Kuwasiliana na Ulimwengu wa Roho—Kwa Sababu Gani Kunazidi Kupendeza Watu?
FRANS ni nguzo ya kanisa la Kiprotestanti la mahali hapa. Kukiwa na kazi ya kanisa, yeye ndiye wa kwanza kusaidia. Wilhelmina ni mcha-Mungu pia. “Lazima uende kanisani,” Wilhelmina anasema, na ndivyo anavyofanya. Esther vivyo hivyo anahudhuria kanisa kwa ukawaida na haachi hata siku moja ipite bila kusema sala zake. Wote watatu wanafanana katika jambo moja: Wao ni vyombo vya kuwasiliana na ulimwengu wa roho.
Wakaaji watatu hao wa Suriname hawako peke yao. Ulimwenguni pote, upendezi wa kuwasiliana na ulimwengu wa roho waovu unavuvumka. Fikiria hili: Katika United States peke yake, karibu magazeti 30 yenye jumla ya mwenezo wa nakala zaidi ya 10,000,000 yanatumiwa sana kuhusiana na maajabu ya ulimwengu wa roho. Watu wanaokadiriwa kuwa 2,000,000 katika Uingereza wanapendezwa na habari iyo hiyo. Uchunguzi wa hivi majuzi katika Netherlands ulionyesha kwamba wenye kuamini matukio yanayoongozwa na nguvu zinazopita zile za kibinadamu wanapatikana miongoni mwa wakaaji wa miji mikubwa, watu wenye elimu ya juu, na vijana. Zaidi ya hilo, kama vile wakaaji wa Afrika, Esia, na Latini Amerika wanavyoweza kushuhudia, katika nchi nyingi sana kuwasiliana na ulimwengu wa roho kumekuwa sehemu ya daima ya maisha ya kila siku. Si ajabu kwamba watungaji John Weldon na Clifford Wilson wanakata shauri hivi katika kitabu chao Occult Shock and Psychic Forces: “Waelezaji wa namna nyingi mbalimbali wanaelekea kuhisi kwamba sisi tumo katika wakati wa mrudio usiotangulia kuwa na kifani wa kufuatia mafumbo ya ulimwengu wa roho.”
Ndiyo, kuwasiliana na ulimwengu wa roho na kufanya mambo ya mafumbo—kwa namna za unajimu, kuongoza matendo ya watu kwa kutia akili zao katika usingizi, kuchunguza mambo yanayofanya akili za watu zione mazingaombwe, kuwa na utambuzi usiotegemea hisia zile za kawaida, kufanya miujiza ya kiuchawi, kufasiri ndoto, na kadhalika—kunavutia watu wa tabaka zote. Kwa sababu gani?
Kwanza, mengine ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yanauachilia tu uwasilianaji na ulimwengu wa roho na hata kuukubali. Yanadokeza kwamba kuwasiliana na ulimwengu wa roho ni njia nyingine tu ya kumkaribia Mungu zaidi.
Kwa mfano, mfikirie Izaak Amelo, mfanyi biashara mwenye umri wa miaka 70 katika Suriname. Kwa miaka saba yeye alikuwa mshiriki mheshimiwa wa baraza la kanisa na wakati ule ule akawa chombo kijulikanacho sana cha kuwasiliana na ulimwengu wa roho. Yeye anakumbuka hivi: “Kila Jumamosi baraza zima la kanisa letu lilikusanyika nje ya kijiji kuomba habari kwa roho waovu. Tuliendelea usiku kucha. Asubuhi ilipofika, shemasi alikuwa akitazama saa yake ya mkononi, na kama saa kumi na moja hivi, akatuashiria tuache. Ndipo tulipooga, tukabadili mavazi yetu, na kuelekea kanisani—tukafika kabla tu ibada ya Jumapili asubuhi haijaanza. Miaka yote hiyo mchungaji hakusema hata neno moja la kukataa jambo hilo.”
Baada ya kuchunguza ukamatano uliopo kati ya kuwasiliana na ulimwengu wa roho na makanisa katika Suriname, Profesa Mholanzi R. van Lier anahakikisha kwamba watu wengi wanaona kuwasiliana na ulimwengu wa roho kuwa “dini nyongeza.” Katika uchunguzi mmoja uliochapishwa hivi majuzi na Chuo Kikuu cha Leiden, yeye anasema pia kwamba uwasilianaji na ulimwengu wa roho unabainiwa kuwa “sehemu ya muundo mpana wa kidini ambamo unasimama upande mmoja na Ukristo.”
Lakini huenda wewe ukataka kujua, ‘Je! makanisa yanapokubali uwasilianaji na ulimwengu wa roho huo ni uhakikisho wa kwamba unakubaliwa na Mungu? Je! kuwasiliana na roho kutakuleta karibu zaidi na yeye? Biblia inasema nini hasa juu ya kuwasiliana na ulimwengu wa roho?’
[Picha katika ukurasa wa 3]
Izaak Amelo anakumbuka kwamba baraza zima la kanisa lilishiriki katika mikutano ya kuwasiliana na ulimwengu wa roho