Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa—United States ya Amerika
KATIKA kusanyiko la 1942 ilitangazwa kwamba wajumbe wa Watch Tower Society wangetembelea makundi ya watu wa Mungu kwa kawaida. (Hapo kwanza watumishi wa eneo la dunia ndio waliokuwa wakifanya kazi hiyo, lakini kazi zao pamoja na za watumishi wa majimbo, zilikomeshwa Desemba 1, 1941.) Wajumbe wenye kusafiri wa Sosaiti wangeanza kutumwa tena Oktoba 1. 1942. Ndugu hao walijulikana kama “watumishi wa akina ndugu,” ambao ndio waangalizi wa mizunguko wa siku hizi. “Walikuwa wakichunguza maandishi ya makundi na kusaidia ndugu waendeleze faida za Ufalme,” asema Dada J. Norris. “Jambo hilo lilitujulisha kwamba Yehova huangalia watu wake kwa kutumia tengenezo lake.”
WAKRISTO WASIOKUWAMO WASIMAMA IMARA
Usimamizi mpya wa Watch Tower Society ulipoendelea miaka michache iliyofuata 1940, Vita ya Ulimwengu ya Pili ilikuwa ikiendelea na wanaume kadha wa Kikristo walipatwa na jaribu la kuendeleza ukamilifu wao kwa Yehova. Mwaka wa 1940 vijana wa zaidi ya miaka kumi na minane waliagizwa kuingia utumishi wa kijeshi katika United States, lakini “wahudumu wa kawaida wa dini au walioagizwa karibuni” walipewa ruhusa ya kutoingia. Mashahidi wa Yehova wengi walikataliwa wasipangwe katika jamii moja ya wahudumu hao. Wao hawakufitini serikali, wala hawakujiingiza katika mambo ya kijeshi wala ya serikali za kibinadamu. Walakini, Mashahidi wenyewe waliamua kabisa kuendelea kutokuwamo katika mambo hayo kama Wakristo. (Yohana 17:16) Tena, walikuwa ‘wamefua panga zao zikawa majembe.’—Isa. 2:2-4.
Katika visa vingi sana, wakuu wa sheria walipinga wakisema ilikuwa lazima Mashahidi waingie jeshini kabla ya kuomba watetewe katika mahakma za serikali. Kwa hiyo baada ya kuwa katika mahakma za wilaya wenye kuendeleza ukamilifu walipelekwa gerezani, wengi wao wakahukumiwa kifungo cha miaka mitano na faini ya dola elfu kumi (shilingi 80,000 za sasa au 5.000Z).
KUKUSANYIKA KAMA SOSAITI YA ULIMWENGU MPYA
Hatua nyingine kubwa katika historia ya kitheokrasi ilifikiwa mwaka wa 1953. Watu wa Mungu walingojea kwa hamu siku za Julai 19-26 zifike. Walikuja kutoka nchi 96 zilizo nje ya United States, hata wakajaa katika uwanja Yankee Stadium wa mji wa New York. Sosaiti ya Ulimwengu Mpya Kusanyiko la siku nane lilitolea ulimwengu ushuhuda mwingi sana kwamba kuna umoja wa mataifa yote kati ya mashahidi wa Yehova wa Kikristo.
Tena, maelfu ya wajumbe wa kusanyiko walitafutiwa mahali pa kulala katika nyumba za watu. Wengine walilala katika hoteli na wengine 45,000 wakakaa katika New World Society Trailer City, maili 40 kutoka uwanja wa kusanyiko, karibu na New Market, New Jersey.
Kusanyiko hilo kubwa lilikumbukwa sana kama lenye kusisimua. Roger Morgan aandika hivi: “Hotuba iliyonipendeza zaidi katika kusanyiko la 1953 Yankee Stadium ni ya Ndugu Franz iliyosema ‘Sosaiti ya Ulimwengu Mpya Yashambuliwa kutoka Kaskazini ya Mbali.’”
Onyo lilitolewa jioni ya Alhamisi hiyo, Julai 23, 1953. Msimamizi mdogo wa Sosaiti, F. W. Franz, alieleza wazi juu ya shambulio litakaloletwa na Gogu wa Magogu na majeshi yake juu ya watu wa Mungu. Alijulisha kwamba Gogu, anayehusika hasa katika unabii, ni Shetani. Franz alionyesha pia kwamba nchi ya Magogu ndiyo makao madogo ya kiroho ya viumbe vibaya vya kiroho karibu na ujirani wa dunia baada ya kufukuzwa kwao mbinguni kufika mwaka wa 1918 (W.K.). (Ufu. 12:7-9) Msemaji alionyesha kwamba ufanisi wa sasa, umoja na usalama wa sasa wa watu wa Yehova ungemfanya Gogu na majeshi yake wawashambulie. Lakini lijapokuwapo shambulio hilo la kutisha Yehova angehifadhi sosaiti ya Ulimwengu Mpya. Wasikilizaji 112,700 walithamini sana onyo hilo la kuendelea kumtumaini Yehova na kuzitangaza habari njema za ufalme wake unaopitia kwa Kristo!
Wajumbe wa kusanyiko walipendezwa sana Jumapili alasiri, Julai 26. Watu 165,829 walikusanyika ndani ya Yankee Stadium, katika hema zenye kusongamana sana na katika Trailer City, wasikie hotuba ya watu wote ya N. H. Knorr iliyosema “Baada ya Har–Magedoni—Ulimwengu Mpya wa Mungu.”
MAPENZI YA KIMUNGU KUSANYIKO LA MATAIFA YOTE
“Wakati mwaka wa 1958 unapotajwa hata sasa,” aliandika Angelo C. Manera, Mdogo, “liko tukio moja kubwa linalokumbukwa na Mashahidi wa Yehova—lile ‘kusanyiko kubwa,’ Mapenzi ya Kimungu Kusanyiko la Mataifa Yote la Mashahidi wa Yehova. Hilo lilikuwa kusanyiko!” Wajumbe wa visiwa na nchi zisizopungua 123 walifika kwenye kusanyiko hilo linalojulikana sana. Ingawa wakati huo kulikuwa na mizozo kati ya mataifa, kukiwa na maelekeo ya kutokea vita katika Mashariki ya Kati, watu wa Yehova walikutana kwa amani na umoja katika uwanja Yankee Stadium wa mji wa New York na katika Polo Grounds zilizo karibu Julai 27 mpaka Agosti 3, 1958.
Kusanyiko kubwa hilo lilihudhuriwa na watu 253,922! Kwa kulinganisha na wasikilizaji waliokuwapo Ijumaa, bila shaka watu wa nje waliohudhuria walikuwa karibu 60,000. Wakati huo umati wa watu walisikia uhakikisho wa Maandiko wenye kusadikisha kwamba ufalme wa Mungu ulikuwa umekwisha anza kutawala tangu mwaka wa 1914 W.K. na kwamba mwisho wa ulimwengu u karibu.
KUSANYIKO LA KUZUNGUKA ULIMWENGU
Jambo la maana sana kwa watu wa Yehova lilianza katika Milwaukee, Wisconsin, Juni 30 likamalizika Septemba 8, 1963, katika Pasadena, California. Hilo lilikuwa “Habari Njema za Milele” Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova, nalo kweli lilikuwa kusanyiko la kuzunguka ulimwengu lililofanywa katika zaidi ya miji 24. Kwa ujumla, wajumbe 583 waliizunguka dunia Wasafiri hao mbalimbali wenye kwenda njia tofauti kidogo, walikusanyika pamoja na makundi ya waamini wenzao katika miji kama London, Stockholm, Munich, Jerusalem, New Delhi, Rangoon, Bangkok, Singapore, Melbourne, Hong Kong, Manila, Seoul na Honolulu.
Katika miezi iliyofuata kusanyiko hilo, sinema yenye kuvuta fikira ilimalizwa kutengenezwa na Sosaiti. Sinema hiyo ya saa mbili na yenye rangi yenye kujulikana kama “Kutangaza ‘Habari Njema za Milele’ Ulimwenguni Pote,” ilikuwa ya kusisimua sana. Sinema hiyo yaonyesha makusanyiko ya 1963 ya “Habari Njema za Milele” yaliyofanywa duniani pote, na jumla ya watu 580,509 walikusanyika kusikia hotuba ya watu wote ya kupendeza sana yenye kichwa “Wakati Mungu Ni Mfalme juu ya Dunia Yote.”
Miaka ya karibuni, waangalizi wa mizunguko wameonyesha vipande vya picha (slides) katika mikutano ya watu wote wakati wa kutembelea makundi ya watu wa Mungu. Vipande vya kwanza vilianza kuonyeshwa Septemba 1970. Hotuba yenye picha hizo za kwanza ilikuwa “Kutembelea Makao Makuu ya Ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova,” nayo ilikusudiwa kufahamisha watu tengenezo la Mungu kwa njia itakayowaongoza kuchukua hatua inayofaa. Nyingine yenye kujulikana kama “Kuchunguza Makanisa Zaidi,” ilisaidia watazamaji wajue kwamba wale wanaopenda kweli na haki hawapaswi kwenda katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Hotuba hiyo yenye picha ilitaka wajitenge na milki ya ulimwengu ya dini ya uongo na pia washiriki kusaidia wengine wakimbie Bebeli Mkuu. Hiyo ni mifano tu ya programu zenye vipande vya picha zilizotolewa na waangalizi wa mizunguko kama vielezo vya kutolea mafundisho ya Maandiko.
JAMBO JIPYA LA KUSISIMUA!
“Sikiliza Maneno ya Danieli kwa Siku Zetu.” Je! wewe wakumbuka sehemu hiyo ya “Wana wa Mungu wa Uhuru” Makusanyiko ya Wilaya ya 1966? Wajumbe walipokuwa wakiisikiliza hotuba hiyo, jambo la kushangaza lilitokea. Sauti mbalimbali zilitokea katika vipaza sauti zikifananisha Danieli, wale Waebrania watatu waaminifu—hata malaika. Kulikuwa na muziki, nao Waebrania watatu hao wakapewa nafasi ya mwisho waiinamie sanamu ya dhahabu iliyosimamishwa na Nebukadreza katika Uwanda wa Dura. Walakini, wao waliendelea na ufamilifu wao, wakakataa kuinama, wakakombolewa na Yehova.—Dan. sura ya 3.
Basi, mwaka wa 1966 ulikuwa mwanzo wa jambo fulani njia mpya ya kufundisha katika makusanyiko ya watu wa Mungu. Tangu mwaka wa 1966 michezo ya kuigiza ya Biblia imekuwa ikifanywa kwa kawaida katika makusanyiko makubwa ya watu wa Yehova. Mara nyingi michezo hiyo ya kuigiza inakuwa imekwisha fanywa mapema zaidi wakati wa kuhitimu kwa wanafunzi wa Watchtower Bible School of Gilead, na wanafunzi wenyewe ndio huchukua sehemu za watu wa kale na wa nyakati za kisasa.
MKAZO JUU YA KUFANYA WANAFUNZI
Vingine vya vitabu vya Kikristo wanavyopata watu wa Yehova vimetengenezwa hasa kwa kusudi la kusaidia watu wa Yehova watimize agizo lao la kuzihubiri habari njema na kufanya wanafunzi. (Mt. 24:14; 28:19, 20) “Let God Be True” kilikuwa kitabu cha namna hiyo, nacho kilichapwa mara ya kwanza mwaka wa 1946. Kilihusu mafundisho ya msingi ya Biblia. Halafu mwaka wa 1950 kitabu “This Means Everlasting Life” kilitoa habari zilizokuwa zenye maelezo mengi zaidi ya Biblia na juu ya maisha ya Kikristo. Fikiria pia kitabu chenye kurasa 416 “Mambo Mawili Yasiyobadilika Asiyoweza Mungu Kusema Uongo,” kilichochapwa mwaka wa 1965 kwa Kiingereza na 1968 kwa Kiswahili. Kwa kuwa kina masomo ya msingi ya Biblia, kimesaidia sana watangazaji wa Ufalme.—Kutoka 1975 Yearbook of Jehovah’s Witnesses.