Jumuiya ya Wakristo Kukutana Sasa na Uharibifu
(Makala ya funzo la kitabu)
1. Je! Jumuiya ya Wakristo inafurahia leo paradiso ya kiroho, na matumaini yake ni nini ya kuingia katika Paradiso yo yote ya Mungu?
KULINGANA na mambo yote ya hakika yanayotajwa mara nyingi, je! mtu mwenye unyofu wa moyo atasema kwamba Jumuiya ya Wakristo pamoja na washirika wake wengi, inajifurahisha paradiso ya kiroho leo kama inavyosimuliwa katika Biblia Takatifu? Je! wakati wa kufa, washirika wake wameandikiwa kwenda mbinguni wakale ya “mti wa uzima, ulio katika paradiso ya Mungu?” (Ufu. 2:7, NW) Au Jumuiya ya Wakristo itaachwa isiharibiwe na Yehova Mungu kwa sababu ina jina la kidini na madai yake iokoke taabu ya sasa ya ulimwengu na kuifurahia paradiso halisi ya kidunia wakati wa utawala wa miaka elfu unaokaribia wa Mwana wa Mungu, Yesu Kristo? (Luka 23:43, NW; SCB) Hakuna msingi wa Maandiko wa kusema Ndiyo kwa maulizo haya. Badala yake, linaloingojea Jumuiya ya Wakristo lilifananishwa na lililoipata nchi ya Edomu katika utimizo wa unabii wa Isaya, sura ya 34.
2. Nani leo wanaomtumaini Yehova kama Mwamuzi, Mfanya sheria na Mfalme wao, kama ilivyotabiriwa na Isaya, na kwa hiyo wanalindwa na magonjwa gani?
2 Ile mistari mitatu inayotangulia mwanzo wa sura hii ya 34 ya Isaya inatangaza hali ya kidini ambayo haijachukuliwa ama na Jumuiya ya Wakristo ama na dini ya Kiyahudi. Mistari hiyo inasomwa hivi: “[Yehova] ndiye mwamuzi wetu; [Yehova] ndiye mfanya sheria wetu; [Yehova] ndiye mfalme wetu; ndiye atakayetuokoa. Kamba zako [za meli za adui mwenye kushambulia] zimelegea; hawakuweza kukaza sana shina la mlingoti wao; hawakuweza kulikunjua tanga; ndipo mapato ya mateka yaligawanywa, hata wachechemeao [wa watu wa Yehova waliokombolewa] walipata mateka. Wala hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa [kiroho]; watu wakaao humo watasamehewa uovu wao.” (Isa. 33:22-24) Tofauti kabisa na Jumuiya ya Wakristo na dini ya Kiyahudi, mashahidi wa Kikristo wa Yehova, wanaokaa katika paradiso ya kiroho ya kibali na ulinzi wake, ndio wamemkubali Yehova kama Mfalme wao, Mfanya-sheria wao, Mwamuzi wao, Mwokozi wao. Kwa hiyo, hao ndio wanaolindwa na magonjwa ya kiroho na mapigo yanayosumbua Jumuiya ya Wakristo na dini ya Kiyahudi.—Zab. 91:1-10.
3, 4. (a) Katika Isaya sura ya 34, Yehova anayaarifu mataifa kwamba wamo katika nini? (b) Wanaarifiwa kwamba matokeo ya kesi hii yatakuwa nini?
3 Ikiufuatia sana unabii huo, sura ya 34 ya unabii wa Isaya inatoa maoni yenye kuogofya sana kwa mataifa ya kilimwengu. Maoni haya yatoa msingi wa kutofautishia hata ile paradiso ya kiroho yenye matumaini mema inayosimuliwa katika sura (35) inayofuata inakuwa wazi kabisa. Kwa sababu msiba uko mbele ya mataifa na kwa sababu watoka kwake Yeye, Yehova anatangulia kuyapasha mataifa na vikundi vya mataifa habari. Huenda leo mataifa yakadhani kwamba Mungu hashughuliki na jambo hilo, kwamba wao hawamo katika shauri lo lote na Mungu, kwamba wanaendesha mambo yao wenyewe kama wanadamu wenye fikira za kimwili na hawana lawama lo lote kwa Mungu Mkuu, kwa Muumba. Lakini kupitia kwa nabii Isaya, Yehova Mungu anavuta fikira za mataifa na kuwakumbusha kwamba kwa kweli wanashiriki kesi iliyo mbele ya Mahakma Kuu ya Ulimwengu Wote, na kwamba, kwa sababu hiyo, watahukumiwa.
4 Hivyo, ili kuanza sura ya 34, mneni wa Mungu asema hivi: “Karibuni, enyi mataifa, mpate kusikia; sikilizeni, enyi kabila za watu; dunia na isikie, nacho kiijazacho, ulimwengu na vitu vyote viutokavyo. Maana [Yehova] ana ghadhabu juu ya mataifa yote, na hasira kali juu ya jeshi lao lote; amewaangamiza kabisa, amewatoa waende kuchinjwa. Watu wao waliouawa watatupwa nje, na uvundo wa maiti zao utapaa juu, na milima itayeyushwa kwa damu yao. Na jeshi lote la mbinguni litafumuliwa, na mbingu zitakunjwa kama karatasi, na jeshi lao lote litanyauka kama vile jani la mzabibu linyaukavyo na kupukutika, na kama jani la mtini linyaukavyo na kupukutika.”—Isa. 34:1-4.
5. Hapa mataifa yanahukumiwa na Mungu kwa sababu gani, na ni mataifa gani yenye hatia zaidi?
5 Tunaloambiwa hapa ni hatia ya damu ya mataifa, ambayo miongoni mwao mataifa ya Jumuiya ya Wakristo yamekuwa yenye hatia zaidi kuliko yote. Wameilowesha dunia, si kwa damu ya wanyama-mwitu tu wanaouawa kwa mchezo tu, lakini zaidi kwa damu ya wanadamu. Hasa ni nani ambaye imemfaa kuwadai mataifa haya damu hii yote ambayo wamemwaga, akiitaka kutoka kwa mataifa kwa sababu damu ni mfano wa uhai uliopewa na Mungu? Si mwingineyo ila Muumba mwenyewe, Mpaji-Uzima, aliyewapa wanadamu damu yenye kuendeleza uhai. Mataifa yote ya leo yana majeshi yao ambayo yametayarishwa kwa wingi zaidi kuliko wakati wo wote zamani, na yote yako tayari wakiwa na vifaa na kuzoezwa kumwaga zaidi damu ya kibinadamu katika mapigano ya mataifa yote.
6. (a) Sheria ya Mungu kwamba ni lazima nafsi iwe kwa nafsi ni nzito kadiri gani? (b) Ni nini linaloonyeshwa na usemi wa kwamba “milima itayeyushwa kwa damu yao”?
6 Yehova Mungu hakuwa akicheza alipokuwa akieleza sheria yake ya haki, ni lazima Uzima uwe kwa uzima; nafsi kwa nafsi. (Mwa. 9:4-6; Kut. 21:23-25) Akiwa mwaminifu kwa sheria hii isiyoweza kutanguka, Yeye atatiririsha damu ya mataifa hayo hata wafe. Kuongezeka kwa hatia ya damu ya mataifa ni kukubwa sana hata ile damu inayodaiwa ili kumlipa Mpaji-Uzima ingetoa umajimaji wa kutosha kama kuyeyusha milima. Ndiyo, kuharibiwa kwa majeshi ya mataifa ya kilimwengu kungefuatana na kuharibiwa kwa serikali zao, ambazo, mara nyingine zinafananishwa katika unabii wa Biblia na “milima.”
