Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 10/1 kur. 449-453
  • Makuhani Wawezao Kutusaidia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Makuhani Wawezao Kutusaidia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUTIWA MAFUTA KWA MAKUHANI
  • KATIKA “UA”
  • KATIKA “PATAKATIFU”
  • UFUFUO KWENYE MBINGU
  • FAIDA KWA WANADAMU WOTE
  • Je! Tunahitaji Ukuhani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Hekalu Kubwa la Kiroho la Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Je! kwa Kweli Twahitaji Makuhani?
    Amkeni!—1993
  • Thamini Pendeleo Lako la Kuabudu Katika Hekalu la Kiroho la Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 10/1 kur. 449-453

Makuhani Wawezao Kutusaidia

Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi

1-3. Watu wanahitaji msaada gani, na je! padre wa kidunia aweza kutoa yote yanayohitajiwa?

INAKUBALIWA na madaktari wengi kwamba hali njema ya kiroho na ya akilini ya mgonjwa ni ya maana sana kwa kupata kwake nafuu kama vile utabibu ulivyo wa maana. Kwa hiyo, kuna haja ya makuhani wa Mungu wawezao kuwasaidia na kuwafariji wagonjwa na wenye afya vile vile.

2 Bila shaka, padre duniani hawezi kumsaidia sana mgonjwa kwa njia ya kimwili. Wala hawezi kukuondoa kutokamilika kwa kimwili kwa mtu mwenye afya ya kawaida. Kwa maana sote tu wasiokamilika, watenda dhambi. Walakini, kuhani wa Mungu aweza kutoa msaada wa kiroho.

3 Lakini Mungu amepanga wawepo makuhani watakaowarudishia wanadamu afya ya kimwili na ya kiroho pia. Twajuaje?

4. Twawezaje kuwa na hakika kwamba Mungu amepanga wawepo makuhani wawezao kutusaidia kweli kweli?

4 Twaweza kujua bila shaka kwa kuchunguza kwa ufupi mpango ambao Mungu ameufanya. Humo twauona ushuhuda thabiti, wenye kukata shauri hata shaka lo lote lisiachwe kwamba ukuhani wa kweli wa Mungu ni hakika, na kwamba makuhani hawa watautoa msaada wanaouhitaji wanadamu. Mungu alilihifadhi kumbukumbu hili katika Biblia kwa kusudi la kutuhakikishia hasa.

5. Ni njia gani moja ambavyo kuhani mkuu wa Mungu hana kifani?

5 Anayetupendeza kwanza ni Kuhani Mkuu. Kuhani Mkuu wa Mungu aliye wa kweli hana kifani, kwa maana Huyu aliutoa uhai wake mwenyewe wa kibinadamu kama dhabihu. (Yohana 6:51) Kwa njia hii angeweza kuwa na kitu cha thamani kubwa kama bei ya kuwanunua wanadamu. Yaani, angeweza kuipata haki ya kusimama mahali ambapo Adamu alikuwa amepaacha kwa kutotii kwake, akiwapa watoto wake urithi wa mauti. (Rum. 5:15, 17) Halafu, akiwa amefufuliwa katika roho, Yesu Kristo angeweza kuwa Baba ya kizazi kipya cha wale ambao kati ya taifa la kibinadamu wangeikubali dhabihu yake kwa imani na utii.​—1 Kor. 15:45; Isa. 53:10; Yohana 3:16.

KUTIWA MAFUTA KWA MAKUHANI

6. Makuhani katika Israeli walitiwaje mafuta?

6 Mungu aliwawekea Israeli wa kale ukuhani, ili kuufananisha ukuhani wake wa kimbinguni hasa. Alimchagua Haruni ndugu yake Musa, wa kabila ya Lawi, kama kuhani mkuu. Musa alimtia Haruni mafuta ya halisi. Kwa hiyo Haruni angeweza kuitwa “mtiwa mafuta” au “Masihi.” Baada ya hili Musa aliwatia mafuta wana wanne wa Haruni wawe makuhani wadogo. (Kut. 40:1, 2, 12-16) Halafu, makuhani walipokufa na kurithiwa na wana wao, kuhani mkuu peke yake ndiye aliyetiwa mafuta; kwa kuwa wana wa Haruni walikuwa wamekwisha tiwa mafuta kwanza hakukuwa na haja ya makuhani wadogo waliofuata kutiwa mafuta tena. Kuvikwa mavazi rasmi ya kuhani mdogo kulionwa kama kumetosha.​—Hes. 3:1-3.

7. Yesu alitiwaje mafuta, na je! kutiwa mafuta huku kulipaswa kurudiwe?

7 Sasa, haya yote yalifananisha uhakika wa kwamba wakati wa ubatizo wake Yesu Kristo alitiwa mafuta, si kwa mafuta ya halisi, bali kwa roho takatifu ya Mungu. (Mt. 3:16; Matendo 10:38) Haikuwa lazima wakati wo wote kutiwa mafuta huku kurudiwe, kama vile kwa habari ya makuhani wakuu wa Israeli wa kale, kwa maana Yesu hana warithi, kwa sababu ya kufufuliwa kwake kwenye uzima usio na mwisho na Baba yake.​—1 Tim. 6:14-16.

8. Makuhani wadogo wa kweli walitiwaje mafuta?

8 Kupitia kwa Mwanawe, Yehova Mungu alimimina roho takatifu juu ya wanafunzi wake siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E., akiwatia mafuta. (Marko 1:7, 8; Yohana 1:33; Matendo 2:1-4, 16, 17) Baada ya hapo, roho ya Mungu iliendelea kumiminika kupitia kwa Kristo, na wengine wakapata kuzamishwa katika mwili wa Kristo, kwa njia hiyo nao pia wakapata kuwa watiwa mafuta na makuhani wadogo. (Rum. 6:3) Mtume Yohana aliwaandikia Wakristo wenzake hivi: “Nanyi mmepakwa mafuta na Yeye aliye Mtakatifu nanyi mnajua nyote.”​—1 Yohana 2:20.

9. Ni kazi gani nyingine roho takatifu inayoifanya wakati makuhani wanapotiwa mafuta?

9 Wakati wanapochaguliwa na Mungu wawe makuhani na kutiwa mafuta na roho ya Mungu wanazaliwa pia kwa roho, wakiwa na matumaini ya uzima mbinguni. ‘Wanatiwa muhuri’ kwa hiyo roho takatifu. Mtume Paulo alikuwa mmoja wao naye aliwaandikia watiwa mafuta wengine hivi: “Yeye atufanyaye imara pamoja nanyi katika Kristo [Mtiwa Mafuta], na kututia mafuta, ni Mungu, naye ndiye aliyetutia muhuri akatupa arabuni ya [roho] mioyoni mwetu.”​—2 Kor. 1:21, 22; 5:5; Efe. 1:13, 14.

10. Twaijuaje jumla ya makuhani hawa wadogo?

10 Jumla ya watiwa mafuta wanaopatikana mwishowe wakiwa na “muhuri” ya kudumu ni 144,000, kulingana na Ufunuo 7:1-8. (Ufu. 14:1-4) Hawa ni “ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu.” Ndio aliowanunua Kristo kwa damu yake kwa ajili ya Mungu “wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa,” ‘akawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu.’​—1 Pet. 2:9; Ufu. 5:9, 10.

11. Ni ruhusa gani waliyo nayo makuhani wadogo wa kweli wasiyokuwa nayo makuhani wa Kiyahudi waliotumikia hekaluni?

11 Kama vile makuhani wa kale wa Kiebrania walivyokuwa na ruhusa ya kula sehemu fulani za dhabihu zilizotolewa, ndivyo na hawa “makuhani kwa Mungu wetu” walivyo na ruhusa ya kula sehemu ya dhabihu ya Yesu Kristo juu ya madhabahu ya “mapenzi” ya Mungu, haki wasiyokuwa nayo makuhani Wayahudi wa Kilawi kwa sababu walimkataa Yesu kama Masihi au Kristo.​—Ebr. 13:10-15; Yohana 6:48-58.

KATIKA “UA”

12. Makuhani wadogo wamo katika “ua” uliofananishwa kwa njia gani?

12 Hii yamaanisha kwamba, wanapokuwa duniani wamo katika hali iliyofananishwa na ua (wa hema na mahekalu yaliyokubaliwa na Mungu zamani) mlimokuwamo madhabahu ya dhabihu. Hii ndiyo hali ya kutangazwa kuwa wenye haki na Mungu kwa sababu ya imani yao katika dhabihu ya Yesu Kristo. Mtume aliandika hivi: “Tumekwisha tangazwa kuwa wenye haki kwa sababu ya imani,” na “tumekwisha tangazwa kuwa wenye haki sasa kwa damu yake.”​—Rum. 5:1, 9, NW.

13, 14. Makuhani wadogo hawa wawezaje kuhesabiwa kuwa wenye haki wanapokuwa wenye mwili unaolemewa na dhambi, na je! wanauongezea ubora wa dhabihu ya Kristo cho chote?

13 Wanapokuwa duniani, makuhani hawa wangali wana mwili usiokamilika wenye kulemewa na dhambi, na hali wanahesabiwa kuwa wenye haki kwa sababu ya matumizi ya ubora wa dhabihu ya Kristo. Hali yao ni yenye haki, isiyolaaniwa. Paulo anapaza sauti hivi: “Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu. Basi, kama ni hivyo, mimi mwenyewe kwa akili zangu [akili za Kikristo zilizofanywa upya] naitumikia sheria ya Mungu, bali kwa mwili wangu sheria ya dhambi. Sasa, basi, hakuna hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu. Kwa sababu sheria ya [roho ya uzima] ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha huru, mbali na sheria ya dhambi na mauti.”​—Rum. 7:25–8:2.

14 Kwa kuwa haki yao hawakujipatia wenyewe hawawezi kuongeza cho chote kwa ubora wa dhabihu ya Kristo. Huo peke yake ndio uwezao kulipia dhambi. Lakini wanaweza kumtolea Mungu ‘dhabihu za sifa’ kupitia kwa Kristo na kumfanyia mema ya Kikristo.​—Ebr. 13:15, 16.

KATIKA “PATAKATIFU”

15. Ni kwa njia gani makuhani wadogo wanavyotumikia katika ‘Patakatifu’ palipofananishwa?

15 Kwa kuwa wanahesabiwa kama wanadamu wenye haki, wanakubaliwa na Mungu na kuzaliwa kama wana wa kiroho. Kwa njia hii wao ni kama makuhani mbele za Mungu, wakimtumikia katika chumba cha Patakatifu cha hekalu la kweli la kiroho lisilosimamishwa kwa mikono ya kibinadamu. (Ebr. 9:11) Wanapokuwa wangali wenye miili ya nyama wanafurahia mwangaza wa kiroho, kama ulivyofananishwa na kinara cha taa cha dhahabu cha Patakatifu. Wanakula chakula cha kiroho kama kilivyofananishwa na chungu mbili za mikate ya wonyesho katika meza ya dhahabu. Wanamtolea Mungu sala na utumishi wa bidii kana kwamba wakitoa uvumba juu ya madhabahu ya uvumba ya dhahabu katika Patakatifu.

16. Wanawatumikiaje wengine wanapokuwa wangali duniani?

16 Pia, wanapokuwa wangali duniani, wanatoa utumishi wa kikuhani kwa ajili ya wengine, sawa na makuhani wa kale wa Kiebrania walivyofanya. Kwa maana wanaangazishwa na kulishwa kwa kiroho, wanawaangazisha wengine katika ufahamu wa Neno la Mungu, na kuwalisha chakula cha kiroho. Wanajengana na kutiana moyo, na sasa wanasaidia mamia ya maelfu ya wengine wasafishe maisha zao na kumtumikia Mungu wakiwa na tumaini la kuishi milele duniani chini ya utawala wa miaka elfu wa Kristo na washirika wake wa kifalme na wa kikuhani mbinguni.

17. Ni utumishi gani wanaoufanya makuhani wa Mungu?

17 Watu wengi wamevunjika moyo, wamelemewa, wamekata tamaa​—wamo katika hali mbaya sana kwa kiroho. Wengi wanauona ubatili wa kuitegemea hii taratibu ya mambo pamoja na mapadre wake wa kidini wa kilimwengu, kama ilivyopata kuwa kabla ya Yerusalemu wa kale kuharibiwa. (Eze. 9:4) Habari njema za Ufalme kama zinavyotangazwa na makuhani wa kweli wa Mungu wanapomtolea Yeye utumishi wa bidii zinawasaidia wengine kuwa na tumaini la uzima. Wanafundishwa namna ya kufanya upya maisha zao wapatane na Mungu. Kama mabalozi wa Mungu makuhani hawa wanasaidia wengine wajipatanishe naye. (2 Kor. 5:20) Hivyo wanafanya kazi ya kiroho ya maana sana, ya kuponya.

UFUFUO KWENYE MBINGU

18, 19. Mwandikaji wa kitabu cha Waebrania aliyeongozwa na roho ya Mungu anasema makuhani wadogo wanaingiaje mbinguni?

18 Hawa waliotiwa mafuta kwa roho wanatazamia kuingia mbinguni hasa katika wakati wake. Ni kama vile mmoja wa makuhani wenzao alivyosema: “[Matumaini] tuliyo nayo kama nanga ya roho, yenye salama, yenye nguvu, yaingiayo hata mle mlimo ndani ya pazia, alimoingia Yesu kwa ajili yetu, mtangulizi wetu, amekuwa kuhani mkuu hata milele kwa mfano wa Melkizedeki.”​—Ebr. 6:19, 20.

19 Yesu alikufa, akiuacha mwili wake, kama ilivyofananishwa na kupita pazia kwa kuhani mkuu na kuingia katika Patakatifu Sana. “Basi, ndugu,” asema mwandikaji wa Waebrania 10:19-22 aliyeongozwa na roho ya Mungu, “kwa kuwa tuna ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu, njia ile aliyotuanzia iliyo mpya, iliyo hai, ipitayo katika pazia, yaani, mwili wake; na kuwa na kuhani mkuu juu ya nyumba ya Mungu; na tukaribie wenye moyo wa kweli, kwa utimilifu wa imani.”

20. Watatoa utumishi gani mbinguni?

20 Watakapohuhishwa katika “ufufuo wa kwanza” wakiisha kutumikia kwa uaminifu hata kufa, wataruhusiwa kuingia katika Patakatifu Sana pa kimbinguni. Wataingia mbele za Mungu, si kufanya kama Kuhani Mkuu Yesu Kristo katika kuutoa ubora wa dhabihu yake kamilifu ya kibinadamu, bali kutumikia pamoja na Kuhani Mkuu wao katika kueneza baraka za dhabihu ya Kristo kwa wanadamu wenye shida. (Ufu. 20:6) Wakati huo watawatolea watu wa kidunia, si mapozo ya kiroho tu, bali pia mapozo ya kimwili.

FAIDA KWA WANADAMU WOTE

21, 22. Twawezaje kuwa na hakika kwamba wengine wengi mbali na hao makuhani wadogo wa Mungu watafaidika kutokana na dhabihu ya Kristo?

21 Hizi ni habari njema kwa wanadamu wote, kwao wenyewe na kwa wafu wao, watakaofufuliwa waishi tena duniani. Kwa maana mtume Yohana aliandikia makuhani wadogo wenzake kwa uhakikisho: “Watoto wangu wadogo, nawaandikia haya ili kwamba msitende dhambi. Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki, naye ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.”​—1 Yohana 2:1, 2.

22 Kwa hiyo, Yesu Kristo hataacha kuutumia ubora wa dhabihu yake baada ya kuutumia kwa makuhani wake wadogo 144,000. Yeye ni asiyependelea, kama Baba yake. (Matendo 10:34) Amelinunua taifa zima la kibinadamu. Hataacha sehemu yo yote ya dhabihu yake ipite bila ya kutumiwa. Vipimo vya haki visingesawazika kama angezitumia faida za dhabihu yake kwa wachache peke yao. Kwa kuwa aliwanunua wote, atafurahi na kuona wajibu wa kusaidia wanadamu wengi kama iwezekanavyo watakaoonyesha imani na utii wapate uzima wa milele katika ukamilifu.​—Yohana 3:16.

23. Je! mtu ye yote, hata mtenda dhambi mbaya sana, aweza kupata msaada kutoka kwa ukuhani huu?

23 Lo! ni furaha namna gani basi iliyomo akibani kwa dunia nzima wakati wafalme na makuhani wenye haki na waliokamilishwa wanapowatumikia wanadamu! Wote, pamoja na Kuhani Mkuu wao, wamepatwa na yote yanayowapata wanadamu maishani. (Ebr. 4:15) Wanaijua kabisa hali ya wanadamu, mawazo yao ya ndani na tamaa. Bila ya kujali ni maisha ya namna gani ambayo huenda mtu aliishi zamani, anaweza kupokea msaada wa kikuhani anapousikia mpango wa Mungu kupitia kwa Kristo. Kwa maana “Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi.” (Rum. 5:8) Walipokuwa duniani, makuhani wake wadogo waliwahubiri watu wa namna zote, kutia na watenda dhambi waovu sana, walioisikiliza kweli na kubadili maisha zao. Walifanywa safi kwa imani nao waliionyesha imani hiyo wazi kwa matendo kulingana na Neno la Mungu.​—Kol. 3:5-9.

24. Twawezaje kuwa na hakika kwamba tutapokea msaada kutoka kwa ukuhani wa Mungu?

24 Kwa hiyo makuhani aliowatia mafuta Mungu na anaowatukuza mbinguni wanaijua kila shida ya wanadamu. Makuhani hao wadogo wanayo huruma na rehema aliyo nayo Kristo, kwa sababu wamepatanishwa na mfano wake. (Rum. 8:29) Watakuwa na uwezo wa kuhakikisha kwamba mapenzi ya Mungu yanatimizwa, kufanya dunia ijazwe na watu kwa haki. (Mwa. 1:28; Zab. 150:6) Kwa hiyo wote wapendao uzima na kutamani yaliyo haki na mema watazipokea faida zote za ukuhani huu. Uzima wa milele ndio huu.​—Ufu. 21:1-5.

25. Lazima tufanye nini sasa hivi tupokee msaada kutoka kwa ukuhani wa Mungu?

25 Sasa hivi twauhitaji msaada wa ukuhani huu ili kuiokoka “dhiki kubwa,” itakayoiharibu hii taratibu ya mambo. (Mt. 24:21) Ikiwa twataka kuwamo kati ya wale watakaoianza jamii mpya na yenye haki ya kibinadamu itakayowapokea wafu na kuiona dunia ikiwa paradiso, lazima tushirikiane na wajumbe wa Mungu wa kikuhani sasa. Twaweza kufanya hivi kwa kuzisikiliza habari njema za Ufalme kama wanavyozitangaza, kujifunza makusudi ya Mungu na kuchukua hatua kwa kuzipatanisha maisha zetu nayo.

​—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki