Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 4/15 kur. 12-16
  • Njia ya Uzima ni Nyembamba Lakini ni Huru

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Njia ya Uzima ni Nyembamba Lakini ni Huru
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UNYOFU WA TABIA UNAHITAJIWA SANA KATIKA NJIA YA UZIMA
  • JE! UCHAWI UNATOA UONGOZI UNAOFAA?
  • UNAJIMU SI UONGOZI WENYE KUTEGEMEKA
  • WAJIBU WA KUND! LA KIKRISTO JUU YA WATU WAZOEAO DHAMBI
  • Kwa Nini Uepuke Kuwasiliana na Pepo?
    Amkeni!—2008
  • Kuwasiliana na Ulimwengu wa Roho—Kunaonwaje na Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Je, Kuwasiliana na Pepo Kuna Madhara?
    Vijana Huuliza
  • Mbona Wengi Wanapendezwa na Uwasiliani-roho?
    Amkeni!—2000
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 4/15 kur. 12-16

Njia ya Uzima ni Nyembamba Lakini ni Huru

1. Katika Mathayo 7:14, ni nini maana ya neno “nyembamba”?

YESU KRISTO alisema: “Mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani.” (Mt. 7:14) Neno la Kigiriki ambalo Mathayo alitumia kueleza maneno ya Yesu “limetumiwa kwa usemi wa mfano katika Mathayo 7:13, 14, kuhusu mlango unaoelekeza watu kwenye uzima wa milele, ulio mwembamba kwa sababu haupatani na maelekeo ambayo watu wanazaliwa wakiwa nayo.”​—⁠Kamusi ya W. E. Vine iitwayo Expository Dictionary of New Testament Words.

2. Ni kwa njia gani ‘wembamba’ wa “ile Njia” usivyozuia mtu kuwa na uhuru wa kweli?

2 Basi ‘wembamba’ wa “ile Njia” hauna maana ya kutofikiria maoni ya watu wengine, kujionyesha utawa kupita kiasi. Si njia ya kujitenga na watu wengine, kama katika makao ya watawa. ‘Wembamba’ wake unamaanisha kutokuwa na upotovu wa tabia, kuwa na kusudi maishani, kutosita-sita. Ni “nyembamba” kwa sababu inazuia mtu asifanye mambo yenye madhara. Kuwa na uhuru wa kweli hakumpi mtu leseni ya kufanya jambo lo lote atakalo, kwa sababu kufanya hivyo kunaharibu uhuru wa wengine. Baada ya muda mfupi huo utakuwa si uhuru tena, kwa maana utaleta ugomvi, chuki, hata uuaji. Kwa mfano, sheria za serikali za ulimwengu zisipotiiwa kabisa kutakuwa na mchafuko na hali mbaya sana hata kusiwe na mtu mwenye uhuru halisi wala furaha.

3. Ni kwa njia gani mwendo wa Mkristo ni wa ‘kujitahidi’?

3 Mkristo ana makosa mengi ya kutokamilika sawa na mtu mwingine ye yote. Anapojaribu kuyasahihisha, tamaa mbaya za mwili zinamhuzunisha kwa sababu analazimika kuzizuia sana. (Rum. 7:24) Katika Luka 13:24, Yesu alisema: “Jitahidini kwa nguvu nyingia mpate kuingia kupitia mlango ule mwembamba.” (NW) Tunahitaji kujitahidi kama wapiga mbio katika Michezo ya Olympic ya kale na ya kisasa, si kwa sababu “njia” ya uzima inachukiza, bali kwa sababu ulimwengu na utu wetu wenyewe usio mkamilifu unatuletea mikazo. Kanuni za “ile Njia” hazifikiwi bila jitihada, lakini mtu akizifikia anapata uradhi, furaha na uhuru ulio mkubwa zaidi.

4. Kwa sababu gani Mkristo wa kweli anaweza kutumainiwa, kwama yanavyoonyesha maandiko yaliyo katika fungu hili?

4 Unyofu ni mojawapo matakwa ya “ile Njia” yanayoifanya iwe nyembamba. Mtu anawezaje kujiona na usalama na furaha katika ulimwengu ambamo hawezi kutumaini mwanadamu mwenzake? Kwa kuwa hawezi, Wakristo wanafuata njia ya unyofu, si kwa maneno tu, bali kwa matendo pia. (1 Yohana 3:18) Mkristo wa kweli hataiba wala kuzoea unyang’anyi. Katika biashara hatatumia njia za mkato au zilizo haramu, huku akitoa habari zisizo za kweli, akiwadai kwa siri wafanya kazi anaowasimamia wamrudishie kiasi fulani kati ya mshahara wao. Yeye hatafanya mapatano ya kibiashara kwa kupitia “mlango wa nyuma” wala kuhonga watu ili apate mapendeleo ya pekee. (Kut. 23:8; Zab. 26:9, 10) Iwezekanapo atarudishia watu hata vitu walivyopoteza, bila kuomba wala kutamani apewe zawadi.​—⁠Kum. 22:1-3.

5. Je! Mkristo anaweza kufuata njia ya unyofu katika ulimwengu huu?

5 Lakini je! Mkristo anaweza kuendelea kufanya hivyo katika taratibu hii ya ulimwengu inayoendeshwa na kanuni za udanganyifu, au uchoyo? Wale wanaofuata Ukristo wa kweli wamepatwa na magumu fulani, hata wakafutwa kazi kwa sababu ya kukataa kufanyia matajiri wao jambo la udanganyifu. Lakini, kwa ujumla, wameona kwamba matajiri wao wanawaheshimu na kuwapa madaraka makubwa zaidi kwa sababu ya kufanya kazi kwa bidii ili wasipate malipo ya bure. Wanatambuliwa kuwa wenye kutegemeka, wenye kutimiza wajibu wao kwa uaminifu, tena wanatumainika na wanaweza kushughulika na wengine bila kukosana-kosana. Ushujaa unatakiwa ili kusimama imara ufanye mambo ya unyofu, lakini Mkristo anaweza kutegemea mashauri ya Biblia na ahadi ya Mungu iliyo katika Waebrania 13:5, 6: “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa. Hata twathubutu kusema, Bwana ndiye anisaidiaye, sitaogopa; mwanadamu atanitenda nini?”

UNYOFU WA TABIA UNAHITAJIWA SANA KATIKA NJIA YA UZIMA

6. (a) Ni matunda gani yanayozaliwa na “tabia mpya”? (b) Mtume Paulo anauelezaje mwendo wa ufisadi na matunda yake?

6 Mtu ye yote anayesoma Biblia anajua kwamba njia ya uzima haiwezi kufuatwa bila kuwa na unyofu wa tabia na usafi. Lakini, watu wengi wanasema leo kwamba maoni hayo ni ya kikale na kwamba “tabia mpya” ya upotovu na ya kuachilia watu wafanye mambo watakayo inawaweka huru wafurahie maisha mazuri zaidi. Je! ni kweli? Ebu iangalie hali iliyopo leo. Hiyo “tabia mpya” imezaa matunda gani? Imezaa matatizo yenye kusumbua akili za watu, ikafanya jamaa ziwe na mgawanyiko, kuwe na magonjwa na kifo. Mtu hawezi kuingiza ufisadi katika maisha yake bila kujiharibia furaha. Mtume Paulo anaeleza matokeo ya ufisadi, nasi leo tunaiona hali hiyo kuhakikisha kwamba alisema kweli. Aliandika yafuatayo juu ya watu fulani walioachilia matendo mabaya:

“Walipomjua Mungu hawakumtukuza kama ndiye Mungu wala kumshukuru; bali walipotea katika uzushi wao, na mioyo yao yenye ujinga ikatiwa giza. Wakijinena kuwa wenye hekima walipumbazika . . . Kwa ajili ya hayo Mungu aliwaacha katika tamaa za mioyo yao, waufuate uchafu, hata wakavunjiana heshima miili yao. Kwa maana waliibadili kweli ya Mungu kuwa uongo, wakakisujudia kiumbe na kukiabudu badala ya Muumba . . . Hivyo Mungu aliwaacha wafuate tamaa zao za aibu, hata wanawake wakabadili matumizi ya asili kwa matumizi yasiyo ya asili; wanaume nao vivyo hivyo waliyaacha matumizi ya mke, ya asili, wakawakiana tamaa, wanaume wakiyatenda yasiyopasa, wakapata nafsini mwao malipo ya upotevu wao yaliyo haki yao. Na kama walivyokataa kuwa na Mungu katika fahamu zao, Mungu aliwaacha wafuate akili zao zisizofaa, wayafanye yasiyowapasa.”​—⁠Rum. 1:21-28.

