Kukung’uta Lile Kongwa la Kuwasiliana na Ulimwengu wa Roho
BALAA ilipiga jamaa yetu nilipokuwa msichana wa miaka 14. Wakati huo, mwuaji mwovu sana alianza kumaliza-maliza watu wa ukoo wangu. Watu wa kwanza aliomaliza walikuwa watoto wa dada yangu—wote tisa. Ndipo akageuka dhidi ya mume wake. Muda mfupi baada ya hapo, akaua mmoja wa dada zangu pia. Wanne zaidi wa ndugu na dada zangu wakafuata, mpaka tukabaki mama yangu na mimi tu. Niliogopa, wee!
Wakati wa miaka iliyofuata, nilikula, nikafanya kazi, na kulala kila siku nikitetema mtetemo mkuu. Nilijiuliza: ‘Atashambulia lini? Na itakuwa zamu ya nani—Mama au mimi?’
Malezi Yangu
Kukusaidia ufahamu yaliyotukia baadaye, acha nikusimulie malezi yangu. Katika 1917, nilizaliwa nikiwa mshiriki wa kabila la Wanigro-Mashamba wa Paramaccaner katika kisiwa kimoja cha Mto Maroni katika Suriname. Babu zangu walikuwa den lowenengre, au watumwa watoro, waliokuwa wamekimbia wakaingia porini ili wajitafutie riziki katika maisha ya jasho lakini yenye uhuru. Basi, kwa kweli yalikuwa maisha yenye uhuru wa kutokuwa katika utumwa wa wanadamu lakini si kutoka na uhuru kwa utumwa wa mashetani.
Kila siku maisha katika kijiji chetu yalitawalwa na ibada ya mashetani na wazazi wa kale waliokufa. Ili kufunga watu kwa kuwanuizia uchawi na kuleta magonjwa na kifo juu ya wanadamu wenzao, watu fulani walitumia wisi, ulozi. Au waliomba msaada wa koenoe (linatamkwa koo noo), mchokozi. Wachokozaji hao wanaaminiwa kuwa watu waliotendwa vibaya na mshiriki fulani wa jamaa. Baada ya wao kufa, wanasemekana kuwa wanarudia jamaa ile kuonyesha kisasi chao. Hata hivyo, kwa kweli wachokozi hao ni mashetani walioshuka tabia ambao wanalazimisha watu kuwaabudu.
Nikiwa mshiriki wa Jumuiya ya Undugu wa Waevanjeli, kanisa ambalo ni la Kiprotestanti, nilijifunza pia habari fulani juu ya Mungu. Ingawa niliachwa gizani nisijue jinsi ya kumwabudu, msitu wenye mvua ulionizunguka ulinipa uthibitisho mwingi kwamba yeye ni Mwandalizi mwema. ‘Mimi nataka kuabudu Mungu mwema si roho mwovu anayeleta taabu,’ nikawaza. Nilijua kwamba wachokozi wanafurahia kutesa-tesa watu wasiotaka kuwaabudu mpaka wanawaua.
Wazia jinsi nilivyoshtuka kujua kwamba adui za jamaa yetu walikuwa wametupelekea koenoe. Mimi nilikuwa na umri wa miaka 14 alipojiondokea kuanza tume yake ya kuua. Miaka 26 baadaye, Mama na mimi tu ndio tuliobaki.
Mkabiliano wa Kwanza
Mama alikuwa mfanya kazi mwenye bidii. Siku moja, alipokuwa akitembea kuelekea shamba lake, aliangushwa chini asiweze kuinuka. Yule koenoe alikuwa amemchagua mama yangu. Afya yake ilidhoofika naye akapooza. Alihitaji msaada—msaada wangu. Lakini fikira zangu zilivurugika kati ya kumpenda yeye na kuogopa shetani lililompagaa. Hata hivyo, wakati wa mashambulio ya koenoe yule, maskini Mama alipaaza sauti kwa maumivu mengi sana nisiweze kuvumilia tena, nikalaza kichwa chake katika paja langu kumfariji. Ndipo alipotulia, lakini mimi nikahisi “mikono” ikifinya mwili wangu.
Nilipotaka kukimbia, Mama alilia tena. Kwa hiyo nikabaki pale kwa ajili yake na kuvumilia kabiliano langu la kwanza lenye kutetemesha na mwuaji huyo. Nilikuwa mwenye umri wa miaka 40.
Mashambulio ya Nguvu Zaidi
Mama akafa. Siku tatu tu baadaye, nikasikia sauti yenye urafiki ikisema: “Lintina, Lintina, kwani hunisikii? Mimi ninakuita.” Huo ulikuwa ndio mwanzo wa huzuni kubwa sana hata nikajitakia kifo cha haraka.
Kwanza shetani hilo lilinisumbua nilipokuwa nikienda kulala. Nilipokuwa karibu kusinzia, sauti ile ilikuwa ikiniamsha, ikisema juu ya makaburi na kifo. Kupoteza usingizi kulifanya nihisi nimedhoofika, ingawa niliendelea kutunza watoto wangu.
Baadaye shetani lile likaongeza mashambulio yake. Mara kadha nilihisi kama kwamba lilikuwa likininyonga. Ingawa nilijaribu kukimbia, sikuweza kwa sababu ilielekea ni kama uzito mwingi ulinifinya mwili. Nilitaka kupiga ukelele lakini sikuweza kutokeza hata kisauti kimoja. Hata hivyo, nilikataa kumwabudu mshambuliaji wangu.
Nilipokuwa nikipata nafuu baada ya kila shambulio, nilirudia ukulima, kukuza muhogo na miwa na kuiuza sokoni katika mji mmoja mdogo wa pwani. Ikawa rahisi zaidi kutafuta riziki, lakini taabu zangu zilizo mbaya zaidi zilikuwa mbele.
Kutafuta Maponyo
Siku moja niliisikia sauti yenye utabiri mbaya ikisema, “Nitavimbisha tumbo lako liwe kama mpira.” Muda fulani baadaye, kidonge kigumu kilitokea katika tumbo langu kikazidi-zidi kuwa kikubwa mpaka nikaonekana mwenye mimba. Kwa kuogopa sana, nilijiuliza hivi: ‘Je! Mungu, Muumba, anaweza kunisaidia nimwondolee mbali koenoe huyu? Je! Yeye anaweza kutuma roho mwema mwenye nguvu zaidi amfukuze huyu?’ Ili nipate habari, niliendea bonoeman, mchawi.
Mchawi wa kwanza alinipa tapoes, au hirizi, lakini mvimbo ule ukabaki tu. Kwa kupiga moyo konde nipate maponyo, nilisafiri kutoka kwa bonoeman mmoja hadi kwa mwingine—lakini wapi. Kati ya ziara hizo, niliendelea kulima nipate pesa za kununua pombe, divai, divai-shampeni, na shuka za kujifunga kiunoni ili kuwalipa wachawi. Mara nyingi walinishauri hivi: “Mpigie magoti koenoe huyo. Msihi kama bwana-mkubwa. Mwabudu yeye, naye atakuacha.” Lakini ningewezaje kupigia magoti roho aliyenitesa-tesa na kutaka kuniua? Singeweza.
Hata hivyo, kwa sababu ya shida yangu kubwa nilifanya kila jambo jinginelo nililoambiwa na wachawi hao. Mmoja wao alinitibu kwa miezi mitano. Aliniogesha kwa miti-shamba na kukamulia utomvu wa mimea 11 mbalimbali ndani ya macho yangu—“ili kuyatakatisha,” akasema huku mimi nikitoa ukelele wa maumivu. Lakini mwishoni mwa matibabu hayo, nilienda nyumbani bila hata peni moja, nikiwa nimevunjiwa heshima, na nikiwa mgonjwa kuliko wakati mwinginewo wote.
“Huu Ndio Mwisho Wako”
Mmoja wa wanangu, anayeishi katika Netherlands, alinipelekea pesa niendelee kutafuta msaada. Kwa hiyo nikaendea daktari wa dawa za kawaida katika mji mkuu. Baada ya kunichunguza, akasema: “Siwezi kukusaidia. Nenda ukaone bonoeman.” Kwa hiyo nikajaribu chombo cha kuwasiliana na ulimwengu wa roho mwenye asili ya East Indies—lakini bado sikupata msaada. Nikaanza kuelekea nyumbani lakini niliweza tu kuwasili kwenye mji mkuu, nikafikia nyumba ya mmoja wa binti zangu. Pale nikazimia—nikiwa nimefilisika na mgonjwa. Nilikuwa nimetumia bure tu miaka 17 na guilder 15,000 (U.S. dola 8,300) nikitafuta maponyo. Nilikuwa na umri wa miaka 57.
Halafu, lile shetani likatisha hivi: “Nimechoka na wewe. Huu ndio mwisho wako.”
“Lakini wewe si Mungu, wewe si Yesu,” nikapaaza sauti.
“Hata Mungu hawezi kunizuia,” shetani lile likajibu. “Siku zako zina namba.”
Mng’ang’ano wa Mwisho
Majuma kadha yalipita. Meena, bibi mmoja jirani aliyekuwa mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, akauliza binti yangu juu ya hali yangu na kusema: “Mama yako anaweza kusaidiwa kwa kutumia Biblia tu.” Niliposikia maongezi hayo kwa mbali, nikatembea kuwaelekea. Hata hivyo, kabla sijawafikia, nilitupwa chini. Meena akafanya haraka kuja na kusema: “Shetani hilo halitakuacha. Mtu mmoja tu anayeweza kukusaidia ni Yehova, hakuna mwingineye yote.” Ndipo akasali pamoja nami kwa Yehova Mungu na kuanza kunitembelea. Lakini kadiri alivyozidi kunitembelea, ndivyo mashambulio ya shetani lile yalipozidi kuwa makali. Wakati wa usiku, mwili wangu ulitikisika kwa fujo sana hata hakuna mtu katika nyumba hiyo aliyeweza kulala. Niliacha kula na nikawa na dakika ambazo nilirukwa na akili kabisa.
Hali yangu ikawa mbaya sana hata wanangu wakatoka mashambani wanipeleke kijijini nikafie huko. Kwa kuwa nilikuwa dhaifu mno nisiweze kusafiri, nilikataa. Lakini kwa kuhisi kifo kikikaribia, nilimwita Shahidi yule kumpa salamu zangu za mwisho. Meena alieleza kutokana na Biblia kwamba hata kama ningekufa, kuna tumaini la ufufuo.
“Ufufuo? Wamaanisha nini?”
“Mungu anaweza kukuinua uishi katika Paradiso,” yeye akajibu. Huo ukawa ni mwonzi wa tumaini!
Lakini usiku huo huo shetani lile likanipagaa. Nikiwa katika hali ya njozi, ilikuwa ni kama naona koenoe yule akifuatwa na kutano la watu. Yeye alidhihaki hivi: “Ati mwanamke huyu anafikiri atapata ufufuo.” Ndipo kutano lile likacheka na kucheka. Lakini ndipo mimi nilipofanya jambo ambalo sijapata kamwe kufanya. Niliita hivi: “Yehova! Yehova!” Hivyo tu ndivyo nilivyojua kusema. Na shetani lile likaondoka!
Wana wangu walikuja tena wakanisihi: “Mama, usifie mjini. Acha tukupeleke kijijini.” Mimi nilikataa, kwa maana nilitaka kujifunza mengi zaidi juu ya Yehova. “Haya, labda bado mimi nitakufa,” nikawaambia, “lakini angalau nitakuwa nimetumikia Muumba.”
Kama Mnara Wenye Nguvu
Meena na Mashahidi wengine waliendelea kunitembelea. Walinifunza kupelekea Yehova sala. Miongoni mwa mambo mengine, waliniambia juu ya suala lililopo kati ya Yehova na Shetani na jinsi Ibilisi alivyoleta taabu juu ya Ayubu ili kumfanya amkane Mungu. Kujifunza mambo hayo kuliutia nguvu usadikisho wangu nisiliabudu kamwe shetani lile. Mashahidi walisoma andiko lililokuja kuwa andiko nilipendalo: “Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Ndani yalo mwenye uadilifu anapiga mbio naye anapewa himaya.”—Mithali 18:10, NW.
Polepole nguvu zangu zikarudi. Mwanangu aliporudi, nikamwambia angojee nje. Nilivaa nguo na kufutika blausi ndani ya rinda langu kuonyesha kwamba mvimbo ule ulikuwa karibu kwisha. Ndipo nikatembea kwenda nje.
“Huyu ni Mama Lintina?” mwanangu akaboboka.
“Ndiyo, ni mimi—asante kwa Yehova, Mungu wangu!”
Kuchukua Msimamo Wangu
Kuanzia dakika ile nilipoweza kutembea kidogo, nilienda kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Kule nilipokea kitiamoyo kingi sana kutoka kwa akina rafiki mpaka nikahudhuria mikutano bila kuacha kamwe. Miezi michache baadaye, niliandamana na Mashahidi katika kazi ya kuhubiri peupe. Muda mfupi baada ya hapo, nilibatizwa nikawa mtumishi wa Yehova, Mwokoaji wangu mwenye upendo. Nilikuwa na umri wa miaka 58.
Hata hivyo, jambo fulani lilibaki kufanywa. Miaka mingi hapo mwanzoni niliporudi katika kijumba changu cha nyasi kijijini, nilikuwa nimejenga madhabahu ambayo juu yayo ningewatolea dhabihu wazazi wangu wa kale waliokufa. Ili niwe safi kiroho, nililazimika kuiharibu. Nilimwomba Yehova msaada, kwa kuwa kitendo changu kingeweza kuleta zahama miongoni mwa wanakijiji. Nilipofikia kijumba changu na kufungua mlango, mtu fulani alipiga uyowe hivi: “Pingos!” (Nguruwe-mwitu!) Kundi lao lilikuwa likivuka kisiwa kile na kuruka mtoni ili kuogelea kwenda ng’ambo ya pili. Bila kukawia, vijana kwa wazee wakakiacha kijiji wakakamate mlo ule uliopatikana kwa urahisi. Nilisisimuka, nikapiga magoti na kumpigia Yehova asante kwa tukio hilo. Nikafanya haraka kuiburuta nje madhabahu ile, nikaimwagia mafuta-taa na kuiwasha moto. Madhabahu iliteketea kabla ya kundi lile la watu kurudi. Bila shaka, waligundua nililofanya, lakini hawangeweza tena kuirudisha. Hivyo, nikiwa na amani ya akili, nikaurudia mji mkuu.
Kutoka Kwenye Huzuni Kubwa Kuja Kwenye Furaha
Baraka nyingi zilinijia. Mwanangu aliyekuwa Netherlands hakuamini hadithi alizokuwa amesikia juu yangu naye akapanda ndege kuja Suriname ajionee mwenyewe. Alifurahi sana kuniona mwenye afya hata akaninunulia nyumba nzuri katika mji mkuu huo, ninakoishi sasa. Lo, nimepata badiliko lililoje—kuacha kuwa mtumwa wa mashetani asiye na hata peni moja na kuwa mtumishi wa Yehova mwenye kutunzwa vizuri.
Miaka kumi na mmoja baada ya ubatizo wangu, nina sababu hata zaidi ya kuwa mwenye shukrani. Kwa kusukumwa na baraka nyingi nilizopokea, watatu kati ya watoto wangu na mwana-mkwe mmoja walikuja pia kupendezwa na ukweli wa Biblia na hatimaye wakatoa maisha zao wakfu kwa Yehova Mungu. Nami nimesimulia tena na tena mambo yaliyonipata kuhusiana na ushetani wakati ndugu na dada wameenda nami kuona wanafunzi wao wa Biblia wasio na ushujaa wa kuwa huru kwa kuvunja uhusiano na mashetani. Kwa njia hiyo hata miaka ile yenye kunitetemesha kwa woga imekuwa yenye mafaa fulani katika utendaji wa kuuhubiri Ufalme.
Sina maneno ya kutosha kueleza shukrani zangu kwa Yehova, Mungu wangu. Kwa uhakika, mimi nimeona mkono wake wa nguvu zote ukifanya kazi kwa ajili yangu. Kweli kweli, Yehova amekuwa mwema kwangu!—Linganisha Zaburi 18:17-19.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Katika kuwa huru na uhusiano wa uwasilianaji na ulimwengu wa roho, Lintina van Geenen alijifunza kwamba “jina la Yehova ni mnara wenye nguvu”
[Picha katika ukurasa wa 9]
Suriname bara ambako watu wengi ni mateka wa uwasilianaji na ulimwengu wa roho