Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 5/1 kur. 213-215
  • Nimlipe Yehova Nini?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nimlipe Yehova Nini?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Habari Zinazolingana
  • Sisi Tutamlipaje Yehova Marudishio?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Kukunjulia Wenye Shida Mkono kwa Ukarimu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Yote Hayo Hugharimiwaje?
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Namna Ufalme wa Mungu Unavyoweza Kukufaidi Wewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 5/1 kur. 213-215

Nimlipe Yehova Nini?

NI WATU waliofundishwa na Biblia wenye nia ya upole peke yao wanaoweza kuelekea kuliuliza ulizo juu ya kumlipa Mungu kwa ajili ya faida zote alizovipa viumbe vyake vya kibinadamu. Watu wengi wanafikiria zaidi na kuzungumza juu ya taabu zao, sababu zao za kulalamika, maoni yao mabaya yasiyo na msingi mzuri, kuliko mambo ambayo wangeweza kuwa wenye shukrani kwa ajili yake. Shukrani ya kweli haionekani sana. Wengi wamepofushwa sana na mapendezi yao wenyewe wasiweze hata kuona wingi wa sababu za kushukuru. Hali hii ilitabiriwa waziwazi na mwandikaji aliyeongozwa na roho ya Mungu wa karne ya kwanza C.E. kwa maneno haya: “Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, . . . wasio na shukrani, wasio safi,... wasiopenda mema.”​—2 Tim. 3:2, 3.

Roho hiyo ya kukosa shukrani ni ya kuambukiza. Yaweza kuenea na kuambukiza wengine kama ugonjwa wenye kudhuru sana. Yaweza kutia sumu akilini mwa hata wale walioigeukia ibada ya Mungu wa pekee wa kweli, Yehova, ikiwa kwa njia yo yote wanaacha kuitia imani yao nguvu na kumtumaini Yeye wanayemwabudu. Basi, ni muhimu namna gani kuzitafakari mara kwa mara faida zote ambazo Yehova ametumiminia​—ndiyo, hata mbele ya sisi kuujua utawala wake mwema juu ya ulimwengu wote! Na kuna sababu za pekee kuwa wenye shukrani kwamba tu hai katika kipindi hiki cha historia ya kibinadamu, kwamba tunao ufahamu katika makusudi ya Mungu yaliyo mazuri ajabu kwa wanadamu na sayari hii ya kidunia iliyoumbwa ipate kuwa makao ya milele yaliyo mazuri ya mwanadamu.​—Yer. 9:24.

Kumbuka, sote tulizaliwa katika taifa lenye kufa. Tangu siku yenyewe ya kuzaliwa tumetiishwa na hofu ya kufa kwa urithi kutoka kwa wazazi wetu waliotenda dhambi. Tumekuwa mikononi mwa watawala wachoyo na waonezi na watu ambao, kama wanyama-mwitu, wamekuwa wenye pupa ya mateka. Tumedanganywa, tukanyang’anywa, tukafukarishwa, si kwa habari ya mambo ya kimwili tu, lakini, lililo baya zaidi, na kwa habari ya mambo ya kiroho. Tumejikwaa-kwaa katika ulimwengu wenye giza na mkatili ye yote asielekee kuijali hali yetu. (Eze. 34:2-6) Huenda ikawa hata tuliomba msaada tusijue tulisali kwa nani.

Wengi wetu hata walikuwa wamefikia hatua ya hatari maishani, pengine hali isiyoweza kutatulika, kama ilivyoelekea kuwa. Kama vile ndege walionaswa mtegoni na waliomo mikononi mwa wategaji, hao hawakuweza kujisaidia, wakiwa wanakaribia kufa au kukata tamaa ya kuishi. Wao walijisikia wasingeweza kusaidiwa. Wengine, wakiwa wamebumbuazwa na mambo ya maisha katika taratibu mbovu ya mambo, wamejitia katika ufisadi wa namna moja au nyingi katika jitihada ya kuyasahau maumivu yenye kuchoma ya kukata tamaa ya mambo ambayo yanawezekana maishani. Hii, vile vile, imekuwa kazi bure.

Lakini basi, katika wakati uliowafaa sana, Yehova alijitia ndani. Huenda ikawa ilikuwa kupitia kwa mmojawapo wa Mashahidi wake aliyeleta habari njema za Ufalme. Huenda ikawa ilikuwa ni kwa kusoma kimojawapo cha vitabu vingi vinavyosaidia watu wajifunze Biblia vinavyochapwa na mashahidi wa Yehova. Matokeo yalikuwa ya kustaajabisha! Macho na masikio yalifunguliwa yaone na kusikia mambo yasiyoonwa wala yasiyosikiwa, mambo mazuri ajabu ya kiroho! Maana ya Neno la Mungu, Biblia, ilianza kufahamika kidogo kidogo. Maono mapya ya uzima na manufaa yalitokea kwa sababu ya ahadi zenye kung’aa za taratibu mpya.

Kisha tulijifunza kwamba kuna wengine zaidi waliokuwa wamepita katika mambo yale yale yenye kukatisha tamaa na yenye kuvunja moyo maishani na ambao sasa, kama ilivyotukia kwetu, wamesisimuliwa na matumaini yaliyoko mbele, tumaini la uzima katika taratibu mpya ya mambo ambamo haki itazidi. (2 Pet. 3:13) Tena tuliona kwamba walikusanyika katika Jumba la Ufalme, ambapo kila mkutano ulikuwa wa kuendeleza ujuzi wetu wa Mungu na mpango wake wa wokovu. Lo! namna ushirika huo ulivyokuwa tofauti sana na wo wote tuliokuwa tumeuona katika vikundi vya kijamii vya kilimwengu na vya kidini! Kwa kweli tulikuwa na sababu nyingi za kufikiria kumlipa Mpaji mwenye ukarimu wa mambo haya yote mazuri!

Katika ushirika huu mpya na wenye kuburudisha wa pamoja na wengine wenye shukrani, lilikuja kuwa pendeleo letu kujitoa kwa ukarimu kwa nia na utendaji wa kikundi. Tulipokuwa tukiyafurahia manufaa ya Jumba la Ufalme tulijua kwamba lazima igharimu kiasi fulani ili kudumisha mahali kama hapo. Hakukuwa na haja ya ye yote kutikisa kisahani cha sadaka puani petu au kutugawia bahasha zenye maandishi ya kiasi tunachohitajiwa kulipa, kama ilivyo desturi katika nyumba nyingi za kidini za Kristendomu. Hakuna anayepaswa kuomba fedha ili kuiendeleza kazi ya Mwenyeji mkuu wa ulimwengu wote, ndivyo tulivyojifunza. Ndiyo, tulikuja kujua kwamba ni jambo la kuchukiza kuomba-omba, kurai-rai na kukaza watu watoe michango. Tuliona kwamba wanaume wenye madaraka katika kundi walijua sana kwamba uombaji huo haupatani na roho wala kanuni za Ukristo.

Bila shaka, hatukuyasahau maoni yanayofaa juu ya shauri hilo. Inagharimu kiasi fulani kuyadumisha Majumba ya Ufalme, kuingiza umeme na vifaa vyenye kuleta joto na vitu vingine vyenye manufaa vinavyoyafanya yafae kwa kazi ya kuongoza shughuli ya elimu ya Biblia. Mara kwa mara wanaume wazee katika kundi walikuwa wakiwajulisha wale waliokusanyika juu ya gharama zinazoletwa, na juu ya nafasi ya wote wenye hiari ya kushiriki kulipa gharama, si kila mtu, wala si kwa lazima, bali kulingana na uwezo na hiari ya wachangaji. Katika kila Jumba la Ufalme mna kisanduku cha mchango, kisichoonekana waziwazi sana, ambacho ndani yake ye yote aweza kutumbukiza upaji wake. Mpango wote ni tofauti kabisa na uombaji. Ni upaji uliotolewa kwa hiari tu unaothaminiwa na Yehova na watumishi wake wa Kikristo.​—2 Kor. 9:7.

Nyumaye tulijifunza kazi ya mashahidi wa Yehova ilikuwa imeenea katika nchi 207 za dunia nzima; shughuli nyingi sana za kufika katika nchi hizo na ujumbe wa Ufalme, kuzoeza na kutuma wamisionari, kusaidia watu wa nchi hizo kuichukua kazi ii hii njema na kuiendeleza kati ya wananchi wenzao. Haya yote, tulijua, yanagharimu kiasi fulani. Nalo hili ndilo lililotuharakisha, kila mmoja, kulitokeza ulizo hili: Mimi nawezaje kushiriki kwa uhakika katika utendaji huu mzuri ajabu wa dunia nzima, ijapokuwa simo katika hali ya kuondoka nyumbani kwangu?

Basi, karibuni tulipata jibu. Lo! namna tulivyofurahi kujua kwamba ingefaa kutuma michango yetu wenyewe kwa ajili ya kazi hii kubwa yenye kutoa uzima kwenye afisi ya tawi ya Sosaiti inayosimamia utendaji wa mashahidi wa Yehova katika nchi yetu wenyewe! Kwa mfano. kwa watu waishio United States anwani ifaayo ya kutumia kwa kusudi hili, tuligundua, ni Watchtower Bible and Tract Society ya New York, Inc., 117 Adams Street, Brooklyn, New York 11201.

Njia nyingine za muhimu za kujitahidi kwa njia yetu ndogo tumlipe Yehova kwa ajili ya baraka zake tulipata kuzifahamu nyumaye. Tukajua kwamba yawezekana kushiriki wenyewe katika kazi kubwa ya kuhubiri na kufundisha ambayo inatimiliza kusudi la Mungu lililoapwa la kutafuta na kuangalia umati wa wanaume wenye mfano wa kondoo na wanawake wanaopotea katika siku hizi za haraka mbele ya hii taratibu ya mambo ya kale kufikia kikomo chake wakati wa dhiki kubwa. (Eze. 34:11) Kwa kuhudhuria kwa kawaida penye mikutano ya Jumba la Ufalme, mazoezi ya ushirika huo yanapokewa na vile vile faraja nyingi kwa kushirikiana na wengine wenye shukrani. Na lo! ni furaha kama nini kujifunza kufanya mambo ambayo Kristo Yesu na wanafunzi wake walikuwa wakifanya karibu miaka 1,900 iliyopita! Inasisimua vile vile kujua kwamba katika wakati huu wa mwisho kungali kuna nafasi za watu wanaojaribu kuzifuata nyayo za Bwana Yesu!

Tunapotazama nyuma kuona namna ambavyo Yehova Mungu wetu ametuongoza muda mrefu, faida alizotupa kwa ukarimu sana, je! twaweza kuukomesha msisimko wa shukrani unaopanda mioyoni mwetu? Je! twaweza kuzisahau fadhili zake zote za upendo na kurudia-rudia kuzitaja shida zetu ndogo ndogo na malalamiko? Sivyo, bali pamoja na mtunga zaburi aliyeongozwa na roho ya Mungu twaweza kutangaza hivi kwa furaha: “Nafsi yetu imeokoka kama ndege katika mtego wa wawindaji, mtego umevunjika, nasi tumeokoka. Msaada wetu u katika jina la [Yehova], aliyezifanya mbingu na nchi.” (Zab. 124:7, 8) “Mungu mwenye rehema na neema” (NW) ametukomboa katika ubatili wa maisha yasiyomcha Mungu, katika kuvunjika moyo kwa sababu ya maisha ya kujifikiria kwa mtu peke yake, ndiyo, katika ‘kamba za kifo kinachozingira,’ kwa maana je! yeye hakutupa sisi tumaini la uzima kupitia kwa Yesu Kristo?

Tumepokea bure; na tutoe bure kwa wengine wenye kuhitaji. Tunapojitoa wenyewe na mali zetu, na tuwe na matumaini kwamba Yehova anapendezwa na jitihada zetu za unyenyekevu za kuliitikia ulizo hili: “Nimlipe Yehova nini kwa ajili ya faida zake kwangu mimi?”​—Zab. 116:12, NW.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki