Maoni ya Biblia
Je! kwa Kweli Twahitaji Makuhani?
“TOENI shukrani kwa karama ya Ukuhani,” akasema John Paul 2 katika barua yake ya kila mwaka kwa makuhani (leo huitwa makasisi) siku ya “Alhamisi Takatifu,” katika 1992. Si Wakatoliki tu bali wengine pia wametambua kwa uchungu makosa yao wenyewe. Wamehisi uhitaji wa kuwa na mtu anayekubalika kwa Mungu anayeweza kuwaambia mapenzi ya Mungu, kumtolea Yeye dhabihu, na kuwaombea mbele za Mungu. Mtu kama huyo huitwa kuhani. Je! kwa kweli twahitaji kuhani ili atusaidie tupate msamaha wa Mungu?
Wazo la makuhani na dhabihu halikutokana na wanadamu bali lilitokana na Mungu. Kama hakungalikuwa dhambi dhidi ya Mungu, kusingalikuwa uhitaji wa makuhani. Katika Edeni, mwanadamu mkamilifu Adamu hakuhitaji kuhani. Yeye aliumbwa akiwa bila dhambi.—Mwanzo 2:7, 8; Mhubiri 7:29.
Makuhani wa Kwanza Walikuwa Akina Nani?
Sisi sote leo tumerithi hali ya kuwa wenye dhambi kwa sababu Adamu alifanya dhambi kimakusudi na sisi ni wazao wake. (Warumi 3:23) Habili, mwana wa mwanadamu wa kwanza, Adamu, alitambua hilo. Biblia husema hivi juu yake: “Kwa imani Habili alimtolea Mungu dhabihu.” (Waebrania 11:4) Ingawa Habili na watu wengine wa kale wenye imani—kama vile Noa, Abrahamu, na Ayubu—hawakuitwa makuhani, wao walitoa dhabihu kwa Mungu kwa ajili yao wenyewe au familia zao. Kwa kielelezo, Biblia yasema hivi juu ya Ayubu na wanae: ‘Ayubu alisongeza sadaka za kuteketezwa kama hesabu yao wote ilivyokuwa; kwani Ayubu alisema, humkini kwamba hawa wanaangu wamefanya dhambi.’ (Ayubu 1:5) Hata hivyo, makuhani na dhabihu zilikujaje kuwa mambo ya kawaida katika tamaduni nyingi?
Fikiria matukio yaliyomzunguka mzee wa kale Noa. Noa na familia yake ndio waliokuwa wanadamu pekee waliookoka Gharika ya tufeni pote. Walipotoka nje kwenye ardhi iliyooshwa ikawa safi, Noa alijenga madhabahu na kutoa dhabihu kwa kuthamini huruma na mkono wenye kulinda wa Yehova. Kwa kuwa mataifa yote ni wazao wa Noa, hakuna shaka walifuata kigezo chake na muda si muda wakasitawisha unamna-namna wa mapokeo yanayohusiana na waombezi na dhabihu kwa ajili ya dhambi.—Mwanzo 10:32.
Zaidi ya karne moja baadaye, uasi dhidi ya Mungu ulitokea katika Babeli. Mungu alivuruga lugha ya watu hao nao wakatawanyika. (Mwanzo 11:1-9) Makuhani fulani, sasa wakichochea itikadi zilizopindika na za kushusha heshima, walisitawisha desturi zenye kuhofisha katika mabara ambako walitawanyika. Hata hivyo, Mungu aliona uhitaji wa kufunza waabudu wake juu ya uhitaji wao wa kuwa na ukuhani wa kweli wenye ku-hani mkuu, makuhani wa chini, na dhabihu zinazokubalika kwake.
Sababu Iliyofanya Mungu Awaweke Makuhani
Baadaye Yehova alilipatia taifa la Israeli makuhani waliofanya mambo mawili ya msingi. Kwanza, wao walimwakilisha Mungu mbele za watu wakiwa waamuzi na walimu wa Sheria ya Mungu. (Kumbukumbu la Torati 17:8, 9; Malaki 2:7) Pili, wao waliwakilisha watu mbele za Mungu kwa kumtolea dhabihu kwa ajili ya watu. Barua ya Paulo kwa Wakristo Waebrania inaeleza hivi: “Kila kuhani mkuu aliyetwaliwa katika wanadamu amewekwa kwa ajili ya wanadamu katika mambo yamhusuyo Mungu, ili atoe matoleo na dhabihu kwa ajili ya dhambi. . . . Na hapana mtu ajitwaliaye mwenyewe heshima hii, ila yeye aitwaye na Mungu.”—Waebrania 5:1, 4.
Paulo aendelea kueleza kwamba ukuhani wa Israeli haukuwa njia ya mwisho ya Mungu ya kujipatanishia watu Kwake. Kazi za makuhani zilikuwa ufananisho ulioelekeza kwenye mambo bora zaidi, ‘mambo ya kimbingu.’ (Waebrania 8:5) Mambo hayo ya kimbingu yalipowasili, mambo ya ufananisho hayakuhitajiwa tena. Kutoa kielezi: Unaweza kuhifadhi tangazo fulani la bidhaa unayohitaji sana, lakini ungelitupa tangazo hilo mara baada ya kupata bidhaa hiyo, sivyo?
Muda mrefu kabla ya taifa la Israeli kuwapo, Mungu alikusudia kuwe na ukuhani ambao ungetumika kwa ajili ya baraka, si za Israeli tu, bali kwa ajili ya ainabinadamu yote. Mwanzoni, Israeli lilipendelewa kwa kupewa fursa ya kuandaa washiriki wa ukuhani huo. Taifa hilo lilipofanyizwa, Yehova aliambia Israeli hivi: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli . . . , mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.” (Kutoka 19:5, 6; linganisha Mwanzo 22:18.) Kwa kusikitisha, mara nyingi taifa hilo halikutii sauti ya Mungu. Hivyo, Yesu aliwaambia makuhani na Mafarisayo: “Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu, nao watapewa taifa lingine lenye kuzaa matunda yake.” Ni nani sasa watakaotumikia wakiwa makuhani kwa ajili ya baraka za ainabinadamu?—Mathayo 21:43.
Wakristo Wanahitaji Ukuhani Gani?
Kwa sababu tumerithi dhambi kutoka kwa Adamu, wokovu kwenye uhai wa milele unawezekana tu kupitia dhabihu kamilifu iliyoandaliwa na Yesu. (1 Yohana 2:2) Yesu mwenyewe hutuombea akiwa Kuhani Mkuu, kama vile ilivyotangulia kufananishwa katika ukuhani wa Israeli. Waebrania 9:24 lasema: “Kristo hakuingia katika patakatifu palipofanyika kwa mikono, ndio mfano wa patakatifu halisi; bali aliingia mbinguni hasa, aonekane sasa usoni pa Mungu kwa ajili yetu.” Hivyo, ubora wa ukuhani mkuu wa Kristo unaopita mwingine wote hufanya kusiwe na uhitaji wa makuhani wa kibinadamu wakiwa waombezi. Lakini, utumishi wa makuhani wa chini unahitajiwa. Kwa njia gani?
Ni lazima makuhani ‘watoe dhabihu za roho, zinazokubaliwa na Mungu, kwa njia ya Yesu Kristo.’ (1 Petro 2:5) Kwa habari ya aina ya matoleo hayo, Paulo aliandika hivi: “Tumpe Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo.” (Waebrania 13:15) Kwa hiyo, wale watakaofanyiza ukuhani wa kifalme, wakiwa wangali duniani, wanawakilisha Mungu mbele za wanadamu wakiwa Mashahidi wake, si wakiwa waombezi. Baadaye, wakiwa mbinguni pamoja na Yesu Kristo, wanawakilisha wanadamu mbele za Mungu, wakitoa manufaa za dhabihu ya Kristo na kuponya maradhi yote.—Linganisha Marko 2:9-12.
Ingawa waamini wote wapaswa watoe ushahidi, ni wachache tu kwa kulinganisha watakaotumikia katika “ufalme wa makuhani” wa kimbingu. Yesu alisema hivi: “Msiogope, enyi kundi dogo; kwa kuwa Baba yenu ameona vema kuwapa ule ufalme.” (Luka 12:32; Ufunuo 14:1) Hao watafufuliwa kwenda mbinguni na “watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala pamoja naye hiyo miaka elfu.”—Ufunuo 20:6.
Mungu amepanga ili makuhani hao wa kimbingu watende katika maana ya kiroho na kimwili ambayo hakuna ukuhani umepata kutenda kamwe. Hivi karibuni, watakapotumia manufaa za dhabihu ya fidia ya Yesu, wataweza kushiriki katika kurudisha ainabinadamu yote waaminifu kwenye ukamilifu wa kibinadamu. Kisha, Isaya 33:24 litakuwa na utimizo mzuri ajabu. Hilo linasema hivi: “Hapana mwenyeji atakayesema, mimi mgonjwa; watu wakaao humo watasamehewa uovu wao.”
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]
“Benediction of the Wheat at Artois” 1857, by Jules Breton: France/Giraudon/Art Resource, N.Y.