7. Katika unabii huu, usemi huu “jeshi lote la mbinguni” wamaanisha nini, na jambo gani lalipata?
7 Nabii anaposema, “jeshi lote la mbinguni,” hamaanishi nyota na sayari za anga letu kama vile jua, mwezi na makundi ya nyota za mbali sana. Badala yake, serikali zilizo juu ya wanadamu zafananishwa na mbingu juu ya jamii ya kibinadamu ya kidunia kwa sababu ziko juu sana kama mamlaka zilizo juu. (Rum. 13:1-4) Hivyo ‘jeshi la mbinguni’ lingekuwa mwungano wa majeshi ya serikali hizi za wanadamu zilizo mfano wa mbingu. “Jeshi” hili, kwa wazi sehemu yenye nguvu zaidi ya serikali zilizo juu kama mbingu, “litafumuliwa,” litayeyuka, kama kitu fulani chenye kuharibika. Mbingu halisi juu yetu zaonekana kuwa zenye kupindwa kama kitabu cha kale cha kukunja, ambacho maandishi juu yake kwa kawaida yalikuwa upande wa ndani. Jua, mwezi na nyota za anga zetu zinaonekana kuwa upande uliokunjuliwa wa anga zetu, kama mambo yaliyoandikwa katika upande wa ndani wa kitabu cha kukunja.
8. Mbingu za mfano zinakuwa “kama karatasi” (kitabu cha kukunja) na “kama jani la mtini linyaukavyo na kupukutika” namna gani?
8 Wakati mambo yaliyoandikwa upande wa ndani wa kitabu cha kukunja yamepita mbele ya macho ya msomaji, ndipo kile kitabu cha kukunja kilichomalizwa kinapokunjwa na kuwekwa. Vivyo hivyo, “mbingu zitakunjwa kama karatasi” kitabu cha kukunja, katika maana ya kwamba serikali zilizo mfano wa mbingu ambazo “jeshi” lazo limeshiriki kwa kuonekana kurasa za historia ya kibinadamu lazima ziufikie mwisho wao, lazima zifikie ukurasa wa mwisho wa historia yao, na, kwa sababu hiyo, lazima zikomeshwe, ziharibiwe, ziondolewe zisiruhusiwe tena na Mungu kuwako. Zile za “jeshi” lao lenye kuvuta sana macho hupoteza hali ya kuwa na uzima na kuanguka, hutoweka machoni pa wale ambao wamesoma historia yao, kama majani yenye kunyauka na kupukutika katika mzabibu na kama tini lenye kunyauka linalopukutika katika mtini. Majira yao yameisha.—Linganisha usemi wa Ufunuo 6:12-14.
9, 10. Mistari inayofuata ya unabii wa Isaya yaonyeshaje kwamba zile “mbingu” zinazotajwa hapa si mbingu za kiroho zisizoonekana za makao ya Mungu?
9 Kwamba “mbingu,” ambazo “jeshi” lazo hufumuliwa au huyauka, hazipaswi kufahamika kama zile mbingu za kiroho zisizoonekana za makao ya Mungu, inaonyeshwa na sehemu zaidi ya unabii wa Isaya. Akijisema humo, Yehova asema.
10 “Maana upanga wangu umekunywa na kushiba mbinguni; tazama, utashukia Edomu [Idumaya, greek LXX], na juu ya watu wa laana yangu, ili kuwahukumu. Upanga wa [Yehova] umeshiba damu, umenona kwa unono, kwa damu ya wanakondoo na mbuzi, kwa mafuta ya figo za kondoo waume; maana [Yehova] umeshiba damu, umenona kwa unono, kwa damu ya wana-kondoo na mbuzi, kwa mafuta ya figo za kondoo waume; maana [Yehova] ana dhabihu huko Bozra [mji mkuu wa Edomu au Idumaya], machinjo makubwa katika nchi ya Edomu. Na nyati watatelemka pamoja nao, na mahasai pamoja na mafahali, na nchi yao italewa kwa damu, na mavumbi yake yatanoneshwa kwa shahamu. Maana ni siku ya kisasi cha [Yehova], mwaka wa malipo, ili kushindania Sayuni.”—Isa. 34:5-8.
11. Waedomu walikuwa akina nani, na walikaa katika nchi ya namna gani?
11 Ile nchi ya Waedomu, iliyoenea Araba kati ya Bahari ya Chumvi na Ghuba ya Aqaba, iliitwa “kilima cha Esau.” (Oba. 8, 9, 19, 21) Esau ndilo lililokuwa jina asili la mwanamume aitwaye Edomu. Jina la kupanga Edomu, maana yake’ “Mwekundu,” alipewa Esau kwa sababu alimwuzia haki yake ya uzaliwa pacha mdogo wake Yakobo (Israeli) ili apate chakula chekundu. (Mwa. 25:29-34; Ebr. 12:16, 17) Esau (au Edomu) alijaa chuki ya uuaji kwa ndugu yake pacha mwenye kufikiria mambo ya kiroho kwa sababu Yakobo alichukua haki yenye thamani ya uzaliwa. (Mwa. 27:30-45) Kwa sababu ya Esau kukaa katika sehemu yenye milima, alikaa juu, kana kwamba katika mbingu. Alipokuwa akiwaambia watu wa Esau (Waedomu) kwa kinywa cha nabii wake Obadia, Yehova alinena mambo kwa maoni hayo hivi:
“Kiburi cha moyo wako kimekudanganya, wewe ukaaye katika pango za majabali, mwenye makao yako juu sana; asemaye moyoni, Ni nani atakayenishusha mimi? Ujapopanda juu kama tai, ijapokuwa kioto chako kimewekwa kati ya nyota, nitakushusha kutoka huko; asema [Yehova].”—Oba. 3, 4.
12. (a) Ni nini linalomaanishwa na usemi wa kwamba upanga wa Mungu ungekunywa (ungelowa) na kushiba “mbinguni,” katika Isaya 34:5? (b) Wakubwa na wadogo katika Edomu wanatajwa kwa maneno gani?
12 Kwa hiyo anaposema juu ya kuharibu kwake taifa la Edomu kwa “upanga” wa vita, Yehova angeweza kusema kwa jinsi ya mfano kwamba upanga wake ungekunywa (ungelowa) “mbinguni,” ungejaa damu. Yeye alikuwa amewatoa Waedomu waharibiwe kwa haki, na uharibifu huu ungeifikia sehemu iliyo juu zaidi ya taifa la Edomu, kama inavyofananishwa na mji wake mkuu wa Bozra. Yehova anayasema machinjo ya taifa hili la uadui kama dhabihu, kwa maana ni katika kufikiliza hukumu yake na katika kujishuhudia kama Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote. Wakubwa na wadogo Yehova anawasema kama “nyati” na “mahasai pamoja na mafahali” na kama “wana-kondoo na mbuzi.” Nchi ya taifa hili lenye nia ya uuaji na lenye hatia ya damu lazima ilowe kwa damu yao wenyewe kwa njia ya “upanga” wa machinjo wa Yehova.
13-15. Waedomu walikuwa wamefanya nini hata wastahili tendo hili kubwa mikononi mwa Mungu?
13 Nchi ya Edomu ilistahili tendo hili kubwa; ama sivyo, lisingalikuwa tendo la haki ya kimungu. “Maana ni siku ya kisasi cha [Yehova], mwaka wa malipo, ili kushindania Sayuni.” (Isa. 34:8) Sayuni wa kale, ambako “kiti cha enzi cha [Yehova]” kilikuwa kimekaliwa na wafalme watiwa mafuta wa wateule wa Yehova, ulihusika. Katika mwaka wa 607 K.W.K., majeshi ya Kibabeli yalikuwa yameharibu mji mtakatifu na kuupindua Ufalme wa Yuda na kuwahamisha Wayahudi waliosalia kwenye nchi ya kipagani ya Babeli. Pindi hii moyo wa taifa la Edomu juu ya watu wa Yehova walioadhibiwa ulijionyesha wazi. Kwa namna gani?
14 Yehova anawaambia kwa njia ya nabii wake Obadia, akisema:
“Siku ile uliposimama upande, siku ile wageni [Wababeli] walipochukua mali [za Israeli], na watu wa kabila nyingine walipoingia katika malango yake, na kutupa kura juu ya Yerusalemu, wewe nawe ulikuwa kama mmoja wao.
“Lakini usiitazame siku ya ndugu yako, siku ya mashaka yake, wala usisimange juu ya wana wa Yuda siku ya kuangamizwa kwao; wala usinene maneno ya kiburi katika siku ya shida yao. Usiingie katika lango la watu wangu, siku ya msiba wao; naam, usiyatazame mateso yao, siku ya msiba wao; wala usitie mikono yako juu ya mali zao, siku ya msiba wao. Wala usisimame penye njia panda, ili kuwakatilia mbali watu wake wakimbiao; wala usiwatoe watu wake waliosalia, katika siku ya dhiki. Kwa maana hiyo siku ya [Yehova] i karibu juu ya mataifa yote; kama ulivyotenda, ndivyo utakavyotendwa; malipo yako yatakurudia juu ya kichwa chako mwenyewe. Kwa maana kama vile mlivyokunywa juu ya mlima wangu mtakatifu, ndivyo mataifa yote watakavyokunywa daima; naam, watakunywa na kubabaika, nao watakuwa kana kwamba hawakuwa kamwe.”—Oba. 11—16.
15 Mtunga zaburi aliyeongozwa alikumbusha juu ya mwendo ule ule wenye nia mbaya upande wa taifa ambalo ni la udugu, aliposali kwa Yehova na kusema: “Ee [Yehova], uwakumbuke wana wa Edomu, siku ya Yerusalemu. Waliosema, Bomoeni! Bomoeni hata misingini! Ee binti Babeli, uliye karibu na kuangamia, heri atakayekupatiliza, ulivyotupatiliza sisi.”—Zab. 137:7, 8.
MFANO WA KISASA WA EDOMU
16. Ni nini ulio mfano wa kisasa wa “nchi ya Edomu”?
16 Vilevile unabii wa Yehova hautakosa kutimizwa juu ya mfano wa kisasa, kile kilichofananishwa na “nchi ya Edomu.” Ni nini hicho kilichofananishwa? Ni Jumuiya ya Wakristo. Kama vile taifa la kale la Kiyahudi na Yerusalemu lilivyotumiwa na Yehova Mungu katika njia ya mfano, kufananisha mambo juu ya Jumuiya ya Wakristo, hivyo ndivyo na taifa la udugu la Edomu lilivyotumiwa na Yeye katika njia ya mfano. (1 Kor. 10:6, 11; Kol. 2:16, 17) Watu wa Edomu walikuwa wazao wa kimwili wa Esau, aliyepewa jina la kupanga la Edomu (“Mwekundu”). Babu yao wa taifa alikuwa ndugu-pacha mkubwa wa Yakobo, aliyekuja kuitwa Israeli. Kwa sababu ya kuwa mzaliwa wa kwanza wa Isaka na Rebeka, Esau aliona kwamba alikuwa na haki ya asili ya uzaliwa ambayo babu yake Ibrahimu alipitisha kwake.
17. Ni katika njia gani Jumuiya ya Wakristo imejionyesha kuwa sawa na Esau au Edomu?
17 Kama Esau au Edomu, Jumuiya ya Wakristo imejidai kuwa na ahadi ya Ibrahimu na inajiona kuwa uzao wa kiroho wa Ibrahimu, warithi wa ufalme wa kimbinguni pamoja na Yesu Kristo. Kulingana na madai yao ya kidini, washiriki wa Jumuiya ya Wakristo wanajifanya wenyewe kuwa ndugu-mapacha ya wale walio warithi halisi wa Kikristo wa ufalme wa Kimasihi wa Mungu, wanafunzi wa kweli wa Yesu Masihi. Hata hivyo, Jumuiya ya Wakristo haipendi wanafunzi hawa waaminifu wa Kristo waliotiwa mafuta. Inawachukia kwa chuki ya uuaji. (1 Yohana 3:12-15) Tangu mwanzo wa Jumuiya ya Wakristo katika kame ya nne W.K., imewachukia wale ambao ni Wakristo wa kweli. Hawa hufuata maneno na mfano wa Yesu katika kutokuwa sehemu ya ulimwengu huu, lakini Jumuiya ya Wakristo imejifanya yenyewe rafiki wa ulimwengu huu kwa kuwa sehemu yake. Kwa hiyo kile, ambacho ulimwengu unachukia nayo yakichukia. (1 Yohana 2:15-17; Yohana 15:19; 17:14, 16; Yak. 4:4) Kwa kuwatesa Wakristo wa kweli, inadhani inamtolea Mungu utumishi (ibada) mtakatifu.—Yohana 16:2.
18. Kama Waedomu wakati wa kuharibiwa kwa Jerusalemu katika mwaka wa 607 K.W.K., Jumuiya ya Wakristo iliwatendaje Waisraeli wa kiroho wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza?
18 Historia ya sasa ya karne ya 20 inashuhudia uhakika huu. Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza mabaki yenye uaminifu ya Israeli wa kiroho yalichukiwa na mataifa yote, kama Yesu Kristo alivyokuwa ametabiri kwa habari ya wafuasi wake wa kweli. (Mt. 24:9; 10:7-22) Sababu ya chuki hii ya ulimwengu ilikuwa kwa vile mabaki waliotiwa mafuta walitangaza ufalme wa Kimasihi wa Mungu kama ndio utawala wa dunia yote unaofaa, tumaini peke yake la wanadamu wote. (Marko 13:10-13) Wakati wa mateso na taabu yote juu ya mabaki yenye uaminifu, Jumuiya ya Wakristo haikutoa neno la kuwasikitikia. Kwa kweli, ushuhuda wa maandishi waonyesha kwamba mapadre wa Jumuiya ya Wakristo walichochea mateso haya juu ya watangazaji hawa wa “habari njema” za ufalme wa Kimasihi wa Mungu. Ilifurahi pamoja na mataifa yenye kupigana vita ya Jumuiya ya Wakristo juu ya kuzuiwa kwa watangazaji hawa wa Ufalme na kukomesha kazi yao ya kutoa ushuhuda wa hadhara, kama vile Waedomu walivyofurahi pamoja na Wababeli juu ya uharibifu wa Yerusalemu katika mwaka wa 607 K.W.K.—Ufu. 11:7-10.
19, 20. (a) Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, Jumuiya ya Wakristo ilionyeshaje tena kwamba ilikuwa na roho ya Edomu wa kale? (b) Katika utimizo wa neno la Mungu kupitia kwa Isaya, ni nini sasa linalowaelekea Waedomu wa kisasa, watu wa Jumuiya ya Wakristo, vilevile dini ya Kiyahudi?
19 Ikionyesha chuki kwa mabaki ya Waisraeli wa kiroho walioonekana kuwa tofauti kama Wakristo wa kweli na washiriki wake wa kanisa walioshiriki kumwaga damu katika vita vikali, Jumuiya ya Wakristo haikufurahi wakati mashahidi wa Ufalme waliozuiwa walipoamshwa kwa roho ya Mungu katika mwaka wa 1919 W.K. Haikufurahia paradiso ya kiroho walimoingizwa wale Waisraeli waliorudishwa. (Isa. 35:10) Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili ya miaka ya 1939-1945 W.K., iliyotokea mipakani mwake yenyewe, tena Jumuiya ya Wakristo ilichochea mateso ya kidini na ikajaribu vikali kuiharibu paradiso ya kiroho ya mabaki ya Israeli wa kiroho na waabudu wenzao wa Yehova Mungu. Lakini yote bure! Mashahidi wa Kikristo wa Yehova walisalimika wakatoka katika vita ya ulimwengu ya pili wakiongezeka idadi zaidi kuliko wakati wo wote zamani. Kwa sababu ya chuki hiyo kali upande wa Jumuiya ya Wakristo juu ya mashahidi wa Kikristo wa Yehova, je! Yehova Mungu ‘anashindania Sayuni’? Je! ‘mwaka wake wa malipo’ umefika juu ya Waedomu wa kisasa, “siku ya kisasi” ya Yehova?—Isa. 34:8.
20 Jibu ni Ndiyo! Na hivyo sasa Jumuiya ya Wakristo yakutana na uharibifu. Dini ya Kiyahudi pia yakutana na jambo lilo hilo!—Kutoka Kitabu Man’s Salvation Out of World Distress at Hand!, sura ya 12