FIBI
(Fibi) [Safi; Angavu; Nururifu].
Dada Mkristo katika kutaniko la karne ya kwanza la Kenkrea. Katika barua yake kwa Wakristo huko Roma, Paulo ‘anamtambulisha’ dada huyo kwa ndugu na anawaomba wampe msaada wowote ambao huenda akahitaji kwa kuwa ‘alikuwa mtetezi wa wengi, kutia ndani yeye mwenyewe.’ (Ro 16:1, 2) Huenda Fibi alipeleka barua ya Paulo katika jiji la Roma au aliandamana na mtu aliyefanya hivyo.
Paulo anamrejelea Fibi kuwa “mhudumu wa kutaniko lililo huko Kenkrea.” Usemi huo unazusha swali la ni katika maana gani neno di·aʹko·nos (mhudumu) linatumika hapa. Baadhi ya watafsiri huona neno hilo katika maana rasmi na hivyo hulitafsiri kumaanisha “mhudumu wa kike.” Hata hivyo, Maandiko hayasemi lolote kuhusu watumishi wa huduma wa kike. Tafsiri ya Goodspeed huutafsiri usemi huo kwa ujumla kuwa “msaidizi.” Hata hivyo, Paulo alipomrejelea huenda alikuwa akizungumzia kutangazwa kwa habari njema, huduma ya Kikristo, na alikuwa akimzungumzia Fibi akiwa mhudumu wa kike aliyekuwa akishirikiana na kutaniko la Kenkrea.—Linganisha Mdo 2:17, 18.
Fibi alitumikia akiwa “mtetezi wa wengi.” Neno linalotafsiriwa “mtetezi” (pro·staʹtis) kimsingi linaweza kumaanisha “mlinzi” au “msaidizi,” hivyo linarejelea si kuwa mkarimu tu bali pia kuwasaidia wenye uhitaji. Linaweza kutafsiriwa pia “mlezi.” Kwa kuwa Fibi aliweza kusafiri na kulihudumia kutaniko kwa kiasi kikubwa, huenda alikuwa mjane na alikuwa tajiri kadiri fulani. Kwa sababu hiyo, huenda alikuwa na uwezo wa kutumia nafasi yake katika jamii kuwasaidia Wakristo waliokuwa wakishtakiwa isivyo haki, kwa kuwatetea kwa njia hiyo; au huenda aliwatunza ndugu na dada walipokabili hatari, akitumikia kama mlinzi. Masimulizi hayasemi chochote kuhusu hilo.