wenyewe na matatizo tunayokabili. Njia hiyo ya kufikiri inaweza kuathiri maamuzi yetu. Bila shaka, sisi sote tunahitaji wakati wa kuwa peke yetu, hasa tunapokabili hali ngumu sana. Hata hivyo, tukijitenga na wengine kwa muda mrefu, huenda tukawa tunakataa njia ambayo Yehova anatumia ili kututegemeza. Hivyo, kubali msaada wa familia, marafiki, na wazee wa kutaniko. Waone kuwa njia ya Yehova ya kukutegemeza.—Met. 17:17; Isa. 32:​1, 2. w24.01 24 ¶12-13

Jumanne, Januari 21

Hakuna wembe utakaogusa kichwa chake.—Hes. 6:5.

Wanadhiri waliweka nadhiri ya kutokata nywele zao. Hiyo ilikuwa njia ya kuonyesha wanajitiisha kikamili kwa Yehova. Kwa kusikitisha, nyakati fulani katika historia ya Israeli, Wanadhiri hawakuthaminiwa au kuungwa mkono. Wakati mwingine, Wanadhiri walihitaji kuwa jasiri sana ili washikamane na nadhiri yao na kuwa tofauti na wengine. (Amo. 2:12) Kwa sababu tunachagua kujitiisha chini ya mapenzi ya Yehova, sisi pia tunakuwa tofauti na watu wanaotuzunguka. Tunahitaji kuwa na ujasiri ili kujitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova tukiwa kazini au shuleni. Na kadiri mtazamo na mwenendo wa ulimwengu huu unavyoendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi, inaelekea ndivyo itakavyokuwa vigumu zaidi kuishi kulingana na kanuni za Biblia na kuwahubiria wengine habari njema. (2 Tim. 1:8; 3:13) Hata hivyo, sikuzote kumbuka kwamba ‘tunaufanya moyo wa Yehova ushangilie’ tunapoonyesha ujasiri na kuwa tofauti na watu ambao hawamtumikii.—Met. 27:11; Mal. 3:18. w24.02 16 ¶7; 17 ¶9

Jumatano, Januari 22

Mkaribishane.—Rom. 15:7.

Fikiria watu wa malezi mbalimbali waliokuwa katika kutaniko la Roma. Kati yao kulikuwa na Wayahudi ambao tangu utotoni walizoezwa kutii Sheria ya Musa, na pia kulikuwa na Watu wa Mataifa ambao walikuwa na malezi tofauti kabisa. Inaelekea kwamba baadhi ya Wakristo walikuwa watumwa na wengine walikuwa watu huru—au hata baadhi yao walimiliki watumwa. Wakristo hao wangeshindaje tofauti hizo na kuimarisha upendo wao? Mtume Paulo aliwahimiza ‘wakaribishane.’ Alimaanisha nini? Neno lililotafsiriwa ‘karibisha’ linamaanisha kumpokea mtu kwa fadhili, au kwa ukarimu kama vile nyumbani au katika kikundi cha marafiki. Kwa mfano, Paulo alimwambia Filemoni jinsi ya kumkaribisha Onesimo, mtumwa aliyekuwa amekimbia: “Mpokee kwa fadhili.” (Flm. 17) Na Akila na Prisila walimkaribisha Apolo ambaye hakujua mengi kuhusu Ukristo kwa ‘kumchukua’ ajiunge nao. (Mdo. 18:26) Badala ya kuruhusu watenganishwe na tofauti katika malezi yao, Wakristo hao walishinda tofauti zao na walikaribishana. w23.07 6 ¶13

Alhamisi, Januari 23

Nitamtimizia Yehova nadhiri zangu.—Zab. 116:14.

