Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 10/1 kur. 14-18
  • Jina La Mungu Na Litukuzwe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jina La Mungu Na Litukuzwe
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUSUDI LA MAISHA ZETU
  • MBELE YA WATU WA KARIBU NA WA MBALI
  • MBELE YA JAMAA
  • EPUKA KUJIFIKIRIA KUPITA KIASI
  • KUWA MSHIRIKI WA HABARI NJEMA
  • Kwa Nini Ni Lazima Tujue Jina la Mungu
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • Yehova Analikweza Jina Lake
    Ufalme wa Mungu Unatawala!
  • Liheshimu Jina Kuu La Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Mfalme wa Umilele
    “Ufalme Wako Uje”
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 10/1 kur. 14-18

Jina La Mungu Na Litukuzwe

“Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe.”​—Mt.6:9.

1. Jambo la kwanza na kuu ambalo inatupasa tuombe ni jambo gani?

Ye yote anayejidai kuwa Mkristo amesoma au akasikia sala ambayo Yesu alitoa kama kielelezo wa wanafunzi wake walipomwuliza: “Bwana, tufundishe sisi kusali.” Kama jambo la kwanza kabisa, Yesu alisema hivi: “Baba [yetu uliye mbinguni] Jina lako litakaswe.”​—Luka 11:1, 2.

2. Jina la Yehova linawakilisha mambo gani?

2 Kati ya majina yote yaliyoko katika ulimwengu wote, jina la Baba, Yehova, lapita yote katika kung’aa, utukufu na heshima. Si kwamba tu yeye ndiye Muumba, mwenyezi na mwenye maarifa yasiyo na kikomo, anayetekeleza hukumu kamilifu, lakini hata zaidi ya hayo, fadhili zake zisizostahilika na rehema zinafanya jina lake listahili heshima na sifa iliyo kuu zaidi, ndiyo, hata ibada. Musa alipoomba auone utukufu wa Mungu, alielekezwa aende katika Mlima Sinai, “[Yehova] akashuka ndani ya lile wingu, akasimama pamoja naye huko, akalitangaza jina la [Yehova. Yehova] akapita mbele yake, akatangaza, [Yehova, Yehova], Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe; mwenye kuwapatiliza watoto uovu wa baba zao, na wana wa wana wao pia, hata kizazi cha tatu na cha nne.”​—Kut. 33:18-23; 34:4-7.

3. Sifa kuu za Mungu ni sifa gani, na ni kwa sababu gani anasema hatamwachilia mtu ye yote bila kumhukumu?

3 Upendo na rehema za Yehova zimeonyeshwa hapa kuwa kati ya sifa zake zilizo kuu. Walakini Aliye Juu Zaidi hatamwachilia mtu mwovu apotoe rehema zake kama sababu ya kuendeleza upotovu. Kama sivyo, hawezi kuuongoza ulimwengu wote kwa faida ya wale wanaotaka kufanya yaliyo mema. Mmojawapo mitume wa Kristo anasema juu ya watu fulani: “Na kama walivyokataa kuwa na Mungu katika fahamu zao, Mungu aliwaacha wafuate akili zao zisizofaa, wafanye yasiyowapasa. Wamejawa na udhalimu wa kila namna.” (Rum. 1:28, 29) Njia yao ya maisha, kutia na ibada yao ya sanamu na ufisadi bila shaka ilikuwa na matokeo mabaya katika watoto wao. (Rum. 1:21-23) Walakini hata watoto hawa wanaweza kupokea rehema za Mungu wakimgeukia kwa msaada.​—Eze. 18:21, 22.

KUSUDI LA MAISHA ZETU

4. Sisi kama Mashahidi wa Yehova, ni jambo gani tunalopaswa kufanya hazina yetu na jambo la kujisifia?

4 Kwa hiyo, Yehova anatueleza sisi wanadamu jambo ambalo tunapaswa kufanya kuwa hazina yetu. Anasema hivi: “Mwenye hekima asijisifu kwa sababu ya hekima yake, wala mwenye nguvu asijisifu kwa sababu ya nguvu zake, wala tajiri asijisifu kwa sababu ya utajiri wake; bali ajisifuye na ajisifu kwa sababu hii, ya kwamba ananifahamu mimi, na kunijua, ya kuwa mimi ni [Yehova], nitendaye wema, na hukumu, na haki, katika nchi; maana mimi napendezwa na mambo hayo.”​—Yer. 9:23, 24.

5. Yesu alionaje moyoni mwake kutakasa jina la Yehova kuwa jambo kuu?

5 Kwa hiyo, jina la Yehova na yote yanayowakilishwa nalo yanapaswa kuwa ndiyo ya maana zaidi katika mioyo yetu. Yesu alipokuwa duniani, mambo yaliyomwuudhi zaidi yalikuwa lawama lililoletewa jina la Mungu, sana sana na watu wa Mungu wenyewe, Wayahudi. Alisema: “Nafanya sikuzote yale yampendezayo [Mungu],” (Yohana 8:29) Katika dhiki yake katika bustani ya Gethsemane, jambo lililomhangaisha zaidi halikuwa kwamba alikaribia kufa. Alikuja duniani, akazaliwa kama mwanadamu kwa kusudi la kufa kifo cha dhabihu, naye alitembea bila kugeuka kuelekea mwisho huo. Lakini jambo lililomlemea sana usiku huo wa mwisho kabla ya kifo chake lilikuwa lawama ambayo kifo chake chini ya shtaka la kumkufuru Mungu kingeletea jina la Yehova​—yeye, Mwana wa Mungu na wakili wa Mungu, kufa katika njia hii yenye lawama sana mbele ya ulimwengu wote. Kwa habari yake iliandikwa hivi: “Malaumu yao waliokulaumu wewe yalinipata mimi.”​—Rum. 15:3.

6. Usemi unaopatikana katika Warumi 15:3 unapaswa kuwa na matokeo gani kwetu sisi Wakristo, kama alivyoonyesha mtume Paulo?

6 Mtume Paulo anatumia usemi huu awatie moyo Wakristo wafikirie jambo jingine zaidi ya kujipendeza tu​—kwamba wanapaswa kuwa na nia ya kujitoa wasaidie wengine. (Rum. 15:1, 2) Kristo aliishi na kufa kwa ajili ya hilo, akiyachukua malaumu yote, ili watu wawe na maoni yanayofaa kuelekea Baba yake, tena wamjue na kumtukuza Mungu. Akizungumza kwa Wakristo, Paulo alisali hivi: “[Mnie] mamoja ninyi kwa ninyi, kwa mfano wa Kristo Yesu; ili kwa moyo mmoja na kwa kinywa kimoja mpate kumtukuza Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo.”​—Rum. 15:5, 6.

MBELE YA WATU WA KARIBU NA WA MBALI

7. Mkristo anawezaje kutakasa jina la Mungu (a) faraghani, (b) katika jamaa yake, na (c) kundini?

7 Mkristo ambaye ameitwa kwa jina la Yehova anawezaje kuwa na hakika kwamba analitukuza jina la Mungu sikuzote? Bila shaka, yeye anafanya hivyo hata kwa faragha kwa kuliona jina la Mungu kuwa takatifu moyoni na akilini mwake. Anafanya hivyo katika jamaa yake kwa kuzungumza mambo yanayofaa na kwa kuwaangalia kwa upendo kila mmoja wao, akionyesha sifa ambazo Mungu anaonyesha jamaa yake. Kuelekea ndugu zake katika kundi la Kikristo yeye analitukuza jina la Mungu kwa kuwasaidia kila apatapo nafasi, akichukuliana na udhaifu wa wengine ambao hawana nguvu za kiroho kama zake. (Gal. 6:10) Kwa kuwa anaitwa kwa jina la Yehova, yeye anajua kwamba yale anayoyasema na kutenda yatalipasa jina la Mungu.

8. Mtu anaweza kutakasaje jina la Mungu machoni pa walioko nje, na ni maoni gani ya Mungu anayopaswa kuwa nayo?

8 Yeye analitukuzaje jina la Mungu machoni pa watu walioko nje? Kwa kumwiga Mungu na kwa kuwajulisha wengine sababu ya kufanya hivyo. Kwa hiyo inampasa awapende kama anavyowapenda Mungu. Mungu angeweza kuwaona wanadamu wote kama wenye dhambi wenye kuchukiza, kujitafutia makuu na wasiofaa kitu. Kwa haki yeye angeweza kuonyesha nia ya uchafu na iliyoshushwa sana, ujinga wao pamoja na mazoea yao ya kipumbavu. Walakini, Mungu hakuwa na maoni hayo. Yeye aliona mambo haya ambayo hakuyapenda. Lakini, “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Naye Kristo alitufia sisi “hapo tulipokuwa hatuna nguvu, . . . tulipokuwa tungali wenye dhambi, . . . tulipokuwa adui.”​—Rum. 5:6-10.

9. Mkristo anawezaje kulitakasa jina la Mungu anaposema na wengine wasioijua kweli?

9 Mojawapo wa njia za moja kwa moja za kulitukuza jina la Mungu ni kuwaambia wengine mipango ya Mungu kwa wanadamu, wawe wanaonekana kupendezwa au hapana, kila wakati Mkristo atakumbuka kulitukuza jina la Mungu. Hii inamaanisha kwamba mwenendo na usemi wetu unapaswa uwe ule ambao, ikiwezekana, utamtia mtu moyo awe na maoni ya kirafiki zaidi kuelekea kwa Mungu. Tunapaswa tukumbuke kwamba yule mtu tunayezungumza naye haoni mambo namna tunavyoyaona sisi. Yeye anaona kwa wepesi zaidi nia yetu nyofu, yenye fadhili, na yenye kusaidia pamoja na adabu nzuri, kuliko anavyosikiliza maneno yetu. Ikiwa atakosa kuona mambo hayo, yeye hatasikiliza yale tuyasemayo.

10. Tunapozungumza na wale walioko nje, ni jambo gani tunalotaka kuepuka na ni jambo gani tutakalokazia?

10 Kupatana na hayo, tunapoenda nyumba kwa nyumba, tunapaswa kuwa na maoni yanayofaa. Kulaumu mambo ambayo mwenye nyumba anaamini au yale anayozoea kufanya hakutamsaidia. Ni lazima tujaribu kusaidia aone kwamba yale tunayomtolea katika jina la Yehova ni mema. Lazima yamvutie kama jambo bora zaidi, au jambo ambalo litamsaidia, si kumlaumu.

11. (a) Je! tunapaswa kuona kwamba sisi tuko bora zaidi ya wale walioko nje ya kundi kwa sababu tunaijua kweli? (b) Mtume Paulo anasema kwamba kusudi la Kristo kumwonyesha fadhili ingawa alikuwa mtenda dhambi sana lilikuwa nini?

11 Vilevile maoni yetu juu yake, na juu ya watu wote katika ulimwengu, yanapaswa yawe kama yale aliyoyaonyesha mtume Paulo. Yeye hakujiona kuwa mtu bora zaidi akiwa kama kiumbe cha kibinadamu chenye makosa kuliko wale aliokuwa akihubiri, ati kwa sababu tu alikuwa na pendeleo la kuijua kweli. Alisema hivi: “Kwa maana najua ya kuwa ndani yangu, yaani, ndani ya mwili wangu, halikai neno jema.” (Rum. 7:18) Alimwambia mwenzake Timotheo hivi: “Nami namshukuru Kristo Yesu Bwana wetu, aliyenitia nguvu kwa sababu aliniona kuwa mwaminifu, akaniweka katika utumishi wake; ingawa hapo kwanza nalikuwa mtukanaji, mwenye kuudhi watu, mwenye jeuri; lakini nalipata rehema kwa kuwa nalitenda hivyo kwa ujinga, na kwa kutokuwa na imani. Na neema ya Bwana wetu ilizidi sana, pamoja na imani na pendo lililo katika Kristo Yesu. Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza ni mimi. Lakini kwa ajili hii nalipata rehema, ili katika mimi wa kwanza, Yesu Kristo audhihirishe uvumilivu wake wote; niwe kielelezo kwa wale watakaomwamini baadaye, wapate uzima wa milele.”​—1 Tim. 1:12-16.

MBELE YA JAMAA

12. Ni hali gani inayoweza kutokea mmoja wa washiriki wa jamaa anapokuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova?

12 Mlango mkubwa ulio wazi kwa wengi wetu kutukuza jina la Yehova unahusiana na jamaa zetu ambao si Mashahidi wa Yehova. Huenda tukawa na unyofu tunapowatolea kweli, walakini huenda tusiwafikirie jamaa zetu inavyofaa, ambao hawajui au hawaoni na kukubali mambo ya Biblia katika njia ile ile tuyaonavyo.

13. Kwa mfano, ni mwendo gani unaoweza kuchukuliwa na mke, akiijua kweli kabla ya mume na washiriki wengine wa jamaa?

13 Kwa mfano, huenda mke akapata kweli, akaona kwamba mambo fulani ambayo yeye, mumewe na washiriki wengine wa jamaa yake walizoea kufanya hapo mbele hayafai. Huenda mumewe pamoja na washiriki wengine wa jamaa wakaona kwamba anafuata dini sana bila kutumia akili akijaribu kuwalazimisha wakubaliane na maoni yake. Huenda akawaambia waziwazi kwamba mambo haya yote wanayozoea, kama vile kuadhimisha sikukuu fulani, ni makosa, hivyo huenda akawazuia wasimsikilize. Ni njia gani ambayo huenda ikiwa bora zaidi?

14. Mmoja wa Mashahidi wa Yehova anapaswa awe na maoni gani yanayofaa juu ya watu wa ukoo wake wasioijua kweli, tena awatendeeje?

14 Onyesha subira, kuwafikiria na huruma! Fikiria wakati unaotumia ukiwatembelea watu usiojuana nao milangoni pao, ukiwasaidia kwa uangalifu wawe na msingi imara kabla ya kujaribu kuwafanya wabadili njia zao, mashirika yao, na mengineyo. Kwa hiyo, kwa sababu gani uwe na haraka kupita kiasi ujaribu kuwalazimisha washiriki wa jamaa yako wakubaliane na maoni yako? Kabla hujaacha kushirikiana nao au kuwafanya wakuache, kwa sababu gani usione jambo hilo kama njia mojawapo ya kumtumikia Mungu unapoendelea kuwa na urafiki, mwenye kusaidia na mpole kama zamani? Katika njia hii utakuwa ukionyesha sifa za Mungu na kulitukuza jina lake hivi kwamba unapokuwa na nafasi ya kuwajulisha mambo mema ya mipango ya Mungu, wanakuwa tayari kusikiliza, kwa sababu wameona sifa za Mungu ndani yako.

EPUKA KUJIFIKIRIA KUPITA KIASI

15, 16. Musa alijiachilia aingie katika mwendo gani usio wa hekima katika jangwa la Sini?

15 Kwa habari ya wale wasioijua kweli, inatupasa tufikiri sikuzote, kama tunavyofanya na ndugu zetu Wakristo hivi: Je! lile ninalofanya au ninaloelekea kufanya linatanguliza kulitukuza jina la Mungu? Ni jambo rahisi kukosa subira na kuudhika au kujiona mwenye haki zaidi ya wengine, na kusahau kumtegemea Yehova kabisa. Huo ni mwendo usio wa hekima. Musa alifanya kosa hili lenye kuhuzunisha sana pindi moja. Waisraeli walikuwa waasi sana na walimsumbua sana Musa. Katika jangwa la Sini walianza kuteta na Musa kwa sababu hawakuwa na maji. Ndipo Yehova aliposema na Musa akamwambia auambie mwamba utoe maji. Lakini Musa aliwaambia watu hivi: “Sikieni sasa, enyi waasi; je! tuwatokezee maji katika mwamba huu?” Mahali pa kusema na ule mwamba, yeye aliupiga mara mbili baada ya kuvuta fikira zao kwake na kuwaita “waasi,” maji yakatokea,​—Hes. 20:1, 2, 7-11.

16 Musa aliweza kuwapa watu hao maji. Lakini Yehova alisema nini?​—“Kwa sababu hamukuniamini, kwa kunitakasa machoni mwa wana wa Israeli, kwa hivi hamutaingiza kusanyiko hili ndani ya inchi niliyowapa.”​—Hes. 20:12, ZSB.

KUWA MSHIRIKI WA HABARI NJEMA

17. (a) Je! sisi kama Mashahidi wa Yehova tuna deni lo lote na watu walioko nje? (b) Eleza jambo moja moja la yale yaliyosemwa na mtume Paulo katika 1 Wakorintho 9:19-27, utumie kanuni hiyo kwa Mashahidi wa Yehova?

17 Kwa kuwa Mungu ametupa pendeleo la kuijua kweli, kwa kweli yeye ametutia katika wajibu kwa habari ya watu walioko nje, pamoja na ndugu zetu. Mtume Paulo alieleza jambo hili kwa Wakristo katika Rumi katika njia hii: “Nawiwa na Wayunani na wasio Wayunani, nawiwa na wenye hekima na wasio na hekima. Kwa hiyo, kwa upande wangu, mimi ni tayari kuihubiri Injili hata na kwenu ninyi mnaokaa Rumi.” (Rum. 1:14, 15) Vilevile Paulo alisema hivi: “Maana ingawa nimekuwa huru kwa watu wote, nalijifanya mtumwa wa wote, ili nipate watu wengi zaidi. Nalikuwa kama Myahudi kwa Wayahudi, ili niwapate Wayahudi; kwa wale walio chini ya sheria, nalikuwa kama chini ya sheria (ingawa mimi mwenyewe si chini ya sheria,) ili niwapate walio chini ya sheria. Kwa wale wasio na sheria nalikuwa kama sina sheria, (si kwamba sina sheria mbele za Mungu, bali mwenye sheria mbele za Kristo), ili niwapate hao wasio na sheria. Kwa wanyonge nalikuwa mnyonge, ili niwapate wanyonge. Nimekuwa hali zote kwa watu wote, ili kwa njia zote nipate kuwaokoa watu. Nami nafanya mambo yote kwa ajili ya Injili ili kuishiriki pamoja na wengine.” Paulo hakutaka akataliwe apoteze baraka za “habari njema” baada ya kuwahubiri wengine.​—1 Kor. 9:19-27.

18. Tunawezaje kufanya kulingana na sala yetu ‘jina la Mungu na litakaswe’?

18 Hivyo, tunaposali, “Baba [yetu uliye mbinguni], Jina Lako litakaswe,” tunakuwa tukimwomba Mungu atusaidie tuweke mambo mengine yote kando ili yale tuyafanyayo yatukuze jina lake sikuzote na kulifanya lionekane kuwa takatifu. Kisha tutafanya kulingana na sala yetu kwa kutoweka kikwazo cho chote mbele ya wengine wanapoitafuta kweli. Tutakuwa waangalifu tuonyeshe upendo zaidi ya kulaumu. Sikuzote tutakumbuka kwamba lengo letu si kuhukumu, bali ni ‘kuwa mshiriki wa habari njema na baraka zake’ pamoja na wengine.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kwa kushindwa kulitakasa jina la Yehova, Musa alipoteza pendeleo kubwa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki