Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • rs uku. 176-uku. 180
  • Manabii wa Uwongo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Manabii wa Uwongo
  • Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mtu Akisema—
  • Manabii Walikuwa na Kazi Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Manabii Wawongo Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Jinsi ya Kutambua Dini ya Kweli
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Ujumbe Ambao Ni Lazima Tuutangaze
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
Pata Habari Zaidi
Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
rs uku. 176-uku. 180

Manabii wa Uwongo

Maana: Mtu mmoja-mmoja na mashirika yanayotangaza ujumbe ambao wanadai hautoki kwa wanadamu, lakini ujumbe huo hautoki kwa Mungu wa kweli na haupatani na mapenzi yake yaliyofunuliwa.

Manabii wa kweli na wa uwongo wanaweza kutambuliwaje?

Manabii wa kweli hutangaza imani yao katika Yesu, lakini mengi yanahitajiwa kuliko kudai kuhubiri katika jina lake

1 Yoh. 4:1-3: “Yajaribuni maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatokana na Mungu, kwa sababu manabii wengi wa uwongo wameingia ulimwenguni. Mnalijua neno lililoongozwa na roho kutoka kwa Mungu kwa njia hii: Kila neno lililoongozwa na roho linalomkiri Yesu Kristo kuwa alikuja katika mwili hutokana na Mungu, lakini kila neno lililoongozwa na roho ambalo halimkiri Yesu halitokani na Mungu.”

Mt. 7:21-23: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia. Wengi wataniambia siku hiyo, ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako . . . ?’ Na hata hivyo nitawaambia waziwazi: Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu, ninyi wenye matendo ya uasi-sheria.”

Manabii wa kweli hutumia jina la Mungu, lakini kudai tu kumwakilisha hakutoshi

Kum. 18:18-20: “Nitawainulia wao nabii kutoka katikati ya ndugu zao, kama wewe; nami nitaweka maneno yangu katika kinywa chake, naye atasema nao yote nitakayomwamuru. Na itatukia kwamba mtu ambaye hatasikiliza maneno yangu ambayo atayasema katika jina langu, mimi mwenyewe nitamtaka ajibu. Hata hivyo, nabii atakayethubutu kusema katika jina langu neno ambalo sijamwamuru kusema au atakayesema katika jina la miungu mingine, nabii huyo lazima afe.” (Linganisha na Yeremia 14:14; 28:11, 15.)

Yesu alisema: “Sifanyi jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; bali kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya.” (Yoh. 8:28) Yeye alisema: “Nimekuja katika jina la Baba yangu.” (Yoh. 5:43) Pia Yesu alisema: “Yule ambaye husema mambo aliyotunga yeye mwenyewe anatafuta utukufu wake mwenyewe.”—Yoh. 7:18.

Ikiwa mtu mmoja-mmoja au mashirika yanadai kumwakilisha Mungu lakini yanakataa kulitumia jina la kibinafsi la Mungu, nao huzoea kutoa maoni yao wenyewe juu ya mambo, je, wanatimiza sifa hiyo muhimu ya nabii wa kweli?

Uwezo wa kufanya “ishara kubwa,” au “miujiza,” si lazima uwe uthibitisho wa nabii wa kweli

Mt. 24:24: “Makristo wa uwongo na manabii wa uwongo watatokea na kutoa ishara kubwa [“miujiza,” NAJ] na maajabu ili kuwapotosha, ikiwezekana, hata wale waliochaguliwa.”

2 The. 2:9, 10: “Kuwapo kwa huyo mwasi-sheria ni kulingana na utendaji wa Shetani pamoja na kila tendo lenye nguvu na ishara za uwongo na mambo ya ajabu na pamoja na kila udanganyifu usio wa uadilifu kwa wale wanaoangamia, kuwa malipo kwa sababu hawakukubali kuipenda ile kweli ili wapate kuokolewa.”

Kwa upande mwingine, Musa alifanya miujiza kwa mwelekezo wa Yehova. (Kut. 4:1-9) Yehova pia alimpa Yesu uwezo wa kufanya miujiza. (Mdo. 2:22) Lakini mbali na miujiza hiyo, mambo mengine zaidi yalithibitisha kwamba kweli Mungu alimtuma.

Yale ambayo manabii wa kweli wanatabiri hutimia, lakini huenda wasifahamu mambo hayo yatatimizwa wakati gani au jinsi gani

Dan. 12:9: “Nenda, Danieli, kwa sababu maneno hayo yamewekwa siri na kufungwa kwa muhuri mpaka wakati wa mwisho.”

1 Pet. 1:10, 11: “Manabii . . . waliendelea kuchunguza ni majira gani hasa au ni majira ya namna gani ambayo roho iliyokuwa ndani yao ilikuwa ikionyesha kumhusu Kristo ilipokuwa ikitoa ushahidi kimbele juu ya mateso ya Kristo na juu ya utukufu ambao ungefuata hayo.”

1 Kor. 13:9, 10: “Tuna ujuzi wa sehemu tu nasi tunatoa unabii kwa sehemu tu; lakini wakati kile kilicho kamili kitakapofika, kile kilicho kwa sehemu tu kitaondolewa mbali.”

Met. 4:18: “Lakini njia ya waadilifu ni kama nuru inayong’aa, inayozidi kuongezeka mpaka mchana mkamilifu.”

Mitume na wanafunzi wengine wa kwanza wa Kristo walikuwa na matarajio fulani yenye makosa, lakini Biblia haiwahesabu pamoja na “manabii wa uwongo.”—Ona Luka 19:11; Yohana 21:22, 23; Matendo 1:6, 7.

Nathani nabii alimtia moyo Mfalme Daudi afanye yale yaliyokuwa moyoni mwake kuhusu kujenga nyumba kwa ajili ya ibada ya Yehova. Lakini baadaye Yehova alimwambia Nathani amwambie Daudi kwamba si yeye atakayeijenga. Yehova hakumkataa Nathani kwa sababu ya yale aliyokuwa amesema mapema bali aliendelea kumtumia kwa sababu alisahihisha jambo hilo kwa unyenyekevu Yehova alipomweleza waziwazi.—1 Nya. 17:1-4, 15.

Maneno ya nabii wa kweli huendeleza ibada ya kweli na hupatana na mapenzi ya Mungu yaliyofunuliwa

Kum. 13:1-4: “Ikiwa nabii au mwotaji wa ndoto atainuka katikati yenu naye awape ishara au kitu cha ajabu, nayo ishara hiyo au kitu hicho cha ajabu kiwe kweli alichokuambia, akisema, ‘Na tuifuate miungu mingine, ambayo wewe hukuijua, nasi tuitumikie,’ usisikilize maneno ya nabii huyo au mwotaji huyo wa ndoto, kwa sababu Yehova Mungu wenu anawajaribu apate kujua ikiwa ninyi mnampenda Yehova Mungu wenu kwa moyo wenu wote na kwa nafsi yenu yote. Mnapaswa kumfuata Yehova Mungu wenu, nanyi mnapaswa kumwogopa yeye, nanyi mnapaswa kuzishika amri zake, nanyi mnapaswa kuisikiliza sauti yake, nanyi mnapaswa kumtumikia yeye, nanyi mnapaswa kushikamana naye.”

Kwa kuwa Biblia inasema kwamba “rafiki ya ulimwengu” ni adui ya Mungu, je, makasisi wanaowahimiza waumini wao wajiingize katika mambo ya ulimwengu wanaendeleza ibada ya kweli? (Yak. 4:4; 1 Yoh. 2:15-17) Mungu wa kweli alisema kwamba mataifa “watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova,” na Biblia inasema kwamba Mungu angechukua kutoka katika mataifa “watu kwa ajili ya jina lake,” lakini je, mashirika ya kidini yanayopuuza umuhimu wa kulitumia jina la kibinafsi la Mungu yanatenda kupatana na mapenzi hayo ya Mungu yaliyofunuliwa? (Eze. 38:23; Mdo. 15:14) Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali kuhusu Ufalme wa Mungu, na Biblia inaonya mtu asiwatumaini watu wa udongo, kwa hiyo je, makasisi au mashirika ya kisiasa yanayowahimiza watu wautumaini utawala wa wanadamu ni manabii wa kweli?—Mt. 6:9, 10; Zab. 146:3-6; linganisha na Ufunuo 16:13, 14.

Manabii wa kweli na wa uwongo wanaweza kutambuliwa kwa matunda wanayoonyesha katika maisha yao na maisha ya wafuasi wao

Mt. 7:15-20: “Jihadharini na manabii wa uwongo ambao wanakuja kwenu katika mavazi ya kondoo, lakini ndani wao ni mbwa-mwitu wenye kunyafua. Kwa matunda yao mtawatambua. . . . Kila mti mzuri huzaa matunda mazuri, lakini kila mti uliooza huzaa matunda yasiyofaa . . . Basi, kwa kweli kwa matunda yao mtawatambua watu hao.”

Wana maisha ya aina gani? “Matendo ya mwili ni . . . uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu, ibada ya sanamu, mazoea ya kuwasiliana na pepo, uadui, mizozo, wivu, milipuko ya hasira, magomvi, migawanyiko, madhehebu, husuda, vipindi vya kulewa, karamu za kupindukia, na mambo kama hayo. . . . Wale walio na mazoea ya kufanya mambo ya namna hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu. Kwa upande mwingine, matunda ya roho [ya Mungu] ni upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.”—Gal. 5:19-23; 2 Pet. 2:1-3.

Je, Mashahidi wa Yehova hawajawahi kukosea katika mafundisho yao?

Mashahidi wa Yehova hawadai kuwa manabii wanaoongozwa na roho. Nyakati nyingine wao hukosea. Kama mitume wa Yesu Kristo, mara nyingine wao wamekuwa na matarajio fulani yenye makosa.—Luka 19:11; Mdo. 1:6.

Maandiko hutaja wakati mbalimbali kuhusiana na kuwapo kwa Kristo, na Mashahidi wa Yehova wamejifunza mambo hayo kwa makini sana. (Luka 21:24; Dan. 4:10-17) Yesu pia alisimulia ishara yenye mambo mengi, ambayo ingeambatana na utimizo wa unabii mbalimbali unaohusu wakati, ili kutambulisha kizazi ambacho kingeishi kione mwisho wa mfumo mbovu wa mambo wa Shetani. (Luka 21:7-36) Mashahidi wa Yehova wameonyesha uthibitisho wa kutimizwa kwa ishara hiyo. Ni kweli kwamba nyakati nyingine Mashahidi wamekosea katika kuelewa yale ambayo yangetukia kwenye mwisho wa vipindi fulani vya wakati, lakini hawajafanya kosa la kupoteza imani wala kuacha kukesha kuhusiana na kutimia kwa makusudi ya Yehova. Wameendelea kukumbuka kabisa shauri hili ambalo Yesu alitoa: “Endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.”—Mt. 24:42.

Mambo ambayo yamesahihishwa si makubwa yanapolinganishwa na kweli muhimu za Biblia ambazo wamefahamu na kuzitangaza. Baadhi ya kweli hizo ni: Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli. Yesu Kristo si sehemu ya Utatu bali yeye ni Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu. Kukombolewa katika dhambi kunawezekana tu kupitia imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo. Roho takatifu si mtu bali ni nguvu za utendaji za Yehova, na lazima matunda ya roho hiyo yaonekane katika maisha ya waabudu wa kweli. Nafsi ya mwanadamu inaweza kufa, si kama wapagani wa kale walivyodai kwamba haifi; hiyo hufa, na tumaini kwa ajili ya uzima wa wakati ujao ni kupitia ufufuo. Mungu ameruhusu uovu kwa sababu ya lile suala la enzi kuu ya ulimwengu wote. Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee la wanadamu. Tangu mwaka wa 1914, tumekuwa tukiishi katika siku za mwisho za mfumo mbovu wa mambo wa ulimwenguni pote. Wakristo waaminifu 144,000 pekee ndio watakaokuwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo mbinguni, lakini wanadamu wengine watiifu watapata uzima wa milele katika paradiso duniani.

Jambo lingine la kufikiria kuhusu mafundisho ya Mashahidi wa Yehova ni hili: Je, kweli yameboresha maadili ya watu? Je, wale wanaofuata mafundisho hayo wanajulikana katika jamii zao kwa sababu ya unyoofu wao? Je, maisha ya familia zao yamekuwa bora kwa kufuata mafundisho hayo? Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangetambuliwa kwa urahisi kwa sababu ya kuwa na upendo kati yao. (Yoh. 13:35) Je, sifa hiyo inaonekana wazi kati ya Mashahidi wa Yehova? Mambo ya hakika yanaonyesha wazi.

Mtu Akisema—

‘Kasisi wangu alisema Mashahidi wa Yehova ndio manabii wa uwongo’

Unaweza kujibu hivi: ‘Hebu nikuulize, Je, alikuonyesha lolote katika Biblia linaloeleza mambo tunayoamini au kutenda na linalosema kwamba watu wa aina hiyo wangekuwa manabii wa uwongo? . . . Je, nikuonyeshe jinsi Biblia inavyoeleza manabii wa uwongo? (Kisha tumia jambo moja au zaidi kati ya yale yaliyo katika ukurasa wa 176-179.)’

Au unaweza kusema: ‘Nina hakika utakubali kwamba shtaka hilo zito linapaswa kuthibitishwa na jambo hususa. Je, kasisi wako alitaja mifano yoyote hususa? (Ikiwa mwenye nyumba anataja yanayodaiwa kuwa “matabiri” ambayo hayakutimia, tumia habari katika ukurasa wa 177, 178, na ukurasa wa 179, 180.)’

Pia unaweza kujibu: ‘Nina hakika kwamba ikiwa mtu fulani angekushtaki juu ya jambo kama hilo, ungetumia nafasi angalau kueleza msimamo wako au maoni yako, sivyo?  . . . Basi, je, nikuonyeshe katika Biblia  . . . ?’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki