Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Wakorintho wa Kwanza 7:14 linasema kwamba watoto wa wazazi wenye kuamini “ni watakatifu.” Je! ubatizo unatiwa ndani katika ‘utakatifu’ wa mtoto machoni pa Mungu? Namna gani kama maendeleo ya akili ya mtoto ni ya polepole?
Hapa mtume Paulo anazungumza matatizo ya jamaa ambayo katika hiyo wengine hawaamini. Alimtia mwenzi anayeamini moyo asimwache yule asiyeamini kisha akasema haya kama sababu yenye nguvu ya kuzuia ndoa isiharibike: “Kwa maana yule mume asiyeamini hutakaswa katika mkewe; na yule mke asiyeamini hutakaswa katika mumewe; kama isingekuwa hivyo, watoto wenu wangekuwa si safi; bali sasa ni watakatifu.” (1 Kor. 7:14) Hili laonyesha kwamba Mungu anaona watoto hao kulingana na kanuni ya kustahili kwa jamaa. Kustahili kwa jamaa maana yake ni utakatifu ule ambao Mungu anawaheshia watoto wachanga ambao ni watiifu, kwa kadiri mtoto anavyoweza kuwa na wajibu. Kustahili huku kunatokea kwa sababu ya sifa bora ya utakatifu na matendo mema waliyo nayo “wazazi . . . katika Bwana.” (Efe. 6:1) Kustahili huku kwa jamaa kunatumika hata wakati mmoja tu kati ya wazazi anaamini, kama maneno ya Paulo yaliyotangulia kutajwa yanavyoonyesha.
Basi, namna gani ubatizo? Mtoto mdogo anayefundishwa kwa uaminifu Neno la Mungu ataendelea katika maarifa na ufahamu, na mwisho afikie hali ya kuongozwa na roho ya Mungu ajiweke mwenyewe wakf kwa Yehova na kutaka kubatizwa. (1 Pet. 3:21) Ili awe tayari kubatizwa, inampasa afahamu uhitaji wake wa kutubu, kugeuka na kuingia katika uhusiano unaofaa pamoja na Mungu. (Matendo 3:19; 8:34-36) Baada ya ubatizo, hangekuwa tena chini ya kustahili au kibali ya wazazi, bali angeonwa kama ‘mtakatifu’ kwa ajili yake mwenyewe, akiwa mwenye daraka mbele za Mungu kufuatia maisha ya kujiweka wakf.—1 Pet. 1:14-16; Kol. 1:21-23.
Je! wazazi wa watoto ambao maendeleo ya akili zao ni ya polepole waone kwamba watoto wanatakiwa wabatizwe ili waonwe na Mungu kuwa wanastahili kulindwa katika nyakati za hukumu, kama vile wakati wa “dhiki kubwa” iliyotabiriwa? Linaloamua ni kadiri ya namna maendeleo ya akili yamekuwa ya polepole, kwa kuwa wengine wa watoto hao wanaendelea kuwa na akili ile ile ya mtoto mwenye umri wa miaka minne au mitano hata wanapokuwa watu wazima. Labda mtoto anaweza kufahamu mafundisho fulani ya msingi ya Neno la Mungu na kuyataja wakati anapoulizwa. Labda anatii wazazi na kuepuka kufanya mambo fulani ambayo ameambiwa kuwa ni mabaya na ni kinyume cha mapenzi ya Mungu. Lakini je! mtoto huyo aweza kujifanyia maamuzi mwenyewe, anaweza kuamua juu ya mwendo wa maisha anaotaka kufuata kwa akili na moyo wake mwenyewe (si kwa akili na moyo wa wazazi)? Je! anaweza kufahamu na kutafuta kuwa na uhusiano wa kipekee na Mungu, uhusiano usiotegemea wazazi wake? Je! anaweza kusimama mbele ya halmashauri ya hukumu, kwa sababu ya kosa analoweza kufanya? Kama hawezi, basi kwa wazi mtoto huyo hawezi kubatizwa ila angeendelea kuwa chini ya kustahili kwa jamaa machoni pa Mungu, ahesabiwe naye kuwa ‘mtakatifu’ katika maana hiyo.
Kwa sababu hiyo, shauri hili lisitazamwe kwa maono ya ndani bali juu ya msingi wa mafundisho ya Maandiko. Ikiwa akili za mtoto si ndogo sana na mtoto anaweza kweli kuwa mwanafunzi wa Mwana wa Mungu, amtumikie Mungu kwa ‘moyo, nafsi, akili na nguvu’ zake zote, basi anaweza kusaidiwa afikie hali ya kubatizwa. (Marko 12:30) Ndipo angeweza ‘kuchukua furushi lake mwenyewe’ la daraka la kiroho. (Gal. 6:5) Kama wana mashaka, wazazi wanaweza kuomba shauri kutoka kwa wazee.
Namna inavyotia imani nguvu na kufariji kujua kwamba watoto wanaweza kuonwa kama “watakatifu” kwa sababu ya kustahili kwa jamaa!