7. Mtume anaonyesha kwamba mtu anayekuwa Mkristo anahitaji sana kufanya badiliko gani?

7 Ndipo mtume alipoendelea kutaja uhalifu mwingi na mazoea mapotovu tunayoaona yakiwa yameenea ulimwenguni pote leo. (Rum. 1:29-32) Katika barua nyingine, aliwaambia Wakristo hivi: “Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani, ndiyo ibada ya sanamu: kwa ajili ya mambo hayo huja ghadhabu ya Mungu. Katika hayo ninyi nanyi mlitembea zamani, mlipoishi katika hayo. Lakini sasa yawekeni mbali nanyi haya yote, hasira, na ghadhabu, na uovu, na matukano, na matusi vinywani mwenu.” (Kol. 3:5-8) Wale ambao wameifuata njia hiyo kadiri ambavyo wameweza, wakamwomba Mungu awasaidie, wamepata maisha yenye furaha zaidi kwa kuepuka ufisadi na mambo hayo mengine yaliyotajwa na Paulo.​—⁠ 1 Tim. 4:8.

JE! UCHAWI UNATOA UONGOZI UNAOFAA?

8. (a) Kwa sababu gani leo watu wengi wanaendea wenye mazoea ya mafumbo wakapashwe habari, na je! wanapata uongozi wa kiroho? (b) Maandiko ya Kiebrania yanafunuaje maoni ya Mungu juu ya uchawi?

8 Watu wanahitaji msaada leo kweli kweli. Kuna mambo mengi yenye kuwafadhaisha, nao wanautafuta msaada kwa kuviendea vyanzo vingi vinavyodai kwamba vinaweza kuwapa uongozi. Kimojawapo ni mazoea ya mafumbo, yaani, uchawi, kuagua na mambo kama hayo. Je! kutafuta msaada katika vyanzo hivyo kutamweka mtu katika njia ya uzima? Je! vyanzo hivyo vinatoa uongozi wa kiroho? Hapana, Biblia inapanga uchawi kati ya “matendo ya mwili” kwa sababu unatosheleza tamaa za kimwili, si za kiroho. (Gal. 5:19-21) Neno la Yehova linafunua maoni yake juu ya namna zote za uchawi au mazoea ya mafumbo, na vilevile juu ya wale wanaotafuta msaada kwa vyanzo hivyo. Aliwaambia Waisraeli watu wake wa kale hivi:

“Usijifunze kutenda kwa mfano wa machukizo ya mataifa yale [yaliyo katika Kanaani]. Asionekane kwako . . . mtu atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu. Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa [Yehova].”​—⁠Kum. 18:9-12.

9. Wakati mtu anapoendea wachawi wampe maarifa anakuwa akimwomba nani hasa amsaidie?

9 Kwa kuwa uchawi unakatazwa na Mungu, ni wazi kwamba mtu anayeomba wachawi maarifa au msaada hawi akimwomba Mungu. Huyo anategemea chanzo kinachopingana na Mungu, nayo Biblia inatujulisha ni chanzo gani. Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo hivi: “Vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu; nami sipendi ninyi kushirikiana na mashetani. Hamwezi . . . kushirikiana katika meza ya Bwana na katika meza ya mashetani. Au twamtia Bwana wivu? Je! tuna nguvu zaidi ya yeye?”​—⁠l Kor. 10:20-22.

10. Mtu anayetegemea uchawi ataingia katika hatari gani kubwa?

10 Kwa hiyo, mtu ye yote akiliepuka Neno la Mungu na kutegemea kitu kingine kimtatulie tatizo la maisha, anamkana Mungu na kuingia katika mikono ya adui wabaya zaidi wa Mungu na wanadamu, yaani, mashetani waovu, malaika walioasi wenye kuendesha shughuli zao kwa kusimamiwa na “mkuu wa pepo,” Shetani Ibilisi,​—⁠Luka 11:15; 1 Pet. 3:19, 20; 2 Pet. 2:4; Yuda 6; Efe. 6:11, 12; 2 Kor. 4:4.

