Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 11/1 kur. 495-498
  • Jihadhari na Uchafu wa Kiroho

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jihadhari na Uchafu wa Kiroho
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MFANO WA KIHISTORIA WA BIBLIA
  • FUNDISHO KWA WAKRISTO LEO
  • UFANISI WA KIROHO KWA WALIO SAFI
  • Kitabu Cha Biblia Namba 37—Hagai
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • “Iweni Safi”!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Fuatia “Utakatifu Katika Kumwogopa Mungu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Yehova Anataka Watu Wake Wawe Safi
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 11/1 kur. 495-498

Jihadhari na Uchafu wa Kiroho

Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi

1. Ni kwa njia gani Wakristo wa kweli “si wa ulimwengu,” kama vile Yesu alivyowaambia wanafunzi wake?

YESU Kristo alisema hivi juu ya wanafunzi wake: “Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” (Yohana 17:14) Je! hii maana yake ni kwamba imewapasa Wakristo wa kweli wawe wakiishi peke yao na kujitenga na watu wengine? Sivyo, kwa maana kama ingalikuwa hivyo ingaliwapasa kutoka ulimwenguni. (1 Kor. 5:10) Wao “si wa ulimwengu” kwa sababu hawajiungi na ulimwengu katika utafutaji wake wa mamlaka, utajiri, anasa zisizozuiliwa na mazoea mabaya. (Mt. 6:31, 32; 1 Pet. 4:3) Wengi wao wana kazi zile zile, wanavaa mavazi yale yale na kufurahia njia nyingi zinazofanana na za watu wengine za kujiburudisha. Lakini wao hawashiriki katika ugomvi wa ulimwengu wala katika mipango yake ya kisiasa na ya kidini ili kuendeleza taratibu ya mambo yenye kuharibika pamoja na matumaini yake yenye kuvunja moyo.

2, 3. Mkristo anaweza kuwa mchafu machoni pa Mungu kwa njia gani?

2 Wakristo wakijitia katika njia za ulimwengu za ufisadi, za udanganyifu na za kujitafutia faida zao wenyewe, wangekuwa wachafu machoni pa Mungu. Wangekuwa wasioweza kutumiwa katika ibada safi kama ‘vyombo’ vya matumizi ya Yehova.​—2 Kor. 6:17; 2 Tim. 2:21, 22.

3 Vivyo hivyo, Mkristo hawezi akajaribu kuacha-acha kidogo kidogo maisha ya Kikristo na kufuata njia za ulimwengu akaendelea kuwa safi. Mtu wa namna hiyo ni mwenye nia mbili, hakujitoa kabisa kwa Mungu. Ataendelea kupuza mambo ya kiroho na kuwa mwenye kusitasita katika uaminifu.​—Yak. 1:6-8.

MFANO WA KIHISTORIA WA BIBLIA

4, 5. (a) Mabaki ya Waisraeli walirudi kutoka Babeli kwa kusudi gani, na Mungu alikuwa amewafanyia nini? (b) Wengi waliingia katika hali gani mbaya? (c) Ni kwa njia gani Yehova aliwaamsha wakaona?

4 Hata kushirikiana sana na watu wa namna hiyo wenye kupuza kunaweza kuharibu hali ya kiroho ya wengine. Kupitia kwa nabii wake Hagai, Mungu alionyesha Waisraeli waliokuwa wamerudi kutoka uhamishoni Babeli jambo hili waziwazi. Yehova alikuwa amewafungua kwa fadhili na kulinda mabaki madogo kati yao waliorudi katika safari ndefu yenye hatari kwa kupitia jangwani. Wakati huo mioyo yao ilikuwa tayari kurudisha ibada ya Yehova kwa kujenga upya hekalu la Mungu. Walifika Yerusalemu ambao wakati huo ulikuwa ukiwa. Yehova aliendelea kubariki utendaji wao walipokuwa wakiweka msingi wa hekalu. Nchi ikalimwa nao wakajijengea nyumba.

5 Hata hivyo, ingawa walipokea baraka hizo walipokuwa waaminifu, watu wengi kati ya kikundi hiki kidogo kilichorudishwa makwao walilisahau kusudi lenyewe la kurudishwa kwao na Mungu. Wakawa wenye ubaridi wasimalize hekalu​—wasitukuze jina la Mungu katika ibada ya kweli. Walihangaikia zaidi kupamba nyumba zao wenyewe kuliko kuhangaikia nyumba ya Yehova. Lakini Yehova aliwaamsha wakaona. Aliwashtaki juu ya hali yao mbaya ya kiroho kulingana na maneno ya makuhani wao walioijua Torati. Aliwauliza hivi: “Mtu akichukua nyama takatifu katika upindo wa nguo yake, naye akagusa kwa upindo wake mkate, au ugali, au divai, au mafuta, au chakula cho chote, je! kitu hicho kitakuwa kitakatifu?” Makuhani wakajibu: “La.”​—Hag. 2:10-12.

6. Ni nini iliyokuwa maana ya ulizo la kwanza la Hagai na jibu la makuhani?

6 “Nyama takatifu” ilikuwa nyama ya mnyama aliyekuwa ametolewa kwa Yehova kama dhabihu. Kipande walichopokea makuhani kilipaswa kiliwe ndani ya “mahali patakatifu” au “mahali palipo safi.” (Law. 10:14, 17) Lakini hata ingawa mtu alichukua nyama takatifu katika nguo yake, nguo hiyo isingeweza nayo kukipa chakula kingine ilichogusa utakatifu.

7. Ni nini lililoonyeshwa na ulizo la pili la Hagai na jibu alilopata?

7 Halafu “Hagai akasema, Kama mtu aliyetiwa unajisi kwa kugusa maiti, akigusa kimojawapo cha vitu hivi, je! kitakuwa najisi? Makuhani wakajibu wakasema, Kitakuwa najisi.” (Hag. 2:13; linganisha Hesabu 19:11-13.) Hapa makuhani walikubali kwamba kitu cho chote kichafu (najisi) kilichafua kitu kingine kilichokigusa.

8. Maulizo na majibu ambayo Mungu aliuliza kupitia kwa Hagai yalitimiaje?

8 Kwa kuwa Waisraeli walikuwa wakipuza ibada ya Mungu kwa sababu ya kuwa wenye shughuli wakitimiza tamaa zao za kujitafutia faida zao wenyewe, walikuwa wachafu. Kwa sababu hiyo, uchafu wao ulipitishwa kwa kila kitu walichogusa. Mungu alisema hivi: “Hivyo ndivyo lilivyo taifa hili mbele zangu, asema [Yehova]; na hivyo ndivyo ilivyo kila kazi ya mikono yao; na kitu hicho wakitoacho sadaka huko [katika madhabahu ya muda waliyokuwa wamesimamisha] ni najisi.” (Hag. 2:14) Kwa hiyo, upanzi wao wa mimea haukupata baraka ya Mungu juu ya mazao ya mashamba yao wala juu ya kazi ya mikono yao. Bali, ulipatwa na ukungu na ukavu.​—Hag. 2:15-19.

9, 10. Je! Waisraeli waliendelea kuwa wenye ubaridi juu ya kujenga hekalu? Yote yakawaje kwao?

9 Yehova asingeweza kuwabariki mpaka ‘wamrudie’ kwa kujisafisha waondoe ubaridi wao. Bado walitoa dhabihu, ndiyo, lakini Yehova anahesabu utii na uaminifu wa moyo wote kuwa wa maana zaidi kuliko dhabihu tu, au kuliko kujionyesha kwa mtu tu kuwa mwenye utawa.​—1 Sam. 15:22.

10 Jambo lenye kufurahisha ni kwamba historia ya Biblia inaonyesha Waisraeli hao walisikiliza mashauri ya Hagai na Zekaria wakamaliza ujenzi wa hekalu. Biblia inaonyesha pia kwamba Israeli walipata ufanisi, kama vile Mungu alivyokuwa ameahidi katika Kumbukumbu la Torati 28:1-14,​—Hag. 2:18, 19.

FUNDISHO KWA WAKRISTO LEO

11. Tunajuaje kwamba tunaweza kufaidika kwa kufikiria lililotukia kwa sababu ya Waisraeli kuwa wenye ubaridi juu ya ibada ya kweli?

11 Aliyosema Yehova na kufanya juu ya taifa la Israeli huko nyuma hayakuwa ya kuwafaidia wao peke yao. Yalifunua njia Yake ya kuwaza na kutenda. Kwa kufikiria mambo haya, sisi tunaweza kurekebisha maisha zetu sawasawa. Mtume Paulo aliandika hivi: “Basi mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi, tuliofikiliwa na miisho ya zamani.”​—1 Kor. 10:11.

12. Ni kanuni gani inayoonyeshwa na uhakika wa kwamba utakatifu usingeweza kupitishwa wakati nguo yenye “nyama takatifu” ilipogusa chakula fulani?

12 Tunaweza kufikiria mazungumzo ya Hagai pamoja na makuhani yanayohusu usafi na uchafu huku tukiyakumbuka maneno ya Paulo ili tuamue ni wapi yanapotuonya. Hapo tunaona kanuni ya kwamba mtu anayechukua kitu kitakatifu akiwa “chombo” cha Yehova hawezi kumpa mtu mwingine utakatifu vivi hivi tu au kwa vyepesi, bila jitihada. Kwa mfano, Wakristo wa kweli wanayo kweli ndani yao na roho ya Mungu ‘inakaa ndani yao,’ kuwafanya safi au watakatifu machoni pa Mungu. (2 Pet. 1:12; Rum. 8:9) Lakini inahitaji jitihada kwa upande wao kusema kweli na kuishi kulingana na kweli, kuendelea kuweka vyombo vyao “katika utakatifu na heshima.” (1 The. 4:4) Na watu wa ulimwengu mchafu wanaoonana tu na Wakristo hawawi watakatifu wala safi kwa sababu hiyo tu. Hata wakiikubali kweli ya habari njema, inahitaji wakati na jitihada kuwafundisha na kuwaonyesha mfano unaofaa, na bidii kwa upande wao wenyewe ili waweze kusikiliza, kujifunza na kusafisha maisha zao.

13. Ni kanuni gani inayoonekana katika uhakika wa kwamba kitu kichafu kilivifanya vitu kilivyogusa kuwa vichafu?

13 Kwa upande mwingine, Mkristo aweza kwa vyepesi kuchafuliwa kwa kushirikiana na wale wasiothamini kweli wala kanuni za Biblia. Ni kama vile mtume Paulo wa Kikristo alivyoonyesha: “Hamjui kwamba chachu kidogo hulichachusha donge zima?” (1 Kor. 5:6) Kwa hiyo, lazima Wakristo wajihadhari sana juu ya mashirika yao, kwa maana humo mna hatari kubwa. Walakini, linalosikitisha ni kwamba, ingawa jambo hili ni la kweli, wengine wanaoshirikiana na makundi ya mashahidi wa Yehova huenda wakadhani kwamba hakuna hatari yo yote kushirikiana sana na watu wasiobatizwa, wasio watumishi wa Yehova waliojitoa. Huu waweza kuwa mtego.

14. (a) Ni kwa kadiri gani imetupasa kushirikiana na wale tunaojifunza nao na wanaopenda kweli? (b) Kwa sababu gani ingekuwa hatari kushirikiana sana hata na watu ‘wenye kuheshimika’ wasiopendezwa sana na kweli?

14 Bila shaka, wako watu ambao pengine unajifunza nao, na wengine wa hawa ni watu wazuri sana, wanafanya maendeleo, wanapenda kushirikiana na wewe na washiriki wa kundi. Hawa wanahitaji kushirikiana na wewe kwa kadiri iliyo ya lazima ili uwatie moyo na kuwasaidia. Lakini wako wale wasiopendezwa na yanayosemwa na Biblia, au wasiotaka sana kusikiliza habari njema. Wengine wa watu hawa huenda wakawa wanyofu, watu wenye kuheshimika kulingana na kanuni za ulimwengu. Lakini kushirikiana sana nao ni kubaya, kwa maana watu wote ambao si Wakristo waliojitoa wanafanya mambo yasiyompendeza Mungu nao wanaweza kuchafua wengine. Wanaweza kumaliza wakati wa Mkristo, kuondoa akili na moyo wake katika ibada ya kweli. Katika Waefeso 2:3 mtume anawakumbusha Wakristo hivi: “Zamani, sisi sote nasi tulienenda kati yao, katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia, tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira kama na hao wengine.”

15. Ikiwa Mkristo ni mwenye ubaridi kwa ibada ya Mungu, anaweza kuingia katika mtego gani, naye anaweza kuwa na matokeo gani juu ya wengine?

15 Vivyo hivyo, ikiwa mtu aliyemo katika kundi la Kikristo ni mwenye ubaridi juu ya ibada safi na utumishi wa Mungu, kutojali na kupuza huko kungeweza kuwa chachu ya kiroho na kuambukia wengine kundini. Kwa hiyo, ikiwa wewe u Mkristo, jihadhari. Unaweza kuwa mchafu kwa kuwa mwenye kupuza ibada ya kweli. Unaweza kusitawisha ulegevu wa kutoshirikiana na watu wa Yehova mikutanoni, katika utumishi wa shambani, katika makusanyiko. Upendo wako kwa akina ndugu unaweza kupoa. Unaweza hata kupoteza imani, “dhambi ile ituzingayo kwa upesi.” (Ebr. 12:1) Halafu wewe mwenyewe unaweza hasa kuchafua wengine. Kwa kushirikiana sana na walimwengu, au hata na Wakristo ambao ni wenye moyo nusu-nusu, walio baridi au wenye woga kuelekea ibada safi, unaweza kukosa baraka za kiroho na hata uzima wenyewe.

UFANISI WA KIROHO KWA WALIO SAFI

16. Wakristo wa kweli wanatazamia baraka za namna gani kwanza kwa kufuata mwendo wa uaminifu, nao ushuhuda unaonyesha nini juu ya jambo hili?

16 Wale wanaojiendeleza kuwa safi, wakiendeleza imani yenye nguvu na kupendezwa na ibada safi na Wakristo wenzao, hawatazamii kupata ufanisi mwingi wa kimwili. Wao wanatafuta baraka na ufanisi wa kiroho. Wakati uo huo wanahakikishwa kwamba watapokea vitu vya kimwili ambavyo wanavihitaji kweli. (Mt. 6:31-34) Kuna ushuhuda wenye nguvu kwamba Yehova amemimina kwa wingi ufanisi wa kiroho juu ya mashahidi wake wa Kikristo katika wakati huu. Wao wametia kila jitihada kuhubiri habari njema za Ufalme mbali kama inavyowezekana. Kuhubiri kwao kumepanuka kufikia zaidi ya nchi 200, nalo ongezeko kubwa ajabu la mamia ya maelfu ya watu wanaojiunga nao kila mwaka katika ibada safi linashuhudia kwamba Yehova amewabariki. Haya ni mambo ya hakika ambayo yamewekwa katika kumbukumbu, nayo yanaweza kupatikana katika safu za Mnara wa Mlinzia na katika Yearbook cha kila mwaka cha mashahidi wa Yehova.

17. Tukiendelea kukesha, tunaweza kuwa na hakika ya jambo gani?

17 Yehova anawapenda sana watu wake naye atasaidia wale wanaompenda wafaulu. Nasi tukiendelea kukesha tunaweza kufurahia kwa uhakika matokeo yanayotajwa na mwandikaji wa Biblia: “Lakini sisi hatumo miongoni mwao wasitao na kupotea, bali tumo miongoni mwa hao walio na imani ya kutuokoa [nafsi] zetu.”​—Ebr. 10:39.

​—Kutoka Kitabu Paradise Restored to Mankind​—by Theocracy!

[Maelezo ya Chini]

a Tazama toleo la Julai 1 la kila mwaka.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki