“Mbingu Mpya na Nchi Mpya” Zatazamiwa
(Funzo la kitabu)
1. Mashahidi wa Kikristo wa Yehova sasa wanatazamia nini kwa shauku?
MASHAHIDI wa Kikristo wa Yehova sasa wanafanya zaidi kuliko ‘kutazamia ile siku ya Yehova, na kuihimiza’ ambayo katika hiyo “mbingu” za mfano na “vitu vya asili,” na “dunia na kazi zilizomo” zitayeyuka, zitaharibiwa. Wanatazamia kwa shauku katika imani kile kitakachofuata mara hiyo “siku” hii ya kuyeyuka kwa taratibu hii ya mambo na kutiwa kwa Shetani na malaika zake za kishetani katika shimo refu lisilopimika. Wanasema pamoja na mtume Petro hivi: “Lakini, kama ilivyo ahadi yake, tunatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki yakaa ndani yake.”—2 Pet. 3:13.
2. Utimizo wa ahadi hiyo iliyoandikwa na Petro wapatanaje na utimizo wa ndoto ya Nebukadreza?
2 Kuja kwa “mbingu mpya na nchi mpya” kwapatana na wakati wa utimizo wa ile sehemu ya mwisho ya ndoto ya unabii ya Nebukadreza, yaani: “Na lile jiwe lililopiga sanamu liligeuka kuwa mulima mukubwa, na kujaza dunia nzima.” (Dan. 2:35, ZSB) Katika njia hii ule ufalme wa mbinguni wa Kimasihi unafananishwa kama mlima duniani, ‘ukiijaza dunia nzima.’
3, 4. Mbingu mpya na nchi mpya ni “kama ilivyo ahadi yake,” yaani, ahadi ya Yehova, katika njia gani?
3 Mtume Petro anasema kwamba zile “mbingu mpya na nchi mpya” zinazotazamiwa ni “kama ilivyo ahadi yake,” ahadi ya Yehova, ambaye Petro alitaja katika mstari unaotangulia. Ahadi ya kimungu ya namna hii, unamopatikana ule usemi uliotumiwa na Petro, imo katika Isaya 65:17, 18 na 66:22. Kwa uongozi wa Mungu, imeandikwa humo hivi:
4 “Maana, tazama, mimi ninaumba mbingu mpya na dunia mpya, na maneno ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini mufurahi, na mushangilie daima, kwa ajili ya hivi ninavyoumba; maana, tazama, ninaumba Yerusalema uwe shangwe, na watu wake wawe furaha.” “Kama vile mbingu mpya na inchi mpya, nitakazozifanya, zitabaki mbele yangu, BWANA anasema, ndivyo uzao wenu na jina lenu litabaki.”—Biblia ya Kiswahili ya Zaire.
5. Unabii huo wa Isaya ulipata utimizo mdogo wapi na wakati gani?
5 Ijapokuwa ulitumiwa na mtume Petro kuhusu wakati ujao, unabii huu wa Isaya ulioandikwa wapata mwaka wa 732 K.W.K., ulikuwa umetimizwa kwa kadiri ndogo karne fulani baada ya unabii wa Isaya. Hii ilikuwa wakati ile miaka 70 ya ukiwa na kushika sabato kwa nchi ya Yuda na Yerusalemu ilipomalizika na mabaki waaminifu wa Wayahudi waliohamishwa wakarudi kutoka Babeli kwenda kwenye nchi waliyopewa na Mungu katika mwaka wa 537 K.W.K. Yerusalemu ulijengwa tena na hekalu lake likajengwa upya karibu na mwaka wa 515 K.W.K., siku ya tatu ya mwezi Adari. (Ezra 6:13-22) Katika mwaka wa 455 K.W.K. kuta za Yerusalemu zilijengwa upya kwa usimamizi wa Nehemia, na huu ulikuwa ndio wakati wa mwadhimisho wenye shangwe. (Neh. 6:15) Mwisho Yerusalemu ukawa mji wenye kujulikana sana tena katika ulimwengu.—Dan. 9:24, 25.
6. Ni nini zilizokuwa “mbingu mpya” katika utimizo mdogo?
6 Katika utimizo mdogo huu wa unabii wa Isaya, zile “mbingu mpya” zilikuwa serikali mpya yenye haki ya Gavana Zerubabeli na waliomfuata. Serikali hii yenye makao makuu katika mji wa Yerusalemu uliorudishwa ilichukua mahali pa ile serikali mbaya ya Wafalme Yehoyakimu, Yehoyakini, na Sedekia, iliyopinduliwa na Wababeli katika mwaka wa 607 K.W.K. Vilevile Gavana Zerubabeli alitumiwa awe mfano wa aliye Zerubabeli Mkubwa Zaidi katika unabii ufuatao wa Hagai 2:23: “Katika siku ile, asema [Yehova] wa majeshi, nitakutwaa wewe, Ee Zerubabeli, mtumishi wangu, mwana wa Shealtieli, asema [Yehova], nami nitakufanya kuwa kama pete yenye muhuri; kwa kuwa nimekuchagua, asema [Yehova] wa majeshi.”
7. (a) Ni nini iliyokuwa “dunia mpya” wakati huo? (h) Je! unabii huo ulitimizwa kabisa-kabisa kule katika nchi ya Yuda iliyokaliwa tena?
7 “Mbingu mpya” hizo za mfano zilizotandaa kama serikali juu ya nchi ya Yuda iliyokaliwa tena zilikuwa na “dunia mpya” chini yazo. “Dunia mpya” hiyo walikuwa mabaki ya Kiyahudi waliotakaswa na kurudishwa waliokuwa wametoka Babeli wakajenga upya Yerusalemu na hekalu lake takatifu ili katika hilo wamtolee Yehova ibada safi iliyoamriwa na Torati ya Musa kupatana na agano Lake. (Isa. 66:8) Kwa vile utimizo huo wa kale wa unabii huo ulikuwa utimizo wa mfano na ulio mdogo tu, ule unabii unaosimulia hali za maisha chini ya “mbingu mpya” na katika “dunia mpya” ulitimizwa kwa kadiri ndogo tu: “Hawatadhuru wala kuharibu katika mlima wangu wote mtakatifu wote, asema [Yehova].” (Isa. 65:19-25) Zile “mbingu mpya” na “dunia mpya” katika utimizo ulio mkubwa zaidi wa Isaya 66:22 ndizo zilizotazamiwa kukaa mbele za Yehova Mungu milele.
8, 9. (a) Ni “mbingu mpya” gani tunazotazamia kama ilivyo ahadi ya Mungu? (b) Ufalme wa Kimasihi unakuwaje ‘mlima unaoijaza dunia nzima,’ kama ilivyotabiriwa na Danieli?
8 Hivyo, zile “mbingu mpya” ambazo Mashahidi wa Kikristo wa Yehova walikuwa wakitazamia kwa muda mrefu kama ilivyo ahadi Yake ni ule ufalme wa Mungu wa Kimasihi, mikononi mwa Mrithi wa Milele wa Mfalme Daudi. Kwa kuwa ufalme huu ndilo lile “jiwe” la kifalme linalowaponda-ponda wafalme wote wa kidunia na serikali zao katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni, haitaacha utawala wa kibinadamu wa kisiasa ukiwapo katika dunia yetu. Kwa sababu hiyo, ufalme huo wa Kimasihi ulio mfano wa jiwe wapaswa uwe kama mlima mkubwa unaoijaza na kuifunika dunia nzima. Je! hili lamaanisha kwamba ule ufalme wa Kiisraeli wa Daudi utasimamishwa tena na Kristo papa hapa duniani? Hapana! Hakutakuwako hata kuonekana kwa kidunia kwa ufalme wa Daudi katika uso wa dunia. Yesu Kristo, Mrithi wake wa Milele, hatatawala katika mwili, kwa kuonekana, katika mji wa Yerusalemu kule Mashariki ya Kati.
9 Makao yake ya serikali yatakuwa “mji wa Mungu aliye hai, Yerusalemu wa mbinguni.” (Ebr. 12:22; Ufu. 14:1) Serikali yake iliyo mfano wa mlima itachukua mahali pa serikali zote za kibinadamu za kisiasa zilizokuwa “mbingu” za mfano za taratibu ya kale ya mambo. (Isa. 34:3-5) Ndivyo zitakavyokuwako “mbingu mpya” za kiserikali zitakazokuwa hasa katika mbingu zisizoonekana, za kiroho.
10, 11. (a) Yesu Kristo atauondoaje uvutano wa Kishetani ambao umetawala “mbingu” za kiserikali za taratibu hii ya mambo? (b) Kwa sababu gani ahadi ya “mbingu mpya” ni yenye thamani sana kwa wale Walio Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho? (c) Katika Ufunuo 21:1-4, nini zilizo “mbingu za kwanza,” “dunia ya kwanza” na “bahari,” zinazotajwa, na mahali pazo panachukuliwa na nini?
10 Shetani Ibilisi amekuwa “mtawala” asiyeonekana ambaye ametawala “mbingu” hizo za kiserikali za taratibu hii ya mambo duniani. Ule “moto” wenye uharibifu wa “siku” ile ya Yehova utaziyeyusha, kuziharibu, “mbingu” hizo za kiserikali na kumwacha Shetani Ibilisi bila “mbingu” hizo ambazo ametawala juu yake kwa maelfu ya miaka. (Ufu. 13:1, 2; 19:19-21) Bila shaka hatatawala juu ya zile “mbingu mpya.” Cheo chake kisichoonekana cha kutawala mambo ya kidunia kitachukuliwa na utawala usioonekana na usio wa kibinadamu wa Mrithi wa Milele wa Daudi, Yesu Kristo, ambaye, kwa kufufuliwa kutoka kwa wafu, alifanywa kuwa roho asiyeweza kufa, asiyeweza kuharibika, mwenye nguvu zaidi kushinda Shetani Ibilisi na malaika zake wote wa kishetani. Shetani na malaika zake wataondolewa wasiwe karibu na dunia na kutiwa kizuizini wafungwe katika shimo refu lisilopimika ambalo katika hilo hawataweza kutawala “mbingu” zo zote ambazo zimetawala dunia. (Ufu. 20:1-3) Kwa kuwa sasa Yesu Kristo ni Mfalme wa kiroho wa mbinguni, “mbingu mpya” zake zitakuwa mbingu katika maana halisi. Mbingu nyingine za kiserikali hazitakuwako. Mtume Petro na Wakristo wenzake waliotiwa mafuta na kuzaliwa kwa roho waliweza kutazamia kwa shauku kusimamishwa kwa “mbingu mpya” hizo zilizoahidiwa. Kwa sababu gani? Kwa sababu wanayo ‘ahadi yenye thamani na yenye maana sana’ kutoka kwa Mungu kwamba watakuwa sehemu ya hizo “mbingu mpya” pamoja na Yesu Kristo, wakiwa waaminifu mpaka kufa. Wao ni warithi wa Mungu na warithi washirika pamoja na Yesu Kristo. (2 Pet. 1:4, NW; Rum. 8:16, 17) Wao kama kundi zima watakuwa sehemu ya “bibi-arusi” wa Mfalme Yesu Kristo. Hivyo zaidi ya karne nane Mungu alipokwisha kumtumia Isaya kutabiri juu ya “mbingu mpya na dunia mpya” Mungu alitoa ahadi zaidi ya mambo matukufu kupitia kwa mtume Yohana, aliyeandika hivi:
11 “Nikaona mbingu mpya na dunia mpya; kwa maana mbingu za kwanza [serikali za kisiasa pamoja na Shetani na malaika zake za kishetani] na dunia ya kwanza [jamii ya kibinadamu isiyomwogopa Mungu] zimekwisha kupita, wala hapana bahari tena [wanadamu wasiotulia, wenye msukosuko]. Mimi Yoane nikaona muji ule mutakatifu, Yerusalema mupya ukishuka toka mbinguni kwa Mungu, umewekwa tayari, kama bibi-arusi aliyekwisha kupambwa kwa mume wake. Nikasikia sauti kubwa toka mbinguni, ikisema: Tazama, hema ya Mungu ni pamoja na watu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake, na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao, atakuwa Mungu wao. Naye atapangusa kila chozi katika macho yao; wala mauti haitakuwa tena; wala maombolezo, wala kilio, wala uchungu hautakuwa tena; kwa maana maneno ya kwanza yamekwisha kupita. . . . Akasema nami, akisema: Kuja hapa, nami nitakuonyesha yule bibi-arusi, muke wa Mwana-Kondoo. Akanichukua katika Roho mupaka mulima mukubwa, murefu, akanionyesha ule muji mutakatifu, Yerusalema, ukishuka toka mbinguni, kwa Mungu.”—Ufu. 21:1-4, 9, 10, Biblia ya Kiswahili ya Zaire.
“DUNIA MPYA” YENYE HAKI
12. “Mkutano mkubwa” utakuwa nini katika “nchi mpya,” nao wataanza kufanya kazi wakiwa na hali gani zinazofaa?
12 Ule “mkutano mkubwa” wa wanaotazamiwa kuokoka “dhiki ile iliyo kuu” unazitazamia pia kwa shauku sana “mbingu mpya na nchi mpya.” “Nchi mpya” hii itakuwa ndiyo ile jamii mpya ya kibinadamu itakayokuwa ikiishi chini ya “mbingu mpya.” (Ufu. 7:9-14) Kama vile Nuhu na jamaa yake walivyoiokoka gharika ya dunia yote wakawa ndicho kiini cha jamii mpya ya kibinadamu duniani, ndivyo na “mkutano mkubwa” utakavyoiokoka “dhiki ile iliyo kuu” inayokaribia nao watafanyiza kiini cha milele cha jamii mpya ya kibinadamu, “nchi mpya” ya mfano. Wataanza kuishi katika paradiso ya kiroho itakayookoka “dhiki ile iliyo kuu” pamoja nao, lakini ndipo watakapoanza kuigeuza dunia halisi iwe paradiso ya kuenea dunia nzima. Wanyama wa mwitu na wa kufugwa, watakuwa katika amani pamoja nao.
13. Hali hiyo wakati huo itakuwaje bora zaidi kuliko ile ya Waisraeli waliorudishwa wakati unabii wa Isaya ulipopata utimizo mdogo?
13 Pendeleo la kuishi wakati huo katika dunia safi bila uchafu chini ya “mbingu mpya” zenye haki litakuwa lisilolinganishwa, lenye kupita ubora wa yale ambayo Waisraeli waliorudishwa waliona katika utimizo mdogo wa unabii wa Isaya katika jimbo la Uajemi la Yuda. Lo! ebu wazia kuishi duniani wakati “mambo ya kwanza yamekwisha kupita,” wakati mauti haitakuwapo tena, wakati kuombolezea wafu hakutakuwapo tena, wala kilio wala uchungu wa moyo!
14. Yehova atawafanyia hata wafu nini wakati huo?
14 Chini ya utawala wa Baba wa Milele, Yesu Kristo, na warithi washirika wake wa Ufalme, wale washiriki wa “mkutano mkubwa” watakuwa wakielekea uzima usio na mwisho katika paradiso ya dunia yote ya uzuri, shibe, furaha na amani. Hakutakuwako na uhitaji wa kuombolezea wapendwa waliokufa, kwa maana kupitia kwa “mbingu mpya” Mungu Yehova Mwenye Nguvu Zote atawafufua wanadamu waliokufa watakaofaidika na dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo iliyotolewa kwa ajili yao. (Yohana 11:25, 26; 5:28, 29; Matendo 24:15; Ufu. 20:11-14) Hawa watakaookolewa, kutia na wanaume na wanawake wenye imani tangu Habili mpaka Yohana Mbatizaji, watakuwa na nafasi ya kuwa sehemu ya “nchi mpya.”
15. (a) Tunawezaje kuwa na hakika kwamba, ijapo hali za ulimwengu ziwe mbaya zaidi, kutakuwako wokovu huo wa wanadamu? (b) Twahitaji kufanya nini kila mmoja sasa tuwe tayari kufaidika na wokovu huo?
15 Yaonekana kuwa jambo lisilosadikika kwamba taraja hilo lenye kufariji liko karibu mbele yetu sisi wa kizazi hiki. Hata hivyo ni lenye kusadikika! Hali za ulimwengu hazijapata kuendelea kuwa mbaya zaidi zamani kama zilivyo sasa. Taabu ya ulimwengu yaongezeka. Kutoweza kwa wanadamu kunazidi kuonekana zaidi. Haiwezekani faraja itokane na vyanzo vya kibinadamu. Hata hivyo wanadamu wataokolewa katika taabu mbaya zaidi ya dunia. Jamaa ya kibinadamu haitakufa imalizike. Haitauawa yote. Watakuwako wale wa jamaa ya kibinadamu watakaookoka taabu ya ulimwengu waingie katika taratibu mpya yenye haki ambayo ndani yake taabu ya ulimwengu ya namna hiyo haitatokea tena. Neno la Mungu Mwenye Nguvu Zote mwenyewe lasema hivyo. Kuishi kwetu sasa tukiwa na imani kamili katika neno hilo la kimungu kutatuwezesha tuokolewe katika taabu ya ulimwengu. Ule wokovu u karibu!—Mt. 24:21, 22; Nah. 1:9.—Kutoka Kitabu Man’s Salvation Out of World Distress at Hand! sura ya 17.