Kumpenda Yehova ndiyo sababu kuu ya kujiweka wakfu kwake. Upendo wako hautegemei hisia tu. Badala yake, unategemea “ujuzi sahihi” na “utambuzi wa kiroho,” yaani, mambo uliyojifunza kumhusu Yehova ambayo yalifanya upendo wako kwake usitawi. (Kol. 1:9) Kujifunza Maandiko kulikusadikisha kwamba (1) Yehova ni halisi, (2) Biblia ni Neno lake lililoongozwa na roho, na (3) anatumia tengenezo lake kutimiza mapenzi yake. Wale wanaojiweka wakfu kwa Yehova wanapaswa kujua mafundisho ya msingi yanayopatikana katika Neno la Mungu na kuishi kulingana na viwango vyake. Wanajitahidi kadiri wawezavyo kuwaambia wengine kuhusu mambo ambayo wamejifunza. (Mt. 28:​19, 20) Upendo wao kwa Yehova umekua, na tamaa yao ya kutoka moyoni ni kumtumikia yeye peke yake. Je, wewe unafanya hivyo? w24.03 4-5 ¶6-8

Ijumaa, Januari 24

Watakuwa mwili mmoja.—Mwa. 2:24.

Abigaili aliolewa na Nabali, ambaye Biblia inasema alikuwa mkali na mwenye tabia mbaya. (1 Sam. 25:3) Ni lazima ilikuwa vigumu sana kwa Abigaili kuishi na mwanamume huyo. Je, Abigaili alipata njia rahisi ya kutoka katika ndoa hiyo? Ndiyo, alipata nafasi hiyo wakati Daudi, mfalme wa wakati ujao wa Israeli, alipoenda kumuua mume wake kwa sababu alikuwa amemtukana Daudi na wanaume wake. (1 Sam. 25:​9-13) Abigaili angeweza kutoroka na kumwacha Daudi atekeleze mpango wake. Hata hivyo, aliingilia kati na kumshawishi Daudi asimuue Nabali. (1 Sam. 25:​23-27) Kwa nini alifanya hivyo? Abigaili alimpenda Yehova na aliheshimu viwango vyake vya ndoa. Alijua Yehova anaiona ndoa kuwa mpango mtakatifu. Alitaka kumfurahisha Mungu, na hilo lilimchochea kufanya chochote alichoweza ili kuwaokoa watu wa nyumbani mwake, kutia ndani mume wake. Alichukua hatua haraka ili kumzuia Daudi asimuue Nabali. w24.03 16-17 ¶9-10

Jumamosi, Januari 25

Ningewaimarisha kwa maneno ya kinywa changu.—Ayu. 16:5.

Je, katika kutaniko lenu kuna baadhi ya ndugu na dada ambao wanajaribu kurahisisha maisha yao ili washiriki zaidi katika utendaji wa kitheokrasi? Je, unawafahamu vijana ambao kwa ujasiri wanakubali kuwa tofauti na wengine shuleni, hata ingawa kufanya hivyo si rahisi kwao? Namna gani wale wanaopambana ili kuendelea kuwa waaminifu licha ya upinzani kutoka kwa watu wa familia? Acheni tutumie kila fursa tunayopata kuzungumza na waabudu wenzetu wapendwa kwa njia yenye kutia moyo, na kuwaeleza jinsi tunavyothamini roho yao ya kujidhabihu na ujasiri wao. (Flm. 4, 5, 7) Yehova ana uhakika kwamba tunatamani kutoka moyoni kumfurahisha na kwamba tuko tayari kujidhabihu ili kuishi kulingana na nadhiri tuliyotoa tulipojiweka wakfu. Anaonyesha kwamba anatuheshimu kwa kutupa fursa ya kumwonyesha upendo wetu kwa njia ya kibinafsi. (Met. 23:​15, 16) Acheni tuazimie kuendelea kumtumikia Yehova, na kumtolea kwa hiari kilicho bora kabisa. w24.02 18 ¶14; 19 ¶16

Jumapili, Januari 26

Akapita katika nchi akitenda mema na kuwaponya.—Mdo. 10:38.

Wazia jinsi hali ilivyokuwa mwishoni mwa mwaka wa 29 W.K. mwanzoni mwa huduma ya Yesu. Yesu na Maria, mama yake, wanaalikwa katika karamu ya ndoa huko Kana. Inaonekana Maria anasaidia kuwatunza wageni. Lakini wakati wa karamu hiyo, tatizo linatokea—divai inakwisha. Maria anaenda upesi kwa mwanaye na kusema: “Hawana divai.” (Yoh. 2:​1-3) Yesu anafanya nini? Anabadili maji kimuujiza kuwa “divai nzuri.” (Yoh. 2:​9, 10) Baadaye, Yesu alifanya miujiza mingi wakati wa huduma yake. Alitumia uwezo wake wa kufanya miujiza kuwasaidia makumi ya maelfu ya watu. Kwa mfano, miujiza yake miwili tu—kuwalisha wanaume 5,000 na baadaye wanaume 4,000—huenda ilihusisha jumla ya watu zaidi ya 27,000 ikiwa tutatia ndani wanawake na watoto waliokuwepo. (Mt. 14:​15-21; 15:​32-38) Katika pindi hizo mbili, Yesu aliwaponya pia watu wengi waliokuwa wagonjwa.—Mt. 14:14; 15:​30, 31. w23.04 2 ¶1-2

Jumatatu, Januari 27

Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika kwa nguvu mkono wako wa kulia, Mimi ninayekuambia, “Usiogope. Nitakusaidia.”—Isa. 41:13.

Baada ya kupitia hali ngumu sana, huenda pindi fulani tukahisi tukiwa dhaifu kimwili na kihisia. Kama Eliya, tunaweza kushindwa hata kuamka na kutamani kuendelea kulala tu. (1 Fal. 19:​5-7) Huenda tukahitaji msaada ili kuendelea na utendaji wetu katika utumishi wa Yehova. Katika hali kama hizo, Yehova anatuhakikishia msaada wake kama inavyotajwa katika andiko la leo. Mfalme Daudi alipata msaada huo kutoka kwa Yehova. Alipokabili majaribu na maadui, alimwambia hivi Yehova: “Mkono wako wa kuume hunitegemeza.” (Zab. 18:35) Mara nyingi, Yehova anatutegemeza kwa kuwachochea wengine watusaidie. Kwa mfano, Daudi alipokuwa dhaifu, Yonathani, rafiki yake, alimtembelea ili kumwimarisha na kumtia moyo. (1 Sam. 23:​16, 17) Vivyo hivyo, Yehova alimchagua Elisha ili amsaidie Eliya kwa njia hususa.—1 Fal. 19:​16, 21; 2 Fal. 2:2. w24.01 23-24 ¶10-12

Jumanne, Januari 28

Yehova mwenyewe hutoa hekima; na kinywani mwake hutoka ujuzi na utambuzi.—Met. 2:6.

Yehova ni mkarimu, naye hutuandalia vitu kwa wingi. Sifa hizo zinaonekana katika “hekima ya kweli,” ambayo kwenye Methali sura ya 9 inalinganishwa na mwanamke. Simulizi hilo linasema kwamba mwanamke huyo wa mfano ametayarisha kabisa nyama yake, amechanganya divai yake, na kupanga meza yake katika nyumba yake. (Met. 9:​2, maelezo ya chini) Isitoshe, kulingana na mstari wa 4 na 5, mwanamke huyo anayefananishwa na hekima ya kweli, “humwambia yule asiye na busara: ‘Njoo, ule mkate wangu.’” Kwa nini tunapaswa kukubali mwaliko wa kwenda kwenye nyumba ya hekima ya kweli na kula chakula cha mwanamke huyo? Yehova angependa watoto wake wawe wenye hekima na wawe salama. Hataki tujifunze masomo maishani kwa njia ngumu, yaani, kupitia kufanya makosa ambayo yatatusababishia majuto. Ndiyo sababu yeye “huwahifadhia wanyoofu hekima inayotumika.” (Met. 2:7) Tukisitawisha woga unaofaa kumwelekea Yehova, tutatamani kumfurahisha. Tunasikiliza ushauri wake wenye hekima, na tunafurahi kuufuata.—Yak. 1:25. w23.06 23 ¶14-15

Jumatano, Januari 29

Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu.—Ebr. 6:10.

Hata ikiwa tunahisi hatuwezi kufanya yote tunayotamani katika utumishi wa Mungu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anathamini yote tunayofanya kutoka moyoni ili kumfurahisha. Tunajuaje hilo? Katika siku za Zekaria, Yehova alimwomba nabii huyo atengeneze taji kutokana na dhahabu na fedha iliyotolewa na Wayahudi waliokuwa uhamishoni Babiloni. (Zek. 6:11) “Taji lenye utukufu” lilikuwa “ukumbusho” wa michango yao ya ukarimu. (Zek. 6:​14, maelezo ya chini) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova hatasahau jitihada zetu za kumtumikia kutoka moyoni, tunapokabili changamoto zisizotarajiwa. Bila shaka, tutaendelea kukabili changamoto zisizotarajiwa katika siku hizi za mwisho, na huenda hali zikawa mbaya zaidi wakati ujao. (2 Tim. 3:​1, 13) Hata hivyo, hatuhitaji kulemewa na mahangaiko. Kumbuka maneno ambayo Yehova aliwaambia watu wake katika siku za Hagai: “Niko pamoja nanyi . . . Msiogope.” (Hag. 2:​4, 5) Sisi pia tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakuwa pamoja nasi tukijitahidi kadiri tuwezavyo kufanya mapenzi yake. w23.11 19 ¶20-21

Alhamisi, Januari 30

Mimi ni mtu mwenye dhambi.—Luka 5:8.

Ingekuwa rahisi kwa Yehova kuhakikisha kwamba makosa ya mtume Petro hayaandikwi katika Biblia. Hata hivyo, yaliandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu ili tujifunze kutokana nayo. (2 Tim. 3:​16, 17) Mambo tunayojifunza kutokana na mwanamume huyo aliyekuwa na udhaifu na hisia kama zetu yanaweza kutusaidia kuelewa kwamba Yehova hatarajii tuwe wakamilifu. Anataka tuendelee kuwa waaminifu—tuendelee kujitahidi—licha ya udhaifu wetu. Kwa nini ni muhimu tujitahidi kuendelea kuwa waaminifu? Kwa sababu hata tunapohisi kwamba tumeshinda udhaifu fulani huenda tukafanya makosa tena. Lakini bado tunaendelea kujitahidi kufikia lengo letu. Sisi sote husema au kufanya mambo ambayo baadaye tunajutia; hata hivyo, ikiwa hatutakata tamaa, Yehova atatusaidia tuendelee kusonga mbele. (1 Pet. 5:10) Huruma ambayo Yesu alimwonyesha Petro licha ya makosa yake, inaweza kutuchochea tuendelee kumtumikia Yehova. w23.09 20-21 ¶2-3

Ijumaa, Januari 31

Bwana, kama ungekuwa hapa ndugu yangu hangekufa.—Yoh. 11:21.

Yesu angeweza kumponya Lazaro, kama Martha alivyosema katika andiko la leo. Lakini Yesu alikusudia kufanya jambo lenye kustaajabisha hata zaidi. Alimwahidi hivi: “Ndugu yako atafufuka.” Pia, alisema: “Mimi ndiye ufufuo na uzima.” (Yoh. 11:​23, 25) Naam, Mungu alikuwa amempa Yesu nguvu za kuwafufua wafu. Hapo awali, alikuwa amemfufua msichana mdogo muda mfupi baada ya kufa na pia alikuwa amemfufua mwanamume kijana, inaelekea siku ileile ambayo kijana huyo alikufa. (Luka 7:​11-15; 8:​49-55) Lakini je, angeweza kumfufua mtu ambaye alikuwa amekufa kwa siku nne na ambaye mwili wake ulikuwa umeanza kuharibika? Maria, yule dada mwingine wa Lazaro, alienda kukutana na Yesu. Alirudia maneno ambayo dada yake alikuwa amesema: “Bwana, kama ungekuwa hapa, ndugu yangu hangekufa.” (Yoh. 11:32) Yesu alipoona na kumsikia Maria na wengine waliokuwa pamoja naye wakilia, naye pia alihuzunika sana. Akichochewa na huruma nyororo kuelekea rafiki zake, Yesu alitokwa na machozi. Anaelewa jinsi tunavyoumia sana tunapofiwa na mpendwa wetu. Kwa kweli, alitamani kuwaondolea jambo lililowaletea machozi! w23.04 10-11 ¶12-13

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki