Mahubiri ya Mlimani—Je! Wote Wataingia Katika Ufalme?
BAADA ya kuonya juu ya manabii wa uongo ambao wasikilizaji wake wangeweza kukutana nao wakati wa karne ya kwanza W.K., Yesu alisema hivi: “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni.”—Mt. 7:21; linganisha Luka 6:46.
Ili watu wafurahie baraka za ufalme wa Mungu, lazima wakubali ubwana wa Yesu Kristo. (Rum. 10:9; Flp. 2:11) Walakini mengi zaidi yanatiwa ndani zaidi ya kumtolea Mwana wa Mungu ibada ya mdomo kwa kumwita “Bwana, Bwana.”
‘Afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni” ndiye peke yake anayekubaliwa apate baraka zote za Ufalme. “Mapenzi” yao yameandikwa ifaavyo katika Mahubiri ya Mlimani. Yanahitaji ‘kazi njema’ zifanywe katika kutangaza kweli za Ufalme kwa wengine. Vilevile yanatia ndani kubadili utu wa mtu ili kuonyesha sifa kama vile upole, usafi, uaminifu, ukarimu, upendo unyofu na imani.—Tazama Mathayo 5:16, 21, 22, 27-30, 33-48; 6:1-18, 25-34.
Maneno yanayofuata ya Yesu yanaonyesha kwamba wengi ambao wangedai kuwa wafuasi wake hawangetimiza jambo hilo: “Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.”—Mt. 7:22, 23.
“Siku ile,” wakati Mungu atakapofikiliza hukumu juu ya adui zake (Zek. 14:1-3; 2 The. 2:1, 2; 2 Pet. 3:10-12), “wengi” watataka wafikiriwe kwa kupendelewa kwa kudai kuwa walifanya mambo ya ajabu ‘katika jina lake,’ yaani, kama kwamba ni wawakilishi wa Yesu Kristo na kupitia kwa uwezo wa kimungu waliopata kwake.
Watauliza hivi: “Hatukufanya unabii [yaani, kupashana habari za kimungu na pengine matabiri ya matukio ya wakati ujao] kwa jina lako?” Walakini ‘kutabiri’ huko si kitambulisho hakika cha uanafunzi wa kweli wa Kikristo. Kulingana na Maandiko, matabiri ambayo nyakati nyingine yalitimia, pamoja na ujumbe uliotolewa kama kwamba kwa mamlaka ya kimungu, nayo vilevile yalitangazwa na manabii wa uongo.—Kum. 13:1-3; Yer. 14:14.
Wengine wangejivuna kwamba ‘walitoa pepo kwa jina lake.’ Kuna watu fulani katika Jumuiya ya Wakristo leo wanaodai kuwa na uwezo wa namna hiyo. Walakini zoea hilo la kutoa pepo (kwa sherehe zisizoelezeka) sikuzote limekuwa sehemu ya dini zisizo za Kibiblia. Zaidi ya hayo, Wayahudi fulani wa karne ya kwanza W.K. walitoa pepo kupitia kwa njia za kimwujiza za kutokeza tendo walizoamini kwamba zilipokezanwa na Mfalme Sulemani.a
Si kutabiri kwa njia ipitayo uwezo wa kibinadamu, kutoa pepo wala “miujiza” mingineyo inayotambulisha Wakristo wa kweli. Yesu alitangaza hivi: “Watatokea makristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu; wapate kuwapoteza, kama yamkini, hata walio wateule.” (Mt. 24:24) Hao manabii wa uongo, mabandia (wadanganyaji), watatokea mle mle katika kundi la Kikristo nao wangejaribu kupotoa washiriki wake wengi.—Matendo 20:29; 2 Pet. 2:2, 3, 10-22; Yuda 4, 8-13, 16-19.
Kama ilivyoonyeshwa hapo juu, Yesu alitaja kwamba Wakristo wa kweli wangekuwa wale wenye ‘kufanya mapenzi ya Baba yangu.’ Nayo “mapenzi” ya Baba wakati huu ni yapi? Kama ilivyotabiriwa na Yesu, ni kwamba ‘habari njema hizi za ufalme [uliosimamishwa] . . . zihubiriwe katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote’ kabla ya mwisho kuja. (Mt. 24:14, NW) Je! madhehebu ya Jumuiya ya Wakristo yanatangaza kwamba ufalme wa Mungu umekaribia? Sivyo, kwa kuwa wanauona kuwa jambo lililomo mioyoni mwa watu tu, au ambalo ni la wakati ujao ulio mbali. Kwa unafiki wanamtolea Yesu ibada ya mdomo, bali wanajiepusha kufanya mapenzi ya Baba yake. ‘Kutangaza habari njema za mambo mema’ ya makusudi ya Ufalme wa Mungu ‘kufika miisho ya dunia inayokaliwa na watu’ kumeachiwa kikundi kidogo kinachojulikana kama Mashahidi wa Yehova.—Rum. 10:15, 18, NW; tazama pia 1 Wakorintho 9:16.
Wote wanaodai kuwa na uhusiano pamoja na Yesu Kristo, bila kufanya kazi za Ufalme na kuvaa utu ulio kama wa Kristo kweli kweli, watapatwa na mabaya atakapofikiliza kisasi cha kimungu juu ya taratibu ya mambo iliyopo. Kisha Yesu ‘atakiri,’ au kuonyesha waziwazi, kwamba ‘hakuwajua’ wale ambao Ukristo wao ulikuwa wa kutoa ibada ya mdomo na kinachoitwa zawadi za ‘kuvuta watu.’ “Miujiza mingi” wanayojivunia haikumpumbaza Mwana wa Mungu kamwe. Mahali pa kuonyesha haki, kwa kweli walikuwa ‘watenda maovu.’ Hivyo, wakati Yesu atakapochukua hatua kama mwuaji mwenye kutumiwa na Mungu katika “dhiki kubwa” inayokuja, atawatangazia hivi: “Ondokeni kwangu.” Wakristo hao wa bandia watakataliwa njia ya kuingia katika baraka za milele za ufalme wa Mungu.—Linganisha Mathayo 24:21, 22; 25:41, 46.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari ya Wayahudi kutoa pepo, twasoma hivi katika kitabu Exorcism Through the Ages (Kupunga Pepo Wakati wa Vizazi Vyote): “Jambo kubwa la kupunga pepo kwa Kiyahudi ni kupa jina kwa majina yanayoaminika kuwa yanafaa, yaani, majina ya malaika wema, ambayo ama yanatumiwa peke yake au kwa kuunganisha pamoja na El (=Mungu); hakika kutegemea majina tu kulikuwa kumekuwa ushirikina wa Wayahudi zamani sana, na lilionekana kuwa jambo la muhimu sana kwamba majina yanayofaa, ambayo yalitofautiana nyakati na pindi mbalimbali, yatumiwe. Lilikuwa sadikisho hilo la ushirikina, bila shaka, lililowasukuma wana wa Skewa, ambao walikuwa wameshuhudia kupunga pepo kulikofanikiwa kwa Mtakatifu Paulo katika jina la Yesu, wajaribu kwa kujitakia wenyewe njia hiyo, ‘Nawaapisha kwa jina la Yesu ambaye Paulo anamhubiri,’ wakawa na matokeo yenye msiba (Matendo, 19:13). Lilikuwa sadikisho la Kiyahudi lenye kupendwa na watu wengi, lililokubaliwa hata Yosefo mtu asiyependelea taifa lo lote ambaye alikuwa amesoma sana, kwamba Sulemani alikuwa amepata uwezo wa kutoa pepo, na kwamba alikuwa amebuni na kupokezana njia fulani ambazo zililifaa kusudi hilo. Mwanahistoria huyo Myahudi ameandika namna Eleazari fulani, mbele ya Mfalme Vespasian na maafisa (wakuu) wake, alivyofaulu, kwa kutumia pete ya kimwujiza iliyowekwa puani mwa mtu aliyepagawa, kuvuta pepo puani—uwezo huo wa pete ukiwa ni kwa ajili ya uhakika wa kwamba ilikuwa na mzizi fulani usio wa kawaida ndani yake ambao ulionyeshwa katika njia za kutokeza tendo za Sulemani, na ambao ulikuwa haupatikani kwa urahisi hata kidogo.”—Tazama kitabu Antiquities of the Jews cha Yosefo, Kitabu 8, sura 2, sehemu 5 na kitabu The Jewish War, Kitabu 7, sura 6, sehemu 3.