Kuwasiliana na Ulimwengu wa Roho—Kunaonwaje na Mungu?
“KUPENDA na kutopenda mambo mamoja, hilo ndilo jambo linalofanyiza urafiki imara,” akasema Sallust mwanahistoria Mroma. Kweli kweli, rafiki ni mtu ambaye mnapatana katika mambo yaliyo mengi, mtu unayeweza kutumaini. Vivyo hivyo, Mungu anatutazama sisi kuwa rafiki na kuturuhusu tumkaribie zaidi ikiwa tunapenda na kutopenda mambo mamoja na yeye. Hiyo inamaanisha kwamba tunavutiwa na sifa za Mungu kama vile upendo, amani, fadhili, na wema, na kwamba sisi tunafanya jitihada za bidii nyingi ili kuiga vitabia hivyo katika maisha yetu.—Wagalatia 5:22, 23, NW.
Basi, ili tuone kama kuwasiliana na ulimwengu wa roho kunakubaliwa na Mungu, labda kwanza tunaweza kuchunguza kunazaa tunda gani. (Mathayo 7:17, 18) Je! kunatusaidia sisi tukuze sifa za kimungu zenye kuvutia? Ili tuone jambo hilo, acheni tutazame mifano miwili ya maisha halisi.
Uaguzi, Kunyanyaswa-nyanyaswa, na Kifo
Asamaja Amelia, mwanamke wa makamo katika Suriname, alikuwa na umri wa miaka 17 alipohusika kwa mara ya kwanza katika uaguzi, namna moja ya kuwasiliana na ulimwengu wa roho. Kwa kuwa matabiri yake yalikuwa kweli na wauliza-habari walinufaika na mashauri yake, yeye alistahiwa sana katika mtaa wake. (Linganisha Matendo 16:16.) Lakini jambo moja lilimsumbua.
“Roho waliosema kupitia kwangu waliwafadhili wale waliotafuta msaada wao,” akasema, “lakini wakati ule ule walifanya maisha yangu yawe yenye huzuni. Baada ya kila kikao, nilihisi nikiwa nimepigwa-pigwa na ni kwa shida sana kwamba niliweza kuondoka nilipokuwa. Usiku ulipoingia, nilitumainia kupata pumziko kidogo, lakini roho hao hawakuniacha. Waliendelea kunisumbua, wakisema nami na kunizuia nisilale. Tena we, walisema mambo makubwa kama nini!” Mwanamke huyo anatweta na kutazama chini, akitikisa kichwa kwa kuchukizwa sana. “Walipenda kusema juu ya ngono na walisisitiza kwamba wafanye ngono nami. Ilikuwa vibaya sana. Mimi nilikuwa nimeolewa. Sikutaka kukosa uaminifu na niliwaambia hivyo. Hiyo haikusaidia. Wakati mmoja kani fulani isiyoonekana ilinishinda nguvu, ikagusa mwili wangu na kuufinya-finya, hata ikaniuma. Nilihisi nikiwa ovyo sana.”
‘Ati roho watie moyo ukosefu wa adili kingono? hayo yametungwa tu!’ huenda wewe ukapaaza sauti. Je! kweli roho hao wameshuka tabia kwa kadiri hiyo?
“Mambo ni mabaya hata zaidi ya hivyo!” anasema Izaak, aliyetangulia kutajwa. “Usiku mmoja tuliitwa tukasaidie mwanamke mmoja mgonjwa aliyesumbuliwa na roho mmoja. Kiongozi wa kikundi—aliye chombo cha kuwasiliana na roho mwenye nguvu zaidi—alijaribu kufukuza roho yule. Muda wa siku nzima tukaomba sana roho wake asaidie. Tulicheza dansi na kuzipiga ngoma, na pole kwa pole mwanamke huyo akapata nafuu. Kiongozi aliagiza roho wa mwanamke yule amtoke, naye akamtoka. ‘Tumepata ushindi,’ kiongozi akasema aking’aa kwa furaha. Ndipo tukaketi na kustarehe.”
Izaak anaipumzisha kwa muda mikono yake yenye kutoa-toa ishara huku akitulia kwa njia inayomaanisha kuna jambo. Ndipo anapoendelea kusema: “Kwa muda fulani kulikuwa na utulivu, lakini ndipo ukelele ulipomaliza kimya kile. Tulipiga mbio kwenda kwenye nyumba ulikotoka tukamwona mke wa kiongozi. Alikuwa akilia kwa bumbuazi. Ndani ya nyumba, tukakuta binti yake mdogo—kichwa chake kikiwa kimetazama nyuma! Kani fulani ilikuwa imemsongonyoa shingo ikavunjika, ikamwua kama kuku—ikaonekana ni kisasi kutoka kwa roho yule aliyetupwa nje. Po! Roho hao ni wauaji wasio na huruma!”
Kuwasiliana na Ulimwengu wa Roho na “Kazi za Mwili”
Uchafu, ukosefu wa adili kingono, na uuaji—kama ulivyoonekana katika visa hivyo viwili vilivyohusu uwasilianaji na ulimwengu wa roho—ni vitabia vinavyopingana kabisa na utu wa Mungu. Na hiyo inasaidia kutambulisha kweli kweli roho hao ni akina nani. Huenda wakasingizia kuwa wajumbe wa Mungu, lakini kazi zao za ukosefu wa adili na uuaji zinawafunua kuwa waigaji wa adui ya Mungu ambaye ndiye mwuaji wa kwanza katika historia, Shetani Ibilisi. (Yohana 8:44) Yeye ndiye kiongozi wao. Wao ni wasaidizi wake—malaika waovu, au mashetani,—Luka 11:15-20.
Lakini huenda wewe ukauliza: ‘Je! ni katika pindi chache tu vitabia hivyo vya kishetani vinapoonekana-onekana katika kuwasiliana na ulimwengu wa roho? Je! kwa ujumla kuwasiliana na ulimwengu wa roho kungeweza kunifanya mimi niwasiliane na roho wema ambao wangesaidia kuleta mimi karibu zaidi na Mungu?’ Hapana, Biblia inaorodhesha “zoea la kuwasiliana na ulimwengu wa roho” pamoja na “kazi za mwili” zingine zinazopingana moja kwa moja na sifa za Kikristo.—Wagalatia 5:19-21, NW.
Kwenye Ufunuo 21:8, NW, “wale wanaozoea kuwasiliana na ulimwengu wa roho” (“wale wanaofanya maongezi pamoja na mashetani,” The Living Bible) wanawekwa katika kikundi kimoja na “wale wasio na imani na wale wanaochukiza katika kinyaa chao na wauaji na waasherati . . . na waabudu-sanamu na waongo wote.” Yehova anawaonaje waongo, waasherati, wauaji, na wazoeao kuwasiliana na ulimwengu wa roho kwa makusudi? Yeye anachukia matendo yao!—Mithali 6:16-19.
Basi, kujaribu-jaribu kuwasiliana na ulimwengu wa roho ni sawa na kupenda anayochukia Yehova Mungu. Ni kama kumkataa Yehova, kuwa katika kambi ya Shetani, na kujipanga upande mmoja na adui mkubwa zaidi wa Mungu na wasaidizi wake. Sasa fikiria jambo hili: Je! ungetaka kuwa karibu na mtu anayejipanga upande mmoja na adui zako? Bila shaka sivyo. Bali, ungekaa mbali kabisa na mtu huyo. Ni wazi, basi, kwamba tunaweza kutazamia Yehova Mungu aone ivyo hivyo. Inasema Mithali 15:29, NW, “Yehova yuko mbali sana na waovu.” —Ona pia Zaburi 5:4.
Kuwasiliana na Ulimwengu wa Roho Kunaongoza Kwenye Kifo
Kuchezea-chezea uwasilianaji na ulimwengu wa roho kunahatarisha uhai pia. Mungu aliliona jambo hilo kuwa sababu ya adhabu ya kifo miongoni mwa watu wake katika Israeli ya kale. (Walawi 20:27; Kumbukumbu 18:9-12) Kwa hiyo usiwe mshangao kwetu kwamba wanaozoea kuwasiliana na ulimwengu wa roho “hawatarithi ufalme wa Mungu.” (Wagalatia 5:20, 21, NW) Badala ya hivyo, “kisehemu chao kitakuwa katika ziwa lile linalowaka moto,” linalomaanisha “kifo cha pili,” au uharibifu wa milele. (Ufunuo 21:8, NW) Ni kweli, leo huenda mengine ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yakauvumilia uwasilianaji na ulimwengu wa roho, lakini maoni ya Biblia hayajabadilika.
Namna gani ikiwa wewe tayari umekwisha kuchukua hatua za kwanza katika barabara inayoenda kwenye uwasilianaji na ulimwengu wa roho? Basi utafanya vema kuacha pasipo kukawia na kugeuka. Fuata shauri lenye roho ya Mungu ambalo Isaya nabii wa Mungu aliwapa Waisraeli wa kale. Hali yao inafanana na ile ya watu wa leo wanaojitia katika mazoea machafu lakini wanafikiri wanaabudu Mungu wakati ule ule. Kwa sababu hiyo, kuna masomo muhimu katika mambo yaliyowapata. Masomo gani?
Tii Onyo la Isaya
Kutazama sura ya kwanza ya Isaya kunaonyesha kwamba Waisraeli walikuwa ‘wamemwacha Yehova’ na ‘wakageukia nyuma.’ (Mstari 4, NW) Ingawa walikuwa wamekengeuka, waliendelea kutoa dhabihu, kushika miadhimisho ya kidini, na kutoa sala. Lakini wapi! Kwa kuwa hawakuwa na tamaa ya kindani ya kutaka kufurahisha Muumba wao, Yehova alisema: “Mimi naficha macho yangu kutoka kwa ninyi. Hata ingawa mwatoa sala nyingi, mimi siwi ninasikiliza.” Waisraeli hao walikuwa wameasi dhidi yake kwa kuanza kufuata mazoea machafu hata kufikia hatua ya ‘kujaza mikono yao umwagaji wa damu.’—Mistari 11-15, NW.
Ni chini ya hali gani Yehova angewakubali wamrudie? Yaangalie matakwa yaliyotajwa wazi kwenye Isaya 1:16, NW. Yeye anasema: “Jiosheni wenyewe; jisafisheni wenyewe.” Kwa hiyo tukichukua shauri hilo kwa uzito, tutaacha mazoea machafu au tujiepushe nayo, kutia na uwasilianaji na ulimwengu wa roho, ambayo ni moja ya “kazi za mwili.” Kwa kuwa tunajua kwamba akili mbovu inayounga mkono kuwasiliana na ulimwengu wa roho ni ile ya Shetani Ibilisi, tutakuza uchukivu wa jambo hilo.
Ndipo tunapopaswa kuondoa vitu vyote vinavyohusiana na kuwasiliana na ulimwengu wa roho. Izaak alifanya hivyo. Yeye anasema: “Siku moja nilikusanya mali zangu zote za kuwasiliana na ulimwengu wa roho nikaziweka mbele ya nyumba yangu, nikavuta shoka, nikazichanja-chanja vipande vipande. Jirani yangu alipiga kelele kwamba ningejuta kwa nililokuwa nimefanya. Mwanamke huyo alipokuwa akipiga kelele, nilimimina petroli juu ya vipande hivyo nikachoma kila kimoja cha vitu hivyo. Hakuna kilichobaki.”
Hiyo ilikuwa miaka 28 iliyopita. Je! Izaak alijuta kwa kitendo chake? Sivyo. Leo, yeye anatumikia Yehova kwa furaha akiwa mhudumu Mkristo katika moja la makundi ya Mashahidi wa Yehova.
Isaya 1:17 inatoa shauri hili zaidi: “Jifunzeni kutenda mema.” Ili kufanya hivyo, inatakiwa kujifunza Neno la Yehova, Biblia, ili kujua ni nini yaliyo “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Warumi 12:2, NW) Na kutumia maarifa hayo uliyoyapata karibuni kutaongoza kwenye baraka zinazoburudisha. Hivyo ndivyo Asamaja alivyoona.
Ijapokuwa alipingwa vikali na watu wa ukoo na jirani zake, Asamaja alijifunza Biblia kwa ushujaa pamoja na Mashahidi wa Yehova na muda mfupi baada ya hapo akaacha kuwasiliana na ulimwengu wa roho. Ndipo mwanamke huyo alipoweka maisha yake wakfu kwa Yehova Mungu na akabatizwa wakati wa kusanyiko moja. Sasa, karibu miaka 12 baadaye, anasema hivi kwa kushukuru: “Tangu ubatizo wangu, mimi sijasumbuliwa na roho hao.” Naye anakumbuka hivi kwa tabasamu: “Usiku uliofuata ubatizo wangu, usingizi wangu ulikuwa mzito sana na usiosumbuliwa hata nikafika nimechelewa kwenye programu ya kusanyiko ya asubuhi iliyofuata.”
Manufaa Zinazodumu
Leo, wote wawili Izaak na Asamaja wanaweza kwa uthamini wa moyo kusema hivi pamoja na mtunga zaburi Asafu: “Nami kumkaribia Mungu ni kwema kwangu.” (Zaburi 73:28) Kweli kweli, kukaribia Yehova kumewaletea wao manufaa za kimwili na za moyoni. Lakini zaidi ya yote, kumewapa amani ya kindani na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova.
Baraka hizo zinayapita kwa mbali maumivu na mng’ang’ano unaotakiwa ili kulikung’uta kongwa la kuwasiliana na ulimwengu wa roho. Ingawa hivyo, kuvunja uhusiano na jambo hilo kunaweza kuwa pambano kubwa kweli kweli. Lintina van Geenen, mwanamke mmoja katika Suriname, alipatwa na jambo hilo. Sasa, tutaona jinsi yeye alivyominyana na jambo hilo kwa miaka mingi lakini mwishowe akafanikiwa.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Asamaja Amelia anasimulia hivi: “Roho wale . . . walifanya maisha yangu yawe yenye huzuni. . . . Tena we, walisema mambo makubwa kama nini!”