UNAJIMU SI UONGOZI WENYE KUTEGEMEKA

11. (a) Wanajimu wanakana kwamba mwanadamu hakuumbwa akiwa na uwezo gani wa ndani? (b) Badala ya kutegemea nyota zituongoze, Biblia inatushauri tufanye nini? (c) Mazoea ya namna mbalimbali za uchawi yalifanya Babeli wa kale upatwe na nini?

11 Wanajimu pia (yaani, wenye kubashiri mambo kwa kutazama nyota) wanamkana Mungu na enzi kuu aliyo nayo juu ya wanadamu. Kulingana na unajimu, mwanadamu si kiumbe chenye uhuru wa kujichagulia mambo; kila upande wa maisha yake unaongozwa na nyota na sayari kwa kutegemea mahali zilipo, kwa hiyo mwanadamu ni mashine yenye kuongozwa vyo vyote tu itakiwavyo. Lakini mwanadamu alifanywa kwa mfano na sura ya Mungu. Ana hiari ya kujichagulia mambo. Anaweza kuchagua mwendo anaotaka kufuata na hivyo anaweza kujiamulia mambo anayotaka yampate mwishowe maishani. Biblia inataja mara nyingi kwamba ana uhuru huo wa kujichagulia mambo, kisha inamshauri aifuate njia anayoonyeshwa na Mungu ikiwa anataka kupata uzima wa milele akiwa mwenye furaha. (Kum. 30:19, 20; Mt. 6:33; Matendo 17:26, 27; Ufu. 22:17) Tena, Mungu anamwonya ‘asishangae kwa sababu ya ishara za mbinguni.’ (Yer. 10:2) Babeli wa kale ulikuwa adui ya Mungu, nao uliharibiwa kwa sababu ya namna zake mbalimbali za unajimu, uchawi na ibada ya mashetani. Mungu aliuambia Babeli hivi:

“Simama sasa na uganga wako, na wingi wa uchawi wako, uliojitaabisha nao tangu ujana wako; labda utaweza kupata faida, labda utaweza kushinda. Umechoka kwa wingi wa mashauri yako; basi, na wasimame hao wajuao falaki, wazitazamao nyota, watabirio kila mwezi mambo ya mwezi huo, wakakuokoe na mambo yatakayokupata. Tazama, watakuwa kama mabua makavu; moto utawateketeza; hawatajiokoa na nguvu za mwali wa moto . . . Hapatakuwa na mtu wa kukuokoa.”​—⁠Isa. 47:12-15.

WAJIBU WA KUND! LA KIKRISTO JUU YA WATU WAZOEAO DHAMBI

12. (a) Kwa sababu gani ni lazima kundi la Kikristo lisiwe na mazoea ya kufanya makosa, na ni hatua gani inayochukuliwa kuhakikisha kwamba jambo hilo halitukii? (b) Hatua hiyo inayochukuliwa juu ya watenda makosa inawafanyaje washiriki wa kundi la Kikristo wafurahie maisha?

12 Kupatana na maoni ya Mungu na kanuni ambazo ameweka katika Neno lake lililoandikwa, lazima makundi ya Mashahidi wa Yehova yajiepushe na lawama la kufanya makosa ili yaendelee kuwa na ‘upendeleo wa Mungu. Lazima yawe safi machoni pa Mungu. Kwa hiyo makundi hayo yanawataka washiriki wake waendelee kuifuata njia ya maisha ya Kikristo. Wale wanaozidi kuvunja kanuni za Biblia za kweli, za adili na unyofu, na vilevile watu wenye kujitia katika mazoea ya kiuchawi, lazima waondolewe katika makundi au watengwe na ushirika. (1 Kor. 5:11) Hivyo, uchafu wala upotovu ambao umeziharibu madhehebu za kidini za Jumuiya ya Wakristo haupati nafasi katika kundi lililo la Kikristo kweli kweli. Ni furaha kweli kweli kushirikiana na watu safi kiroho katika ibada safi ya Yehova Mungu, yenye kutakata.

13. Kuzitii “habari njema” kunaleta faida gani sasa na wakati ujao?

13 Zaidi ya hilo, kuzitii “habari njema” za Mungu, kuutafuta kwanza Ufalme na haki ya Mungu, ndiyo njia ya uzima yenye kutosheleza watu na kuleta furaha sasa. Juu ya hayo, chini ya utawala wa Ufalme wake Mungu hatawapa uzima duniani wale wanaotaka kuchafua usafi na utulivu wa dunia hiyo. Katika njozi yake iliyoandikwa katika kitabu cha mwisho cha Biblia, mtume Yohana anaeleza mambo haya:

“Nikaona mbingu mpya na nchi mpya; kwa maana mbingu za kwanza na nchi ya kwanza zimekwisha kupita, wala hapana bahari tena. Nami nikauona mji ule mtakatifu, Yerusalemu mpya, ukishuka kutoka mbinguni kwa Mungu, umewekwa tayari, kama bibi-arusi aliyekwisha kupambwa kwa mumewe. Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha enzi ikisema, Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”​—⁠Ufu. 21:1-4.

14. Kulingana na maelezo ya Ufunuo juu ya “nchi mpya,” je! mtu mwenye kuzoea ufisadi, unyang’anyi, na mambo kama hayo, ataiingia nchi hiyo?

14 Je! uongo, uasherati, uzinzi, hali ya kulalana kwa wanaume na wenzao na wanawake na wenzao, ulevi, matumizi mabaya ya dawa za kulevya, uchawi, unajimu, mazoea ya mafumbo, kucheza kamari, unyang’anyi, ugomvi na uuaji utaruhusiwa katika jamii hiyo ya kibinadamu? Je! dunia yenye mambo hayo mabaya inaweza kukosa machozi na kifo? Hata kidogo. Mungu mwenyewe anaendelea kutuhakikishia hivyo, akisema: “Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauaji, na wazinzi, na wachawi, na hao waabuduo sanamu, na waongo wote, sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti. Hii ndiyo mauti ya pili.”​—⁠Ufu. 21:8.

15. Mungu anatoa uhakikisho gani wa kusaidia mtu anayetaka kufanya yaliyo haki kwa moyo mweupe?

15 Lakini Yehova Mungu hakuwaacha bila msaada wale ambao mioyo yao inaelekea mambo yanayofaa, wanaotaka sana kuishi kwa amani pamoja na wanadamu wenzao. Amewaonyesha fadhili kwa kuwapa nguvu za kutosha, ushujaa na usaidizi kutoka kwa Wakristo wenzao ili waifuate njia ya uzima inayompendeza Yeye na kuwapa upendeleo wake. Mwandikaji aliyeongozwa na Mungu anasema haya: “Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu. Kwa kuwa hatuna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi. Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”​—⁠Ebr. 4:14-16; linganisha 1 Wakorintho 10:13.

16. Mtu akizisikia “habari njema,” aanze kutembea katika “ile Njia” bila kuiacha, anaweza kuwa na hakika kwamba atafaulu?

16 Mungu amefanyia wanadamu mpango mzuri kweli kweli, wamfikie yeye, wapate upendeleo wake na kutembea katika njia ya utii! Na wakati wale wanaochagua kumtii wanapotembea katika njia ya uzima, anawaonyesha fadhili kwa kuwapa nguvu zinazopita zile za kawaida, ili mtu anayetii kwa moyo mweupe afaulu kutembea katika “ile Njia.” (2 Kor. 4:7; Isa. 40:10,11, 29-31) Tena, kuifuata njia hiyo kunaleta uhuru​—⁠amani ya akili, kusudi la kuishi, uhuru wa kutokuwa na hofu nyingi mno kuhusu hali za uchumi, vita na kifo. Kunakuwa na uhuru mwingi zaidi wa kusaidia watu wengine, kwa sababu Mkristo wa kweli ana kitu cha kuwapa kinachowasaidia na kuwafariji kikweli. ​—⁠Kutoka The Watchtower, Oct. 15,1977.

[Maelezo ya Chini]

a ‘Kuona maumivu makali,’ ‘kuwa ukijikakamua’: angalia kamusi ya Vine iitwayo Expository Dictionary of New Testament Words, chini ya neno “strive” (jitahidi), Authorized Version, maelezo ya pembeni; Kingdom Interlinear Translation.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Kila mahali watu wanahitaji uongozi. Wengi wanategemea uchawi. Kweli wanakuwa na hali nzuri zaidi kwa kufanya hivyo?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki