Ufahamu Katika Habari
Matata ya Useja
● Amri ya karne nyingi ya useja kwa mapadre wa Kikatoliki inaleta matata kwa mara nyingine.
Si ajabu kwamba inafanya hivyo. Takwa hilo linapingana moja kwa moja na mafundisho ya Biblia.
Siku ya Desemba 23, gazeti la Vatican “L’Osservatore Romano,” likiwasihi mapadre wasiache huduma yao, lilisema kwamba lazima kila padre “afanye lisilowezekana aweze kubaki katika cheo chake.” Takwa hilo “lisilowezekana” kwa kweli latokana na kuanguka na kuiacha ibada ya kweli kulikoanza baada ya kufa kwa mitume wa Yesu Kristo. Mtume Paulo alitabiri kwamba mojawapo ya sehemu za ukafiri huo ingekuwa ‘kuzuia watu wasioe.’ Je! hiyo inakushangaza? Angalia mwenyewe katika tafsiri yo yote ya Biblia, katika 1 Timotheo 4:1-3. Kwa wazi Kanisa la Katoliki limeiacha kanuni ya Biblia kwa kuipendelea yake lenyewe, na hii yaleta matata.
Makala katika “L’Osservatore” iliendelea kuwaambia wale ambao ni mapadre hivi: “Ukitenda makosa ya ufisadi—haikupasi kufanya hivyo, lakini huenda ikawa hivyo, kwa maana u dhaifu mno—una vitulizo vingi.” Kulingana na “Newsweek” (Desemba 3, 1973), mapadre wengine wanatafuta ‘kitulizo’ chao wenyewe kwa kushirikiana sana na wanawake na, nyakati nyingine, kwa kufanya ngono nao wajapokuwa wanaendelea kutooa.
Bila shaka, hilo si jambo jipya. Wakatoliki wengi wamejua mapadre wanaofanya hivyo kwa muda mrefu. Lakini kinachohangaisha kanisa siyo ufisadi wa mapadre hawa, bali uhakika wa kwamba wengi sasa wanaacha upadre wakaoe. Hesabu ya mapadre imepungua kwa kiasi cha karibu 20,000 miaka mitatu iliyopita.