“Wakuu Katika Nchi Zote”
1. Ni mapendeleo gani yatakayopatikana kwa raia za kidunia za Mfalme Yesu Kristo kama inavyoonyeshwa katika Zaburi 45:16?
MAPENDELEO ya pekee ya utumishi yatatolewa kwa “mkutano mkubwa” wa raia za Mfalme Yesu Bwana-arusi, walio mfano wa kondoo. Mapendeleo hayo makubwa ya utumishi wa kidunia yanatajwa katika Zaburi 45:16: “Badala ya baba zako watakuwapo watoto wako, utawafanya kuwa wakuu katika nchi zote.”
2. Ni wanaume gani wanaostahili miongoni mwa wale watakaookoka Har–Magedoni ambao katika hao Mfalme anaweza kuchagua “wakuu katika nchi zote,” nao watakuwa wamepata ujuzi gani?
2 Wakiwa waokokaji duniani wa taabu ya ulimwengu ambayo katika hiyo “ulimwengu wa wale wasioogopa Mungu” utaharibiwa, watapatikana mara hiyo ili Baba wa Milele anayetawala achague kutoka kati yao wanaume wanaostahili, “watoto” wake, wawekwe kama “wakuu katika nchi zote.” Hata katikati ya makumi ya maelfu ya makundi ya Mashahidi wa Kikristo wa Yehova leo kuna maelfu ya wanaume waliojiweka wakf na kubatizwa, ambao wamewekwa kitheokrasi katika cheo cha kutumikia kama wazee. Wanatumikia kama “waangalizi” na kufanya kazi ya uchungaji katikati ya makundi wanayoshirikiana nayo. (Matendo 20:17-28; Flp. 1:1; 1 Tim. 3:1-7; Tito 1:5-9; 1 Pet. 5:1-4) Wanaongoza pia katika kazi ambayo Yesu Kristo alitabiria huu “mwisho wa taratibu ya mambo,” yaani: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14, NW) Katika njia hii wanajaribu kutimiza daraka lao kwa ufalme wa Kimasihi wa kimbinguni uliosimamishwa wakati Majira ya Mataifa yalipokwisha katika mwaka wa 1914.
3. Wazee hawa wa makundi wamekwishaanza kutumikia katika cheo gani, kama ilivyotabiriwa katika Isaya 32:1, 2?
3 Wazee au waangalizi hawa wa makundi wanautimiza kwa uaminifu mfano wa unabii wa “wakuu” wanaosimuliwa katika Isaya 32:1, 2: “Tazama, mfalme atamiliki kwa haki, na wakuu watatawala kwa hukumu. Na mwanadamu atakuwa kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” Kwa njia hiyo si “wakuu” wa kidini wenye kuonea, kama wale katika madhehebu za kidini za Jumuiya ya Wakristo wanaoitwa “Wakuu wa Kanisa.” Pahali pa kufanya hivyo, kila mmoja wa wazee hawa wa makundi anatafuta kuwa mtoaji wa faraja, burudisho, kwa washiriki wa kundi lake. Anakuwa mwangalifu kutumikia kama vile wazee katika Israeli wa kale wangetumikia, “kwa hukumu” peke yake. Kwa njia hiyo anafuata mfano wa Mfalme wake wa kimbinguni, anayetawala “kwa haki” peke yake.—Luka 22:25-27.
4, 5. (a) Je! “dhiki kubwa” itawaondoa wazee katika cheo chao cha kitheokrasi? (b) Hivyo, watapatikana wafanye utumishi gani kwa kutii mapenzi ya Yesu Kristo, Mfalme wa kimbinguni?
4 Wakati “dunia mpya,” jamii ya kibinadamu itakayoanzishwa chini ya ufalme wa “mbingu mpya” itakapoanza kutenda kazi, kutakuwako na uhitaji wa waangalizi na wasimamizi wa jamii za watu na matendo. Wazee watakaookoka ile “dhiki kubwa” na kuwa sehemu ya “dunia mpya” watakuwa wamepata ujuzi mwingi kwa utumishi wao wanaotoa sasa katika makundi ya Mashahidi wa Kikristo wa Yehova. Ile “dhiki kubwa” haitakuwa imewaondoa katika cheo cha kitheokrasi cha wazee na waangalizi miongoni mwa washiriki wa makundi yatakayookoka pamoja nao kuingia katika Taratibu Mpya yenye haki ya Mungu. Wataendelea na cheo hiki, ikiwa yatakuwa mapenzi ya Yesu Kristo Mfalme.
5 Kwa vyo vyote, wazee wenye ujuzi na waangalizi watapatikana ili Mfalme wa Kimasihi awaweke kama “wakuu katika nchi zote,” tangu mwanzo wenyewe wa utawala wake wa miaka elfu. Lo! litakuwa pendeleo lao namna gani kuwa wajumbe watakaokuwa wakionekana duniani wa Ufalme wa miaka elfu!
6, 7. (a) Ni wakati gani watakaporudi kutoka kwa wafu kwa njia ya ufufuo, nani wengine watakaotiwa kati ya “wakuu katika nchi zote”? (b) Ni kwa sababu gani haitazamiwi kwamba hawatapata taabu yo yote kubwa katika kuzizoelea hali mpya duniani?
6 Waokokaji wote wa “dhiki kubwa” watatazamia kwa shauku ufufuo wa wanadamu waliokufa waliokombolewa. Wataitazamia “saa” hiyo ambayo katika hiyo wale wote waliomo katika makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti ya Yesu, Mwana wa Adamu aliyetukuzwa, na hawa wote watakaosikia watatoka kwenye ufufuo wa nafasi zenye kutoa uzima chini ya Ufalme wa miaka elfu. (Yohana 5:28, 29; 11:25, 26; Matendo 24:15; 1 Tim 2:5, 6) Hasa watatazamia ufufuo wa “baba” waaminifu wa Mfalme Bwana-arusi. Lo! namna watakavyoshangilia kufufuliwa kwa Henoko, Nuhu, Shemu, Ibrahimu, Isaka, Yakobo, Boazi, Daudi, Hezekia na Yosia! Hawa watakuwa vifaa bora kuwekwa katika utumishi wa kuwa “wakuu katika nchi zote.” Wakiwa tena katika nchi ya walio hai na sasa katika utumishi wa kuwa wakuu, watamwongezea Mfalme wa Kimasihi heshima zaidi ambaye zamani walipendelewa kuwa babu zake za kidunia.
7 Namna gani, pia, manabii wengine wote na wale wenye kuonyesha mfano wa imani, kama vile Habili, Ayubu, Musa, Isaya, Yeremia, Ezekieli, Danieli, na wengine, mpaka Yohana Mbatizaji, mtangulizi wa kidunia na “rafiki yake bwana arusi,” Yesu Kristo? Kulingana na ushuhuda mzuri wa Biblia juu ya watu hawa, wamejionyesha kustahili kuwekwa kama “wakuu katika nchi zote” na yeye waliyetazamia kuja kwake kama Masihi, wengi wao hata wakakutabiri. Bila taabu kubwa, na kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu, wanaume hawa wenye uwezo wataweza kuzizoelea hali mpya duniani wakati wa kipindi cha saba cha miaka elfu ya kuwapo wanadamu duniani. Sifa zote za Biblia zinaonyesha wanafaa heshima ya kutumikia kama “wakuu katika nchi zote.” Wazee na waangalizi wa makundi watakaookoka “dhiki kubwa” wataweza kuwapa wote hawa msaada wa mambo ya karibuni.
8. (a) “Wakuu” hao watakuwa wajumbe wa nani watakapokuwa wakiifanya kazi yao? (b) Ni kwa sababu gani kutakuwako kazi kubwa mno ya kutoa elimu itakayofanywa wakati huo?
8 Kuwa na “wakuu katika nchi zote” watakaotawala “kwa hukumu” yenyewe kunatoa uhakikisho wa kwamba katika “dunia mpya” kweli haki itakaa, itadumu milele. “Mbingu mpya” za Kimasihi zikiwako juu, na “wakuu” kama hawa wakitumikia kama wajumbe wanaoonekana wa “mbingu mpya” hizo, kazi ya kuipamba dunia itasonga mbele ipate kuwa makao ya milele ya kiparadiso ya wanadamu. Maelfu ya mamilioni ya wafu watakaofufuliwa watashiriki kwa njia hiyo kupamba dunia yote kwa utukufu wa Paradiso. (Luka 23:43, NW; ZSB) Kazi ya elimu ulimwenguni pote itaendelea kupanuka wakati kizazi baada ya kizazi cha wanadamu watakaporudi kutoka makaburi ya ukumbusho. Wataonyeshwa namna Biblia Takatifu ilivyo historia ya kweli ya matendo ya Mungu pamoja na wanadamu na namna unabii wote wa Biblia umetimia na bado utatimia. Watapashwa habari ya mambo yaliyomo katika vile “vitabu” vyenye maagizo ya kimungu vitakavyofunguliwa wakati huo.—Ufu. 20:12.
9. (a) Mashahidi wa Yehova wanaoshiriki kwa bidii kazi ya sasa ya kutoa elimu wana matumaini gani yenye furaha mbele yao? (b) Ni katika njia gani Yesu Kristo, Baba wa Milele, atakuwa “roho yenye kuhuisha” (roho yenye kutoa uzima)?
9 Matazamio ya mashahidi wote wa Yehova waliojiweka wakf na kubatizwa wanaofanya leo kazi ya elimu ya Biblia kwa bidii katika dunia yote inayokaliwa na watu, ni yenye furaha kweli kweli. Ni kazi yenye kutoa uzima itakayowezesha watu wasio na hesabu waokoke kufikilizwa kwa hukumu za uharibifu za Mungu katika “dhiki kubwa” inayokuja. Ni kazi inayowatayarisha na kuwawezesha kufanya kazi iliyo kubwa zaidi ya kutoa elimu kwa ajili ya wanadamu waliokufa waliokombolewa ambao Yesu Kristo Mfalme anayetawala ataita watoke ili awe Baba yao wa Milele. Ndiye anayetajwa na 1 Wakorintho 15:45: “Adamu wa mwisho ni roho yenye kuhuisha.” Akiwa hivyo, atawapa uzima kwa kufufuliwa kwao na pia kwa kuwalea wapate uzima wakati wa utawala wake wa miaka elfu.
10. (a) Ni wakati gani wenye utii wote watakapopewa zawadi ya uzima wa milele? (b) “Usimamizi” wa Yehova unaotajwa katika Waefeso 1:9, 10 utatimiza namna gani kusudi lake tukufu kwa kufaa, wakati huo?
10 Karibu na mwisho wa utawala wake wenye kutoa uzima wenye kuitikia na wenye utii wote wataifikia hali tukufu ya ukamilifu kama aliokuwa nao Adamu wa kwanza katika paradiso ya kwanza, Bustani ya Edeni. Zawadi yao itakuwa uzima wa milele, wakionyesha ushikamanifu wao katika jaribu la mwisho kwa Baba wa Kimbinguni na Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote. Ndipo ikiwa imepambwa kila mahali katika uzuri wa Paradiso, dunia itaungana tena na mbingu takatifu. Mpango wa Yehova wa “usimamizi” utakuwa umetimiza kabisa kusudi lake tukufu. “Vitu vyote,” “vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani,” vitakuwa vimekusanywa tena pamoja “katika Kristo,” katika yeye ambaye Yehova Mungu amefanya Kichwa cha tengenezo lake kuu, Yesu Kristo Mwanawe. Wakifurahia paradiso ya kiroho na paradiso kama ile ya Edeni, wanadamu tena watakuwa sehemu ya tengenezo la Yehova la ulimwengu wote. Umoja na amani yatakuwamo miongoni mwa viumbe vyake mbinguni na duniani. (Efe. 1:9, 10, NW) Wanyama wa duniani watatii wanadamu.
TUTAFANYA NINI SASA?
11. Ni lazima tukaze sana macho yetu ya imani juu ya nini, na kwa sababu gani tunaweza kuwa na hakika ya kwamba yatatimizwa?
11 Maoni ambayo Neno hakika la Mungu linatoa kwenye macho yetu ya imani juu ya wakati ujao, ni mazuri sana! Jambo la kufanya sasa ni kutopoteza maoni hayo. Tusiache macho yetu yaondolewe katika maoni hayo hata kidogo. Si jambo la kuwaza tu, si madanganyo tu ya macho, si ndoto tu. Yale mambo mazuri ajabu yatakayokuja—upesi—yanahakikishwa kabisa katika unabii wa Neno lake lisiloharibika kwa jina la Mungu mwenyewe. Tunayaelekea kwa kadiri wakati unavyosonga mbele. Ndio mradi uliowekwa mbele yetu na Mungu ambaye “huwapa thawabu wale wamtafutao.” (Ebr. 11:6) Tukishikamana na imani yetu na kuishi na kutenda kupatana nayo, hakuna jambo litakalotuzuia kuipata zawadi ambayo Mungu anatutolea na kutuahidi.
12. Je! kuharibiwa kwa Babeli Mkuu kutaondoa vizuizi vyote, au hali itakuwa namna gani?
12 Bila shaka wanaotaka kuzuia watajitokeza mbele yetu. Ijapokuwa ile siku na saa ile ya kutokea “dhiki kubwa” haikufunuliwa kwetu, imewekwa na Mungu nayo haitakawia. (Hab. 2:3) Ile “dhiki kubwa” imo katika kusudi la Mungu lililotangazwa na ni lazima itakuja. Na tukumbuke kwamba kuharibiwa kwa Babeli Mkuu wa kidini katika sehemu ya kwanza ya ile dhiki hakutatuondolea kizuizi kabisa. Kunatoa nafasi tu ya wenye kuzuia wengine wa mwisho watuzuie kwa umoja tusiufikie mradi wetu tuliowekewa na Mungu. Hapo tutafanya nini?
13. Ile hali yenye hatari itakayokuwako wakati huo yatukumbusha hali gani iliyotukia zamani?
13 Ile hali yenye hatari itakayojitokeza mbele yetu wakati huo inatukumbusha juu ya Waisraeli walioonekana kama wamenaswa upande wa Misri wa Bahari ya Shamu upesi baada ya Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 1513 K.W.K. Bahari yazuia mbele yao njia yao ya moja kwa moja kuelekea Mlima wa Mungu, Mlima Sinai, katika mkono wa nchi wa Arabuni. Kambi yao karibu na bahari yatishwa kutoka upande wa nyuma. Wamisri hawa wanakuja! Magari ya vita na wapanda farasi wakiongozwa na mfalme Farao wa Misri yanaijia kambi ya Israeli. Itachukua muda gani kabla majeshi ya vita ya Farao hayajawashambulia? Lo! mambo yanaogofya kweli kweli! Katika hali hizo vilio vyamfikia Mungu, ambaye hawawezi kufahamu sababu yake anawaongoza katika hali hii yenye hatari.
14. Wakipatwa na hali hii yenye kuogofya sana, ni jambo gani lililoonekana haliwezekani ambalo Mungu aliwaamuru wafanye?
14 Sasa wanasikia amri gani? Kwa namna mambo yalivyo, haisadikiki, haiwezekani! Amri ya kimungu yaamuru kuvunja kambi, si kwa kukimbia adui kwa woga wa ghafula, bali watoke mbali nao. Hiyo ilimaanisha—kuingia baharini! Ndiyo, Kusonga mbele! “Yule Wa Milele akamwambia Musa, ‘Kwa nini kunililia mimi? Waambie Waisraeli wasonge mbele. Na wewe, inua fimbo yako na kuunyosha mkono wako juu ya bahari; uitenge katika sehemu mbili, ili Waisraeli wapate kupita katika nchi kavu kupitia baharini. Nitawafanya Wamisri kuwa wagumu sana hata wataingia wawafuatie, nami nitajipatia heshima kutoka kwa Farao na jeshi lake lote, magari na wapanda farasi wake—niwafundishe Wamisri ya kwamba mimi ndimi Wa Milele, wakati nitakapojipatia heshima tena kutoka kwa Farao na magari yake na wapanda farasi wake.’”—Kut. 14:15-18, Moffatt; Byington; Jerusalem Bible; An American Translation; Revised Standard Version.
15. (a) Adui walinaswa katika mtego namna gani wakaharibiwa kabisa? (b) Wakati huo Waisraeli wakawa na sababu ya kufanya nini?
15 Baada ya kuvunja kambi watu wa Mungu wenye kutishwa wanasonga mbele wakipita katika njia ambayo Mungu Mwenye Nguvu Zote amefanya katika Bahari ya Shamu. Wanapita moja kwa moja mpaka kwenye pwani za mkono wa nchi wa Sinai. Ile njia ya kuokokea baharini yaachwa wazi iwashawishi Wamisri. Wamisri waliozuiwa kwa muda wasiishambulie kambi ya Waisraeli, sasa wanaanza tena shambulio lao kali. Wajitupia katika ile njia iliyoachwa katikati ya bahari na kufuatia kwa ukali. Karibu wote wamo ndani ya njia ya baharini. Ndipo magari yaanza kusumbua na kuzuia maendeleo. Haya—rudini nyuma kabla Mungu wa Waisraeli hajawapigania! Lakini ni kuchelewa mno. Kwa ishara ya Musa akiwa na fimbo yake ya nabii, ule mtego wafyatuka. Yale maji ya bahari iliyotengwa yaenda pamoja kwa nguvu. Majeshi yote ya vita ya Farao yagharikishwa. Maiti zao zinatupwa kwenye pwani za mkono wa nchi wa Sinai. Haya nyie, Waisraeli, imbeni na kucheza sasa kwa ajili ya kuokolewa kwa mkono wa Yehova.—Kut. 14:19 mpaka 15:21.
16. (a) Mambo hayo yaliandikwa katika Biblia ili nani wafundishwe? (b) Tutakaposhambuliwa kabisa na Shetani Ibilisi na vikosi vyake vya mataifa yote, itatupasa tushikamane na azimio gani?
16 Mambo hayo, yaliyotangulia kuandikwa, yaliandikwa ili kutufundisha sisi katika wakati wenye hatari kuliko wakati wote. (Rum. 15:4) Lile shambulio litakalofanywa wakati ujao na zile pembe kumi na yule mnyama-mwitu mwekundu sana ambaye wakati huo atakuwa bila wa kumpanda litakuwa tisho kuu kwa maisha yetu na kwa paradiso yetu ya kiroho, watakapokwisha kuharibu kwa chuki ile milki ya ulimwengu ya Kibabeli ya dini ya uongo. (Ufu. 17:14) Shambulio lote la Gogu wa mfano wa nchi ya Magogu (Shetani Ibilisi) na vikosi vyake vya mataifa yote litalengwa juu ya uhusiano wetu na Yehova Mungu uliorudishwa na kusimama kwetu imara kwa ajili ya enzi kuu ya ulimwengu wote na ufalme wake wa Kimasihi. (Eze. 38:10-17) Mataifa yote yanayopinga dini yatawachukia sana sana Mashahidi wa Yehova. Basi sisi tutafanya nini—tukate tamaa? Hasha (hata kidogo)! Azimio letu lililokwisha kupitishwa ili kupambana na hali hiyo yenye hatari, ni kushikamana na mwendo utakaofanya Yehova ashuhudiwe haki ya kuwa Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote!
17. Amri ya kusonga mbele kwa umoja itakuwa na maana gani kwetu?
17 Ijapokuwa huenda likaonekana kuwa jambo lisilowezekana, ile amri kutoka kwa Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu kupitia kwa Musa wake Mkubwa zaidi, Yesu Kristo, itasikika sana na waziwazi masikioni mwetu, ikisema, ‘Songeni mbele! Nendeni kwa umoja!’ Maana yake, Endeleeni kufanya mapenzi ya Yehova Mungu kama mtawala kuliko kutii wanadamu. Endelea kuwa, mwanafunzi wa yeye ambaye Yehova ametia mafuta awe Mfalme wa Kimasihi juu ya wanadamu kwa muda wa miaka elfu inayokuja! Basi, songa mbele, ukiutazamia mradi. Bado uko mbele. Kusonga mbele bila kugeuka upande huu wala huu kutatufikisha huko kwa ushindi. (Ebr. 10:39) Hata adui ajaribu sana kuturudisha katika utumwa wa ulimwengu huu usiomwogopa Mungu, atashindwa.. Mungu Mwenye Nguvu Zote atatufungulia njia ya kupitia kuelekea pwani za uhuru. Yule adui, akiwafuatia-fuatia waabudu wenye kusonga mbele wa Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu kwa kusudi la kujilipiza kisasi, ataingia katika mtego wa uharibifu.
18. Ni pendeleo gani ambalo halitatolewa tena litakalokuwa fungu la wale watakaokuwa hai wakati huo?
18 Huo utakuwa wakati mtukufu tutakapoweza kumwiga nabii Musa na Waisraeli baada ya kuokolewa kwao katika Bahari ya Shamu na kuimba wimbo wetu wenyewe tukiyasimulia matendo ya uhodari ya Yehova, “mtu [hodari] wa vita” katika Har–Magedoni na kufikia upeo wa wimbo wa mwadhimisho kwa kusema: “[Yehova] atatawala milele na milele.” (Kut. 15:1-18) Bila shaka mbingu na pia watazamaji wa ushindi wa mwisho wa Yehova watakaookoka duniani wataimba kwa umoja sifa za Mfalme wa sasa wa ulimwengu wote asiyepingwa. Lo! namna litakavyokuwa pendeleo lisiloweza kutolewa tena kujikuta tumo miongoni mwa waimbaji hao wa ushindi!
19, 20. (a) Maneno ya Zaburi 66:10-12 yanapatana namna gani na yaliyowapata wale ambao, kama Mashahidi wa Kikristo wa Yehova, wameishi kupitia matukio ya tangu mwaka 1914 W.K.? (b) Bila kujali taabu zilizoko mbele ya mabaki ya Israeli wa kiroho, wana maneno gani yenye maana na yenye kutumainisha katika Isaya 43?
19 Taabu ya ulimwengu isiyo na mfano wake iko mbele yetu sasa hivi, lakini na tukutane nayo pasipo kuogopa. Sisi wazee wa “kizazi hiki” tuliovipita vita’ viwili vya ulimwengu tangu mwaka wa 1914 W.K. tukapatwa pia na mateso ya kidini juu ya Mashahidi wa Kikristo wa Yehova ambayo yametukia miaka yote tangu mwaka 1914, twaweza kusema kweli kweli pamoja na mtunga zaburi wa Biblia wa kale hivi: “Umetupima, Ee Mungu, umetujaribu inavyojaribiwa fedha. Ulituingiza ndani ya wavu, na kuweka viunoni mwetu mzigo uliotulemea. Uliwapandisha watu juu ya vichwa vyetu. Tulipita motoni na majini; ukatutoa na kutuleta kunako wingi.” (Zab. 66:10-12) Huenda bado ikatupasa kupita “motoni na majini” katikati ya taabu ya ulimwengu iliyo kali zaidi kupita taabu zote ambayo sasa iko mbele yetu. Lakini watiwa mafuta wa Israeli wa kiroho wanayo maneno haya yenye kutumainisha kutoka kwa Yehova Mungu:
20 “Lakini sasa, [Yehova] aliyekuumba, Ee Yakobo, naye alikufanya, Ee Israeli, anasema hivi: Usiogope, maana nimekukomboa, nimekuita kwa jina lako; wewe ni wangu. Wakati unapopita katikati ya maji nitakuwa pamoja nawe; na katikati ya mito, haitakugarikisha; wakati unapotembea katikati ya moto, hutaungua, wala ulimi wa moto hautakuchoma. Maana mimi ni [Yehova] Mungu wako, Mutakatifu wa Israeli, Mwokozi wako. . . . Ninyi ni washuhuda wangu, [Yehova] anasema, mutumishi wangu niliyemuchagua; mupate kujua na kuniamini, na kufahamu ya kuwa mimi ndiye.”—Isa. 43:1-3, 10, ZSB.
21. Bila kujali yaliyoko wakati ujao, Sefania 3:16, 17 huwasihi watumishi wa Yehova wafanye nini, wakiwa na hakika gani?
21 Basi, hata kama bado itawapasa Washuhuda wa Kikristo wa Yehova wapite katika kile kinacholingana na moto na maji, yeye atakuwa pamoja nao. Atajionyesha kuwa Mungu yule yule wa ukombozi. Sasa hakuna msingi wa kulegeza mkono wetu na kulegeza bidii yetu katika utumishi kama washuhuda wake wa Ufalme. Kuogopa wakati ujao ulio karibu duniani kusituogofye na kutufanya tuache kutenda. Yeye anafurahia yale ambayo tumefanya katika utumishi wake wa Ufalme mpaka sasa, kwa sababu hiyo ametubariki sana. Maneno ya unabii yaliandikwa kwa ajili yetu na sasa yanatuhusu sisi: “Katika siku ile Yerusalemu utaambiwa, Usiogope, Ee sayuni; mikono yako isilegee. [Yehova], Mungu wako, yu katikati yako shujaa awezaye kuokoa; atakushangilia kwa furaha kuu, atatulia [atanyamaza; atastarehe; ataridhika] katika upendo wake. Atakufurahia kwa kuimba.”—Sef. 3:16, 17.
22. Basi, imetupasa tutumie mikono yetu kwa uhodari tufanye kazi gani?
22 Na tuendelee kumpa Mungu aliye hai wa “Yerusalemu wa mbinguni” sababu kuu ya kufurahi na kutushangilia. Hivyo mikono yetu hii ambayo imekuwa na bidii sana mpaka sasa katika kumhudumia Yehova Mungu katika hekalu lake la kiroho—isilegee sasa. Na tuitumie kwa uhodari tufanye kazi yenye kuokoa uhai ambayo bado yatakiwa ifanywe kabla taabu ya sasa ya ulimwengu haijafikia upeo wake katika “dhiki kubwa.”
23. (a) “Habari njema ya ufalme” itahubiriwa mpaka wakati gani? (b) Ni nani atakayepewa shukrani kwa sababu ya kuokolewa kwa wanadamu wenye kutii katika taabu ya ulimwengu?
23 “Habari njema ya ufalme” ilitabiriwa na Yesu Kristo ihubiriwe mpaka mwisho wa taratibu hii ya mambo utakapokuja. (Mt. 24:14) Hakuna mwendo mwingine mzuri unaojitokeza kwetu sisi kama wanafunzi wake waaminifu na wenye utii isipokuwa kuendelea kuhubiri ulimwenguni pote mpaka ufalme wa “mbingu mpya” utakapokuwa si “habari njema” tena bali, Furaha wee! kitu halisi chenye utukufu pamoja na “dunia mpya,” jamii mpya ya kibinadamu, kitakachojaa Paradiso itakayorudishwa pamoja na haki. Ndipo shukrani zote zitakapotolewa kwa Yehova anayeokoa wanadamu wenye utii katika taabu ya ulimwengu kuingia katika “dunia mpya” yake yenye amani.
—Man’s Salvation, sura 19, maf. 25-46.